-
Jina la Mungu—Maana na MatumiziBiblia Inafundisha Nini Hasa?
-
-
Isitoshe, watu wasipolitumia jina la Mungu, hawawezi kuelewa maana muhimu ya jina hilo. Jina la Mungu linamaanisha nini?
Mungu mwenyewe alimweleza mtumishi wake mwaminifu Musa maana ya jina lake. Musa alipomwuliza Mungu jina lake, Yehova alimjibu: “Nitakuwa kile nitakachokuwa.” (Kutoka 3:14) Tafsiri ya Rotherham inatafsiri hivi maneno hayo: “Nitakuwa chochote Nipendacho kuwa.” Kwa hiyo, Yehova anaweza kuwa chochote kinachohitajika ili kutimiza makusudi yake.
Hebu wazia kwamba ungeweza kuwa chochote ambacho ungependa kuwa. Ungewafanyia nini rafiki zako? Ikiwa mmoja wao angekuwa mgonjwa sana, ungeweza kuwa daktari stadi na kumtibu. Ikiwa mwingine angefilisika, ungeweza kuwa tajiri na kumsaidia. Hata hivyo, ukweli ni kwamba wewe huna uwezo wa kuwa chochote ambacho ungependa kuwa. Hakuna yeyote kati yetu aliye na uwezo huo. Unapoendelea kujifunza Biblia, utafurahi kuona jinsi Yehova huwa chochote kinachohitajika ili kutimiza makusudi yake. Naye anapenda kutumia nguvu zake kwa niaba ya wale wanaompenda. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Wale wasiojua jina la Yehova hawawezi kuuona uwezo wake wa kuwa chochote anachopenda kuwa.
Ni wazi kwamba, jina Yehova linapaswa kuwa katika Biblia. Kujua maana yake na kulitumia kwa uhuru katika ibada yetu kunaweza kutusaidia sana kumkaribia Baba yetu wa mbinguni Yehova.a
-
-
Jinsi Unabii wa Danieli Ulivyotabiri Kutokea kwa MasihiBiblia Inafundisha Nini Hasa?
-
-
NYONGEZA
Jinsi Unabii wa Danieli Ulivyotabiri Kutokea kwa Masihi
NABII Danieli aliishi zaidi ya miaka 500 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu. Hata hivyo, Yehova alimpa Danieli ujumbe ambao ungefanya iwezekane kujua wakati hususa ambapo Yesu angetiwa mafuta au kuwekwa rasmi kuwa Masihi au Kristo. Danieli aliambiwa hivi: “Ujue na ufahamu kwamba tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62.”—Danieli 9:25.
Ili kujua wakati ambapo Masihi angetokea, kwanza tunahitaji kujua mwanzo wa kile kipindi ambacho Masihi angetokea mwishoni mwake. Kulingana na unabii huo, kingeanza wakati ambapo ‘lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu lingetolewa.’ Neno hilo lilitolewa wakati gani? Kulingana na Nehemia, mwandishi wa Biblia, neno la kujenga upya kuta za Yerusalemu lilitolewa “katika mwaka wa 20 wa Mfalme Artashasta.” (Nehemia 2:1, 5-8) Wanahistoria wanathibitisha kwamba mwaka wa 474 K.W.K., ndio uliokuwa mwaka wa kwanza wa utawala wa Artashasta. Kwa hiyo, mwaka wa 20 wa utawala wake ni mwaka wa 455 K.W.K. Kwa hiyo, kile kipindi cha unabii wa Danieli kuhusu Masihi kingeanza mwaka wa 455 K.W.K.
Pili, Danieli anaonyesha urefu wa kipindi hicho ambacho “Masihi aliye Kiongozi” angetokea. Unabii huo unataja “majuma 7, pia majuma 62”—jumla ya majuma 69. Kipindi hicho kina urefu gani? Tafsiri kadhaa za Biblia zinaonyesha kwamba hayo si majuma ya siku saba, bali ya miaka. Yaani, kila juma linawakilisha miaka saba. Wayahudi wa kale walizoea kuhesabu majuma ya miaka, au vipindi vya miaka saba. Kwa mfano, kila mwaka wa saba ulikuwa mwaka wa Sabato. (Kutoka 23:10, 11) Kwa hiyo, yale majuma 69 ya unabii yalikuwa vipindi 69 vya miaka 7 kila kimoja, au jumla ya miaka 483.
Sasa tunachohitaji ni kupiga hesabu tu. Tukihesabu miaka 483 kuanzia mwaka wa 455 K.W.K., tutafika mwaka wa 29 W.K. Huo ndio mwaka hususa ambao Yesu alibatizwa na kuwa Masihi!a (Luka 3:1, 2, 21, 22) Je, huo si utimizo wenye kustaajabisha wa unabii wa Biblia?
a Kuanzia mwaka wa 455 K.W.K. hadi mwaka wa 1 K.W.K. ni miaka 454. Kuanzia mwaka wa 1 K.W.K. hadi 1 W.K. ni mwaka mmoja (hakukuwa na mwaka sufuri). Na kuanzia mwaka wa 1 W.K. hadi mwaka wa 29 W.K. ni miaka 28. Tukijumlisha miaka hiyo tunapata jumla ya miaka 483. Yesu “alikatiliwa mbali” alipouawa mwaka wa 33 W.K., katika juma la 70 la miaka. (Danieli 9:24, 26) Unaweza kupata habari zaidi kuhusu unabii huo katika kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! sura ya 11, na Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 899-901 au Étude Perspicase, Buku la 2, ukurasa wa 995-997. Vitabu hivyo vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Yesu Kristo—Masihi AliyeahidiwaBiblia Inafundisha Nini Hasa?
-
-
NYONGEZA
Yesu Kristo—Masihi Aliyeahidiwa
ILI kutusaidia kumtambua Masihi, Yehova Mungu aliwaongoza manabii wengi wa Biblia waandike habari kuhusu kuzaliwa, huduma, na kifo cha Mkombozi aliyeahidiwa. Unabii wote huo wa Biblia ulitimizwa maishani mwa Yesu Kristo. Unabii huo ni sahihi sana na una habari kamili. Kwa mfano, hebu tuchunguze unabii mbalimbali uliotabiri kuzaliwa kwa Masihi na maisha yake ya utotoni.
Nabii Isaya alitabiri kwamba Masihi angetokea katika ukoo wa Mfalme Daudi. (Isaya 9:7) Kwa kweli, Yesu alizaliwa katika ukoo wa Daudi.—Mathayo 1:1, 6-17.
Mika, nabii mwingine wa Mungu alitabiri kwamba hatimaye mtoto huyo angekuwa mtawala na kwamba angezaliwa “Bethlehemu Efratha.” (Mika 5:2) Wakati ambapo Yesu alizaliwa, kulikuwa na miji miwili huko Israeli iliyokuwa ikiitwa Bethlehemu. Mji mmoja ulikuwa karibu na Nazareti, kaskazini mwa nchi hiyo, nao ule mwingine ulikuwa karibu na Yerusalemu huko Yuda. Mji wa Bethlehemu, uliokuwa karibu na Yerusalemu, ulikuwa ukiitwa Efratha zamani. Yesu alizaliwa katika mji huo, kama vile tu unabii ulivyokuwa umetabiri!—Mathayo 2:1.
Unabii mwingine wa Biblia ulitabiri kwamba Mwana wa Mungu angeitwa “kutoka Misri.” Mtoto huyo, Yesu, alipelekwa Misri. Alirudishwa kutoka huko baada ya kifo cha Herode, na hivyo, unabii huo ukatimia.—Hosea 11:1; Mathayo 2:15.
Katika chati yenye kichwa “Unabii Kumhusu Masihi,” maandiko yaliyoorodheshwa chini ya kichwa “Unabii” yanaeleza mambo mengi zaidi kumhusu Masihi. Tafadhali linganisha maandiko hayo na yale yaliyo chini ya kichwa “Utimizo.” Kufanya hivyo kutaimarisha zaidi imani yako katika ukweli wa Neno la Mungu.
Unapochunguza maandiko hayo kumbuka kwamba maandiko yenye unabii yaliandikwa mamia ya miaka kabla ya kuzaliwa kwa Yesu. Yesu alisema: “Mambo yote yaliyoandikwa katika sheria ya Musa na katika Manabii na Zaburi juu yangu lazima yatimizwe.” (Luka 24:44) Biblia inaonyesha wazi kwamba unabii huo ulitimia kabisa!
-
-
Ukweli Kuhusu Baba, Mwana, na Roho TakatifuBiblia Inafundisha Nini Hasa?
-
-
NYONGEZA
Ukweli Kuhusu Baba, Mwana, na Roho Takatifu
WATU wanaoamini Utatu husema kwamba kuna Mungu Baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu. Wote wanasemekana kuwa sawa, wenye nguvu zote, na hawana mwanzo. Kwa hiyo, kulingana na fundisho la Utatu, Baba ni Mungu, Mwana ni Mungu, na Roho Mtakatifu ni Mungu, hata hivyo, Mungu ni mmoja tu.
-