Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 12/1 kur. 8-13
  • Wachukiwa kwa Sababu ya Imani Yao

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wachukiwa kwa Sababu ya Imani Yao
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Gharama” ya Kuwa Mwanafunzi
  • Wenye Kuchukia na Kuchukiwa
  • Wakristo wa Mapema Walichukiwa na Nani?
  • Kwa Nini Wakristo wa Mapema Walichukiwa Katika Ulimwengu wa Roma?
  • Bila Wazo la Kuridhiana!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Wakristo na Jamii ya Kibinadamu Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Kutetea Imani Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Wakristo wa Mapema na Ulimwengu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 12/1 kur. 8-13

Wachukiwa kwa Sababu ya Imani Yao

“Nanyi mtakuwa vitu vya kuchukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.”—MATHAYO 10:22.

1, 2. Je, waweza kusimulia mambo halisi yaliyoonwa ambayo Mashahidi wa Yehova wamevumilia kwa sababu ya kutenda kulingana na itikadi zao za kidini?

MWENYE duka mmoja anayefuatia haki wa kisiwa cha Krete akamatwa zaidi ya mara nyingi na kupelekwa tena na tena mbele ya mahakama za Ugiriki. Kwa jumla, yeye atumikia kifungo cha zaidi ya miaka sita gerezani, mbali na mke wake na watoto wake watano. Huko Japani mwanafunzi mwenye umri wa miaka 17 afukuzwa shuleni, ingawa yeye ni mwenye tabia njema na huwa wa kwanza katika darasa lake lenye wanafunzi 42. Katika Ufaransa watu wengi sana waachishwa kazi mara moja, hata ingawa wana sifa nzuri sana ya kufanya kazi kwa bidii na kwa kudhamiria. Mambo hayo halisi yaliyoonwa yana ufanani gani?

2 Watu wote wanaohusika ni Mashahidi wa Yehova. “Uhalifu” wao ni nini? Kimsingi, ni kutenda kulingana na itikadi zao za kidini. Kwa kutii mafundisho ya Yesu Kristo, huyo mwenye duka alikuwa akifundisha wengine imani yake. (Mathayo 28:19, 20) Alipatikana na hatia chini ya sheria ya kale ya Ugiriki ambayo hufanya kugeuza watu imani kuwe kosa la jinai. Yule mwanafunzi alifukuzwa kwa sababu dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia haingemruhusu ashiriki mazoezi ya kendo (ustadi wa Kijapani wa kupigana kwa upanga). (Isaya 2:4) Nao walioachishwa kazi katika Ufaransa walijulishwa kwamba sababu pekee ya kufukuzwa kwao ilikuwa kwamba, walijitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova.

3. Kwa nini kuteseka sana kwa Mashahidi wa Yehova mikononi mwa wanadamu wengine si tukio la kawaida kwa kulinganishwa?

3 Magumu hayo yaliyowapata ni mifano hasa ya yale ambayo Mashahidi wa Yehova wamevumilia hivi majuzi katika nchi fulani. Hata hivyo, kwa Mashahidi wa Yehova walio wengi, kuteseka sana mikononi mwa wanadamu wengine ni tukio lisilo la kawaida kwa kulinganishwa. Watu wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa sababu ya mwenendo wao mwema—sifa ambayo haimpi mtu yeyote sababu halali ya kuwadhuru. (1 Petro 2:11, 12) Wao hawali njama au kushiriki katika mwenendo wenye kuumiza. (1 Petro 4:15) Kinyume cha hilo, wao hujaribu kuishi kupatana na kanuni ya Biblia ya kuwa wenye kujitiisha kwanza kwa Mungu, kisha kwa serikali za kilimwengu. Wao hulipa kodi zitakwazo na sheria na hujitahidi sana ‘kuwa wenye kufanya amani na watu wote.’ (Waroma 12:18; 13:6, 7; 1 Petro 2:13-17) Katika kazi yao ya kufundisha Biblia, wao hutia watu moyo wastahi sheria, kanuni za kifamilia, na maadili. Serikali nyingi zimewasifu kwa kuwa raia wenye kutii sheria. (Waroma 13:3) Hata hivyo, kama vile fungu la kwanza lionyeshavyo, nyakati nyingine wamekuwa shabaha ya mnyanyaso—hata kupigwa marufuku na serikali katika nchi fulani. Je, hilo litushangaze?

