Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Utasimamaje Mbele ya Kiti cha Hukumu?
    Mnara wa Mlinzi—1995 | Oktoba 15
    • Utasimamaje Mbele ya Kiti cha Hukumu?

      “Wakati Mwana wa binadamu awasilipo katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu.”—MATHAYO 25:31, NW.

      1-3. Tuna sababu gani ya kuwa na matazamio mazuri juu ya haki?

      ‘UNA HATIA AU HUNA HATIA?’ Wengi hushangaa wasikiapo ripoti kuhusu kesi fulani za mahakamani. Mahakimu na washiriki wa baraza la kuhukumu wanaweza kujaribu kuwa wafuatiaji haki, lakini je, kweli haki hushinda? Je, hujasikia juu ya ukosefu wa haki na kuonyesha upendeleo katika mfumo wa kihukumu? Ukosefu huo wa haki si jambo jipya, kama tuonavyo katika kielezi cha Yesu kinachopatikana katika Luka 18:1-8, NW.

      2 Hata uwe umepata maono gani juu ya haki ya kibinadamu, ona umalizio wa Yesu: “Je, Mungu hatasababisha haki ifanywe kwa ajili ya wachaguliwa wake ambao wampaazia kilio mchana na usiku . . . ? Mimi nawaambia, Yeye atasababisha haki ifanywe kwao kasi. Hata hivyo, Mwana wa binadamu awasilipo, je, kwa kweli atapata imani duniani?”

      3 Ndiyo, Yehova atahakikisha kwamba hatimaye watumishi wake wapata haki. Pia Yesu anahusika, hasa sasa kwa sababu tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo mwovu wa sasa. Karibuni Yehova atatumia Mwana wake mwenye nguvu kuondoa kabisa uovu duniani. (2 Timotheo 3:1; 2 Wathesalonike 1:7, 8; Ufunuo 19:11-16) Twaweza kupata ufahamu wenye kina wa fungu la Yesu kutokana na kimoja cha vielezi vya mwisho alivyotoa, ambacho mara nyingi huitwa mfano wa kondoo na mbuzi.

      4. Tumeelewaje wakati wa utimizo wa mfano wa kondoo na mbuzi, lakini kwa nini tuchunguze mfano huu sasa? (Mithali 4:18)

      4 Kwa muda mrefu tumeelewa kwamba mfano huu ulionyesha Yesu akiketi akiwa Mfalme katika 1914 na tangu wakati huo akitoa hukumu—uhai udumuo milele kwa watu wanaothibitika kuwa wenye mfano wa kondoo, na kifo kidumucho milele kwa wenye mfano wa mbuzi. Lakini kuchunguza tena mfano huu kwaonyesha uelewevu uliorekebishwa juu ya wakati unapotimizwa na kile unachofananisha. Usahihisho huu unaimarisha umaana wa kazi yetu ya kuhubiri na umuhimu wa itikio la watu. Ili kuona msingi wa uelewevu huu wenye kina zaidi wa huu mfano, ebu tuchunguze kile Biblia huonyesha kuhusu Yehova na Yesu, wote wakiwa Wafalme na vilevile Mahakimu.

      Yehova Akiwa Hakimu Mkuu

      5, 6. Kwa nini yafaa kumwona Yehova kuwa Mfalme na Hakimu vilevile?

      5 Yehova atawala ulimwengu wote mzima kwa uwezo juu ya wote. Bila kuwa na mwanzo wala mwisho, yeye ni “Mfalme wa milele.” (1 Timotheo 1:17; Zaburi 90:2, 4; Ufunuo 15:3) Ana mamlaka ya kufanyiza amri, au sheria, na kuzitekeleza. Lakini mamlaka yake yatia ndani kuwa Hakimu. Isaya 33:22 lasema: “BWANA ndiye mwamuzi [“hakimu,” NW] wetu; BWANA ndiye mfanya sheria wetu; BWANA ndiye mfalme wetu; ndiye atakayetuokoa.”

      6 Kwa muda mrefu watumishi wa Mungu wamemtambua Yehova kuwa Hakimu wa kesi na masuala. Kwa kielelezo, baada ya “Mhukumu [wa] ulimwengu wote” kupima uthibitisho kuhusu uovu wa Sodoma na Gomora, alitoa hukumu kwamba wakazi hao walistahili kuharibiwa naye vilevile akatekeleza hukumu hiyo ya uadilifu. (Mwanzo 18:20-33; Ayubu 34:10-12) Tunapaswa kufarijika kama nini kujua kwamba Yehova ni Hakimu mwadilifu awezaye sikuzote kutekeleza hukumu zake!

      7. Yehova alitendaje akiwa Hakimu aliposhughulika na Israeli?

      7 Katika Israeli la kale, nyakati nyingine Yehova alitoa hukumu moja kwa moja. Je, usingefarijika huko nyuma kujua kwamba Hakimu mkamilifu alikuwa akiamua mambo? (Mambo ya Walawi 24:10-16; Hesabu 15:32-36; 27:1-11) Pia Mungu aliandaa “maamuzi ya kihukumu” yaliyofaa kutumiwa yakiwa viwango vya kuhukumu. (Mambo ya Walawi 25:18, 19, NW; Nehemia 9:13, NW; Zaburi 19:9, 10; 119:7, 75, 164; 147:19, 20; NW) Yeye ni “Hakimu wa dunia yote,” kwa hiyo sisi sote tunahusika.—Waebrania 12:23, NW.

      8. Danieli aliona ono gani linalohusika?

      8 Tuna uthibitisho wa “mashahidi waliojionea” jambo hili. Nabii Danieli alipewa ono la mahayawani wakali waliowakilisha serikali au milki mbalimbali. (Danieli 7:1-8, 17) Yeye aliongezea: “Viti vya ufalme viliwekwa na Mkale wa Siku akaketi. Mavazi yake yalikuwa meupe kama theluji.” (Danieli 7:9, NW) Ona kwamba Danieli aliona viti vya ufalme “na Mkale wa Siku [Yehova] akaketi.” Jiulize, ‘Je, hapa Danieli alikuwa akishuhudia kule kuwa Mfalme kwa Mungu?’

      9. Maana moja ya ‘kuketi’ katika kiti cha ufalme ni nini? Toa vielelezo.

      9 Tusomapo kwamba mtu ‘ameketi’ katika kiti cha ufalme, twaweza kufikiri kwamba anakuwa mfalme, kwa sababu nyakati nyingine Biblia hutumia lugha hiyo. Kwa kielelezo: “[Zimri] alipoanza kutawala, mara tu alipoketi juu ya kiti chake cha ufalme, yeye . . .” (1 Wafalme 16:11, NW; 2 Wafalme 10:30; 15:12; Yeremia 33:17) Unabii wa kimesiya ulisema hivi: “Ni lazima aketi na kutawala katika kiti chake cha ufalme.” Kwa hiyo, ‘kuketi katika kiti cha ufalme’ kwaweza kumaanisha kuwa mfalme. (Zekaria 6:12, 13, NW) Yehova anafafanuliwa kuwa Mfalme aketiye katika kiti cha ufalme. (1 Wafalme 22:19; Isaya 6:1; Ufunuo 4:1-3) Yeye ni “Mfalme wa milele.” Lakini, alipoonyesha upande mpya wa enzi kuu, angeweza kusemwa kuwa amekuwa Mfalme, kana kwamba anaketi upya katika kiti chake cha ufalme.—1 Mambo ya Nyakati 16:1, 31; Isaya 52:7; Ufunuo 11:15-17; 15:3; 19:1, 2, 6.

      10. Kazi kubwa ya wafalme wa Israeli ilikuwa nini? Toa kielezi.

      10 Lakini, hili ndilo jambo kuu: Kazi kubwa ya wafalme wa kale ilikuwa ile ya kusikiliza kesi na kutoa hukumu. (Mithali 20:8; 29:14) Kumbuka hukumu yenye hekima ya Sulemani wanawake wawili walipodai kuwa mama wa yule mtoto mmoja. (1 Wafalme 3:16-28; 2 Mambo ya Nyakati 9:8) Mojayapo majengo yake ya kiserikali lilikuwa “baraza ya kiti cha enzi [“ufalme,” NW], ili ahukumu ndani yake,” lililoitwa pia “baraza ya hukumu.” (1 Wafalme 7:7) Yerusalemu lilifafanuliwa kuwa mahali “vili[po]wekwa viti vya hukumu.” (Zaburi 122:5) Kwa wazi, ‘kuketi katika kiti cha ufalme’ kwaweza kumaanisha pia kutekeleza mamlaka ya kihukumu.—Kutoka 18:13; Mithali 20:8.

      11, 12. (a) Ni nini kilichokuwa maana ya kuketi kwa Yehova, kunakotajwa katika Danieli sura ya 7? (b) Maandiko mengine yathibitishaje kwamba Yehova aketi ili kuhukumu?

      11 Sasa ebu turudie ile mandhari ambayo Danieli aliona ‘Mkale wa Siku akiketi.’ Danieli 7:10, (NW) laongezea hivi: “Mahakama ikaketi, na kulikuwa na vitabu vilivyofunguliwa.” Ndiyo, Mkale wa Siku aliketi kutoa hukumu juu ya utawala wa ulimwengu na pia kuhukumu Mwana wa binadamu kuwa anastahili kutawala. (Danieli 7:13, 14) Kisha twasoma kwamba “Mkale wa Siku alikuja na hukumu yenyewe ikatolewa kwa upendeleo wa watakatifu,” wale waliohukumiwa kuwa wenye kustahili kutawala na Mwana wa binadamu. (Danieli 7:22, NW) Hatimaye “Mahakama yenyewe ikaketi” na kutoa hukumu kali juu ya mamlaka ya mwisho ya ulimwengu.—Danieli 7:26, NW.a

      12 Basi, kwa Danieli kumwona Mungu ‘akiketi katika kiti cha ufalme’ kulimaanisha kuja Kwake kutoa hukumu. Mapema zaidi Daudi aliimba: “[Wewe Yehova] umenifanyia hukumu na haki; umeketi kitini pa enzi [“ufalme,” NW] ukihukumu kwa haki.” (Zaburi 9:4, 7) Na Yoeli aliandika: “Mataifa na wajihimize, wakapande juu katika bonde la Yehoshafati; maana huko ndiko [mimi Yehova] nitakakoketi niwahukumu mataifa yote.” (Yoeli 3:12; linganisha Isaya 16:5.) Yesu na Paulo vilevile walikuwa katika hali za kihukumu ambamo mwanadamu fulani aliketi ili kusikiza kesi na kutoa hukumu.b—Yohana 19:12-16; Matendo 23:3; 25:6.

      Cheo cha Yesu

      13, 14. (a) Watu wa Mungu walikuwa na uhakikishio gani kwamba Yesu angekuja kuwa Mfalme? (b) Ni lini Yesu aliketi katika kiti chake cha ufalme, na ni katika maana gani alitawala tangu 33 W.K. na kuendelea?

      13 Yehova ni Mfalme na Hakimu vilevile. Vipi Yesu? Malaika atangazaye kuzaliwa kwake alisema: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, . . . na kutakuwa hakuna mwisho wa ufalme wake.” (Luka 1:32, 33, NW) Yesu angekuwa mrithi wa daima wa ufalme wa Kidaudi. (2 Samweli 7:12-16) Angetawala kutoka mbinguni, kwa kuwa Daudi alisema: “Neno la BWANA kwa Bwana wangu [Yesu], Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako. BWANA atainyosha toka Sayuni fimbo ya nguvu zako. [Akisema] Uwe na enzi kati ya adui zako.”—Zaburi 110:1-4.

      14 Hilo lingetukia lini? Yesu hakutawala akiwa Mfalme alipokuwa binadamu. (Yohana 18:33-37) Katika 33 W.K., alikufa, akafufuliwa, akapaa mbinguni. Waebrania 10:12 lasema: “Huyu, alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu.” Yesu alikuwa na mamlaka gani? “[Mungu] [ali]mketisha kwenye mkono wake wa kuume katika mahali pa kimbingu, juu zaidi sana kuliko kila serikali na mamlaka na nguvu na ubwana . . . na kumfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko.” (Waefeso 1:20-22, NW) Kwa sababu wakati huo Yesu alikuwa na mamlaka ya kifalme juu ya Wakristo, Paulo aliandika kwamba Yehova “alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake.”—Wakolosai 1:13; 3:1.

      15, 16. (a) Kwa nini tunasema kwamba Yesu hakuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu katika 33 W.K.? (b) Ni lini Yesu alianza kutawala katika Ufalme wa Mungu?

      15 Hata hivyo, wakati huo Yesu hakutenda akiwa Mfalme na Hakimu juu ya mataifa. Alikuwa ameketi kando ya Mungu, akingojea wakati wa kutenda akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Paulo aliandika hivi juu yake: “Je! yuko malaika aliyemwambia wakati wo wote, Uketi mkono wangu wa kuume hata nitakapoweka adui zako chini ya nyayo zako?”—Waebrania 1:13.

      16 Mashahidi wa Yehova wamechapisha uthibitisho mwingi kwamba kipindi cha Yesu cha kungojea kiliisha 1914, alipokuja kuwa mtawala wa Ufalme wa Mungu katika mbingu zisizoonekana. Ufunuo 11:15, 18 lasema: “Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.” “Na mataifa walikasirika, hasira yako nayo ikaja.” Ndiyo, mataifa yalionyeshana ghadhabu katika Vita ya Ulimwengu 1. (Luka 21:24) Vita, matetemeko ya dunia, magonjwa ya kuambukiza, upungufu wa chakula, na mambo kama hayo, ambayo tumeona tangu 1914 yathibitisha kwamba Yesu anatawala sasa katika Ufalme wa Mbinguni, na mwisho kabisa wa ulimwengu u karibu.—Mathayo 24:3-14, NW.

      17. Ni mambo gani makuu ambayo tumethibitisha kufikia sasa?

      17 Kwa kupitia kifupi: Mungu aweza kusemwa kuwa ameketi katika kiti cha ufalme akiwa Mfalme, lakini kwa maana nyingine anaweza kuketi katika kiti chake cha ufalme ili kuhukumu. Katika 33 W.K., Yesu aliketi upande wa kuume wa Mungu, naye sasa ni Mfalme wa Ufalme. Lakini, je, Yesu, anayetawala sasa akiwa Mfalme, pia atumika akiwa Hakimu? Na kwa nini jambo hili lituhusu, hasa wakati huu?

      18. Kuna uthibitisho gani kwamba Yesu angekuwa Hakimu pia?

      18 Yehova, ambaye ana haki ya kuweka rasmi mahakimu, alimchagua Yesu kuwa Hakimu anayefikia viwango Vyake. Yesu alionyesha hilo alipokuwa akisema juu ya watu kuwa hai kiroho: “Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu yote.” (Yohana 5:22) Lakini, fungu la Yesu la kihukumu lapita aina hiyo ya hukumu, kwani yeye ni hakimu wa walio hai na wafu. (Matendo 10:42; 2 Timotheo 4:1) Pindi moja Paulo alitangaza: “[Mungu] ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule [Yesu] aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.”—Matendo 17:31; Zaburi 72:2-7.

      19. Kwa nini ni sahihi kusema juu ya Yesu kuwa anaketi akiwa Hakimu?

      19 Basi, je, tuna haki ya kukata kauli kwamba Yesu aketi katika kiti cha ufalme chenye utukufu katika fungu hususa la Hakimu? Ndiyo. Yesu aliwaambia mitume: “Katika uumbaji-upya wakati Mwana wa binadamu aketipo juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu, nyinyi ambao mmenifuata mtaketi nyinyi wenyewe pia juu ya viti vya ufalme kumi na viwili, mkihukumu yale makabila kumi na mawili ya Israeli.” (Mathayo 19:28, NW) Ingawa Yesu sasa ni Mfalme wa Ufalme, utendaji wake wa ziada unaotajwa katika Mathayo 19:28 utatia ndani kuketi katika kiti cha ufalme ili kuhukumu katika Mileani. Wakati huo atahukumu wanadamu wote, waadilifu na wasio waadilifu. (Matendo 24:15) Yafaa kukumbuka hili tugeuziapo fikira zetu mmojawapo mifano ya Yesu unaohusu wakati wetu na maisha zetu.

      Mfano Huu Wasema Nini?

      20, 21. Mitume wa Yesu waliuliza nini kinachohusu wakati wetu, kikitokeza swali gani?

      20 Muda mfupi kabla ya Yesu kufa, mitume wake walimwuliza hivi: “Mambo haya yatakuwa wakati gani, nayo ni nini itakuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3, NW) Yesu alitabiri matukio muhimu ambayo yangetokea duniani kabla ya ‘mwisho kuja.’ Muda mfupi kabla ya mwisho huo, mataifa “yatamwona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbinguni na nguvu na utukufu mkubwa.”—Mathayo 24:14, 29, 30, NW.

      21 Lakini, itakuwaje kwa watu katika mataifa hayo Mwana wa binadamu afikapo katika utukufu wake? Ebu tuone kutokana na mfano wa kondoo na mbuzi, unaoanza kwa maneno haya: “Wakati Mwana wa binadamu awasilipo katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanywa mbele yake.”—Mathayo 25:31, 32, NW.

      22, 23. Ni mambo yapi yaonyeshayo kwamba mfano wa kondoo na mbuzi haukuanza kutimizwa katika 1914?

      22 Je, mfano huu unahusu wakati Yesu alipoketi katika mamlaka ya kifalme katika 1914, kama ambavyo tumeelewa kwa muda mrefu? Naam, Mathayo 25:34 lasema juu yake akiwa Mfalme, kwa hiyo kwa kupatana na akili mfano huu wahusu tangu wakati Yesu alipokuwa Mfalme katika 1914. Lakini ni hukumu gani aliyofanya upesi baadaye? Haikuwa hukumu ya “mataifa yote.” Badala ya hivyo, alielekeza uangalifu wake kwa wale wanaodai kufanyiza “nyumba ya Mungu.” (1 Petro 4:17, italiki ni zetu.) Kwa kupatana na Malaki 3:1-3, Yesu, akiwa mjumbe wa Yehova, alikagua kihukumu Wakristo watiwa-mafuta waliosalia duniani. Pia ulikuwa wakati wa kutoa adhabu ya kihukumu juu ya Jumuiya ya Wakristo, waliodai kwa uwongo kuwa “nyumba ya Mungu.”c (Ufunuo 17:1, 2; 18:4-8) Lakini hakuna chochote kionyeshacho kwamba wakati huo, au tangu wakati huo, Yesu aliketi ili kuhukumu watu wa mataifa yote hatimaye kuwa kondoo au mbuzi.

      23 Tukichanganua utendaji wa Yesu katika mfano huu, twamwona hatimaye akihukumu mataifa yote. Mfano huu hauonyeshi kwamba kuhukumu huko kungeendelea kwa kipindi kirefu cha miaka mingi, kana kwamba kila mtu aliyekufa katika miongo hii ambayo imepita alihukumiwa kustahili kifo kidumucho milele au uhai udumuo milele. Yaonekana kwamba wengi ambao wamekufa katika miongo ya majuzi wameenda katika kaburi la kawaida la wanadamu. (Ufunuo 6:8; 20:13) Hata hivyo, huu mfano waonyesha wakati ambapo Yesu ahukumu watu wa “mataifa yote” ambao wakati huo wako hai na wanakabili utekelezaji wa adhabu yake ya kihukumu.

      24. Ni lini mfano wa kondoo na mbuzi utakapotimizwa?

      24 Kwa maneno mengine, mfano huu waelekezea wakati ujao ambapo Mwana wa binadamu atakuja katika utukufu wake. Ataketi ili kuhukumu watu wanaoishi wakati huo. Hukumu yake itategemea kile ambacho wamejidhihirisha wenyewe kuwa. Wakati huo ‘upambanuzi kati ya wenye haki na waovu’ utakuwa umethibitishwa wazi. (Malaki 3:18) Kule kutangaza hasa na kutekeleza hukumu kutafanywa kwa kipindi kifupi. Yesu atatoa maamuzi yenye haki yanayotegemea yale ambayo watu mmoja-mmoja watakuwa wamedhihirisha wazi.—Ona pia 2 Wakorintho 5:10.

      25. Mathayo 25:31 laonyesha nini likisema juu ya Mwana wa binadamu akiketi katika kiti cha utukufu?

      25 Basi, hii yamaanisha kwamba ‘kuketi kwa Yesu katika kiti chake cha utukufu’ ili kutoa hukumu, kunakotajwa katika Mathayo 25:31, kwahusu wakati ujao wakati Mfalme huyu mwenye nguvu atakapoketi kutangaza na kutekeleza hukumu dhidi ya mataifa. Ndiyo, mandhari ya hukumu inayohusu Yesu katika Mathayo 25:31-33, 46 yalingana na mandhari iliyo katika Danieli sura ya 7, ambamo Mfalme anayetawala, Mkale wa Siku, aliketi ili kutekeleza fungu lake akiwa Hakimu.

      26. Ni maelezo gani mapya ya huu mfano yanayodhihirika?

      26 Kuelewa huu mfano wa kondoo na mbuzi kwa njia hii kwaonyesha kwamba kutoa hukumu juu ya kondoo na mbuzi ni kwa wakati ujao. Kutatokea baada ya “dhiki” inayotajwa katika Mathayo 24:29, 30 kufyatuka na Mwana wa binadamu ‘kufika katika utukufu wake.’ (Linganisha Marko 13:24-26, NW.) Ndipo, mfumo huu wote ukiwa umefikia mwisho wao, Yesu atafanya mahakama na kutoa na kutekeleza hukumu.—Yohana 5:30; 2 Wathesalonike 1:7-10.

      27. Tunapaswa kupendezwa kujua nini kuhusu mfano wa mwisho wa Yesu?

      27 Hili lasahihisha uelewevu wetu juu ya wakati wa utimizo wa mfano wa Yesu, unaoonyesha wakati kondoo na mbuzi watakapohukumiwa. Lakini hilo latuhusuje sisi tunaohubiri kwa bidii habari njema ya Ufalme? (Mathayo 24:14) Je, hilo lafanya kazi yetu isiwe na umaana zaidi, au laleta daraka kubwa zaidi? Ebu tuone katika makala ifuatayo jinsi tunavyohusika.

  • Kuna Wakati Ujao Gani kwa Kondoo na Mbuzi?
    Mnara wa Mlinzi—1995 | Oktoba 15
    • Kuna Wakati Ujao Gani kwa Kondoo na Mbuzi?

      “Atatenganisha watu, kama vile mchungaji atenganishavyo kondoo na mbuzi.”—MATHAYO 25:32, NW.

      1, 2. Kwa nini mfano wa kondoo na mbuzi utupendeze?

      HAKIKA Yesu Kristo alikuwa Mwalimu mkubwa kupita wote duniani. (Yohana 7:46) Mojayapo njia zake za kufundisha ilikuwa kutumia mifano, au vielezi. (Mathayo 13:34, 35) Mifano hiyo ilikuwa sahili lakini yenye nguvu sana katika kujulisha kweli za ndani za kiroho na za kiunabii.

      2 Katika mfano wa kondoo na mbuzi, Yesu alielekezea wakati wake wa kutenda katika fungu la kipekee: “Wakati Mwana wa binadamu awasilipo katika utukufu wake, na . . . ” (Mathayo 25:31, NW) Hili lapaswa litupendeze kwa sababu hicho ndicho kielezi ambacho Yesu amalizia katika kujibu lile swali: “Ni nini itakuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3, NW) Lakini hili lamaanisha nini kwetu?

      3. Mapema katika maneno yake, Yesu alisema nini kingetukia mara tu baada ya dhiki kubwa kuanza?

      3 Yesu alitabiri matukio makubwa ambayo yangetukia “mara baada ya” kufyatuka kwa dhiki kubwa, matukio tunayongoja. Alisema kwamba ndipo “ishara ya Mwana wa binadamu” itatokea. Hili litaathiri kabisa “makabila yote ya dunia” ambayo “yatamwona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbinguni na nguvu na utukufu mkubwa.” Mwana wa binadamu ataandamana na “malaika zake.” (Mathayo 24:21, 29-31, NW)a Vipi juu ya mfano wa kondoo na mbuzi? Biblia za kisasa huuweka katika sura ya 25, lakini huo ni sehemu ya jibu la Yesu, ukieleza mambo mengine zaidi kuhusu kuja kwake katika utukufu na kukazia hukumu yake juu ya “mataifa yote.”—Mathayo 25:32, NW.

      Wahusika Katika Huu Mfano

      4. Mfano wa kondoo na mbuzi wataja nini mwanzoni kuhusu Yesu, na ni nani pia wanaotajwa?

      4 Yesu aanza huu mfano kwa kusema: “Wakati Mwana wa binadamu awasilipo.” Yaelekea unajua “Mwana wa binadamu” ni nani. Waandikaji wa Gospeli mara nyingi walitumia usemi huo kumhusu Yesu. Hata Yesu mwenyewe aliutumia hivyo, bila shaka akikumbuka ono la Danieli la “mtu kama mwana wa binadamu” akimwendea Mkale wa Siku ili kupokea “utawala na heshima na ufalme.” (Danieli 7:13, 14, NW; Mathayo 26:63, 64, NW; Marko 14:61, 62, NW) Ingawa Yesu ndiye mhusika-mkuu katika mfano huu, hayuko peke yake. Mapema katika maneno yake, kama yalivyonukuliwa katika Mathayo 24:30, 31, alisema kwamba Mwana wa binadamu ‘ajapo na nguvu na utukufu mkubwa,’ malaika zake watatimiza fungu muhimu. Vivyo hivyo, mfano wa kondoo na mbuzi waonyesha malaika wakiwa na Yesu aketipo ‘juu ya kiti cha ufalme chenye utukufu’ ili kuhukumu. (Linganisha Mathayo 16:27.) Lakini Hakimu na malaika zake wako mbinguni, basi, je, wanadamu wanazungumzwa katika huu mfano?

      5. Tunaweza kutambulishaje “ndugu” za Yesu?

      5 Kutazama huu mfano kwafunua vikundi vitatu tunavyohitaji kutambulisha. Mbali na kondoo na mbuzi, Mwana wa binadamu aongezea kikundi cha tatu ambacho kitambulisho chacho ni muhimu sana katika kutambulisha kondoo na mbuzi. Yesu akiita hiki kikundi cha tatu ndugu zake wa kiroho. (Mathayo 25:40, 45) Ni lazima wawe waabudu wa kweli, kwa kuwa Yesu alisema: “Ye yote atakayefanya mapenzi ya Baba yangu . . ., huyu ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu.” (Mathayo 12:50; Yohana 20:17) Kihususa, Paulo aliandika juu ya Wakristo walio sehemu ya “mbegu ya Abrahamu” na ambao ni wana wa Mungu. Yeye aliwaita hawa “ndugu” za Yesu na “washiriki wa wito wa kimbingu.”—Waebrania 2:9–3:1, NW; Wagalatia 3:26, 29, NW.

      6. Ni nani walio “wadogo zaidi sana” wa ndugu za Yesu?

      6 Kwa nini Yesu alitaja ‘mdogo zaidi sana’ wa ndugu zake? Maneno hayo yarudia maneno yale mitume walimsikia akisema hapo awali. Alipokuwa akilinganisha Yohana Mbatizaji, aliyekufa kabla ya Yesu na hivyo kuwa na tumaini la kidunia, pamoja na wale wanaopata uhai wa kimbingu, Yesu alisema: “Hakujainuliwa mkubwa zaidi ya Yohana Mbatizaji; lakini mtu ambaye ni mdogo zaidi katika ufalme wa mbingu ni mkubwa zaidi kuliko yeye.” (Mathayo 11:11, NW) Wengine wanaoenda mbinguni huenda walikuwa mashuhuri katika kutaniko, kama vile mitume, na wengine wakiwa si mashuhuri hivyo, lakini wote ni ndugu za Yesu wa kiroho. (Luka 16:10; 1 Wakorintho 15:9; Waefeso 3:8; Waebrania 8:11) Hivyo, hata kama wengine walionekana kuwa hawana umashuhuri duniani, wao walikuwa ndugu zake nao wangalipaswa kutendewa hivyo.

      Ni Nani Walio Kondoo na Mbuzi?

      7, 8. Yesu alisema nini kuhusu kondoo, basi tunaweza kukata kauli gani kuwahusu?

      7 Twasoma kuhusu kuhukumiwa kwa kondoo: “[Yesu] atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu [“tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu,” NW]; kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika; nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia. Ndipo wenye haki [“waadilifu,” “NW”] watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? ni lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia? Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo [“zaidi sana,” NW], mlinitendea mimi.”—Mathayo 25:34-40, italiki ni zetu.

      8 Kwa wazi, kondoo wanaohukumiwa kustahili kuwa upande wa kuume wa Yesu wa heshima na upendeleo wanawakilisha jamii fulani ya wanadamu. (Waefeso 1:20; Waebrania 1:3) Wao walifanya nini na lini? Yesu alisema kwamba kwa fadhili, staha, na ukarimu, walimlisha, wakamnywesha, na kumvika, wakimsaidia alipokuwa mgonjwa au alipokuwa gerezani. Kondoo wasemapo kwamba hawakuwa wamefanya hivyo kwa Yesu binafsi, yeye asema kwamba wao waliwaunga mkono ndugu zake wa kiroho, wale mabaki wa Wakristo watiwa-mafuta, basi katika maana hiyo walimfanyia hayo.

      9. Kwa nini huu mfano hauhusu Mileani?

      9 Huu mfano hauhusu wakati wa Mileani, kwa kuwa wakati huo watiwa-mafuta hawatakuwa wanadamu wenye kupatwa na njaa, kiu, ugonjwa, au kufungwa gerezani. Lakini wengi wao wamejionea hayo katika umalizio wa mfumo huu wa mambo. Tangu Shetani atupwe duniani, amefanya mabaki kuwa shabaha yake maalumu ya ghadhabu yake, akifanya wadhihakiwe, wateswe, na kuuawa.—Ufunuo 12:17.

      10, 11. (a) Kwa nini si jambo la akili kufikiri kwamba kondoo watia ndani kila mtu atendalo tendo moja la fadhili kwa ndugu za Yesu? (b) Kwa kufaa kondoo wanawakilisha nani?

      10 Je, Yesu anasema kwamba kila mtu anayeonyesha fadhili fulani ndogo kwa mmojawapo ndugu zake, kama vile kumpa kipande cha mkate au gilasi ya maji, anastahili kuwa mmoja wa kondoo hawa? Ni kweli kwamba kuonyesha fadhili kama hizo kwaweza kuwa fadhili ya kibinadamu, lakini kwa kweli, yaonekana kuwa kuna mengi zaidi yanayohusika na kondoo wa huu mfano. Kwa kielelezo, Yesu hakuwa akirejezea wasioamini kuwapo kwa Mungu au makasisi ambao kwa kutukia waweza kufanya tendo moja la fadhili kwa mmojawapo wa ndugu zake. Kinyume cha hilo, mara mbili Yesu aliwaita kondoo “waadilifu.” (Mathayo 25:37, 46, NW) Kwa hiyo ni lazima kondoo wawe wale ambao kwa kipindi cha wakati wamesaidia—kuwaunga mkono kwa matendo—ndugu za Kristo na ambao wamedhihirisha imani kwa kadiri ya kupokea msimamo mwadilifu mbele ya Mungu.

      11 Katika karne ambazo zimepita, wengi kama vile Abrahamu wamekuwa na msimamo mwadilifu. (Yakobo 2:21-23) Noa, Abrahamu, na waaminifu wengine wanatiwa miongoni mwa “kondoo wengine” ambao wataurithi uhai katika Paradiso chini ya Ufalme wa Mungu. Katika nyakati za majuzi mamilioni zaidi wamekubali ibada ya kweli wakiwa kondoo wengine nao wamekuja kuwa “kundi moja” na watiwa-mafuta. (Yohana 10:16; Ufunuo 7:9) Hawa wenye tumaini la kidunia huwatambua ndugu za Yesu kuwa mabalozi wa Ufalme na hivyo kuwasaidia—kihalisi na kiroho. Yesu huona kana kwamba ametendewa jambo ambalo kondoo wengine hutendea ndugu zake duniani. Watu kama hao wanaokuwa wangali hai anapokuja kuhukumu mataifa watahukumiwa kuwa kondoo.

      12. Kwa nini kondoo huenda wakauliza ni jinsi gani walivyomtendea Yesu kwa fadhili?

      12 Ikiwa kondoo wengine sasa wanahubiri habari njema pamoja na watiwa-mafuta na kuwasaidia, kwa nini waulize: “Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha?” (Mathayo 25:37) Kwaweza kuwa na sababu kadhaa. Huu ni mfano tu. Kuupitia, Yesu aonyesha hangaiko lake la ndani kwa ndugu zake wa kiroho; yeye ahisi pamoja nao, akiteseka pamoja nao. Mapema Yesu alikuwa amesema: “Awapokeaye ninyi, anipokea mimi; naye anipokeaye mimi; ampokea yeye aliyenituma.” (Mathayo 10:40) Katika kielezi hiki, Yesu aendeleza kanuni hiyo, akionyesha kwamba yale yanayofanywa (mazuri au mabaya) kwa ndugu zake hufika hata mbinguni; ni kana kwamba anafanyiwa hayo mbinguni. Pia, Yesu hapa alikazia kiwango cha Yehova cha kuhukumu, akielewesha wazi kwamba hukumu ya Mungu, iwe yenye upendeleo au ya adhabu, ni ya kweli na ya haki. Mbuzi hawawezi kutoa udhuru, ‘Laiti tungalikuona wewe binafsi.’

      13. Kwa nini wenye mfano wa mbuzi huenda wakamwita Yesu “Bwana”?

      13 Mara tuelewapo wakati hukumu hiyo inayotajwa katika huu mfano inapotolewa, twafahamu kwa wazi zaidi ni nani walio mbuzi. Utimizo wao ni wakati “ishara ya Mwana wa binadamu itakapoonekana mbinguni, na ndipo makabila yote ya dunia yatakapojipiga yenyewe kwa maombolezo, nayo yatamwona Mwana wa binadamu akija . . . na nguvu na utukufu mkubwa.” (Mathayo 24:29, 30, NW) Waokokaji wa dhiki juu ya Babiloni Mkubwa ambao waliwatendea ndugu za Mfalme kwa madharau wanaweza sasa kumwita huyo Hakimu kwa mafadhaiko kuwa “Bwana,” wakitumaini kuokoa uhai wao.—Mathayo 7:22, 23; linganisha Ufunuo 6:15-17.

      14. Ni kwa msingi gani Yesu atahukumu kondoo na mbuzi?

      14 Hata hivyo, hukumu ya Yesu haitategemea madai yenye mafadhaiko ya wale waliokuwa waenda-kanisa, wasioamini kuwapo kwa Mungu, au wengine. (2 Wathesalonike 1:8) Badala ya hivyo, hakimu atachunguza hali ya moyo na matendo yaliyopita ya watu kuelekea hata ‘mmoja wa wadogo zaidi sana wa ndugu zake.’ Ni kweli kwamba idadi ya Wakristo watiwa-mafuta wanaosalia duniani inapunguka. Hata hivyo, maadamu watiwa-mafuta, wakifanyiza “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” waendeleapo kuandaa chakula na mwelekezo wa kiroho, wale wenye matazamio ya kuwa kondoo wana fursa ya kufanya mema kwa jamii ya mtumwa, kama vile ‘umati mkubwa wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha’ wamefanya.—Ufunuo 7:9, 14.

      15. (a) Wengi wamejionyeshaje kuwa kama mbuzi? (b) Kwa nini tuepuke kusema kama mtu ni kondoo au mbuzi?

      15 Ndugu za Kristo na mamilioni ya kondoo wengine ambao wameungana nao kuwa kundi moja wametendewaje? Huenda watu wengi binafsi hawajawashambulia wawakilishi wa Kristo, lakini pia hawajawatendea watu wake kwa upendo. Wakipendelea ulimwengu mwovu, watu wenye mfano wa mbuzi hukataa ujumbe wa Ufalme, iwe wausikia kwa njia ya moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja. (1 Yohana 2:15-17) Bila shaka, katika uchanganuzi wa mwisho, Yesu ndiye amewekwa rasmi kutoa hukumu. Si juu yetu kuamua ni nani walio kondoo na ni nani walio mbuzi.—Marko 2:8; Luka 5:22; Yohana 2:24, 25; Warumi 14:10-12; 1 Wakorintho 4:5.

      Kuna Wakati Ujao Gani kwa Kila Kikundi?

      16, 17. Kondoo watakuwa na wakati ujao gani?

      16 Yesu alitoa hukumu yake juu ya kondoo: “Njoni, nyinyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, rithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.” Huo ni mwaliko mchangamfu kama nini—“Njoni”! Wapate nini? Uhai udumuo milele, kama alivyoeleza katika umalizio wake: “Waadilifu [wataingia] katika uhai udumuo milele.”—Mathayo 25:34, 46, NW.

      17 Katika mfano wa talanta, Yesu alionyesha kile kinachohitajika kwa wale watakaotawala pamoja naye mbinguni, lakini katika mfano huu yeye aonyesha kile kinachotazamiwa kwa raia wa Ufalme. (Mathayo 25:14-23) Hasa, kwa sababu ya kuunga mkono kwa moyo wote ndugu za Yesu, kondoo watarithi sehemu katika makao ya kidunia ya Ufalme wake. Wao watafurahia uhai katika dunia iliyo paradiso—tazamio ambalo Mungu aliwatayarishia “tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu” wa wanadamu wawezao kukombolewa.—Luka 11:50, 51, NW.

      18, 19. (a) Yesu atatoa hukumu gani kwa mbuzi? (b) Tunaweza kuwaje na hakika kwamba mbuzi hawatakabili mateso ya milele?

      18 Hukumu itekelezwayo juu ya mbuzi ni tofauti kama nini! “Kisha atawaambia na wale walioko mkono wake wa kushoto, Ondokeni kwangu, mliolaaniwa, mwende katika moto wa milele, aliowekewa tayari Ibilisi na malaika zake; kwa maana nalikuwa na njaa, msinipe chakula; nalikuwa na kiu, msininyweshe; nalikuwa mgeni, msinikaribishe; nalikuwa uchi, msinivike; nalikuwa mgonjwa, na kifungoni, msije kunitazama. Ndipo hao pia watajibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona wewe una njaa, au una kiu, au u mgeni, au u uchi, au u mgonjwa, au u kifungoni, tusikuhudumie? Naye atawajibu, akisema, Amin, nawaambia, Kadiri msivyomtendea mmojawapo wa hao walio wadogo [“zaidi sana,” NW], hamkunitendea mimi.”—Mathayo 25:41-45.

      19 Wanafunzi wa Biblia wajua kwamba hilo haliwezi kumaanisha kwamba nafsi zisizoweza kufa za wenye mfano wa mbuzi zitateseka katika moto wa milele. La, kwa kuwa wanadamu ni nafsi; hawana nafsi zisizoweza kufa. (Mwanzo 2:7; Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4) Kwa kuhukumu mbuzi kwa “moto wa milele,” Hakimu anamaanisha uharibifu usio na tumaini la wakati ujao, ambao pia utakuwa mwisho wa daima wa Ibilisi na roho waovu wake. (Ufunuo 20:10, 14) Hivyo, Hakimu wa Yehova atoa hukumu hizo zilizo tofauti. Awaambia kondoo, “Njoni”; mbuzi, “Ondokeni kwangu.” Kondoo watarithi “uhai udumuo milele.” Mbuzi watapatwa na “kukatiliwa-mbali kudumuko milele.”—Mathayo 25:46, NW.b

      Hilo Lamaanisha Nini Kwetu?

      20, 21. (a) Wakristo wana kazi gani ya maana ya kufanya? (b) Ni mgawanyiko upi unaoendelea sasa? (c) Hali ya watu itakuwa nini wakati mfano wa kondoo na mbuzi uanzapo kutimizwa?

      20 Wale mitume wanne waliosikia jibu la Yesu kuhusu ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo walikuwa na mengi zaidi ya kufikiria. Wangehitaji kukesha na kulinda. (Mathayo 24:42) Pia wangehitaji kufanya kazi ya kutoa ushahidi inayotajwa katika Marko 13:10. Mashahidi wa Yehova wanafanya kwa bidii kazi hiyo leo.

      21 Hata hivyo, uelewevu huu mpya wa mfano wa kondoo na mbuzi wamaanisha nini kwetu? Naam, tayari watu wanachukua misimamo. Wengine wamo katika ‘barabara pana iongozayo katika uharibifu,’ huku wengine wakijaribu kudumu katika ‘barabara yenye kufinyana iongozayo katika uhai.’ (Mathayo 7:13, 14, NW) Lakini wakati ambapo Yesu atatangaza hukumu ya mwisho juu ya kondoo na mbuzi wanaoonyeshwa katika huu mfano ungali mbele. Mwana wa binadamu ajapo katika fungu la Hakimu, yeye ataamua kwamba Wakristo wengi wa kweli—hasa “umati mkubwa” wa kondoo waliojiweka wakfu—watastahili kupita sehemu ya mwisho ya “dhiki kubwa” na kuingia katika ulimwengu mpya. Tazamio hilo lapaswa sasa kuwa chanzo cha shangwe. (Ufunuo 7:9, 14, NW) Kwa upande mwingine, halaiki ya watu kutoka kwa “mataifa yote” watakuwa wamejithibitisha kuwa mbuzi washupavu. Wao “[wataingia] katika kukatiliwa-mbali kudumuko milele.” Liwazo lililoje kwa dunia!

      22, 23. Kwa kuwa utimizo wa huu mfano ungali mbele, kwa nini kazi yetu ya kuhubiri leo ni muhimu?

      22 Ingawa kule kuhukumu kama kunavyofafanuliwa katika huu mfano kuko karibu sana, hata sasa jambo muhimu linatukia. Sisi Wakristo tunashiriki katika kazi ya kuokoa uhai ya kutangaza ujumbe unaotokeza mgawanyiko kati ya watu. (Mathayo 10:32-39) Paulo aliandika: “Kwa kuwa, Kila atakayeliitia Jina la Bwana ataokoka. Basi wamwiteje yeye wasiyemwamini? Tena wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri?” (Warumi 10:13, 14) Huduma yetu ya hadharani inafikia watu katika nchi zaidi ya 230 kwa jina la Mungu na ujumbe wake wa wokovu. Ndugu za Kristo watiwa-mafuta wangali wakiongoza kazi hii. Kondoo wengine wapatao milioni tano wamejiunga nao sasa. Na watu duniani pote wanauitikia ujumbe unaotangazwa na ndugu za Yesu.

      23 Wengi hupata ujumbe wetu tuhubiripo nyumba kwa nyumba au kivivi-hivi. Wengine huenda wakajifunza juu ya Mashahidi wa Yehova na kile tunachowakilisha katika njia tusizojua. Wakati wa hukumu ufikapo, Yesu atafikiria kwa kadiri gani ustahili wa kijumuiya na ustahili wa kifamilia? Hatujui, na hakuna haja ya kukisia. (Linganisha 1 Wakorintho 7:14.) Wengi sasa hupuuza kimakusudi, hudhihaki, au hushiriki moja kwa moja katika kuwanyanyasa watu wa Mungu. Hivyo, huu ni wakati muhimu; watu kama hao huenda wanaelekea kuwa wale ambao Yesu atahukumu kuwa mbuzi.—Mathayo 10:22; Yohana 15:20; 16:2, 3; Warumi 2:5, 6.

      24. (a) Kwa nini ni jambo la maana kwa watu mmoja-mmoja kuitikia ifaavyo kuhubiri kwetu? (b) Funzo hili limekusaidia wewe binafsi kuwa na mtazamo gani kuelekea huduma yako?

      24 Ingawa hivyo, kwa furaha wengi huitikia ifaavyo, hujifunza Neno la Mungu, na kuwa Mashahidi wa Yehova. Wengine ambao sasa wanaonekana kuwa wenye mfano wa mbuzi huenda wakabadilika na kuwa kama kondoo. Jambo kuu ni kwamba wale wanaoitikia na kuunga mkono kwa matendo mabaki ya ndugu za Kristo wanatoa uthibitisho sasa ambao utawawekea msingi wa kuwekwa kwenye mkono wa kuume wa Yesu aketipo, hivi karibuni, katika kiti chake cha ufalme ili kutoa hukumu. Hawa wanabarikiwa nao wataendelea kubarikiwa. Hivyo, huu mfano wapaswa kutuchochea kwenye utendaji wa bidii zaidi katika huduma ya Kikristo. Kabla ya kuchelewa mno, tunataka tufanye yote tuwezayo ili kutangaza habari njema ya Ufalme na hivyo kuwapa wengine fursa ya kuitikia. Kisha ni juu ya Yesu kutoa hukumu, ya adhabu au ya upendeleo.—Mathayo 25:46.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki