SURA YA 15
Nitashindaje Mkazo Kutoka kwa Vijana Wenzangu?
“Shuleni kuna vishawishi vingi sana—kuvuta sigara, dawa za kulevya, ngono, na kadhalika. Unajua kwamba kile ambacho vijana wenzako wanataka ufanye hakifai. Lakini wakati mwingine unaona kwamba ukikataa utaonekana kuwa mwoga.”—Eve.
KILA mtu hutaka kukubaliwa na wengine. Na kwa sababu ya tamaa hiyo, sisi hutaka kuwa sawa na wengine. Kwa mfano, ikiwa umelelewa na wazazi Wakristo, unajua kwamba mambo kama kufanya ngono kabla ya ndoa na matumizi mabaya ya pombe ni dhambi. (Wagalatia 5:19-21) Hata hivyo, vijana wenzako wanakusihi ujiunge nao katika mambo hayo. Je, walifikiria mambo hayo na kujiamulia wenyewe kuyafanya? Haielekei. Mara nyingi wanafuata tu upepo. Kwa sababu wanataka kukubaliwa, wanawafuata wengine kama vipofu. Je, ndivyo unavyofanya pia? Au unaweza kuwa na msimamo?
Haruni, ndugu ya Musa alilemewa na mkazo kutoka kwa wengine, angalau katika pindi moja. Waisraeli walipomzunguka na kusisitiza awatengenezee mungu, Haruni alikubali kufanya walivyotaka! (Kutoka 32:1-4) Hebu wazia—yeye ndiye aliyezungumza na Farao uso kwa uso na kumpa ujumbe kutoka kwa Mungu bila woga. (Kutoka 7:1, 2, 16) Lakini Waisraeli wenzake waliposisitiza sana, Haruni aliingiwa na hofu. Inaonekana ilikuwa rahisi kwake kuwa na uhodari wa kumkabili mfalme wa Misri kuliko kuwakabili Waisraeli wenzake!
Namna gani wewe? Je, wewe huona ni vigumu kuchukua msimamo unaofaa? Je, ungependa kujua jinsi ya kufanya hivyo bila kuonekana kuwa mwoga? Unaweza! Siri ni kufikiria mapema hali inayoweza kutokea na kuamua jinsi utakavyotenda. Hatua nne zinazofuata zitakusaidia kufanya hivyo.
1. Fikiria mapema hali zinazoweza kutokea. (Methali 22:3) Mara nyingi unaweza kuona hatari mapema. Kwa mfano, unatupa jicho na kuwaona wanafunzi wenzako wakija huku wakivuta sigara. Kuna uwezekano kwamba watakupa sigara? Kwa kufikiria mapema tatizo linaloweza kutokea, utakuwa tayari kuliepuka au kulikabili.
2. Tafakari. (Waebrania 5:14) Jiulize, ‘Nikijiunga nao, nitahisi namna gani baadaye?’ Ni kweli kwamba huenda mwanzoni ukakubaliwa na vijana wenzako. Lakini utahisi namna gani baadaye, ukiwa na wazazi wako au Wakristo wenzako? Uko tayari kupoteza msimamo wako mzuri pamoja na Mungu ili tu uwafurahishe wanafunzi wenzako?
3. Fanya uamuzi. (Kumbukumbu la Torati 30:19) Mwishowe, lazima watumishi wote wa Mungu wafanye uamuzi ikiwa watakuwa waaminifu na kupata baraka au ikiwa watakosa kuwa waaminifu na kuvuna mabaya. Watu kama vile Yosefu, Ayubu, na Yesu walifanya maamuzi mazuri, lakini Kaini, Esau, na Yuda walifanya maamuzi mabaya. Huu ni wakati wako wa kufanya uamuzi. Utafanya uamuzi gani?
4. Chukua hatua. Huenda ukafikiri kwamba kufanya hivyo ndilo jambo gumu zaidi. Lakini sivyo! Ikiwa tayari umefikiria kuhusu matokeo na kufanya uamuzi, huenda ikawa rahisi kutangaza msimamo wako kuliko unavyofikiri, nawe unaweza kupata matokeo mazuri. (Methali 15:23) Usiwe na shaka, huhitaji kuwatolea mahubiri marefu ya Biblia. Huenda ikatosha tu kuwaambia kwa uthabiti, ‘Hapana.’ Au ili kujulisha waziwazi msimamo wako usiobadilika, huenda ukaamua kusema:
“Niacheni!”
“Sifanyi mambo kama hayo!”
“Inaonekana hamnijui!”
Jambo kuu ni kujibu kwa usadikisho na bila kusita. Ukifanya hivyo, huenda ukashangaa kuona vijana wenzako wakiacha usumbufu wao mara moja! Namna gani wakikudhihaki? Utafanya nini wakisema, “Una shida gani? Hebu mwone, ni mwoga kama kuku?” Badala ya kukasirishwa na dhihaka hizo, kumbuka kwamba wanasema hivyo ili kuzidisha mkazo. Unaweza kufanya nini? Kuna angalau mambo matatu unayoweza kufanya.
● Unaweza kukubali dhihaka hizo. (“Ni kweli, ninaogopa!” Kisha waeleze kifupi kwa nini unaogopa.)
● Unaweza kupiga chenga. Waeleza msimamo wako, pasipo ubishi.
● Dawa ya moto ni moto. Waeleze sababu yako ya kukataa kisha waambie jambo ambalo litawafanya waone upumbavu wa mambo wanayofanya. (“Mtu mwenye akili timamu hawezi kuvuta sigara!”)
Vijana wenzako wakiendelea kukudhihaki, nenda zako! Unavyozidi kukaa hapo, ndivyo mkazo unavyozidi kuongezeka. Hata ukilazimika kuondoka, kumbuka: Ulitenda inavyofaa. Hukuwaruhusu vijana wenzako wakufanyie maamuzi.
Baadhi ya vijana wenzako wanaweza kukudhihaki na kusema kwamba hutumii akili yako. Sivyo hata kidogo! Yehova angependa ujithibitishie mwenyewe kwamba kufanya mapenzi yake ndilo jambo bora zaidi. (Waroma 12:2) Kwa hiyo mbona uwaruhusu vijana wenzako wakutumie kama kikaragosi? (Waroma 6:16) Chukua msimamo imara upande unaofaa!
Ukweli ni kwamba, huwezi kuepuka kabisa mkazo kutoka kwa vijana wenzako. Lakini unaweza kujua msimamo wako, unaweza kuwajulisha wengine msimamo wako, na kutopoteza usawaziko wako. Mwishowe, uamuzi ni wako!—Yoshua 24:15.
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 9
Je, una nyuso mbili? Kuna faida yoyote wazazi wako wakijua maisha yako?
MAANDIKO MUHIMU
“Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” —Methali 13:20.
PENDEKEZO
Ili kuwa na ujasiri zaidi, soma mambo yaliyoonwa ambayo yamechapishwa kuhusu watumishi wa Yehova wa siku zetu, ambao wamesimama imara na kutetea yaliyo sawa.
JE, WAJUA . . .?
Ni wachache sana kati ya wanafunzi wenzako watakaokuwa wakiwasiliana nawe mwaka mmoja baada ya kumaliza shule. Labda hata wengi wao hawatakumbuka jina lako. Lakini sikuzote familia yako, na hata zaidi Yehova Mungu, watapendezwa na hali njema yako.—Zaburi 37:23-25.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ninaweza kujitayarisha kupinga mkazo kutoka kwa vijana wa rika langu kwa ․․․․․
Vijana wenzangu wakinilazimisha nifanye jambo lisilofaa, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Ni katika hali gani mambo manne yaliyo katika sura hii yanaweza kukusaidia?
● Ni nini kinachoweza kutokea ukishindwa na mkazo kutoka kwa vijana wenzako?
● Unaweza kushinda jinsi gani mkazo kutoka kwa vijana wenzako?
[Blabu katika ukurasa wa 131]
“Vijana wengi wanajua mimi ni Shahidi, na wananiheshimu. Wakitaka kuzungumzia jambo lisilofaa, wanasema, ‘Mike, tunataka kuongea mambo yetu, kwa hiyo ikiwa unataka kuondoka, ondoka.’’’—Mike
[Chati katika ukurasa wa 132, 133]
Ukurasa wa Mazoezi
Kukabiliana na mkazo
Kielelezo
1 Fikiria mapema
Ni hali gani inayoweza kutokea? Kuvuta sigara.
Ni wapi hasa inapoweza kutokea? Katika chumba cha kubadili mavazi au chooni.
2 Tafakari
Itakuwaje nikilegeza msimamo wangu?
Nitamchukiza Yehova na wazazi wangu. Nitakuwa na dhamiri mbaya. Itakuwa vigumu zaidi kukataa wakati ujao.
Itakuwaje nikisimama? imara?
Huenda nikadhihakiwa au kutukanwa. Huenda baadhi ya marafiki wangu shuleni wakaanza kuniepuka. Lakini nitamfurahisha Yehova, nami nitakuwa mtu mwenye msimamo.
3 Amua
Itakuwaje nikilegeza, msimamo wangu?
sijajitayarisha vya kutosha kushinda mikazo kutoka kwa vijana wenzangu Ninaona kwamba ni afadhali kuwapendeza vijana wenzangu kuliko kumpendeza Yehova.
Nitasimama imara kwa sababu
ninajua kwamba kuvuta sigara ni chukizo machoni pa Yehova na kufanya hivyo kunaweza kudhuru afya yangu.
4 Tenda
Hali hiyo ikitokea
Nitakataa na kuondoka mara moja.
Dhihaka za Marika
Kijana mwenzangu akisema: “Acha mambo yako, vuta. sigara moja tu. Mbona wewe ni mwoga hivyo?”
Ninaweza kukabili mkazo huo kwa
Kukubali dhihaka
“Ni kweli. Naogopa sigara. Sitaki kupata kansa ya mapafu.”
Kuwapiga chenga
“Msipoteze sigara zenu bure kwa kunipa.”
Dawa ya moto ni moto
“Hapana. Nilifikiri mna akili ya kutosha kutovuta sigara!”
TAARIFA: Ondoka mahali hapo mara moja ikiwa vijana wenzako wanaendelea kukushinikiza. Kadiri unavyozidi kukaa, ndivyo unavyozidi kuhatarisha azimio lako la kusimama imara. Sasa, jaza mwenyewe ukurasa unaofuata.
Kukabiliana na mkazo
Nakili ukurasa huu!
1 Fikiria mapema
Ni hali gani inayoweza kutokea? ․․․․․
Ni wapi hasa inapoweza kutokea? ․․․․․
2 Tafakari
Itakuwaje nikilegeza msimamo wangu?
․․․․․
Itakuwaje nikisimama imara?
․․․․․
3 Amua
Nikilegeza msimamo wangu, itakuwa ni kwa sababu . . .
․․․․․
Nitasimama imara kwa sababu . . .
․․․․․
4 Tenda
․․․․․
Hali hiyo ikitokea nita . . .
․․․․․
Dhihaka za Marika
Kijana mwenzangu akisema: ․․․․․
Ninaweza kukabili mkazo huo kwa
Kukubali dhihaka
․․․․․
Kuwapiga chenga
․․․․․
Dawa ya moto ni moto
․․․․․
Ukiwa na mzazi au rafiki mkomavu, fanya mazoezi naye.
[Picha katika ukurasa wa 135]
Ukikubali kuongozwa na vijana wenzako, unakuwa kama kikaragosi