Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 8/15 kur. 4-7
  • Namna ya Kuimarisha Vifungo vya Ndoa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Namna ya Kuimarisha Vifungo vya Ndoa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uandalizi wa Sheria ya Kimusa
  • Msingi Halali wa Pekee wa Talaka
  • Mbegu za Matatizo ya Familia Zapandwa
  • Zungumzia Matatizo
  • Talaka Biblia Inasema Nini Hasa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Maisha ya Jamaa—Namna Unavyoweza Kufanikiwa
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Kujitahidi Kufanya Maendeleo Katika Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Heshimu “Kile Ambacho Mungu Ameunganisha”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 8/15 kur. 4-7

Namna ya Kuimarisha Vifungo vya Ndoa

“JE! NI halali mtu kumwacha mkewe kwa kila sababu?” wakauliza Mafarisayo waliokuwa wakijaribu kumnasa Mfundishaji Mkuu, Yesu Kristo. Aliwajibu kwa kurejezea ndoa ya kwanza ya kibinadamu akaweka kiwango juu ya jambo hilo: “Aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.”

Mafarisayo walibisha kwamba Musa alikuwa amefanya maandalizi ya talaka kwa kuagiza kwamba “hati ya talaka” itolewe. Yesu akawajibu hivi: “Musa, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu, aliwapa ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi. Nami nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa azini.”—Mathayo 19:3-9.

Mwanzoni, ndoa ilipaswa iwe kifungo cha kudumu. Hata kifo kisingaliwatenganisha mume na mke wa kwanza, kwani waliumbwa wakiwa wanadamu wakamilifu wenye tumaini la uhai wa milele. Hata hivyo, walitenda dhambi. Dhambi yao iliharibu ndoa ya kibinadamu. Yule adui kifo akaanza kuwatenganisha waume na wake zao. Mungu huona kifo kuwa mwisho wa ndoa, kama tusomavyo katika Biblia: “Mwanamke hufungwa maadamu mumewe yu hai, lakini ikiwa mumewe amefariki, yu huru kuolewa na mtu ye yote amtakaye; katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Hilo ni tofauti sana na mawazo ya kidini kama vile desturi ya mjane wa kihindu, ambayo wakati wa kifo cha mume wake, mke anashawishwa au kushurutishwa ajiteketeze hadi kifo kwa kuamini kwamba kifungo cha ndoa huendelea kwenye maisha ya baadaye.

Uandalizi wa Sheria ya Kimusa

Kufikia wakati Sheria ya Kimusa ilipotolewa, mahusiano ya ndoa yalikuwa yamezorota sana kufikia hatua ambapo Yehova, kwa sababu ya ugumu wa mioyo ya Waisraeli, alifanya uandalizi wa talaka. (Kumbukumbu la Torati 24:1) Mungu hakukusudia Waisraeli watumie vibaya sheria hiyo ili wataliki wake zao kwa sababu ya kasoro ndogo-ndogo, kama inavyoonekana wazi katika amri yake kwamba walipaswa kumpenda jirani yao kama nafsi zao. (Mambo ya Walawi 19:18) Hata kutoa hati ya talaka kulikuwa kizuizi kwa sababu, hatua moja ya kuandika hati hiyo ilikuwa kwamba, yule mume aliyetaka talaka angalipaswa awaendee wanaume wenye mamlaka ya haki, ambao wangalijaribu sana kupatanisha mambo. La, Mungu hakutoa sheria hiyo ili kusitawisha haki yoyote ya mtu kumtaliki mke wake “kwa kila sababu.”—Mathayo 19:3.

Hata hivyo, hatimaye Waisraeli walipuuza kusudi na maana halisi ya sheria, wakatumia kwa ubinafsi kifungu hicho cha maneno ili kutaliki kwa msingi wowote waliopenda. Kufikia karne ya tano K.W.K., walikuwa wakiwatenda wake wa ujana wao mambo ya hiana wakiwataliki kwa kila sababu. Yehova aliwaambia kwa uthabiti kwamba alichukia kutaliki. (Malaki 2:14-16) Hiyo ndiyo hali ambamo Yesu alilaumu talaka kama ilivyokuwa ikizoewa na Waisraeli katika siku yake.

Msingi Halali wa Pekee wa Talaka

Lakini, Yesu alitaja msingi mmoja halali wa talaka: uasherati. (Mathayo 5:31, 32; 19:8, 9) Neno linalotafsiriwa hapa kuwa “uasherati” latia ndani kufanya aina yoyote ya ngono haramu nje ya ndoa ya Kimaandiko, iwe ni pamoja na mtu wa jinsia moja au wa jinsia nyingine au pamoja na mnyama.

Hata hivyo, Yesu hakuwa akipendekeza kwamba watu wataliki wenzi wasio waaminifu. Ni uamuzi wa mwenzi asiye na hatia kupima matokeo yanayohusika na kuamua kama yeye ataka talaka. Wake wanaofikiria talaka kwa msingi huo wa Kimaandiko huenda pia wakataka kufikiria taarifa ya Mungu alipomhukumu mwanamke wa kwanza kwa ajili ya dhambi yake. Kuongezea hukumu ya kifo, Mungu alimwambia Hawa kimahususi: “Tamaa yako [uchu wako, New World Translation] itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala.” (Mwanzo 3:16) Commentary on the Old Testament, ya C. F. Keil na F. Delitzsch, inaeleza “uchu” huo kuwa “tamaa iliyo kama ugonjwa.” Kwa kweli, uchu huo si wenye nguvu hivyo katika kila mke, lakini mke asiye na hatia anapofikiria talaka, angekuwa na hekima kufikiria mahitaji ya hisia za moyoni ambayo wanawake wamerithi kutoka kwa Hawa. Hata hivyo, kwa kuwa ngono ya nje ya ndoa kwa upande wa mwenzi mwenye hatia ingeweza kumsababisha mwenzi asiye na hatia aambukizwe magonjwa ya kupitishwa kingono, kutia na UKIMWI, wengine wameamua kutaliki kama vile Yesu alivyoeleza.

Mbegu za Matatizo ya Familia Zapandwa

Msingi wa ugumu wa mioyo ya watu ni dhambi ambayo mume na mke wa kwanza wa kibinadamu walitenda dhidi ya Mungu. (Warumi 5:12) Mbegu za ugomvi wa familia zilipandwa wakati mume na mke wa kwanza wa kibinadamu walipotenda dhambi dhidi ya Baba yao wa kimbingu. Kwa jinsi gani? Mwanamke wa kwanza, Hawa, aliposhawishwa na nyoka ale kutoka mti uliokatazwa, alikula tunda hilo moja kwa moja. Ni baada tu ya kufanya uamuzi huo mkubwa kwamba aliongea na mume wake juu ya yale ambayo nyoka alikuwa amemwambia. (Mwanzo 3:6) Naam, alikuwa ametenda bila kushauriana na mume wake. Hicho ndicho chanzo cha matatizo yanayokabiliwa na familia nyingi leo—ukosefu wa uwasiliano wa kinagaubaga.

Baadaye, walipokabiliwa na matokeo ya dhambi yao, Adamu na Hawa pia walitumia mbinu zilezile zinazotumiwa na waume na wake wengi leo wanapokuwa taabani, yaani, kulaumiana. Mwanamume wa kwanza, Adamu, alimlaumu mke wake na Yehova pia kwa lile alilokuwa amefanya, kwa kusema: “Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala.” Mwanamke naye akasema: “Nyoka alinidanganya, nikala.”—Mwanzo 3:12, 13.

Hukumu ya Yehova juu ya Adamu na Hawa ilitabiri chanzo kingine zaidi cha matatizo ambayo yangetokea. Kuhusu uhusiano wake na mume wake, Yehova alimwambia Hawa hivi: “Atakutawala.” Waume wengi leo, kama vile Isao aliyetajwa katika makala yetu ya kwanza, wanawatawala wake zao katika njia isiyo na huruma bila kufikiria hisia za wake zao. Lakini, wake wengi wanaendelea kuwa na uchu wa kuvuta fikira za waume zao. Uchu huo usiporidhishwa, huenda wake wakadai ufikirio huo kwa lazima na kutenda kwa ubinafsi. Kwa kuwa waume wengi ni wenye kutawala na wake wengi wana uchu wa kuvuta fikira za waume zao, ubinafsi huenea, na amani kutoweka. Katika ripoti moja yenye kichwa “Namna ya Kuchanganua Talaka za Leo,” Shunsuke Serizawa alisema hivi: “Tukipuuza tatizo la msingi linalohusu suala hili, yaani, kwamba watu wana mwelekeo wa kutanguliza mapendezi yao wenyewe, kwa ghafula ingekuwa haiwezekani tena kuchanganua talaka leo.”

Hata hivyo, Yehova ameandaa mwongozo katika Neno lake ili waume na wake watiifu waweze kuonea shangwe kadiri fulani ya furaha ya ndoa hata wakiwa katika hali yao ya kutokamilika. Isao alifuata mwelekezo wa Mungu na sasa anaonea shangwe maisha ya familia yenye furaha. Acheni tuone jinsi kanuni za Biblia zinavyowasaidia watu waimarishe kifungo cha ndoa.

Zungumzia Matatizo

Katika ndoa nyingi, ukosefu wa uwasiliano, mwelekeo wa kulaumu wengine, na mitazamo ya ubinafsi hufanya iwe vigumu kwa mume na mke kuelewa hisia za moyoni za mmoja na mwenzake. “Kwa kuwa kushiriki hisia ni jambo la lazima ili kuwe na ukaribu, ukaribu unahitaji [sifa ya] kutumaini kikamili. Na leo kutumaini si [sifa ya] kawaida,” asema mtafiti Caryl S. Avery. Kwa kawaida kushirikiana hisia za ndani kabisa hujenga sifa hiyo ya kutumaini. Hilo lataka uwasiliano wa kinagaubaga kati ya mume na mke.

Kitabu cha Mithali kinatumia kielezi ili kutia moyo watu washirikiane mawazo ya ndani, ikisema hivi: “Mashauri ya moyoni ni kama kilindi; lakini mtu mwenye ufahamu atayateka.” (Mithali 20:5) Ni lazima waume na wake wawe na utambuzi na kuyavuta mawazo yaliyo ndani sana katika mioyo ya wenzi wao. Ebu wazia kwamba mwenzi wako ameudhika. Badala ya kuitikia: “Hata mimi nimekuwa na siku ngumu,” kwa nini usiulize hivi kwa fadhili: “Je! ulikuwa na siku ngumu leo? Ni nini lililotukia?” Huenda ikachukua wakati na jitihada kumsikiliza mwenzi wako, lakini kwa kawaida ni jambo lenye kupendeza zaidi, lenye kuridhisha zaidi, na lenye kuokoa wakati zaidi kutumia wakati hivyo kuliko kumpuuza mwenzi wako na kulazimika kushughulikia hasira itakayolipuka baadaye.

Ili kupata kutumainiana, ni lazima kila mmoja awe mwenye moyo mweupe na ajaribu kueleza hisia kwa njia ambayo yule mwenzi mwingine anaweza kuelewa. “Mkaseme kweli,” Neno la Mungu lahimiza, “kwa maana tu viungo, kila mmoja kiungo cha [m]wenzake.” (Waefeso 4:25) Kusema kweli kunahitaji utambuzi. Labda mke ahisi kwamba hasikiwi. Kabla ya yeye kusema, anapaswa afikirie mithali hii: “Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; na mwenye roho ya utulivu ana busara.” (Mithali 17:27) Badala ya kumshtaki mume wake, “Wewe hunisikilizi kamwe!” ingefaa zaidi kama angeeleza hisia zake kwa upole kabla ya hali ya kufadhaika na ya kukata tamaa haijaanza kusitawi ndani yake. Labda angeweza kufunua jinsi anavyohisi kwa kusema jambo kama, “Ninajua una shughuli nyingi, lakini kuwa na wakati zaidi kidogo pamoja na wewe kungenifurahisha sana.”

Kwa kweli, “pasipo mashauri makusudi hubatilika.” (Mithali 15:22) Mwenzi wako akupenda, lakini hilo halimaanishi kwamba aweza kujua unalofikiri. Ni lazima umjulishe mwenzi wako jinsi unavyohisi kwa njia ya busara. Hilo litawasaidia nyinyi, mkiwa mume na mke Wakristo, kufanya marekebisho yenye upendo ili “kuuhifadhi umoja wa Roho katika kifungo cha amani.”—Waefeso 4:2, 3.

Chukua kielelezo cha Kazuo, aliyekuwa mume mwenye kutawalwa na mke wake na aliyetamani sana kucheza kamari. Alijipata mwenyewe akiwa na madeni mengi sana yaliyojumlika kuwa dola elfu mia kadhaa. Akiwa anakopa fedha ili kulipa madeni yake, alizidi kudidimia katika tatizo hilo. Halafu alianza kujifunza Biblia na mwishoni akapata ujasiri wa kumwambia mke wake juu ya matatizo yake. Alikuwa tayari kukabili mashtaka yake. Hata hivyo, alishtuka wakati mke wake, aliyekuwa amejifunza Biblia kwa muda mrefu zaidi, aliposema kwa upole: “Acha tujaribu kuona jinsi tunavyoweza kulipa madeni haya.”

Kuanzia siku iliyofuata, waliwatembelea wadai wao wakaanza kulipa madeni yao, hata kuuza nyumba yao. Ilichukuwa karibu mwaka mmoja kulipa madeni hayo. Ni nini lililombadili Kimie, mke wake? Yeye asema hivi: “Kwa kweli maneno yanayopatikana kwenye Wafilipi sura 4, mistari 6 na 7, ni ya kweli. ‘Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.’” Aliongeza hivi: “Rafiki yangu mmoja, akishangaa kuona jinsi nilivyokuwa mwenye furaha yajapokuwa magumu, alianza kujifunza Biblia pamoja nami.” Tangu wakati huo Kazuo na mke wake wamebatizwa na sasa wanaonea shangwe maisha ya familia yenye furaha.

Kuongezea kutumainiana kwa kusema kweli, waume na wake waliokuwa na maono yaliyotajwa juu walifanya jambo fulani linalosaidia waume na wake wasuluhishe matatizo yao ya ndoa. Waliwasiliana na Mwanzilishi wa mpango wa ndoa, Yehova Mungu. Ijapokuwa misongo na magumu yanayowakabili waume na wake, yeye atawabariki kwa kuwapa amani ya Mungu ipitayo akili zote wakifanya wawezavyo kutumia kanuni zake na kuacha yaliyobaki mkononi mwake. Kusali pamoja kunasaidia hasa. Mume anapaswa kuongoza na ‘kuufunua moyo wake’ mbele za Mungu, akitafuta mwongozo na mwelekezo wake juu ya tatizo lolote ambalo yeye na mke wake wanakabili. (Zaburi 62:8) Bila shaka Yehova Mungu atasikia sala za jinsi hiyo.

Naam, kifungo cha ndoa kinaweza kuimarishwa. Hata sasa, tukiwa tunaishi katika jamii yenye msukosuko pamoja na kutokamilika kwetu kote, waume na wake wanaweza kupata shangwe nyingi katika uhusiano wao. Unaweza kupata madokezo zaidi na mashauri zaidi ya kimungu yatumikayo katika kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc. Zaidi ya hayo, waume na wake wanaojitahidi kutumia kanuni za Biblia wana tumaini la kuunganishwa katika upendo katika ule ulimwengu mpya wenye kufanyizwa na Mungu ulio karibu kuja.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki