“Zawadi ya Ajabu Kutoka kwa Yehova”
TOLEO la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1996, lilikuwa na mazungumzo yenye kina kirefu juu ya kutokuwamo kwa Kikristo na jinsi ya kusawazisha madaraka yetu kuelekea Yehova na kuelekea “Kaisari.” (Mathayo 22:21) Maelezo mengi ya kuonyesha uthamini yamesikiwa kuhusu ile habari mpya iliyoandaliwa. Miongoni mwayo ni barua ifuatayo, iliyoandikwa na Shahidi mmoja katika Ugiriki na kuelekezewa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova:
“Nataka kuwashukuru sana nyinyi ndugu wote wapendwa kwa ajili ya kutushughulikia vizuri sana kiroho. Nikiwa nimekuwa gerezani miaka tisa kwa sababu ya imani yangu ya Kikristo, kwa kweli nathamini yale mawazo ya ajabu katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1996. (Isaya 2:4) Hiyo ilikuwa zawadi ya ajabu kutoka kwa Yehova.—Yakobo 1:17.
“Nilipokuwa nikizifurahia makala hizo, nilikumbuka elezo katika Mnara wa Mlinzi la mapema (Agosti 1, 1994, ukurasa 14): ‘Kwa wazi, kukubali sababu ni sifa yenye thamani sana, sifa inayotusukuma tumpende Yehova hata zaidi.’ Ndiyo, ndugu, namshukuru Yehova kwamba mimi ni sehemu ya tengenezo lake lenye fadhili na lenye upendo, ambalo huonyesha hekima yake kwa wazi.—Yakobo 3:17.
“Ile nuru iliyoongezeka katika Mnara wa Mlinzi la Mei 1 imepokewa vema hapa Ugiriki, hasa na wale waliokuwa gerezani miaka kadhaa au ambao wangali gerezani kwa sababu ya imani yao. Asanteni tena. Yehova na awaimarishe kwa roho yake ili mwendelee kutuandalia chakula hiki cha kiroho chenye thamani katika nyakati hizi zenye taabu.”