Maoni ya Biblia
Je! Kweli Kuna Ibilisi?
WEWE ulipokuwa mtoto, je! uliogopa giza? Labda uliwazia dubwana lenye kuotea nje ya dirisha lenu, likingoja kukunyakua kutoka kwa wazazi wako. Sasa ukiwa mtu mzima, awezaye kusoma habari za uhakika na kufikiri kiakili zaidi, hofu za utoto wako zaonekana za upuuzi. “Hivyo basi,” husema wachambuzi fulani, “kwa nini usichukue hatua moja zaidi na kumpanga Ibilisi katika hali iyo hiyo—kwamba yeye ni kama tu dubwana la kuwaziwa na mtoto?”
Je! hakuna Ibilisi halisi? Hivyo hasa ndivyo kigazeti kimoja cha kidini chakuhakikishia: “Biblia haijui lolote juu ya dubwana kama hilo la uovu” na, “Katika mitajo Ibilisi na Shetani tuna ile . . . kanuni ya dhambi na uovu ambayo imerithiwa katika asili ya kibinadamu.” Au kama vile mwalimu mmoja wa shule ya Jumapili katika United States alivyoweka wazo hilo: “Wanadamu ndio maibilisi wa pekee.” Je! jambo lote hilo laonekana kusahilishwa sana—labda kusahilishwa mno?
Kueleza Tabia ya Kibinadamu
Ikiwa sisi wanadamu ndio maibilisi wa pekee, basi mbona karibu sisi sote huonyesha hangaiko kwa halinjema ya familia yetu? Kwa kielelezo, watu walio wengi wakiwa mmoja mmoja huandalia familia zao chakula; hawajitilii sumu kwa kujua, nao huepuka hatari zenye kuhatarisha uhai. Hilo si jambo la kiibilisi kamwe! Hata hivyo, watu ao hao watendapo kijumuiya wakiwa mataifa mazima, kitu fulani hufunga mwono wao juu ya halinjema yao ya ujumla.
Wakiwa mataifa mazima, wao huacha chakula cha ziada kioze badala ya kulisha idadi za watu wao wenye njaa. Wao huchafuza mazingira ya dunia. Wao hurundika silaha za kuangamizana kabisa—vita ya nyukilia. Ni ajabu kwamba wana tabia ya kujiharibu wenyewe!Ni uvutano gani uletao upofu huu wa kutoona mambo vizuri katika mwenendo wa kibinadamu? Je! ni akili ya kufuata maoni ya umati? Je! ni kuongozwa na viongozi wachache wasiotumia fikira nzuri? Hakika mengi zaidi yahusika. Biblia pekee ndiyo hutambulisha mtu fulani ambaye ‘amepofusha akili’ za “mfumo wa mambo” usioamini wa ulimwenguni pote. Nani? “Mmoja ambaye huitwa Ibilisi na Shetani, ambaye anaongoza vibaya dunia nzima yote inayokaliwa.” Yeye hufanikiwa sana kuwatumia wanadamu waliopangwa kitengenezo kwa njia atakayo hivi kwamba Biblia yamwita “mungu” wa mfumo wa ulimwengu huu.—2 Wakorintho 4:4; Ufunuo 12:9, NW.
“Mungu” huyu si zimwi linalojificha nje ya dirisha lako. Bali ni mjuzi hodari sana kwa kupanga mambo kisiasa, kiumbe roho asiyeonekana, ambaye, katika jaribio lisilofanikiwa la kuvunja utiifu wa Yesu, aliweza kumtolea Yesu kila ufalme wa ulimwengu. (Luka 4:6, 7) Yaonekana kwamba Shetani alikuwa amewapa wengine mamlaka hiyo kabla hajamtolea Yesu, kwa maana kitabu cha Biblia cha Danieli hufunua kwamba malaika waasi, wakiwa manaibu, walikuwa wamekubali mamlaka juu ya milki za ulimwengu—wakiwa na vyeo rasmi kama “mkuu wa Uajemi,” na “mkuu wa Uyunani.”—Danieli 10:20, 21.
Hivyo, Shetani amejenga tengenezo kubwa sana—akiwa “mtawala wa ulimwengu [uonekanao]” na pia “mtawala wa roho waovu [wasioonekana].” (Yohana 14:30; 16:11; Mathayo 12:24, NW) Muono-ndani huu, kwamba Ibilisi huongoza tengenezo la ulimwenguni pote, wafafanua mengi.
Sababu Yeye Huongoza Tengenezo
Kama vile mkubwa wa uhalifu uliopangwa kitengenezo aweza kuwa na uangalizi juu ya shughuli nyingi zisizo halali—dawa za kulevya, umalaya, wizi, kucheza kamari, ulanguzi, na kadhalika—bila yeye binafsi kujifunua kwa watu wake wenye vyeo vidogo, ndivyo Shetani hutumia tengenezo kudhibiti watu wengi kuliko wale ambao angeweza kuwadhibiti akiwa peke yake. Mbinu yake ni nini? Zaidi ya kusumbua watu mmoja mmoja, yeye na roho wake waovu hutendea matungamo ya watu kana kwamba wao ni kundi la ng’ombe. Hakuna uhitaji wa kuelekeza kila mmoja kibinafsi. Geuza wachache tu walio mbele ya kundi hilo, na walio wengi watafuata. Halafu kaza fikira juu ya wale walioacha njia.
Ndiyo, Ibilisi ni halisi sana, lakini utambulisho wake wa kweli haufanani na miigizo ambayo sisi huona katika michoro ya ucheshi wala haufanani na nadharia zisizo dhahiri za wanatheolojia. Zisizo dhahiri? Ndiyo, kama vile kitabu Satan, A Portrait kisemavyo: “Imani katika Shetani ikawa isiyo dhahiri sana” katika karne ya 19, na wanatheolojia “walijitahidi kueleza Shetani kuwa ni kitu tofauti na roho aliyeko aliye mtu.”
Nani Anasema Ukweli Juu ya Ibilisi?
Utayari wa dini za ki-siku-hizi kuwa na tashwishi juu ya isemayo Biblia kuhusu Ibilisi ni kwa kusudi la kuifaa jamii iaminiyo vitu vionekanavyo tu ambayo imekuwa haina uhakika wa Mungu mwenyewe yuko. “Leo,” asema Ruth Ansher katika kitabu chake The Reality of the Devil, “Ibilisi ametoweka na . . . Mungu mwenyewe amejitenga akaenda ng’ambo ya mbali kabisa.”
Kwa kuwa na tashwishi juu ya maoni ya Biblia, “wastadi” wa kidini wa ki-siku-hizi wamekosa kuujali uhakika mmoja ufanyao historia iwe kama ilivyo. Kama vile mwandika tamthilia Mromania Eugène Ionesco alivyokiri kwa gazeti moja la Kijeremani: “Historia ingekuwa isiyoweza kueleweka kama sisi tungeliondoa nje lile wazo la roho ovu.”—Welt am Sonntag, Septemba 2, 1979.
Je! mtu yeyote ana moyo mkuu wa kuutegemeza ukweli juu ya sehemu ya Ibilisi katika hali mbaya ya leo ulimwenguni? Ndiyo, ni wazi! Fikiria lile “Julisho Rasmi Dhidi ya Shetani na kwa Ajili ya Yehova” lililopitishwa kwa kauli moja kwenye mkusanyiko mmoja katika 1928. Liliwatia Mashahidi wa Yehova katika rehani ya kupiga mbiu, kama kwa kelele ya pigano dhidi ya adui ya binadamu, Shetani, kwamba pigano kubwa linalokuja la Har–Magedoni litakomesha Shetani na tengenezo lake ovu karibuni.
Kwa kweli, historia yashuhudia kwamba Ibilisi ni adui halisi kwa kila mmoja wetu. Lakini, kwa wazi, Yehova Mungu hajatuacha peke yetu. Kwa nini usijifunze zaidi? Kuna faida ya kumjua adui yetu, “Shetani asije akapata kutushinda; kwa maana hatukosi kuzijua fikira zake.”—2 Wakorintho 2:11.
[Blabu katika ukurasa wa 27]
“Leo Ibilisi ametoweka na . . . Mungu mwenyewe amejitenga akaenda ng’ambo ya mbali kabisa.”
[Picha katika ukurasa wa 26]
Ibilisi wa halisi hafanani na picha za kidini wala na nadharia zisizo dhahiri za wanatheolojia
[Hisani]
Gustave Doré