Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 9/8 kur. 12-13
  • “Si Sehemu ya Ulimwengu”—Yamaanisha Nini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Si Sehemu ya Ulimwengu”—Yamaanisha Nini?
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wakristo Si Wasiopatana na Watu
  • ‘Msiseme kwa Ubaya juu ya Yeyote’
  • ‘Fanya Lililo Jema Kuelekea Wote’
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Ufanye Nini Iwapo Watu wa Ukoo Si wa Dini Yako?
    Amkeni!—2003
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Wachukiwa kwa Sababu ya Imani Yao
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 9/8 kur. 12-13

Maoni ya Biblia

“Si Sehemu ya Ulimwengu”—Yamaanisha Nini?

KATIKA karne ya nne W.K., maelfu ya waliodai kuwa Wakristo waliacha mali zao, jamaa, na njia yao ya maisha ili waishi katika upweke katika majangwa ya Misri. Wakaja kujulikana kama waankoriti, kutokana na neno la Kigiriki a·na·kho·reʹo, linalomaanisha “najiondoa.” Mwanahistoria mmoja awafafanua kuwa wanaojitenga na wengine. Waankoriti walifikiri kwamba kwa kujiepusha na jamii ya kibinadamu, walikuwa wakitii takwa la Kikristo la kuwa “si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 15:19.

Biblia huwaonya Wakristo kwa upole wafulize kuwa “bila doa kutokana na ulimwengu.” (Yakobo 1:27) Maandiko huonya kwa wazi hivi: “Wanawake wazinzi, je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote yule atakaye kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu.” (Yakobo 4:4) Hata hivyo, je, hii yamaanisha kuwa Wakristo wanatakiwa kuwa waankoriti, wakijiondoa kihalisi kutoka kwa wengine? Je, wapaswa kujiepusha na wale wasioshiriki nao itikadi zao za kidini?

Wakristo Si Wasiopatana na Watu

Dhana ya kuwa si sehemu ya ulimwengu imezungumziwa katika masimulizi mengi ya Biblia yanayokazia uhitaji wa Wakristo kujitenga na tungamo la jamii ya kibinadamu lililotengana na Mungu. (Linganisha 2 Wakorintho 6:14-17; Waefeso 4:18; 2 Petro 2:20.) Hivyo, Wakristo wa kweli kwa busara huepuka kabisa mitazamo, usemi, na mwenendo unaopingana na njia adilifu za Yehova, kama vile ufuatiaji wenye bidii wa utajiri, umashuhuri, na kujiingiza kupita kiasi katika raha. (1 Yohana 2:15-17) Wao pia hujitenga na ulimwengu kwa kudumisha kutokuwamo katika mambo ya vita na siasa.

Yesu Kristo alisema kuwa wanafunzi wake wangekuwa “si sehemu ya ulimwengu.” Lakini pia akasali kwa Mungu: “Nakuomba wewe, si uwachukue kutoka ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu.” (Yohana 17:14-16) Kwa wazi, Yesu hakutaka wanafunzi wake wawe wasiopatana na watu, wakiepuka kabisa mahusiano yoyote na wasio Wakristo. Kwa hakika, kujitenga kungemzuia Mkristo kutimiza utume wake wa kuhubiri na kufundisha “hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba.”—Matendo 20:20; Mathayo 5:16; 1 Wakorintho 5:9, 10.

Shauri la kubaki bila doa kutokana na ulimwengu haliwapi Wakristo msingi wowote wa kujifikiria wenyewe kuwa bora zaidi kuliko wengine. Wale wanaomwogopa Yehova huchukia “majivuno.” (Mithali 8:13, Zaire Swahili Bible) Wagalatia 6:3 husema kwamba “ikiwa yeyote afikiri yeye ni kitu wakati yeye si kitu, anadanganya akili yake mwenyewe.” Wale wahisio kuwa bora zaidi hujidanganya wenyewe kwa sababu “wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.”—Waroma 3:23.

‘Msiseme kwa Ubaya juu ya Yeyote’

Katika siku ya Yesu kulikuwa na watu waliodharau wote ambao hawakuwa sehemu ya vikundi vyao vya kidini visivyohusisha wengine. Miongoni mwa hawa walikuwa Mafarisayo. Waliijua vema Sheria ya Kimusa na vilevile mambo madogo-madogo ya mapokeo ya Kiyahudi. (Mathayo 15:1, 2; 23:2) Walionea fahari kufuata kwa uangalifu sana desturi nyingi za kidini. Mafarisayo walitenda kana kwamba walikuwa bora zaidi kuliko wengine kwa sababu tu ya matimizo yao ya kiakili na hadhi yao ya kidini. Walionyesha mtazamo wao wa kumcha Mungu na wa kudharau kwa kusema: “Umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa.”—Yohana 7:49.

Mafarisayo hata walikuwa na neno la dharau kwa wasio Mafarisayo. Neno la Kiebrania ʽam ha·ʼaʹrets lilitumiwa kwanza katika njia chanya kuonyesha washiriki wa kawaida wa jamii. Lakini baada ya wakati fulani viongozi wa kidini wa Yuda wenye kujigamba walibadili maana ya ʽam ha·ʼaʹrets kuwa yenye madharau. Vikundi vingine, kutia ndani wanaodai kuwa Wakristo, wametumia maneno kama “wapagani” na “kafiri” kwa njia ya kushusha kurejezea watu wenye itikadi za kidini zilizo tofauti na zao.

Ingawa hivyo, Wakristo wa karne ya kwanza waliwaonaje wale ambao hawakuwa wamekubali Ukristo? Wanafunzi wa Yesu walionywa kwa upole wawatendee wasioamini “kwa upole” na “staha yenye kina kirefu.” (2 Timotheo 2:25; 1 Petro 3:15) Mtume Paulo aliweka kielelezo chema katika hili. Alikuwa mwenye kufikika, hakuwa mwenye kujigamba. Badala ya kujiinua juu ya wengine, alikuwa mnyenyekevu na mwenye kujenga. (1 Wakorintho 9:22, 23) Katika barua yake iliyopuliziwa aliyoandikia Tito, Paulo atoa onyo la upole ‘tusiseme kwa ubaya juu ya yeyote, tusiwe wataka-vita, tuwe wenye kukubali sababu, tukionyesha wazi upole wote kuelekea watu wote.’—Tito 3:2.

Katika Biblia neno “asiyeamini” wakati mwingine hutumika kurejezea wasio Wakristo. Hata hivyo, hakuna uthibitisho kuwa neno “asiyeamini” lilitumika likiwa mtajo au jina rasmi. Bila shaka, halikutumika kuwashusha au kuwadharau wasio Wakristo, kwani hili lingekuwa kinyume cha kanuni za Biblia. (Mithali 24:9) Mashahidi wa Yehova leo huepuka kuwa wakali au wenye kujigamba kuelekea wasioamini. Wanaona kuwa ni ufidhuli kuwaita jamaa au majirani wasio Mashahidi kwa majina yenye kushusha. Wao hufuata shauri la Biblia lisemalo: “Mtumwa wa Bwana . . . ahitaji kuwa mwanana kuelekea wote.”—2 Timotheo 2:24.

‘Fanya Lililo Jema Kuelekea Wote’

Ni muhimu kutambua hatari za kuwa karibu sana na ulimwengu, hasa na wale wanaoonyesha kwa uzito kutostahi viwango vya Mungu. (Linganisha 1 Wakorintho 15:33.) Lakini, Biblia inaposhauri “tufanye lililo jema kuelekea wote,” neno “wote” hutia ndani hata wale wasioshiriki itikadi za Kikristo. (Wagalatia 6:10) Kwa wazi, chini ya hali fulani Wakristo wa karne ya kwanza walishiriki milo pamoja na wasioamini. (1 Wakorintho 10:27) Kwa sababu hiyo, leo Wakristo huwatendea wasioamini katika njia iliyosawazika, wakiwaona kama wanadamu wenzao.—Mathayo 22:39.

Ingekuwa kosa kukata kauli kwamba mtu hana adabu au hana adili kwa sababu tu hafahamu kweli za Biblia. Watu na hali hutofautiana. Hivyo, kila Mkristo lazima aamue ni kwa kiwango gani atajihusisha na wasioamini. Hata hivyo, haingekuwa lazima na haingepatana na maandiko kwa Mkristo kujitenga kihalisi kama walivyofanya waankoriti au kujihisi kuwa bora zaidi kama walivyofanya Mafarisayo.y

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki