-
Je, Niko Tayari Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 1
Je, Niko Tayari Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?
“Kuna mkazo mwingi sana wa kuwa na mpenzi. Isitoshe kuna wavulana wengi sana wenye kuvutia.”—Whitney.
“Wasichana fulani hawasiti kusema kwamba wangependa tuwe wapenzi, nami ningependa pia. Lakini nikiwauliza wazazi wangu, ninajua hawatakubali.”—Phillip.
TAMAA ya kuwa pamoja na mtu fulani anayekuvutia, ambaye pia anavutiwa na wewe, inaweza kuwa na nguvu sana, nayo inaweza kuanza mapema sana maishani. Jenifer anakumbuka hivi: “Nilianza kupata mkazo wa kuwa na rafiki wa kiume nilipokuwa na umri wa miaka 11.” Brittany anasema: “Shuleni, usipokuwa na mpenzi, unaonwa kuwa hufai. Ni afadhali uwe na mpenzi yeyote yule, angalau uonekane kuwa una mpenzi!”
Namna gani wewe? Je, uko tayari kuanzisha urafiki wa kimapenzi? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji kwanza kufikiria swali moja la msingi:
“Urafiki wa Kimapenzi” Ni Nini?
Jibu maswali yanayofuata kwa kutia alama mahali panapofaa:
Una kawaida ya kwenda matembezi pamoja na mtu wa jinsia tofauti. Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?
□ Ndiyo
□ Hapana
Unavutiwa na mtu wa jinsia tofauti ambaye anavutiwa nawe pia. Mara kadhaa kwa siku mnatumiana ujumbe mfupi kwenye simu au kupigiana simu. Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?
□ Ndiyo
□ Hapana
Kila mara mnapokuwa katika tafrija pamoja na marafiki, unatumia muda mwingi pamoja na mtu yuleyule wa jinsia tofauti. Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?
□ Ndiyo
□ Hapana
Labda haikuwa vigumu kwako kujibu swali la kwanza. Lakini huenda ulisita kidogo kabla ya kujibu swali la pili na la tatu. Urafiki wa kimapenzi ni nini hasa? Urafiki wa kimapenzi ni urafiki kati ya watu wawili wanaovutiana kimahaba na unatia ndani shughuli yoyote ya kirafiki ambayo wanafanya pamoja. Kwa hiyo, jibu la maswali yote matatu ni ndiyo. Iwe kwa simu, uso kwa uso, mbele ya watu, au mahali pasipo na watu, ikiwa wewe na rafiki yako wa jinsia tofauti mnaonyeshana mahaba na mnawasiliana kwa ukawaida, basi huo ni urafiki wa kimapenzi. Je, uko tayari kuanzisha urafiki wa aina hiyo? Kufikiria maswali matatu kutakusaidia kujua kama uko tayari.
Kwa Nini Unataka Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?
Katika jamii nyingi, urafiki wa kimapenzi unaonwa kuwa njia inayofaa ya watu wawili kufahamiana vizuri. Hata hivyo, urafiki huo unapaswa kuwa na kusudi lenye kuheshimika, yaani, kumsaidia mwanamume na mwanamke kujua ikiwa wanaweza kufunga ndoa.
Labda vijana wenzako hawauoni urafiki huo kuwa jambo zito. Pengine wanafurahia tu kuwa na rafiki wa pekee wa jinsia tofauti bila kusudi lolote la kufunga ndoa. Huenda hata wengine wao wanawaona rafiki hao kuwa “tuzo” au “pambo” ambalo linawafanya waheshimiwe. Hata hivyo, mara nyingi urafiki huo usio na msingi mzuri haudumu. Msichana mmoja anayeitwa Heather alisema hivi: “Vijana wengi ambao wanaanzisha urafiki wa kimapenzi, wanauvunja baada ya juma moja au mawili. Wanaanza kuwa na maoni ya kwamba urafiki kama huo ni wa muda tu, na maoni hayo yanawatayarisha kwa talaka badala ya ndoa.”
Ni wazi kwamba unapoanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu fulani, hisia zake zinahusika. Kwa hiyo, hakikisha kwamba una nia nzuri. Hebu fikiria: Je, ungependa mtu fulani achezee hisia zako kama vile mtoto anavyocheza-cheza na kitu cha kuchezea kisha anakiacha? Msichana anayeitwa Chelsea anasema hivi: “Wakati mwingine ninaona kwamba urafiki wa kimapenzi unapaswa kuwa jambo la kujifurahisha tu, lakini haliwezi kuwa jambo la kujifurahisha tu ikiwa mtu mmoja anauchukulia urafiki huo kwa uzito naye yule mwingine anauona kuwa mchezo tu.”
Ati Una Miaka Mingapi?
Unafikiri kijana anapaswa kuanzisha urafiki wa kimapenzi akiwa na umri gani? ․․․․․
Sasa muulize mmoja wa wazazi wako au wote wawili swali hilohilo kisha uandike jibu. ․․․․․
Inawezekana kwamba namba ya kwanza uliyoandika ni ndogo kuliko ya pili. Au labda sivyo! Labda wewe ni mmoja kati ya vijana wengi ambao kwa busara wameahirisha kuanzisha urafiki wa kimapenzi mpaka watakapokuwa na umri wa kutosha kujielewa vizuri. Hivyo ndivyo Danielle, aliye na umri wa miaka 17, alivyoamua kufanya. Anasema hivi: “Miaka miwili iliyopita, sifa ambazo nilitaka rafiki yangu wa karibu awe nazo ni tofauti sana na zile ambazo ninapendezwa nazo sasa. Kwa kweli, hata sasa sina hakika kwamba ninaweza kufanya uamuzi mzito kama huo. Baada ya miaka kupita, nikiona kwamba utu wangu umekomaa, nitafikiria kuanzisha urafiki wa kimapenzi.”
Kuna sababu nyingine nzuri ya kungoja. Biblia inatumia maneno “upeo wa ujana” kufafanua kipindi cha maisha ambapo tamaa za ngono na hisia za mahaba zinaanza kuwa zenye nguvu. (1 Wakorintho 7:36) Kuwa na urafiki wa karibu na mtu yuleyule wa jinsia tofauti ukiwa katika kipindi hicho kunaweza kuwasha tamaa hizo na kukufanya utumbukie katika mwenendo mbaya. Ni kweli kwamba huenda marafiki wako wasione hilo kuwa jambo zito. Wengi wao wanatamani sana kufanya ngono. Lakini unaweza kuwa tofauti na wao! (Waroma 12:2) Biblia inakuhimiza “uukimbie upotovu wa kingono.” (1 Wakorintho 6:18, New International Version) Ukingoja mpaka upite upeo wa ujana, unaweza ‘kuuondolea mbali msiba.’—Mhubiri 11:10.
Je, Uko Tayari Kufunga Ndoa?
Ili uweze kujibu swali hilo, jichunguze kwa makini. Fikiria mambo haya:
Uhusiano wako na wengine. Wewe huwatendea wazazi wako na ndugu na dada zako jinsi gani? Je, mara nyingi unashindwa kujizuia unaposhughulika nao, labda kwa kutumia maneno makali au ya dhihaka unapotoa maoni? Wao wanaweza kusema nini kuhusu jambo hilo? Jinsi unavyoshughulika na watu wa familia yenu ndivyo utakavyomtendea mwenzi wako.—Soma Waefeso 4:31.
Mtazamo. Je, wewe hutazamia mema au unaona mambo yote kuwa mabaya? Je, una usawaziko, au sikuzote unasisitiza mambo yafanywe kwa njia yako? Je, wewe huwa mtulivu chini ya mkazo? Je, una subira? Kukuza matunda ya roho ya Mungu sasa kutakusaidia ujitayarishe kuwa mume au mke.—Soma Wagalatia 5:22, 23.
Matumizi ya Pesa. Je, unatumia pesa vizuri? Je, una madeni mengi? Je, wewe huachishwa kazi mara kwa mara? Ikiwa ndivyo, ni kwa nini? Je, ni kwa sababu ya kazi yenyewe au yule aliyekupa kazi? Au ni kwa sababu ya zoea au tabia fulani ambayo unapaswa kurekebisha? Ikiwa hutumii vizuri pesa zako mwenyewe, je, utaweza kutumia vizuri pesa za familia?—Soma 1 Timotheo 5:8.
Hali ya Kiroho. Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, una sifa gani za kiroho? Je, una mpango wa kusoma Neno la Mungu, kuhubiri, na kushiriki katika mikutano ya Kikristo? Mtu ambaye utafunga ndoa pamoja naye anastahili kupata mwenzi aliye imara kiroho.—Soma Mhubiri 4:9, 10.
Mambo Ambayo Unaweza Kufanya
Kuwa chini ya mkazo wa kuanzisha urafiki wa kimapenzi kabla ya kuwa tayari ni kama kulazimishwa kufanya mtihani wa somo ambalo umeanza tu kujifunza. Bila shaka, utahisi kwamba umeonewa! Unahitaji wakati wa kujifunza somo hilo ili uwe na habari zitakazokuwezesha kupita mtihani huo.
Ndivyo ilivyo pia kuhusiana na urafiki wa kimapenzi. Kama tulivyoona, urafiki wa kimapenzi si mchezo. Kwa hiyo, kabla ya kuwa tayari kumkazia fikira mtu mmoja hususa, unahitaji kujifunza “somo” muhimu sana—jinsi ya kujenga urafiki. Baadaye, utakapompata mtu anayekufaa, utakuwa tayari kujenga urafiki wenye kudumu. Kusema kweli, ndoa nzuri ni muungano wa marafiki wawili wakubwa.
Kungoja muda upite kabla ya kuanzisha urafiki wa kimapenzi hakukunyimi uhuru. Badala yake, kunakupa uhuru zaidi wa ‘kushangilia katika ujana wako.’ (Mhubiri 11:9) Nawe utakuwa na wakati wa kujitayarisha kwa kuboresha utu wako, na zaidi ya yote, hali yako ya kiroho.—Maombolezo 3:27.
Kwa sasa, unaweza kufurahia kushirikiana na watu wa jinsia tofauti. Jinsi gani? Njia bora ni kushirikiana nao mkiwa katika vikundi vyenye mchanganyiko wa wavulana na wasichana ambavyo vinasimamiwa vizuri. Msichana anayeitwa Tammy anasema: “Nafikiri inafurahisha zaidi mambo yanapofanywa kwa njia hiyo. Ni afadhali kuwa na marafiki wengi.” Monica anakubaliana naye. Anasema: “Kushirikiana katika vikundi ni wazo zuri, kwa sababu unaona watu wenye nyutu tofauti-tofauti.”
Kwa upande mwingine, ukimkazia fikira mtu mmoja tu mapema sana maishani, huenda ukavunjwa moyo. Kwa hiyo, usiwe na haraka. Tumia wakati huu wa maisha yako kujifunza jinsi ya kusitawisha na kudumisha urafiki. Baadaye, ukichagua kuanzisha urafiki wa kimapenzi, utakuwa umejifahamu vizuri zaidi na kufahamu sifa ambazo ungependa mwenzi wa ndoa awe nazo.
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 29 NA 30
Je, unataka kuanzisha urafiki wa kimapenzi bila wazazi wako kujua? Huenda usijue kwamba kuna hatari nyingi za kufanya hivyo.
MAANDIKO MUHIMU
“Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.
PENDEKEZO
Ili kujitayarisha kwa ajili ya urafiki wa kimapenzi na ndoa, soma 2 Petro 1:5-7 na uchague sifa moja ambayo unahitaji kufanyia kazi. Baada ya mwezi mmoja, jichunguze uone kadiri ambavyo umejifunza kuhusu sifa hiyo na kuiboresha.
JE, WAJUA . . .
Uchunguzi mbalimbali umeonyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa wa ndoa ya watu wenye umri wa chini ya miaka 20 kuvunjika kwa talaka kabla ya miaka mitano kuisha.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ili kujitayarisha kwa ajili ya ndoa, ninahitaji kufanyia kazi sifa hizi: ․․․․․
Ninaweza kufanyia kazi sifa hizo kwa ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Unaweza kuchangamana na watu wa jinsia tofauti katika hali gani zinazofaa?
● Unaweza kufanya nini ili kumsaidia ndugu au dada yako ambaye anataka kuanzisha urafiki wa kimapenzi akiwa na umri mdogo sana?
● Ukianzisha urafiki wa kimapenzi bila nia ya kufunga ndoa, unaweza kuathiri jinsi gani hisia za mwenzako?
[Babu katika ukurasa wa 18]
“Nafikiri unapaswa kuanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu ambaye kwa kweli unampenda na unaona kwamba uhusiano wenu unaweza kukua. Unamjali mtu mwenyewe bali si msisimuko tu wa kuwa na urafiki wa kimapenzi.’’—Amber
[Picha katika ukurasa wa 16, 17]
Ukianzisha urafiki wa kimapenzi bila nia ya kufunga ndoa, unatenda kama mtoto anayecheza-cheza na kitu cha kuchezea kisha anakiacha
-
-
Kuna Ubaya Gani Kuwa na Urafiki wa Kimapenzi wa Siri?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 2
Kuna Ubaya Gani Kuwa na Urafiki wa Kimapenzi wa Siri?
Jessica alijikuta mashakani. Kijana mmoja darasani anayeitwa Jeremy alianza kupendezwa naye. “Alikuwa na sura nzuri sana,” Jessica anasema, “na marafiki wangu walisema kwamba sitapata kamwe mvulana mwingine mzuri kama huyo. Wasichana wengi walikuwa wamejaribu kuanzisha urafiki naye, lakini hakupendezwa nao. Alipendezwa na mimi tu.”
Muda si muda, Jeremy alimwomba Jessica wawe marafiki. Jessica alijibu kwamba kwa kuwa yeye ni Shahidi wa Yehova hangeruhusiwa kuanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu ambaye si wa dini yake. “Hata hivyo,” Jessica anasema, “Jeremy alikuwa na wazo lingine. Aliuliza, ‘Kwa nini tusiwe na urafiki bila wazazi wako kujua?’”
IKIWA mtu fulani ambaye wewe unavutiwa naye angependekeza muwe na urafiki wa aina hiyo, ungefanya nini? Huenda ukashangaa kujua kwamba Jessica alikubali wazo la Jeremy. “Nilisadiki kwamba tukiwa marafiki, ninaweza kumsaidia ajifunze kumpenda Yehova,” Jessica anasema. Matokeo yalikuwa nini? Tutaona baadaye. Kwanza, acheni tuone jinsi ambavyo wengine wameingia katika mtego wa kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri.
Kwa Nini Wanafanya Urafiki Wao Uwe Siri?
Kwa nini wengine huanzisha urafiki wa siri? Kijana anayeitwa David anasema hivi waziwazi: “Wanajua kwamba wazazi wao hawatakubali, kwa hiyo hawawaambii.” Jane anaeleza sababu nyingine. Anasema: “Urafiki wa kimapenzi wa siri ni ishara ya uasi. Ukiona kwamba hutendewi kama mtu mzima, unaamua kufanya jambo lolote unalotaka bila kuwaambia wazazi wako.”
Je, unaweza kufikiria sababu nyingine zinazowafanya wengine wawe na urafiki wa kimapenzi wa siri? Ikiwa unajua, ziorodheshe hapa chini.
․․․․․
Bila shaka, unajua kwamba Biblia inakuagiza uwatii wazazi wako. (Waefeso 6:1) Na ikiwa wazazi wako wanaona kwamba hupaswi kuanzisha urafiki wa kimapenzi, bila shaka wana sababu nzuri. Hata hivyo, si ajabu ukiwa na maoni haya:
● Ninaona kwamba ninakosa kitu fulani kwa sababu kila mtu isipokuwa mimi ana mpenzi.
● Ninavutiwa na mtu ambaye si wa dini yangu.
● Ningependa kuwa na urafiki wa kimapenzi pamoja na Mkristo mwenzangu, hata ingawa sijafikia umri wa kufunga ndoa.
Huenda unajua maoni ya wazazi wako kuhusu taarifa zilizo juu. Nawe unajua moyoni kwamba wazazi wako wana haki ya kuwa na maoni hayo. Hata hivyo, huenda ukawa na maoni kama ya msichana anayeitwa Manami, anayesema: “Mkazo wa kuwa na urafiki wa kimapenzi ni wenye nguvu sana hivi kwamba nyakati nyingine mimi huwa na mashaka kuhusu msimamo wangu. Kwa maoni ya vijana wa leo, kutokuwa na mpenzi ni jambo lisilowazika. Isitoshe, hakuna raha yoyote maishani ukiwa peke yako!” Wengine walio katika hali kama hiyo wameanzisha urafiki wa kimapenzi na kuwaficha wazazi wao. Jinsi gani?
“Tuliambiwa Tusimwambie Yeyote”
Ili kuendeleza urafiki wa kimapenzi wa siri, udanganyifu fulani unahusika. Wengine wanadumisha urafiki wao ukiwa siri kwa kuwasiliana hasa kupitia simu au Intaneti. Wakiwa mbele ya watu wanaonekana kuwa marafiki tu, lakini barua-pepe, ujumbe mfupi wa simu, na mazungumzo yao kwenye simu yanaonyesha hali tofauti kabisa.
Njia nyingine ya ujanja ambayo vijana wanatumia ni kupanga tafrija huku wakiwa na lengo la kujitenga wakiwa wawili-wawili baadaye. James anasema hivi: “Siku moja tulialikwa mahali tukiwa kikundi, lakini baadaye tukagundua kwamba tafrija hiyo ilipangwa ili tu vijana fulani wawili waweze kuwa pamoja. Tuliambiwa tusimwambie yeyote.”
Kama James alivyosema, kwa kawaida marafiki husaidia kuendeleza urafiki huo ukiwa siri. Carol anasema: “Angalau rafiki mmoja hujua kinachoendelea lakini anaamua kunyamaza kwa sababu aliahidi kutomwambia yeyote.” Nyakati nyingine udanganyifu ulio wazi unahusika. Beth, mwenye umri wa miaka 17, anasema: “Wengi huendeleza urafiki wao wa siri kwa kuwadanganya wazazi wao kuhusu mahali ambapo wanaenda.” Misaki, mwenye umri wa miaka 19, alifanya hivyo. Anasema: “Ilinibidi nitunge hadithi za uwongo kwa makini. Nilikuwa mwangalifu nisiseme uwongo kuhusu mambo mengine isipokuwa tu yale yanayohusiana na urafiki wangu wa siri ili wazazi wangu waendelee kuniamini.”
Hatari za Urafiki wa Siri
Ukishawishiwa kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri, au ikiwa tayari umeanzisha urafiki wa aina hiyo, inafaa ujiulize maswali mawili yafuatayo:
Udanganyifu wangu utakuwa na matokeo gani? Je, unakusudia kufunga ndoa pamoja na mtu huyo hivi karibuni? Evan, mwenye umri wa miaka 20, anasema: “Mtu anayeanzisha urafiki wa kimapenzi bila kuwa na nia ya kufunga ndoa, ni kama mtu anayepeleka kitu fulani sokoni bila nia ya kukiuza.” Ni nini kinachoweza kutokea? Methali 13:12 inasema: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” Je, kwa kweli ungependa kumfanya mtu unayemjali augue moyoni? Unapaswa kufikiria jambo hili pia: Kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri kunakunyima mashauri yenye upendo kutoka kwa wazazi wako na watu wazima wengine wanaokujali. Kwa sababu hiyo kuna uwezekano mkubwa wa kutumbukia katika upotovu wa kingono.—Wagalatia 6:7.
Yehova Mungu ana maoni gani kuhusu yale ninayofanya? Biblia inasema: “Vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Waebrania 4:13) Kwa hiyo, ikiwa unaficha urafiki wako wa kimapenzi au wa rafiki yako, tayari Yehova anajua jambo hilo. Na ikiwa umedanganya, unapaswa kuhangaishwa na jambo hilo. Yehova Mungu anachukia sana udanganyifu. Kwa kweli, Biblia inataja waziwazi kwamba “ulimi wa uwongo” ni kati ya mambo ambayo anachukia!—Methali 6:16-19.
Kufunua Siri
Bila shaka ingekuwa vema uzungumze na wazazi wako au Mkristo mkomavu ikiwa una urafiki wowote wa siri. Na ikiwa una rafiki aliye na rafiki wa kimapenzi wa siri, usishiriki katika matendo yake kwa kumsaidia kuficha urafiki huo. (1 Timotheo 5:22) Ungehisi jinsi gani ikiwa urafiki huo ungesababisha madhara? Je, hungelaumika kwa kiasi fulani?
Tuseme rafiki yako ambaye ana ugonjwa wa kisukari anakula keki kwa siri. Utafanya nini ukijua jambo hilo lakini rafiki yako anakusihi usimwambie mtu yeyote? Utachukua hatua gani—utaficha jambo hilo au utachukua hatua ambayo inaweza kuokoa uhai wake?
Ndivyo ilivyo ikiwa unajua kwamba rafiki yako ana urafiki wa kimapenzi wa siri. Usiogope kwamba urafiki wenu utavunjika. Baada ya muda, rafiki wa kweli atatambua kwamba ulichukua hatua kwa sababu unamjali.—Zaburi 141:5.
Ni Siri au Ni Faragha?
Si siri zote zinazohusiana na urafiki wa kimapenzi zinazohusisha udanganyifu. Tuseme mwanamume kijana na mwanamke kijana wangependa kujuana vizuri zaidi lakini wanataka kufanya hivyo kwa siri kwa muda fulani. Labda kama kijana anayeitwa Thomas anavyosema, “hawataki kuulizwa-ulizwa maswali kama, ‘Mtafunga ndoa siku gani?’”
Mikazo kutoka kwa wengine inaweza kuwa hatari. (Wimbo wa Sulemani 2:7) Hivyo, mwanzoni mwa uhusiano, huenda kwa busara watu fulani wakaamua kutowajulisha wengine kuhusu urafiki wao. (Methali 10:19) Anna, mwenye umri wa miaka 20, anasema: “Hilo linawawezesha watu hao wawili kuwa na wakati wa kuamua ikiwa wanataka kuendeleza urafiki huo. Baada ya kufanya uamuzi huo, ndipo wanaweza kuwajulisha wengine.”
Wakati huohuo, haifai kuwaficha watu ambao wana haki ya kujua kuhusu urafiki huo, kama vile wazazi wako au wazazi wa rafiki yako. Ikiwa hutaki urafiki huo ujulikane, unapaswa kujiuliza ni kwa nini. Je, tayari umeona kwamba wazazi wako wana sababu ya kuukataa?
“Nilijua Hatua Ambayo Ninapaswa Kuchukua”
Jessica, aliyetajwa mwanzoni, alibadili maoni yake kuhusu kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri pamoja na Jeremy aliposikia kuhusu Mkristo mwingine ambaye alikuwa katika hali kama hiyo. “Baada ya kusikia jinsi Mkristo huyo alivyovunja urafiki huo,” Jessica anasema, “nilijua hatua ambayo ninapaswa kuchukua.” Je, ilikuwa rahisi kuvunja urafiki huo? Hapana! Jessica anasema: “Hakuna mvulana mwingine ambaye nimepata kumpenda kama nilivyompenda huyo. Nililia kila siku kwa majuma kadhaa.”
Hata hivyo, Jessica alijua kwamba anampenda Yehova. Na ingawa alikuwa amekengeushwa, alitaka sana kufanya lililo sawa. Baadaye, uchungu wa kuuvunja urafiki huo ulipungua. Jessica anasema: “Sasa uhusiano wangu pamoja na Yehova umekuwa mzuri sana kuliko wakati mwingine wowote. Ninashukuru sana kwamba anatupa mwongozo tunaohitaji kwa wakati unaofaa!”
Tuseme kwamba uko tayari kuanzisha urafiki wa kimapenzi na umempata mtu unayempenda. Unaweza kujua jinsi gani kwamba anakufaa?
MAANDIKO MUHIMU
“Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.
PENDEKEZO
Si lazima utangazie ulimwengu mzima kuhusu urafiki wenu. Lakini waambie wale walio na haki ya kujua. Kwa kawaida watu hao wanatia ndani wazazi wako na wazazi wa rafiki yako.
JE, WAJUA . . .?
Ili uwe na urafiki wenye kudumu ni lazima uwe mwenye kutumainika. Wazazi wako hawatakutumaini ikiwa una urafiki wa kimapenzi wa siri, na kufanya hivyo kunadhoofisha msingi wa uhusiano wako pamoja na rafiki yako.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ikiwa nina urafiki wa kimapenzi wa siri na Mkristo mwenzangu, nita ․․․․․
Ikiwa rafiki yangu ana urafiki wa kimapenzi wa siri nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Fikiria tena mambo matatu ambayo yameandikwa kwa herufi nzito katika ukurasa wa 22. Ni jambo gani kati ya mambo hayo linalofafanua jinsi unavyohisi nyakati fulani?
● Unaweza kushughulikia jinsi gani jambo hilo bila kuanzisha urafiki wa kimapenzi wa siri?
● Ikiwa ungejua kwamba rafiki yako ana urafiki wa kimapenzi wa siri, ungeshughulikia jambo hilo jinsi gani, na kwa nini ungechagua kulishughulikia hivyo?
[Blabu katika ukurasa wa 27]
“Nilivunja urafiki wa kimapenzi wa siri. Kusema kweli, haikuwa rahisi kwenda shuleni na kumwona mvulana huyo kila siku. Hata hivyo, Yehova Mungu anaona kila kitu, lakini sisi hatuwezi. Tunahitaji tu kumtegemea Yehova.’’—Jessica
[Picha katika ukurasa wa 25]
Kuficha urafiki wa kimapenzi wa rafiki yako ni kama kujua kwamba rafiki yako mwenye ugonjwa wa kisukari anakula keki lakini husemi
-
-
Je, Ananifaa?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 3
Je, Ananifaa?
Tafadhali jibu maswali yanayofuata:
Ni sifa gani ambazo sasa unaona kwamba yule atakayekuwa mwenzi wako wa ndoa anapaswa kuwa nazo? Katika orodha iliyo hapa chini tia alama hii ✔ kando ya sifa nne unazoona kuwa muhimu zaidi.
□ Mwenye sura nzuri □ Anayethamini mambo ya kiroho
□ Mwenye urafiki □ Mwenye kuaminika
□ Anayependwa na wengi □ Mwenye maadili mema
□ Mcheshi □ Anayeweka miradi na kuifikia
Ulipokuwa na umri mdogo, je, kuna wakati ulipohisi kwamba unampenda sana mtu fulani ambaye hakukuwa na matumaini yoyote ya kuwa na uhusiano naye? Katika orodha iliyo juu, tia alama hii × kando ya sifa ya mtu huyo iliyokuvutia zaidi wakati huo.
KATIKA sifa zote zilizoonyeshwa juu, hakuna yoyote iliyo mbaya. Kila moja inaweza kukuvutia. Hata hivyo, je, si kweli kwamba unapompenda mtu ambaye hakuna matumaini yoyote ya kuwa na uhusiano naye, ambaye hata hajui kwamba unampenda, unakazia fikira sifa za nje, kama zile zilizo upande wa kushoto?
Lakini unapoendelea kukomaa, unaanza kutumia utambuzi kuchunguza sifa za ndani, kama zile zilizo upande wa kulia. Kwa mfano, unaanza kutambua kwamba msichana anayevutia zaidi katika mtaa wenu hata si mwaminifu au mvulana anayependwa zaidi darasani hata hana maadili mema. Ikiwa umepita upeo wa ujana, inaelekea hutachunguza sifa za nje tu unapojibu swali hili, “Je, ananifaa?”
Kwanza Jifahamu
Kabla hujafikiria mtu anayekufaa, unahitaji kujifahamu vizuri. Ili kujichunguza zaidi, jibu maswali yanayofuata:
Nina sifa gani nzuri? ․․․․․
Nina udhaifu gani? ․․․․․
Nina mahitaji gani ya kihisia na ya kiroho? ․․․․․
Kujifahamu si kazi rahisi, lakini maswali kama hayo yaliyo hapo juu yanaweza kukusaidia. Kadiri unavyojifahamu, ndivyo utakavyoweza kupata mtu ambaye atakusaidia kuboresha sifa zako nzuri badala ya kuzidisha udhaifu wako.a Namna gani ikiwa unafikiri kwamba tayari umekwishampata mtu huyo?
Je, Yeyote Tu Anafaa?
“Ningependa tuwe marafiki!” Maneno hayo yanaweza kukushtua au kukusisimua—ikitegemea ni nani anayeyasema. Tuseme umekubali ombi hilo. Kadiri muda unavyopita, ni kwa njia gani unaweza kujua kama anakufaa?
Tuseme unataka kununua viatu vipya. Unaenda dukani na kuona viatu vinavyokupendeza. Unapima viatu hivyo kwa kuvivaa, lakini kwa kusikitisha, vinakubana sana. Utafanya nini? Je, utavinunua tu? Au utatafuta vingine? Bila shaka, jambo la hekima ni kuvirudisha na kutafuta vingine. Si jambo la busara hata kidogo kuvaa viatu ambavyo vinakubana!
Ndivyo ilivyo pia kuhusu kuchagua mwenzi wa ndoa. Kadiri muda unavyopita, utavutiwa na watu mbalimbali. Lakini si yeyote tu anayekufaa. Ukweli ni kwamba unahitaji mtu ambaye utafurahia kuwa pamoja naye—mtu ambaye utu wenu na miradi yenu inafaana. (Mwanzo 2:18; Mathayo 19:4-6) Je, umempata mtu kama huyo? Ikiwa umempata, unaweza kujua jinsi gani ikiwa anakufaa?
Kutoangalia Mambo Kijuujuu
Ili kujibu swali hilo, kwanza mtazame mwenzako pasipo upendeleo. Hata hivyo, uwe mwangalifu! Huenda ukaona tu mambo unayotaka kuona. Kwa hiyo, usiwe na haraka. Jaribu kutambua jinsi rafiki yako alivyo kikweli. Jitihada zinahitajika. Na hilo halipaswi kukushangaza. Kwa mfano: Wazia kwamba unataka kununua gari. Utalichunguza kadiri gani? Je, utatosheka tu na sura ya nje? Je, halingekuwa jambo la busara kulichunguza kwa undani zaidi—labda kujitahidi kujua mengi iwezekanavyo kuhusu hali ya injini yake?
Kutafuta mwenzi ni jambo zito zaidi kuliko kuchagua gari la kununua. Hata hivyo, wengi wanaoanzisha urafiki wa kimapenzi hawachunguzi mambo kwa undani. Badala yake, wao hutaja tu mambo yanayowapendeza wote wawili: ‘Tunapenda muziki uleule.’ ‘Tunapendezwa na mambo yaleyale.’ ‘Tunakubaliana katika kila jambo!’ Hata hivyo, kama ilivyotajwa awali, ikiwa kwa kweli umepita upeo wa ujana, hutachunguza mambo kijuujuu tu. Unahitaji kumtambua “yule mtu wa siri wa moyoni.”—1 Petro 3:4; Waefeso 3:16.
Kwa mfano, badala ya kukazia fikira mambo mnayokubaliana, huenda mkapata kujuana hata zaidi kwa kuona inavyotokea mnapokosa kukubaliana. Kwa maneno mengine, anatenda jinsi gani kutoelewana kunapotokea? Je, anasisitiza maoni yake? Je, ‘analipuka kwa hasira’ na kuanza ‘kutukana’? (Wagalatia 5:19, 20; Wakolosai 3:8) Au anaonyesha usawaziko, kwa kukubali mambo ili kuwe na amani wakati ambapo hakuna kanuni yoyote inayovunjwa?—Yakobo 3:17.
Jambo lingine unalopaswa kufikiria ni: Je, mtu huyo anapenda kukusukuma ufanye mambo anayotaka, kukutawala, au ni mwenye wivu? Je, anadai umwambie kila kitu unachofanya? Msichana mmoja anayeitwa Nicole anasema hivi: “Mimi husikia kuhusu watu wenye urafiki wa kimapenzi wanaozozana kwa sababu mmoja wao amekasirika kwa kuwa mwenzake hampigii simu na kumweleza mahali alipo. Kwa maoni yangu, hiyo ni dalili ya matatizo.”—1 Wakorintho 13:4.
Mambo kama hayo ambayo yametajwa yanakazia fikira utu na mwenendo. Hata hivyo, ni muhimu pia kujua sifa za rafiki yako. Wengine wana maoni gani kumhusu? Ingefaa kuzungumza na watu ambao wamemfahamu kwa muda fulani, kama vile watu wakomavu kutanikoni. Kwa njia hiyo utajua ikiwa ‘anashuhudiwa vema.’—Matendo 16:1, 2.
Kuandika maoni yako kuhusu rafiki yako katika mambo yafuatayo, kwa kutegemea habari ambazo tumezungumzia kufikia sasa, kunaweza kukusaidia kumfahamu vizuri zaidi.
Utu ․․․․․
Mwenendo ․․․․․
Sifa ․․․․․
Pia utafaidika kwa kuchunguza sanduku lenye kichwa “Je, Atakuwa Mume Anayenifaa?” katika ukurasa wa 39 au “Je, Atakuwa Mke Anayenifaa?” katika ukurasa wa 40. Maswali yaliyo humo yatakusaidia kujua ikiwa rafiki yako atakuwa mwenzi wa ndoa anayekufaa.
Namna gani ikiwa baada ya kufikiria kwa uzito, unaona kwamba huenda mtu huyo asikufae? Ikiwa ndivyo, basi una uamuzi mzito wa kufanya:
Je, Tuvunje Urafiki Wetu?
Nyakati nyingine, kuna faida kuvunja urafiki. Fikiria kisa cha Jill. Anasema, “Mwanzoni nilifurahi kwamba mpenzi wangu alikuwa akitaka kujua niko wapi, ninafanya nini, na niko na nani. Lakini ilifikia hatua ya kwamba singeweza kuwa na mtu mwingine yeyote isipokuwa yeye. Hata aliona wivu nilipokuwa pamoja na watu wa familia yetu—hasa baba yangu. Nilipovunja uhusiano huo, nilihisi kana kwamba nimetua mzigo mzito sana!”
Sarah alikuwa pia katika hali kama hiyo. Alianza kutambua kwamba John ni mwenye dhihaka, mwenye kudai mno, na asiye na heshima. Sarah anakumbuka hivi: “Siku moja alikuja kwetu akiwa amechelewa kwa saa tatu! Alimpuuza mama yangu aliyemfungulia mlango, kisha akasema: ‘Twende. Tumechelewa.’ Si kwamba yeye amechelewa, bali ‘Tumechelewa.’ Alipaswa kuomba msamaha au kueleza sababu ya kuchelewa. Isitoshe, alipaswa kumwonyesha heshima mama yangu!” Ni kweli kwamba kisa kimoja chenye kuvunja moyo au tabia fulani isiyopendeza haimaanishi kwamba urafiki wenu hautadumu. (Zaburi 130:3) Hata hivyo, Sarah alipotambua kwamba John alikuwa na mazoea ya kukosa heshima, aliamua kuuvunja urafiki wao.
Kama ilivyokuwa katika visa vya Jill na Sarah, ungefanya nini ukitambua kwamba mpenzi wako hastahili kuwa mwenzi wako wa ndoa? Ikiwa ndivyo ilivyo, usipuuze hisia zako! Ijapokuwa ni vigumu kukubali ukweli wa mambo, huenda ikafaa kuvunja urafiki huo. Andiko la Methali 22:3 linasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” Kwa mfano, ikiwa rafiki yako anaonyesha dalili moja au zaidi kati ya zile zilizo katika ukurasa wa 39 na 40 huenda ikafaa kuvunja urafiki huo—angalau mpaka tatizo lenyewe lirekebishwe. Ni kweli, huenda isiwe rahisi kuvunja urafiki. Lakini ndoa ni muungano wa kudumu. Afadhali kuumia kwa muda mfupi sasa kuliko kujuta maisha yako yote baadaye!
Kumjulisha Uamuzi Wako
Unaweza kuuvunja urafiki wenu jinsi gani? Kwanza, chagua kikao kinachofaa. Ni kikao gani kinachofaa? Fikiria jinsi ambavyo wewe mwenyewe ungependa kutendewa katika hali kama hiyo. (Mathayo 7:12) Je, ungependa kujulishwa uamuzi huo mbele ya watu? Sivyo. Isipokuwa iwe lazima, haingefaa kuvunja urafiki huo kwa kuacha ujumbe kwenye mashini ya kujibu simu, kutuma ujumbe mfupi kwenye simu, au kupitia barua-pepe. Badala yake, chagua mahali na wakati unaofaa ili kuzungumzia jambo hilo zito.
Unapaswa kusema nini? Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo ‘wasemezane kweli.’ (Waefeso 4:25) Hivyo, njia bora ni kutumia busara na kuwa thabiti. Sema waziwazi kwa nini unahisi kwamba urafiki huo hautadumu. Huhitaji kutaja orodha ndefu ya makosa au kumshambulia kwa mashtaka. Badala ya kusema, “Wewe hufanyi” hili au lile au “Hujapata kamwe” kufanya hivi au vile, afadhali kutumia maneno yanayoonyesha hisia zako kama vile, “Mimi ninahitaji mtu ambaye . . . ” au “Mimi ninaona kwamba hatuwezi kuendelea kuwa marafiki kwa sababu . . . ”
Huo si wakati wa kuyumba-yumba au kushawishiwa ubadili maoni yako. Kumbuka kwamba kuna sababu nzito ambazo zimekusukuma ufikie uamuzi wa kuvunja urafiki huo. Kwa hiyo uwe mwangalifu rafiki yako akijaribu kutumia ujanja kubadili maoni yako. “Nilipovunja urafiki wetu,” anasema msichana mmoja anayeitwa Lori, “mvulana niliyekuwa na urafiki naye alianza kujifanya kwamba ana huzuni kila wakati. Nafikiri alifanya hivyo ili nimhurumie. Nilimsikitikia. Lakini sikuruhusu jambo hilo libadili uamuzi wangu.” Kama Lori, uwe na hakika kuhusu unachotaka. Shikamana na uamuzi wako. Acha siyo yako imaanishe siyo.—Yakobo 5:12.
Matokeo ya Kuvunja Urafiki Huo
Usishangae ukihuzunika sana kwa muda fulani baada ya kuvunja urafiki huo. Huenda hata ukahisi kama mtunga-zaburi aliyesema: “Nimeingiwa na wasiwasi, nimeinama kupita kiasi; nimetembea huku na huku kwa huzuni mchana kutwa.” (Zaburi 38:6) Huenda marafiki wenye nia nzuri wakajaribu kukusaidia kwa kukutia moyo uanzishe tena urafiki huo. Uwe mwangalifu! Wewe ndiwe utakayeathiriwa na matokeo ya uamuzi wako, si marafiki hao. Kwa hiyo, usiogope kuwa imara—hata ingawa huenda ukahuzunishwa na yaliyotokea.
Uwe na hakika kwamba muda si muda huzuni yako itatoweka. Kwa sasa, unaweza kuchukua hatua zinazofaa, kama zile zifuatazo, ili kushughulikia hali hiyo.
Mweleze mtu unayemwamini jinsi unavyohisi.b (Methali 15:22) Sali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. (Zaburi 55:22) Jishughulishe na mambo mengine. (1 Wakorintho 15:58) Usijitenge na watu! (Methali 18:1) Bila kukawia, anza kushirikiana na watu ambao watakujenga. Jitahidi kufikiria mambo ambayo yanajenga.—Wafilipi 4:8.
Baada ya muda, huenda ukapata rafiki mwingine. Na utakapofanya hivyo utakuwa na maoni yenye usawaziko zaidi. Huenda wakati huo jibu lako kwa swali hili “Je, ananifaa?” litakuwa ndiyo!
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 31
Ikiwa tayari mna urafiki wa kimapenzi, ni mipaka gani mnayoweza kuweka kuhusiana na kuonyeshana mahaba?
[Maelezo ya Chini]
a Unaweza kujifunza hata zaidi juu yako mwenyewe kwa kuchunguza maswali katika Sura ya 1 chini ya kichwa kidogo “Je, Uko Tayari Kufunga Ndoa?”
b Wazazi wako au watu wazima wengine kama vile wazee Wakristo wanaweza kukusaidia. Huenda hata ukagundua kwamba wao pia walipatwa na hali kama hiyo walipokuwa vijana.
MAANDIKO MUHIMU
“Kwa matendo yake, mvulana hujitambulisha kama utendaji wake ni safi na mnyoofu.” —Methali 20:11.
PENDEKEZO
Fanyeni pamoja mambo yanayofunua sifa za mtu:
● Jifunzeni Neno la Mungu pamoja.
● Chunguzaneni mnapokuwa katika mikutano ya kutaniko na katika huduma.
● Shirikini katika kusafisha Jumba la Ufalme na katika miradi ya ujenzi.
JE, WAJUA . . .?
Uchunguzi mbalimbali unaonyesha kwamba ndoa kati ya watu wa dini tofauti mara nyingi huishia kwenye talaka.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Nikivutiwa na mtu asiye mwamini, nita ․․․․․
Nikitaka kujua sifa za mtu ambaye nina urafiki wa kimapenzi naye, ninaweza ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Ni sifa gani nzuri ulizo nazo zinazoweza kufanya ndoa yenu ifanikiwe?
● Ni sifa gani muhimu ambazo ungependa mwenzi wako wa ndoa awe nazo?
● Ni matatizo gani yanayoweza kutokea ukifunga ndoa na mtu wa dini nyingine?
● Unaweza kujua jinsi gani utu, tabia, na sifa ya mtu ambaye una urafiki wa kimapenzi naye?
[Blabu katika ukurasa wa 37]
“Jinsi rafiki yako anavyowatendea watu wa familia yao, ndivyo atakavyokutendea.’’—Tony
[Sanduku katika ukurasa wa 34]
“Msifungwe Nira Isivyo Sawa”
“Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” Huenda unakubaliana na kanuni hiyo ya Biblia, inayopatikana katika 2 Wakorintho 6:14. Hata hivyo, huenda bado ukavutiwa na mtu asiye mwamini. Kwa nini? Labda unavutiwa na sura yake tu. Mvulana anayeitwa Mark anasema: “Kuna msichana niliyekuwa nikimwona kila siku wakati wa mazoezi. Kila mara alihakikisha kwamba amekuja kuzungumza nami. Haikuwa vigumu kuanzisha urafiki naye.”
Ikiwa unajijua vizuri na unasadiki kwamba viwango vya maadili unavyofuata vinafaa—na ikiwa una ukomavu wa kutosha kutotawaliwa na hisia zako—basi unajua jambo unalopaswa kufanya. Kwa kweli, mtu huyo—hata awe mwenye kuvutia jinsi gani, hata awe mwenye kupendeza namna gani, au hata aonekane kuwa na sifa nzuri kadiri gani—hatakusaidia kuboresha urafiki wako na Mungu.—Yakobo 4:4.
Bila shaka, ikiwa tayari urafiki wa kimapenzi umeanza, haitakuwa rahisi kuuvunja. Ndivyo msichana mmoja anayeitwa Cindy alivyogundua. Anasema: “Nililia kila siku. Nilimfikiria mvulana huyo nyakati zote, hata wakati wa mikutano ya Kikristo. Nilimpenda sana hivi kwamba nilihisi afadhali nife kuliko kumwacha.” Hata hivyo, muda si muda, Cindy alifuata shauri lenye hekima la mama yake kuhusu kutokuwa na urafiki wa kimapenzi na mtu asiye mwamini. Anasema: “Ni vizuri kwamba niliuvunja urafiki huo. Nina hakika kabisa kwamba Yehova atanitimizia mahitaji yangu.”
Je, uko katika hali kama ya Cindy? Ikiwa ndivyo, si lazima ung’ang’ane ukiwa peke yako! Unaweza kuzungumza na wazazi wako. Ndivyo Jim alivyofanya alipojikuta akivutiwa na msichana fulani shuleni. Anasema: “Mwishowe niliwaomba wazazi wangu wanisaidie. Kufanya hivyo kulinisaidia sana kushinda hisia zangu.” Wazee wa kutaniko wanaweza kukusaidia pia. Usiogope kuzungumza na mmoja wao kuhusu mambo unayokabili?—Isaya 32:1, 2.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 39]
Ukurasa wa Mazoezi
Je, Atakuwa Mume Anayenifaa?
Sifa za Msingi
□ Anatumia jinsi gani mamlaka yoyote aliyo nayo?—Mathayo 20:25, 26.
□ Ana miradi gani?—1 Timotheo 4:15.
□ Je, sasa anajitahidi kufikia miradi hiyo?—1 Wakorintho 9:26, 27.
□ Anawatendea jinsi gani watu wa familia yao?—Kutoka 20:12.
□ Rafiki zake ni nani?—Methali 13:20.
□ Anapenda kuzungumza juu ya nini?—Luka 6:45.
□ Ana maoni gani kuhusu pesa?—Waebrania 13:5, 6.
□ Anapenda kujiburudisha na mambo gani?—Zaburi 97:10.
□ Anaonyesha namna gani kwamba anampenda Yehova?—1 Yohana 5:3.
Sifa zenye Manufaa
□ Je, ana bidii?—Methali 6:9-11.
□ Je, ana usawaziko kuhusu matumizi ya pesa?—Luka 14:28.
□ Je, anashuhudiwa vema?—Matendo 16:1, 2.
□ Je, anawajali wengine?—Wafilipi 2:4.
Dalili za Matatizo
□ Je, anakasirika upesi?—Methali 22:24.
□ Je, anajaribu kukushawishi ushiriki katika mwenendo mpotovu kingono?—Wagalatia 5:19.
□ Je, anapenda kupigana au kuwatusi wengine?—Waefeso 4:31.
□ Je, ni lazima anywe pombe ili awe na furaha?—Methali 20:1.
□ Je, ni mtu mwenye wivu, anayejifikiria mwenyewe tu? —1 Wakorintho 13:4, 5.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 40]
Ukurasa wa Mazoezi
Je, Atakuwa Mke Anayenifaa?
Sifa za Msingi
□ Anaonyesha jinsi gani ujitiisho katika familia na kutanikoni?—Waefeso 5:21, 22.
□ Anawatendea jinsi gani watu wa familia yao?—Kutoka 20:12.
□ Rafiki zake ni nani?—Methali 13:20.
□ Anapenda kuzungumza juu ya nini?—Luka 6:45.
□ Ana maoni gani kuhusu pesa?—1 Yohana 2:15-17.
□ Ana miradi gani?—1 Timotheo 4:15.
□ Je, sasa anajitahidi kufikia miradi hiyo?—1 Wakorintho 9:26, 27.
□ Anapenda kujiburudisha na mambo gani?—Zaburi 97:10.
□ Anaonyesha namna gani kwamba anampenda Yehova?—1 Yohana 5:3.
Sifa zenye Manufaa
□ Je, ana bidii?—Methali 31:17, 19, 21, 22, 27.
□ Je, ana usawaziko kuhusu matumizi ya pesa?—Methali 31:16, 18.
□ Je, anaripotiwa vema?—Ruthu 3:11.
□ Je, anawajali wengine?—Methali 31:20.
Dalili za Matatizo
□ Je, ni mgomvi?—Methali 21:19.
□ Je, anajaribu kukushawishi ushiriki katika mwenendo mpotovu kingono?—Wagalatia 5:19.
□ Je, anapenda kupigana au kuwatusi wengine? —Waefeso 4:31.
□ Je, lazima anywe pombe ili awe na furaha?—Methali 20:1.
□ Je, ni mtu mwenye wivu, anayejifikiria mwenyewe tu?—1 Wakorintho 13:4, 5.
[Picha katika ukurasa wa 30]
Si kiatu chochote tu kinachoweza kukutosha; vivyo hivyo si mtu yeyote tu atakayekufaa
[Picha katika ukurasa wa 31]
Unapochagua gari, je, unafikiri ni muhimu kulichunguza kwa undani badala ya kuangalia sura yake ya nje tu? Hivyo basi unahitaji kuwa mwangalifu hata zaidi unapochagua mwenzi wa ndoa!
-
-
Ni Wakati Gani Ambapo Mtu Anakuwa Amepita Mipaka?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 4
Ni Wakati Gani Ambapo Mtu Anakuwa Amepita Mipaka?
Kweli au si kweli . . .
Ni kosa kwa watu wawili walio na urafiki wa kimapenzi kushikana katika hali yoyote ile.
□ Kweli
□ Si kweli
Watu wawili wanaweza kuwa na hatia ya uasherati hata ikiwa hawajafanya ngono.
□ Kweli
□ Si kweli
Wapenzi wasipofanya mambo kama vile kubusiana na kukumbatiana, basi hawapendani kikweli.
□ Kweli
□ Si kweli
HAPANA shaka umefikiria jambo hilo sana. Kwa kweli, ikiwa uko katika urafiki wa kimapenzi, inaweza kuwa vigumu kujua mipaka ambayo unapaswa kuweka kuhusu kuonyeshana mahaba. Acheni tuzungumzie taarifa tatu zilizo juu na tuone jinsi Neno la Mungu linavyotusaidia kujibu swali hili, “Ni wakati gani ambapo mtu anakuwa amepita mipaka?”
● Ni kosa kwa watu wawili walio na urafiki wa kimapenzi kushikana katika hali yoyote ile.
Si kweli. Biblia haikatazi kuonyeshana mahaba kwa njia iliyo safi. Kwa mfano, Biblia inazungumzia kisa cha msichana Mshulami na mvulana mchungaji waliopendana. Uchumba wao ulikuwa safi. Hata hivyo, inaonekana kwamba walionyeshana mahaba kwa njia fulani kabla ya kufunga ndoa. (Wimbo wa Sulemani 1:2; 2:6; 8:5) Leo watu wawili wanaofikiria kwa uzito kufunga ndoa wanaweza kuhisi kwamba hakuna ubaya kuonyeshana mahaba katika njia fulani safi.a
Hata hivyo, watu wawili wenye urafiki wa kimapenzi wanapaswa kuwa waangalifu sana. Kubusiana, kukumbatiana, au kufanya jambo lolote linaloamsha tamaa ya ngono kunaweza kuongoza katika mwenendo mpotovu kingono. Ni rahisi sana hata kwa watu wawili ambao hawana nia mbaya kupoteza usawaziko na kutumbukia katika upotovu wa kingono.—Wakolosai 3:5.
● Watu wawili wanaweza kuwa na hatia ya uasherati hata ikiwa hawajafanya ngono.
Kweli. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “uasherati” (por·neiʹa) lina maana pana. Linatia ndani mahusiano yote ya ngono nje ya ndoa na linakazia matumizi yasiyofaa ya viungo vya uzazi. Hivyo, zaidi ya kufanya ngono, uasherati unatia ndani matendo kama vile kumpiga mtu mwingine punyeto, iwe ni mwanamume au mwanamke, na pia ngono ya kinywa na ulawiti au ufiraji.
Isitoshe, zaidi ya kushutumu uasherati, Biblia inashutumu mambo mengine pia. Mtume Paulo aliandika: “Matendo ya mwili ni wazi, nayo ni uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu.” Kisha akaongeza: “Wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”—Wagalatia 5:19-21.
“Uchafu,” au “ukosefu wa usafi,” ni nini? Neno la Kigiriki linatia ndani uchafu wa kila namna, iwe ni katika maneno au matendo. Kwa kweli, ni tendo chafu kuingiza mikono ndani ya nguo za mtu, kumvua mtu nguo, au kumpapasa-papasa mtu sehemu za siri, kama vile matiti. Katika Biblia kuyapapasa matiti kunahusianishwa na shangwe inayopaswa kufurahiwa tu na watu wawili waliofunga ndoa.—Methali 5:18, 19.
Vijana fulani wanakaidi viwango vya Mungu. Wanapita mipaka kimakusudi, au wanatafuta kwa pupa watu mbalimbali wanaoweza kushiriki pamoja nao uchafu wa kingono. Vijana hao wanaweza kuwa na hatia ya kile ambacho mtume Paulo alikiita “mwenendo mpotovu.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mwenendo mpotovu” linamaanisha ‘matendo ya kupita kiasi, ya kupindukia, ufidhuli, uchu usiozuilika.’ Bila shaka hungependa kufikia hatua ya “kuishiwa na ufahamu wote” kwa kujitoa mwenyewe ili kuwa na “mwenendo mpotovu na kufanya ukosefu wa usafi wa kila namna kwa pupa.”—Waefeso 4:17-19.
● Wapenzi wasipofanya mambo kama vile kubusiana na kukumbatiana, basi hawapendani kikweli.
Si kweli. Tofauti na maoni ya watu fulani, kufanya mambo kama vile kubusiana na kukumbatiana hakuzidishi urafiki. Badala yake, kunafanya watu wasiheshimiane wala kuaminiana. Fikiria kisa cha Laura. “Siku moja wakati mama yangu hakuwapo, mpenzi wangu alikuja nyumbani eti ili kutazama televisheni,” anasema. “Mwanzoni alinishika mkono tu. Kisha, akaanza kunipapasa-papasa. Niliogopa kumwambia aache; nilidhani kwamba atakasirika na kuondoka.”
Una maoni gani? Je, mpenzi wa Laura alimjali kikweli, au alitaka tu kutosheleza tamaa yake? Je, mtu anayejaribu kukuingiza katika mwenendo mchafu anakupenda kweli?
Mvulana anapomchochea msichana kukaidi mazoezi yake ya Kikristo na dhamiri yake, anavunja sheria ya Mungu na hapaswi kudai kwamba anampenda msichana huyo kikweli. Vilevile, msichana anayekubali, anajiachilia atumiwe vibaya. Zaidi ya yote, msichana huyo ameshiriki tendo chafu—pengine hata uasherati.b—1 Wakorintho 6:9, 10.
Weka Mipaka Iliyo Wazi
Ikiwa mna urafiki wa kimapenzi, mnaweza kufanya nini ili mwepuke kuonyeshana mahaba kwa njia zisizofaa? Njia ya hekima ni kuweka mipaka iliyo wazi mapema. Andiko la Methali 13:10 linasema: “Wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.” Hivyo, zungumza na mpenzi wako kuhusu njia zinazofaa za kuonyeshana mahaba. Kujaribu kuweka mipaka baada ya tamaa kuwaka ni kama kuweka king’ora cha moto katika nyumba baada ya nyumba hiyo kushika moto.
Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kuzungumzia mambo hayo—hata linaweza kuwa jambo lenye kuaibisha—hasa mwanzoni mwa uchumba. Lakini kuweka mipaka kunaweza kusaidia sana kuzuia matatizo makubwa yasitokee baadaye. Mipaka inayowekwa kwa hekima ni kama vifaa vya kutambua moshi ambavyo vinawasha king’ora mara tu vinapotambua dalili ya moto. Isitoshe, kufaulu kwenu kuzungumzia mambo hayo kunaweza kuonyesha pia ikiwa urafiki wenu utafanikiwa. Kwa hakika, kujizuia, subira, na kutokuwa na ubinafsi ndio msingi wa mahusiano mazuri ya ngono katika ndoa.—1 Wakorintho 7:3, 4.
Kusema kweli, kushikamana na viwango vya Mungu si rahisi. Lakini unaweza kutegemea mashauri ya Yehova. Katika Isaya 48:17, Yehova anasema kwamba yeye ndiye “Anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake.” Yehova anakutakia kila la heri!
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 24
Kuwa bikira si kasoro. Badala yake, kutunza ubikira ndilo jambo la hekima. Pata kujua ni kwa nini.
[Maelezo ya Chini]
a Katika sehemu fulani za ulimwengu, watu ambao hawajafunga ndoa wanapoonyeshana mahaba mbele ya watu, hilo huonwa kuwa jambo lisilofaa na lenye kuchukiza. Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu wasijiendeshe kwa njia inayoweza kuwakwaza wengine.—2 Wakorintho 6:3.
b Bila shaka, mambo yanayozungumziwa katika fungu hili yanawahusu watu wa jinsia zote.
MAANDIKO MUHIMU
“Upendo . . . haujiendeshi bila adabu.”—1 Wakorintho 13:4, 5.
PENDEKEZO
Fanyeni mambo mkiwa pamoja na wengine, au usisitize kuwe na mtu wa tatu. Epukeni hali hatari, kama vile kuwa peke yenu katika gari lililoegeshwa au katika nyumba au chumba.
JE, WAJUA . . .?
Ikiwa mnachumbiana, mnahitaji kuzungumzia mambo fulani ya siri. Lakini kuzungumzia mambo waziwazi mkiwa na kusudi la kuamsha tamaa ya ngono ni mojawapo ya mambo machafu —hata mambo hayo yakizungumziwa kupitia simu au ujumbe mfupi.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ninaweza kuepuka kushawishiwa kutumbukia katika mwenendo usiofaa kwa ․․․․․
Mpenzi wangu akijaribu kunishawishi nishiriki katika mwenendo mchafu, nita ․․․․․
Maswali ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu jambo hili ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Ni mipaka gani ambayo unaweza kuweka kuhusu kuonyeshana mahaba na mtu wa jinsia tofauti?
● Eleza tofauti kati ya uasherati, uchafu, na mwenendo mpotovu.
[Blabu katika ukurasa wa 46]
Mimi na mchumba wangu tumesoma pamoja makala za Biblia zinazozungumzia jinsi ya kuendelea kuwa safi kiadili. Tunathamini jinsi ambavyo zimetusaidia kuendelea kuwa na dhamiri safi.’’—Leticia
[Sanduku katika ukurasa wa 44]
Namna Gani Ikiwa Tumepita Mipaka?
Namna gani ikiwa umetumbukia katika mwenendo usiofaa? Usijidanganye kwa kufikiri kwamba unaweza kutatua tatizo hilo mwenyewe. Kijana mmoja alisema: “Nyakati nyingine ningesali hivi, ‘Tusaidie tusifanye hivyo tena.’ Nyakati nyingine kufanya hivyo kulisaidia, lakini nyakati fulani hakukusaidia.” Hivyo, zungumza na wazazi wako. Pia, Biblia inatoa shauri hili zuri: ‘Waite wanaume wazee wa kutaniko.’ (Yakobo 5:14) Wachungaji hao Wakristo wanaweza kukupa mashauri na karipio ili urekebishe uhusiano wako pamoja na Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 47]
Je, ungeweka king’ora cha moto katika nyumba baada ya nyumba hiyo kushika moto? Basi msingoje mpaka wakati ambapo tamaa zenu zimewaka ndipo mjaribu kuweka mipaka kuhusu kuonyeshana mahaba
-
-
Kwa Nini Uendelee Kuwa Bikira?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 5
Kwa Nini Uendelee Kuwa Bikira?
“Kuna mkazo mwingi wa kufanya ngono.”—Kelly.
“Ninahisi kana kwamba nina kasoro kwa kuwa bado mimi ni bikira.”—Jordon.
“BADO wewe ni bikira?” Swali hilo linaweza kukushtua! Katika sehemu nyingi, kijana ambaye bado ni bikira anaweza kuonwa kuwa mtu wa ajabu au mwenye kasoro. Ndiyo sababu vijana wengi wanafanya ngono mapema maishani!
Kuvutwa na Tamaa, Kusukumwa na Marika
Ikiwa wewe ni Mkristo, unajua kwamba Biblia inakuambia ‘ujiepushe na uasherati.’ (1 Wathesalonike 4:3) Hata hivyo, huenda ikawa vigumu kwako kudhibiti tamaa zako za ngono. Kijana mmoja anayeitwa Paul anakiri hivi: “Nyakati nyingine, mimi huanza tu kufikiri kuhusu ngono bila sababu yoyote hususa.”
Uwe na hakika kwamba hizo ni hisia za kawaida. Hata hivyo, kudhihakiwa na kusumbuliwa sikuzote kwa sababu ya kuwa bikira si jambo la kupendeza! Kwa mfano, namna gani marafiki wako wakikwambia kwamba wewe si mwanamume au mwanamke halisi ikiwa hujafanya ngono? “Marafiki huzungumzia ngono kana kwamba ni raha tupu na jambo la kawaida,” Ellen anasema. “Ikiwa hujihusishi na ngono unaonwa kuwa mshamba.”
Lakini huenda marafiki wako wasikuambie matokeo ya kufanya ngono kabla ya ndoa. Kwa mfano, Maria ambaye alifanya ngono na mvulana aliyekuwa rafiki yake anakumbuka: “Baadaye nilifedheheka na kuona aibu. Nilijichukia na kumchukia mvulana huyo.” Hali kama hizo hutokea mara nyingi kuliko vijana wengi wanavyofikiri. Ukweli ni kwamba, kufanya ngono kabla ya ndoa mara nyingi hutokeza maumivu ya kihisia na madhara makubwa!
Hata hivyo, msichana anayeitwa Shanda anauliza, “Kwa nini Mungu aliwapa vijana tamaa za ngono akijua kwamba hawapaswi kuzitosheleza kabla ya ndoa?” Hilo ni swali zuri. Lakini fikiria mambo yafuatayo:
Je, tamaa za ngono tu ndizo hisia zenye nguvu unazopata? Hapana. Yehova Mungu alikuumba na uwezo wa kuwa na tamaa na hisia nyingi mbalimbali.
Je, ni lazima utosheleze kila tamaa mara tu inapotokea? Hapana, kwa sababu Mungu alikupa pia uwezo wa kudhibiti matendo yako.
Basi, tuseme nini? Huenda huwezi kuzuia tamaa fulani zisitokee, lakini unaweza kudhibiti matendo yako. Kwa hakika, kutosheleza tamaa yako ya ngono kila mara inapotokea ni kosa na ni kutotumia akili sawa tu na kumpiga mtu kila mara unapokuwa na hasira.
Ukweli ni kwamba Mungu hakukusudia tutumie vibaya nguvu zetu za uzazi. Biblia inasema: “Kila mmoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe [au, mwili wake mwenyewe] katika utakaso na heshima.” (1 Wathesalonike 4:4) Kama vile kuna “wakati wa kupenda na wakati wa kuchukia,” vivyo hivyo kuna wakati wa kutosheleza tamaa za ngono na wakati wa kuepuka kufanya hivyo. (Mhubiri 3:1-8) Vyovyote vile, wewe tu ndiwe unayeweza kudhibiti tamaa zako!
Lakini namna gani mtu akikudhihaki kwa kusema hivi kwa mshangao, “Eti bado wewe ni bikira?” Usiogope. Ikiwa mtu huyo anataka tu kukuaibisha, unaweza kusema: “Ndiyo, bado mimi ni bikira, na ninafurahia jambo hilo.” Au unaweza kusema, “Hilo ni jambo la kibinafsi ambalo silizungumzii na wengine.”a (Methali 26:4; Wakolosai 4:6) Kwa upande mwingine, huenda ukahisi kwamba mtu anayekuuliza swali hilo anahitaji kujua zaidi. Hivyo, unaweza kuamua kumweleza msimamo wako unaotegemea Biblia.
Je, unaweza kufikiria njia nyingine za kujibu unapoulizwa hivi kwa dhihaka “Eti bado wewe ni bikira?” Ikiwa ndivyo, andika majibu hayo hapa chini.
․․․․․
Zawadi Yenye Thamani
Mungu anahisi jinsi gani watu wanapofanya ngono kabla ya ndoa? Wazia kwamba umemnunulia rafiki yako zawadi. Lakini kabla hata hujampa zawadi hiyo, anaifungua kwa sababu ya udadisi! Ungeudhika, sivyo? Wazia basi jinsi ambavyo Mungu angehisi ikiwa ungefanya ngono kabla ya ndoa. Anataka ungoje mpaka utakapofunga ndoa ili ufurahie zawadi ya ngono.—Mwanzo 1:28.
Unapaswa kufanya nini kuhusu hisia zako za ngono? Jizoeze kuzidhibiti. Inawezekana! Mwombe Yehova akusaidie. Roho yake inaweza kuzidisha uwezo wako wa kujizuia. (Wagalatia 5:22, 23) Kumbuka kwamba Yehova “hatawanyima jambo lolote jema wale wanaotembea bila kosa.” (Zaburi 84:11) Kijana mmoja anayeitwa Gordon anasema: “Ninapoanza kufikiria kwamba hakuna ubaya wowote wa kufanya ngono kabla ya ndoa, ninakumbuka hatari za kiroho na kutambua kwamba uhusiano wangu na Yehova ni wenye thamani sana hivi kwamba siwezi kuruhusu uharibiwe na dhambi yoyote ile.”
Ukweli ni kwamba kuwa bikira si jambo la kushangaza wala haimaanishi kwamba una kasoro. Kwa upande mwingine, upotovu katika ngono unasababisha aibu, kuvunjika moyo, na madhara mengine. Kwa hiyo, usiruhusu propaganda ya ulimwengu ikudanganye kufikiri kwamba una kasoro ukishikamana na viwango vya Biblia. Kwa kutunza ubikira wako, unatunza afya yako, hisia zako, na zaidi ya yote, uhusiano wako pamoja na Mungu.
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 24
[Maelezo ya Chini]
a Wakati mmoja, Yesu aliamua kunyamaza Herode alipomuuliza maswali. (Luka 23:8, 9) Mara nyingi hakuna haja ya kujibu maswali ya upuuzi.
MAANDIKO MUHIMU
“Ikiwa yeyote . . . amefanya uamuzi huu katika moyo wake mwenyewe, kutunza ubikira wake mwenyewe, yeye atafanya vema.”—1 Wakorintho 7:37.
PENDEKEZO
Epuka kushirikiana na watu ambao hawafuati viwango vya juu vya maadili, hata wakidai kwamba wana imani kama yako.
JE, WAJUA . . .?
Ni vigumu sana kwa watu wenye mwenendo mpotovu kingono kuacha tabia hiyo eti kwa sababu wamefunga ndoa. Lakini kuna uwezekano mkubwa kwamba wale ambao ni washikamanifu kwa viwango vya Mungu vya maadili kabla ya kufunga ndoa watakuwa washikamanifu kwa wenzi wao baadaye.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ikiwa ninataka kutunza ubikira mpaka nitakapofunga ndoa, ninahitaji ․․․․․
Ikiwa rafiki zangu wanafanya iwe vigumu kushikilia azimio langu, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa maoni yako, unafikiri ni kwa nini watu huwadhihaki wale ambao ni mabikira?
● Kwa nini inaweza kuwa vigumu kutunza ubikira?
● Kuna faida gani za kutunza ubikira mpaka wakati utakapofunga ndoa?
● Ni jinsi gani unaweza kumweleza mdogo wako faida za ubikira?
[Blabu katika ukurasa wa 51]
“Mimi huepuka kishawishi cha kufanya ngono kwa kukumbuka sikuzote kwamba ‘hakuna mwasherati au mtu asiye safi aliye na urithi wowote katika ufalme wa Mungu.’’’ (Waefeso 5:5)—Lydia
[Sanduku katika ukurasa wa 49]
Ukurasa wa Mazoezi
Ni Nini Hasa Kinachotokea Baadaye?
Mara nyingi marafiki wako na burudani zinazopendwa wanatumia ujanja kuficha matokeo mabaya ya kufanya ngono kabla ya ndoa. Ona mambo matatu yanayofuata. Unafikiri ni nini hasa kitakachowapata vijana hawa?
● Mwanafunzi mmoja anajigamba kwamba amefanya ngono na wasichana wengi. Anasema kwamba ni raha na hakuna madhara yoyote. Ni nini hasa kitakachotokea baadaye—kwake na kwa wasichana hao? ․․․․․
● Sinema inaisha ikionyesha vijana wawili ambao hawajafunga ndoa wakifanya ngono ili kuonyeshana upendo. Ni nini kinachoweza kutokea baadaye kihalisi? ․․․․․
● Unakutana na mvulana mwenye sura ya kuvutia anayetaka ufanye ngono naye. Anakuambia kwamba hakuna mtu atakayejua. Ukikubali na kisha ujaribu kuficha jambo hilo, ni nini hasa kinachoweza kutokea baadaye? ․․․․․
[Picha katika ukurasa wa 54]
Kufanya ngono kabla ya ndoa ni kama kufungua zawadi kabla ya kukabidhiwa
-