Sababu kwa Nini Unahitaji Kuhudhuria Mikutano ya Kikristo
KWA miezi kadhaa, Rosario, aishiye Amerika Kusini, alifurahia kujifunza Biblia pamoja na Elizabeth. Rosario alisisimuka kujifunza juu ya Ufalme wa Mungu na jinsi utakavyoleta hali za Paradiso duniani. Lakini, wakati wowote Elizabeth alipomwalika kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme, alikataa. Alihisi kwamba angeweza kujifunza Biblia nyumbani na kuzoea yale inayosema, akifanya hivyo bila kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Je! wewe pia umejiuliza kama kwa kweli mikutano ya Kikristo inakunufaisha? Kwa nini Mungu hupanga ili watu wake wakutane pamoja?
Kwa kuwa Wakristo katika karne ya kwanza walikuwa tofauti sana na watu waliowazunguka, ushirika ufaao ulikuwa muhimu kwa wokovu wao. Mtume Paulo aliandikia hivi kutaniko moja la Wakristo wa mapema: ‘Mlikuja kuwa bila lawama na wasio na hatia miongoni mwa kizazi kilichopotoka na kilicho kombo, ambacho miongoni mwacho mnang’aa mkiwa wamulikaji ulimwenguni.’ (Wafilipi 2:15, NW) Wakristo walikuwa na wakati mgumu hasa katika Yudea, na Paulo aliandika hivi kwao: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Tunahimizanaje katika upendo na kazi nzuri kwa kukutana pamoja?
Jinsi Wakristo ‘Wanavyonoana’
Neno la Kigiriki ambalo Paulo alitumia na linalotafsiriwa ‘himiza’ lamaanisha kihalisi “kunolewa.” Mithali ya Biblia yaeleza jinsi Wakristo ‘wanavyonoana’ inaposema: “Chuma hunoa chuma; ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.” (Mithali 27:17; Mhubiri 10:10) Sisi ni kama vyombo vinavyohitaji kunolewa kwa ukawaida. Kwa kuwa kuonyesha upendo kwa Yehova na kufanya maamuzi yenye msingi wa imani yetu kunamaanisha kuwa tofauti na ulimwengu, tunahitaji daima kufuata mwendo ulio tofauti na ule unaofuatwa na wengi.
Jitihada ya daima ya kuwa tofauti yaweza kutia butu bidii yetu kwa ajili ya kazi nzuri. Lakini tunapokuwa na wengine wanaompenda Yehova, tunanoana—tunahimizana katika upendo na kazi nzuri. Kwa upande ule mwingine, tunapokuwa peke yetu, tunaelekea kujifikiria zaidi. Huenda mawazo yasiyo ya kiadili, yenye ubinafsi, au ya kipumbavu yakaingia katika akili zetu. “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; hushindana na kila shauri jema.” (Mithali 18:1) Ndiyo sababu Paulo aliandikia kutaniko katika jiji la Thesalonike hivi: “Farijianeni na kujengana kila mtu na mwenzake, vile vile kama mnavyofanya.”—1 Wathesalonike 5:11.
Rosario alipomaliza funzo lake la mafundisho ya Biblia ya msingi, bado alisita kushirikiana na kutaniko. Kwa hiyo, aliposhindwa kuandaa msaada zaidi, Elizabeth aliacha kumtembelea. Miezi kadhaa baadaye mwangalizi asafiriye alimtembelea Rosario na kuuliza hivi: “Hata ikiwa kila mshiriki wa familia angeweza kupata chakula kizuri kwa kula katika mkahawa, washiriki wote wangekosa jambo gani kwa kutokula pamoja nyumbani?” Rosario akajibu: “Wangekosa ushirikiano wa familia.” Alielewa jambo hilo, akaanza kuja kwenye mikutano kwa ukawaida. Aliona hilo kuwa lenye kunufaisha sana hivi kwamba amekuwa kwenye karibu kila mkutano tangu wakati huo.
Kuwasikia watu wengine wakieleza imani yao katika mambo yaleyale unayoamini ni kitia-moyo na ndivyo ilivyo unapoona jinsi imani hiyo imebadili maisha zao. Paulo alijionea hayo kibinafsi, na aliandikia kutaniko katika Roma hivi: “Ninatamani sana kuwaona, nipate kuwapa karama ya rohoni, ili mfanywe imara; yaani, tufarijiane mimi na ninyi, kila mtu kwa imani ya mwenzake, yenu na yangu.” (Warumi 1:11, 12) Kwa kweli, ilichukua miaka mingi kabla ya Paulo kuweza kwenda Roma, na alipofanya hivyo, alikuwa mfungwa mikononi mwa Waroma. Lakini alipowaona ndugu kutoka Roma waliokuwa wametembea mwendo wa kilometa zaidi ya 60 kutoka jijini ili kukutana naye, Paulo “alimshukuru Mungu, akachangamka.”—Matendo 28:15.
Kupata Chakula cha Kiroho Katika Nyakati za Hatari
Alipokuwa katika kifungo cha nyumbani katika Roma, Paulo aliwaandikia Waebrania juu ya kutoacha kukutana pamoja. Ni jambo la maana kwetu kwamba aliongeza maneno haya: “Na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:25) Mashahidi wa Yehova wameonyesha kwa upatano kutoka katika Maandiko kwamba mwaka 1914 ulitia alama mwanzo wa wakati wa mwisho wa ulimwengu huu na kwamba “siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu” imekaribia. (2 Petro 3:7) Kulingana na kitabu cha Biblia cha Ufunuo, Ibilisi alipotupwa kutoka mbinguni mwanzoni mwa wakati wa mwisho, alikuwa amekasirika sana “akaenda zake afanye vita juu ya . . . waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.” (Ufunuo 12:7-17) Kwa hiyo, kushika amri za Mungu ni jambo gumu hasa wakati huu; tunahitaji kuzidi kukutana na waamini wenzetu. Mikutano itatusaidia tuimarishe imani yetu na upendo wetu kwa Mungu ili kukinza mashambulio ya Ibilisi.
Upendo wa Mungu na imani si kama majengo yanayodumu mara yanapojengwa. Bali, ni kama vitu vyenye uhai vinavyokua polepole kwa kulishwa daima lakini vinavyonyauka na kufa vikinyimwa chakula. Hiyo ndiyo sababu Yehova huandaa chakula cha kiroho kwa ukawaida ili kuwaimarisha watu wake. Sisi sote tunahitaji chakula hicho, lakini tunaweza kukipata wapi isipokuwa kutoka katika tengenezo la Mungu na mikutano yalo? Hakuna kwingine.—Kumbukumbu la Torati 32:2; Mathayo 4:4; 5:3.
Yesu aliuliza swali linaloweza kutusaidia tuone jinsi anavyolisha kutaniko la Kikristo. Aliuliza hivi: “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo.” (Mathayo 24:45, 46) Yesu alimweka nani katika karne ya kwanza awalishe wafuasi wake, na alipata nani akiwalisha kwa uaminifu aliporudi katika mamlaka ya Ufalme? Bila shaka, hakuna binadamu yeyote ambaye ameishi kupitia muda wa karne hizo zote. Ushuhuda unaonyesha mtumwa huyo kuwa kutaniko la Wakristo wapakwa kwa roho, kama vile taifa la Israeli lilivyokuwa mtumishi wa Mungu katika nyakati za kabla ya Ukristo. (Isaya 43:10) Naam, Yesu huandaa chakula chetu cha kiroho kupitia baraza hilo la ulimwenguni pote la Wakristo wapakwa kwa roho, ambalo leo hutoa chakula cha kiroho kupitia makutaniko ya mahali-mahali ya Mashahidi wa Yehova.
Uandalizi wa Yesu wa njia ya kutoa chakula cha kiroho ulisimuliwa zaidi na mtume Paulo: “Alipopaa juu aliteka mateka, akawapa wanadamu vipawa [zawadi katika wanadamu, NW]. . . . Naye alitoa wengine kuwa mitume; na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti; na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo.”—Waefeso 4:8, 11-13.
Ni katika makutaniko ya mahali-mahali hasa—kwenye mikutano—kwamba “zawadi [hizo] katika wanadamu” waliwajenga ndugu. Kwa kielelezo, katika Antiokia, “Yuda na Sila, kwa kuwa wao wenyewe walikuwa manabii pia, waliwatia moyo ndugu kwa hotuba nyingi na kuwaimarisha.” (Matendo 15:32, NW) Vivyo hivyo hotuba zinazotolewa leo na wanaume wenye sifa za kustahili kiroho zitaimarisha imani yetu ili isinyauke au kuacha kutenda.
Huenda ikawa kweli kwamba tumefanya maendeleo mazuri kwa sababu ya msaada wa kibinafsi kutoka kwa mshiriki mmoja wa kutaniko hata ingawa huenda ikawa hatujaanza kuhudhuria mikutano bado. Biblia husema kwamba kuna wakati ‘unapohitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; na unakuwa unahitaji maziwa wala si chakula kigumu.’ (Waebrania 5:12) Lakini mtu hawezi kuendelea na maziwa milele. Mikutano ya Kikristo huandaa programu ya kuendelea ya maagizo ya Biblia yanayokusudiwa kudumisha upendo wa Mungu na imani katika yeye zikiwa hai na pia kuandaa msaada wenye mafaa katika kutumia “shauri lote la Mungu.” (Matendo 20:27, NW) Hayo si “maziwa” tu. Biblia huendelea kusema hivi: “Chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” (Waebrania 5:14) Habari nyingi huzungumziwa kwenye mikutano ambazo huenda zisiwe sehemu ya masomo ya msingi ya mafunzo ya Biblia nyumbani, kama vile mafunzo ya mstari kwa mstari ya unabii mbalimbali wa Biblia wenye maana na mazungumzo yenye kina kirefu ya jinsi tunavyoweza kumwiga Mungu katika maisha zetu wenyewe.
Vikumbusho vya Yehova —Kama Sauti Iliyo Nyuma Yako
Kupitia mafunzo hayo ya kutaniko, Yehova hutukumbusha kwa ukawaida juu ya namna ya watu tunaopaswa kuwa. Vikumbusho hivyo ni muhimu. Bila hivyo tunaelekea kwa urahisi kuwa wenye ubinafsi, wenye kiburi, na wenye pupa. Vikumbusho kutoka kwa Maandiko vitatusaidia tufurahie mahusiano yenye mafanikio pamoja na wanadamu wengine na pamoja na Mungu mwenyewe. “Nalizitafakari njia zangu, na miguu yangu nalizielekezea shuhuda zako [vikumbusho vyako, NW],” akaungama mwandishi wa Zaburi 119:59.
Tunapohudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, tunajionea wenyewe utimizo wa unabii wa Yehova kupitia Isaya, usemao hivi: “Mfunzi Mtukufu wenu hatajificha mwenyewe tena, na ni lazima macho yenu yawe macho yanayoona Mfunzi Mtukufu wenu. Na masikio yenu wenyewe yatasikia neno nyuma yenu likisema: ‘Njia ni hii. Itembeeni, enyi watu.’” Yehova hutazama maendeleo yetu na kutusahihisha kwa upendo tukichukua hatua isiyo sahihi. (Isaya 30:20, 21, NW; Wagalatia 6:1) Na yeye huandaa msaada zaidi ya hiyo.
Kupokea Roho Takatifu Kupitia Kutaniko
Kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida pamoja na Mashahidi wa Yehova, tunaimarishwa na roho takatifu ya Mungu, iliyo juu ya watu wake. (1 Petro 4:14) Zaidi ya hayo, waangalizi Wakristo katika kutaniko wamewekwa na roho takatifu. (Matendo 20:28) Hiyo kani ya utendaji kutoka kwa Mungu ina uvutano wenye nguvu juu ya Mkristo. Biblia husema: “Tunda la roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” (Wagalatia 5:22, 23, NW) Roho takatifu, ikifanya kazi kupitia tengenezo la Mungu, itatusaidia pia tupate uelewevu wa wazi ajabu juu ya yale ambayo Yehova amewawekea wale wampendao. Baada ya kueleza kwamba watu mashuhuri wa mfumo huu wa mambo hawawezi kuelewa makusudi ya Mungu, Paulo aliandika hivi: “Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho [roho yake, NW].”—1 Wakorintho 2:8-10.
Zaidi ya chakula cha kiroho chenye kuimarisha imani, kutaniko huandaa mazoezi kwa wale wanaotaka kushiriki katika utendaji mkuu wa kutaniko. Huo ni upi?
Mazoezi Yanayoandaliwa na Kutaniko
Kutaniko la Kikristo si klabu ya kijamii ambamo watu hufurahia vitumbuizo tu na labda kutiana moyo kuishi maisha bora zaidi. Yesu aliagiza kutaniko lipeleke habari njema za Ufalme kwa wale wanaoishi katika giza la kiroho. (Matendo 1:8; 1 Petro 2:9) Tangu siku lilipoundwa, katika Pentekoste 33 W.K., lilikuwa tengenezo la wahubiri. (Matendo 2:4) Je! umepata kuwa na ono la kujaribu kumwambia mtu fulani juu ya makusudi ya Yehova lakini ukashindwa kumsadikisha? Mikutano ya kutaniko huandaa mazoezi ya kibinafsi katika ufundi wa kufundisha. Kwa kujifunza vielelezo vya Biblia, tunajifunza jinsi ya kusitawisha msingi wa kuwa na ukubaliano tunaoweza kutumia ili kutoa sababu, jinsi ya kutumia Maandiko yakiwa msingi wa hoja yenye kupatana na akili, na jinsi ya kuwasaidia wengine watoe sababu kwa kutumia maswali na vielezi. Stadi za jinsi hiyo zaweza kukusaidia upate kuona ile shangwe isiyoelezeka ya kumsaidia mtu mwingine aelewe kweli ya Biblia.
Katika ulimwengu huu uliogawanywa na mzozo, na usio na adili, kutaniko la Kikristo ni kimbilio la kiroho la kweli. Hata ingawa lina watu wasio wakamilifu, ni kituo cha amani na upendo. Kwa hiyo, uwe mhudhuriaji wa kawaida kwenye mikutano yalo yote na upate kujionea mwenyewe ukweli wa maneno haya ya mtunga zaburi: “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja. . . . BWANA [Yehova, NW] alikoamuru baraka, naam, uzima hata milele.”—Zaburi 133:1, 3.