Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 2/15 kur. 12-17
  • “Ndoa na Iheshimiwe na Watu Wote”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Ndoa na Iheshimiwe na Watu Wote”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Hali Yenye Kubadilika
  • Kutaniko la Kikristo Laathiriwa
  • Kuvutwa na Kushawishwa
  • Ufunguo wa Kukinza
  • Vishawishi Vinavyowapata Wote
  • Ndoa Inaweza Kufanikiwa Katika Ulimwengu wa Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Acheni Yehova Aimarishe na Kulinda Ndoa Yenu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • “Ndoa na Iheshimiwe”
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Ikiwa Ndoa Imo Katika Hatua ya Kuvunjika
    Siri ya Furaha ya Familia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 2/15 kur. 12-17

“Ndoa na Iheshimiwe na Watu Wote”

“Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi.”—WAEBRANIA 13:4.

1. Watu wengi wamepata kujifunza nini juu ya ndoa yenye kufanikiwa?

MAMILIONI ya watu, hata katika enzi hii ya talaka rahisi, hufurahia ndoa zenye kudumu. Wamepata njia ya kupata mafanikio, zijapokuwa tofauti za kiutu na malezi. Ndoa hizo zapatikana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Katika visa vingi wenzi hao wa ndoa watakubali kwamba wamekuwa na vipindi vya mema na magumu pia, hata wamekuwa na sababu za kulaumiana. Hata hivyo, wamejifunza kuyavumilia magumu madogo-madogo ya ndoa na kuelekeza ndoa yao ifaavyo. Ni baadhi gani ya mambo ambayo yamewawezesha waendelee?—Wakolosai 3:13.

2. (a) Ni nini baadhi ya mambo chanya yanayotegemeza ndoa? (b) Ni nini baadhi ya mambo yanayoweza kuiharibu ndoa? (Ona sanduku kwenye ukurasa 14.)

2 Maelezo kutoka baadhi ya wale ambao ndoa zao za Kikristo zimekuwa na furaha na zenye kudumu ni yenye kufunua mambo mengi. Mume mmoja ambaye amefunga ndoa kwa miaka 16 alisema hivi: “Wakati wowote ambapo tatizo limetokea, tumejitahidi kwelikweli kusikiliza maoni ya kila mmoja.” Hilo lakazia mojayapo mambo yenye kuimarisha katika ndoa nyingi—uwasiliano wa wazi, wenye unyoofu. Mke mmoja, aliyeolewa kwa miaka 31, alitaarifu hivi: “Kushikana mikono na kufanya mambo yenye kufurahisha ili kuendeleza mahaba kati yetu limekuwa jambo la kutanguliza sikuzote.” Na hiyo ni sehemu nyingine ya uwasiliano. Wenzi wengine wa ndoa, ambao wameoana kwa karibu miaka 40, walikazia umaana wa kudumisha hali ya ucheshi, wa kuweza kujicheka mwenyewe na kuchekana. Walisema pia kwamba ilisaidia kuweza kuona yaliyo bora zaidi na mabaya zaidi katika kila mmoja wao na bado waonyeshe upendo mwaminifu-mshikamanifu. Mume alitaja utayari wa kukubali makosa na kisha kuomba msamaha. Mahali palipo nia ya kukubali kosa, ndoa itafaana na hali kuliko kuvunjika.—Wafilipi 2:1-4; 4:5, Kingdom Interlinear.

Hali Yenye Kubadilika

3, 4. Ni mabadiliko gani katika mtazamo ambayo yametukia kwa habari ya uaminifu katika ndoa? Je! waweza kutoa vielelezo?

3 Kwa miongo michache ambayo imepita, kotekote ulimwenguni, maoni yamebadilika kwa habari ya uaminifu katika ndoa. Watu wengine ambao wamefunga ndoa huamini kwamba hakuna kosa lolote kufanya uzinzi, hasa ikiwa mwenzi wa ndoa yule mwingine ajua juu yao na aukubali.

4 Mwangalizi mmoja Mkristo alieleza hivi juu ya hali hiyo: “Ulimwengu karibu umeacha jaribio lolote lenye uzito la kuishi kulingana na sheria za kiadili. Mwenendo safi umekuja kuonwa kuwa mtindo wa zamani.” Watu mashuhuri wa siasa, michezo, na vitumbuizo huhalifu kwa wazi viwango vya Biblia vya mwenendo wa kiadili, na watu hao huendelea kuonwa kuwa mabingwa. Kwa kweli hakuna aibu yoyote inayoshikamanishwa na aina yoyote ya ubaya au upotovu wa adili. Usafi wa kiadili na uaminifu-maadili havithaminiwi sana katika ile iitwayo eti jamii ya watu wa hali ya juu. Kwa hiyo, kwenye ile kanuni kwamba ‘kimfaacho mmoja humfaa yule mwingine,’ watu wengi hufuata kielelezo cha wale waliomo katika ile jamii ya watu wa hali ya juu na huachilia yale ambayo Mungu hukataza. Ni kama vile Paulo alivyoeleza jambo hilo: “Wakiisha kufa ganzi wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani.”—Waefeso 4:19; Mithali 17:15; Warumi 1:24-28; 1 Wakorintho 5:11.

5. (a) Ni nini msimamo wa Mungu juu ya uzinzi? (b) Ni nini kinachotiwa ndani kwa matumizi ya Biblia ya neno “uasherati”?

5 Viwango vya Mungu havijabadilika. Ni msimamo wake kwamba kuishi pamoja bila ndoa ni kuishi katika uasherati. Ukosefu wa uaminifu katika ndoa ungali ni uzinzi.a Mtume Paulo alitaarifu kwa wazi hivi: “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti . . . Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika Roho wa Mungu wetu.”—1 Wakorintho 6:9-11.

6. Tunaweza kupata kitia-moyo gani katika maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 6:9-11?

6 Jambo lenye kutia moyo katika andiko hilo ni usemi wa Paulo “Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa.” Naam, wengi ambao katika wakati uliopita walienenda katika “ufisadi” mlegevu wa ulimwengu wamepata fahamu zao, wakamkubali Kristo na dhabihu yake, na wakaoshwa. Wamechagua kumpendeza Mungu kwa kuwa na maisha ya kiadili na tokeo ni kwamba wao ni wenye furaha zaidi.—1 Petro 4:3, 4.

7. Kuna tofauti gani katika uelewevu wa neno “ukosefu wa adili,” na maoni ya Biblia ni nini?

7 Kwa upande ule mwingine, fasili ya ukosefu wa adili wa ulimwengu wa ki-siku-hizi imedhoofishwa sana hivi kwamba haifaani na maoni ya Mungu. Kamusi moja hufasili “kukosa adili” kuwa “kinyume cha adili inayokubalika.” “Adili inayokubalika” ya leo, inayoachilia ngono ya kabla ya ndoa na ya nje ya ndoa pamoja na ugoni-jinsia-moja, ni jambo ambalo Biblia hushutumu kuwa ukosefu wa adili. Naam, kulingana na maoni ya Kibiblia, ukosefu wa adili ni uhalifu mbaya sana wa sheria za kiadili za Mungu.—Kutoka 20:14, 17; 1 Wakorintho 6:18.

Kutaniko la Kikristo Laathiriwa

8. Ukosefu wa adili unaweza kuathirije wale waliomo kutanikoni?

8 Ukosefu wa adili leo umeenea sana hivi kwamba waweza hata kuwa mbano juu ya wale walio katika kutaniko la Kikristo. Huo unaweza kuwavuta kupitia programu za TV zenye kushusha heshima, vidio, na vichapo vya kipornografia vyenye kuenea sana. Ingawa ni sehemu ndogo tu ya Wakristo inayoathiriwa, ni lazima itambuliwe kwamba visa vingi vya kutengwa na ushirika kutoka miongoni mwa Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya mwenendo usiofaa Mkristo vinahusisha namna fulani ya ukosefu wa adili katika ngono. Katika ule upande chanya, sehemu kubwa ya wale wanaotengwa na ushirika hatimaye hutambua makosa yao, wanaanza tena njia safi ya maisha, na baadaye kurudishwa kutanikoni.—Linganisha Luka 15:11-32.

9. Shetani huwadanganyaje wale wasio macho?

9 Hakuna shaka kwamba Shetani anazunguka-zunguka kama simba angurumaye, akiwa tayari kuwanyafua wale wasio macho. Hila zake, au “matendo yake ya kiufundi,” zinawanasa Wakristo wasio macho kila mwaka. Roho ya ulimwengu wake iliyopo sikuzote ni yenye ubinafsi, yenye kupenda anasa, na yenye kutamani. Inaridhisha tamaa za kimnofu. Inakatalia mbali kujidhibiti.—Waefeso 2:1, 2; 6:11, 12, NW, kielezi chini; 1 Petro 5:8.

10. Ni nani wawezao kushawishwa, na kwa nini?

10 Ni nani kutanikoni wawezao kupatwa na vishawishi vya ukosefu wa adili? Wakristo wengi, wawe ni wazee katika kutaniko la mahali fulani, waangalizi wasafirio, Wanabetheli, mapainia wanaohubiri saa nyingi kila mwezi, wazazi wenye shughuli ya kulea familia, au vijana wanaokabili mbano wa marika. Kishawishi cha kimnofu kinawapata wote. Uvutano wa kingono waweza kuchochewa wakati usiotazamiwa hata kidogo. Hivyo Paulo aliweza kuandika hivi: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke. Jaribu [kishawishi, NW] halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu.” Ni jambo la kusikitisha, lakini Wakristo wengine wenye daraka wameshindwa na ushawishi huo wa ukosefu wa adili.—1 Wakorintho 10:12, 13.

Kuvutwa na Kushawishwa

11-13. Ni nini baadhi ya hali ambazo zimeongoza kwenye ukosefu wa adili?

11 Ni vishawishi vipi na hali zipi zimeongoza wengine kwenye mwenendo mpumbavu wa uzinzi na uasherati? Hizo ni nyingi na ngumu kufahamika na huenda zikatofautiana kutoka nchi au utamaduni mmoja hadi mwingine. Hata hivyo, kuna hali fulani za msingi zinazotokea katika nchi nyingi. Kwa kielelezo, imeripotiwa kwamba wengine wamepanga karamu ambako vileo vingi vinapatikana. Wengine walivutiwa na muziki wa kilimwengu wenye kudokeza ukosefu wa adili na dansi yenye kuamsha nyege. Katika baadhi ya maeneo katika Afrika, kuna wanaume matajiri—wasioamini—walio na masuria; wanawake wengine wameshawishwa kutafuta usalama wa kiuchumi katika hali hiyo hata ingawa hiyo inatia ndani ukosefu wa adili. Katika maeneo mengine waume Wakristo wameziacha familia zao ili kupata riziki katika migodi au kwingineko. Kisha uaminifu wao na ushikamanifu wao hujaribiwa sana au katika njia ambazo usingalijaribiwa nyumbani.

12 Katika nchi zilizositawi wengine wameangukia mtego wa Shetani kwa kuwa mara nyingi pamoja na mshiriki wa jinsia tofauti bila mtu wa tatu kuwapo—kama vile kuwa pamoja kwa ukawaida ndani ya gari kwa ajili ya kufundishwa kuendesha gari.b Wazee wanaofanya ziara za uchungaji wanahitaji kuwa waangalifu ili mmoja asiwe na dada peke yake anapomshauri. Mazungumzo yaweza kujawa na hisia-moyo na kutokeza hali yenye kuwaaibisha wote wawili.—Linganisha Marko 6:7; Matendo 15:40.

13 Hali hizo ambazo zimetangulia kutajwa zimeongoza baadhi ya Wakristo waache kuwa wenye macho na kufanya matendo yenye kukosa adili. Hata kama ilivyotukia katika karne ya kwanza, wamejiruhusu wenyewe ‘wajaribiwe na kuvutwa na tamaa zao wenyewe,’ ambazo zimewaongoza kwenye dhambi.—Yakobo 1:14, 15; 1 Wakorintho 5:1; Wagalatia 5:19-21.

14. Kwa nini ubinafsi ni jambo la msingi katika visa vya uzinzi?

14 Uchunguzi wenye uangalifu wa visa mbalimbali vya kutengwa na ushirika huonyesha kwamba matendo yenye kukosa adili yana mambo fulani ya msingi yanayofanana. Katika visa hivyo kuna namna fulani ya ubinafsi. Kwa nini twasema hivyo? Kwa sababu katika visa vya uzinzi, mtu au watu fulani wasio na hatia wataumia. Huenda mwenzi halali akaumia. Kwa hakika watoto wataumia, ikiwa kuna wowote, kwani ikiwa uzinzi huo watokeza talaka, watoto, wanaotamani usalama wa familia iliyounganika, huenda wakateseka zaidi. Mzinzi anafikiria hasa furaha na faida yake mwenyewe. Huo ni ubinafsi.—Wafilipi 2:1-4.

15. Ni nini huenda vikawa baadhi ya visababishi vilivyoongoza kwenye uzinzi?

15 Kwa kawaida uzinzi si tendo la ghafula la udhaifu. Kumekuwa mzoroto wa kidato kwa kidato, hata usioonekana, katika ndoa yenyewe. Labda uwasiliano umekuwa jambo la kidesturi tu au wenye ubaridi. Huenda ikawa hakukuwa kutiana moyo kwingi. Huenda ikawa kila mmoja alimchukua yule mwingine kivivi hivi tu. Huenda ikawa wenzi hao hawakuwa wakitoshelezana kingono kwa muda fulani. Kwa hakika uzinzi unapotukia, kunakuwa kumekuwa pia upunguo wa uhusiano pamoja na Mungu. Yehova haonwi tena waziwazi kuwa ndiye Mungu aliye hai anayefahamu mawazo na matendo yetu yote. Hata huenda ikawa kwamba katika akili ya mzinzi huyo, “Mungu” anakuja kuwa neno tu, mtu aliyewaziwa ambaye si sehemu ya maisha ya kila siku. Kisha inakuwa rahisi zaidi kutenda dhambi dhidi ya Mungu.—Zaburi 51:3, 4; 1 Wakorintho 7:3-5; Waebrania 4:13; 11:27.

Ufunguo wa Kukinza

16. Mkristo anaweza kukinzaje kishawishi cha kuwa mzinifu?

16 Mkristo yeyote akijipata mwenyewe akiwa anashawishwa kuingia katika mwendo wa kuwa mzinifu, ni mambo gani yanayohitaji kufikiriwa? Kwanza kabisa, maana ya upendo wa Kikristo, yenye kutegemea kwa uthabiti kanuni za Biblia, yapasa ifikiriwe. Upendo wa kimwili au wa kiashiki haupasi kamwe uruhusiwe udhibiti hisia za mtu na kusababisha aanguke katika ubinafsi, ukiwaletea wengine maumivu. Badala ya hivyo, hali hiyo yapasa ionwe kulingana na maoni ya Yehova. Yapaswa ionwe kuhusiana na hali ya ujumla ya kutaniko na ukosefu wa heshima ambao mwenendo huo mbaya ungeletea kutaniko na jina la Yehova. (Zaburi 101:3) Msiba waweza kuzuiwa kwa kupata maoni ya Kristo katika jambo hilo na kisha kutenda kulingana nayo. Kukumbuka, upendo ulio kama wa Kristo usio na ubinafsi haushindwi kamwe.—Mithali 6:32, 33; Mathayo 22:37-40; 1 Wakorintho 13:5, 8.

17. Tuna vielelezo gani vyenye kujenga vya uaminifu?

17 Ufunguo wa kukinza ni kwa mtu kuimarisha imani yake na njozi yake ya tumaini lililoko mbele. Hilo lamaanisha kutanguliza moyoni vielelezo vya uaminifu-maadili ambavyo wanaume na wanawake waaminifu wa zamani, na Yesu mwenyewe, wameacha. Paulo aliandika hivi: “Basi na sisi pia, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba [mti wa mateso, NW] na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.” (Waebrania 12:1-3) Badala ya kuikomesha ndoa, mtu mwenye hekima atafikiria njia za kurekebisha makosa yoyote ili kuiokoa, hivyo akiepuka ule mtego wa uhaini na udanganyifu.—Ayubu 24:15.

18. (a) Kwa nini uhaini si neno lenye nguvu sana la kutumiwa kufafanua uzinzi? (b) Mungu huonaje kulipa nadhiri?

18 Je! uhaini ambao ni usaliti, ni neno lenye nguvu sana kutumiwa kwa habari ya ukosefu wa adili? Usaliti ni kuhalifu amana au matumaini. Kwa hakika nadhiri ya ndoa inatia ndani amana na ahadi ya kupenda na kuthamini, yajapokuwa magumu yote, kupitia nyakati nzuri na mbaya. Inahusisha jambo fulani ambalo wengi huona kuwa la zamani kwa nyakati tunamoishi—uhakikishio wa mtu unaotolewa katika nadhiri ya ndoa. Kusaliti amana hiyo ni kutenda namna fulani ya usaliti dhidi ya mwenzi wa mtu. Maoni ya Mungu juu ya viapo yanataarifiwa katika Biblia: “Wewe ukimwekea Mungu nadhiri, usikawie kuiondoa; kwa kuwa yeye hawi radhi na wapumbavu; basi, uiondoe hiyo uliyoiweka nadhiri.”—Mhubiri 5:4.

19. Ni jambo gani lililo kinyume wakati Shetani anaposhangilia Shahidi anaposhindwa?

19 Kusiwe na shaka juu ya hilo. Kadiri kulivyo kushangilia kwingi mbinguni juu ya wokovu wa mtenda dhambi mmoja, ndivyo kulivyo kushangilia kwingi duniani miongoni mwa vikundi vya Shetani vyenye kuonekana na visivyoonekana, wakati mmoja wa Mashahidi wa Yehova anaposhindwa kushika uaminifu-maadili wake.—Luka 15:7; Ufunuo 12:12.

Vishawishi Vinavyowapata Wote

20. Tunaweza kukinzaje kishawishi? (2 Petro 2:9, 10)

20 Je! ukosefu wa adili hauwezi kuepukika katika visa fulani? Je! mnofu na Shetani ni wenye nguvu sana hivi kwamba Wakristo hawawezi kuwakinza na kushika uaminifu-maadili wao? Paulo atoa kitia-moyo katika maneno haya: “Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe [mshawishwe, NW] kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu [kishawishi, NW] atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.” Katika ulimwengu wa leo huenda tusiepuke kishawishi kabisa, lakini kwa kumgeukia Mungu katika sala, twaweza kwa hakika kuvumilia na kushinda kishawishi chochote.—1 Wakorintho 10:13.

21. Ni maswali gani yatakayojibiwa katika makala yetu inayofuata?

21 Mungu hututolea nini ili kutusaidia tuvumilie vishawishi na kuvishinda? Sisi mmoja mmoja tunahitaji nini ili kuzilinda ndoa zetu, familia zetu, pamoja na sifa ya jina la Yehova na lile la kutaniko? Makala yetu ifuatayo itashughulikia maswali hayo.

[Maelezo ya Chini]

a “Katika maana iliyo pana, neno ‘Uasherati’ kama lilivyotumiwa kwenye Mathayo 5:32 na 19:9 kwa wazi linamaanisha namna nyingi za ngono haramu zisizo halali zinazofanywa nje ya ndoa. Neno porneia [neno la Kigiriki linalotumiwa katika maandiko hayo] linatia ndani matumizi ya kiungo (viungo) cha uzazi kwa njia ya ukosefu mkubwa wa adili cha angaa mwanadamu mmoja (yawe ni matumizi ya kiungo hicho kwa njia ya asili au kwa njia iliyopotoshwa); pia, ili lihesabiwe hivyo ni lazima kuwe kulikuwa na mwingine mwenye kuhusika katika huo ukosefu wa adili—mwanadamu, awe ni mwanamume au mwanamke, au mnyama.” (Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 1984, kurasa 6, 7) Uzinzi: “Uhusiano wa kingono wa hiari kati ya mtu aliyefunga ndoa na mwenzi mwingineye yote asiye mume au mke halali.”—The American Heritage Dictionary of the English Language.

b Kwa wazi, kungekuwako pindi zifaazo ambapo ndugu angemwandalia dada usafiri, na hali hizo hazipaswi kueleweka vibaya.

Je! Unakumbuka?

◻ Ni baadhi ya mambo gani yanayosaidia kuimarisha ndoa?

◻ Kwa nini tunapaswa kuepuka kabisa maoni ya ulimwengu juu ya adili?

◻ Ni baadhi ya vishawishi vipi na hali zipi ziwezazo kuongoza kwenye ukosefu wa adili?

◻ Ni nini ufunguo wa msingi wa kukinza dhambi?

◻ Mungu hutusaidiaje katika nyakati za kishawishi?

[Sanduku katika ukurasa wa 14]

MAMBO YA KAWAIDA KATIKA NDOA ZENYE KUDUMU

◻ Kushikamana sana na kanuni za Biblia

◻ Wenzi wote wawili wana uhusiano imara pamoja na Yehova

◻ Mume humheshimu mke, hisia zake na maoni zake

◻ Uwasiliano mzuri wa kila siku

◻ Hujaribu kupendezana

◻ Hali ya ucheshi; kuweza kujicheka mwenyewe

◻ Kukubali makosa kwa hiari; kusamehe kwa hiari

◻ Kudumisha hali ya kimahaba

◻ Kuungana katika kuwalea na kuwatia nidhamu watoto

◻ Kusali kwa Yehova pamoja kwa ukawaida

MAMBO YASIYOFAA YANAYODHOOFISHA NDOA

◻ Ubinafsi na ushupavu

◻ Kukosa kufanya mambo pamoja

◻ Uwasiliano mbaya

◻ Ukosefu wa kushauriana vya kutosha kati ya wenzi

◻ Kutumia pesa vibaya

◻ Viwango tofauti-tofauti katika kushughulikia watoto na/au watoto wa kambo

◻ Mume kufanya kazi hadi usiku au kupuuza familia kwa ajili ya wajibu mwingine mwingi

◻ Kushindwa kutunza hali za kiroho za familia

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kudumisha ndoa ikiwa yenye kuheshimika kunaleta furaha ya kudumu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki