Theofilo wa Antiokia Alikuwa Nani?
“WEWE waniita Mkristo, kana kwamba ni vibaya sana kuwa na jina hilo, mimi kwa upande wangu, natangaza wazi kwamba mimi ni Mkristo, na nabeba jina hili ili niwe mpendwa wa Mungu, nikitumaini kuweza kutumiwa na Mungu.”
Hivyo Theofilo aanzisha uandishi wake wenye sehemu tatu wenye kichwa Theophilus to Autolycus. Ni mwanzo wa utetezi wake dhidi ya uasi-imani wa karne ya pili. Theofilo ajitambulisha kwa ujasiri kuwa mfuasi wa Kristo. Yeye aonekana kuwa mwenye azimio kuendesha mambo yake ili awe “mpendwa wa Mungu,” kupatana na maana ya jina lake katika lugha ya Kigiriki. Lakini Theofilo alikuwa nani? Yeye aliishi wakati gani? Na alitimiza nini?
Historia ya Kibinafsi
Ni machache sana yajulikanayo juu ya historia ya kibinafsi ya Theofilo. Yeye alilelewa na wazazi wasio Wakristo. Baadaye Theofilo akageuka kuwa Mkristo lakini baada tu ya kujifunza Maandiko kwa uangalifu. Akawa askofu wa kutaniko katika Antiokia ya Siria, iitwayo leo Antakya, katika Uturuki.
Kupatana na amri ya Yesu, Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri miongoni mwa watu wa Antiokia. Luka alirekodi mafanikio yao, akisema: “Mkono wa Bwana ukawa pamoja nao, watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana.” (Matendo 11:20, 21) Kama ilivyoelekezwa kimungu, wafuasi wa Yesu Kristo wakaja kuitwa Wakristo. Usemi huu ulitumika kwa mara ya kwanza katika Antiokia ya Siria. (Matendo 11:26) Katika karne ya kwanza W.K., mtume Paulo alisafiri hadi Antiokia ya Siria na hapo pakawa makao yake ya kuanzia safari zake. Barnaba na Paulo, wakiandamana na Yohana Marko, walianza safari yao ya kimishonari ya kwanza kutoka Antiokia.
Lazima Wakristo wa mapema wa Antiokia wawe walitiwa moyo sana na ziara za kimitume kwa jiji lao. Itikio lao lenye idili kwa kweli ya Neno la Mungu bila shaka kwa sehemu lilikuwa kwa sababu ya ziara zenye kuimarisha imani za wawakilishi wa karne ya kwanza wa baraza linaloongoza. (Matendo 11:22, 23) Jinsi walivyotiwa moyo kuona wakazi wengi mno wa Antiokia wakiweka maisha zao wakfu kwa Yehova Mungu! Hata hivyo, ilikuwa zaidi ya miaka 100 baadaye kwamba Theofilo aliishi katika Antiokia.
Mwanahistoria Eusebio alitaarifu kwamba Theofilo alikuwa askofu wa sita wa Antiokia, akihesabu kutoka wakati wa mitume wa Kristo. Theofilo aliandika mazungumzo kadhaa na mikanusho dhidi ya uzushi. Yeye atiwa ndani ya watetezi Wakristo 12 hivi wa siku yake.
Kutazama Maandishi Yake
Akijibu mazungumzo ya mapema zaidi, Theofilo amwandikia Atoliko mpagani kwa maneno haya ya ufunguzi: “Ulimi wenye ufasaha na usemi mzuri hutoa raha na sifa kama ile ifurahiwayo na ubatili, kwa watu waovu ambao akili zao zimefisidiwa.” Theofilo aeleza, akisema: “Mpenda-kweli hatoi uangalifu kwa maneno yaliyorembeshwa, bali huchunguza maana yenyewe ya maneno . . . Wewe umenishambulia kwa maneno yenye utupu, ukijiringia miungu yako ya mbao na mawe, iliyotengenezwa kwa nyundo na iliyosubiwa, iliyochongwa na kunakshiwa, ambayo haiwezi wala kuona wala kusikia, kwa kuwa hiyo ni sanamu, kazi ya mikono ya wanadamu.”—Linganisha Zaburi 115:4-8.
Theofilo afunua kosa la ibada ya sanamu. Katika namna yake ya kawaida ya uandishi, yeye ajitahidi kutaarifu hali asili ya Mungu wa kweli kwa ufasaha wenye kuchochea, ingawa kwa kurudia-rudia. Yeye aeleza hivi: “Sura ya Mungu haiwezi kuelezeka, na haiwezi kuonwa na macho ya binadamu. Kwa kuwa katika utukufu Yeye hawezi kufahamika, katika ukuu asiyetambulikana, katika kimo asiyewazika, katika uwezo asiyelinganika, katika hekima asiye na kifani, katika wema asiyeigika, katika fadhili asiyeelezeka.”
Akiongezea kwa ufafanuzi huu wa Mungu, Theofilo aendelea hivi: “Lakini yeye ni Bwana, kwa sababu Yeye atawala ulimwengu wote mzima; Baba, kwa sababu ndiye aliye kabla ya kila kitu; Mbuni na Mfanyi, kwa sababu Yeye ndiye muumba na mfanyi wa ulimwengu wote mzima; Aliye Juu Zaidi, kwa sababu ya kuwa Kwake juu ya kila kitu; na Mweza Yote, kwa sababu Yeye Mwenyewe hutawala na huona kila kitu.”
Halafu, akielekeza fikira kwa matimizo hususa ya Mungu, Theofilo aendelea katika namna ya kawaida ya mtindo wake wa kukazia ambao ni kama wa kurudia-rudia, akisema: “Kwa kuwa mbingu ni kazi Yake, dunia uumbaji Wake, bahari ni kazi ya mikono Yake; mwanadamu ni mfanyizo Wake na mfano Wake; jua, mwezi, na nyota ni uumbaji Wake, viliumbwa ili kuwa ishara, na majira, na siku, na miaka, ili kwamba vitumikie na kuwa watumwa wa mwanadamu; na vitu vyote Mungu amevitengeneza kutoka vitu ambavyo havikuwapo hadi kuwa vitu vyote vilivyopo, ili kwamba kupitia kazi Zake ukuu Wake ujulikane na kufahamika.”
Kielelezo kingine zaidi cha shambulizi la Theofilo kwa miungu bandia ya siku yake chaonekana katika maneno yafuatayo kwa Atoliko: “Majina ya wale usemao kuwa wawaabudu, ni majina ya watu waliokufa. . . . Na walikuwa watu wa aina gani? Je, Sarateni hajajulikana kuwa mla-mnofu wa viumbe aina yake mwenyewe, akiharibu na kunyafua watoto wake mwenyewe? Na ikiwa wamwita mwana wake Sumbula, . . . jinsi alivyonyonyeshwa na mbuzi . . . Na matendo yake mengine,—ngono zake za maharimu, na uzinzi, na uchu.”
Akizidisha bishano lake, Theofilo atia nguvu msimamo wake katika kupinga ibada ya sanamu ya wapagani. Yeye aandika hivi: “Je, nitaje pia wanyama wengi walioabudiwa na Wamisri, wote wanyama-watambazi, na ng’ombe, na hayawani mwitu, na ndege, na samaki wa mtoni . . . Wagiriki na mataifa mengine, huabudu mawe na mbao, na namna nyinginezo za vitu vionekanavyo.” “Lakini mimi namwabudu Mungu, Mungu anayeishi na wa kweli,” atangaza Theofilo.—Linganisha 2 Samweli 22:47; Matendo 14:15; Warumi 1:22, 23.
Ushahidi Wenye Thamani
Maonyo na mashauri katika uandishi wa Theofilo kumpinga Atoliko wenye sehemu tatu yana sehemu nyingi na hueleza mambo mengi. Maandishi mengine ya Theofilo yalielekezwa dhidi ya Hamogene na Maseni. Yeye pia aliandika vitabu vya maagizo na kufundisha mema, akiongeza maelezo kwenye Gospeli. Hata hivyo, ni vitabu vitatu tu vilivyoelekezwa kwa Atoliko ambavyo vimehifadhiwa katika hati moja.
Kitabu cha kwanza ni utetezi ulioandikiwa Atoliko kutetea dini ya Ukristo. Kitabu cha pili kinachoelekezwa kwa Atoliko chajadili dini ipendwayo ya kikafiri, ukisiaji-kisiaji, wanafalsafa, na washairi. Vitabu vya kikafiri vinalinganishwa na Maandiko katika kitabu cha tatu cha Theofilo.
Katika kuanzishwa kwa kitabu cha tatu cha Theofilo, yaonekana Atoliko bado alikuwa na maoni kwamba Neno la kweli lilikuwa hekaya tu. Theofilo amchambua Atoliko, akidai hivi: “Wewe huvumilia wapumbavu kwa furaha. Sivyo hungesukumwa na maneno yenye utupu ya watu wasio na akili, na kuamini uvumi ulioenea sana.”
Huo “uvumi ulioenea sana” ulikuwa nini? Theofilo afunua chanzo. Wachongezi “wenye midomo isiyomhofu Mungu hutushtaki, [sisi] ambao ni waabudu wa Mungu, na tuitwao Wakristo, wakidai kwamba wake zetu ni wa kila mtu na hushirikiwa kwa makusudi ya kingono; na kwamba sisi hata hufanya ngono ya maharimu na dada zetu wa kimwili, na, jambo lisilo na staha na la kishenzi kupita yote, kwamba sisi hula mnofu wa binadamu.” Theofilo alifanya kazi ngumu kupambana na maoni haya yasiyo sahihi kabisa ya waliodai kuwa Wakristo wa karne ya pili. Yeye alitumia nuru ya kweli ipatikanayo katika Neno la Mungu lililopuliziwa.—Mathayo 5:11, 12.
Jambo linalotoa ushahidi kwamba Theofilo alifahamu Neno la Mungu ni utumizi wake wa mara kwa mara na marejezo kwa maandiko ya Biblia yote ya Kiebrania na Kigiriki. Yeye alikuwa mmoja wa watoa-maelezo juu ya Gospeli wa mapema zaidi. Marejezo mengi ya Theofilo kwa Maandiko hutoa ufahamu mwingi wenye kina wa kufikiri kulikoenea sana katika siku yake. Yeye alitumia ufahamu wake mwingi wa maandishi yaliyopuliziwa ili kudhihirisha ubora wayo juu ya falsafa ya kipagani.
Mpangilio wa habari ya Theofilo, hali yake ya kufundisha, na namna ya kujirudia-rudia huenda isivutie watu fulani. Hatuwezi kusema kwa wakati huu ni kwa kadiri gani uasi-imani uliotabiriwa ulivyoathiri usahihi wa maoni yake. (2 Wathesalonike 2:3-12) Hata hivyo, kufikia wakati wa kifo chake, karibu 182 W.K., yaonekana Theofilo alikuwa amekuwa mtetezi asiyechoka, ambaye maandishi yake yanapendeza Wakristo wa kweli wa muhula wetu wa kisasa.
[Picha katika ukurasa wa 30]
Theofilo alikanusha kwa ujasiri ubishi wa Atoliko
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 28]
Picha kwenye kurasa 28 na 30 zilitolewa kutoka Illustrirte Pracht - Bibel/Heilige Schrift des Alten und Neuen Testaments, nach der deutschen Uebersetzung D. Martin Luther’s