-
Unabii wa Biblia Hutimia KikamiliMnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
Unabii wa Biblia Hutimia Kikamili
“Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi.”—YOSHUA 23:14.
BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Utabiri wa kale haukueleweka vizuri wala haukutegemeka, nao uaguzi unaofanya leo kwa kutumia nyota, vilevile hautegemeki. Wanadamu hujaribu kutabiri mambo yatakayotokea wakati ujao kwa kuchunguza mambo yanayotukia leo, lakini mara nyingi, hawatabiri matukio hususa yatakayotukia miaka mingi ijayo. Kinyume na hayo, unabii wa Biblia hutaja mambo hususa na siku zote hutimia, hata ikiwa unatabiri “kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.”—Isaya 46:10.
MFANO: Katika karne ya sita K.W.K., nabii Danieli aliona maono yaliyotabiri kwamba milki ya Ugiriki ingeshinda kwa ghafla Muungano wa Umedi na Uajemi. Pia, yalitabiri kwamba muda mfupi baada ya mfalme wa Ugiriki kupata ushindi na ‘kuwa na nguvu,’ ufalme wake ‘ungevunjwa.’ Nani angekuwa mfalme badala yake? Danieli aliandika: “Kuna falme nne zitakazosimama kutoka katika taifa lake, lakini si kwa nguvu zake.”—Danieli 8:5-8, 20-22.
MAONI YA WANAHISTORIA: Zaidi ya miaka 200 baada ya kipindi ambacho nabii Danieli aliishi, Aleksanda Mkuu alianza kutawala milki ya Ugiriki. Miaka kumi tu baada ya kuanza kutawala, Aleksanda alikuwa ameshinda Milki ya Umedi na Uajemi na kupanua utawala wa Ugiriki kufikia Mto Indus (kwa sasa uko Pakistan). Lakini alikufa kwa ghafula akiwa na umri wa miaka 32. Mwishowe, vita vilivyopiganwa karibu na kijiji cha Ipsus, katika Asia Ndogo, vilifanya milki yake igawanyike. Washindi wanne wa pigano hilo waligawana Milki ya Ugiriki. Hata hivyo, hakuna yeyote kati yao aliyewahi kuwa na nguvu kama za Aleksanda.
UNA MAONI GANI? Je, kuna kitabu kingine chochote kinachoweza kudai kwamba unabii wake umetimia kikamili? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?
“Biblia ina unabii . . . mwingi hivi kwamba haiwezekani kudai kuwa unatimia tu wenyewe.”—KITABU A LAWYER EXAMINES THE BIBLE, CHA IRWIN H. LINTON
-
-
Historia Sahihi, Wala Si HadithiMnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
Historia Sahihi, Wala Si Hadithi
“Nimefuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi.”—LUKA 1:3.
BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Hadithi na hekaya hueleza mambo yenye kuvutia lakini hazitaji mahali, tarehe, na majina hususa ya watu. Kinyume cha hilo, Biblia ina habari nyingi za kihistoria ambazo zinawahakikishia wasomaji kwamba ina “maneno ya kweli kabisa.”—Zaburi 119:160, The Psalms for Today, iliyotafsiriwa na R. K. Harrison.
MFANO: Biblia inasema kwamba “Nebukadneza mfalme wa Babiloni . . . [aka]mpeleka Yehoyakini [Mfalme wa Yuda] uhamishoni Babiloni.” Baadaye, “Evil-merodaki mfalme wa Babiloni, katika mwaka wa kuwa kwake mfalme, akakiinua kichwa cha Yehoyakini mfalme wa Yuda kutoka katika nyumba ya kifungo.” Zaidi ya hayo, “[Yehoyakini] alipewa posho daima kutoka kwa mfalme, kila siku kama inavyostahili, siku zote za maisha yake.”—2 Wafalme 24:11, 15; 25:27-30.
MAMBO AMBAYO WATAALAMU WA VITU VYA KALE WAMEGUNDUA: Katika magofu ya Babiloni la kale, wataalamu wa vitu vya kale waligundua hati za usimamizi zilizokuwa na tarehe ya wakati wa utawala wa Nebukadneza wa Pili. Hati hizo zina orodha ya kiwango cha chakula ambacho wafungwa na watu wengine waliotegemea nyumba ya kifalme walipewa. Orodha hiyo inatia ndani “Yaukini [Yehoyakini],” ambaye alikuwa “mfalme wa nchi ya Yahud (Yuda),” pamoja na familia yake. Vipi kuhusu kuwapo kwa Evil-merodaki, mfalme aliyetawala baada ya Nebukadneza? Chombo fulani kilichopatikana karibu na jiji la Susa kilikuwa na maandishi haya: “Jumba la kifalme la Amili-Marduki [Evil-merodaki], Mfalme wa Babiloni, mwana wa Nebukadneza, Mfalme wa Babiloni.”
UNA MAONI GANI? Je, kuna kitabu kingine chochote kitakatifu na cha kale ambacho kina habari hususa na sahihi za kihistoria? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?
[Blabu katika ukurasa wa 5]
“Habari za mfuatano wa matukio na za kijiografia zilizo katika Biblia ni sahihi kabisa na ni zenye kutegemeka kuliko zile zinazotolewa na hati nyingine zozote za kale.”—KITABU A SCIENTIFIC INVESTIGATION OF THE OLD TESTAMENT, CHA ROBERT D. WILSON
[Picha katika ukurasa wa 5]
Hati yA Babiloni inayomtaja Mfalme Yehoyakini wa Yuda
[Picha Hisani katika ukurasa wa 5]
© bpk, Berlin/Vorderasiatisches Museum, SMB/Olaf M. Tessmer/Art Resource, NY
-
-
Sahihi KisayansiMnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
Sahihi Kisayansi
“Je, kufikia sasa sikukuandikia mashauri na ujuzi, nikuonyeshe ukweli wa maneno ya kweli, ili urudishe maneno yaliyo kweli.”—METHALI 22:20, 21.
BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Vitabu vya kale vina habari zisizotegemeka na mawazo hatari ambayo sayansi ya kisasa imethibitisha kuwa ni ya uwongo. Hata leo, waandishi wengi wanalazimika kubadili habari zilizo katika vitabu vyao ili zipatane na uvumbuzi wa kisasa. Lakini Biblia inadai kwamba ilitungwa na Muumba na Neno lake “linadumu milele.”—1 Petro 1:25.
MFANO: Sheria ya Musa iliwaamuru Waisraeli wachimbe na kufunika mavi yao “nje ya kambi.” (Kumbukumbu la Torati 23:12, 13) Ikiwa wangegusa mnyama au mwanadamu aliyekufa, Waisraeli walipaswa kujisafisha kwa maji. (Mambo ya Walawi 11:27, 28; Hesabu 19:14-16) Watu waliokuwa na ugonjwa wa ukoma walitengwa hadi uchunguzi wa kitiba ulipothibitisha kwamba hawangewaambukiza watu wengine.—Mambo ya Walawi 13:1-8.
MAMBO AMBAYO TIBA YA KISASA IMETHIBITISHA: Kuondoa kinyesi kwa njia inayofaa, kunawa mikono, na kutenga wagonjwa bado ndiyo njia bora ya kupambana na magonjwa. Ikiwa hakuna vyoo karibu au mfumo wa kuondoa maji machafu na takataka, Vituo vya Kudhibiti Magonjwa ya Kuambukiza vya Marekani (CDC) vinatoa ushauri huu: “Funika mavi angalau mita 30 hivi kutoka mahali penye maji.” Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, watu wanapohakikisha kwamba wanaondoa kinyesi kwa njia inayofaa, wanapunguza magonjwa ya kuharisha kwa asilimia 36. Miaka isiyozidi 200 iliyopita, madaktari waligundua kwamba waliwaambukiza wagonjwa wengi wakati walipowagusa kabla ya kunawa mikono baada ya kugusa maiti. CDC inasema kwamba kunawa mikono ndiyo “njia pekee iliyo na matokeo zaidi katika kuzuia kusambaa kwa magonjwa.” Vipi kuhusu kuwatenga watu walio na ukoma au magonjwa mengine? Hivi karibuni, jarida linaloitwa Saudi Medical Journal lilisema hivi: “Janga la ugonjwa wa kuambukiza linapokumba eneo fulani, mbinu pekee ya kuzuia kusambaa kwa ugonjwa huo ni kuwatenga watu ambao tayari wameambukizwa.”
UNA MAONI GANI? Je, ungetazamia kitabu kingine chochote kitakatifu na cha kale kiwe na habari zinazopatana na sayansi ya kisasa? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?
“Ni jambo lenye kuvutia kusoma mambo yanayohusu usafi yaliyofuatwa wakati wa Sheria ya Musa.”—KITABU MANUAL OF TROPICAL MEDICINE, CHA DAKT. ALDO CASTELLANI NA DAKT. ALBERT J. CHALMERS
-
-
Kitabu Chenye UpatanoMnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
Kitabu Chenye Upatano
“Unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.”—2 PETRO 1:21.
BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Mara nyingi, hati za kale hazipatani hata iwe ziliandikwa wakati uleule.Vitabu ambavyo vimeandikwa na watu mbalimbali, wakiwa mahali tofauti, na wakati tofauti-tofauti huwa havipatani katika sehemu zote. Hata hivyo, Biblia inadai kwamba vitabu vyake vyote 66 vilitungwa na Mtu mmoja, hivyo vina ujumbe unaopatana.—2 Timotheo 3:16.
MFANO: Musa, mchungaji aliyeishi katika karne ya 16 K.W.K., aliandika katika kitabu cha kwanza cha Biblia kwamba kuna “uzao” ambao ungekuja kuokoa wanadamu. Baadaye, kitabu hicho kilitabiri kwamba uzao huo ungetokana na ukoo wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo. (Mwanzo 3:15; 22:17, 18; 26:24; 28:14) Miaka 500 hivi baadaye, nabii Nathani alifunua kuwa uzao huo ungetokea katika ukoo wa kifalme wa Daudi. (2 Samweli 7:12) Miaka elfu moja baadaye, mtume Paulo alieleza kwamba uzao huo ungetia ndani Yesu na kikundi cha wafuasi wake waliochaguliwa. (Waroma 1:1-4; Wagalatia 3:16, 29) Hatimaye, kufikia mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., kitabu cha mwisho katika orodha ya Biblia kilitabiri kwamba washiriki wa ule uzao wangetoa ushahidi kumhusu Yesu duniani, wainuliwe hadi mbinguni, na kutawala pamoja naye kwa miaka 1,000. Uzao huo utamharibu Ibilisi na kuokoa wanadamu.—Ufunuo 12:17; 20:6-10.
MAONI YA WACHAMBUZI WA BIBLIA: Baada ya kuchunguza kwa kina vitabu vyote 66 vya Biblia, Louis Gaussen aliandika kwamba alishangazwa na “upatano wa ajabu wa vitabu hivyo, ambavyo viliandikwa katika kipindi cha miaka 1,500 na waandikaji wengi, . . . ambao walijaribu kutimiza lengo moja, na wakaendelea kufunua mambo kwa utaratibu fulani, ingawa wao wenyewe hawakuelewa kwa ukamili, yaani, historia ya ukombozi wa ulimwengu kupitia Mwana wa Mungu.”—Theopneusty—The Plenary Inspiration of the Holy Scriptures.
UNA MAONI GANI? Je, Ungetazamia kitabu kilichoandikwa kwa kipindi cha zaidi ya miaka 1,500 na waandikaji tofauti-tofauti wapatao 40 kiwe na upatano kamili? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?
“Maandishi haya yanapounganishwa, yanafanyiza kitabu kimoja . . . Hakuna kitabu kingine chochote ulimwenguni kinachoweza kulinganishwa nacho.”—KITABU THE PROBLEM OF THE OLD TESTAMENT, CHA JAMES ORR
-
-
Biblia Ina Manufaa Hata LeoMnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
Biblia Ina Manufaa Hata Leo
“Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.”—ZABURI 119:105.
BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Vitabu vingine vinaweza kuonekana kwamba vimeandikwa kwa ustadi, lakini havifai kutoa mwongozo maishani. Pia, vitabu vya kisasa vya kutoa maelekezo vinahitaji kufanyiwa marekebisho mara kwa mara. Kwa upande mwingine, Biblia inadai kwamba “mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi.”—Waroma 15:4.
MFANO: Ingawa haikuandikwa kwa kusudi la kutoa mwongozo wa kitiba, Biblia ina mapendekezo yanayofaa kuhusu jinsi ya kuwa na afya nzuri na hisia zinazofaa. Kwa mfano, inasema kwamba “moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.” (Methali 14:30) Biblia pia inaonya hivi: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” (Methali 18:1) Vilevile, inasema kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
MAMBO AMBAYO UTAFITI UMEFUNUA: Utulivu, urafiki mzuri, na ukarimu unaweza kuboresha afya yako. Gazeti The Journal of the American Medical Association linasema hivi: “Wanaume wanaopandwa na hasira haraka wako katika hatari mara mbili zaidi ya kupatwa na ugonjwa wa kupooza kuliko wanaume wanaoweza kudhibiti hasira yao.” Utafiti uliofanywa kwa miaka kumi nchini Australia ulionyesha kwamba wazee ambao “wana marafiki wa karibu na pia watu wanaowaeleza mambo yao ya siri,” wanaweza kuishi kwa muda mrefu zaidi. Na katika mwaka wa 2008, watafiti nchini Kanada na Marekani waligundua kwamba “kutumia pesa kuwasaidia wengine hufanya mtu awe na furaha zaidi kuliko kutumia pesa kujinufaisha mwenyewe.”
UNA MAONI GANI? Je, unaweza kutumaini ushauri wa kitiba kutoka katika kitabu kilichoandikwa karibu miaka 2,000 iliyopita? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?
[Blabu katika ukurasa wa 8
“Ninavutiwa sana na Biblia . . . kwa sababu ina ushauri mzuri wa kitiba.”—HOWARD KELLY, M.D., MMOJA WA WAANZILISHI WA KITENGO CHA KITIBA KATIKA CHUO KIKUU CHA THE JOHNS HOPKINS
-