Je! Mungu Amekuita Wewe Kwenye Amani?
“Yule asiyeamini akiondoka, na aondoke. Hapo huyo ndugu mume au ndugu mke hafungiki. Lakini Mungu ametuita katika amani [ameita nyinyi kwenye amani, NW].”—1 WAKORINTHO 7:15.
1. Kimaandiko, kunapasa kuwa na rai gani juu ya ndoa?
YEHOVA hakukusudia kamwe kifungo cha ndoa kiongoze kwenye mtengano au talaka inayoleta kihoro kingi cha moyoni. Ndoa ilipasa kuwa kifungo chenye kudumu cha ‘mnofu mmoja,’ kinachotokeza shangwe, pumziko, na amani. (Mwanzo 2:24, NW; Ruthu 1:9) Kwa ujumla, Maandiko yanashauri watu waliofunga ndoa wabaki pamoja, hata ikiwa mwenzi mmoja ni Mkristo na yule mwingine si mwitikadi. (1 Wakorintho 7:12-16) Waaidha, mishughulikiano yenye hila inayotokeza utengano wa vifungo vya ndoa inafanya mmoja awe na ustahili wa kiadili kumtolea hesabu Mungu, ambaye ‘huchukia talaka.’—Malaki 2:13-16, NW.
2. Wakristo wanakuwa na rai ya jinsi gani juu ya mtengano na talaka?
2 Kutokamilika kwa kibinadamu na mambo mengine yameongoza nyakati nyingine kwenye mtengano au talaka hata miongoni mwa watumishi wa Mungu waliobatizwa. Hata hivyo, kwa sababu ya staha kubwa ambayo Wakristo wanayo kwa kifungo cha ndoa, kwa kawaida hatua hizo zinachukuliwa baada tu ya jitihada endelevu za kudumisha ndoa zikiwa pamoja. Katika habari hiyo, Mungu mwenyewe aliweka kielelezo bora kupita vyote. Akiwa “mwenyeji-mume” wa Israeli wa kale, yeye alivumilia karne nyingi za ugumu wa kichwa, uasi, na uzinzi wa kiroho kwa upande wa watu wake. (Isaya 54:1-5; Yeremia 3:14-17, NW; Hosea 1:10, 11; 3:1-5) Ni baada tu ya wao kupita hatua ya kurudika kwamba Yehova aliwatupa wakiwa taifa.—Mathayo 23:37, 38.
3. (a) Ni kwa sababu gani zinazoruhusika Kimaandiko Mkristo angeweza kujitenga na mwenzi wa ndoa? (b) Talaka ya Kimaandiko inawezekana chini ya mastakimu gani?
3 Nyakati nyingine, wazee wa kundi wanafikiwa na waitikadi wenzao wakitaka msaada kuhusu matatizo mazito ya ndoa. Wazee hawapewi mamlaka ya kuambia mmoja yeyote aende zake au ataliki mwenzi wa ndoa, lakini wanaweza kuonyesha yale ambayo Neno la Mungu linasema juu ya mambo hayo. Kama ilivyoonyeshwa katika makala iliyotangulia, mtengano unaruhusika Kibiblia katika kisa cha kutoandaa riziki kimakusudi, kutendwa vibaya kimwili kwa njia ya kupita kiasi, au kuhatarishwa kabisa kwa hali ya kiroho. Imeonwa pia kwamba talaka ya Kimaandiko iliyo na uwezekano wa kufunga ndoa tena wakati ujao pamoja na mwenzi mwingine inawezekana ikiwa mwenzi wa ndoa amefanya “uasherati,” ambao unatia ndani namna kadhaa za ngono zisizo za kiadili. (Mathayo 19:9) Kama ilivyo kiasili, mtengano au talaka haipasi kuwa neno lililokwisha kukatwa mapema, kwa kuwa huenda ikawezekana kurudisha amani ya ndoa, na hata uzinzi au namna nyingine za uasherati zinaweza kusamehewa na mwenzi wa ndoa asiye na hatia.—Mathayo 5:31, 32; linganisha Hosea 3:1-3.
4. (a) Toa kifupi muhtasari wa yale ambayo Paulo aliambia Wakristo waliofunga ndoa kwenye 1 Wakorintho 7:10-16. (b) Ni wakati gani inapoweza kusemwa: ‘Mungu ameita nyinyi kwenye amani’?
4 Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, mtume Paulo alihimiza Wakristo waliofunga ndoa wasiache wenzi wao wa ndoa. (1 Wakorintho 7:10-16) Kulingana na maneno ya Paulo, ikiwa mwenzi wa ndoa asiye mwitikadi anachagua kubaki pamoja na mwenzi wake wa ndoa aliye Mkristo, mwitikadi anapaswa kujaribu kumsaidia kiroho. (1 Petro 3:1-4) Kuongolewa kwake kungesaidia sana kufanya maskani iwe mahali pa pumziko na amani. Hata hivyo, ikiwa yule asiye mwitikadi anakinza imani ya mwenzi wake mwitikadi vikali sana hivi kwamba anachagua kufanya mtengano, Mkristo anaweza kufanya nini? Ikiwa aliye mwitikadi angejaribu kumlazimisha akae naye, huenda huyo asiye mwitikadi akafanya hali iwe isiyopendeka sana mpaka Mkristo huyo akose kabisa amani. Kwa hiyo mwitikadi anaweza kuacha asiye mwitikadi aende zake ili kuwe na amani. (Mathayo 5:9) Ni wakati tu mwenzi wa ndoa asiye mwitikadi anapoenda zake kwamba inaweza kusemwa hivi: ‘Mungu ameita nyinyi kwenye amani.’ Maneno hayo hayawezi kutumiwa kwa kufaa kutetea uhaki wa kutengana kwa wenzi wawili walio Wakristo juu ya misingi isiyo ya kimaandiko au iliyo ya kipuuzi.
5. Ni maswali gani ambayo sasa yanastahili tuyafikirie?
5 Kila mtengano au talaka ina vijambo vyayo yenyewe, na hakuna “kanuni ya mwongozo” ambayo inashughulikia kila kisa. Lakini ni matatizo gani huenda Mkristo aliye katika mtengano au talaka akakabili? Ni nini laweza kufanywa kuhusu matatizo hayo? Na wengine wanaweza kusaidia jinsi gani?
Mahitaji ya Kihisia-Moyo au ya Kingono
6. Kuhusu matatizo, inaweza kusemwa nini juu ya mtengano au talaka
6 Mtengano au talaka inayoruhusika Kimaandiko itatatua matatizo fulani. Lakini kwa msingi hatua hizo zinabadilisha fungu moja la matatizo kwa kupokea fungu jingine. Mathalani, Mkristo mmoja aliye katika talaka alisema hivi: “Ni sharti mimi nimpe Yehova asante kwamba sasa nina amani.” Lakini mwanamke huyo alikiri hivi: “Si rahisi kulea watoto ukiwa mzazi mmoja. Na nyakati fulani mmoja anaweza kuwa mpweke na kushuka sana moyo. Hata kingono mambo si rahisi. Inakuwa lazima mmoja ajirekebishe kulingana na maisha yaliyo tofauti kabisa.”a
7. Kwa nini Mkristo anapaswa afikiri kwa uangalifu juu ya matokeo ya mtengano au talaka?
7 Kwa hiyo, ikiwa Mkristo ana uchaguzi wa kufanya, anapaswa kufikiria kwa uangalifu yanayowezekana kuwa matokeo ya mtengano au talaka. Mathalani, fikiria mahitaji ya kihisia-moyo, labda tamaa ya mwanamke ya uandamani wa kiume. (Linganisha Mwanzo 3:16.) Huenda mwanamke aliye katika talaka akawa ana matumaini imara ya kufunga ndoa tena. Wanawake fulani hutamani kupata ufungulio kutoka kwenye ndoa yenye majaribu, lakini je! wao wako tayari kukubali uwezekano wa kwamba huenda kusiwe na fursa ya kufunga ndoa tena?
8. (a) Kulingana na 1 Wakorintho 7:11, wenzi Wakristo waliotengana wanapaswa kufikiria nini kwa sala? (b) Ni mahitaji gani yasiyopasa kukadiriwa umaana mdogo wakati wa kufikiria mtengano au talaka?
8 Paulo aliandika hivi: “Ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe.” (1 Wakorintho 7:11) Kwa kufanya jitihada ya kadiri fulani, huenda ikawezekana mwanamke ‘kupatana’ na mume wake. Basi, ikiwa wenzi wa ndoa walio Wakristo wametengana inawapasa wafikirie kwa uzito na kwa sala kufanya upatano. Waaidha, haiwapasi kupuuza uhakika wa kwamba vichochezi vya hisia za ngono huenda vikatokeza hatari. Mungu ataelekea kuwa na rai gani juu yao ikiwa kutopatana kwao kunafanya watumbukie katika ukosefu wa adili? Linalotoa kielezi cha hatari hiyo ni jambo lililopata mwanamke fulani aliyebatizwa. Baada ya talaka, yeye alianza kufanya matembezi pamoja na mwanamume mlimwengu, baada ya muda mfupi akapata mimba, na kutengwa na ushirika. Ingawa baadaye alirudishwa, lililompata linakazia uhitaji wa hadhari na utegemeo wenye sala juu ya Yehova ili kuepuka ‘kutenda dhambi dhidi ya Mungu.’ (Mwanzo 39:7-12, NW) Ni wazi pia kwamba mahitaji ya kihisia-moyo na ya kingono hayapasi kukadiriwa umaana mdogo wakati mtengano au talaka inapofikiriwa hapo kwanza.
Upweke Unaweza Kupunguzwa
9. Ni jinsi gani sisi tungeweza kusaidia Wakristo walio katika mtengano au talaka wapambane na upweke?
9 Ikiwa mtengano au talaka haiepukiki, itakuwa lazima kukabili matatizo yanayotokana nayo. Mathalani, upweke ni tatizo zito kwa Wakristo fulani walio katika mtengano au talaka. Wengine wanaweza kufanya nini juu ya jambo hilo? Basi, wazee wa kundi na wengine wanaweza kuonyesha upendezi wa kiroho katika watu mmoja mmoja, wakitafuta kuwatia moyo. (Linganisha 1 Wathesalonike 5:14.) Miongoni mwa mambo mengine, tungeweza pindi kwa pindi kualika watu hao na watoto wao kwenye maskani yetu kwa ajili ya mlo wa kiasi na kuwa na maongezi yenye kujenga pamoja na jamaa yetu. Si lazima kuwaandikia karamu nono, kwa maana “chakula cha mboga penye mapendano; ni bora kuliko ng’ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.” (Mithali 15:17) Jioni hiyo ingeweza kutia ndani kusimulia mambo yaliyoonwa yakafurahiwa katika huduma au funzo la kikundi katika kujitayarishia mkutano fulani wa Kikristo.
10, 11. (a) Mkristo aliye katika mtengano au talaka angeweza kusaidiwa kwa njia gani nyingine? (b) Kuna sababu gani ya kuwa na hadhari?
10 Kufanya mzazi aliye katika talaka au mtengano ajiunge na jamaa yako pamoja na watoto wake katika huduma ya shambani kunaweza pia kuwasaidia wakabiliane na upweke. Bila shaka, wengine hawawezi kuchukua mahali pa mzazi asiyekuwapo, lakini mwanamke mmoja Mkristo aliye katika talaka alisema: “Magumu ya kulea watoto wangu bila mwanamume katika nyumba yamepunguzwa sana na usaidizi wa wazee na watumishi katika kundi ambao wamejaribu kujazia nafasi hiyo kwa njia zenye mafaa.”
11 Hata hivyo, kuna sababu ya kuwa na hadhari. Dada mmoja alikiri hivi: “Kwa kuwa mwana wangu hana baba, ndugu mmoja alipendezwa naye kwa fadhili sana. . . . Mimi nilianza kuona jinsi alivyokuwa mwenye fadhili na ukarimu kwa mwana wangu, na tamaa mbaya zikaanza kusitawi ndani yangu. Ilikuwa sawasawa na vile Daudi alivyokuza tamaa mbaya kwa kitu kisichokuwa chake.” (2 Samweli 11:1-4) Ingawa ukosefu wa adili katika ngono haukutukia, mwanamke huyo aliaibikia fikira zake na vitendo vya mzaha wa kimapenzi, akatafuta msamaha wa Yehova, na kuvunja ushirika wake na ndugu yule. Jambo hilo linatoa kielezi kizuri kama nini juu ya uhitaji wa kukataa tamaa mbaya na “chochote kilicho na sura ya uovu”!—1 Wathesalonike 5:22, The New American Bible; Wagalatia 5:24.
12. Mtu angeweza kupunguza upweke wake kwa kuchukua hatua gani ya mwelekeo chanya?
12 Huenda upweke ukapunguzwa kwa kufanya mambo kwa ajili ya wengine. “Ukiwa una shughuli nyingi kujinyoosha na kusaidia wengine, hakuna nafasi ya kujisikitikia wala ya upweke,” akasema dada mmoja ambaye vifungo vyake vya ndoa vilikuwa vimetiwa utengano. “Kujinyoosha” huko kwa mtu aliye katika mtengano au talaka kungeweza kutia ndani kualika jamaa fulani kwenye maskani ya mmoja kwa ajili ya jioni ya ushirika wenye kujenga kiroho. Ikiwa jambo hilo linawezekana mara chache tu kwa sababu za kifedha au nyinginezo, ungeweza kuzuru na kuwatia moyo walio wagonjwa au wengine. Ungeweza pia kusaidia walio wazee-wazee kwa ununuzi wao au kazi mbalimbali za nyumbani. Jitoe kwa njia kama hizo, na utapata ithibati iliyoongezeka kwamba “kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35, NW.
13. Ni nini msaada mwingine wa kushinda upweke?
13 Msaada mwingine wa kushinda upweke ni kuwa na ukawaida wa kuchukua hatua ya kwanza kujiunga na waitikadi wenzako katika kazi ya kuhubiri Ufalme. “Nyakati fulani, mimi nahisi nikiwa mpweke kwa kuhitaji mume,” akakiri dada mmoja, “bali kwa kuwa na utumishi wa shambani ulioongezeka na uhuru mpya nilio nao kufanya ushirika pamoja na akina ndugu na dada, vipindi hivyo vinakuwa vichache sana na vya muda mfupi tu.” Kutoa ushuhuda wa nyumba kwa nyumba kwa ukawaida huenda kukaongoza kwenye ziara za kurudia na mafunzo ya nyumbani ya Biblia pamoja na watu wenye kupendezwa, ambao baadhi yao huenda wakawa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu. Bila shaka, kushinda upweke siyo sababu yetu ya kujitia katika huduma, lakini huenda hiyo ikawa athari moja ya utendaji huo wenye shangwe nyingi na ulio na baraka.—Mithali 10:22.
14. Ni utendaji gani unaopasa kuwa na athari njema juu ya Wakristo walio katika mtengano au talaka?
14 Watu wote wa Yehova wanaweza kunufaika kiroho kutokana na kushiriki katika huduma, wakishiriki katika mikutano ya Kikristo, na ‘kutafuta kwanza Ufalme.’ (Mathayo 6:33, NW) Kwa kuwa utendaji huo wenye mafaa una athari nzuri sana juu ya watumishi wa Yehova kwa ujumla, mifuatio hiyo inaweza pia kujenga Wakristo walio katika mtengano au talaka. Hapana, utendaji huo hautatatua matatizo yao yote, lakini unapasa kuleta maendeleo katika mtazamio wao.
Sala Hutimiza Fungu Muhimu
15. Sala inaweza kutimiza fungu gani katika maisha za wale wanaolazimika kujirekebisha walingane tena na hali za useja?
15 Dada mmoja Mkristo aliyelazimika kujirekebisha alingane tena na hali za useja alisaidiwa kwa “kuendelea kuwa mwenye shughuli katika utumishi wa shambani . . . na kuzuru walio wagonjwa, wazee-wazee, na wasio watendaji.” Lakini yeye aliongezea hivi: “Wakati wowote ninapohisi mpweke, mimi ninafanya ziara na kusali nipate imara, nikijua kwamba Shetani ana shughuli nyingi sana.” Ndiyo, sala yenye kuhisiwa moyoni ni muhimu ili kudumisha ukamilifu kwa Mungu. Sala za Wakristo walio katika mtengano au talaka zinaweza kutia ndani maombi ya kutaka roho ya Yehova na tunda layo la kujidhibiti ili kuendelea kuchunga vizuri vichochezi vya hisia ya ngono. (Luka 11:13; Wagalatia 5:22, 23, NW; Wakolosai 3:5, 6) Waaidha, kwa kuwa huenda kufanya maamuzi ambayo hapo kwanza yalifanywa na mume kukatokeza matatizo kwa wanawake walio katika mtengano au talaka, huenda wao pia wakahitaji kusali wapate msaada wa Mungu katika kuamua mambo kwa hekima na kukabiliana na majaribu mbalimbali.—Yakobo 1:2-8.
16. Kuhusiana na mtengano au talaka, ni nini lingeweza kusemwa juu ya hisia za hatia?
16 Huenda hisia za hatia zikathibitika kuwa zenye majaribu. Mkristo mmoja alikiri hivi: “Hatia ambayo unahisi wakati wa talaka, hata ikiwa si wewe uliye na hatia, inaweza kulemea sana hisia.” Bila shaka, hisia za hatia zinaeleweka ikiwa mtengano au talaka ilitukia kwa sababu mmoja alikataa isivyo haki kutimiza wajibu wa ndoa. (1 Wakorintho 7:3-5) Lakini ikiwa mtengano au talaka ilitukia kwa sababu ya Kimaandiko baada ya fikira yenye sala, ingefaa kusali ili kupata msaada wa Yehova kushinda hisia zisizofaa za hatia. Inaweza kuongezewa kwamba wazee wa kundi wanapaswa kuwa waangalifu watoe shauri lenye msingi wa Biblia wala wasitoe ushauri wao kwa njia ambayo Mkristo anafanywa ahisi kuwa ana hatia akijipatia au akiruhusu mtengano au talaka inayoruhusika Kibiblia.
Kulindwa na “ile Amani ya Mungu”
17. Ni jambo gani linaloweza kusaidia Wakristo wote wawe wenye furaha na wathibitifu katika ulimwengu huu wenye msukosuko?
17 Wakristo walio katika mtengano au talaka mara nyingi huwa na matatizo ya kipekee. Hata hivyo, kwa kadiri fulani, “mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu [zetu] walioko duniani.” (1 Petro 5:6-11) Mathalani, mnyanyaso huathiri wote wanaotumikia Yehova, na Wakristo walio wengi wanakabiliana na matatizo ya kifedha au ya kiafya, mitamauko, vishawishi, na kadhalika. Kwa hiyo, kama mashahidi wengine wa Yehova, Mkristo aliye katika mtengano au talaka anahitaji kuendelea kutimiza mahitaji ya kiroho kwa funzo la Biblia, hudhurio la ukawaida la mikutano, huduma ya shambani iliyo na utendaji, maisha ya utumishi mtakatifu yaliyosawazika vizuri pande zote, na sala ya daima ili kubaki karibu na Yehova. (Mathayo 5:3) Kutofanya hivyo kungehatarisha hali ya kiroho ya Mkristo yeyote, hali ‘kutafuta kwanza Ufalme’ humpa kila shahidi wa Yehova aliye mshikamanifu kipimo kikubwa cha furaha na uthibitifu katika ulimwengu huu wenye msukosuko.
18. Ni maswali na hatua gani ambazo zinastahili kufikiriwa kwa uzito na wenzi Wakristo walio katika mtengano?
18 Uthibitifu wetu wa kiroho unategemea utumizi wa kibinafsi wa Neno la Mungu. Kwa hiyo, ikiwa wewe ni Mkristo mwenye kujitenga kutoka kwa mwenzi wa ndoa aliyejiweka wakfu pia kwa Mungu, je! umethamini moyoni shauri la Paulo kwenye 1 Wakorintho 7:10-16? Hasa ikiwa mtengano huo umeendelea kwa muda fulani, ingefaa usali kwa moyo wa bidii juu ya kufanya upatano. Ungeweza pia kujiuliza hivi: Yehova anatarajia nini kwangu mimi niliye mtu aliyefunga ndoa? Je! wenzi wa ndoa walio Wakristo hawapaswi kupatanisha maisha zao na matakwa ya kimungu kwa wale ambao wameingia kifungo cha ndoa? Je! ingeweza kuwa kwamba sisi tunakosa baraka ya Yehova kwa sababu tumeshindwa kuheshimu nadhiri zetu za ndoa? Ebu fikiria mema ambayo huenda yakatimizwa mkizungumzia mambo kwa unyenyekevu, msali kwa moyo wa bidii, na kufanya bidii kutumia Neno la Mungu maishani. Lingekuwa jambo zuri namna gani kama nyinyi wawili mngeweza kutatua matatizo yenu ya ndoa na kufurahia tena kuishi pamoja katika maskani ya pumziko na amani!
19. Kulingana na Wafilipi 4:6, 7, ni jambo gani lenye thamani kubwa ambalo watumishi wote wa Yehova wanaweza kufurahia?
19 Watumishi wote waaminifu wa Yehova wanahitaji na wanaweza kufurahia kitu fulani chenye thamani kubwa—“ile amani ya Mungu ambayo inapita mno fikira yote.” Sisi Wakristo tunaweza kuwa na amani hiyo iliyo hazina kubwa tukitii maneno ya Paulo: “Msijisumbue juu ya jambo lolote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-asante acheni maombi rasmi yenu yajulishwe kwa Mungu; na ile amani ya Mungu ambayo inapita mno fikira yote italinda mioyo yenu na nguvu zenu za kiakili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7, NW.
20. (a) Ni nini “ile amani ya Mungu”? (b) Hata kama hali yetu ya ndoa ni nini, inatupasa sisi kufanya nini?
20 Amani hiyo ni utulivu mwingi na ushwari unaopewa na Mungu, hata katikati ya mastakimu zenye majaribu sana. Shina layo ni uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na maarifa ya kujua kwamba sisi tunatenda yaliyo ya kufurahisha machoni pake. Wale walio na “ile amani ya Mungu” wanaruhusu roho yake iwatendeshe, nao hawalemewi mno na hisia ya wasiwasi. Kwa nini? Kwa sababu wanajua kwamba hakuna jambo linaloruhusiwa kuwapata ambalo haliwi kwa ruhusa ya kimungu. (Waefeso 4:30; linganisha Matendo 11:26.) Kwa hiyo tuwe tu waseja au tuliofunga ndoa, tuwe tu katika mtengano au talaka, acheni sisi tuthamini sana “ile amani ya Mungu.” Tuwe na uhakika ule ule aliokuwa nao Daudi, ambaye alitangaza hivi: “Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, maana Wewe, BWANA [Yehova, NW], peke yako, ndiwe unijaliaye kukaa salama.”—Zaburi 4:8.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate zungumzio la jamaa zenye mzazi mmoja, tafadhali ona Mnara wa Mlinzi wa Machi 1, 1981, kurasa 4-16.
Wewe Ungejibu Jinsi Gani?
◻ Ni chini ya mastakimu gani inaweza kusemwa: ‘Mungu ameita nyinyi kwenye amani’?
◻ Upweke unaweza kupunguzwa jinsi gani?
◻ Ni fungu gani ambalo sala inapaswa kutimiza katika maisha ya Mkristo aliye katika mtengano au talaka?
◻ Wewe ungeeleza jinsi gani “ile amani ya Mungu” inayolinda mioyo ya watumishi wa Yehova walio waseja, waliofunga ndoa, walio katika mtengano, au talaka?
[Picha katika ukurasa wa 29]
Sala inaweza kuletea Wakristo wote waaminifu “ile amani ya Mungu” ambayo italinda mioyo yao na nguvu za kiakili