Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Biblia Inasema Nini Kuhusu Useja na Ndoa?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
    • Biblia Inasema Nini Kuhusu Useja na Ndoa?

      Katika tamaduni fulani, inaaminiwa kwamba mtu hawezi kuwa na furaha ikiwa hajafunga ndoa. Hata hivyo, si watu wote waliofunga ndoa walio na furaha na si waseja wote wasio na furaha. Biblia inasema kwamba useja na ndoa ni zawadi kutoka kwa Yehova.

      1. Kuna manufaa gani ya kuwa mseja?

      Biblia inasema hivi: “Yeyote anayefunga ndoa anafanya vema, lakini yeyote asiyefunga ndoa atafanya vema zaidi.” (Soma 1 Wakorintho 7:32, 33, 38.) Ni katika njia gani mseja anaweza ‘kufanya vema zaidi’? Wakristo waseja hawana jukumu la kumtunza mwenzi wa ndoa. Kwa hiyo, wana uhuru mwingi. Kwa mfano, baadhi yao wanaweza kupanua huduma yao kwa kuhamia katika nchi nyingine ili kuhubiri habari njema. Jambo muhimu zaidi, wanaweza kutumia muda mwingi zaidi kumkaribia Yehova.

      2. Kuna manufaa gani ya kufunga ndoa kisheria?

      Kama ilivyo na useja, ndoa ina manufaa ya kipekee. Biblia inasema kwamba “wawili ni afadhali kuliko mmoja.” (Mhubiri 4:9) Hilo ni kweli hasa kwa Wakristo wanaofuata kanuni za Biblia katika ndoa yao. Wakristo wanaofunga ndoa kisheria wanaahidi kwamba watapendana, wataheshimiana, na kutunzana. Kwa hiyo, wanajihisi wakiwa salama zaidi tofauti na mwanamume na mwanamke wanaoishi pamoja bila kufunga ndoa. Na ndoa inaandaa mazingira salama ya kulea watoto.

      3. Yehova ana maoni gani kuhusu ndoa?

      Yehova alipoanzisha ndoa ya kwanza alisema hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.” (Mwanzo 2:24) Yehova anataka mume na mke wapendane na waishi pamoja maisha yao yote. Anaruhusu talaka ikiwa mwenzi mmoja wa ndoa anafanya uzinzi. Katika hali kama hiyo, Yehova anamruhusu mwenzi asiye na hatia aamue ikiwa atatafuta talaka.a (Mathayo 19:9) Yehova anakataza Wakristo kuwa na ndoa za wake wengi.​—1 Timotheo 3:2.

      CHIMBA ZAIDI

      Jifunze jinsi unavyoweza kuwa na furaha na kumfurahisha Yehova, iwe wewe ni mseja au umefunga ndoa.

      4. Tumia vizuri zawadi ya useja

      Yesu aliona useja kuwa zawadi. (Mathayo 19:11, 12) Soma Mathayo 4:23, kisha mzungumzie swali hili:

      • Yesu alitumiaje zawadi ya useja kumtumikia Baba yake na kuwasaidia wengine?

      Kama Yesu, Wakristo wanaweza kufurahia zawadi ya useja. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

      VIDEO: Waseja Waaminifu (3:15)

      • Wakristo wanawezaje kutumia zawadi ya useja kwa njia yenye kuthawabisha?

      Je, wajua?

      Biblia haitaji umri wa kufunga ndoa. Hata hivyo, inawatia moyo vijana wasubiri hadi ‘wapite upeo wa ujana,’ kipindi ambacho hisia zenye nguvu za ngono zinaweza kufanya iwe vigumu kwa kijana kufanya uamuzi kwa hekima.​—1 Wakorintho 7:36.

      5. Chagua mwenzi wa ndoa kwa hekima

      Kuchagua mwenzi wa ndoa ni mojawapo ya uamuzi muhimu zaidi ambao utafanya. Soma Mathayo 19:4-6, 9, kisha mzungumzie swali hili:

      • Kwa nini Mkristo anapaswa kufikiria kwa makini kabla ya kufanya uamuzi wa kufunga ndoa?

      Biblia inaweza kukusaidia kutambua sifa za mwenzi wa ndoa anayekufaa. Jambo muhimu zaidi, chagua mwenzi wa ndoa ambaye anampenda Yehova.b Soma 1 Wakorintho 7:39 na 2 Wakorintho 6:14. Kisha mzungumzie maswali haya:

      • Kwa nini Mkristo anapaswa kufunga ndoa tu na Mkristo mwenzake?

      • Unafikiri Yehova atahisije tukiamua kufunga ndoa na mtu ambaye hampendi Yehova?

      Ng’ombe dume mwenye nguvu na punda mdogo waking’ang’ana wakiwa wamefungwa nira ya mbao.

      Wanyama wawili walio tofauti sana wakifungwa nira pamoja, wataumia. Vivyo hivyo, Mkristo anayefunga ndoa na mwenzi ambaye si mwamini atapatwa na matatizo mengi

      6. Sitawisha maoni ya Yehova kuhusu ndoa

      Katika Israeli la kale, baadhi ya wanaume waliwapa talaka wake zao kwa sababu ya ubinafsi. Soma Malaki 2:13, 14, 16, kisha mzungumzie swali hili:

      • Kwa nini Yehova anachukia watu wanapotalikiana kwa sababu zisizo na msingi wa Maandiko?

      Mama aliyevunjika moyo anamtazama mume wake akihama nyumbani. Binti yao aliyehuzunika anamkumbatia mama yake.

      Uzinzi na talaka husababisha maumivu mengi kwa mwenzi asiye na hatia na pia kwa watoto

      Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

      VIDEO: Ndoa​—Kifungo cha Kudumu (4:31)

      • Ikiwa umefunga ndoa na mtu ambaye si mwamini, unaweza kufanya nini ili kuwa na ndoa yenye furaha?

      7. Fuata viwango vya Yehova kuhusu ndoa

      Huenda mtu akahitaji kufanya jitihada nyingi ili kufuata viwango vya Yehova kuhusu ndoa.c Lakini Yehova anawabariki wale wanaofanya hivyo. Onyesha VIDEO.

      VIDEO: Unaweza Kufuata Viwango vya Yehova Kuhusu Ndoa (4:14)

      Soma Waebrania 13:4, kisha mzungumzie maswali haya:

      • Je, unafikiri viwango vya Yehova kuhusu ndoa vinafaa? Kwa nini?

      Yehova anatarajia Wakristo waandikishe kisheria ndoa na talaka zao kwa sababu katika nchi nyingi, hiyo ni sheria iliyowekwa na serikali. Soma Tito 3:1, kisha mzungumzie swali hili:

      • Ikiwa umefunga ndoa, je, umehakikisha kwamba ndoa yenu inatambuliwa kisheria serikalini?

      HUENDA MTU AKAULIZA: “Kwa nini ufunge ndoa? Mwanamume na mwanamke wanaweza kuishi pamoja bila kufunga ndoa.”

      • Wewe una maoni gani?

      MUHTASARI

      Useja na ndoa ni zawadi kutoka kwa Yehova. Waseja na watu waliofunga ndoa wanaweza kuwa na furaha na kuridhika maishani ikiwa wataishi kulingana na viwango vya Yehova.

      Ungejibuje?

      • Mtu anawezaje kutumia vizuri useja wake?

      • Kwa nini Biblia inasema kwamba Mkristo anapaswa kufunga ndoa tu na Mkristo mwenzake?

      • Ni nini msingi pekee wa Kimaandiko kuhusu talaka?

      Lengo

      CHUNGUZA ZAIDI

      Kuoa au kuolewa “katika Bwana tu” kunamaanisha nini?

      “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” (Mnara wa Mlinzi, Julai 1, 2004)

      Ona video mbili fupi zinazoweza kukusaidia kufanya maamuzi mazuri kuhusu uchumba na ndoa.

      Kujitayarisha kwa Ajili ya Ndoa (11:53)

      Jifunze kwa nini ndugu mmoja anahisi kwamba jambo ambalo Yehova amempa ni lenye thamani kuliko vitu vyote alivyoacha.

      Nilitarajia Mchumba Wangu Angejifunza Ukweli (1:56)

      Ni baadhi ya mambo gani ambayo mtu anapaswa kufikiria kabla ya kuamua kutengana au kutafuta talaka?

      “Heshimu ‘Kile Ambacho Mungu Ameunganisha’” (Mnara wa Mlinzi, Desemba 2018)

      a Ona Maelezo ya Ziada 4 kuhusu kutengana ikiwa hakuna hatia ya uzinzi.

      b Katika tamaduni fulani, wazazi huamua mtu atakayefunga ndoa na mwana au binti yao. Katika visa kama hivyo, wazazi wenye upendo huchunguza kwanza ikiwa mtu huyo anampenda Yehova, bali si uwezo wake wa kifedha, au jinsi watu wanavyomwona katika jamii.

      c Ikiwa unaishi na mtu ambaye hujafunga naye ndoa, unaweza kuamua kumwacha au kufunga naye ndoa, huo ni uamuzi wako.

  • Jinsi Familia Yako Inavyoweza Kuwa na Furaha—Sehemu ya 1
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
    • 3. Mume na mke wanawezaje kuimarisha ndoa yao?

      Biblia inasema hivi kuhusu watu waliofunga ndoa: “Hao wawili watakuwa mwili mmoja.” (Mathayo 19:5) Hilo linamaanisha kwamba wanapaswa kujitahidi sana kuepuka jambo lolote linaloweza kudhoofisha upendo kati yao. Wanafanya hivyo kwa kutumia muda mwingi pamoja, na pia kuzungumza waziwazi na kwa upendo kuhusu mawazo na hisia zao. Hawaruhusu mtu au kitu kingine chochote kuwa muhimu kuliko mwenzi wao wa ndoa, isipokuwa Yehova. Wanakuwa waangalifu sana ili wasisitawishe uhusiano usiofaa na mtu mwingine yeyote.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki