-
Biblia Inasema Nini Kuhusu Ngono?Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
SOMO LA 41
Biblia Inasema Nini Kuhusu Ngono?
Watu wengi hawapendi kuzungumza kuhusu ngono. Hata hivyo, Biblia inazungumza kuhusu ngono kwa njia iliyo wazi na ya heshima. Tunanufaika na mambo ambayo Biblia inasema, na tunatarajia iwe hivyo kwa sababu Yehova ndiye Muumba wetu. Basi anajua mambo yanayotufaa kabisa. Anatuambia mambo tunayopaswa kufanya ili kumfurahisha, na mambo yatakayotusaidia kufurahia maisha milele.
1. Yehova ana maoni gani kuhusu ngono?
Ngono ni zawadi kutoka kwa Yehova. Anataka mwanamume na mwanamke waliofunga ndoa wafurahie zawadi hiyo. Zawadi hiyo inasaidia mume na mke kupata watoto, na pia kuonyeshana upendo mwororo kwa njia ya asili na yenye kufurahisha. Ndiyo sababu Neno la Mungu linasema hivi: “Na ushangilie pamoja na mke wa ujana wako.” (Methali 5:18, 19) Yehova anatarajia Mkristo aliyefunga ndoa awe mshikamanifu kwa mwenzi wake wa ndoa. Hivyo, wenzi wa ndoa hawapaswi kamwe kufanya uzinzi.—Soma Waebrania 13:4.
2. Uasherati ni nini?
Biblia inatuambia kwamba “waasherati . . . hawataurithi Ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10) Waandikaji wa Biblia walioandika kwa lugha ya Kigiriki, walitumia neno por·neiʹa kumaanisha uasherati. Neno hilo linatia ndani (1) kufanya ngonoa na mtu ambaye si mume au mke wako, (2) ngono kati ya watu wa jinsia moja, na (3) kufanya ngono na mnyama. ‘Tunapojiepusha na uasherati,’ tunanufaika na pia tunamfurahisha Yehova.—1 Wathesalonike 4:3.
CHIMBA ZAIDI
Chunguza jinsi unavyoweza kuepuka uasherati na jinsi utakavyonufaika kwa kudumisha maadili safi.
3. Ukimbieni uasherati
Mwanamume mwaminifu Yosefu alikataa kufanya uasherati aliposhawishiwa kufanya ngono na mke wa mtu mwingine. Soma Mwanzo 39:1-12, kisha mzungumzie maswali haya:
Ni sababu gani iliyofanya Yosefu akimbie?—Ona mstari wa 9.
Je, unafikiri Yosefu alifanya uamuzi unaofaa? Kwa nini?
Leo, vijana wanawezaje kumwiga Yosefu na kukimbia uasherati? Onyesha VIDEO.
Yehova anataka sisi sote tujiepushe na uasherati. Soma 1 Wakorintho 6:18, kisha mzungumzie maswali haya:
Ni hali gani ambazo zinaweza kufanya mtu ashawishike kufanya uasherati?
Unawezaje kuukimbia uasherati?
4. Unaweza kupinga vishawishi
Ni nini kinachoweza kufanya iwe vigumu kupinga kishawishi cha kufanya uasherati? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.
Ndugu katika video hiyo alifanya nini alipotambua kwamba mawazo na matendo yake yangefanya akose kuwa mwaminifu kwa mke wake?
Wakati mwingine, hata Wakristo waaminifu hupambana ili kudumisha mawazo safi. Unawezaje kuacha kufikiria mawazo machafu? Soma Wafilipi 4:8, kisha mzungumzie maswali haya:
Tunapaswa kufikiria mambo gani?
Kusoma Biblia na kuwa na shughuli nyingi katika utumishi wa Yehova, kunawezaje kutusaidia kupinga vishawishi vya kutenda dhambi?
5. Viwango vya Yehova hutunufaisha
Yehova anajua mambo yanayotufaa kabisa. Anatufundisha jinsi ya kudumisha maadili safi na manufaa ya kufanya hivyo. Soma Methali 7:7-27 au onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.
Kijana huyo aliingiaje katika kishawishi?—Ona Methali 7:8, 9.
Kulingana na Methali 7:23, 26, uasherati unaweza kuwa na matokeo mabaya sana. Tukidumisha maadili safi tutaepuka matatizo gani?
Kuwa na maadili safi kunawezaje kutusaidia kufurahia maisha milele?
Baadhi ya watu wanafikiri kwamba mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja, si jambo la upendo kuwaelekea watu hao. Lakini Yehova ni Mungu mwenye upendo na anataka watu wote wafurahie maisha milele. Ili tustahili kuishi milele, lazima tufuate viwango vyake vya maadili. Soma 1 Wakorintho 6:9-11, kisha mzungumzie swali hili:
Je, Mungu anachukizwa tu na ngono kati ya watu wa jinsia moja au kuna mambo mengine yanayomchukiza?
Ili tumfurahishe Mungu, sisi sote tunahitaji kufanya mabadiliko. Je, tunanufaika tunapofanya mabadiliko hayo? Soma Zaburi 19:8, 11, kisha mzungumzie maswali haya:
Je, unafikiri viwango vya Yehova kuhusu maadili vinafaa? Kwa nini?
Yehova amewasaidia watu wengi watii viwango vyake vya maadili. Anaweza kukusaidia pia
WATU FULANI HUSEMA: “Ni sawa kwa watu wawili kufanya ngono ikiwa wanapendana.”
Wewe una maoni gani?
MUHTASARI
Ngono ni zawadi ambayo Yehova amempa mume na mke ili waifurahie.
Ungejibuje?
Uasherati unatia ndani mambo gani?
Ni nini ambacho kitatusaidia kuepuka uasherati?
Tunanufaikaje tunapofuata viwango vya maadili vya Yehova?
CHUNGUZA ZAIDI
Jifunze kwa nini Mungu anataka mwanamume na mwanamke wafunge ndoa kabla ya kuishi pamoja.
“Biblia Inasema Nini Kuhusu Kuishi Pamoja Bila Kufunga Ndoa?” (Makala iliyo kwenye mtandao)
Jifunze kwa nini viwango vya Biblia kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja havichochei chuki.
“Je, Ni Kosa Kufanya Ngono Kati ya Watu wa Jinsia Moja?” (Makala iliyo kwenye mtandao)
Jifunze jinsi sheria za Mungu zinavyotulinda inapohusu matendo yote ya ngono.
“Je, Ngono ya Mdomo Ni Ngono?” (Makala iliyo kwenye mtandao)
Katika simulizi “Walinionyesha Heshima,” ona jambo lililomchochea mtu aliyekuwa na zoea la kufanya ngono na watu wa jinsia yake abadili maisha yake ili amfurahishe Mungu.
a Vitendo hivyo vya ngono visivyo halali vinatia ndani mambo mbalimbali kama vile kufanya ngono kwa mdomo, ngono ya mkundu, kupapasa viungo vya uzazi vya mtu mwingine ili kuamsha hamu ya ngono, na ngono kati ya mwanamume na mwanamke ambao hawajafunga ndoa.
-
-
Biblia Inasema Nini Kuhusu Useja na Ndoa?Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
SOMO LA 42
Biblia Inasema Nini Kuhusu Useja na Ndoa?
Katika tamaduni fulani, inaaminiwa kwamba mtu hawezi kuwa na furaha ikiwa hajafunga ndoa. Hata hivyo, si watu wote waliofunga ndoa walio na furaha na si waseja wote wasio na furaha. Biblia inasema kwamba useja na ndoa ni zawadi kutoka kwa Yehova.
1. Kuna manufaa gani ya kuwa mseja?
Biblia inasema hivi: “Yeyote anayefunga ndoa anafanya vema, lakini yeyote asiyefunga ndoa atafanya vema zaidi.” (Soma 1 Wakorintho 7:32, 33, 38.) Ni katika njia gani mseja anaweza ‘kufanya vema zaidi’? Wakristo waseja hawana jukumu la kumtunza mwenzi wa ndoa. Kwa hiyo, wana uhuru mwingi. Kwa mfano, baadhi yao wanaweza kupanua huduma yao kwa kuhamia katika nchi nyingine ili kuhubiri habari njema. Jambo muhimu zaidi, wanaweza kutumia muda mwingi zaidi kumkaribia Yehova.
2. Kuna manufaa gani ya kufunga ndoa kisheria?
Kama ilivyo na useja, ndoa ina manufaa ya kipekee. Biblia inasema kwamba “wawili ni afadhali kuliko mmoja.” (Mhubiri 4:9) Hilo ni kweli hasa kwa Wakristo wanaofuata kanuni za Biblia katika ndoa yao. Wakristo wanaofunga ndoa kisheria wanaahidi kwamba watapendana, wataheshimiana, na kutunzana. Kwa hiyo, wanajihisi wakiwa salama zaidi tofauti na mwanamume na mwanamke wanaoishi pamoja bila kufunga ndoa. Na ndoa inaandaa mazingira salama ya kulea watoto.
3. Yehova ana maoni gani kuhusu ndoa?
Yehova alipoanzisha ndoa ya kwanza alisema hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.” (Mwanzo 2:24) Yehova anataka mume na mke wapendane na waishi pamoja maisha yao yote. Anaruhusu talaka ikiwa mwenzi mmoja wa ndoa anafanya uzinzi. Katika hali kama hiyo, Yehova anamruhusu mwenzi asiye na hatia aamue ikiwa atatafuta talaka.a (Mathayo 19:9) Yehova anakataza Wakristo kuwa na ndoa za wake wengi.—1 Timotheo 3:2.
CHIMBA ZAIDI
Jifunze jinsi unavyoweza kuwa na furaha na kumfurahisha Yehova, iwe wewe ni mseja au umefunga ndoa.
4. Tumia vizuri zawadi ya useja
Yesu aliona useja kuwa zawadi. (Mathayo 19:11, 12) Soma Mathayo 4:23, kisha mzungumzie swali hili:
Yesu alitumiaje zawadi ya useja kumtumikia Baba yake na kuwasaidia wengine?
Kama Yesu, Wakristo wanaweza kufurahia zawadi ya useja. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.
Wakristo wanawezaje kutumia zawadi ya useja kwa njia yenye kuthawabisha?
Je, wajua?
Biblia haitaji umri wa kufunga ndoa. Hata hivyo, inawatia moyo vijana wasubiri hadi ‘wapite upeo wa ujana,’ kipindi ambacho hisia zenye nguvu za ngono zinaweza kufanya iwe vigumu kwa kijana kufanya uamuzi kwa hekima.—1 Wakorintho 7:36.
5. Chagua mwenzi wa ndoa kwa hekima
Kuchagua mwenzi wa ndoa ni mojawapo ya uamuzi muhimu zaidi ambao utafanya. Soma Mathayo 19:4-6, 9, kisha mzungumzie swali hili:
Kwa nini Mkristo anapaswa kufikiria kwa makini kabla ya kufanya uamuzi wa kufunga ndoa?
Biblia inaweza kukusaidia kutambua sifa za mwenzi wa ndoa anayekufaa. Jambo muhimu zaidi, chagua mwenzi wa ndoa ambaye anampenda Yehova.b Soma 1 Wakorintho 7:39 na 2 Wakorintho 6:14. Kisha mzungumzie maswali haya:
Kwa nini Mkristo anapaswa kufunga ndoa tu na Mkristo mwenzake?
Unafikiri Yehova atahisije tukiamua kufunga ndoa na mtu ambaye hampendi Yehova?
Wanyama wawili walio tofauti sana wakifungwa nira pamoja, wataumia. Vivyo hivyo, Mkristo anayefunga ndoa na mwenzi ambaye si mwamini atapatwa na matatizo mengi
6. Sitawisha maoni ya Yehova kuhusu ndoa
Katika Israeli la kale, baadhi ya wanaume waliwapa talaka wake zao kwa sababu ya ubinafsi. Soma Malaki 2:13, 14, 16, kisha mzungumzie swali hili:
Kwa nini Yehova anachukia watu wanapotalikiana kwa sababu zisizo na msingi wa Maandiko?
Uzinzi na talaka husababisha maumivu mengi kwa mwenzi asiye na hatia na pia kwa watoto
Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.
Ikiwa umefunga ndoa na mtu ambaye si mwamini, unaweza kufanya nini ili kuwa na ndoa yenye furaha?
7. Fuata viwango vya Yehova kuhusu ndoa
Huenda mtu akahitaji kufanya jitihada nyingi ili kufuata viwango vya Yehova kuhusu ndoa.c Lakini Yehova anawabariki wale wanaofanya hivyo. Onyesha VIDEO.
Soma Waebrania 13:4, kisha mzungumzie maswali haya:
Je, unafikiri viwango vya Yehova kuhusu ndoa vinafaa? Kwa nini?
Yehova anatarajia Wakristo waandikishe kisheria ndoa na talaka zao kwa sababu katika nchi nyingi, hiyo ni sheria iliyowekwa na serikali. Soma Tito 3:1, kisha mzungumzie swali hili:
Ikiwa umefunga ndoa, je, umehakikisha kwamba ndoa yenu inatambuliwa kisheria serikalini?
HUENDA MTU AKAULIZA: “Kwa nini ufunge ndoa? Mwanamume na mwanamke wanaweza kuishi pamoja bila kufunga ndoa.”
Wewe una maoni gani?
MUHTASARI
Useja na ndoa ni zawadi kutoka kwa Yehova. Waseja na watu waliofunga ndoa wanaweza kuwa na furaha na kuridhika maishani ikiwa wataishi kulingana na viwango vya Yehova.
Ungejibuje?
Mtu anawezaje kutumia vizuri useja wake?
Kwa nini Biblia inasema kwamba Mkristo anapaswa kufunga ndoa tu na Mkristo mwenzake?
Ni nini msingi pekee wa Kimaandiko kuhusu talaka?
CHUNGUZA ZAIDI
Kuoa au kuolewa “katika Bwana tu” kunamaanisha nini?
“Maswali Kutoka kwa Wasomaji” (Mnara wa Mlinzi, Julai 1, 2004)
Ona video mbili fupi zinazoweza kukusaidia kufanya maamuzi mazuri kuhusu uchumba na ndoa.
Jifunze kwa nini ndugu mmoja anahisi kwamba jambo ambalo Yehova amempa ni lenye thamani kuliko vitu vyote alivyoacha.
Ni baadhi ya mambo gani ambayo mtu anapaswa kufikiria kabla ya kuamua kutengana au kutafuta talaka?
“Heshimu ‘Kile Ambacho Mungu Ameunganisha’” (Mnara wa Mlinzi, Desemba 2018)
a Ona Maelezo ya Ziada 4 kuhusu kutengana ikiwa hakuna hatia ya uzinzi.
b Katika tamaduni fulani, wazazi huamua mtu atakayefunga ndoa na mwana au binti yao. Katika visa kama hivyo, wazazi wenye upendo huchunguza kwanza ikiwa mtu huyo anampenda Yehova, bali si uwezo wake wa kifedha, au jinsi watu wanavyomwona katika jamii.
c Ikiwa unaishi na mtu ambaye hujafunga naye ndoa, unaweza kuamua kumwacha au kufunga naye ndoa, huo ni uamuzi wako.
-