Je! Wakumbuka?
Je! wewe umefurahia kusoma matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ikiwa ndivyo, bila shaka utaliona kuwa jambo lenye kupendeza kukumbuka yafuatayo:
▫ Ni uthibitisho gani wenye kusadikisha uliotolewa na utendaji mbalimbali wa roho takatifu katika karne ya kwanza?
Utendaji huo mbalimbali uliandaa uthibitisho wenye kuonekana kwamba Mungu hakuwa tena akitumia lile kundi la Israeli lenye umri wa miaka 1,500 kuwa watu wake wa pekee, lakini kibali chake kilikuwa juu ya lile kundi jipya la Kikristo, lililoanzishwa na Mwana wake mzaliwa wa pekee. (Linganisha Waebrania 2:2-4.)—8/15, ukurasa 5.
▫ Ni nini kinachosababisha ule ukuzi wa ajabu unaoonwa na Mashahidi wa Yehova?
Hasa ni kwa sababu ya baraka ya Mungu. Ni kazi ya Mungu. Yale ambayo Mashahidi wa Yehova hufundisha katika kazi yao ya kueneza evanjeli yanategemea Biblia. Ufunguo mwingine wa mafanikio yao ni kutambua kwao kikamili Kristo Yesu akiwa ndiye Kichwa kilichowekwa rasmi cha kundi la Kikristo.—9/1, ukurasa 19.
▫ Kwa nini Yehova alimwonyesha Daudi rehema kuhusiana na dhambi yake kubwa pamoja na Bath-sheba?
Ilikuwa kwa sababu ya lile agano la Ufalme hasa ambalo Mungu alikuwa amefanya na Daudi, lakini ilikuwa pia kwa sababu ya rehema ya Daudi mwenyewe na toba yake ya kweli. (1 Samweli 24:4-7; 2 Samweli 7:12; 12:13; Zaburi 51:1, 2, 17)—9/15, kurasa 10, 11.
▫ Ni uthibitisho wa aina gani tatu unaotolewa na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ili kutegemeza Umesiya wa Yesu?
Nasaba ya Yesu ni uthibitisho wa kwanza. (Mathayo 1:1-16; Luka 3:23-38) Uthibitisho mwingine ni unabii uliotimizwa. Kuna unabii mwingi sana kihalisi, kama vile ule unaopatikana kwenye Danieli 9:25, unaomtambulisha Yesu kuwa ndiye Mesiya. Uthibitisho wa tatu ni ushuhuda wa Mungu mwenyewe; aliuandaa katika pindi tatu kwa sauti yake mwenyewe. (Mathayo 17:5; Luka 3:21, 22; Yohana 12:28)—10/1, ukurasa 10, 12.
▫ Yesu alimaanisha nini aliposema, kama ilivyorekodiwa kwenye Mathayo 24:37, NW: “Kama vile siku za Nao zilivyokuwa, ndivyo kuwako kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa”?
Nao alikuwa akijenga safina na alikuwa akiwaonya waovu kwa kipindi cha miongo kadhaa kabla ya Furiko kuwasili na kufutilia mbali ule mfumo wa ulimwengu mfisadi. Vilevile, kuwapo kwa Kristo kusikoonekana kunachukua kipindi cha miongo kadhaa, ambamo ushahidi wa duniani pote unatolewa, kabla ya kuwako huko pia kufikie upeo katika uharibifu mkubwa.—10/1, ukurasa 16.
▫ Ni nini baadhi ya mambo muhimu ili kuwe na Funzo la Biblia la familia zuri?
Ni lazima wakati ununuliwe kwa ajili ya funzo hilo. Hatupaswi kuruhusu TV au vikengeusho vingine vichukue mahali palo. Ni lazima mahitaji mahususi ya familia yafikiriwe. Tumia maulizo ya maoni ili kuhakikisha watoto wanaelewa yale wanayojifunza. (Mathayo 17:25) Dumisha hali ikiwa yenye ustarehe. Uwe mchangamfu, na uhusishe kila mtu katika funzo.—10/15, ukurasa 17.
▫ Wakristo wanapaswa wahangaike kadiri gani kwamba sehemu za damu huenda zikawa zimeongezwa katika vyakula?
Wakristo wanapaswa wajihadhari wasisumbuliwe na uwezekano tu au uvumi, na kusababu kuzuri kunahitajiwa hata kwa habari ya kuchunguza vibandiko au kuhoji-hoji wachinja nyama. Hata hivyo, kama inajulikana kwamba damu inatumiwa sana mahali fulani—iwe ni katika chakula au katika matibabu—Wakristo wanapaswa wawe waangalifu kutii amri ya Mungu ya kuepukana na damu. (Matendo 15:28, 29) —10/15, kurasa 30-1.
▫ Kitabu cha Mithali kinakaziaje kina cha kiroho cha njia za kufundisha zilizotumiwa katika Israeli?
Kitabu cha Mithali kinaonyesha kwamba kusudi lacho lilikuwa kuwafundisha “wajinga” mambo bora kama vile hekima, nidhamu, uelewevu, mwono-ndani, hukumu, werevu, maarifa, na uwezo wa kufikiri—yote hayo katika “kumcha BWANA [Yehova, NW].” (Mithali 1:1-7; 2:1-14)—11/1, ukurasa 12.
▫ Vijana leo wanapaswa wawe na maoni gani yenye usawaziko juu ya elimu?
Wakristo wanapaswa waone elimu kuwa njia ya kutimiza kusudi fulani. Kusudi lao katika siku hizi za mwisho ni kumtumikia Yehova kwa kadiri kubwa na kwa mafanikio zaidi iwezekanavyo katika huduma ya wakati wote ikiwa wanaweza.—11/1, ukurasa 18.
▫ Kwa nini Yehova alitaka taifa la Israeli lilipe sehemu za kumi?
Kwanza, ili waweze kuonyesha kwa njia yenye kuonekana uthamini wao kwa ajili ya wema wa Yehova. Pili, ili waweze kuchangia utegemezo wa Walawi, ambao wangeweza sasa kukaza fikira kwenye wajibu wao mbalimbali, kutia ndani kufundisha Sheria. (Ona 2 Mambo ya Nyakati 17:7-9.)—12/1, ukurasa 9.
▫ Ni nini sehemu ya kumi ambayo Wakristo wanaalikwa walete? (Malaki 3:10)
Sehemu ya kumi inawakilisha sehemu ya vitu vyetu tunayomletea Yehova au kutumia katika utumishi wake. Huo ni wonyesho wa upendo wetu kwake na utambuzi wetu wa kwamba sisi ni mali yake.—12/1, ukurasa 15.