Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 6/1 kur. 28-31
  • Kutegemezwa Katika Majaribu Makali Mno

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutegemezwa Katika Majaribu Makali Mno
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Malezi ya Kiyahudi
  • Kuanza kwa Majaribu
  • Jaribu Langu Lililo Baya Zaidi
  • Kipindi cha Kitulizo
  • Kuokoka Katika Auschwitz
  • Kuokoka Katika Kambi Nyingine
  • Kuachiliwa na Maisha Baadaye
  • Kuendeleza Imani Pamoja na Mume Wangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Nilitegemezwa kwa Kumwamini Mungu Kabisa
    Amkeni!—2001
  • Kwa Msaada wa Yehova, Tuliokoka Serikali za Kimabavu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • “Wafungwa kwa Sababu ya Imani Yao”
    Amkeni!—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 6/1 kur. 28-31

Kutegemezwa Katika Majaribu Makali Mno

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ÉVA JOSEFSSON

Tukiwa kikundi kidogo tulikuwa tumekusanyika katika Újpest, wilaya ya Budapest iliyoko Hungaria, kwa ajili ya mkutano mfupi kabla ya kuondoka kwenda katika huduma ya Kikristo. Ulikuwa mwaka wa 1939, punde kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kuanza, na kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa chini ya marufuku katika Hungaria. Walioshiriki katika kufundisha Biblia hadharani siku hizo, mara nyingi walikamatwa.

KWA kuwa hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kushiriki katika utendaji huo, lazima nilionekana mwenye wasiwasi kidogo na nimegeuka rangi kuwa mweupe. Ndugu Mkristo mwenye umri mkubwa zaidi alinigeukia na kusema hivi: “Éva, huhitaji kuogopa kamwe. Kumtumikia Yehova ni heshima iliyo kubwa zaidi ambayo binadamu aweza kupata.” Maneno hayo yenye ufikirio na yenye kuimarisha, yalisaidia kunitegemeza katika majaribu makali mno.

Malezi ya Kiyahudi

Mimi ndiye niliyekuwa mtoto mwenye umri mkubwa zaidi katika familia ya Kiyahudi yenye watoto watano. Mama hakuwa ameridhika na Dini ya Kiyahudi, na alianza kuchunguza dini nyinginezo. Hivyo ndivyo alivyojuana na Erzsébet Slézinger, mwanamke mwingine Myahudi ambaye pia alikuwa akitafuta kweli ya Biblia. Erzsébet alimjulisha Mama kwa Mashahidi wa Yehova, na tokeo ni kwamba, mimi pia nilipendezwa sana na mafundisho ya Biblia. Upesi nilianza kushiriki na wengine yale niliyokuwa nimejifunza.

Nilipofika umri wa miaka 18 katika kiangazi cha mwaka wa 1941, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova Mungu kwa njia ya ubatizo katika Mto Danube. Mama alibatizwa wakati huohuo, lakini Baba hakushiriki imani yetu mpya ya Kikristo. Upesi baada ya ubatizo wangu, nilifanya mipango ili nipainie, yaani, nishiriki katika huduma ya wakati wote. Nilihitaji kupata baiskeli, hivyo nikaanza kufanya kazi katika maabara ya kiwanda kikubwa cha kutengeneza nguo.

Kuanza kwa Majaribu

Wanazi walikuwa wametwaa Hungaria, na kiwanda ambako nilifanya kazi kilikuwa chini ya usimamizi wa Ujerumani. Siku moja wafanyakazi wote waliitwa waende mbele ya wasimamizi ili kula kiapo cha utii kwa Wanazi. Tuliambiwa kwamba kukataa kufanya hivyo kungekuwa na matokeo mabaya. Wakati wa hiyo sherehe ambako tulihitajika kumwita Hitler mwokozi, nilisimama kwa staha lakini sikufanya tendo nililohitajika kufanya. Niliitwa ofisini siku hiyohiyo, nikapewa mshahara wangu, na kuambiwa niondoke. Kwa kuwa ilikuwa nadra kupata kazi, nilijiuliza kile ambacho kingepata mipango yangu ya kupainia. Hata hivyo, siku iliyofuata nilipata kazi mpya yenye mshahara wa juu hata zaidi.

Sasa tamaa yangu ya kupainia ingeweza kutimizwa. Nilikuwa na mapainia wenzi kadhaa, na Juliska Asztalos, ndiye aliyekuwa painia mwenzangu wa mwisho. Tukiwa bila fasihi yoyote ya kutolea watu, tulitumia Biblia yetu tu katika huduma. Tulipopata watu wenye kupendezwa, tulifanya ziara za kurudia, na kuwaazima fasihi.

Juliska nami tulilazimika kubadilisha tena na tena eneo tulilokuwa tukihubiri. Tulifanya hivyo kwa sababu, kasisi alipojua kwamba tulikuwa tukizuru ‘kondoo zake,’ angetangaza kanisani kwamba Mashahidi wa Yehova wakiwazuru, ni lazima waripoti jambo hilo kwake au kwa polisi. Watu wenye urafiki walipotuambia juu ya tangazo la namna hiyo, tungehamia eneo jingine.

Siku moja Juliska nami tulizuru mvulana mchanga aliyeonyesha kupendezwa. Tulifanya miadi ya kufanya ziara ya kurudia ili kumwazima kitu fulani cha kusoma. Lakini tuliporudi, polisi walikuwa hapo, na tulikamatwa na kupelekwa kwenye kituo cha polisi katika Dunavecse. Huyo mvulana alikuwa ametumiwa akiwa chambo ili watunase. Tulipowasili kwenye kituo cha polisi, tulimwona kasisi fulani huko, tukajua kwamba yeye pia alihusika.

Jaribu Langu Lililo Baya Zaidi

Huko kwenye kituo cha polisi, nywele zangu zote zilinyolewa, na nikalazimishwa kusimama nikiwa uchi mbele ya polisi wapatao 12. Walinihoji, wakitaka kujua ni nani aliyekuwa kiongozi wetu katika Hungaria. Niliwaeleza kwamba sisi hatukuwa na kiongozi mwingine ila Yesu Kristo. Ndipo wakanipiga kikatili kwa virungu, lakini sikuwasaliti ndugu zangu Wakristo.

Baadaye, walifunga miguu yangu pamoja, wakainua mikono yangu juu ya kichwa changu na kuifunga pamoja pia. Kisha wote, ila polisi mmoja, wakanibaka mmoja baada ya mwingine. Nilikuwa nimefungwa kwa mkazo sana hivi kwamba, miaka mitatu baadaye bado nilikuwa na alama kwenye viwiko vyangu vya mikono. Nilitendwa kinyama sana hivi kwamba, niliwekwa katika sehemu ya nyumba iliyo chini ya ardhi kwa majuma mawili hadi majeraha yangu yaliyokuwa mabaya zaidi, yakapona kwa kiwango fulani.

Kipindi cha Kitulizo

Baadaye nilipelekwa kwenye gereza katika Nagykanizsa, ambako kulikuwa na Mashahidi wa Yehova wengi. Miaka miwili yenye furaha kwa kadiri ilifuata, licha ya kifungo chetu. Tulifanya mikutano yetu yote kwa siri, na utendaji wetu ulikuwa sawa kabisa na wa kutaniko. Tulikuwa pia na fursa nyingi za mahubiri ya vivi hivi. Ilikuwa katika gereza hilo ambapo nilijuana na Olga Slézinger, dada wa kimwili wa Erzsébet Slézinger, mwanamke aliyekuwa amejulisha mama yangu nami, kweli ya Biblia.

Kufikia mwaka wa 1944, Wanazi waliokuwa Hungaria walikuwa wameazimia kuwaua Wayahudi wa Hungaria, kama vile walivyokuwa wakiwaua kwa utaratibu katika maeneo mengine yaliyotekwa. Siku moja walikuja kuchukua Olga nami. Tulijazwa katika mabehewa ya garimoshi ya kubebea ng’ombe, na baada ya safari ngumu kupitia Chekoslovakia, tukafika mwisho wa safari yetu—kambi ya kifo iliyoitwa Auschwitz—huko kusini mwa Poland.

Kuokoka Katika Auschwitz

Nilihisi salama nilipokuwa na Olga. Angeweza kuwa mwenye ucheshi hata katika hali zenye kujaribu. Tulipofika Auschwitz, tulienda mbele ya Dakt. Mengele, mtu mwenye sifa mbaya, ambaye kazi yake ilikuwa kutenga watu wenye kuwasili karibuni ambao walikuwa wenye nguvu na afya kimwili, kutoka kwa wale ambao hawakufaa kufanya kazi. Hao wasiokuwa na afya nzuri kuweza kufanya kazi walipelekwa kwenye vyumba vya kuulia watu kwa gesi yenye sumu. Zamu yetu ilipofika, Mengele alimwuliza Olga, “Una miaka mingapi?”

Kwa ujasiri, na kwa macho yenye kumetameta kwa ucheshi, alijibu, “20.” Kwa kweli umri wake ulikuwa mara mbili ya huo aliotaja. Lakini Mengele alicheka na kumruhusu aende upande wa kulia na hivyo kubaki hai.

Wafungwa wote katika Auschwitz walitiwa alama kwa ishara zilizokuwa kwenye mavazi yao ya gereza—Wayahudi walikuwa na alama ya Nyota ya Daudi, nao Mashahidi wa Yehova walikuwa na alama ya pembetatu ya zambarau. Walipotaka kushonelea hiyo Nyota ya Daudi kwenye mavazi yetu, tuliwaeleza kwamba sisi tulikuwa Mashahidi wa Yehova na tulitaka pembetatu ya zambarau. Hatukufanya hivyo kwa sababu tuliaibikia asili yetu ya Kiyahudi, lakini sasa tulikuwa Mashahidi wa Yehova. Walijaribu kutulazimisha tukubali hiyo ishara ya Wayahudi kwa kutupiga mateke na kutuchapa. Lakini tulisimama imara hadi walipotukubali kuwa Mashahidi wa Yehova.

Baada ya muda, nilikutana na dada yangu Elvira, aliyekuwa mchanga zaidi kuliko mimi kwa miaka mitatu. Familia yetu yote ya watu saba ilikuwa imepelekwa Auschwitz. Elvira nami ndio tuliokubaliwa kuwa tulifaa kufanya kazi. Baba, Mama, na ndugu zetu watatu walikufa katika vyumba vya kuulia watu kwa gesi yenye sumu. Elvira hakuwa Shahidi wakati huo, na hatukukaa katika sehemu ileile ya kambi. Aliokoka, akahamia Marekani, akawa Shahidi huko Pittsburgh, Pennsylvania, na baadaye kufia huko mwaka wa 1973.

Kuokoka Katika Kambi Nyingine

Katika majira ya baridi ya mwaka wa 1944/1945, Wajerumani waliamua kuhamisha watu kutoka Auschwitz, kwa kuwa Warusi walikuwa wakikaribia. Hivyo tulihamishwa hadi Bergen-Belsen, sehemu ya kaskazini ya Ujerumani. Upesi baada ya kuwasili kwetu, Olga nami tulipelekwa Braunschweig. Hapa tulipaswa kusaidia kuondoa mabaki ya nyumba baada ya mashambulizi makali ya mabomu ya majeshi ya Muungano. Olga nami tulizungumzia jambo hilo. Kwa kuwa hatukuwa na hakika kama kufanya kazi hiyo kungehalifu hali yetu ya kutokuwamo, sote wawili tuliamua kutoifanya.

Uamuzi wetu ulishtusha sana. Tulipigwa kwa mijeledi ya ngozi, kisha tukapelekwa mbele ya kikosi cha kupiga risasi. Tulipewa dakika moja ya kulifikiria jambo hilo tena, tukaambiwa kwamba ikiwa hatungebadili akili zetu, tungepigwa risasi. Tulisema hatukuhitaji muda wa kufikiria jambo hilo kwa sababu tulikuwa tumeamua. Hata hivyo, kwa kuwa kamanda wa kambi hakuwapo, na ndiye peke yake aliyekuwa na mamlaka ya kutoa amri ya kufisha, ilibidi kufishwa kwetu kukawizwe.

Wakati huohuo tulilazimishwa kusimama siku nzima katika uwanja wa kambi. Tulilindwa na askari wawili wenye silaha, ambao walibadilishwa baada ya kila muda wa saa mbili. Hatukupewa chakula chochote, na tuliteseka mno kutokana na baridi, kwa kuwa ulikuwa mwezi wa Februari. Juma moja la kutendwa hivyo lilipita, lakini kamanda hakufika. Hivyo tulitiwa nyuma ya lori, na tulishangaa kujikuta tumerudi Bergen-Belsen.

Kufikia wakati huo, Olga nami tulikuwa katika hali mbaya mno. Nilikuwa nimepoteza nywele zangu nyingi na nilikuwa na homa kali. Ilikuwa tu kwa jitihada kubwa sana kwamba ningeweza kufanya kazi kidogo. Ule mchuzi mwepesi wa kabichi na kipande kidogo cha mkate kila siku, havikutosha. Lakini ulikuwa wa lazima ili tufanye kazi kwa sababu wale ambao hawangeweza kufanya kazi walifishwa. Dada Wajerumani waliofanya kazi jikoni walinisaidia kupata pumziko la kiasi fulani. Wakati walinzi wenye kufanya ukaguzi walipokuwa wakija, hao dada walinionya ili kwamba niweze kusimama kwenye benchi ya kufanyia kazi, nikionekana kana kwamba nilikuwa nikifanya kazi kwa bidii.

Siku moja Olga hakuwa na nguvu kabisa ya kwenda mahali pake pa kazi, na baada ya siku hiyo hatukumwona tena. Nilipoteza rafiki na mwandamani jasiri, mmoja ambaye alikuwa msaada mkubwa kwangu wakati wa miezi hiyo migumu katika kambi mbalimbali. Akiwa mfuasi mtiwa-mafuta wa Bwana wetu Yesu Kristo, lazima alipokea mara moja thawabu yake ya kimbingu.—Ufunuo 14:13.

Kuachiliwa na Maisha Baadaye

Vita ilipoisha katika Mei 1945 na ukombozi ukaja, nilikuwa dhaifu sana hivi kwamba, singeweza kushangilia kwamba hatimaye nira ya hao waonezi ilikuwa imepondwa; wala singeweza kujiunga na misafara iliyokuwa ikiwapeleka waliokombolewa hadi katika nchi zilizokuwa tayari kuwapokea. Nilibaki katika hospitali miezi mitatu ili nipate nguvu tena. Baadaye nilipelekwa Sweden, iliyopata kuwa makao yangu mapya. Niliwasiliana mara moja na ndugu na dada zangu Wakristo, na baada ya muda nikaanza ile kazi yenye thamani sana ya huduma ya shambani.

Katika mwaka wa 1949, niliolewa na Lennart Josefsson, ambaye alikuwa ametumikia miaka mingi akiwa mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova. Yeye pia alikuwa ametiwa gerezani wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili kwa sababu ya kudumisha imani yake. Tulianza maisha yetu pamoja tukiwa mapainia katika Septemba 1, 1949, na tulipewa mgawo wa kutumikia katika mji wa Borås. Wakati wa miaka yetu ya kwanza huko, tuliongoza mafunzo kumi ya Biblia kwa ukawaida kila juma pamoja na watu wenye kupendezwa. Tulishangilia kuona kutaniko katika Borås likikua kuwa makutaniko matatu katika muda wa miaka tisa, na sasa kuna makutaniko matano.

Sikuweza kuendelea kuwa painia kwa muda mrefu kwa sababu mwaka wa 1950 tulipata mtoto wa kike, na miaka miwili baadaye, tukapata wa kiume. Hivyo nilikuwa na pendeleo lenye kupendeza la kuwafundisha watoto wetu kweli yenye thamani ambayo ndugu mpendwa katika Hungaria alinifunza nilipokuwa na umri wa miaka 16 tu, yaani: “Kumtumikia Yehova ni heshima iliyo kubwa zaidi ambayo binadamu aweza kupata.”

Nifikiriapo maisha yangu, mimi hung’amua kwamba nimepata kuona ukweli wa yale mwanafunzi Yakobo aliandika alipotukumbusha juu ya uvumilivu wa Yobu: “Yehova ni mwenye wororo sana katika shauku na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11) Ingawa mimi pia nilipatwa na majaribu makali mno, nimebarikiwa sana kupata watoto wawili, wenzi wao, na wajukuu sita—ambao wote ni waabudu wa Yehova. Mbali na hayo, nina watoto na wajukuu wengi sana wa kiroho, ambao baadhi yao wanatumikia wakiwa mapainia na wamishonari. Sasa tumaini langu kubwa ni kukutana na wapendwa wanaolala katika kifo na kuwakumbatia watakapoinuka kutoka katika makaburi yao ya ukumbusho.—Yohana 5:28, 29.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Nikiwa katika huduma huko Sweden baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili

[Picha katika ukurasa wa 31]

Nikiwa na mume wangu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki