Mungu Mwenye Unyenyekevu Usiolinganika
YEHOVA Mungu ndiye Mwenye Enzi Kuu Zaidi, naye hayuko chini ya mtu mwingine ye yote wala hana wajibu wa kutii mtu ye yote. Yeye hahitaji kushauriwa na mtu ye yote kwa kuwa ni Mungu mwenye hekima yote. (Isa. 40:13) Yeye ndiye mwenye kielelezo bora cha mema yote, yaliyo ya haki na ya upendo. Uwezo wake haupingiki. Cheo chake hakiwezi kuharibiwa na mambo yanayoweza kufanywa au kukosa kufanywa na kiumbe cho chote.
Sisi wanadamu tusiokamilika hatuna cho chote cha kumpa Yehova Mungu kimfaidi. Kijana Elihu alimkumbusha Ayubu hivi: “Ikiwa umefanya dhambi, umefanya nini juu yake [“wamdhuruje Mungu,” NE]? Yakiwa makosa yako yameongezeka, wamfanyia nini yeye [“wamwumizaje yeye,” NE]? Ikiwa u mwenye haki, wampa kitu gani? Au yeye hupokea nini mkononi mwako? Uovu wako waweza kumwumiza mtu kama wewe; na haki yako yaweza kumfaa mwanadamu.”—Ayubu 35:6-8.
Ijapokuwa wanadamu wenye dhambi hawawezi kuharibu cheo cha Yehova Mungu, yeye ana nia ya kushughulika nao kwa sababu ya unyenyekevu wake mkuu. Mtunga zaburi mwenye kuongozwa na Mungu aliandika hivi: “Ni nani aliye mfano wa [Yehova], Mungu wetu aketiye juu; anyenyekeaye kutazama, mbinguni na duniani? Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, na kumpandisha maskini kutoka jaani. Amketishe pamoja na wakuu.”—Zab. 113:5-8.
Lo! Yehova yu tofauti namna gani na wanadamu wasiokamilika! Mara nyingi watu wenye elimu ya juu na akili wanakosa kuonyesha saburi kwa watu wasioelewa mambo upesi. Kwa kweli, huenda hata wakajivuna wasishirikiane na wale wasio na uwezo mwingi. Lakini Yehova Mungu hunyenyekea aonyeshe upendeleo juu ya wanaoweza kudharauliwa na wanadamu, yaani, wenye hali ya chini na maskini.
Hali ya kuhurumika ya wanaojikuta jaani [katika shimo la majivu, NW] yaonyeshwa katika habari ya mwanamume Ayubu. Baada ya kupoteza kila kitu, Ayubu mgonjwa aliketi “majivuni,” pengine akiwa kama mtu aliyelaaniwa katika jaa la taka ya mji. (Ayubu 2:8) Wakati mmoja alikuwa amefurahia kuwa na cheo cha heshima akiwa mzee na hakimu mwenye kuheshimiwa katika lango la mji. Lakini alipopata taabu nyingi alidharauliwa sana na watu wanyonge. Alisema hivi: “Sasa mimi nimekuwa wimbo wao, naam, nimekuwa simo kwao. Wao hunichukia, na kujitenga nami, hawaachi kunitemea mate usoni.”—Ayubu 30:9, 10.
Ebu fikiria hilo, Yehova Mungu amekuwa na nia ya kusaidia watu wenye kudharauliwa kama Ayubu mwenye taabu nyingi. Amewatukuza mara nyingi wale walioonekana na wanadamu kuwa si kitu.
Mtu mmoja aliyefahamu jambo hili ni Daudi. Kwa kuthamini aliyotendewa na Mungu, alisema hivi: “Unyenyekevu wako umenikuza.” (2 Sam. 22:36) Kwa kuwa Daudi alikuwa ndiye mvulana mdogo zaidi kati ya wana wa Yese, ilionekana kwamba ilikuwa vigumu kwake kuchaguliwa awe mfalme juu ya Israeli wote. Baba yake hata hakumwita alikokuwa akilisha kondoo amjulishe kwa nabii Samweli, bali aliwaleta wana wake saba wengine. Baada ya kusihiwa na Samweli ndipo Yese alipomwita Daudi kutoka malishoni. Kisha Samweli alimtia Daudi mafuta “kati ya ndugu zake.” (1 Sam. 16:6-13) Kwa hiyo unyenyekevu wa Yehova katika kumfikiria Daudi kijana ndio uliomfanya mchungaji huyo awe mkuu.
Vilevile, Yehova amechagua watawala wenzi wa Mwanawe Yesu Kristo kati ya wenye kudharauliwa ulimwenguni. Akieleza jambo hilo, mtume Paulo wa Kikristo aliandika hivi: “Si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko.”—1 Kor. 1:26-28.
Jambo la kutokeza ni kwamba Yehova Mungu aliwavumilia Waisraeli wenye kumwasi mara nyingi, kwa sababu ya unyenyekevu wake mkuu. Alisema hivi kupitia kwa nabii wake Isaya: “Mchana kutwa nimewanyoshea mikono yangu watu walioasi, watu waendao katika njia isiyo njema, wakifuata mawazo yao wenyewe.”—Isa. 65:2.
Unyenyekevu huo ni wa kusifika sana. Yehova Mungu aliendelea ‘kuwanyoshea’ Waisraeli mikono yake, akiwaomba sana wamrudie awabariki. Alifanya hivyo ijapokuwa ushupavu wao ulimwudhi sana. Maandiko yatuambia hivi: “Wao wenyewe waliasi na kuudhi roho takatifu yake.” (Isa. 63:10, NW) Baada ya kuwasihi kwa karne nyingi ndipo Yehova alipowaacha mwishowe Waisraeli wasiotii mikononi mwa adui zao. Hata hivyo, hakuzuia watu mmoja mmoja kati yao wasimrudie. Aliwataka watubu na kufuata njia itakayomfanya awakubali na kuwabariki. Aliendelea kuwaomba hivi kwa uchangamfu: “Nirudieni mimi, nami nitawarudia ninyi.”—Mal. 3:7.
Namna gani leo? Maneno aliyosema mtume Paulo katika Athene yangali yatumika: “[Mungu] anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu.” (Matendo 17:30) Yehova Mungu alimtoa Mwanawe kwa ajili ya ulimwengu, kwa unyenyekevu wake mkuu na upendo wake usio na mipaka. Hiyo ilifungulia wanadamu njia ya kuingia katika hali yenye kukubalika mbele zake, wakitumainia kupata uzima wa milele.—Yohana 3:16.
Kwa kuwa Yehova ni Mungu mwenye unyenyekevu huo usiolinganika, hawezi kuvumilia mtu ye yote mwenye kiburi. Biblia yatuambia hivi: “Kila mwenye moyo wa kiburi ni chukizo kwa [Yehova].” (Mit. 16:5) “Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.”—Yak. 4:6.
Kwa kuwa Yehova Mungu ni mnyenyekevu, hiyo yahakikishia watumishi wake wanyenyekevu kwamba atawasaidia bila shaka. Ingawa yeye ndiye mtawala mkuu zaidi ya wote, aliye mdogo zaidi kati ya watumishi wake hapaswi kuogopa kwamba atasahauliwa. “Ingawa [Yehova] yuko juu,” yasema Zaburi 138:6, “amwona mnyenyekevu, naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali.” Mtu ambaye huenda akawa mkubwa wa cheo lakini mwenye kutawalwa na kiburi hatambuliwi na Yehova. Lakini mtu mnyenyekevu ni mwenye thamani nyingi machoni pake. Yesu Kristo aliwatia wanafunzi wake moyo kwa kuwaambia hivi: “Je! mashomoro watano hawauzwi kwa senti mbili? wala hasahauliwi hata mmojawapo mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi, bora ninyi kuliko mashomoro wengi.”—Luka 12:6, 7.
Sisi sote twaweza kushukuru sana kwamba Yehova ni Mungu mnyenyekevu. Kama asingalikuwa mnyenyekevu, kusingalikuwa na uwezekano kwetu wa kuwa na hali yenye kukubalika mbele zake. Unyenyekevu wa Yehova wapaswa kutufanya tumwige yeye. Imetupasa tujipatanishe kabisa na maneno ya hekima ya Mithali 8:13: “Kiburi na majivuno, na njia mbovu, na kinywa cha ukaidi pia nakichukia.” Ikiwa tunajitahidi kusitawisha nia ya kuwa na chuki ya namna hiyo, twaweza kuwa na hakika kwamba Mungu mwenye unyenyekevu usiolinganika, Yehova, ataendelea kutuangalia kwa upendeleo.