Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 1/1 kur. 26-29
  • Acheni Tukirihi Lililo Ovu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Acheni Tukirihi Lililo Ovu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kulidumisha Kutaniko Likiwa Safi
  • Matokeo Yasiyoepukika
  • Mkristo Aliyejiweka Wakfu Afanyapo Dhambi
  • Namna Gani Mwenye Kuwasumbua Watoto Kingono?
  • Kupambanua Udhaifu, Uovu, na Toba
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Yehova Husamehe kwa Njia Kubwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Kubali Sikuzote Nidhamu ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Je, Umeitendea Dhambi Roho Takatifu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 1/1 kur. 26-29

Acheni Tukirihi Lililo Ovu

YEHOVA ni Mungu mtakatifu. Katika nyakati za kale alikuwa “Mtakatifu wa Israeli,” na akiwa hivyo alitaka kwamba Israeli liwe safi, bila doa. (Zaburi 89:18) Aliwaambia watu wake wachaguliwa hivi: “Mtakuwa watakatifu, kwa kuwa mimi ni Mtakatifu.” (Mambo ya Walawi 11:45) Yeyote yule aliyetaka “[ku]panda katika mlima wa BWANA” alihitaji kuwa “na mikono safi na moyo mweupe.” (Zaburi 24:3, 4) Hilo lilimaanisha mengi zaidi kuliko kuepuka tu matendo yenye dhambi. Lilimaanisha “kuchukia uovu.”—Mithali 8:13.

Kwa upendo, Yehova aliweka sheria zilizotia ndani mambo mengi ili taifa la Israeli liweze kutambua na kuepuka makosa. (Waroma 7:7, 12) Sheria hizo zilitia ndani miongozo kamili juu ya adili. Uzinzi, matendo ya ugoni-jinsia-moja, mahusiano ya ngono ya maharimu (watu wa ukoo), na ngono na mnyama, mambo hayo yote yalitambuliwa kuwa vichafuzi vya kiroho visivyo vitakatifu. (Mambo ya Walawi 18:23; 20:10-17) Wale waliokuwa na hatia ya kufanya matendo hayo ya kushusha walikatiliwa mbali kutoka katika taifa la Israeli.

Kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta lilipopata kuwa “Israeli wa Mungu,” liliwekewa viwango vivyo hivyo vya adili. (Wagalatia 6:16) Wakristo walipaswa pia ‘kukirihi lililo ovu.’ (Waroma 12:9) Maneno ya Yehova kwa Israeli yaliwahusu pia: “Lazima mwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.” (1 Petro 1:15, 16) Matendo yasiyo matakatifu kama uasherati, uzinzi, matendo ya ugoni-jinsia-moja, ngono na mnyama, na ngono ya maharimu hayakupaswa kufisidi kutaniko la Kikristo. Wale waliokataa kuacha kufanya mambo hayo wasingekubaliwa katika Ufalme wa Mungu. (Waroma 1:26, 27; 2:22; 1 Wakorintho 6:9, 10; Waebrania 13:4) Katika “siku [hizi] za mwisho,” viwango vivyo hivyo vyahusu “kondoo wengine.” (2 Timotheo 3:1; Yohana 10:16) Likiwa tokeo, Wakristo watiwa-mafuta na kondoo wengine hufanyiza watu walio safi na wenye utimamu katika maadili wawezao kulichukua jina la Mungu wao wakiwa Mashahidi wa Yehova.—Isaya 43:10.

Kulidumisha Kutaniko Likiwa Safi

Kinyume cha hilo, ulimwengu huruhusu namna zote za ukosefu wa adili. Ingawa Wakristo wa kweli wako tofauti, hawapaswi kusahau kwamba wengi wanaomtumikia Yehova sasa walikuwa ulimwenguni wakati mmoja. Kuna wengi ambao, kabla ya kumjua Mungu wetu mtakatifu, hawakuona sababu ya kutoridhisha tamaa na mawazo ya mwili wao wenye dhambi, wakigaagaa katika “dimbwi lilelile la chini la ufasiki.” (1 Petro 4:4) Mtume Paulo, baada ya kufafanua yale mazoea ya kuchukiza sana ya watu walioshushwa wa mataifa, alisema hivi: “Baadhi yenu ndivyo mlivyokuwa.” Hata hivyo, aliendelea kusema hivi: “Lakini mmeoshwa mkawa safi, lakini mmetakaswa, lakini mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.”—1 Wakorintho 6:11.

Hiyo ni taarifa yenye kufariji kama nini! Lolote lile alilofanya mtu mapema maishani, yeye abadilika wakati habari njema tukufu kuhusu Kristo inapovuta moyo wake. Anadhihirisha imani na kujiweka wakfu kwa Yehova Mungu. Kutoka wakati huo na kuendelea anaishi maisha yaliyotakata kiadili akiwa ameoshwa akawa safi machoni pa Mungu. (Waebrania 9:14) Dhambi alizofanya hapo awali zinasamehewa, naye aweza “kujinyoosha mbele kwenye mambo ya mbele.”a—Wafilipi 3:13, 14; Waroma 4:7, 8.

Yehova alimsamehe Daudi mwenye kutubu uuaji kimakusudi na uzinzi, na Yeye alimsamehe Manase mwenye kutubu ibada ya sanamu isiyo ya adili na umwagaji mwingi sana wa damu. (2 Samweli 12:9, 13; 2 Mambo ya Nyakati 33:2-6, 10-13) Twaweza kushukuru kikweli kwamba yuko tayari pia kutusamehe tukitubu na kumfikia katika weupe wa moyo na unyenyekevu. Bado, ingawa Yehova aliwasamehe Daudi na Manase, wanaume hao wawili—na Israeli pamoja nao—walilazimika kustahimili matokeo ya matendo yao yenye dhambi. (2 Samweli 12:11, 12; Yeremia 15:3-5) Kwa njia hiyohiyo, ingawa Yehova husamehe watenda-dhambi wenye kutubu, huenda kukawa na matokeo ya vitendo vyao ambayo hayawezi kuepukwa.

Matokeo Yasiyoepukika

Kwa kielelezo, mtu anayeishi maisha ya ufasiki usio wa adili na kupatwa na UKIMWI huenda akaikubali kweli na kufanya mabadiliko maishani mwake kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Sasa yeye ni Mkristo aliye safi kiroho mwenye uhusiano pamoja na Mungu na mwenye tumaini la ajabu kwa wakati ujao; lakini bado ana UKIMWI. Hatimaye huenda akafa kwa sababu ya maradhi hayo, likiwa tokeo lenye kuhuzunisha bali lisiloepukika la mwenendo wake wa zamani. Kwa Wakristo fulani matokeo ya ukosefu mzito wa adili wa zamani huenda yakadumu katika njia nyinginezo. Kwa miaka mingi baada ya ubatizo wao, labda kwa baki la maisha zao katika mfumo huu wa mambo, huenda wakahitaji kupigana na tamaa katika miili yao za kurudi kwenye mtindo-maisha wao wa hapo awali usio wa adili. Kwa msaada wa roho ya Yehova, wengi hufanikiwa katika kuzikinza. Lakini ni lazima wapige vita ya daima.—Wagalatia 5:16, 17.

Hao hawafanyi dhambi maadamu wanadhibiti tamaa zao. Lakini ikiwa wao ni wanaume, huenda wakaamua kwa hekima ‘kutofikilia’ madaraka kutanikoni huku wakihitaji bado kushindana na misukumo ya kimwili yenye nguvu. (1 Timotheo 3:1) Kwa nini? Kwa sababu wanajua jinsi kutaniko lilivyo na itibari katika wazee. (Isaya 32:1, 2; Waebrania 13:17) Wanang’amua kwamba wazee huombwa shauri juu ya mambo mengi ya usiri na wanahitaji kushughulikia hali zenye kuhitaji busara. Lisingekuwa jambo la upendo, lenye hekima, wala lifaalo kwa mtu anayepiga vita ya daima dhidi ya tamaa za kimwili zisizo safi kufikilia wadhifa huo wenye madaraka.—Mithali 14:16; Yohana 15:12, 13; Waroma 12:1.

Kwa mtu aliyekuwa mwenye kuwasumbua watoto kingono kabla ya kubatizwa, huenda kukawa na tokeo jingine. Ajifunzapo kweli, yeye anatubu na kugeuka, haleti dhambi hiyo katili ndani ya kutaniko. Baadaye huenda akafanya maendeleo mazuri, akashinda kabisa misukumo yake mibaya, na hata kuwa mwenye mbetuko wa ‘kufikilia’ wadhifa wenye madaraka kutanikoni. Lakini namna gani, ikiwa anahitaji bado kukabili sifa mbaya katika jumuiya ya kuwa mwenye kuwasumbua watoto kingono hapo zamani? Je, angekuwa “asiyelaumika, . . . [mwenye] ushuhuda bora kutoka kwa watu walio nje, . . . [asiye na] shtaka”? (1 Timotheo 3:1-7, 10; Tito 1:7) La, asingekuwa hivyo. Kwa sababu hiyo, yeye asingekuwa na sifa za kustahili kuwa na mapendeleo ya kutaniko.

Mkristo Aliyejiweka Wakfu Afanyapo Dhambi

Yehova huelewa kwamba sisi ni dhaifu na kwamba hata baada ya ubatizo huenda tukatumbukia katika dhambi. Mtume Yohana aliwaandikia Wakristo wa siku yake hivi: “Nawaandikia nyinyi mambo haya ili msifanye dhambi. Na bado, ikiwa yeyote afanya hasa dhambi, tuna msaidiaji kwa Baba, Yesu Kristo, aliye mwadilifu. Na yeye ni dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:1, 2) Ndiyo, kwa msingi wa dhabihu ya Yesu, Yehova atawasamehe Wakristo waliobatizwa wanaotumbukia katika dhambi—wakitubu kikweli na kuacha mwendo wao mbaya.

Kielelezo cha hilo kilionwa katika kutaniko la karne ya kwanza huko Korintho. Mtume Paulo alisikia juu ya kisa cha uasherati wa ngono ya maharimu katika kutaniko hilo lililofanyizwa karibuni, naye akatoa maagizo kwamba yule mtu aliyehusika atengwe na ushirika. Baadaye huyo mtenda-dhambi alitubu, na Paulo akahimiza kwa bidii kwamba hilo kutaniko limrudishe. (1 Wakorintho 5:1, 13; 2 Wakorintho 2:5-9) Hivyo, kwa nguvu za kuponya za fadhili-upendo za Yehova na kwa ile thamani kubwa ya dhabihu ya fidia ya Yesu, mtu huyo alisafishwa dhambi yake. Huenda mambo hayohayo yakatukia leo. Lakini tena, hata ikiwa mtu aliyebatizwa anayefanya dhambi nzito anatubu na kusamehewa machoni pa Yehova, huenda bado kukawa na matokeo yenye kuendelea ya dhambi yake.—Mithali 10:16, 17; Wagalatia 6:7.

Kwa kielelezo, msichana aliyejiweka wakfu akifanya uasherati, huenda akajuta tendo lake kwa uchungu na hatimaye kurudishwa kwenye afya ya kiroho kwa msaada wa kutaniko. Lakini namna gani ikiwa yeye ni mja mzito kwa sababu ya ukosefu wake wa adili? Basi maisha yake yote yamebadilishwa kwa njia isiyoepukika na yale aliyofanya. Mwanamume afanyaye uzinzi huenda akatubu na asitengwe na ushirika. Lakini mwenzi wake asiye na hatia ana msingi wa Kimaandiko wa kumtaliki, na huenda akachagua kufanya hivyo. (Mathayo 19:9) Akifanya hivyo, huyo mwanamume, ingawa amesamehewa na Yehova, ataishi sehemu inayobaki ya maisha yake akistahimili tokeo hilo kubwa la dhambi yake.—1 Yohana 1:9.

Namna gani mtu amtalikiye mkeye kwa njia isiyo ya upendo ili kumwoa mwanamke mwingine? Labda atatubu hatimaye na kurudishwa kutanikoni. Kadiri miaka ipitavyo, huenda akafanya maendeleo na “kusonga mbele kwenye ukomavu.” (Waebrania 6:1) Lakini maadamu mke wake wa kwanza aishi bila mwenzi, yeye hatastahili kutumikia katika wadhifa wenye madaraka kutanikoni. Yeye si “mume wa mke mmoja” kwa sababu hakuwa na haki ya Kimaandiko ya kumtaliki mke wake wa kwanza.—1 Timotheo 3:2, 12.

Je, hizo si sababu zenye nguvu za kumfanya Mkristo asitawishe hali ya kukirihi lililo ovu?

Namna Gani Mwenye Kuwasumbua Watoto Kingono?

Namna gani ikiwa Mkristo mtu mzima aliyebatizwa amsumbua mtoto kingono? Je, huyo mtenda-dhambi ni mwovu sana hivi kwamba Yehova hatamsamehe kamwe? Si lazima iwe hivyo. Yesu alisema kwamba ‘ukufuru dhidi ya roho takatifu’ ulikuwa hausameheki. Na Paulo alisema kwamba hakuna tena dhabihu yoyote kwa mtu anayezoea dhambi kwa kusudi ijapokuwa anaijua kweli. (Luka 12:10; Waebrania 10:26, 27) Lakini hakuna kokote ambako Biblia husema kwamba Mkristo mtu mzima amtendaye mtoto vibaya kingono—iwe ni kwa ngono ya maharimu au vingine—hawezi kusamehewa. Kwa kweli, dhambi zake zaweza kuoshwa ziwe safi akitubu kwa moyo mweupe kutoka moyoni na kugeuza mwenendo wake. Hata hivyo, huenda bado akalazimika kung’ang’ana na misukumo mibaya ya kimwili aliyositawisha. (Waefeso 1:7) Na huenda kukawa na matokeo ambayo hawezi kuepuka.

Kwa kutegemea sheria ya nchi anamoishi, ni yamkini kwamba huyo mwenye kusumbua kingono atalazimika kufungwa gerezani kwa muda fulani au kukabili adhabu nyingine kutoka kwa Serikali. Kutaniko halitamkinga dhidi ya hayo. Juu ya hayo, mtu huyo amefunua udhaifu mzito ambao ni lazima ufikiriwe kutoka wakati huo. Ikiwa aonekana kuwa mwenye kutubu, atatiwa moyo kufanya maendeleo ya kiroho, kushiriki katika utumishi wa shambani, hata kuwa na sehemu katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na katika sehemu zisizo za kufundisha katika Mkutano wa Utumishi. Ingawa hivyo, hilo halimaanishi kwamba atakuwa na sifa za kustahili kutumikia katika wadhifa wenye madaraka kutanikoni. Ni zipi sababu za Kimaandiko kwa jambo hilo?

Kwanza, lazima mzee awe “mwenye kujidhibiti.” (Tito 1:8) Ni kweli, hakuna yeyote wetu aliye mwenye kujidhibiti kikamilifu. (Waroma 7:21-25) Lakini Mkristo mtu mzima aliyejiweka wakfu atumbukiaye katika dhambi ya kumtenda mtoto vibaya kingono afunua udhaifu wa kimwili usio wa kiasili. Mambo yaliyoonwa yameonyesha kwamba yaelekea mtu mzima wa jinsi hiyo atasumbua watoto wengine kingono. Ni kweli, si kila mtu mwenye kusumbua mtoto kingono arudiaye dhambi hiyo, lakini wengi hufanya hivyo. Na kutaniko haliwezi kuchunguza mioyo ili kuona ni nani atakayewasumbua na nani hatawasumbua watoto kingono tena. (Yeremia 17:9) Kwa sababu hiyo, shauri la Paulo kwa Timotheo lahusika kwa mkazo katika kisa cha watu wazima waliobatizwa ambao wamewasumbua watoto kingono: “Usiweke kamwe mikono yako haraka-haraka juu ya mtu yeyote; wala usiwe mshiriki katika dhambi za wengine.” (1 Timotheo 5:22) Ili kuwakinga watoto wetu, mtu ajulikanaye kuwa alikuwa mwenye kuwasumbua watoto kingono hana sifa za kustahili kuwa na wadhifa wenye madaraka kutanikoni. Isitoshe, hawezi kuwa painia wala kutumika katika utumishi mwingine wa pekee, wa wakati wote.—Linganisha ile kanuni kwenye Kutoka 21:28, 29.

Huenda wengine wakauliza, ‘Je, wengine hawakufanya dhambi za namna nyinginezo na kuonekana kama wametubu, kisha wakarudia dhambi yao baadaye?’ Ndiyo, hilo limetukia, lakini kuna mambo mengine ya kufikiria. Kwa kielelezo, mtu akimtongoza mtu mzima mwingine, huyo mtu mzima apaswa kuweza kukinza utongozi wake. Ni rahisi zaidi kuwadanganya, kuwatatanisha, au kuwatisha watoto. Biblia husema juu ya ukosefu wa hekima wa watoto. (Mithali 22:15; 1 Wakorintho 13:11) Yesu alitumia watoto kuwa kielelezo cha unyenyekevu wenye weupe wa moyo. (Mathayo 18:4; Luka 18:16, 17) Weupe wa moyo wa watoto hutia ndani kuwa bila uzoefu wowote. Watoto walio wengi ni wanyoofu, wenye hamu ya kupendeza, na hivyo rahisi kutendwa vibaya na mtu mzima mwenye kutunga hila wanayemjua na kuwa na itibari katika yeye. Kwa hiyo, kutaniko lina daraka mbele ya Yehova la kuwakinga watoto walo.

Watoto waliozoezwa vema hujifunza kutii na kuwaheshimu wazazi wao, wazee, na watu wazima wengine. (Waefeso 6:1, 2; 1 Timotheo 5:1, 2; Waebrania 13:7) Ungekuwa upotovu wa kushtua ikiwa mmoja wa watu hao wenye mamlaka angetumia vibaya itibari yenye moyo mweupe ya mtoto huyo ili kumtongoza au kumlazimisha anyenyekee matendo ya kingono. Mara nyingi wale ambao wamesumbuliwa kingono katika njia hiyo hung’ang’ana kwa miaka mingi ili kushinda vurugu ya kihisia-moyo inayotokea. Kwa sababu hiyo, mtu huyo mwenye kuwasumbua watoto kingono atapatwa na nidhamu kali na vizuizi vikali vya kutaniko. Jambo la kuhangaikia si wadhifa wake akiwa mwenye mamlaka, bali ni utakato usio na waa wa kutaniko.—1 Wakorintho 5:6; 2 Petro 3:14.

Mwenye kuwasumbua watoto kingono akitubu kwa moyo mweupe, yeye atatambua hekima ya kutumia kanuni za Biblia. Akijifunza kikweli kukirihi lililo ovu, atachukia sana lile alilofanya na kung’ang’ana ili aepuke kuirudia dhambi yake. (Mithali 8:13; Waroma 12:9) Zaidi, kwa hakika atamshukuru Yehova kwa ukubwa wa upendo Wake, ambao kwa sababu yao mtenda-dhambi mwenye kutubu, kama vile yeye, aweza bado kumwabudu Mungu wetu mtakatifu na kutumaini kuwa miongoni mwa ‘wanyoofu’ watakaokaa duniani milele.—Mithali 2:21.

[Maelezo ya Chini]

a Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1996.

[Blabu katika ukurasa wa 28]

Ingawa Yehova huwasamehe watenda-dhambi wenye kutubu, huenda kukawa na matokeo ya vitendo vyao yasiyoweza kuepukwa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki