-
Miaka Zaidi ya 50 ya ‘Kuvuka’Mnara wa Mlinzi—1996 | Novemba 1
-
-
Miaka Zaidi ya 50 ya ‘Kuvuka’
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA EMMANUEL PATERAKIS
Karne 19 zilizopita mtume Paulo alipokea mwaliko huu usio wa kawaida: “Vuka, uje Makedonia utusaidie.” Paulo alikubali kwa utayari fursa hiyo mpya ya ‘kuhubiri habari njema.’ (Matendo 16:9, 10) Ingawa mwaliko niliopokea si wa zamani hivyo, hata hivyo ni miaka zaidi ya 50 iliyopita nilipokubali ‘kuvuka’ kwenda maeneo mapya kwa roho ya Isaya 6:8: “Mimi hapa, nitume mimi.” Safari zangu kadha wa kadha zilinipatia lakabu Mtalii wa Sikuzote, lakini utendaji wangu mbalimbali haukufanana sana na utalii. Zaidi ya mara moja, nilipofika tu kwenye chumba changu cha hoteli, nilipiga magoti na kumshukuru Yehova kwa ajili ya ulinzi wake.
NILIZALIWA Januari 16, 1916, huko Hierápetra, Krete, katika familia ya Kiothodoksi yenye kufuatia dini sana. Tangu wakati nilipokuwa kitoto kichanga, mama alikuwa akinipeleka pamoja na dada zangu watatu kanisani Jumapili. Naye baba yangu, alipendelea kukaa nyumbani na kusoma Biblia. Nilimpenda sana baba yangu—mwanamume mwenye kufuatia haki, mwema, na mwenye kusamehe—na kifo chake, nilipokuwa na umri wa miaka tisa, kiliniathiri sana.
Nakumbuka kwamba nilipokuwa na umri wa miaka mitano, nilisoma maandishi shuleni yaliyosema hivi: “Kila kitu kinachotuzunguka hutangaza kuwako kwa Mungu.” Nilipokuwa nikikua, nilisadiki hilo kabisa. Hivyo, nilipofika umri wa miaka 11, niliamua kuandika insha, Zaburi 104:24 ikiwa kichwa chayo: “Ee BWANA, jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.” Nilivutiwa na maajabu ya maumbile, hata na vitu sahili kama mbegu zenye mabawa madogo ili zipeperushwe na upepo kutoka katika kivuli cha mti-mzazi. Juma lililofuata baada ya mimi kutoa insha yangu, mwalimu wangu aliisoma kwa darasa zima, kisha kwa shule nzima. Wakati huo, walimu walikuwa wakipigana dhidi ya mawazo ya Ukomunisti nao walifurahi kusikia utetezi wangu wa kuwako kwa Mungu. Nami, nilifurahi tu kueleza itikadi yangu katika Muumba.
Majibu kwa Maswali Yangu
Kukabili kwangu Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza katika miaka ya mapema ya 1930 kungali dhahiri katika kumbukumbu langu. Emmanuel Lionoudakis alikuwa amekuwa akihubiri katika miji yote na vijiji vyote vya Krete. Nilikubali vijitabu kadhaa kutoka kwake, lakini kile kijitabu chenye kichwa Where Are the Dead? ndicho kilichopata uangalifu wangu. Nilihofu kifo vibaya hivi kwamba hata nisingaliingia chumba alimofia baba yangu. Nilipokuwa nikisoma kijitabu hicho tena na tena nikajifunza yale ambayo Biblia hufundisha juu ya hali ya wafu, nilihisi hofu yangu ya kishirikina ikipotea.
Mara moja kila mwaka wakati wa kiangazi, hao Mashahidi walizuru mji wetu na kuniletea fasihi zaidi za kusoma. Hatua kwa hatua uelewevu wangu wa Maandiko ukaongezeka, lakini niliendelea kuhudhuria Kanisa Othodoksi. Hata hivyo, kitabu Deliverance, kilitokeza badiliko kubwa. Kilionyesha waziwazi tofauti kati ya tengenezo la Yehova na lile la Shetani. Kuanzia wakati huo na kuendelea, nilianza kujifunza kwa ukawaida zaidi Biblia na fasihi zozote za Watch Tower Society ambazo ningeweza kupata. Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku Ugiriki, nilijifunza kisiri-siri usiku. Na bado, nilikuwa mwenye idili sana juu ya yale niliyokuwa nikijifunza hivi kwamba sikuweza kujizuia nisizungumze na kila mtu juu yayo. Upesi polisi wakaanza kunichunguza, wakinitembelea kwa ukawaida wakati wowote wa mchana na usiku ili kutafuta fasihi.
Katika 1936, nilihudhuria mkutano kwa mara ya kwanza, maili 75 kutoka Iráklion. Nilifurahi sana kukutana na Mashahidi. Wengi wao walikuwa watu sahili, walio wengi wakiwa wakulima, lakini walisaidia kunisadikisha kwamba hii ndiyo kweli. Wakfu wangu kwa Yehova ukafanywa papo hapo.
Ubatizo wangu ni tukio ambalo sitasahau kamwe. Usiku mmoja mwaka wa 1938, wawili wa wanafunzi wangu wa Biblia nami tulichukuliwa na Ndugu Lionoudakis katika giza tititi hadi ufuoni. Baada ya kusali, akatutumbukiza majini.
Kukamatwa
Mara ya kwanza kabisa niliyoenda kuhubiri ilikuwa yenye kujaa matukio, bila kusema sana. Nilikutana na rafiki wa shule wa zamani ambaye alikuwa amekuwa kasisi, nasi tukawa na mazungumzo mazuri sana pamoja. Lakini baadaye akaeleza kwamba kwa kupatana na agizo la askofu, alilazimika kuhakikisha nimekamatwa. Tulipongojea kwenye ofisi ya meya kuwasili kwa polisi kutoka kijiji cha jirani, umati ulikusanyika nje. Kwa hiyo nikachukua Biblia ya Agano Jipya katika Kigiriki iliyokuwa ofisini humo na kuanza kuwatolea hotuba yenye kutegemea Mathayo sura ya 24. Mwanzoni watu hawakutaka kusikiliza, lakini yule kasisi akaingilia. “Mwacheni aseme,” akasema. “Ni Biblia yetu.” Niliweza kuongea kwa muda wa saa moja na nusu. Hivyo, siku yangu ya kwanza katika huduma ilikuwa pia pindi ya hotuba yangu ya watu wote ya kwanza. Kwa kuwa polisi hawakuwa wamefika bado nilipomaliza, meya na yule kasisi wakaamua kuagiza kikundi cha watu kinilazimishe kuondoka mjini. Kwenye kona ya kwanza barabarani, nilianza kukimbia upesi nilivyoweza ili kuepuka mawe waliyorusha.
Siku iliyofuata polisi wawili, wakiwa wameandamana na yule askofu, walinikamata nikiwa kazini. Kwenye kituo cha polisi, niliweza kuwatolea ushahidi kutoka katika Biblia, lakini kwa kuwa fasihi zangu za Biblia hazikuwa zimetiwa muhuri wa askofu kama ilivyotakiwa kisheria, nilishtakiwa juu ya kugeuza-imani za watu na kugawanya fasihi zisizoidhinishwa. Niliachiliwa nikisubiri kesi.
Kesi yangu ilifanywa mwezi mmoja baadaye. Katika kujitetea nilionyesha kwamba nilikuwa tu nikitii amri ya Kristo ya kuhubiri. (Mathayo 28:19, 20) Hakimu akajibu kwa kejeli: “Mwanangu, Yule aliyetoa amri hiyo alisulubishwa. Kwa kusikitisha, sina mamlaka ya kukupa adhabu hiyohiyo.” Hata hivyo, wakili mchanga ambaye sikumjua alisimama ili kunitetea, akisema kwamba kukiwa na Ukomunisti na uatheisti mwingi, mahakama yapaswa kuona fahari kwamba kuna wanaume wachanga walio tayari kulitetea Neno la Mungu. Kisha akaja na kunipa hongera kwa uchangamfu kwa sababu ya utetezi wangu ulioandikwa, uliokuwa katika faili yangu. Kwa kuwa alivutiwa kwamba nilikuwa mchanga sana, alijitolea kunitetea bila malipo. Badala ya ile hukumu ya miezi isiyopungua mitatu, nilihukumiwa siku kumi tu gerezani na faini ya drakma 300. Ulilofanya upinzani huo ni kutia nguvu tu azimio langu la kumtumikia Yehova na kuitetea kweli.
Pindi nyingine nilipokamatwa, hakimu aliona nilivyonukuu Biblia kwa urahisi. Akamwomba yule askofu aondoke ofisini mwake, akisema hivi: “Umefanya kazi yako. Nitamshughulikia.” Kisha akatoa Biblia yake, nasi tukaongea juu ya Ufalme wa Mungu alasiri yote. Visa kama hivyo vilinitia moyo niendelee licha ya magumu.
Hukumu ya Kifo
Katika 1940, niliitwa kufanya utumishi wa kijeshi nami nikaandika barua nikieleza sababu iliyonifanya nisikubali kuandikishwa. Siku mbili baadaye polisi walinikamata na kunipiga vibaya. Kisha nikatumwa vitani Albania, nilikohukumiwa na mahakama ya jeshi kwa sababu nilikataa kupiga vita. Wenye mamlaka jeshini waliniambia kwamba walichotaka kujua si kama nilikuwa nikifanya lililo sawa au lisilo sawa, bali tokeo ambalo kielelezo changu kingekuwa nalo juu ya wanajeshi. Nilihukumiwa kifo, lakini kwa sababu ya kosa la kisheria, kwa kitulizo changu kikubwa, hukumu hiyo ilibadilishwa kuwa miaka kumi ya kazi ngumu. Nilipisha miezi michache iliyofuata ya maisha yangu katika gereza la kijeshi katika Ugiriki chini ya hali ngumu sana, ambazo kutokana nazo ningali napatwa na athari za kimwili.
Hata hivyo, gereza halikunizuia nisihubiri. Hata kidogo! Ilikuwa rahisi kuanzisha mazungumzo, kwa kuwa wengi walijiuliza kwa nini raia alikuwa katika gereza la kijeshi. Mojawapo mazungumzo hayo pamoja na mwanamume mchanga mwenye moyo mweupe yaliongoza kwenye funzo la Biblia katika ua wa gereza. Miaka 38 baadaye nilikutana na mwanamume huyo tena kwenye kusanyiko. Alikuwa ameikubali kweli naye alikuwa akitumikia akiwa mwangalizi wa kutaniko katika kisiwa cha Lefkás.
Majeshi ya Hitler yalipovamia Yugoslavia mwaka wa 1941, tulihamishwa kusini zaidi kwenye gereza katika Preveza. Wakati wa safari hiyo, mlolongo wetu ulivamiwa na walipua mabomu Wajerumani, nasi wafungwa hatukupewa chakula chochote. Mkate mdogo niliokuwa nao ulipoisha, nilisali kwa Mungu hivi: “Ikiwa ni mapenzi yako nife njaa baada ya kuniokoa kutoka katika hukumu ya kifo, basi mapenzi yako na yatendeke.”
Siku iliyofuata ofisa mmoja aliniita kando wakati wa kusoma majina ya watu na, baada ya kujua nilikotoka, wazazi wangu walikuwa nani, na kwa nini nilikuwa gerezani, akaniambia nimfuate. Alinipeleka kwenye jumba la kulia la maofisa mjini, akanielekeza kwenye meza yenye mkate, jibini, na mwana-kondoo aliyechomwa, na kuniambia nile. Lakini nikaeleza kwamba kwa kuwa wale wafungwa wengine 60 hawakuwa na chochote cha kula, dhamiri yangu isingeniruhusu nile. Ofisa huyo akajibu hivi: “Mimi siwezi kulisha kila mtu! Baba yako alikuwa mkarimu sana kwa baba yangu. Nawajibika kimaadili kwako wewe bali si kwa wale wengine.” “Ikiwa ndivyo ilivyo basi nitarudi tu,” nikajibu. Aliwaza kwa kitambo kidogo kisha akanipa mfuko mkubwa nitie chakula kingi niwezavyo.
Niliporudi gerezani, niliuweka huo mfuko chini na kusema hivi: “Mabwana, chakula hiki ni chenu.” Ikatukia kwamba, jioni iliyotangulia, nilikuwa nimeshtakiwa kwamba nilichangia matatizo ya wale wafungwa wengine kwa sababu sikujiunga nao katika sala zao kwa Bikira Mariamu. Hata hivyo, Mkomunisti alinitetea. Sasa alipoona kile chakula, aliwaambia wengine hivi: “Yu wapi ‘Bikira Mariamu’ wenu? Mlisema kwamba tungekufa kwa sababu ya mtu huyu, naye ndiye anayetuletea chakula.” Kisha akanigeukia na kusema: “Emmanuel! Njoo usali.”
Muda mfupi baadaye, kusonga mbele kwa jeshi la Ujerumani kulisababisha walinzi wa gereza watoroke, kukifungua milango ya kifungo. Nilienda Patras ili kutafuta Mashahidi wengine kabla ya kuelekea Athene mwishoni mwa Mei 1941. Huko niliweza kupata nguo na viatu kadhaa na kuoga mara ya kwanza baada ya zaidi ya mwaka mmoja. Hadi mwisho wa umilikaji, Wajerumani walinisimamisha kwa ukawaida nilipokuwa nikihubiri, lakini hawakunikamata kamwe. Mmoja wao alisema hivi: “Huko Ujerumani sisi huwapiga risasi Mashahidi wa Yehova. Lakini hapa tungetaka adui zetu wote wawe Mashahidi!”
Utendaji Mbalimbali wa Baada ya Vita
Kana kwamba Ugiriki haikuwa imepata mapigano ya kutosha, iligawanywa zaidi na vita ya wenyewe kwa wenyewe kutoka 1946 hadi 1949, ikisababisha maelfu ya vifo. Ndugu walihitaji kitia-moyo kingi ili wabaki imara wakati ambapo kuhudhuria mikutano tu kungeweza kufanya mtu akamatwe. Ndugu kadhaa walihukumiwa kifo kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo. Lakini licha ya hayo, watu wengi waliitikia ujumbe wa Ufalme, nasi tulikuwa na ubatizo wa mtu mmoja au wawili kila juma. Kuanzia 1947, nilianza kufanya kazi kwenye ofisi za Sosaiti katika Athene wakati wa mchana, na kutembelea makutaniko nikiwa mwangalizi asafiriye wakati wa usiku.
Katika 1948, nilikuwa na shangwe ya kualikwa nihudhurie Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, huko Marekani. Lakini kulikuwa na tatizo. Kwa sababu ya vifungo vyangu vya awali, sikuweza kupata pasipoti. Hata hivyo, mmoja wa wanafunzi wangu wa Biblia alikuwa anapatana na jenerali. Kwa msaada wa mwanafunzi huyo, baada ya majuma machache tu, nilikuwa na pasipoti. Lakini nilihangaika wakati ambapo, muda mfupi kabla ya wakati nilipopaswa kuondoka, nilishikwa kwa sababu ya kugawanya Mnara wa Mlinzi. Polisi alinipeleka kwa mkuu wa State Security Police katika Athene. Kwa mshangao wangu mkubwa, yeye alikuwa mmoja wa majirani wangu! Yule polisi alieleza sababu ya kukamatwa kwangu na kumpa lile furushi la magazeti. Jirani yangu akatoa rundo la magazeti ya Mnara wa Mlinzi kutoka katika dawati lake na kuniambia: “Sina toleo la karibuni zaidi. Je, naweza kuchukua nakala moja?” Nilitulizwa kama nini kuona mkono wa Yehova katika mambo hayo!
Darasa la 16 la Gileadi, katika 1950, lilikuwa jambo lenye kujenga sana. Mwishoni, nilipewa mgawo wa kwenda Saiprasi, ambapo upesi niligundua kwamba upinzani wa makasisi ulikuwa mkali kama vile ulivyokuwa katika Ugiriki. Mara nyingi tulilazimika kukabili umati wa watu wa kidini wenye siasa kali waliochochewa kufanya ghasia na makasisi wa Othodoksi. Katika 1953 visa yangu ya kuishi Saiprasi haikufanywa upya, nami nikapewa mgawo mwingine kwenda Istanbul, Uturuki. Hapo napo, nilikaa kwa muda mfupi. Mikazo ya kisiasa kati ya Uturuki na Ugiriki ilimaanisha kwamba, licha ya matokeo mazuri katika kazi ya kuhubiri, nililazimika kuondoka na kwenda kwenye mgawo mwingine—Misri.
Nilipokuwa gerezani, nilikuwa nikikumbuka Zaburi 55:6, 7. Hapo Daudi alieleza tamaa ya kutorokea jangwani. Sikuwazia kamwe kwamba siku moja huko ndiko ningekuwa barabara. Katika 1954, baada ya safari yenye kuchosha ya siku kadhaa kwa gari la moshi, na mashua kwenye mto Naili, hatimaye nilifika mwisho wa safari yangu—Khartoum, Sudan. Nilitaka tu kuoga na kulala. Lakini nilisahau kwamba ilikuwa adhuhuri. Maji, yaliyokuwa ndani ya tangi kwenye paa, yalinichoma, nikalazimika kuvaa kofia ya chuma iliyo nyororo upande wa ndani kwa miezi kadhaa mpaka ngozi yangu ya kichwani ilipopona.
Mara nyingi nilihisi nikiwa pekee huko, peke yangu katikati ya Sahara, maili elfu moja kutoka kutaniko la karibu zaidi, lakini Yehova alinitegemeza na kunipa nguvu ya kuendelea. Nyakati nyingine kitia-moyo kilitoka katika vyanzo visivyotarajiwa kabisa. Siku moja nilikutana na mkurugenzi wa Museum of Khartoum. Alikuwa na akili iliyofunguka, nasi tukawa na mazungumzo mazuri. Alipojua kuwa nilikuwa na chanzo cha Kigiriki, aliniuliza ikiwa ningeweza kumfanyia hisani ya kwenda kwenye lile jumba la kuhifadhi vitu vya kale ili kutafsiri maandishi fulani kwenye vyombo vilivyofanywa na watu vilivyopatikana katika kanisa la karne ya sita. Baada ya muda wa saa tano kwenye orofa ya chini yenye vitu vingi, nilipata kijisahani kilichoandikwa jina la Yehova, ile Tetragramatoni. Ebu wazia shangwe yangu! Huko Ulaya ni kawaida kuona jina la kimungu makanisani, lakini kulipata jina hilo katikati ya Sahara ni jambo lisilo la kawaida!
Baada ya kusanyiko la kimataifa mwaka wa 1958, nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa kanda ya dunia ili niwatembelee ndugu katika nchi na maeneo 26 katika Mashariki ya Kati na ya Karibu na kotekote Mediterania. Mara nyingi sikujua jinsi ya kutoka katika hali ngumu, lakini sikuzote Yehova aliandaa njia ya kutokea.
Sikuzote nilivutiwa na utunzaji ambao tengenezo la Yehova huonyesha Mashahidi ambao wako pekee katika nchi fulani-fulani. Pindi moja, nilikutana na ndugu Mhindi anayefanya kazi katika uwanja wa mafuta. Yaonekana alikuwa Shahidi pekee nchini. Katika kabati lake alikuwa na vichapo katika lugha 18 tofauti-tofauti, ambavyo aliwapa wafanyakazi wenzake. Hata hapa mahali ambapo dini zote za kigeni zilikatazwa vikali, ndugu yetu hakusahau daraka lake la kuhubiri habari njema. Wafanyakazi wenzake walivutiwa kuona kwamba mwakilishi wa dini yake alikuwa ametumwa kumtembelea.
Mwaka 1959 nilitembelea Hispania na Ureno. Nchi zote mbili zilikuwa chini ya udikteta wa kijeshi wakati huo, kazi ya Mashahidi wa Yehova ikiwa chini ya marufuku kali. Katika mwezi mmoja niliweza kuongoza mikutano zaidi ya mia moja, nikiwatia moyo ndugu wasichoke licha ya magumu.
Kutokuwa Peke Yangu Tena
Kwa miaka zaidi ya 20, nilikuwa nikimtumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote nikiwa mseja, lakini ghafula nikahisi nimechoka na safari zangu za mfululizo bila kuwa na makao ya kudumu. Ni karibu na wakati huo nilipokutana na Annie Bianucci, painia wa pekee huko Tunisia. Tulioana mwaka wa 1963. Kupenda kwake Yehova na ile kweli, ujitoaji wake kwenye huduma pamoja na usanifu wake wa kufundisha, na kujua kwake lugha mbalimbali kulithibitika kuwa baraka kwelikweli katika kazi yetu ya umishonari na ya kuzunguka huko kaskazini na magharibi mwa Afrika na Italia.
Agosti 1965 mke wangu nami tulipewa mgawo wa kwenda Dakar, Senegal, nilikokuwa na pendeleo la kuanzisha ofisi ya tawi ya mahali hapo. Senegal ilikuwa nchi ya kutokeza kwa kuruhusu kwayo dini, bila shaka ilikuwa kwa sababu ya rais wayo, Leopold Senghor, mmoja wa marais wachache Waafrika walioandikia Rais Banda wa Malawi wakiunga mkono Mashahidi wa Yehova wakati wa ule mnyanyaso mbaya uliotukia Malawi katika miaka ya 1970.
Baraka Tele za Yehova
Katika 1951, nilipoondoka Gileadi kwenda Saiprasi, nilisafiri na masanduku saba. Nilipoondoka kwenda Uturuki, nilikuwa na masanduku matano tu. Lakini kwa kuwa nilikuwa nikisafiri sana, nililazimika kuzoea ule mpaka wa mzigo wa kilo 20 (pauni 44) ulioruhusiwa kwenye ndege, uliotia ndani faili zangu na taipureta yangu ndogo. Siku moja nilimwambia Ndugu Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo: “Wanilinda dhidi ya ufuatiaji vitu vya kimwili. Wanifanya niishi na kilo 20 za mali, nami naridhika.” Sikuhisi kamwe kuwa nimenyimwa kitu fulani kwa sababu ya kutokuwa na mali nyingi.
Wakati wa kipindi cha safari zangu tatizo langu kuu lilikuwa kuingia na kutoka katika nchi mbalimbali. Siku moja, katika nchi ambako kazi ilikuwa imepigwa marufuku, ofisa wa forodha alianza kupekua faili zangu. Hilo lilihatarisha Mashahidi nchini, kwa hiyo nikatoa barua kutoka kwa mke wangu iliyokuwa katika mfuko wa koti langu na kumwambia ofisa wa forodha hivi: “Naona kwamba unapenda kusoma barua. Ungependa kusoma barua hii kutoka kwa mke wangu ambayo haimo katika hizo faili?” Akiwa ameaibika, aliomba radhi na kuniacha nipite.
Tangu 1982 mke wangu nami tumekuwa tukitumikia tukiwa wamishonari katika Nice, kusini mwa Ufaransa. Kwa sababu ya afya yenye kuzorota, siwezi tena kufanya mengi kadiri nilivyokuwa nikifanya. Lakini hilo halimaanishi kwamba shangwe yetu imedidimia. Tumeona kwamba ‘kazi yetu ya jasho si bure.’ (1 Wakorintho 15:58, NW) Nina shangwe ya kuona watu wengi ambao nimekuwa na pendeleo la kujifunza nao miaka iliyopita pamoja na washiriki zaidi ya 40 wa familia yangu wakimtumikia Yehova kwa uaminifu.
Sighairi kamwe dhabihu ambazo maisha yangu ya ‘kuvuka’ yamekuwa nayo. Kwa vyovyote, hakuna dhabihu zozote tufanyazo ziwezazo kulingana na yale ambayo Yehova na Mwanaye, Kristo Yesu, wametufanyia. Nifikiriapo ile miaka 60 iliyopita ambayo nimeijua kweli, naweza kusema kwamba Yehova amenibariki sana. Sawa na isemavyo Mithali 10:22, “baraka ya BWANA hutajirisha.”
Bila shaka, ‘fadhili [za Yehova] ni njema kuliko uhai.’ (Zaburi 63:3) Huku magumu ya uzee yakiongezeka, mara nyingi maneno ya mtunga-zaburi aliyepuliziwa huwa katika sala zangu: “Nimekukimbilia wewe, BWANA, nisiaibike milele. Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU, tumaini langu tokea ujana wangu. Ee Mungu, umenifundisha tokea ujana wangu; nimekuwa nikitangaza miujiza yako hata leo. Na hata nikiwa ni mzee mwenye mvi, Ee Mungu, usiniache.”—Zaburi 71:1, 5, 17, 18.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Pamoja na mke wangu, Annie, leo
-
-
“Zawadi ya Ajabu Kutoka kwa Yehova”Mnara wa Mlinzi—1996 | Novemba 1
-
-
“Zawadi ya Ajabu Kutoka kwa Yehova”
TOLEO la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1996, lilikuwa na mazungumzo yenye kina kirefu juu ya kutokuwamo kwa Kikristo na jinsi ya kusawazisha madaraka yetu kuelekea Yehova na kuelekea “Kaisari.” (Mathayo 22:21) Maelezo mengi ya kuonyesha uthamini yamesikiwa kuhusu ile habari mpya iliyoandaliwa. Miongoni mwayo ni barua ifuatayo, iliyoandikwa na Shahidi mmoja katika Ugiriki na kuelekezewa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova:
“Nataka kuwashukuru sana nyinyi ndugu wote wapendwa kwa ajili ya kutushughulikia vizuri sana kiroho. Nikiwa nimekuwa gerezani miaka tisa kwa sababu ya imani yangu ya Kikristo, kwa kweli nathamini yale mawazo ya ajabu katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1996. (Isaya 2:4) Hiyo ilikuwa zawadi ya ajabu kutoka kwa Yehova.—Yakobo 1:17.
“Nilipokuwa nikizifurahia makala hizo, nilikumbuka elezo katika Mnara wa Mlinzi la mapema (Agosti 1, 1994, ukurasa 14): ‘Kwa wazi, kukubali sababu ni sifa yenye thamani sana, sifa inayotusukuma tumpende Yehova hata zaidi.’ Ndiyo, ndugu, namshukuru Yehova kwamba mimi ni sehemu ya tengenezo lake lenye fadhili na lenye upendo, ambalo huonyesha hekima yake kwa wazi.—Yakobo 3:17.
“Ile nuru iliyoongezeka katika Mnara wa Mlinzi la Mei 1 imepokewa vema hapa Ugiriki, hasa na wale waliokuwa gerezani miaka kadhaa au ambao wangali gerezani kwa sababu ya imani yao. Asanteni tena. Yehova na awaimarishe kwa roho yake ili mwendelee kutuandalia chakula hiki cha kiroho chenye thamani katika nyakati hizi zenye taabu.”
-