-
Unganishweni Na Lugha Iliyo SafiMnara wa Mlinzi—1991 | Mei 1
-
-
Unganishweni Na Lugha Iliyo Safi
“Ndipo nitakapowarudishia mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la BWANA [Yehova, NW], wamtumikie kwa nia moja.”—SEFANIA 3:9.
1. Je! watu wamepata kumsikia Yehova akisema?
LUGHA ya Yehova Mungu ni safi. Lakini je! watu wamepata kumsikia akisema? Ndiyo! Jambo hilo lilitukia wakati Mwana wake, Yesu Kristo, alipokuwa duniani karne 19 zilizopita. Kwa mfano, Yesu alipobatizwa, Mungu alisikiwa akisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” (Mt. 3:13-17) Hiyo ilikuwa taarifa ya ukweli safi, iliyosikiwa na Yesu na Yohana Mbatizaji kwa lugha ya kibinadamu.
2. Ni nini imeonyeshwa na rejezo la mtume Paulo kwenye “lugha za . . . malaika”?
2 Miaka mingine baadaye mtume Mkristo Paulo alisema juu ya “lugha za wanadamu na za malaika.” (1 Wakorintho 13:1) Hiyo inaonyesha nini? Inaonyesha kwamba si wanadamu tu bali watu wa kiroho pia wana lugha na usemi! Bila shaka, Mungu na malaika hawawasiliani kwa kutumia sauti na lugha ambazo tunaweza kusikia na kuelewa. Kwa nini? Kwa sababu anga kama lile liizungukalo dunia li-nahitajiwa ili kueneza mawimbi ya sauti ya usemi ambayo wanadamu wanaweza kusikia na kuelewa.
3. Lugha ya kibinadamu ilianzaje?
3 Lugha ya kibinadamu ilianzaje? Wengine husema kwamba wazazi wetu wa kwanza walijitahidi kuwasiliana kwa kutumia miguno na mikoromo. Chasema kitabu Evolution (Life Nature Library): “Mtu-nyani wa karibu miaka milioni moja iliyopita . . . yawezekana alijifunza sauti chache za usemi.” Lakini Ludwig Koehler mtungaji wa kamusi mwenye kujulikana sana alisema hivi: “Usemi wa kibinadamu ni siri; ni zawadi ya kimungu, mwujiza.” Ndiyo, ‘usemi wa kibinadamu ni zawadi ya kimungu,’ kwa kuwa Mungu alimpa Adamu, mwanadamu wa kwanza, lugha. Kwa wazi ilikuwa ile ambayo hatimaye ilikuja kuitwa Kiebrania. Lugha hiyo ilisemwa na wazao Waisraeli wa “Abramu Mwebrania,” mzee wa ukoo mwaminifu ambaye mzazi wake wa jadi Shemu alikuwa mwana wa Noa yule mjenga-safina. (Mwanzo 11:10-26; 14:13; 17:3-6) Kwa sababu ya baraka ya Mungu ya kiunabii juu ya Shemu, inapatana na akili kukata maneno kwamba lugha yake haikuathiriwa na jambo ambalo Yehova alifanya kimwujiza karne 43 zilizopita.—Mwanzo 9:26.
4. Nimrodi alikuwa nani, naye alitumiwaje na Shetani Ibilisi?
4 Wakati ule “nchi yote ilikuwa na lugha moja na usemi mmoja.” (Mwanzo 11:1) Mwanamume Nimrodi alikuwa akiishi wakati ule, “mwindaji mwenye nguvu katika kupingana na Yehova.” (Mwanzo 10:8, 9, NW) Nimrodi alitumiwa hasa na Shetani, adui mkuu asiyeonekana wa ainabinadamu, aanzishe sehemu ya kidunia ya tengenezo la Ibilisi. Nimrodi alitaka kujifanyia jina, nao mtazamo huo wa kiburi ukaenea kwa wafuasi wake, ambao walianza mradi wa pekee wa ujenzi katika bara la Shinari. Kulingana na Mwanzo sura ya 11, mstari wa 4, walisema: “Haya, na tujijengee mji, na mnara, na kilele chake kifike mbinguni, tujifanyie jina; ili tusipate kutawanyika usoni pa nchi yote.” Mradi huo, uliopinga amri ya Mungu ya ‘kuijaza nchi’ ulifikia mwisho wakati Mungu alipovuruga lugha ya waasi. “Basi,” usimulizi wa Biblia wasema, “BWANA [Yehova, NW] akawatawanya kutoka huko waende usoni pa nchi yote; wakaacha kuujenga ule mji.” (Mwanzo 9:1; 11:2-9) Mji huo uliitwa Babeli, au Babuloni (kumaanisha “Mvurugo”), “kwa sababu huko Yehova alichanganya usemi wa dunia yote.”—Byington.
5. (a) Ni jambo gani lililozuiwa wakati Mungu alipovuruga lugha ya ainabinadamu? (b) Tunaweza kukata shauri gani juu ya lugha ya Noa na Shemu?
5 Mwujiza huo—mvurugo wa lugha ile moja ya wanadamu—uliongoza kwenye kuijaza dunia kama vile Mungu alivyokuwa amemwamuru Noa, na ulizuia mpango wowote ambao huenda Shetani angekuwa nao wa kuanzisha ibada iliyounganika isiyo safi ya kuabudiwa na wanadamu ambao walikuwa wameasi dhidi ya Bwana Mwenye Enzi Kuu wa mbingu na dunia. Kweli, kwa kuzoea dini bandia ya aina yoyote, watu hao walikuwa watekwa wa Ibilisi, na walikuwa wanatumikia roho waovu wakati walipofanya miungu ya kiume na ya kike, kuipa majina katika lugha zao mbalimbali na kuiabudu. (1 Wakorintho 10:20) Lakini tendo lililochukuliwa na yule Mungu wa pekee wa kweli huko Babeli lilizuia kuanzishwa kwa dini moja ya uongo iliyounganika ambayo ingempa Ibilisi ibada ambayo yaonekana alitamani sana. Bila shaka, Noa mwadilifu na mwana wake Shemu hawakuhusika kamwe katika kitukio hicho katika bara la Shinari. Kwa sababu hiyo, kupatana na akili inaweza kukatwa shauri kwamba lugha yao ilibaki ikiwa ile iliyosemwa na Abramu (au Abrahamu) mwaminifu—ile lugha ambayo Mungu aliongea na mwanadamu Adamu katika bustani ya Edeni.
6. Katika siku ya Pentekoste ya 33 W.K., Yehova alionyeshaje kwamba angeweza kutoa uwezo wa kuongea katika lugha mbalimbali?
6 Yehova, aliyevuruga lugha ya kwanza ya ainabinadamu, aweza kutoa uwezo wa kusema katika lugha mbalimbali pia. Kwani, alifanya jambo ilo hilo katika siku ya Pentekoste katika mwaka 33 Wakati wa Kawaida wetu! Kulingana na Matendo 2:1-11, wafuasi wa Yesu Kristo wapatao 120 walikuwa wamekusanyika katika chumba cha ghorofa katika Yerusalemu wakati huo. (Matendo 1:13, 15) Ghafula, kulikuwa na uvumi toka mbinguni “kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi.” ‘Ndimi kama za moto’ zikaonekana na zikagawanyika huku na huku. Ndipo, wanafunzi ‘wakajazwa roho takatifu na kuanza kunena kwa lugha nyingine, kama roho ilivyowajalia kutamka.’ Kwa lugha hizo walizopewa kimungu, walisema juu ya “matendo makuu ya Mungu.” Na huo ulikuwa mwujiza kama nini wakati Wayahudi na waongofu wa lugha tofauti-tofauti kutoka mahali palipotapakaa sana kama vile Mesopotamia, Misri, Libya, na Roma, walipoelewa ule ujumbe wenye kutoa uhai!
Lugha Yenye Kupewa na Mungu Leo!
7. Ni matumaini gani yangeweza kuwako ikiwa lugha moja tu ilikuwa ikisemwa na kueleweka ulimwenguni pote?
7 Kwa kuwa Mungu aweza kuwapa watu lugha tofauti-tofauti kimwujiza, je! halingekuwa jambo zuri ajabu kama angefanya iwezekane lugha moja tu isemwe na ieleweke ulimwenguni pote? Hiyo ingeendeleza ufahamiano mkubwa zaidi katika familia ya kibinadamu. Kama The World Book Encyclopedia kinavyolisema jambo hilo: “Kama vikundi vyote vya watu vingesema lugha ile ile moja, vifungo vya kitamaduni na kiuchumi vingekuwa karibu zaidi, na nia njema ingeongezeka kati ya nchi.” Basi, kumekuwa na lugha za ulimwengu wote angalau 600 zilizopendekezwa muda wa miaka iliyopita. Kati ya hizo, Esperanto imekuwa ndiyo yenye kufanikiwa zaidi kwa sababu watu wapatao 10,000,000 wamejifunza hiyo tangu ilipoundwa katika mwaka 1887. Hata hivyo, jitihada za kibinadamu za kuunganisha ainabinadamu kwa njia ya lugha ya ulimwenguni pote hazijapata kamwe kufanikiwa. Kwa hakika, matatizo mengi na mengi zaidi yanasababisha mgawanyiko katika ulimwengu huu kadiri ‘watu wabaya wazidivyo kuwa waovu.’—2 Timotheo 3:13.
8. Hata ikiwa lugha ya ulimwengu wote ingechaguliwa katika ulimwengu wa leo, ni jambo gani lingekuwako bado, na kwa nini?
8 Kusema kidini, kuna mvurugo mkubwa. Lakini, je, tusitarajie hivyo, kwa kuwa kitabu cha Biblia cha Ufunuo huita milki ya ulimwengu ya dini bandia “Babuloni Mkubwa”? (Ufunuo 18:2, NW) Ndiyo, kwa maana “Babuloni” humaanisha “Mvurugo.” Hata kama lugha ya kubuniwa au lugha fulani ya kiasili, kama vile Kiingereza, Kifaransa, Kijerumani, au Kirusi ingekubaliwa kuwa lugha ya ulimwengu wote mzima katika ulimwengu wa leo, ukosefu wa muunganiko bado ungekuwako kidini na vinginevyo. Kwa nini? Kwa sababu “dunia [ulimwengu mzima, NW] yote pia hukaa katika yule mwovu,” Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Yeye ndiye mfano hususa wa ubinafsi, naye hutamani sana kwa pupa aabudiwe na ainabinadamu wote, kama vile alivyofanya katika siku za Nimrodi na Mnara wa Babeli. Kwani, lugha ya ulimwengu wote mzima ikisemwa na wanadamu wenye dhambi hata ingempa Shetani fursa ya kuanzisha ibada ya Ibilisi iliyounganika! Lakini Yehova hataruhusu hilo kamwe; kwa kweli, karibuni atamaliza dini zote bandia zenye kuongozwa na Ibilisi.
9. Watu wa mataifa na jamii zote wanaunganishwaje sasa?
9 Hata hivyo, uhakika wenye kushangaza ni kwamba watu wema wa mataifa yote na jamii wanaunganishwa sasa hivi. Jambo hilo linatukia kwa masharti ya Mungu na kwa ajili ya ibada yake. Leo, Mungu anawezesha wanadamu kujifunza na kusema lugha iliyo safi pekee duniani. Na kwa kweli hiyo ni lugha ya ulimwengu wote mzima. Kwa kweli, Yehova Mungu anafundisha watu wengi kutoka kwa mataifa yote ya duniani leo lugha hiyo safi. Hilo ni katika utimizo wa ahadi ya Mungu ya kiunabii kupitia nabii na shahidi wake Sefania: “Maana hapo ndipo nitakapowarudishia mataifa lugha iliyo safi [kihalisi, “mdomo safi”], wapate kuliitia jina la BWANA [Yehova, NW], wamtumikie kwa nia moja.” (Sefania 3:9) Ni nini hiyo “lugha iliyo safi”?
Lugha Iliyo Safi Inaelezwa Wazi
10. Lugha iliyo safi ni nini?
10 Lugha iliyo safi ni ukweli wa Mungu una-opatikana katika Neno lake mwenyewe, yale Maandiko Matakatifu. Hasa ni ukweli kuhusu Ufalme wa Mungu, ambao utaleta amani na baraka nyinginezo kwa ainabinadamu. Lugha safi huondolea mbali makosa ya kidini na ibada bandia. Huunganisha wote ambao huisema katika ile ibada yenye utakato, iliyo safi, iletayo hali njema, ya yule Mungu aishiye na wa kweli, Yehova. Leo, lugha zipatazo 3,000 hutenda kama kizuizi cha uelewevu, na mamia ya dini bandia huvuruga ainabinadamu. Kwa hiyo tunaterema kama nini kwamba Mungu anawapa vikundi vya watu badilisho kwenye hii lugha safi iliyo nzuri ajabu!
11. Lugha iliyo safi imewafanyia nini watu wa mataifa na jamii zote?
11 Ndiyo, watu wa mataifa na jamii zote wanajifunza lugha iliyo safi. Ikiwa ndiyo lugha pekee ya kiroho iliyo safi duniani, inatumika ikiwa kani yenye uweza wa kuunganisha. Inawezesha wote wanaoisema ‘kuliitia jina la Yehova, ili wamtumikie kwa nia moja,’ au kihalisi, “kwa bega moja.” Hivyo wanatumikia Mungu “kwa ukubali mmoja,” “kwa ukubali mmoja wa mapatano ya wote na bega moja lililounganishwa.” (The New English Bible; The Amplified Bible) Tafsiri ya Steven T. Byington husomwa hivi: “Ndipo mimi [Yehova Mungu] nitageuza midomo ya vikundi vyote vya watu kuwa safi, kwamba wote waweze kuita juu ya jina la Yehova na kushirikiana katika utumishi wake.” Ushirikiano kama huo wa ulimwenguni pote wa lugha nyingi katika utumishi wa Mungu umo tu miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Katika nchi 212 leo, hao wapiga mbiu ya Ufalme zaidi ya milioni nne wanahubiri habari njema katika lugha nyingi za kibinadamu. Hata hivyo, Mashahidi ‘husema kwa mwafaka’ na ‘wameunganika kwa kufaa katika akili moja na mstari mmoja wa fikira.’ (1 Wakorintho 1:10, NW) Iko hivyo kwa sababu, hata wawe wapi duniani, Mashahidi wa Yehova wote husema ile lugha moja iliyo safi, kwa sifa na utukufu wa Baba yao wa kimbingu.
Jifunze Lugha Iliyo Safi Sasa!
12, 13. (a) Kwa sababu gani uhangaikie kusema lugha iliyo safi? (b) Kwa nini maneno katika Sefania 3:8, 9 ni yenye maana leo?
12 Kwa sababu gani uhangaikie kusema hiyo lugha iliyo safi? Jambo moja, ni kwa sababu uhai wako wategemea kujifunza na kuisema. Kabla tu ya Mungu kuahidi ‘kuwarudishia mataifa lugha iliyo safi,’ alionya hivi: “Basi ningojeni, asema BWANA [Yehova, NW], hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu.”—Sefania 3:8.
13 Maneno hayo ya Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu yalisemwa kwanza karne 26 zilizopita katika Yuda, ambayo Yerusalemu ulikuwa mji mkuu wayo. Lakini taarifa hiyo ilimaanishwa hasa kwa ajili ya siku zetu kwa sababu Yerusalemu ulikuwa kifani cha Jumuiya ya Wakristo. Na wakati wetu, tangu Ufalme wa Mungu wa kimbingu usimamishwe katika 1914, ni siku ya Yehova ya kuleta pamoja mataifa na kukusanya falme. Ameyaleta yote pamoja chini ya uangalio wake kwa njia ya kazi kubwa ya ushahidi. Hilo nalo, limeyasukuma kupinga kusudi lake. Hata hivyo, kwa rehema Yehova Mungu anawezesha baadhi ya watu wa mataifa yote waungane katika kusema lugha iliyo safi. Wakiwa nayo, wote wanaotafuta uhai katika ulimwengu wake mpya ulioahidiwa waweza kumtumikia kwa sauti moja kabla ya mataifa yote kuliwa na wonyesho wenye moto wa ghadhabu ya kimungu kwenye “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,” ambayo kwa kawaida huitwa Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16; 2 Petro 3:13) Kwa furaha, wale wanaosema lugha iliyo safi na kuita juu ya jina la Yehova kwa imani wakiwa waabudu wa kweli waliounganika wataonea shangwe kinga ya kimungu wakati wa joto la msiba huo wa ulimwengu. Mungu atawaleta wakiwa salama katika ulimwengu mpya, ambamo hatimaye ni lugha iliyo safi pekee itakuwa midomoni mwa ainabinadamu yote.
14. Kupitia Sefania, Mungu alionyeshaje kwamba kuokoka mwisho wa mfumo huu wa mambo kunahitaji tendo la sasa hivi?
14 Kupitia nabii wake Sefania, Yehova huelewesha wazi kwamba wale wanaotumaini kuokoka mwisho wa mfumo mwovu wa mambo uliopo lazima wachukue hatua sasa hivi. Kulingana na Sefania 2:1-3, Mungu asema hivi: “Jikusanyeni, naam, jikusanyeni, Ee taifa lisilo na haya; kabla haijazaa hiyo amri, kabla haijapita siku ile kama makapi, kabla haijawajilia hasira kali ya BWANA [Yehova, NW], kabla haijawajilia siku ya hasira ya BWANA [Yehova, NW]. Mtafuteni BWANA [Yehova, NW] enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA [Yehova, NW].”
15. (a) Utimizo wa kwanza wa Sefania 2:1-3 ulikuwa gani? (b) Ni nani waliookoka tekelezo la hukumu la Mungu juu ya Yuda, na ni nini itakayokuwa sawa na wokovu huo katika siku yetu?
15 Maneno hayo yalikuwa na utimizo wa kwanza juu ya Yuda na Yerusalemu ya kale. Watu wenye dhambi wa Yuda hawakuitikia ifaavyo kwa kusihi kwa Yehova, kama ionyeshwavyo na utekelezo wa hukumu yake juu yao mikononi mwa Babuloni katika mwaka 607 K.W.K. Kama vile Yuda lilivyokuwa “taifa lisilo na haya” mbele za Mungu, ndivyo Jumuiya ya Wakristo imekuwa “taifa” lisilo na haya mbele za Yehova. Hata hivyo, kwa sababu ya kutii neno la Yehova, baadhi ya Wayudea na wengine waliokoka, miongoni mwao nabii mwaminifu wa Yehova Yeremia. Waokokaji wengine walikuwa Mwethiopia aitwaye Ebed-meleki na wazao wa Yehonadabu. (Yeremia 35:18, 19; 39:11, 12, 16-18) Vivyo hivyo leo, “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Yesu waliokusanywa kutoka mataifa yote wataokoka Har–Magedoni waingie ndani ya ulimwengu mpya wa Mungu. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:14-16) Wale tu ambao hujifunza na kuisema lugha iliyo safi ndio watakuwa waokokaji wenye shangwe.
16. Ni lazima mtu afanye nini ili kufichwa ‘katika siku ya hasira ya Yehova’?
16 Kama vile ilivyokuwa amri ya Yehova kwamba Yuda na Yerusalemu ifutiliwe mbali, ndivyo ilivyo lazima Jumuiya ya Wakristo ipotelee mbali. Kwa kweli, uharibifu wa dini zote bandia uko karibu, na wale wanaotaka kuokoka lazima watende mara moja. Ni lazima wafanye hivyo “kabla haijapita siku ile kama makapi,” ikipeperushwa kasi na upepo, kama wakati nafaka inaporushwa hewani kwenye sakafu ya kupuria. Ili tukombolewe na ghadhabu ya Mungu, lazima sisi tuseme lugha iliyo safi na kuitikia onyo la Mungu kabla siku ya hasira kali ya Yehova haijatujilia. Katika siku ya Sefania na leo, “wanyenyekevu” hutafuta Yehova, pamoja na uadilifu na unyenyekevu. Kutafuta kwetu Yehova kunamaanisha kumpenda kwa moyo wetu wote, nafsi yetu yote, akili zetu zote, na nguvu zetu zote. (Marko 12:29, 30) ‘Huenda wale wanaofanya hivyo wakafichwa katika siku ya hasira ya Yehova.’ Lakini kwa nini unabii wasema “huenda”? Kwa sababu wokovu wategemea uaminifu na uvumilivu. (Mathayo 24:13) Wale wanaojipatanisha na viwango vya uadilifu vya Mungu na huendelea kusema lugha iliyo safi watafichwa katika siku ya hasira ya Yehova.
17. Ni maswali gani yanayobaki ya kufikiriwa nasi?
17 Kwa kuwa siku ya hasira ya Yehova i karibu na wokovu wategemea kujifunza na kutumia lugha iliyo safi, sasa ndio wakati wa kujihusisha sana katika kujifunza na kuisema. Lakini mtu aweza kujifunzaje hiyo lugha iliyo safi? Na unawezaje kunufaika kutokana na kuisema?
Ungejibuje?
◻ Lugha ya kibinadamu ilianzaje?
◻ Lugha iliyo safi ni nini?
◻ Kwa nini maneno katika Sefania 3:8, 9 ni yenye maana leo?
◻ Ni lazima tufanye nini ili tufichwe ‘katika siku ya hasira ya Yehova’?
-
-
Semeni Lugha Iliyo Safi Mkaishi Milele!Mnara wa Mlinzi—1991 | Mei 1
-
-
Semeni Lugha Iliyo Safi Mkaishi Milele!
“Mtafuteni BWANA [Yehova, NW], . . . itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA [Yehova, NW].”—SEFANIA 2:3.
1. (a) Wanafunzi hutumia njia gani kujifunza lugha ya kigeni? (b) Kwa nini tuseme lugha iliyo safi?
HUENDA wanafunzi wakajifunza lugha mpya kwa kufuata sarufi au kwa kuiga jinsi isemwavyo. Chini ya ile njia ya kufuata sarufi, kwa kawaida wao hutumia vitabu vya mafunzo na hujifunza kanuni za sarufi. Katika ile njia ya kuiga jinsi lugha isemwavyo, wanaiga sauti na violezo vya maneno vinavyosemwa na mwalimu wao. Njia zote mbili hutumika katika kujifunza “lugha iliyo safi.” Na ni muhimu kwamba tuseme lugha hiyo ikiwa tunatumaini ‘kufichwa katika siku ya hasira ya Yehova.’—Sefania 2:1-3; 3:8, 9.
2. Tunaweza kujifunzaje zile zinazoweza kuitwa kanuni za kisarufi za lugha iliyo safi?
2 Kitabu kikuu cha mafunzo kinachotumiwa katika kujifunza lugha iliyo safi ni Biblia. Funzo layo lenye bidii nyendelevu na la vichapo vyenye msingi wa Biblia lakufundisha kile kinachoweza kuitwa kanuni za sarufi za lugha iliyo safi. Funzo la Biblia nyumbani likiongozwa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova ni mwanzo mzuri. Kwa wale walio wakfu tayari kwa Mungu, funzo la kawaida lenye bidii nyendelevu la Maandiko ni la lazima. Lakini je, kuna njia hasa zenye matokeo mazuri za kujifunzia lugha iliyo safi? Na kuna manufaa gani kwa kuisema?
Jinsi ya Kujifunza Lugha Iliyo Safi
3. Njia moja ya kujifunza lugha iliyo safi ni ipi?
3 Njia moja ya kujifunza lugha iliyo safi ni kwa kushirikisha kweli unazojifunza na mambo unayojua tayari, kama vile mwanafunzi wa lugha kwa kuendelea aweza kuhusianisha kanuni za kisarufi. Kwa mfano, wakati mmoja huenda ikawa ulijua kwamba Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu, lakini hukujua mengi kuhusu kazi zake. Tangu hapo, huenda funzo la Biblia likawa lilikufunza kwamba Kristo anatawala sasa akiwa Mfalme wa kimbingu na kwamba katika Utawala wake wa Miaka Elfu, ainabinadamu watiifu watainuliwa kwenye ukamilifu. (Ufunuo 20:5, 6) Ndiyo, ufahamu wako wa lugha iliyo safi huendelezwa unaposhirikisha mambo mapya na yale unayojua tayari.
4. (a) Njia nyingine ya kujifunza ‘kanuni za kisarufi’ za lugha iliyo safi ni ipi, na ni simulizi lipi la Biblia linatumiwa kueleza jambo hilo? (b) Ni nini kilichotokea Gideoni na wanaume wake mia tatu walipoanza kutenda? (c) Simulizi juu ya Gideoni linafundisha somo gani?
4 Njia nyingine ya kujifunza ‘kanuni za kisarufi’ za lugha iliyo safi ni kuona akilini mwako matukio yaliyoandikwa katika Biblia. Ili kutoa kielezi: Jaribu ‘kuona na kusikia’ simulizi lililorekodiwa katika Waamuzi 7:15-23. Tazama! Mwamuzi Mwisraeli Gideoni amegawanya jeshi lake kuwa vikosi vitatu vya mia kila kimoja. Kwa kimya, chini ya kisitiri cha giza, washuka Mlima Gilboa na kuzunguka kambi ya Wamidiani wanaolala usingizi. Je! hawa 300 wana silaha za kutosha? Kijeshi, la. Kwani, wangetokeza kicheko cha dhihaka kwa wanajeshi wenye kiburi! Kila mmoja wao ana pembe tu, mtungi mkubwa mmoja wa maji, na mwanga ndani ya mtungi huo. Lakini sikiliza! Kwa ishara waliyopewa, wale wanaume mia moja walio pamoja na Gideoni wapuliza pembe zao na kuvunja mitungi yao ya maji. Ndivyo na wale wengine 200. Wote wainuapo juu mianga yenye kuwaka, unawasikia wakipaaza sauti: “Upanga wa BWANA [Yehova, NW] na wa Gideoni”! Jinsi hilo linahofisha Wamidiani! Watoka katika mahema yao, huku macho yao yaliyojaa usingizi yakiwa yamekodolewa kwa kuogopeshwa na miwako yenye kuruka ambayo yakuza maumbo yenye kivuli na kuwasha hofu za kishirikina. Wamidiani waanzapo kukimbia, wanaume wa Gideoni wanaendelea kupuliza pembe zao, naye Yehova afanya panga za mahasimu hao ziwe dhidi ya mmoja na mwenzake. Ni somo lenye nguvu kama nini katika lugha iliyo safi! Mungu aweza kukomboa watumishi wake bila jeshi la kibinadamu. Zaidi ya hilo, “BWANA [Yehova, NW], hataacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu.”—1 Samweli 12:22.
5. Mikutano ya Kikristo inaweza kusafishaje usemi wetu?
5 Wanafunzi wanapofunzwa lugha mpya kwa ile njia ya kuiga jinsi lugha isemwavyo, wao hujaribu kurudia sauti na violezo vya maneno ya mwalimu kwa usahihi. Kuna fursa nzuri kama nini za kusema lugha iliyo safi kwenye mikutano ya Kikristo! Humo twasikia wengine wakijieleza wenyewe katika lugha hiyo ya ukweli wa Kimaandiko, na huenda tukawa na pendeleo la kutoa maelezo sisi wenyewe. Je! sisi huhofu kwamba huenda tukasema jambo lisilo sahihi? Acheni hilo lisiwe jambo letu kuu la kuhangaikia, kwa kuwa kosa linalosahihishwa kwa fadhili na mzee anayesimamia mkutano kama vile Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma, laweza kusafisha usemi wetu. Kwa hiyo, hudhuria na ushiriki katika mikutano ya Kikristo kwa ukawaida.—Waebrania 10:24, 25.
Machujo ya Uchafu
6. Kwa sababu gani kuna tofauti kubwa sana kati ya Mashahidi wa Yehova na matengenezo ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo?