“Gharama” ya Kuwa Mwanafunzi

4. Kulingana na Yesu, mtu angeweza kutarajia nini anapokuwa mmoja wa wanafunzi wake?

4 Yesu Kristo alionyesha waziwazi kinachohusishwa na kuwa mwanafunzi wake. “Mtumwa si mkubwa zaidi kuliko bwana-mkubwa wake,” akawaambia wafuasi wake. “Ikiwa wameninyanyasa mimi, watawanyanyasa nyinyi pia.” Yesu alichukiwa “bila sababu.” (Yohana 15:18-20, 25; Zaburi 69:4; Luka 23:22) Wanafunzi wake wangetarajia kufanyiwa hivyohivyo—kunyanyaswa bila msingi halali. Aliwaonya mara nyingi hivi: “mtakuwa vitu vya kuchukiwa.”—Mathayo 10:22; 24:9.

5, 6. (a) Ni kwa sababu gani Yesu aliwahimiza waliotazamiwa kuwa wafuasi wake ‘wakadirie gharama?’ (b) Kwa nini basi tusitatanike tunapokabili upinzani?

5 Kwa sababu hiyo, Yesu aliwahimiza waliotazamiwa kuwa wafuasi ‘wakadirie gharama’ ya kuwa wanafunzi. (Luka 14:28, Biblia Habari Njema) Kwa nini? Si ili waamue kama watakuwa wafuasi wake au la, bali ni ili waazimie kutimiza yanayohusika. Ni lazima tuwe tayari kuvumilia majaribu yoyote au magumu ambayo huambatana na pendeleo hilo. (Luka 14:27) Hakuna yeyote atulazimishaye kumtumikia Yehova tukiwa wafuasi wa Kristo. Ni uamuzi wa hiari na pia wenye kutegemea ujuzi. Twajua kimbele kwamba zaidi ya baraka ambazo sisi hupata kutokana na kuingia katika uhusiano ulio wakfu pamoja na Mungu, tutakuwa “vitu vya kuchukiwa.” Kwa hiyo sisi hatutataniki tukabilipo upinzani. ‘Tumekadiria gharama,’ na tuko tayari kabisa kuilipa.—1 Petro 4:12-14.

6 Kwa nini wengine, kutia ndani mamlaka fulani za kiserikali, watake kupinga Wakristo wa kweli? Ili kupata jibu, inafaa kuchunguza vikundi viwili vya kidini vya karne ya kwanza W.K. Vikundi vyote viwili vilichukiwa—lakini kwa sababu tofauti kabisa.

Wenye Kuchukia na Kuchukiwa

7, 8. Ni mafundisho gani yaliyodhihirisha kudharauliwa kwa wasio Wayahudi, na ni mtazamo gani uliositawi miongoni mwa Wayahudi kama tokeo?

7 Kufikia karne ya kwanza W.K., Israeli lilikuwa chini ya utawala wa Waroma, na kwa ujumla, dini ya Kiyahudi, yaani, mfumo wa kidini wa Kiyahudi, ilikandamizwa na viongozi kama vile Mafarisayo na waandishi. (Mathayo 23:2-4) Viongozi hao washupavu walizichukua kanuni za Sheria ya Kimusa kuhusu kujitenga na mataifa na kuzipotoa ili zifanye kudharauliwa kwa wasio Wayahudi kuwe takwa. Katika kufanya hivyo, walitokeza dini iliyofanya wasio Wayahudi wachukiwe, nao wasio Wayahudi wakawachukia Wayahudi pia.

8 Haikuwa vigumu kwa viongozi wa kidini kutetea kudharauliwa kwa wasio Wayahudi, kwa kuwa wakati huo Wayahudi waliwaona wasio Wayahudi kuwa viumbe wenye kuchukiza. Viongozi wa kidini walifundisha kwamba mwanamke Myahudi hapaswi kuwa peke yake pamoja na wasio Wayahudi, kwa kuwa “wanashukiwa kuwa waasherati.” Mwanamume Myahudi hapaswi “kubaki peke yake pamoja nao kwa kuwa wanashukiwa kumwaga damu.” Maziwa yaliyokamwa na asiye Myahudi hayangeweza kutumiwa isipokuwa Myahudi awe alikuwapo ili kutazama ukamaji huo. Kwa sababu ya uvutano wa viongozi wao, Wayahudi walisitawisha hali ya kujitenga na ya kutojihusisha kabisa na wengine.—Linganisha Yohana 4:9.

9. Ufundishaji wa viongozi Wayahudi kuhusu wasio Wayahudi ulikuwa na matokeo gani?

9 Mafundisho hayo kuwahusu wasio Wayahudi hayakusaidia kukuza mahusiano mazuri baina ya Wayahudi na wasio Wayahudi. Wasio Wayahudi walikuja kuwaona Wayahudi kuwa wachukiaji wa wanadamu wote. Tacitus, mwanahistoria Mroma (aliyezaliwa yapata mwaka wa 56 W.K.), alisema kuwahusu Wayahudi kwamba “wanawachukia wanadamu wale wengine wote sawa na vile wanavyowachukia maadui.” Tacitus pia alidai kwamba wasio Wayahudi waliopata kuwa wageuzwa-imani wa Kiyahudi walifundishwa kukana nchi yao na kutoheshimu familia zao na rafiki zao. Kwa ujumla, Waroma waliwavumilia Wayahudi, ambao walikuwa wengi sana wasiweze kushambuliwa. Lakini uasi wa Wayahudi mwaka wa 66 W.K. ulichochea ulipizaji kisasi wenye ukatili wa Waroma, ukiongoza kwenye kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K.

10, 11. (a) Sheria ya Kimusa ilitaka wageni watendeweje? (b) Twajifunza nini kutokana na yaliyoipata Dini ya Kiyahudi?

10 Maoni hayo kuhusu wageni yalilinganaje na aina ya ibada iliyoonyeshwa katika Sheria ya Kimusa? Sheria ilitokeza hali ya kujitenga na mataifa, lakini jambo hilo lilikusudiwa kuwalinda Waisraeli, hasa ibada yao safi. (Yoshua 23:6-8) Hata hivyo, Sheria ilitaka kwamba wageni watendewe kwa haki na kwa usawa na kwamba wapokewe kwa ukaribishaji-wageni—maadamu tu hawakukosa kutii sheria za Israeli kwa kutojali. (Mambo ya Walawi 24:22) Kwa kuacha maana ifaayo iliyothibitishwa wazi katika Sheria kuhusiana na wageni, viongozi wa kidini Wayahudi wa wakati wa Yesu walitokeza aina ya ibada iliyofanya wageni wachukiwe, nao wakaichukia pia. Mwishowe, taifa la Wayahudi la karne ya kwanza lilipoteza upendeleo wa Yehova.—Mathayo 23:38.

11 Je, kuna somo tunalopata kutokana na hayo? Ndiyo, kunalo. Mtazamo wa kujiona kuwa waadilifu na bora kushinda wengine, ambao huwadharau wale wenye itikadi za kidini tofauti na zetu, hauwakilishi ibada safi ya Yehova, wala haumpendezi. Fikiria Wakristo waaminifu wa karne ya kwanza. Hawakuwachukia wasio Wakristo, wala hawakuasi dhidi ya Roma. Hata hivyo, walikuwa “vitu vya kuchukiwa.” Kwa nini? Na nani?

Wakristo wa Mapema Walichukiwa na Nani?

12. Ni wazi kadiri gani kutokana na Maandiko kwamba Yesu hutaka wafuasi wake wawe na maoni yaliyosawazika kuhusu wasio Wakristo?

12 Ni wazi kutokana na mafundisho ya Yesu kwamba alikusudia wanafunzi wake wawe na maoni yaliyosawazika kuhusu wasio Wakristo. Kwa upande mmoja, alisema kwamba wafuasi wake wangejitenga na ulimwengu—yaani, wangeepuka kabisa mitazamo na mwenendo uliohitilafiana na njia za uadilifu za Yehova. Wangeendelea kutokuwamo katika mambo ya vita na siasa. (Yohana 17:14, 16) Kwa upande mwingine, badala ya kutetea kudharauliwa kwa wasio Wayahudi, Yesu aliwaambia wafuasi wake ‘wawapende maadui wao.’ (Mathayo 5:44) Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo hivi: “Ikiwa adui yako ana njaa, mlishe; ikiwa ana kiu, mpe kitu cha kunywa.” (Waroma 12:20) Pia aliwaambia Wakristo ‘wafanye lililo jema kuelekea wote.’—Wagalatia 6:10.

13. Kwa nini viongozi wa kidini Wayahudi waliwapinga sana wanafunzi wa Kristo?

13 Hata hivyo, punde si punde wanafunzi wa Kristo walijipata wakiwa “vitu vya kuchukiwa” kutokana na vyanzo vitatu. Cha kwanza kilikuwa viongozi wa kidini Wayahudi. Si ajabu kwamba Wakristo walivuta uangalifu wao upesi! Wakristo walikuwa na kanuni za juu za maadili na uaminifu-maadili, nao walitoa ujumbe wenye kuchochea tumaini kwa bidii nyingi sana. Maelfu ya watu waliacha Dini ya Kiyahudi na kukubali Ukristo. (Matendo 2:41; 4:4; 6:7) Kwa viongozi wa kidini Wayahudi, wanafunzi wa Yesu Wayahudi walikuwa tu waasi-imani! (Linganisha Matendo 13:45.) Viongozi hao wenye hasira walihisi kwamba Ukristo ulibatilisha mapokeo yao. Kwani hata uliyakataa maoni yao kuhusu wasio Wayahudi! Kuanzia mwaka wa 36 W.K. na kuendelea, wasio Wayahudi wangeweza kuwa Wakristo, wakishiriki imani ileile na kufurahia mapendeleo yaleyale waliyofurahia Wayahudi Wakristo.—Matendo 10:34, 35.

14, 15. (a) Kwa nini Wakristo walichukiwa na waabudu wapagani? Toa kielelezo. (b) Wakristo wa mapema walikuja kuwa “vitu vya kuchukiwa” na kikundi gani cha tatu?

14 Pili, Wakristo walichukiwa na waabudu wapagani. Kwa kielelezo, katika Efeso la kale, utengenezaji wa vihekalu vya fedha vya mungu-mke Artemisi ulikuwa biashara yenye faida. Lakini Paulo alipohubiri huko, Waefeso wengi waliitikia, wakiacha kuabudu Artemisi. Biashara yao ikiwa imetishwa, wafua-fedha walifanya ghasia. (Matendo 19:24-41) Jambo sawa na hilo lilitokea baada ya Ukristo kuenea hadi Bithinia (sasa kaskazini-magharibi mwa Uturuki). Muda mfupi baada ya kukamilishwa kwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, gavana wa Bithinia, Plini Mchanga, aliripoti kwamba mahekalu ya wapagani yaliachwa na kwamba uuzaji wa chakula cha wanyama wa kutolewa dhabihu ulishuka sana. Wakristo walilaumiwa—na kunyanyaswa—kwa kuwa ibada yao haikuruhusu kuwepo kwa dhabihu za wanyama na sanamu. (Waebrania 10:1-9; 1 Yohana 5:21) Kwa wazi, kuenea kwa Ukristo kuliathiri mambo fulani yenye kunufaisha yaliyohusiana na ibada ya kipagani, nao waliopoteza biashara na fedha waliuchukia.

15 Tatu, Wakristo walipata kuwa “vitu vya kuchukiwa” na Waroma wenye kutukuza taifa. Mwanzoni, Waroma waliwajua Wakristo kuwa kikundi kidogo cha kidini ambacho yaelekea kilikuwa kishupavu. Hata hivyo, baada ya muda, kudai tu kuwa Mkristo kukawa kosa lililostahili adhabu ya kifo. Kwa nini raia wenye kufuata haki, wanaoishi maisha ya Kikristo wangeonekana kuwa watu wastahilio mnyanyaso na kifo?

Kwa Nini Wakristo wa Mapema Walichukiwa Katika Ulimwengu wa Roma?

16. Wakristo walijitenga na ulimwengu katika njia zipi, na kwa nini hilo lilifanya wachukiwe katika ulimwengu wa Waroma?

16 Kimsingi, Wakristo walichukiwa katika ulimwengu wa Roma kwa kutenda kulingana na itikadi zao za kidini. Kwa kielelezo, walijitenga na ulimwengu. (Yohana 15:19) Kwa hiyo, hawakuwa na nyadhifa za kisiasa, nao walikataa utumishi wa kijeshi. Tokeo likawa kwamba, “waliwakilishwa wakiwa wafu kwa habari ya ulimwengu, wasiofaa kwa jambo lolote maishani,” asema mwanahistoria Augustus Neander. Kutokuwa sehemu ya ulimwengu pia kulimaanisha kuepuka njia mbovu za ulimwengu mfisadi wa Waroma. “Zile jumuiya ndogo-ndogo za Wakristo zilikuwa zikiusumbua ulimwengu wa kipagani wenye kutamani sana anasa kwa uchaji na adabu zao,” aeleza mwanahistoria Will Durant. (1 Petro 4:3, 4) Huenda Waroma wakawa walijaribu kuwanyamazisha Wakristo hao wenye kusumbua kwa kuwanyanyasa na kuwaua.

17. Ni nini kionyeshacho kwamba kazi ya kuhubiri ya Wakristo wa karne ya kwanza ilikuwa na matokeo?

17 Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu kwa bidii isiyoridhiana. (Mathayo 24:14) Kufikia mwaka wa 60 W.K., Paulo angeweza kusema kwamba habari njema ilikuwa ‘imehubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:23) Kufikia mwisho wa karne ya kwanza, wafuasi wa Yesu walikuwa wamefanya wanafunzi kotekote katika Milki ya Waroma—katika Asia, Ulaya, na Afrika! Hata washiriki fulani wa “nyumbani mwa Kaisari” wakawa Wakristo.a (Wafilipi 4:22) Kuhubiri huko kwa bidii kulichochea chuki. Neander asema: “Ukristo ulienea hatua kwa hatua miongoni mwa watu wa kila tabaka, ukatisha kuangamiza dini ya taifa.”

18. Kumpa Yehova ujitoaji usiohusisha wengine kuliwafanyaje Wakristo wasipatane na serikali ya Waroma?

18 Wafuasi wa Yesu walimpa Yehova ujitoaji usiohusisha wengine. (Mathayo 4:8-10) Yawezekana sehemu hii ya ibada yao, zaidi ya nyingine yoyote, ndiyo iliyowafanya wasipatane na Roma. Waroma walivumilia dini nyinginezo, maadamu tu wafuasi wake walishiriki pia katika kuabudu maliki. Wakristo wa mapema hawangeweza kabisa kushiriki katika ibada kama hiyo. Walijiona kuwa wenye kuwajibika kwa mamlaka iliyo juu zaidi kuliko hiyo ya Serikali ya Waroma, yaani, Yehova Mungu. (Matendo 5:29) Tokeo likawa kwamba, Mkristo alionwa kuwa adui wa Serikali, hata awe alikuwa raia mwema kadiri gani kuhusiana na mambo yale mengine yote.

19, 20. (a) Ni nani hasa waliohusika na uchongezi mbaya ulioenezwa kuwahusu Wakristo waaminifu? (b) Ni mashtaka gani yasiyo ya kweli yaliyozushwa dhidi ya Wakristo?

19 Bado kuna sababu nyingine iliyofanya Wakristo waaminifu wawe “vitu vya kuchukiwa” katika ulimwengu wa Waroma: Uchongezi mbaya kuwahusu uliaminika kwa urahisi, nao viongozi Wayahudi walihusika kwa kiwango kikubwa katika kuueneza. (Matendo 17:5-8) Paulo alipokuwa Roma akingojea kufanyiwa kesi na Maliki Nero wapata mwaka wa 60 au 61 W.K., viongozi Wayahudi walisema hivi kuwahusu Wakristo: “Kweli kwa habari ya farakano hili yajulikana kwetu kwamba kila mahali huwa lasemwa vibaya.” (Matendo 28:22) Bila shaka, Nero alisikia hadithi za uchongezi kuwahusu. Katika mwaka wa 64 W.K., alipolaumiwa kwa moto ulioteketeza Roma, yaripotiwa kwamba Nero aliwasingizia Wakristo waliokuwa tayari wamesemwa vibaya. Yaonekana jambo hilo lilitokeza mnyanyaso mkubwa wenye jeuri uliokusudiwa kuwaangamiza Wakristo kabisa.

20 Mara nyingi mashtaka hayo yasiyo ya kweli dhidi ya Wakristo yalikuwa mchanganyiko wa uwongo na upotoaji wa itikadi zao. Wao waliitwa waatheisti kwa sababu waliabudu Mungu mmoja na hawakumwabudu maliki. Kwa kuwa washiriki fulani wa familia wasio Wakristo walipinga jamaa zao Wakristo, Wakristo walishtakiwa kwa kuvunja familia. (Mathayo 10:21) Waliitwa wala-watu, shtaka ambalo vyanzo fulani vyasema, lilitegemea kupotoshwa kwa maneno ya Yesu aliyotamka kwenye Mlo wa Jioni wa Bwana.—Mathayo 26:26-28.

21. Wakristo walikuwa “vitu vya kuchukiwa” kwa sababu gani mbili?

21 Kwa hiyo, Wakristo waaminifu walikuwa “vitu vya kuchukiwa” na Waroma kwa sababu mbili za msingi: (1) itikadi zao zilizotegemea Biblia, na (2) mashtaka yasiyo ya kweli dhidi yao. Hata sababu iwe nini, wapinzani walikuwa na lengo moja—kukandamiza Ukristo. Bila shaka, wachochezi halisi wa mnyanyaso huo wa Wakristo walikuwa wapinzani wenye uwezo upitao wa kibinadamu, majeshi yasiyoonekana ya roho waovu.—Waefeso 6:12.

22. (a) Ni kielelezo gani kionyeshacho kwamba Mashahidi wa Yehova hujitahidi sana ‘kufanya lililo jema kuelekea wote’? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 11.) (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

22 Kama Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova wa nyakati za kisasa wamekuwa “vitu vya kuchukiwa” katika nchi mbalimbali. Hata hivyo, wao hawawachukii wasio Mashahidi; wala hawajapata kuanzisha maasi dhidi ya serikali. Kinyume cha hilo, wanajulikana ulimwenguni pote kwa kuonyesha upendo wa kweli ambao huvuka mipaka yote ya kijamii, kitaifa, na kikabila. Basi, ni kwa nini wamenyanyaswa? Nao huitikiaje upinzani? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

a Si lazima usemi “nyumbani mwa Kaisari” uwe warejezea washiriki wa karibu wa familia ya Nero, aliyekuwa akitawala wakati huo. Badala yake, huenda ukarejezea watumishi wa nyumbani na maofisa wa vyeo vya chini, ambao yawezekana walitoa utumishi wa nyumbani kama vile kupika na kusafisha kwa niaba ya familia ya kifalme na wafanyakazi wao.

[Ungejibuje?]

◻ Kwa nini Yesu aliwahimiza waliotazamiwa kuwa wafuasi wakadirie gharama ya kuwa wanafunzi?

◻ Maoni yaliyoenea kuhusu wasio Wayahudi yalikuwa na matokeo gani juu ya Dini ya Kiyahudi, nasi twajifunza nini kutokana na hilo?

◻ Wakristo waaminifu wa mapema walikabili upinzani kutokana na vyanzo gani vitatu?

◻ Wakristo wa mapema walikuwa “vitu vya kuchukiwa” kwa sababu zipi za msingi?

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

‘Kufanya Lililo Jema Kuelekea Wote’

Mashahidi wa Yehova hujitahidi sana kutii onyo la upole la Biblia la ‘kufanya lililo jema kuelekea wote.’ (Wagalatia 6:10) Nyakati za uhitaji, upendo kwa jirani huwachochea wawasaidie wale wenye maoni ya kidini tofauti na yao. Kwa kielelezo, wakati wa hali ya maafa huko Rwanda mwaka wa 1994, Mashahidi kutoka Ulaya walijitolea kwenda Afrika kusaidia katika jitihada za kutoa msaada. Kambi zenye utaratibu mzuri na hospitali za muda zilijengwa haraka ili kutoa msaada. Kiasi kikubwa cha chakula, mavazi, na mablanketi kililetwa kwa ndege. Idadi ya wakimbizi iliyonufaika na jitihada hiyo ya kutoa msaada ilikuwa mara tatu zaidi ya idadi ya Mashahidi katika eneo hilo.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri habari njema kwa bidii isiyoridhiana

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki