-
“Kupata Lulu Moja ya Thamani Kubwa”Mnara wa Mlinzi—2005 | Februari 1
-
-
“Kupata Lulu Moja ya Thamani Kubwa”
“Ufalme wa mbinguni ndio mradi ambao watu wanajikaza kuufikia, na wale wanaojikaza wanaufikia.”—MATHAYO 11:12.
1, 2. (a) Yesu alionyesha sifa gani isiyo ya kawaida katika mojawapo ya mifano yake kuhusu Ufalme? (b) Yesu alisema nini katika mfano wa lulu ya thamani kubwa?
JE, KUNA kitu fulani unachothamini sana hivi kwamba unaweza kuwa tayari kuacha kila kitu ulicho nacho ili kukipata? Ingawa watu hujitoa ili kufuatilia mradi fulani kama vile kupata pesa, umashuhuri, mamlaka, au cheo, si jambo la kawaida mtu kupata kitu fulani kinachotamanika sana kiasi cha kwamba yuko tayari kuacha kila kitu ili kukipata. Katika mojawapo ya mifano mingi yenye kuchochea fikira kuhusu Ufalme wa Mungu, Yesu Kristo alitaja sifa isiyo ya kawaida lakini yenye kuvutia.
2 Mfano huo ambao Yesu aliwaeleza wanafunzi wake faraghani mara nyingi huitwa mfano wa lulu ya thamani kubwa. Yesu alisema hivi: “Ufalme wa mbinguni ni kama mwanabiashara msafiri anayetafuta lulu nzuri. Akiisha kupata lulu moja ya thamani kubwa, alienda zake na mara moja akauza vitu vyote alivyokuwa navyo na kuinunua.” (Mathayo 13:36, 45, 46) Yesu alitaka wasikilizaji wake wajifunze nini kutokana na mfano huo? Nasi tunaweza kunufaikaje na maneno ya Yesu?
Thamani Kubwa ya Lulu
3. Kwa nini lulu nzuri zilikuwa zenye thamani sana nyakati za kale?
3 Tangu zamani, lulu zimeonwa kuwa vitu vya kujipamba vyenye thamani. Kichapo kimoja kinasema kwamba kulingana na msomi Mroma Pliny Mkubwa, lulu zilikuwa na “thamani kubwa zaidi kati ya vitu vyote vyenye thamani.” Tofauti na dhahabu, fedha, au mawe mengi yenye thamani, lulu hutokezwa na viumbe vilivyo hai. Inajulikana kwamba aina fulani za chaza wanaweza kugeuza vitu vinavyowasha mwilini kama vile vipande vidogo vya mawe kuwa lulu zenye kumetameta kwa kuvifunika kwa umajimaji unaoitwa lulumizi. Nyakati za kale, lulu bora zaidi zilipatikana hasa katika Bahari Nyekundu, Ghuba ya Uajemi, na Bahari ya Hindi, maeneo yaliyokuwa mbali na nchi ya Israeli. Bila shaka, hiyo ndiyo sababu Yesu alisema kuhusu “mwanabiashara msafiri anayetafuta lulu nzuri.” Ili kupata lulu zenye thamani ya kweli, jitihada kubwa inahitajika.
4. Ni nini lililo jambo muhimu zaidi katika mfano wa Yesu wa mwanabiashara msafiri?
4 Hata ingawa kwa muda mrefu lulu nzuri zimekuwa zenye bei, yaonekana kwamba si bei yake iliyokuwa jambo muhimu zaidi katika mfano wa Yesu. Katika mfano huo, Yesu hakufananisha tu Ufalme wa Mungu na lulu ya thamani kubwa; alielekeza fikira kwa “mwanabiashara msafiri anayetafuta lulu nzuri” na yale aliyofanya baada ya kuipata. Tofauti na mwenye duka wa kawaida, huenda mwanabiashara msafiri wa lulu, au muuzaji alikuwa mtu mwenye ujuzi katika biashara hiyo, mtu ambaye ni makini au anayeweza kutofautisha uzuri wa nje na uzuri uliojificha ambao hufanya lulu iwe ya kipekee. Angejua lulu halisi kwa kuiona tu na hangedanganywa na lulu bandia.
5, 6. (a) Tunapaswa kufikiria jambo gani hasa kuhusu mwanabiashara katika mfano wa Yesu? (b) Mfano wa hazina iliyofichwa huonyesha nini kuhusu mwanabiashara msafiri?
5 Kuna jambo lingine tunalopaswa kufikiria katika mfano huo wa mwanabiashara. Huenda mwanabiashara wa kawaida kwanza akataka kujua bei ya lulu ili aweze kuamua atainunua kwa bei gani kusudi apate faida. Huenda pia akafikiria ikiwa ataweza kuiuza haraka. Yaani, angetaka kupata faida haraka iwezekanavyo kutokana na rasilimali yake, bali si kuiweka iwe yake. Lakini mwanabiashara katika mfano wa Yesu hataki kupata faida ya haraka. Pesa au faida halisi si muhimu kwake. Kwa kweli, alikuwa tayari kuacha “vitu vyote alivyokuwa navyo”—labda vitu vyake vyote na mali zake—ili kupata kile alichokuwa akitafuta.
6 Huenda wanabiashara wengi wangeona kile ambacho yule mtu katika mfano wa Yesu alifanya kuwa jambo lisilo la hekima. Mwanabiashara mwerevu hangefikiria kufanya biashara hiyo ya kujasiria. Lakini mwanabiashara katika mfano wa Yesu alikuwa na maoni tofauti kuhusu vitu vyenye thamani. Shangwe na uradhi wake haikutokana na faida yoyote ya kifedha bali ilitokana na kumiliki kitu chenye thamani kubwa sana. Jambo hilo linafafanuliwa katika mfano mwingine unaofanana na huo ambao Yesu alitoa. Alisema: “Ufalme wa mbinguni ni kama hazina iliyofichwa katika shamba, ambayo mtu aliipata na kuificha; na kwa sababu ya shangwe aliyo nayo, anaenda na kuuza vitu alivyo navyo na kulinunua shamba hilo.” (Mathayo 13:44) Naam, shangwe inayotokana na kuvumbua na kumiliki hazina ilitosha kumchochea mtu huyo auze vitu vyote alivyokuwa navyo. Je, kuna watu kama hao leo? Je, kuna hazina inayoweza kufanya mtu auze vitu vyote alivyo navyo?
Wale Waliotambua Thamani Kubwa ya Ufalme
7. Yesu alionyeshaje kwamba alitambua thamani kubwa ya Ufalme?
7 Yesu alitoa mfano huo alipokuwa akizungumza juu ya “ufalme wa mbinguni.” Bila shaka yeye mwenyewe alitambua thamani kubwa ya Ufalme. Masimulizi ya Injili hutoa uthibitisho wenye nguvu kuhusu jambo hilo. Baada ya kubatizwa mwaka wa 29 W.K., Yesu “alianza kuhubiri na kusema: ‘Tubuni, kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.’” Kwa miaka mitatu na nusu, alifundisha umati wa watu kuhusu Ufalme. Alivuka kutoka upande mmoja wa nchi hadi mwingine na “kusafiri kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.”—Mathayo 4:17; Luka 8:1.
8. Yesu alifanya nini ili kuonyesha mambo ambayo Ufalme utatimiza?
8 Pia kwa kufanya miujiza mingi nchini kote, kutia ndani kuwaponya wagonjwa, kuwalisha wenye njaa, na kutiisha nguvu za asili, na hata kuwafufua wafu, Yesu alionyesha mambo ambayo Ufalme wa Mungu utatimiza. (Mathayo 14:14-21; Marko 4:37-39; Luka 7:11-17) Mwishowe, alithibitisha ushikamanifu wake kwa Mungu na kwa Ufalme huo kwa kutoa uhai wake na kufia imani kwenye mti wa mateso. Kama vile mwanabiashara msafiri alivyokuwa tayari kuuza kila kitu alichokuwa nacho ili kupata “lulu moja ya thamani kubwa,” Yesu aliishi na kufa kwa ajili ya Ufalme.—Yohana 18:37.
9. Wanafunzi wa Yesu wa mapema walikuwa na sifa gani isiyo ya kawaida?
9 Ingawa Yesu alikazia fikira Ufalme maishani mwake, alikusanya pia kikundi kidogo cha wafuasi. Hao pia walitambua thamani kubwa ya Ufalme. Miongoni mwao kulikuwa na Andrea ambaye hapo mwanzoni alikuwa mwanafunzi wa Yohana Mbatizaji. Baada ya kumsikia Yohana akitoa ushahidi kwamba Yesu alikuwa “Mwana-Kondoo wa Mungu,” Andrea na mwanafunzi mwingine wa Yohana, yaelekea mmoja wa wana wa Zebedayo ambaye pia aliitwa Yohana, walivutiwa mara moja kumkaribia Yesu nao wakawa waamini. Lakini mambo hayakuishia hapo. Mara moja, Andrea alienda kwa ndugu yake Simoni na kumwambia: “Tumempata Masihi.” Muda mfupi baadaye, Simoni (ambaye baadaye aliitwa Kefa, au Petro) na vilevile Filipo na rafiki yake Nathanaeli pia walimtambua Yesu kuwa Masihi. Kwa kweli, Nathanaeli alichochewa kumwambia Yesu hivi: “Wewe ndiye Mwana wa Mungu, wewe ndiye Mfalme wa Israeli.”—Yohana 1:35-49.
Wachochewa Kutenda
10. Wanafunzi waliitikiaje Yesu alipokuja na kuwaita muda fulani baada ya kukutana nao mara ya kwanza?
10 Msisimuko ambao Andrea, Petro, Yohana, na wengine walipata walipompata Masihi unaweza kulinganishwa na msisimuko wa mwanabiashara msafiri alipopata lulu ya thamani kubwa. Sasa wangefanya nini? Vitabu vya Injili havituelezi mengi kuhusu yale waliyofanya punde tu baada ya kukutana na Yesu mara ya kwanza. Yaelekea wengi wao walirudia maisha yao ya kawaida. Hata hivyo, yapata miezi sita hadi mwaka mmoja hivi baadaye, Yesu alikutana tena na Andrea, Petro, Yohana, na Yakobo ndugu ya Yohana walipokuwa kwenye biashara yao ya uvuvi kando ya Bahari ya Galilaya.a Alipowaona, Yesu alisema: “Nifuateni, nami nitawafanya ninyi kuwa wavuvi wa watu.” Waliitikiaje? Simulizi la Mathayo linasema hivi kuhusu Petro na Andrea: “Mara moja wakaziacha nyavu, wakamfuata.” Kwa habari ya Yakobo na Yohana, tunasoma hivi: “Mara moja wakaacha ile mashua na baba yao, wakamfuata.” Simulizi la Luka linaongeza kwamba ‘waliacha kila kitu, wakamfuata.’—Mathayo 4:18-22; Luka 5:1-11.
11. Ni nini ambacho huenda kilifanya wanafunzi waitikie kwa haraka mwito wa Yesu?
11 Je, wanafunzi hao walifanya uamuzi wa haraka-haraka? La, sivyo! Hata ingawa walirudia biashara ya familia yao ya uvuvi baada ya kukutana na Yesu mara ya kwanza, hakuna shaka kwamba yale waliyokuwa wameona na kusikia pindi hiyo yalibaki akilini na kugusa mioyo yao. Muda wa mwaka moja hivi ambao ulikuwa umepita, uliwapa wakati wa kutosha kutafakari mambo hayo. Sasa wakati wa kufanya uamuzi ulikuwa umefika. Je, wangekuwa kama mwanabiashara msafiri ambaye moyo wake ulichochewa sana alipopata lulu ya thamani kubwa, hivi kwamba kama Yesu alivyoeleza, “alienda zake na mara moja” akafanya kile alichopaswa kufanya ili anunue lulu hiyo? Ndiyo. Mambo waliyoona na kusikia yalichochea mioyo yao. Walitambua kwamba wakati wa kuchukua hatua ulikuwa umefika. Hivyo, kama masimulizi hayo yanavyotuambia, pasipo kusita-sita waliacha kila kitu walichokuwa nacho na kuwa wafuasi wa Yesu.
12, 13. (a) Wengi waliomsikia Yesu waliitikiaje? (b) Yesu alisema nini kuhusu wanafunzi wake waaminifu, nayo maneno yake yanamaanisha nini?
12 Wanafunzi hao waaminifu walikuwa tofauti sana na watu wengine waliotajwa baadaye katika vitabu vya Injili. Wengi walikuwa wameponywa au kulishwa na Yesu lakini waliendelea tu na shughuli zao za kawaida. (Luka 17:17, 18; Yohana 6:26) Baadhi yao hata walitoa visingizio Yesu alipowaalika wawe wafuasi wake. (Luka 9:59-62) Tofauti na hao, Yesu alisema hivi baadaye kuhusu wanafunzi wake waaminifu: “Tangu siku za Yohana Mbatizaji mpaka sasa ufalme wa mbinguni ndio mradi ambao watu wanajikaza kuufikia, na wale wanaojikaza wanaufikia.”—Mathayo 11:12.
13 Neno “Kujikaza” linamaanisha nini? Kitabu Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words kinasema hivi kuhusu kitenzi cha Kigiriki ambacho neno hilo limetolewa: “Kitenzi hicho kinadokeza jitihada yenye bidii.” Naye msomi wa Biblia Heinrich Meyer anasema hivi kuhusu mstari huo: “Neno hilo linafafanua hamu, jitihada isiyozuilika na pambano la kuufikia ufalme wa Kimasihi unaokaribia . . . Wanafuatia ufalme kwa hamu na kwa bidii sana (si kungoja kwa utulivu tu na kutarajia).” Kama yule mwanabiashara msafiri, watu hao wachache walitambua haraka kitu kilichokuwa na thamani ya kweli nao wakawa tayari kuacha vitu vyote walivyokuwa navyo kwa ajili ya Ufalme.—Mathayo 19:27, 28; Wafilipi 3:8.
Wengine Walijiunga Katika Kutafuta
14. Yesu aliwatayarishaje mitume kwa ajili ya kazi ya kuhubiri Ufalme, na matokeo yalikuwa nini?
14 Yesu alipokuwa akiendelea na huduma yake, aliwazoeza na kuwasaidia wengine waufikie Ufalme. Kwanza alichagua 12 kutoka kati ya wanafunzi wake ili wawe mitume, au wale aliowatuma. Yesu aliwapa maagizo mengi kuhusu jinsi ya kutimiza huduma yao na pia maonyo kuhusu majaribu na magumu ambayo wangekabili. (Mathayo 10:1-42; Luka 6:12-16) Kwa miaka miwili hivi iliyofuata, waliambatana na Yesu katika safari zake za kuhubiri nchini kote, nao walifurahia uhusiano wa karibu pamoja naye. Walisikia maneno yake, wakashuhudia kazi zake zenye nguvu, na kuona kielelezo chake. (Mathayo 13:16, 17) Bila shaka, mambo hayo yote yaligusa sana mioyo yao hivi kwamba kama mwanabiashara msafiri, walikuwa na bidii na walijitoa kwa moyo wote kufuatilia Ufalme.
15. Yesu alisema ni kitu gani hasa kingefanya wafuasi wake washangilie?
15 Kwa kuongezea wale mitume 12, Yesu ‘alichagua wengine 70 na kuwatuma wawili-wawili, wamtangulie kuingia katika kila jiji na mahali ambako yeye mwenyewe alikuwa aende.’ Aliwaambia pia kuhusu majaribu na magumu ambayo wangekabili na kuwaagiza wawaambie watu: “Ufalme wa Mungu umekuja karibu nanyi.” (Luka 10:1-12) Wale 70 waliporudi, walikuwa na shangwe na walimwambia Yesu hivi: “Bwana, hata roho waovu wanatiishwa kwetu kwa kutumia jina lako.” Lakini huenda walishangaa Yesu alipowaeleza kuhusu shangwe kubwa ambayo wangepata kwa sababu ya bidii yao kwa ajili ya Ufalme. Aliwaambia: “Msishangilie juu ya hili, kwamba roho wanatiishwa kwenu, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.”—Luka 10:17, 20.
16, 17. (a) Yesu aliwaambia nini mitume wake waaminifu usiku wa mwisho ambao alikuwa pamoja nao? (b) Maneno ya Yesu yaliwapa mitume shangwe na uhakika gani?
16 Mwishowe, usiku wa mwisho ambao Yesu alikuwa pamoja na mitume wake, Nisani 14, 33 W.K., alianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana na kuwaamuru waadhimishe tukio hilo. Usiku huo, Yesu aliwaambia hivi wale 11 waliobaki: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme, ili mpate kula na kunywa mezani pangu katika ufalme wangu, na kuketi juu ya viti vya ufalme kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.”—Luka 22:19, 20, 28-30.
17 Mitume hao waliposikia maneno hayo ya Yesu, mioyo yao ilijawa na furaha na uradhi kama nini! Walikuwa wakipewa pendeleo kubwa sana ambalo mwanadamu anaweza kupata. (Mathayo 7:13, 14; 1 Petro 2:9) Kama yule mwanabiashara msafiri, walikuwa wameacha vitu vingi ili kumfuata Yesu katika kufuatilia Ufalme. Sasa walihakikishiwa kwamba hawakuwa wameacha vitu hivyo bure.
18. Mbali na wale mitume 11, ni nani wengine wangenufaika na Ufalme?
18 Mbali na mitume waliokuwa pamoja na Yesu usiku huo, wengine pia wangenufaika na Ufalme. Mapenzi ya Yehova yalikuwa kwamba jumla ya watu 144,000 waingizwe katika agano la Ufalme wakiwa watawala pamoja na Yesu Kristo katika Ufalme wa mbinguni wenye utukufu. Isitoshe, mtume Yohana aliona katika maono “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, . . . wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo, . . . wakisema: ‘Wokovu unatoka kwa Mungu wetu, anayeketi juu ya kiti cha ufalme, na Mwana-Kondoo.’” Hao ndio raia wa kidunia wa Ufalme huo.b—Ufunuo 7:9, 10; 14:1, 4.
19, 20. (a) Watu wa mataifa yote wamepewa nafasi gani? (b) Ni swali gani litakalozungumziwa katika makala inayofuata?
19 Muda mfupi kabla ya Yesu kupaa mbinguni, aliwaamuru hivi wafuasi wake waaminifu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi na tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:19, 20) Hivyo, watu wa mataifa yote wangekuwa wanafunzi wa Yesu Kristo. Sawa na vile mwanabiashara msafiri alivyofanya kuhusiana na lulu nzuri, hao pia wangeelekeza mioyo yao kwenye Ufalme—iwe ni kwa ajili ya uzima mbinguni au duniani.
20 Maneno ya Yesu yalionyesha kwamba kazi ya kufanya wanafunzi ingeendelea mpaka “umalizio wa mfumo wa mambo.” Kwa hiyo, je, leo bado kuna watu ambao kama yule mwanabiashara msafiri, wako tayari kuacha vyote walivyo navyo ili kufuatilia Ufalme wa Mungu? Swali hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a Huenda Yohana, mwana wa Zebedayo alimfuata Yesu na kushuhudia baadhi ya mambo aliyofanya baada ya kukutana naye mara ya kwanza, na hivyo kumwezesha Yohana kuyaandika mambo hayo waziwazi katika masimulizi yake ya Injili. (Yohana, sura ya 2-5) Hata hivyo, alirudia biashara ya familia yao ya uvuvi kwa muda fulani kabla ya kuitwa na Yesu.
b Kwa habari zaidi, ona sura ya 10 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Kufuatilia ‘Lulu ya Thamani Kubwa’ LeoMnara wa Mlinzi—2005 | Februari 1
-
-
Kufuatilia ‘Lulu ya Thamani Kubwa’ Leo
“Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi.”—MATHAYO 24:14.
1, 2. (a) Wayahudi katika siku za Yesu walikuwa na maoni gani kuhusu Ufalme wa Mungu? (b) Yesu alifanya nini ili kuwasaidia wanafunzi waelewe vizuri zaidi kuhusu Ufalme, na matokeo yalikuwa nini?
YESU alipokuwa duniani, Wayahudi walipendezwa sana kuzungumza kuhusu Ufalme wa Mungu. (Mathayo 3:1, 2; 4:23-25; Yohana 1:49) Hata hivyo, mwanzoni wengi wao hawakuelewa kikamili mamlaka ya Ufalme huo na ukubwa wa eneo ambalo ungetawala; wala hawakuelewa kwamba ungekuwa serikali ya kimbingu. (Yohana 3:1-5) Hata watu fulani ambao walipata kuwa wafuasi wa Yesu hawakuelewa kikamili Ufalme wa Mungu ni nini au mambo waliyopaswa kufanya ili wapate kibali cha kuwa watawala pamoja na Kristo.—Mathayo 20:20-22; Luka 19:11; Matendo 1:6.
2 Kadiri wakati ulivyopita, Yesu aliwafundisha kwa subira wanafunzi wake mambo mengi kutia ndani ule mfano wa lulu ya thamani kubwa ambao tulizungumzia katika makala iliyotangulia, na kuwatajia umuhimu wa kujitahidi kufuatilia Ufalme wa mbinguni. (Mathayo 6:33; 13:45, 46; Luka 13:23, 24) Lazima mambo hayo yawe yaligusa sana mioyo yao kwa sababu punde si punde walitangaza kwa ujasiri na bila kuchoka habari njema ya Ufalme hadi sehemu za mbali za dunia kama kitabu cha Matendo kinavyothibitisha.—Matendo 1:8; Wakolosai 1:23.
3. Kwa habari ya siku zetu,Yesu alisema nini kuhusu Ufalme?
3 Basi, namna gani leo? Mamilioni ya watu wanahubiriwa kuhusu baraka za paradiso hapa duniani chini ya Ufalme. Katika unabii wake muhimu kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alisema hivi kihususa: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:3, 14; Marko 13:10) Pia alieleza kwamba kazi hiyo kubwa itafanywa licha ya vizuizi na magumu yenye kutisha, na hata mateso. Hata hivyo, alitoa uhakikisho huu: “Yule ambaye atavumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:9-13) Mambo hayo yote hutaka tujidhabihu na kujitoa kama yule mwanabiashara msafiri katika mfano wa Yesu. Je, leo kuna watu wanaoonyesha imani na bidii kama hiyo katika kufuatilia Ufalme?
Shangwe ya Kupata Ukweli
4. Kweli ya Ufalme ina matokeo gani kwa watu leo?
4 Mwanabiashara katika mfano wa Yesu alikuwa na shangwe kubwa alipopata kile alichoona kuwa ‘lulu ya thamani kubwa.’ Shangwe hiyo ilimchochea kufanya yote awezayo ili kupata lulu hiyo. (Waebrania 12:1) Vivyo hivyo leo, kweli kumhusu Mungu na Ufalme wake huwavuta na kuwachochea watu. Hilo hutukumbusha maneno ya Ndugu A. H. Macmillan aliyeandika kuhusu jinsi alivyomtafuta Mungu na kusudi Lake kwa wanadamu, katika kitabu Faith on the March. Alisema hivi: “Kile ambacho nimepata, maelfu ya watu bado wanakipata kila mwaka. Nao ni watu kama mimi na wewe, kwa sababu wametoka katika mataifa, rangi, na matabaka mbalimbali na ni wa umri mbalimbali. Kweli haibagui mtu yeyote. Huwavuta watu wa aina zote.”
5. Ni matokeo gani mazuri yanayoonekana katika ripoti ya mwaka wa utumishi wa 2004?
5 Ukweli wa maneno hayo huonekana kila mwaka mamia ya maelfu ya watu wanyoofu wanapochochewa na habari njema ya Ufalme wa Mungu na kujiweka wakfu kwa Yehova na kufanya mapenzi yake. Ndivyo ilivyokuwa mwaka wa utumishi wa 2004 ambao ulianza Septemba 2003 hadi Agosti 2004. Katika miezi hiyo 12, watu 262,416 walionyesha hadharani wakfu wao kwa kubatizwa katika maji. Jambo hilo lilitukia katika nchi 235, ambako Mashahidi wa Yehova wanaongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani 6,085,387 kila juma ili kuwasaidia watu wa matabaka, mataifa, kabila, na lugha zote wapate kweli inayotoa uhai kutoka katika Neno la Mungu.—Ufunuo 7:9.
6. Ni nini kimechangia ongezeko lenye kuendelea kila mwaka?
6 Mambo hayo yote yaliwezekanaje? Hapana shaka kwamba Yehova huwavuta watu hao wenye mwelekeo unaofaa. (Yohana 6:65; Matendo 13:48) Hata hivyo, hatupaswi kupuuza roho ya kujidhabihu na jitihada yenye bidii ya wale ambao wamejitoa kabisa kufuatilia Ufalme. Akiwa na umri wa miaka 79, Ndugu Macmillan aliandika: “Tangu nilipojifunza kwa mara ya kwanza kuhusu ahadi za Biblia kwa wanadamu wanaopatwa na ugonjwa na kifo, tumaini langu katika ujumbe wa Biblia halijafifia. Papo hapo, niliazimia kujifunza mengi kuhusu mafundisho ya Biblia ili niweze kuwasaidia wengine ambao, kama mimi, wanatafuta kumjua Mungu Mweza-Yote, Yehova, na makusudi yake mazuri kuelekea wanadamu.”
7. Ni jambo gani lililoonwa ambalo linaonyesha shangwe na bidii ya wale wanaopata kweli ya Biblia?
7 Bidii hiyo inaonekana pia miongoni mwa watumishi wa Yehova leo. Kwa mfano, fikiria Daniela, kutoka Vienna, Austria. Alisema: “Tangu utoto wangu, Mungu amekuwa rafiki yangu mkubwa zaidi. Sikuzote nilitaka kujua jina lake kwa sababu neno ‘Mungu’ halikuwa na utu hata kidogo. Lakini ilinibidi kungoja hadi nilipofika umri wa miaka 17, wakati Mashahidi wa Yehova waliponitembelea. Walinieleza yote niliyotaka kujua kumhusu Mungu. Mwishowe, nilipata kweli, nayo ilikuwa nzuri sana! Nilisisimuka sana hivi kwamba nilianza kuhubiria kila mtu.” Punde si punde, shauku yake ilifanya wanafunzi wenzake wamdhihaki. Daniela aliendelea kusema, “Hata hivyo, mimi niliona jambo hilo kuwa utimizo wa unabii wa Biblia kwa sababu nilikuwa nimejifunza kwamba Yesu alisema wafuasi wake wangechukiwa na kuteswa kwa ajili ya jina lake. Nilifurahi sana na kushangaa.” Punde si punde, Daniela alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa na akaanza kufuatilia mradi wa kuwa mmishonari. Baada ya kuolewa, Daniela pamoja na mume wake, Helmut, walianza kuwahubiria Waafrika, Wachina, Wafilipino, na Wahindi walioishi Vienna. Sasa Daniela na Helmut wanatumika wakiwa wamishonari kusini-magharibi mwa Afrika.
Hawafi Moyo
8. Wengi wameonyesha upendo wao kwa Mungu na ushikamanifu wao kwa Ufalme wake katika njia gani yenye kuthawabisha?
8 Kwa kweli, utumishi wa umishonari ni mojawapo ya njia ambazo watu wa Yehova leo huonyesha upendo wao kwa Mungu na ushikamanifu wao kwa Ufalme wake. Kama mwanabiashara katika mfano wa Yesu, wale wanaofanya utumishi huo huwa tayari kusafiri hadi sehemu za mbali sana kwa ajili ya Ufalme. Bila shaka, wamishonari hao hawasafiri ili kwenda kutafuta habari njema ya Ufalme; wanapeleka habari hiyo kwa watu wanaoishi sehemu za mbali sana za dunia, wakiwafundisha na kuwasaidia wawe wanafunzi wa Yesu Kristo. (Mathayo 28:19, 20) Katika nchi nyingi, inawabidi kuvumilia magumu yasiyo ya kawaida. Lakini wanathawabishwa sana kwa sababu ya kuvumilia.
9, 10. Ni mambo gani yenye kusisimua ambayo wamishonari wamejionea katika sehemu za mbali, kama vile Jamhuri ya Afrika ya Kati?
9 Kwa mfano, fikiria Jamhuri ya Afrika ya Kati, ambako mwaka jana, watu 16,184, walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Idadi hiyo ilikuwa karibu mara saba ya idadi ya wahubiri wa Ufalme katika nchi hiyo. Kwa kuwa sehemu nyingi za nchi hiyo hazina umeme, kwa kawaida watu hufanya kazi zao za kawaida nje, chini ya kivuli cha mti. Kwa hiyo ni jambo la kawaida kwa wamishonari kufanya kazi yao kwa njia hiyo, yaani, kuongoza mafunzo ya Biblia chini ya kivuli cha mti. Si kwamba tu nje kuna baridi na mwangaza bali pia kuna faida nyingine. Watu wanapenda sana Biblia, na ni jambo la kawaida kuzungumzia mambo ya dini kama vile ilivyo kawaida kuzungumzia habari za michezo au hali ya hewa katika sehemu nyingine za ulimwengu. Mara nyingi, wapita-njia hutazama kinachoendelea na kujiunga na funzo.
10 Hivyo, wakati mmishonari mmoja alipokuwa akiongoza funzo la Biblia nje, kijana mmoja mwanamume aliyeishi ng’ambo ya barabara alikuja na kusema kwamba kwa kuwa hakuwa ametembelewa na Shahidi yeyote, mmishonari huyo alipaswa kwenda kwake na kujifunza Biblia pamoja naye. Bila shaka, mmishonari huyo alikubali kwa furaha, na kijana huyo anafanya maendeleo haraka. Katika nchi hiyo, mara nyingi polisi huwasimamisha Mashahidi barabarani, si ili kuwapa notisi ya kufika mahakamani au kuwatoza faini, bali ili kuomba matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! au ili kuwashukuru kwa makala fulani waliyofurahia kusoma.
11. Licha ya majaribu, wamishonari ambao wametumika kwa muda mrefu huonaje utumishi wao?
11 Wengi ambao walianza utumishi wa umishonari miaka 40 au 50 iliyopita bado wanatumikia kwa uaminifu. Imani na uvumilivu wao ni kielelezo kizuri kama nini kwetu! Kwa miaka 42 iliyopita, wenzi fulani wa ndoa wametumikia wakiwa wamishonari katika nchi tatu. Mume huyo anasema: “Kumekuwa na magumu. Kwa mfano, tumepambana na malaria kwa miaka 35. Hata hivyo, hatukujuta kamwe uamuzi wetu wa kuwa wamishonari.” Mke wake anaongezea hivi: “Sikuzote tumekuwa na sababu nyingi za kuwa wenye shukrani. Huduma ya shambani inaleta shangwe sana, na ni rahisi kuanzisha mafunzo ya Biblia. Kila mara unapowaona wanafunzi wakija kwenye mikutano na kufahamiana, ni kama kikusanyiko cha familia.”
‘Wanaviona Vitu Vyote Kuwa Hasara’
12. Mtu huonyeshaje kwamba anatambua kikweli thamani ya Ufalme?
12 Mwanabiashara msafiri alipopata lulu ya thamani kubwa, “alienda zake na mara moja akauza vitu vyote alivyokuwa navyo na kuinunua.” (Mathayo 13:46) Kuwa tayari kuacha vitu vinavyoonekana kuwa vyenye thamani ni sifa moja ya wale wanaotambua kikweli thamani ya Ufalme. Akiwa mmoja wa wale ambao wangeshiriki na Kristo katika utukufu wa Ufalme, mtume Paulo alisema: “Kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa sababu yake nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kumpata Kristo.”—Wafilipi 3:8.
13. Mtu mmoja katika Jamhuri ya Cheki alionyeshaje kwamba anaupenda Ufalme?
13 Kwa njia hiyohiyo, wengi leo wako tayari kufanya mabadiliko makubwa maishani mwao ili kupata baraka za Ufalme. Kwa mfano, Oktoba 2003, mwalimu-mkuu mwenye umri wa miaka 60 wa shule moja katika Jamhuri ya Cheki alipata kitabu cha kujifunzia Biblia Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Baada ya kukisoma, aliwasiliana mara moja na Mashahidi wa Yehova katika eneo lake ili apate funzo la Biblia. Alifanya maendeleo mazuri ya kiroho na punde si punde akaanza kuhudhuria mikutano yote. Hata hivyo, namna gani mipango yake ya kugombea kiti cha meya na baadaye cha seneta? Aliamua kufuatilia mradi tofauti, yaani, kuwa mtangazaji wa Ufalme. Alisema, “niliwapa wanafunzi wangu shuleni vichapo vingi vya Biblia.” Alionyesha wakfu wake kwa Yehova alipobatizwa katika kusanyiko moja mnamo Julai 2004.
14. (a) Habari njema ya Ufalme imewachochea mamilioni kufanya nini? (b) Kila mmoja wetu anaweza kujiuliza maswali gani yenye kuamsha fikira?
14 Katika njia hiyohiyo, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wameitikia habari njema ya Ufalme. Wametoka katika ulimwengu mwovu, wakavua utu wao wa zamani, wakaacha marafiki wao wa zamani, na kuacha kufuatilia mambo ya ulimwengu. (Yohana 15:19; Waefeso 4:22-24; Yakobo 4:4; 1 Yohana 2:15-17) Kwa nini wanafanya mambo hayo yote? Kwa sababu wanaona baraka za Ufalme wa Mungu kuwa muhimu zaidi kuliko kitu chochote ambacho mfumo huu unaweza kuwapa. Je, wewe unahisi vivyo hivyo kuhusu habari njema ya Ufalme? Je, inakuchochea kufanya mabadiliko yanayohitajiwa ili kupatanisha maisha yako, viwango, na miradi yako na matakwa ya Yehova? Ukifanya hivyo, utapata baraka nyingi sasa na wakati ujao.
Mavuno Yanafikia Upeo
15. Ilitabiriwa kwamba watu wa Mungu wangefanya nini katika siku za mwisho?
15 Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Watu wako watajitoa kwa hiari katika siku ya jeshi lako.” Wale ambao wamejitoa kwa hiari wanatia ndani ‘kundi la vijana kama matone ya umande’ na “jeshi kubwa” la “wanawake wanaotangaza habari njema.” (Zaburi 68:11; 110:3) Katika siku hizi za mwisho, kujidhabihu na jitihada za watu wa Yehova—wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee—zimekuwa na matokeo gani?
16. Toa mfano kuonyesha jinsi watumishi wa Yehova wanavyojitahidi kuwasaidia wengine wajifunze kuhusu Ufalme.
16 Dada mmoja painia au mtangazaji wa Ufalme wa wakati wote nchini India alijiuliza jinsi ambavyo watu zaidi ya milioni mbili viziwi katika nchi hiyo wangeweza kusaidiwa kujifunza kuhusu Ufalme. (Isaya 35:5) Aliamua kujiunga na chuo cha kujifunza lugha ya ishara huko Bangalore. Akiwa huko, aliwaeleza viziwi wengi kuhusu tumaini la Ufalme na vikundi vya kujifunza Biblia vikaanzishwa. Katika muda wa majuma machache, zaidi ya watu 12 walianza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Baadaye, akiwa kwenye sherehe ya arusi, painia huyo alikutana na mwanamume mmoja kijana ambaye ni kiziwi kutoka Calcutta aliyekuwa na maswali mengi na aliyetaka sana kujua mengi kumhusu Yehova. Hata hivyo, kulikuwa na tatizo. Mwanamume huyo kijana alipaswa kurudi Calcutta, umbali wa kilometa 1,600 hivi ili aende chuoni, na huko hakukuwa na Mashahidi waliojua lugha ya ishara. Alijitahidi sana kumshawishi baba yake amruhusu kwenda shule huko Bangalore ili aweze kuendelea kujifunza Biblia. Alifanya maendeleo mazuri ya kiroho, na baada ya mwaka mmoja hivi, alijiweka wakfu kwa Yehova. Yeye pia alijifunza Biblia pamoja na viziwi wengi, kutia ndani rafiki yake mmoja wa tangu utotoni. Sasa ofisi ya tawi nchini India inafanya mipango mapainia wajifunze lugha ya ishara ili waweze kusaidia katika eneo hilo.
17. Simulia mambo unayoona kuwa hasa yenye kutia moyo katika ripoti ya mwaka wa utumishi wa 2004 kwenye ukurasa wa 19 hadi 22.
17 Utapata ripoti ya utendaji ya Mashahidi wa Yehova ya ulimwenguni pote ya mwaka wa utumishi wa 2004 kwenye ukurasa wa 19 hadi 22 wa gazeti hili. Tumia wakati kuichunguza, na ujionee mwenyewe uthibitisho wa kwamba watu wa Yehova ulimwenguni pote wanakazia fikira kufuatilia ‘lulu ya thamani kubwa’ leo.
Endeleeni “Kuutafuta Kwanza Ufalme”
18. Ni habari gani ambayo Yesu hakutaja katika ule mfano wa mwanabiashara msafiri, na kwa nini?
18 Tukirudia mfano wa Yesu wa mwanabiashara msafiri, tunaona kwamba Yesu hakueleza jinsi mwanabiashara huyo angetosheleza mahitaji yake baada ya kuuza vitu vyote alivyokuwa navyo. Kwa kufaa, huenda wengine wakauliza: ‘Mwanabiashara huyo angepataje chakula, nguo, na makao kwa kuwa sasa hakuwa na akiba yoyote? Lulu hiyo ya thamani ingekuwa na faida gani kwake?’ Kwa maoni ya kimwili, maswali hayo yangeonekana kuwa yanafaa. Lakini je, Yesu hakuwahimiza wanafunzi wake hivi: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote”? (Mathayo 6:31-33) Jambo kuu katika mfano huo ni uhitaji wa kujitoa kwa moyo wote kwa Mungu na kuwa na bidii kwa ajili ya Ufalme. Je, tunaweza kujifunza jambo fulani kutokana na hilo?
19. Tunajifunza jambo gani muhimu kutokana na mfano wa Yesu wa lulu ya thamani kubwa?
19 Iwe tumejifunza kuhusu habari njema hivi karibuni au tumekuwa tukifuatilia Ufalme na kuwaeleza wengine kuhusu baraka zake kwa miaka mingi, lazima tuendelee kupendezwa na kukazia fikira Ufalme. Hizi ni nyakati ngumu, lakini tuna sababu nzuri za kuamini kwamba kile tunachofuatilia ni halisi na hakiwezi kulinganishwa na kitu chochote—kama lulu ambayo mwanabiashara alipata. Matukio ya ulimwengu na unabii wa Biblia ambao umetimizwa unatoa uthibitisho wenye kusadikisha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3) Kama mwanabiashara msafiri, acheni tuwe na bidii ya kutoka moyoni kwa ajili ya Ufalme wa Mungu na kufurahia pendeleo la kutangaza habari njema.—Zaburi 9:1, 2.
-