6 Wale wanaojulisha wazi kusudi la Yehova na kutangaza Ufalme wake wa kimbingu wanasema lugha iliyo safi wakiwa Mashahidi wake. Wanajulisha jina lake na kumtumikia “kwa nia moja,” au kwa ukubali mmoja. (Sefania 3:9) Ingawa dini za Jumuiya ya Wakristo zina Biblia, hazisemi lugha iliyo safi wala kuita juu ya jina la Mungu kwa imani. (Yoeli 2:32) Hawana ujumbe wenye upatani unaotegemea Maandiko. Kwa nini? Kwa sababu wao huweka mapokeo ya kidini, falsafa za kilimwengu, na ushikamanifu wa kisiasa juu ya Neno la Mungu. Makusudi, matumaini, na njia zao zote ni za ulimwengu mbovu huu.
7. Kwenye 1 Yohana 4:4-6 ni tofauti zipi zinazoonyeshwa kati ya Mashahidi wa Yehova na dini bandia?
7 Jumuiya ya Wakristo—kwa hakika, milki nzima ya ulimwengu ya dini bandia—haisemi lugha kama ile Mashahidi wa Yehova husema. Kwa kupendeza, mtume Yohana aliwaandikia wale wanaisema lugha iliyo safi hivi: “Mwatokana na Mungu; nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu [aliye katika muungano pamoja na nyinyi, NW] ni mkuu kuliko yeye aliye katika [muungano pamoja na, NW] dunia. Hao ni wa dunia; kwa hiyo wanena ya dunia na dunia huwasikia. Sisi twatokana na Mungu. Yeye amjuaye Mungu atusikia; yeye asiyetokana na Mungu hatusikii.” (1 Yohana 4:4-6) Watumishi wa Yehova wamewashinda walimu bandia kwa sababu Mungu, aliye mmoja na watu wake, “ni mkuu kuliko yeye [Ibilisi, aliye katika muungano pamoja na, NW] dunia,” jamii ya kibinadamu isiyo adilifu. Kwa kuwa waasi-imani “ni wa dunia” na wana roho yayo mbovu, “wanena ya dunia na dunia huwasikia.” Lakini watu walio kama kondoo husikiliza wale ambao hutokana na Mungu, waking’amua kwamba watu wa Yehova husema lugha iliyo safi ya ukweli wa Biblia unaoandaliwa kupitia tengenezo lake.
8. Mtu wa kuasi ni nani?
8 Uasi-imani mkubwa ulitabiriwa, na ‘siri ya uasi’ ilikuwa tayari ikifanya kazi katika karne ya kwanza ya W.K. Wakati ulipopita, wanaume waliokubali—au kunyakua—madaraka ya kufundisha katika kundi walifunza mafundisho mengi bandia. Lugha yao haikuwa safi hata kidogo. Kwa sababu hiyo, alizuka “mtu wa kuasi” mwenye kujumlisha wengi, wale makasisi wa Jumuiya ya Wakristo, waliojifunganisha na mapokeo bandia ya kidini, falsafa ya kilimwengu, na mafundisho yasiyo ya kimaandiko.—2 Wathesalonike 2:3, 7.
Lugha Iliyo Safi Yasikika
Ulimwenguni Pote
9. Ni matukio gani ya kidini yaliyokuwako muda wa karne ya 19?
9 Ni kikundi kidogo tu cha watu wenye kuhofu Mungu ‘kilichoshindania imani waliyokabidhiwa watakatifu.’ (Yuda 3) Waamini kama hao wangepatikana wapi? Kwa karne nyingi, dini bandia iliweka watu wengi katika giza la kiroho, lakini Mungu alijua wale wachache waliokuwa na kibali chake. (2 Timotheo 2:19) Halafu, katikati ya mabadiliko ya kibiashara, kiviwanda, na kijamii ya karne ya 19, kulizuka sauti zilizojitokeza kutoka kwa machafuko yenye mvurugo wa kidini. Vikundi vidogo vilijaribu kusoma ishara za nyakati na kutabiri kuja kwa pili kwa Yesu Kristo, lakini si wote waliokuwa wakisema lugha iliyo safi.
10. Ni kikundi gani cha “kuja kwa pili” kilichochaguliwa na Mungu kusema lugha iliyo safi, na kwa nini ni dhahiri kwamba mkono wa Yehova umekuwa nao?
10 Hata hivyo, katika 1879, ilipata kuwa wazi ni sauti gani ya “kuja kwa pili” ilikuwa ikichaguliwa na Yehova iseme lugha iliyo safi ikiwa Mashahidi wake. Kufikia wakati huo, kikundi kidogo cha funzo la Biblia kikiongozwa na Charles Taze Russell kilikuwa kikikutania Pittsburgh, Pennsylvania, U.S.A. Walikuwa wamekuwa na uhakika kwamba kuja kwa pili kwa Yesu kungeanza kuwapo kwake kusikoonekana, kwamba wakati wa taabu ya ulimwengu ulikuwa mbele, na kwamba ungefuatwa na Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo ambao ungetokeza kurudishwa kwa Paradiso duniani, pamoja na uhai wa milele kwa wanadamu watiifu. Katika Julai 1879 hao Wanafunzi wa Biblia walianza kuchapisha lile gazeti linalojulikana sasa kuwa Mnara wa Mlinzi. Nakala 6,000 tu za toleo lalo la kwanza ndizo zilizogawanywa. Lakini “mkono wa Yehova” ulikuwa pamoja na Mashahidi hao, kwa maana jarida hili linachapishwa sasa kwa lugha 111 likiwa na wastani wa kuchapa wa zaidi ya nakala 15,000,000 kwa kila toleo.—Linganisha Matendo 11:19-21, NW.
11, 12. Ni zipi baadhi ya kweli za Kimaandiko ambazo wale wanaosema lugha iliyo safi huelewa?
11 Kupitia Biblia na vichapo vya Mashahidi wa Yehova, na hasa kwa upigaji mbiu wa hawa Wakristo wenye bidii wa habari njema, lugha iliyo safi imekuja kujulikana duniani pote. Na ni manufaa kubwa kama nini zinazoonewa shangwe na wale wanaoisema! Badala ya kusema kwamba ‘Mungu ni Mungu, Kristo ni Mungu, na Roho Mtakatifu ni Mungu’ katika ile lugha ya kifumbo isiyoeleweka ya Utatu, wanakubaliana na msimamo wa Biblia kwamba Yehova ndiye Mungu Aliye Juu Zaidi, Yesu Kristo aliye mdogo zaidi ni Mwana Wake, na roho takatifu ni kani ya utendaji ya Mungu yenye kustaajabisha. (Mwanzo 1:2; Zaburi 83:18; Mathayo 3:16, 17) Wasemaji wa lugha iliyo safi wajua kwamba mwanadamu hakugeuka-geuka kutoka namna ya chini zaidi ya uhai bali aliumbwa na Mungu mwenye upendo. (Mwanzo 1:27; 2:7) Wanang’amua kwamba nafsi hukoma kuwako wakati wa kufa—uhakika ambao huondolea mbali kuhofu wafu. (Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4) Helo hueleweka kuwa kaburi la kawaida la ainabinadamu, si mahali penye moto wa mateso palipobuniwa na mungu mkatili. (Ayubu 14:13) Wanajua pia kwamba ufufuo ndio tumaini la wafu lililotolewa na Mungu.—Yohana 5:28, 29; 11:25; Matendo 24:15.
12 Wale wanaosema lugha iliyo safi huonyesha staha kwa damu na uhai. (Mwanzo 9:3, 4; Matendo 15:28, 29) Wanang’amua kwamba uhai wa kidunia wa Kristo ndio ukombozi uliolipwa kwa ajili ya wanadamu watiifu. (Mathayo 20:28; 1 Yohana 2:1, 2) Hawasali kamwe kwa “watakatifu,” wakijua kwamba ni lazima sala zao zielekezwe kwa Yehova Mungu kupitia Yesu Kristo. (Yohana 14:6, 13, 14) Kwa kuwa Neno la Mungu linalaumu ibada-sanamu, sanamu hazitumiwi katika ibada yao. (Kutoka 20:4-6; 1 Wakorintho 10:14) Nao huepuka hatari za uhusiano na roho waovu kwa sababu wanakataa uwasiliani-roho, ambao pia umelaumiwa katika Biblia.—Kumbukumbu 18:10-12; Wagalatia 5:19-21.
13. Kwa nini wale ambao husema lugha iliyo safi hawatataniki?
13 Watumishi wa Yehova, ambao husema lugha iliyo safi, hawatataniki wasijue wako wapi katika mkondo wa wakati. Yehova amewafundisha kwamba wako katika “wakati wa mwisho,” Yesu Kristo akiwepo akiwa roho mtukufu asiyeonekana. (Danieli 12:4; Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5; 1 Petro 3:18) Akifuatwa na majeshi ya kimbingu yenye uweza, Kristo yuko karibu kupanda aingie katika pigano kutekeleza hukumu ya Mungu dhidi ya mfumo huu wa mambo. (Danieli 2:44; Ufunuo 16:14, 16; 18:1-8; 19:11-21) Ndiyo, na wale wanaosema lugha iliyo safi wana shughuli sana wakijulisha wazi zile habari njema kwamba karibuni Ufalme wa Mungu chini ya Yesu Kristo utaleta mibaraka mitukufu kwa ainabinadmu wote watiifu katika dunia-paradiso. (Isaya 9:6, 7; Danieli 7:13, 14; Mathayo 6:9, 10; 24:14; Luka 23:43) Yote hayo, na bado tumegusia-gusia kijuujuu tu! Kwa hakika, lugha iliyo safi ndiyo lugha yenye utajiri zaidi, yenye thamani zaidi duniani!
14. Ni manufaa gani nyingine zinazoonewa shangwe na wale wanaosema lugha iliyo safi?
14 Manufaa yanayoonewa shangwe na wale wanaosema lugha iliyo safi, yanatia ndani “amani ya Mungu” inayolinda mioyo na nguvu za kufikiri. (Wafilipi 4:6, 7) Wanatii she-ria za Biblia, ambazo huendeleza afya, furaha, na uradhi ambao hutokana na kumpendeza Yehova. (1 Wakorintho 6:9, 10) Ndiyo, na wasemaji wa lugha iliyo safi wana tumaini la kupata uhai wa milele katika ulimwengu mpya alioahidi Mungu.—2 Petro 3:13.
Uitumie au Uipoteze
15. Wewe utanufaikaje kutokana na ufahamu mzuri wa lugha iliyo safi?
15 Ikiwa utasema lugha iliyo safi katika ulimwengu mpya, ni lazima uijue vizuri sana hivi kwamba inakuwa ndiyo lugha ambayo katika hiyo wewe wafikiri. Wakati mtu anapokuwa akijifunza lugha, kwanza anafikiri katika lugha yake ya kienyeji na kufasiri mawazo yake katika ile mpya. Lakini apatapo kuwa stadi zaidi katika ile lugha mpya, anaanza kufikiri katika hiyo bila kuhitaji kuitafsiri. Vivyo hivyo, kupitia funzo la bidii nyendelevu, waweza kupata ufahamu mzuri wa lugha iliyo safi hivi kwamba utajua jinsi ya kutumia sheria na kanuni za Biblia ili kutatua matatizo na kubaki katika “kile kijia cha uhai.”—Zaburi 16:11, NW.
16. Ni jambo gani ambalo laweza kutokea ikiwa wewe husemi lugha iliyo safi kwa kawaida?
16 Ni lazima uitumie lugha iliyo safi kwa ukawaida, au sivyo utapoteza uwezo wa kuisema kwa ustadi. Kwa kielelezo: Miaka kadhaa iliyopita, baadhi yetu tulijifunza lugha ya kigeni. Huenda tukakumbuka maneno machache katika lugha hiyo lakini yaelekea kwamba tumepoteza ustadi wetu wa kuisema kwa kuwa hatuitumii daima. Jambo ilo hilo laweza kutukia kwa lugha iliyo safi. Tusipoitumia kwa ukawaida, twaweza kupoteza ustadi wetu wa kuisema, na hiyo ingeleta matokeo yenye kuhuzunisha kiroho. Kwa hiyo acheni tuiseme kwa ukawaida kwenye mikutano na katika huduma ya Kikristo. Utendaji huo, pamoja na funzo la kibinafsi, utatuwezesha kusema mambo kwa usahihi katika lugha iliyo safi. Na hilo ni jambo la maana kama nini!
17. Ni nini kinachotoa kielezi kwamba usemi waweza kuwa wenye kuokoa uhai au wenye kuleta kifo?
17 Usemi waweza kuwa wenye kuokoa uhai au kuleta kifo. Hiyo ilionyeshwa wakati wa pigano kati ya kabila la Waisraeli la Waefraimu na Mwamuzi Yeftha wa Gileadi. Ili kuwatambulisha Waefraimu waliokuwa wakijaribu kutorokea ng’ambo ya Mto Yordani, Wagileadi walitumia neno la siri “Shibolethi,” ambalo lilikuwa na sauti “sh” ya kuanzia. Wanaume wa Efraimu walijisaliti wazi kwa askari wa Gileadi kando ya Yordani kwa kusema “Sibolethi” badala ya “Shibolethi,” wakiwa wanatamka vibaya sauti ya kuanzia ya neno hilo. Kama tokeo, Waefraimu 42,000 waliuawa! (Waamuzi 12:5, 6) Vivyo hivyo, yale yanayofundishwa na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo huenda yakasikika kuwa karibu na lugha iliyo safi kwa wale ambao hawafahamu vizuri ukweli wa Biblia. Lakini kusema katika njia bandia ya kidini kutathibitika kuwa na msiba wa kifo katika siku ya hasira ya Yehova.
Tunabaki Tumeunganishwa
18, 19. Maana ya Sefania 3:1-5 ni nini?
18 Kwa kurejezea Yerusalemu wa kale usio mwaminifu na kifani chake cha ki-siku-hizi, Jumuiya ya Wakristo, inasemwa kwenye Sefania 3:1-5 hivi: “Ole wake yeye aliyeasi na kutiwa unajisi, mji wa udhalimu! Hakuitii sauti; hakukubali kurudiwa [nidhamu, NW]; hakumwamini BWANA [Yehova, NW]; hakumkaribia Mungu wake. Wakuu wake walio ndani yake ni simba wangurumao; makadhi wake ni mbwa-mwitu wa jioni; hawasazi kitu cho chote hata siku ya pili. Manabii wake ni watu hafifu, wadanganyifu; makuhani wake wamepatia unajisi patakatifu, wameifanyia sheria udhalimu. BWANA [Yehova, NW] kati yake ni mwenye haki; hatatenda uovu; kila asubuhi hudhihirisha hukumu yake, wala hakomi; bali mtu asiye haki hajui kuona haya.” Ni nini maana ya maneno hayo?
19 Yerusalemu ya kale na pia Jumuiya ya Wakristo ya ki-siku-hizi waliasi dhidi ya Yehova na kujichafuza kwa ibada bandia. Utendaji kosa wa viongozi wao ulitokeza udhalimu. Yajapokuwa maonyo ya Mungu yaliyorudiwa-rudiwa, hawakusikiliza wamkaribie. Wakuu wao wamekuwa kama simba wenye pupa, wakipuuza uadilifu kwa kiburi. Mahakimu wao wamchana-chana haki kama mbwa-mwitu wenye njaa kuu. Makuhani wao ‘wamenajisi kilicho kitakatifu na kufanya jeuri kwa sheria’ ya Mungu. Kwa hiyo, Yehova yuko karibu ‘kukusanya mataifa na kuzikutanisha falme, ili kuzimwagia ghadhabu yake, ukali wote wa hasira yake.’—Sefania 3:8.
20. (a) Ni nini lazima kifanywe ili kuokoka siku ya hasira ya Yehova? (b) Unaweza kupataje tumaini la kuonea shangwe mibaraka ya milele kutoka kwa Mungu?
20 Siku ya hasira ya Yehova inakaribia kwa haraka. Kwa hiyo, ili kuokoka na kuingia ndani ya ulimwengu mpya wa Mungu, jifunze na uiseme lugha iliyo safi bila kukawia. Ni kwa kufanya hivyo tu ndio utapata ulinzi kutokana na msiba wa kiroho sasa na kutokana na afa la tufe lote linalokaribia kwa kasi. Mashahidi wa Yehova wanatangaza rasmi siku ya hasira ya Mungu na ujumbe wenye kutia moyo wa Ufalme wake. Wao hupendezwa kama nini kuongea juu ya umaliki wake wenye utukufu! (Zaburi 145:10-13) Unganishwa nao, nawe waweza kutumaini kuonea shangwe uhai wa milele na mibaraka mingineyo kutoka kwa Mwanzishi wa lugha iliyo safi, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.
Wewe Ungejibuje?
◻ Ni zipi njia mbalimbali za kujifunza lugha iliyo safi?
◻ Kwa nini inanufaisha kusema lugha iliyo safi?
◻ Ni jambo gani linaloweza kutokea ikiwa hutumii lugha iliyo safi kwa ukawaida?
◻ Mtu aweza kuokokaje siku ya hasira ya Yehova na kuonea shangwe mibaraka ya milele?
-