-
“Kazia Uangalifu Zaidi Kuliko Ilivyo Kawaida”Mnara wa Mlinzi—2002 | Septemba 15
-
-
“Kazia Uangalifu Zaidi Kuliko Ilivyo Kawaida”
“Ni lazima kwetu kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo yaliyosikiwa nasi, ili tusipate kamwe kupeperushwa.”—WAEBRANIA 2:1.
1. Toa mfano wa jinsi kukengeushwa kunavyoweza kusababisha msiba.
KILA mwaka aksidenti za magari husababisha vifo vya watu wapatao 37,000 huko Marekani pekee. Wataalamu wanasema kwamba vingi kati ya vifo hivyo havingetokea ikiwa madereva wangekuwa waangalifu zaidi barabarani. Madereva wengine hukengeushwa na ishara na mabango ya matangazo yaliyo kando ya barabara au na simu za mkononi. Pia kuna madereva ambao hupenda kula wanapoendesha gari. Katika hali hizi zote, kukengeushwa kunaweza kusababisha msiba.
2, 3. Paulo aliwapa Wakristo Waebrania ushauri gani, na kwa nini ushauri huo ulifaa?
2 Miaka 2,000 hivi kabla ya magari kuvumbuliwa, mtume Paulo alitaja jambo fulani lililowakengeusha na kuwaletea msiba baadhi ya Wakristo Waebrania. Paulo alikazia kwamba Yesu Kristo aliyefufuliwa alipewa mamlaka kubwa kuliko malaika wote, kwani aliketi mkono wa kuume wa Mungu. Kisha mtume huyo akasema: “Hiyo ndiyo sababu ni lazima kwetu kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo yaliyosikiwa nasi, ili tusipate kamwe kupeperushwa mbali.”—Waebrania 2:1.
3 Kwa nini Wakristo Waebrania walihitaji “kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo yaliyosikiwa” kumhusu Yesu? Ni kwa sababu miaka 30 hivi ilikuwa imepita tangu Yesu aondoke duniani. Kwa kuwa Bwana wao hakuwapo, baadhi ya Wakristo Waebrania walikuwa wanaanza kupeperuka kutoka kwenye imani ya kweli. Walikuwa wakikengeushwa na Dini ya Kiyahudi, ambayo ilikuwa ibada yao ya awali.
Walihitaji Kukazia Uangalifu Zaidi
4. Kwa nini huenda baadhi ya Wakristo Waebrania wangeweza kushawishiwa kurudia Dini ya Kiyahudi?
4 Kwa nini Mkristo angeweza kushawishiwa kurudia Dini ya Kiyahudi? Sababu ni kwamba ibada iliyotegemea Sheria ilihusisha vitu halisi vinavyoonekana. Watu waliwaona makuhani na kusikia harufu ya dhabihu zinazochomwa. Lakini Ukristo ulikuwa na mambo mengine yaliyokuwa tofauti sana. Kuhani wa Cheo cha Juu wa Wakristo, Yesu Kristo, hakuwahi kuonekana duniani kwa miaka 30 kufikia wakati huo. (Waebrania 4:14) Walikuwa na hekalu, lakini mahali pake patakatifu palikuwa mbinguni kwenyewe. (Waebrania 9:24) Tofauti na tohara ya kimwili iliyofanywa chini ya Sheria, tohara ya Kikristo ilifanywa katika “moyo kwa roho.” (Waroma 2:29) Basi, Wakristo Waebrania walianza kuona Ukristo kuwa kama kitu kisicho halisi.
5. Paulo alionyeshaje kwamba ibada iliyoanzishwa na Yesu ilikuwa bora kuliko ibada iliyotegemea Sheria?
5 Wakristo hao Waebrania walipaswa kutambua jambo fulani muhimu kuhusu ibada iliyoanzishwa na Kristo. Ibada hiyo ilitegemea imani wala si vitu vinavyoonekana, na ilikuwa bora kuliko Sheria iliyotolewa kupitia Musa. Paulo aliandika hivi: “Ikiwa damu ya mbuzi na ya mafahali na majivu ya mtamba wa ng’ombe yaliyonyunyizwa juu ya wale ambao wametiwa unajisi hutakasa kufikia kadiri ya usafi wa mwili, je, si zaidi sana damu ya Kristo, ambaye kupitia roho idumuyo milele alijitoa mwenyewe bila waa kwa Mungu, itasafisha dhamiri zetu kutoka kazi zilizokufa ili tupate kutoa utumishi mtakatifu kwa Mungu aliye hai?” (Waebrania 9:13, 14) Hakika msamaha unaotegemea imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo ni bora sana kwa njia nyingi kuliko msamaha uliotegemea dhabihu zilizotolewa chini ya Sheria.—Waebrania 7:26-28.
6, 7. (a) Ni hali gani iliyofanya iwe muhimu kwa Wakristo Waebrania “kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo yaliyosikiwa”? (b) Paulo alipowaandikia Waebrania barua hiyo, ni muda gani uliokuwa umebaki kabla ya uharibifu wa Yerusalemu? (Ona kielezi-chini.)
6 Kuna sababu nyingine pia iliyofanya Wakristo Waebrania wahitaji kukazia uangalifu mambo waliyosikia kumhusu Yesu. Alitabiri kwamba Yerusalemu itaharibiwa. Yesu alisema: “Siku zitakuja juu yako wakati maadui wako watakapojenga kukuzunguka wewe boma lenye miti iliyochongoka nao watakuzunguka na kukutaabisha kutoka kila upande, nao watabwaga kwenye ardhi wewe na watoto wako walio ndani yako, nao hawataacha jiwe juu ya jiwe katika wewe, kwa sababu hukufahamu wakati wa kukaguliwa kwako.”—Luka 19:43, 44.
7 Mambo hayo yangetukia lini? Yesu hakufunua siku yenyewe wala saa. Badala yake, yeye aliwapa tu maagizo haya: “Wakati mwonapo Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwalo kumekaribia. Ndipo waacheni wale walio katika Yudea waanze kukimbia hadi kwenye milima, na waacheni wale walio katikati yalo waondoke, na waacheni wale walio katika sehemu za mashambani wasiingie ndani yalo.” (Luka 21:20, 21) Katika ule muda wa miaka 30 baada ya Yesu kusema hivyo, Wakristo wengine waliokuwa Yerusalemu walikosa kuona umuhimu wa nyakati hizo, wakakengeushwa. Wakawa kama dereva anayekengeushwa anapoendesha gari. Walipaswa kurekebisha maoni yao au sivyo hakika wangepatwa na msiba. Iwe walidhani uharibifu wa Yerusalemu ungekuja au la, uharibifu huo ulikuwa umekaribia sana!a Tunatumaini kwamba ushauri wa Paulo uliwaamsha Wakristo waliolala usingizi wa kiroho huko Yerusalemu.
Kukazia “Uangalifu Zaidi Kuliko Ilivyo Kawaida” Leo
8. Kwa nini tunahitaji “kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida” kweli za Neno la Mungu?
8 Kama ilivyokuwa na Wakristo wa karne ya kwanza, leo sisi pia tunahitaji “kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida” kweli za Neno la Mungu. Kwa nini? Kwa sababu sisi pia tunakabili uharibifu ambao umekaribia kuupata mfumo wote wa mambo na si taifa moja tu. (Ufunuo 11:18; 16:14, 16) Ni kweli kwamba hatujui siku yenyewe wala saa yenyewe ambayo Yehova ataleta uharibifu huo. (Mathayo 24:36) Hata hivyo, tunaona utimizo wa unabii wa Biblia unaothibitisha wazi kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Kwa hiyo tujihadhari na kitu chochote kinachoweza kutukengeusha. Tunapaswa kukazia uangalifu Neno la Mungu na kuendelea kukumbuka umuhimu wa nyakati hizi. Hiyo ndiyo njia pekee ya “kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia.”—Luka 21:36.
-
-
“Kazia Uangalifu Zaidi Kuliko Ilivyo Kawaida”Mnara wa Mlinzi—2002 | Septemba 15
-
-
a Inaelekea barua ya Waebrania iliandikwa mwaka wa 61 W.K. Ikiwa ndivyo, basi Yerusalemu lilizingirwa na majeshi ya Cestius Gallus miaka mitano tu baadaye. Lakini upesi majeshi hayo yakaondoka, na Wakristo waliokuwa macho wakatoroka. Miaka minne baadaye, jiji hilo likaharibiwa na majeshi ya Roma yakiongozwa na Jenerali Tito.
-