Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ‘Alimpendeza Mungu Vema’
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2017 | Na. 1
    • ENOKO ‘ALITOA UNABII KUWAHUSU’

      Huenda Enoko alihisi upweke kwa sababu ya kuwa mtu pekee mwenye imani katika siku zake. Lakini je, Yehova Mungu, alitambua imani yake? Ndiyo. Siku moja, Yehova aliwasiliana na Enoko, mtumishi wake mwaminifu. Alimpa ujumbe kwa ajili ya watu walioishi siku hizo. Hivyo, akamfanya Enoko kuwa nabii wa kwanza ambaye ujumbe wake umeandikwa katika Biblia. Tunajua hilo kwa kuwa karne nyingi baadaye, Yuda, ndugu wa kambo wa Yesu aliandika maneno ya kinabii ya Enoko akiongozwa na roho ya Mungu.a

      Unabii wa Enoko ulisemaje? Ulisema hivi: “Tazama! Yehova alikuja pamoja na watakatifu wake makumi ya maelfu, ili kufanya hukumu juu ya wote, na kuwathibitisha kuwa ni wenye hatia wote wasiomwogopa Mungu kuhusu matendo yao yote ya kutomwogopa Mungu ambayo walitenda kwa njia ya kutomwogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kushtua ambayo watenda-dhambi wasiomwogopa Mungu walisema juu yake.” (Yuda 14, 15) Jambo moja ambalo huenda umegundua ni kwamba Enoko alizungumza kwa wakati uliopita, kana kwamba Mungu tayari alikuwa amefanya kile kilichosemwa kwenye unabii huo. Manabii wengi baadaye walitumia njia hiyo walipotoa unabii wao. Wazo ni hili: Uhakika wa kutimia kwa jambo linalozungumziwa ni mkubwa sana hivi kwamba linaelezwa kana kwamba tayari limetukia!—Isaya 46:10.

      Enoko akiwahubiria watu wasiomwogopa Mungu

      Enoko alitangaza ujumbe wa Mungu katika ulimwengu wa watu wenye vichwa vigumu bila woga

      Hali ilikuwaje Enoko alipokuwa akitangaza ujumbe wake, labda akimhubiria kila mtu aliyekutana naye? Hebu fikiria jinsi ambavyo onyo hilo lilikuwa kali. Maneno “wasiomwogopa Mungu” yalitumiwa mara nne ili kuelezea watu, matendo yao, na jinsi walivyofanya matendo hayo. Hivyo, unabii huo ulionyesha wazi kwamba ulimwengu wa wanadamu tangu kufukuzwa Edeni, ulikuwa umepotoka kwelikweli. Ulimwengu huo ungefikia mwisho wakati ambapo Yehova angekuja kuuharibu akiwa na “watakatifu wake makumi ya maelfu,” yaani, malaika wenye nguvu waliopangwa kivita. Enoko alitangaza onyo hilo bila woga, tena akiwa peke yake! Huenda Lameki ambaye wakati huo alikuwa mdogo, alitazama na kustaajabia ujasiri wa babu yake. Ikiwa alifanya hivyo, tunajua ni kwa nini.

      Kutafakari imani ya Enoko kunatuchochea kujichunguza ikiwa tunauona ulimwengu huu kama Yehova anavyouona. Hukumu ambayo Enoko alitangaza kwa ujasiri inahusu kipindi chetu pia. Kama tu Enoko alivyotabiri, Yehova alileta Gharika katika siku za Noa ili kuangamiza watu wasiomwogopa. Uharibifu huo uliweka kielezo cha uharibifu mkubwa zaidi utakaokuja hivi karibuni. (Mathayo 24:38, 39; 2 Petro 2:4-6) Leo pia, kama ilivyokuwa katika siku za Enoko, Mungu akiwa pamoja na watakatifu wake makumi ya maelfu, anajiandaa kuleta hukumu ya uadilifu kwa ulimwengu wa watu wasiomwogopa. Sote tunapaswa kufikiria kwa uzito onyo la Enoko na kuwahubiria wengine kulihusu. Huenda familia na marafiki wasituunge mkono. Huenda nyakati nyingine tukahisi tuko peke yetu. Lakini Yehova hakumwacha Enoko kamwe; na hatawaacha watumishi wake waaminifu leo!

  • ‘Alimpendeza Mungu Vema’
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2017 | Na. 1
    • a Baadhi ya wasomi wa Biblia wanasema kwamba Yuda alinukuu maneno hayo kutoka kwenye kitabu cha hekaya kinachoitwa Kitabu cha Enoko, ambacho kina habari za kubuniwa kumhusu Enoko. Kitabu hicho kimenukuu kwa usahihi unabii wa Enoko, lakini huenda unabii huo ulitolewa kwenye chanzo cha kale ambacho sasa hakipo kama vile nakala ya maandishi au masimulizi. Huenda Yuda alitumia chanzo hichohicho au alijifunza kuhusu Enoko kupitia Yesu ambaye aliona maisha ya Enoko kutoka Mbinguni.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki