-
Je, Jina Lako Liko Katika “Kitabu cha Uzima”?Mnara wa Mlinzi (Funzo)—2022 | Septemba
-
-
UFUFUO KWENYE UZIMA NA KWENYE HUKUMU
13-14. (a) Zamani, tulielewaje maneno ya Yesu kwenye Yohana 5:29? (b) Tunahitaji kutambua jambo gani kuhusu maneno hayo?
13 Yesu pia alizungumza kuhusu wale watakaofufuliwa hapa duniani. Kwa mfano, alisema: “Saa inakuja ambayo wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka, wale waliotenda mema kwenye ufufuo wa uzima, na wale waliozoea kutenda maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yoh. 5:28, 29) Yesu alimaanisha nini?
14 Zamani, uelewaji wetu ulikuwa kwamba maneno ya Yesu yanarejelea matendo ambayo wale watakaofufuliwa watatenda baada ya kufufuliwa; yaani, baadhi yao watafufuliwa na kutenda mambo mema na wengine watafufuliwa na kutenda mambo mabaya. Hata hivyo, ona kwamba Yesu hasemi wale ambao wametoka tu katika makaburi ya ukumbusho watatenda mambo mema au watazoea kutenda mambo maovu. Anazungumzia matukio ya wakati uliopita. Anazungumza kuhusu watu “waliotenda mema” na wale “waliozoea kutenda maovu.” Hilo linaonyesha kwamba walifanya matendo hayo kabla ya kufa. Hilo linapatana na akili, sivyo? Kwa sababu hakuna mtu atakayeruhusiwa kutenda maovu katika ulimwengu mpya. Ni lazima iwe kwamba wasio waadilifu walizoea kutenda matendo hayo maovu kabla ya kufa. Basi, tunapaswa kuelewaje maneno ya Yesu kuhusu “ufufuo wa uzima” na “ufufuo wa hukumu”?
15. Ni nani ambao watapata “ufufuo wa uzima,” na kwa nini?
15 Waadilifu, ambao walitenda mambo mazuri kabla ya kufa, watapata “ufufuo wa uzima” kwa sababu tayari majina yao yatakuwa yameandikwa katika kitabu cha uzima. Hilo linamaanisha kwamba ufufuo wa “wale waliotenda mema” unaofafanuliwa kwenye Yohana 5:29, ni sawa na ufufuo wa “waadilifu” unaotajwa kwenye Matendo 24:15. Uelewaji huu unapatana na maneno ya andiko la Waroma 6:7, linalosema hivi: “Yule ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.” Dhambi ambazo waadilifu hao walitenda zilifutwa walipokufa, lakini rekodi yao ya uaminifu bado ipo. (Ebr. 6:10) Bila shaka, waadilifu hao ambao watafufuliwa watahitaji kuendelea kuwa waaminifu ili majina yao yabaki katika kitabu cha uzima.
16. “Ufufuo wa hukumu” unamaanisha nini?
16 Namna gani wale waliozoea kutenda maovu kabla ya kufa? Ingawa dhambi zao zilifutwa walipokufa, hawakuwa na rekodi ya uaminifu. Majina yao hayakuwa yameandikwa katika kitabu cha uzima. Basi, ufufuo wa “wale waliozoea kutenda maovu” ni sawa na ufufuo wa “wasio waadilifu” unaotajwa kwenye Matendo 24:15. Watapata “ufufuo wa hukumu.”c Wasio waadilifu watahukumiwa katika maana ya kwamba Yesu atachunguza na kupima matendo yao. (Luka 22:30) Muda utahitaji kupita kabla ya kuamua ikiwa majina yao yanastahili kuandikwa kwenye kitabu cha uzima. Ikiwa watu hao wasio waadilifu watakubali kubadili mwenendo wao mwovu wa zamani na kujiweka wakfu kwa Yehova, ndipo majina yao yatakapoandikwa kwenye kitabu cha uzima.
-
-
Je, Jina Lako Liko Katika “Kitabu cha Uzima”?Mnara wa Mlinzi (Funzo)—2022 | Septemba
-
-
c Zamani, tulifafanua kwamba neno “hukumu” linalotumiwa hapa linamaanisha hukumu isiyofaa, au kupatikana na hatia. Kwa kweli, neno “hukumu” linaweza kuwa na maana hiyo. Lakini katika muktadha huu, inaonekana kwamba Yesu alitumia neno “hukumu” katika maana pana zaidi, akimaanisha kuchunguza na kupima mwenendo au kama kamusi moja ya Kigiriki inavyosema, “kuchanganua tabia.”
-