Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 11/15 kur. 18-23
  • Je, Unatimiza Wajibu Wako Wote kwa Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Unatimiza Wajibu Wako Wote kwa Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je, Mambo Yote Ni Ubatili?
  • Wakfu na Wajibu Wetu kwa Mungu
  • Pima Maamuzi Yako kwa Uangalifu!
  • Mambo Yanayotusaidia Kumkumbuka Muumba Wetu Mtukufu
  • Wajibu Wetu Wote kwa Mungu
  • Timiza Wajibu Wako Wote
  • Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Kitabu Cha Biblia Namba 21—Mhubiri
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • “Kwa Jumla Ndiyo Impasayo Mtu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Kutimiza Wajibu Wetu Mbele za Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 11/15 kur. 18-23

Je, Unatimiza Wajibu Wako Wote kwa Mungu?

“Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.”—MHUBIRI 12:14.

1. Yehova amewafanyia watu wake maandalizi gani?

YEHOVA huwategemeza wale ambao daima humkumbuka kuwa Muumba wao Mtukufu. Neno lake lililopuliziwa huwapa ujuzi unaohitajika ili wampendeze kikamili. Roho takatifu ya Mungu huwaongoza wafanye mapenzi ya kimungu na “kuzaa matunda katika kila kazi njema.” (Wakolosai 1:9, 10) Pia Yehova huandaa chakula cha kiroho na mwongozo wa kitheokrasi kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Basi, kwa njia nyingi, watu wa Mungu hupata baraka za kimbingu wanapomtumikia Yehova na kufanya kazi muhimu ya kuhubiri habari njema za Ufalme.—Marko 13:10.

2. Kuhusu kumtumikia Yehova, ni maswali gani yanayoweza kutokea?

2 Wakristo wa kweli wanafurahi kumtolea Yehova utumishi mtakatifu. Lakini, huenda wengine wakavunjika moyo na kufikiria kwamba jitihada zao hazifai. Kwa mfano, nyakati nyingine huenda Wakristo waliojiweka wakfu wakawa na shaka kama kweli jitihada zao za kudhamiria zinafaa. Kichwa cha familia anapofikiria funzo la familia na utendaji mwingine, yeye aweza kujiuliza maswali kama haya: ‘Je, kweli Yehova anapendezwa na yale tunayofanya? Je, tunatimiza wajibu wetu wote kwa Mungu?’ Maneno yenye hekima ya mhubiri yanaweza kutusaidia kuyajibu maswali hayo.

Je, Mambo Yote Ni Ubatili?

3. Kupatana na Mhubiri 12:8, ubatili mkubwa kabisa ni nini?

3 Huenda wengine wakafikiria kwamba maneno haya ya mwenye hekima yanavunja moyo mtu yeyote—awe kijana au mzee. “Mhubiri asema, Ubatili mtupu; mambo yote ni ubatili!” (Mhubiri 12:8) Kwa kweli, ni ubatili mkubwa kabisa kumpuuza Muumba Mtukufu ujanani, kuzeeka bila kumtumikia, na kwamba jambo pekee ambalo umetimiza maishani ni kuishi maisha marefu. Yote yamekuwa ubatili, au bure, kwa mtu kama huyo, hata akifa akiwa na mali au akiwa mashuhuri katika ulimwengu huu ambao umo katika uwezo wa yule mwovu, Shetani Ibilisi.—1 Yohana 5:19.

4. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba mambo yote si ubatili?

4 Mambo yote si ubatili kwa wale ambao wanaweka hazina mbinguni wakiwa watumishi waaminifu wa Yehova. (Mathayo 6:19, 20) Wao wana mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana yenye kuthawabisha, na kwa hakika kazi hiyo si bure. (1 Wakorintho 15:58) Lakini ikiwa sisi ni Wakristo waliojiweka wakfu, je, tunaendelea kujishughulisha na kazi ambayo Mungu alituagiza tufanye katika hizi siku za mwisho? (2 Timotheo 3:1) Ama tumeanza kuishi maisha ambayo hayatofautiani sana na yale ya jirani zetu kwa ujumla? Huenda wao ni wafuasi wa dini mbalimbali na huenda wakawa wenye kushikilia dini, wakihudhuria ibada zao kwa ukawaida na kujaribu kutimiza matakwa ya ibada yao. Lakini, wao si wahubiri wa ujumbe wa Ufalme. Hawana ujuzi sahihi wa kwamba huu ndio “wakati wa mwisho” na hawana uharaka wowote kuhusu siku hizi tunamoishi.—Danieli 12:4.

5. Kama hangaiko letu kubwa limekuwa kufuatia mambo ya kawaida ya maisha, tunapaswa kufanya nini?

5 Yesu Kristo alisema hivi kuhusu nyakati zetu zenye hatari: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. Kwa maana kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya furiko, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiozwa, hadi siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka furiko likaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Mathayo 24:37-39) Hakuna ubaya wowote wa kula na kunywa ikiwa kunafanywa kwa kiasi, na ndoa ni mpango ulioanzishwa na Mungu mwenyewe. (Mwanzo 2:20-24) Lakini tukitambua kwamba hangaiko letu kubwa limekuwa kufuatia mambo ya kawaida ya maisha, kwa nini tusisali juu ya jambo hilo? Yehova anaweza kutusaidia kutanguliza mambo ya Ufalme, kufanya yaliyo sawa, na kutimiza wajibu wetu kwake.—Mathayo 6:33; Waroma 12:12; 2 Wakorintho 13:7.

Wakfu na Wajibu Wetu kwa Mungu

6. Watu fulani waliobatizwa hushindwa kutimiza wajibu wao kwa Mungu katika njia gani muhimu?

6 Wakristo wengine waliobatizwa wanahitaji kusali kwa bidii kwa sababu hawaishi kwa kupatana na wajibu wa huduma ambao walijitwika walipojiweka wakfu kwa Mungu. Kwa miaka kadhaa sasa zaidi ya watu 300,000 wamekuwa wakibatizwa kila mwaka, lakini jumla ya Mashahidi wa Yehova ambao ni watendaji iko chini kwa kulinganishwa na idadi ya hao wanaobatizwa. Wengine ambao walikuwa wahubiri wa Ufalme wameacha kutangaza habari njema. Lakini, ni lazima watu washiriki ifaavyo katika huduma ya Kikristo kabla ya kubatizwa. Kwa hiyo wanajua agizo ambalo Yesu aliwapa wafuasi wake: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Ila tu wawe na matatizo ya kipekee sana ya kiafya au mambo mengine ambayo yanashinda uwezo wao, watu waliobatizwa ambao hawaendelei kutumikia wakiwa Mashahidi watendaji wa Mungu na wa Kristo, hawaishi kwa kupatana na wajibu wao wote kwa Muumba wetu Mtukufu.—Isaya 43:10-12.

7. Kwa nini twapaswa kukutana pamoja kwa ukawaida kwa ajili ya ibada?

7 Israeli la kale ni taifa lililojiweka wakfu kwa Mungu, na kulingana na agano la Sheria, watu wake walikuwa na wajibu mbele za Yehova. Kwa mfano, wanaume wote walipaswa kukusanyika kwa ajili ya sherehe tatu za kila mwaka, na mtu ambaye hakushika kimakusudi Sikukuu ya Kupitwa ‘alikatiliwa mbali,’ afe. (Hesabu 9:13; Mambo ya Walawi 23:1-43; Kumbukumbu la Torati 16:16) Ili watimize wajibu wao kwa Mungu wakiwa watu wake waliojiweka wakfu, Waisraeli walipaswa kukusanyika kwa ajili ya ibada. (Kumbukumbu la Torati 31:10-13) Hakuna sehemu ya Sheria iliyosema, ‘Fanya hivyo ikiwa hali zinakufaa.’ Kwa wale ambao sasa wamejiweka wakfu kwa Yehova, kwa hakika kukusanyika kwa ajili ya ibada kwakazia maneno ya Paulo: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Naam, kukusanyika kwa ukawaida na waamini wenzetu ni sehemu ya wajibu kwa Mungu wa Mkristo aliyejiweka wakfu.

Pima Maamuzi Yako kwa Uangalifu!

8. Kwa nini kijana aliyejiweka wakfu anapaswa kufikiria kwa sala utumishi wake mtakatifu?

8 Labda wewe ni kijana ambaye amejiweka wakfu kwa Yehova. Utapata baraka tele ukitanguliza daima masilahi ya Ufalme maishani. (Mithali 10:22) Kwa kusali na kupanga mambo kwa uangalifu, unaweza kutumia angalau miaka ya ujana wako katika utumishi fulani wa wakati wote—njia nzuri ya kuonyesha kwamba unamkumbuka Muumba wako Mtukufu. La sivyo, mapendezi ya mambo ya kimwili huenda yakaanza kuchukua muda wako mwingi na fikira zako. Kama watu kwa ujumla, huenda ukafunga ndoa mapema maishani na kuwa na madeni ili upate vitu vya kimwili. Kazi yenye ufanisi yaweza kuchukua wakati wako mwingi na nguvu zako. Ikiwa una watoto, utalazimika kubeba madaraka ya familia kwa miaka mingi. (1 Timotheo 5:8) Labda hutakuwa umemsahau Muumba wako Mtukufu, lakini ni hekima kutambua kwamba kupangia mambo mapema, au kutoyapangia, kwaweza kuamua maisha yako yatakuwaje ukiwa mtu mzima. Katika miaka ya baadaye, unaweza kufikiria yaliyopita na kutamani kwamba laiti ungalitumia angalau maisha yako ya ujana kikamili zaidi katika utumishi mtakatifu kwa Muumba wetu Mtukufu. Mbona usiyafikirie matazamio yako kwa sala sasa, ili upate uradhi katika utumishi wako mtakatifu kwa Yehova katika miaka yako ya ujana?

9. Ni jambo gani linalowezekana kwa mtu ambaye amezidi kuzeeka na ambaye pindi moja alikuwa na madaraka mazito kutanikoni?

9 Ebu fikiria hali nyinginezo—hali ya mtu ambaye pindi moja alitumikia akiwa mchungaji wa “kundi la Mungu.” (1 Petro 5:2, 3) Kwa sababu fulani, yeye aliacha kwa hiari mapendeleo hayo. Ni kweli kwamba sasa amezidi kuzeeka, na huenda ikawa vigumu kwake kuendelea kufanya utumishi wa Mungu. Lakini, je, yeye anapaswa kufikia tena mapendeleo ya kitheokrasi? Mtu kama huyo anaweza kuwa baraka iliyoje kwa wengine ikiwa anaweza kuwa na madaraka zaidi kutanikoni! Na kwa kuwa hakuna mtu anayeishi kwa ajili yake mwenyewe tu, marafiki na wapendwa watafurahi kwamba yeye ameweza kuongeza utumishi wake, kwa utukufu wa Mungu. (Waroma 14:7, 8) Zaidi ya yote, Yehova hatasahau kile ambacho mtu yeyote anafanya katika utumishi wake. (Waebrania 6:10-12) Basi, ni nini kinachoweza kutusaidia kumkumbuka Muumba wetu Mtukufu?

Mambo Yanayotusaidia Kumkumbuka Muumba Wetu Mtukufu

10. Kwa nini mhubiri alikuwa na uwezo wa kuandaa miongozo kuhusu suala la kumkumbuka Muumba wetu Mtukufu?

10 Mhubiri alikuwa na uwezo wa kuandaa miongozo ya kumkumbuka Muumba wetu Mtukufu. Yehova alikuwa amejibu sala yake ya kutoka moyoni kwa kumpa hekima nyingi sana. (1 Wafalme 3:6-12) Solomoni alichunguza sana mambo yanayohusu masuala yote ya wanadamu. Isitoshe, yeye alipuliziwa na Mungu aandike mambo aliyoyapata ili awanufaishe watu wengine. Aliandika hivi: “Walakini, kwa sababu huyo mhubiri alikuwa na hekima, aliendelea kuwafundisha watu maarifa, naam, akatafakari, akatafuta-tafuta, akatunga mithali nyingi. Huyo Mhubiri akatafuta-tafuta ili apate kuona maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.”—Mhubiri 12:9, 10.

11. Kwa nini tunapaswa kukubali mashauri ya Solomoni yenye hekima?

11 Katika Septuagint ya Kigiriki maneno hayo yametafsiriwa kama ifuatavyo: “Na zaidi, kwa sababu mhubiri alikuwa mwenye hekima, kwa sababu alifundisha wanadamu hekima; ili sikio liweze kusikia maneno yenye kupendeza kutokana na mifano, mhubiri alitafuta kwa bidii maneno yapendezayo na maandishi ya unyofu—maneno ya kweli.” (The Septuagint Bible, iliyotafsiriwa na Charles Thomson) Solomoni alijaribu kufikia mioyo ya wasomaji wake kwa maneno yapendezayo na kwa mambo ambayo kweli yalivutia na kufaa. Kwa kuwa alipuliziwa na roho takatifu kuandika maneno yanayopatikana katika Maandiko, twaweza kukubali mara moja matokeo ya uchunguzi wake na mashauri yake yenye hekima.—2 Timotheo 3:16, 17.

12. Kwa maneno yako mwenyewe, unaweza kuelezaje maneno ya Solomoni katika Mhubiri 12:11, 12?

12 Hata bila mbinu za kisasa za uchapishaji, kulikuwa na vitabu vingi katika siku za Solomoni. Fasihi kama hizo zilipasa kuonwaje? Yeye alisema: “Maneno yao wenye hekima huwa mfano wa michokoro; na kama misumari iliyogongomewa sana; ndivyo yalivyo maneno yao walio wakuu wa makusanyiko [“mikusanyo ya maneno,” NW], ambayo yatoka kwa mchungaji mmoja. Tena, zaidi ya hayo, mwanangu, kubali maonyo; hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi; na kusoma sana huuchosha mwili.”—Mhubiri 12:11, 12.

13. Maneno ya wale ambao wana hekima ya kimungu yanawezaje kuwa kama michokoro, na ni nani walio kama ‘misumari inayogongomewa sana’?

13 Maneno ya wale wenye hekima ya kimungu huwa kama michokoro. Kwa njia gani? Hayo huwachochea wasomaji au wasikilizaji wafanye maendeleo kwa kupatana na maneno yenye hekima yanayosomwa au kusikizwa. Pia wale ambao wanajishughulisha mno na “mikusanyo ya maneno,” au maneno ambayo kwa kweli ni yenye hekima na yanafaa, ni kama ‘misumari inayogongomewa sana,’ au inayopigiliwa kabisa. Huenda ikawa hivyo kwa sababu maneno mema ya watu hao yanaonyesha hekima ya Yehova na basi yanaweza kuwategemeza wasomaji au wasikilizaji na kuwafanya wawe thabiti. Ikiwa wewe ni mzazi anayemcha Mungu, je, hupaswi kufanya jitihada nyingi za kukazia kikiki hekima kama hiyo katika akili na moyo wa mtoto wako?—Kumbukumbu la Torati 6:4-9.

14. (a) Hainufaishi “kusoma sana” vitabu vya aina gani? (b) Tunapaswa kuzingatia sana fasihi gani, na kwa nini?

14 Lakini, kwa nini Solomoni aseme hivyo kuhusu vitabu? Kwa kulinganisha na Neno la Yehova, vitabu vingi sana vya ulimwengu huu vina fikira za wanadamu tu. Vingi vinaonyesha fikira za Shetani Ibilisi. (2 Wakorintho 4:4) Kwa hiyo, hakuna manufaa ya kudumu ya ‘kuvisoma sana’ vitabu hivyo vya kilimwengu. Vingi vya vitabu hivyo hata vinaweza kudhuru kiroho. Kama Solomoni, na tutafakari yale ambayo Neno la Mungu lisemayo kuhusu uhai. Kufanya hivyo kutaimarisha imani yetu na kutufanya tuwe karibu zaidi na Yehova. Kuvisoma sana vitabu vingine au mafundisho mengine kunaweza kutuchosha sana. Hasa kama maandishi hayo yanatokana na kusababu kwa kilimwengu ambako kunahitilafiana na hekima ya kimungu basi hayafai na yanaweza kuharibu imani katika Mungu na makusudi yake. Basi, na tukumbuke kwamba maandishi mengi yenye kunufaisha katika siku za Solomoni na katika siku zetu ni yale yaonyeshayo hekima ya “mchungaji mmoja,” Yehova Mungu. Ameandaa vitabu 66 vya Maandiko Matakatifu, na tunapaswa kuvizingatia sana. Biblia na vichapo vyenye msaada vya ‘mtumwa mwaminifu’ hutuwezesha kupata ‘kumjua Mungu.’—Mithali 2:1-6.

Wajibu Wetu Wote kwa Mungu

15. (a) Unaweza kuelezaje maneno ya Solomoni kuhusu “wajibu wote wa mwanadamu”? (b) Ni lazima tufanye nini ili tutimize wajibu wetu kwa Mungu?

15 Akijumlisha uchunguzi wake wote, mhubiri, Solomoni, asema: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu [“ndiyo wajibu wote wa mwanadamu,” NW]. Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.” (Mhubiri 12:13, 14) Kumcha au kumstahi Muumba wetu Mtukufu kwa njia ifaayo, kutatulinda, na twatumaini kutalinda familia zetu pia, tusifuate mwenendo wa kipumbavu wa maisha ambao unaweza kutuletea sisi na wapendwa wetu matatizo mengi na huzuni nyingi. Kicho kifaacho cha Mungu ni safi na ndicho mwanzo wa hekima na ujuzi. (Zaburi 19:9; Mithali 1:7) Tukiwa na ufahamu wa ndani wa Neno la Mungu lililopuliziwa na kutumia mashauri yake katika mambo yote, tutatimiza “wajibu [wetu] wote” kwa Mungu. Kufanya hivyo hakumaanishi kuorodhesha wajibu mbalimbali. Badala yake, inatakikana tuchunguze Maandiko tunapotatua matatizo ya maisha na sikuzote kufanya mambo kwa njia ya Mungu.

16. Kuhusu hukumu, Yehova atafanya nini?

16 Tunapaswa kutambua kwamba hakuna jambo ambalo Muumba wetu Mtukufu hawezi kuona. (Mithali 15:3) Yeye “ataleta hukumuni kila kazi.” Ndiyo, Aliye Juu Zaidi atahukumu mambo yote, hata yale ambayo hayaonekani kwa macho ya wanadamu. Kujua mambo hayo kwaweza kutuchochea tutii amri za Mungu. Lakini kichocheo kikubwa zaidi chapaswa kuwa upendo wetu kwa Baba yetu wa kimbingu, kwa kuwa mtume Yohana aliandika: “Kwa maana hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.” (1 Yohana 5:3) Na kwa kuwa amri za Mungu zimekusudiwa ziendeleze hali-njema yetu ya milele, kwa hakika ni jambo linalofaa na hata lenye hekima kuzitimiza. Huo si mzigo kwa wapendao Muumba Mtukufu. Wanataka kutimiza wajibu wao kwake.

Timiza Wajibu Wako Wote

17. Tutafanya nini ikiwa kwa kweli tunataka kutimiza wajibu wetu wote kwa Mungu?

17 Ikiwa sisi ni wenye hekima na kwa kweli tunatamani kutimiza wajibu wetu wote kwa Mungu, mbali na kuzishika amri zake, tutakuwa na hofu yenye staha ya kutompendeza. Kwa kweli, “kumcha BWANA ndio mwanzo wa hekima,” na wale wanaozishika amri zake wana “akili njema.” (Zaburi 111:10; Mithali 1:7) Basi na tuendelee kutenda kwa hekima na kumtii Yehova katika mambo yote. Na ni muhimu sana sasa kufanya hivyo, kwa kuwa Mfalme Yesu Kristo yupo, na siku yake ya hukumu akiwa Hakimu aliyewekwa na Mungu imekaribia.—Mathayo 24:3; 25:31, 32.

18. Tutapata matokeo gani tukitimiza wajibu wetu wote kwa Yehova Mungu?

18 Kila mmoja wetu sasa anachunguzwa na Mungu. Je, tuna mtazamo wa kiroho, ama tumeruhusu uvutano wa kilimwengu udhoofishe uhusiano wetu pamoja na Mungu? (1 Wakorintho 2:10-16; 1 Yohana 2:15-17) Tuwe vijana au wazee, na tufanye yote tuwezayo ili tumpendeze Muumba wetu Mtukufu. Tukimtii Yehova na kuzishika amri zake, tutakataa mambo ya ubatili ya ulimwengu huu wa kale unaopitilia mbali. Ndipo tunapoweza kuwa na tumaini la uhai udumuo milele katika mfumo mpya wa Mungu ambao aliahidi. (2 Petro 3:13) Hayo ni matazamio mazuri ajabu kama nini kwa wale wote wanaotimiza wajibu wao wote kwa Mungu!

Ungejibuje?

◻ Kwa nini unaweza kusema kwamba mambo yote si ubatili?

◻ Kwa nini kijana Mkristo anapaswa kufikiria kwa sala utumishi wake mtakatifu?

◻ Ni vitabu vya aina gani ambavyo hatupaswi “kusoma sana”?

◻ “Wajibu wote wa mwanadamu” ni nini?

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mambo yote si ubatili kwa wale wanaomtumikia Yehova

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tofauti na vitabu vingi katika ulimwengu huu, Neno la Mungu linaburudisha na lanufaisha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki