Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 8/15 kur. 366-368
  • Kujitahidi Kufanya Maendeleo Katika Ndoa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujitahidi Kufanya Maendeleo Katika Ndoa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UHITAJI WA MAONI YALIYOSAWAZIKA
  • “KWA KILA SABABU?”
  • KUWA “MWILI MMOJA”
  • KANUNI YA UKICHWA WA UPENDO
  • NI NANI ALIYE WA MAANA ZAIDI?
  • WAKATI HAKUNA JAMBO LINALOELEKEA KUSAIDIA
  • Talaka Biblia Inasema Nini Hasa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Heshimu “Kile Ambacho Mungu Ameunganisha”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Maisha ya Jamaa—Namna Unavyoweza Kufanikiwa
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 8/15 kur. 366-368

Kujitahidi Kufanya Maendeleo Katika Ndoa

NDOA ndio uhusiano ulio karibu zaidi wa watu wazima. Wakati mume na mke wanapotendeana vibaya, maumivu yanakuwa mengi na ya muda mrefu. Huenda ikaelekea kuwa talaka ndilo jawabu la pekee.

Hata hivyo, utakubali kwamba kuvunja ndoa ni jambo zito. Je! talaka italeta furaha zaidi kweli? Au ni vizuri zaidi kujitahidi kufanya maendeleo katika ndoa yako?

UHITAJI WA MAONI YALIYOSAWAZIKA

Huenda talaka ikaonekana kuwa njia nyepesi ya kuepuka magumu yasiyopendeza katika ndoa. Lakini maoni yaliyosawazika yanahitajiwa, kwa maana mara nyingi talaka imeharibu mambo zaidi kwa wanaohusika. Gazeti Psychology Today, la Mei 1975, lilitoa maelezo yafuatayo: “Ingawa kuna vitabu vingi vya uchangamshi vinavyotoa maoni juu ya talaka yenye kusaidia, talaka isiyo na ubaya, na kuwa na maisha bora kwa talaka, watu wanaovunja ndoa zao ni wenye huzuni nyingi.” Ugumu mkubwa hasa kwa watu waliotalikana ni upweke.

‘Lakini sababu gani mtu aliyetalikiwa ajione mpweke?’ wauliza. ‘Je! leo wanaume na wanawake wengi sana hawapendi kuishi pamoja bila ya kuoana kwa halali?’ Hata hivyo, wengi hawawezi kuingia katika uhusiano huo usio na utaratibu wakawa na dhamiri njema. Na hata ukichagua kuishi hivyo, mtu asiyeona wema wa kuoana nawe kabisa aweza kukufanya ujisikie wewe ni mali yake? “Ndoa hutimiza uhitaji mkubwa sana wa kutosheleza maono ya moyoni na ya kufungamana pamoja,” asema mshauri wa mambo ya ndoa wa New York. “Huoni jambo hilo likifanywa katika uhusiano wa muda tu.” Je! talaka ingeweza kuongeza magumu yako badala ya kuyaondoa?

Lakini namna gani mtu aliyeoa au aliyeolewa akifanya ngono na mwingine asiye mwenzi wake, pengine hata na mwanamume mwenzake au mwanamke mwenzake? Hii inatokeza mazungumzo yanayopaswa kufikiriwa juu ya talaka yanayopatikana katika Biblia.

“KWA KILA SABABU?”

Katika karne ya kwanza W. K. kulikuwa na mabishano kati ya wanafunzi wa Kiyahudi juu ya sababu zinazokubalika za talaka. Orodha ya sheria za Kiyahudi inayojulikana kama Mishnah yahifadhi mapokeo yafuatayo tangu wakati huo: “Shule ya Shammai yasema: Mwanamume asitaliki mke wake asipokuwa ameona uchafu ndani yake . . . Nayo Shule ya Hillel yasema:

[Aweza kumtaliki] hata ikiwa amempikia vibaya . . . R[abbi] Akiba yasema: Hata ikiwa mume ameona mwingine wa kumfaa zaidi kuliko mkewe.”a

Kwa sababu ya maoni hayo yenye kutofautiana, ambayo yanafanana na maoni ya kisasa, Mafarisayo fulani walimwuliza Yesu Kristo hivi: “Je! ni halali mtu kumwacha [“kumtaliki,” NW] mkewe kwa kila sababu?” (Mt. 19:3) Yesu akajibu: “Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? . . . Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe. Nami nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha [“atakayemtaliki,” NW] mkewe isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini.”​—Mt. 19:4-6, 9.

Neno la Kigiriki porneía, ambalo limetafsiriwa hapa kama “uasherati,” latia ndani uzinzi, kulalana kwa mwanamume na mwenzake na mwanamke na mwenzake pamoja na matendo ya ngono yasiyo ya asili. Kwa hiyo, mambo hayo yakifanywa Maandiko yanaruhusu mtu ajitenge na mwenzi wa ndoa asiye mwaminifu na kuoa au kuolewa tena. Lakini hakuna lazima katika Maandiko ya kutafuta talaka.

Lakini namna gani juu ya hali ambapo mmoja aumiza mwili wa mwenzake, ingawa hafanyi “uasherati”? Hapa shauri linalopatikana katika 1 Wakorintho 7:10, 11 linafaa: “Mke asiachane na mumewe; lakini, ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe; tena mume asimwache mkewe.”

Hivyo, ingawa Neno la Mungu linaruhusu talaka kwa sababu ya “uasherati” na kuruhusu mtengano, halitii mume na mke moyo waachane kabisa. Bali, linawaonya kwa upole wajitahidi kufanya maendeleo katika ndoa, ‘wapatane tena.’ Nayo Biblia ina kanuni nyepesi ambazo zimesaidia maelfu ya waume na wake wafanye maendeleo katika ndoa zao. Acheni tuangalie baadhi ya kanuni hizo.

KUWA “MWILI MMOJA”

Utakumbuka kwamba Yesu alisema hivi juu ya waume na wake: “Wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja.” (Mt. 19:6) Mume na mke wenye kufanya kazi kama “mmoja” wanajua yaliyomo katika akili zao wote wawili nao hupatana juu ya mambo. Ndiyo kusema, wao huzungumza. Wawezaje kufanya hivyo wewe?

Je! ulijua kwamba mara kwa mara Maandiko yamtaja Mungu kama ‘akiwasikiliza’ watu, hata malalamiko yao? (Mwa. 21:17; Kut. 2:23-25; Kum. 9:19; Zab. 69:33; Mal. 3:16) Je! wewe ni msikilizaji mwema? Je! wewe hurudia kuuliza mwenzi wako asema nini ndiyo uhakikishe unaelewa? Kusikiliza kweli kweli ni tofauti sana na kutega sikio moja tu usikie yanayosemwa kisha kusema “oh-ooh,” kumbe unakaza fikira juu ya jambo jingine.

Halafu kuna uhitaji wa kuonyeshana mnathaminiana na kupendana. Biblia inasema kwa upendeleo juu ya “maneno ya mapendezi” yaliyosemwa na mvulana mchungaji na mpenzi wake Mshulami. (Wimbo Ulio Bora 1:2, 4; 4:10; 7:12, NW) Kutabasamu mara kwa mara kwa uchangamfu, kukonyeza jicho la mapenzi, usemi wa kweli wa kufurahia kama “Waonekana mzuri leo, mpenzi,” waweza kusaidia sana kufanya ndoa iendelee vizuri, na hata kujenga upya inayodhoofika.

KANUNI YA UKICHWA WA UPENDO

Jambo jingine linalofanya wengi wafike mahakmani kupata talaka ni kutofahamu daraka la kila mmoja, la mume na la mke. Hata hivyo, fikiria vile ugomvi mwingi ungeweza kuepukwa kwa kufuata kanuni ya Biblia: “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe.”​—Efe. 5:22, 23.

Je! huo unasikika kama mpango wa ukatili? Kabla ya kujibu, angalia yanayoendelea kusemwa na Maandiko: “Enyi waume, wapendeni wake zenu . . . Imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza . . . Lakini kila mtu ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe.”​—Efe. 5:25, 28, 29, 33.

Kichwa cha jamaa mwenye upendo husikiliza maoni ya mkewe juu ya mambo, akijua kwamba huenda mkewe akawa na uwezo mkubwa zaidi kuliko yeye pande fulani. Pia ‘humpa heshima kama chombo dhaifu’ kimwili, bila kutazamia mkewe afanye asiyoweza. (1 Pet. 3:7) Ewe mke, mume wako akitimiza daraka lake kama kichwa cha jamaa na kusaidiwa nawe, je! ndoa yenu haitakuwa na maendeleo?

Walakini, ili ndoa iwe na maendeleo mume na mke wanatakiwa waepuke nia inayofuatwa na watu wengi leo. Nia gani?

NI NANI ALIYE WA MAANA ZAIDI?

Pengine wewe umeona vile watu wanavyokazia uhitaji wa kutimiziwa mambo yao wenyewe tu leo. Kitabu Physician’s World chasema hivi: “Waume na wake pia wanatumaini kupata mengi zaidi siku hizi. Wanajifunza katika magazeti kwamba imewapasa kuendeleza ujana wao, kufurahia maisha bora, na kuchochea nyege zao nyakati zote. Hiyo ni hatari ambayo mara nyingi huleta talaka.”

Biblia, katika 1 Wakorintho 10:24, yasihi watu wawe na maoni yaliyo tofauti: “Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake.” Kwa mfano, Maandiko yashauri hivi juu ya ngono:

“Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe. Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda.”​—1 Kor. 7:3-5.

Kila mmoja wenu akiona jambo la maana zaidi ni kutosheleza mwenzake, je! ndoa yenu haiwezi kuwa na maendeleo?

WAKATI HAKUNA JAMBO LINALOELEKEA KUSAIDIA

Lazima ikubaliwe kwamba watu wengi wamejitahidi sana kwa miaka mingi kufanikisha ndoa yao, lakini wenzi wao hawakushirikiana nao. Je! ndivyo ilivyo hali yako?

Ikiwa ndivyo, usife moyo. Lichukue kwa uzito onyo la upole lililo katika Wagalatia 6:9: “Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.” Mara nyingi waume au wake wenye mioyo migumu wamebadilika kwa sababu ya mwenendo mwema wa wenzi wao.​—1 Pet. 3:1, 2.

Lakini hata isipokuwa hivyo kwako, huna haja ya kudhani jitihada zako njema ni za bure. Mtume Petro aliandika hivi: “Maana huu ndio wema hasa, mtu akivumilia huzuni kwa kumkumbuka Mungu, pale ateswapo isivyo haki.” (1 Pet. 2:19) Kushikamana na kanuni za Biblia mtu akiwa chini ya mkazo kunaleta upendeleo wa Mungu, nalo hilo ndilo jambo la maana zaidi ambalo Wakristo wanaweza ‘kuvuna.’

Je! wewe ungependa kujitahidi kufanya maendeleo katika ndoa yako? Mashahidi wa Yehova watafurahi kuongoza funzo la Biblia la bure kwako. Watakuonyesha kwa furaha kanuni zilizoongozwa na Mungu ambazo zinaweza kuifanikisha ndoa yako.

[Maelezo ya Chini]

a The Mishnah, kilichotafsiriwa na Herbert Danby, kitabu Gittin 9:10.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki