SOMO LA 18
Uwe Rafiki ya Mungu Milele!
Kupata rafiki huhitaji jitihada; wahitaji kujitahidi ili uendelee kuwa na rafiki. Jitihada zako za kuwa rafiki ya Mungu na kuendelea kuwa rafiki yake zitabarikiwa sana. Yesu aliwaambia hivi wale waliomwamini: “Kweli itawaweka nyinyi huru.” (Yohana 8:32) Hilo lamaanisha nini?
Unaweza kufurahia uhuru sasa. Unaweza kuwa huru kutokana na mafundisho yasiyo ya kweli ambayo Shetani ameeneza. Unaweza kuwa na tumaini tofauti na mamilioni ya watu wasiomjua Yehova ambao hawana tumaini maishani. (Waroma 8:22) Rafiki za Mungu hata hawana “hofu ya kifo.”—Waebrania 2:14, 15.
Unaweza kufurahia uhuru katika ulimwengu mpya wa Mungu. Unaweza kufurahia uhuru mzuri kama nini wakati ujao! Katika dunia Paradiso, hakutakuwako vita, magonjwa, na uhalifu. Umaskini na njaa hazitakuwako. Uzee na kifo havitakuwako. Hakutakuwako hofu, kuonewa, na ukosefu wa haki. Biblia yasema hivi kumhusu Mungu: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”—Zaburi 145:16.
Rafiki za Mungu wataishi milele. Uhai wa milele ni zawadi yenye thamani ambayo Mungu atawapa wote wanaojitahidi kuwa rafiki zake. (Waroma 6:23) Ebu wazia tu mambo ambayo uhai usio na mwisho utamaanisha kwako!
Utakuwa na wakati wa kufanya mambo mengi. Labda unataka kujifunza kucheza ala fulani ya muziki. Au labda unataka kujifunza kuchora picha au kuwa seremala. Huenda unataka kujifunza kuhusu wanyama au mimea. Au labda unataka kusafiri na kuona nchi mbalimbali na watu mbalimbali. Kuwa na uhai udumuo milele kutafanya mambo hayo yote yawezekane!
Utakuwa na wakati wa kupata rafiki wengi. Kuishi milele kutakuwezesha ujue watu wengine wengi ambao wamekuwa rafiki za Mungu. Utapata kujua vipawa na sifa zao njema, nao watakuwa rafiki zako pia. Utawapenda, nao watakupenda. (1 Wakorintho 13:8) Kuwa na uhai usio na mwisho kutakupa nafasi ya kuwa rafiki ya kila mtu duniani! Jambo zuri zaidi ya yote ni kwamba urafiki wako pamoja na Yehova utazidi kuongezeka nguvu kadiri karne zipitavyo. Na uwe rafiki ya Mungu milele!