Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb05 kur. 43-64
  • Ripoti ya Ulimwenguni Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ripoti ya Ulimwenguni Pote
  • 2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb05 kur. 43-64

Ripoti ya Ulimwenguni Pote

Afrika

Idadi ya nchi: 56

Idadi ya watu: 770,301,093

Idadi ya wahubiri: 983,057

Idadi ya mafunzo ya Biblia: 1,769,182

Je, unajua kwamba habari njema zinahubiriwa jangwani Sahara? Nafissatou mwenye umri wa miaka 17 anaishi katika mji wenye machimbo ya madini kaskazini mwa Niger. Siku moja, baadhi ya wanafunzi wenzake walipoanza kuongea juu ya mambo machafu, Nafissatou aliondoka. Mwanafunzi mmoja msichana alimfuata na kumwuliza tatizo ni nini. Nafissatou akamjibu kwamba hapendi mazungumzo ya aina hiyo. Kwanza msichana huyo alimdhihaki na kusema kwamba kutazama picha chafu hakuwezi kuleta madhara yoyote. Nafissatou alimweleza kwamba hilo ni jambo zito kwa sababu Muumba hakubali mambo kama hayo. Kisha akatoa katika mkoba wake wa shule kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, na kumwonyesha msichana huyo sehemu inayozungumzia hatari za kutazama picha chafu. Halafu akatoa Biblia yake na kumsomea 2 Wakorintho 7:1. Msichana huyo alikiri kwamba alipotazama video zisizo za maadili, aliingiwa na hisia kali ambazo hakuzielewa. Aliomba nakala ya kitabu Vijana Huuliza. Nafissatou alimpa kitabu hicho na baadaye akaeleza hivi: “Nilipokutana naye tena alikuwa peke yake, kwa hiyo nikamwuliza marafiki wake wameenda wapi. ‘Kitabu hiki ndicho rafiki yangu,’ akasema. Nilianza kujifunza naye, na alihudhuria Ukumbusho.”

Zaidi ya miaka 15 iliyopita, mwanamke fulani alijifunza Biblia pamoja na dada mmishonari nchini Tanzania. Walijifunza kwa miaka kadhaa. Mwanamke huyo alisitasita kukubali kweli kwa sababu alipingwa na familia yake, na hatimaye funzo hilo likakoma. Hata hivyo, binti zake wadogo wawili walikuwa wakisikiliza kwa utulivu mama yao alipokuwa akijifunza. Binti mkubwa alihama nyumbani alipokuwa na miaka 18, naye akaenda moja kwa moja kwenye Jumba la Ufalme kuomba funzo la Biblia. Alifanya maendeleo haraka na kubatizwa. Dada yake mdogo pia aliomba funzo la Biblia, na hata yeye akabatizwa. Mama ya wasichana hao alitiwa moyo na msimamo imara wa binti zake naye akaamua kuanza kujifunza Biblia tena. Alishinda woga wa wanadamu uliokuwa umemzuia asifanye maendeleo, na akabatizwa katika kusanyiko la mzunguko mnamo Mei 2004.

Kutaniko linapotii amri ya “kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao,” bila shaka baraka za Yehova zinamiminika. (Yak. 1:27) Ndugu na dada katika kutaniko moja nchini Lesotho walijionea jambo hilo. Dada mmoja katika kutaniko hili, anayeitwa Mapolo, alikuwa na watoto wadogo wanne. Mapolo ambaye hakuwa na mume, alijua kwamba alikuwa na ugonjwa usiotibika, kwa hiyo, akawazoeza watoto wake ili waweze kujitegemeza. Alijifunza Biblia pamoja nao, akawapeleka mikutanoni, na kuwafundisha kutengeneza fagio, ambazo waliuza kando ya barabara. Mapolo alipokufa mwaka wa 1998, watoto wake mayatima walitunzwa na nyanya yao. Dada mmishonari aliyemsaidia Mapolo kuwa Shahidi aliyebatizwa alizungumza na watu wa shirika fulani la kijamii ili kuomba msaada kwa niaba ya mayatima hao, naye akapata pesa za kulipa karo zao za shule. Mashahidi wengine waliwapa wavulana hao mavazi. Hatimaye nyanya yao akafa. Ndugu mmoja katika kutaniko alijifunza Biblia pamoja nao na kuwalipia kodi ya nyumba. Wavulana wote wanne huhudhuria mikutano kwa ukawaida. Wawili sasa ni wahubiri wasiobatizwa, na yule mkubwa, Rantso aliye na miaka 20 sasa, alibatizwa Machi 2004 kwenye kusanyiko la mzunguko. Rantso alijifunza Biblia pamoja na binamu yake Retselisitsoe, aliyebatizwa siku ileile ambayo Rantso alibatizwa. Rantso anawashukuru sana ndugu ambao kwa miaka mingi walimtunza yeye na ndugu zake wadogo kwa upendo.

Mmishonari mmoja nchini Kamerun anasema hivi: “Kila juma nilipojifunza Biblia pamoja na mwanamume fulani kijana, nilimsikia mtu akiimba nyimbo za dini ndani ya nyumba. Nilimwuliza mwanafunzi wangu, ‘Ni nani mwimbaji huyo asiyetaka kujitokeza?’ Alikuwa Stephen, ndugu yake kipofu. Nilianza kujifunza na Stephen kwa kutumia kaseti ya broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Lengo letu lilikuwa Stephen akumbuke andiko moja la Biblia katika kila somo. Stephen ana kumbukumbu nzuri na aliweka akilini maandiko mengi ya Biblia. Yeye huhudhuria mikutano pia na hutoa maelezo mara kwa mara. Hivi majuzi alitoa hotuba yake ya kwanza katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Hotuba hiyo ilikuwa usomaji wa Biblia, lakini kwa sababu Stephen hajui kusoma maandishi ya vipofu ilimbidi kuweka akilini sehemu yote aliyogawiwa kusoma. Ninatarajia kwa hamu kushika mkono wa Stephen karibuni na kuandamana naye katika huduma. Andiko moja ambalo Stephen analipenda sana ni Isaya 35:5, linalosema: ‘Macho ya vipofu yatafunguliwa.’ Stephen anafurahi kwa sababu tayari macho yake ya kiroho yamefunguliwa, na sasa anamwimbia Yehova sifa na kumshukuru kwa sababu wakati ujao macho yake halisi pia yatafunguliwa.”

Katika nchi ya Liberia iliyokumbwa na vita, mwanamke anayeitwa Nancy alimwendea Shahidi mmoja na kuomba funzo la Biblia. Kasisi wa kanisa lake alikuwa amemwambia kwamba Mungu atawatupa Mashahidi wa Yehova katika moto wa mateso kwa sababu wao ni Wakristo wa uwongo. Hata hivyo, Nancy aliishi karibu na Mashahidi fulani, na alikuwa ameona kwamba vita vilipotulia kidogo, wazee wa kutaniko la eneo hilo walienda kuwajulia hali ndugu zao. Aliona pia kwamba Mashahidi waliwahubiria watu wengine katika vipindi vya amani. Nancy na wengine wengi mjini walivutiwa pia walipoona kwamba gari kutoka ofisi ya tawi ndilo lililokuwa la kwanza kupita eneo la vita ili kuleta vitu vilivyohitajika sana, ambavyo vilichangwa na Mashahidi nchini Ufaransa na Ubelgiji. Alisema hivi: “Ninafikiri kwamba ninyi mnahubiri kweli.” Funzo lake linaendelea vizuri.

Mwanamume mmoja kijana alifika kwenye kijiji fulani nchini Uganda ili kutengeneza nyumba ambayo ndugu hufanyia mikutano. Painia mmoja alimhubiria fundi huyo, naye akapenda ujumbe aliosikia. Hata hivyo, baada ya muda mfupi ilimbidi kurudi kwenye kijiji cha kwao kilicho juu milimani. Kwa sababu hakukuwa Mashahidi katika kijiji hicho, painia huyo alimweleza mahali ambapo angeweza kupata Jumba la Ufalme lililo karibu na kwao. Mwanamume huyo kijana alisafiri kwa baiskeli umbali wa kilometa 30 kwenye vijia vya milimani vyenye vumbi ili kuwatafuta ndugu. Hakupata mtu yeyote kwenye Jumba la Ufalme, kwa hiyo, aliandika barua fupi ya kuomba funzo la Biblia na kuiweka chini ya mlango. Yule painia ambaye baadaye alienda kumtafuta mtu huyo katika kijiji cha kwao alishangaa kuwapata watu 200 hivi wakingoja kusikia ujumbe wa Biblia! Wengi walitaka kujifunza Biblia. Sasa mikutano inafanywa katika eneo hilo la mbali.

Jioni moja katika kijiji kidogo chenye watu 600 hivi kusini-mashariki mwa Nigeria, wanakijiji waliuona mwangaza mwangavu angani na mrudisho wake mtoni. Mwangaza huo ulionekana kama unaelekea kwenye kijiji chao, basi wanakijiji wakakimbilia mahali salama. Wengi walifikiri kwamba mwangaza huo ulisababishwa na uharibifu ambao Mashahidi wa Yehova walikuwa wamehubiri ungekuja, kwa hiyo, wakakimbilia Jumba la Ufalme na kusema: “Jengo hili halitaharibiwa katika Har–Magedoni.” Hatimaye, mwendo wa saa nne hivi usiku, wanakijiji waligundua kwamba mwangaza huo ulitokana na moto mkubwa wa msitu. Ndugu walipowauliza wanakijiji hao kwa nini hawakukimbilia makanisa yaliyo karibu, mwanamume mmoja alijibu hivi: “Makanisa mengine ni ya bure. Har–Magedoni mnayohubiri itaharibu makanisa hayo, lakini haitaharibu Jumba la Ufalme.”

Dada ambaye ni painia wa kawaida katika kambi ya wakimbizi nchini Guinea, anasema hivi: “Nilipokuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba, nilikutana na msichana mlemavu mwenye umri wa miaka minane. Aliniambia kwamba kwa kawaida wazazi wake humwacha nyumbani mchana kutwa na kufunga mlango kwa kufuli. Nilimwambia ningetaka kuwa rafiki yake. Kisha nilipomwuliza angependa Mungu amfanyie nini, akaniambia angetaka amponye ili aweze kutembea. Nilichukua Biblia na kufungua andiko la Isaya 35:5, 6, na kumwonyesha ahadi ya Yehova kwamba walemavu watatembea. Halafu nikafungua broshua Furahia Milele Maisha Duniani! na kumwonyesha picha ya Yesu akiwaponya wagonjwa. Pia nilimwambia kwamba atapata baraka hizo kama atajifunza Biblia na kufanya yale ambayo Yehova anataka afanye. Alikubali funzo la Biblia. Tumekwisha jifunza broshua Maisha Duniani na tunaelekea kumaliza broshua Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu! Baada ya kujifunza kwa majuma matatu, alisema anataka kuhudhuria mikutano. Kwa kuwa hawezi kutembea, mimi humchukua nyumbani na kumbeba mgongoni hadi Jumba la Ufalme. Anapenda mikutano sana hivi kwamba nisipoenda kumchukua yeye huhuzunika sana na hata kulia.”

◼ Amerika

Idadi ya nchi: 56

Idadi ya watu: 868,871,739

Idadi ya wahubiri: 3,165,925

Idadi ya mafunzo ya Biblia: 3,089,453

Marie anayeishi Guadeloupe anasema hivi: “Baadhi ya wageni kwenye hoteli ninayofanya kazi waliniambia kwamba nguo na viatu fulani vilikuwa vimeachwa kwenye jiwe kubwa ufuoni kwa muda wa siku mbili. Nilivichukua vitu hivyo kwa kusudi la kumtafuta mwenyewe. Nilipata kibeti chenye euro 1,067 [dola 1,372 za Marekani]! Watu kadhaa waliokuwa hapo walinishauri nichukue kiasi fulani cha pesa hizo na kuwapa zilizobaki. Niliwaambia mara moja kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova na dhamiri yangu huniongoza kuwa mnyoofu. Kwa hiyo, nikapeleka vitu hivyo vyote mahali pa mapokezi hotelini. Wafanyakazi wa hoteli pia walishangaa kuona kwamba sikuchukua pesa hizo. Niliwaeleza msimamo wangu tena. Niliporudi ufuoni, baadhi ya watu waliokuwapo walitaka kujua zaidi juu ya imani yetu, nami nikawahubiria kwa kutumia Biblia. Miongoni mwao kulikuwa na mwanamke aliyesema, ‘Mimi nitawaajiri Mashahidi wa Yehova tu.’” Sasa mwenye vitu hivyo amepatikana, na polisi walimpongeza dada huyo kwa unyoofu wake.

Antonio ni Mwanabetheli huko Mexico, naye hutumia kila fursa kuongea na watu kuhusu kweli. Alipokuwa akisafiri kwa basi kwenda mkutanoni hivi majuzi, alimpa trakti mwanamume na mwanamke waliokuwa wamevalia vizuri, na walikuwa na mazungumzo mazuri. Antonio alisema hivi: “Niliwaaga tulipofika mahali nilipotaka kushuka, lakini nilishangaa kwa maana walitaka kushuka pia ili tuendelee na mazungumzo, ijapokuwa hawakuwa wamefika mwisho wa safari yao. Baada ya kushuka tuliongea kidogo, na tena nikawaaga. Waliniuliza, ‘Unaenda wapi?’ ‘Ninaenda kuhudhuria mkutano wa kutaniko langu,’ nikajibu. Waliangaliana, kisha wakauliza, ‘Tunaweza kuandamana nawe?’ ‘Nitafurahi kwenda nanyi!’ nikajibu.” Mwanamke huyo, ambaye ni wakili, na mpwa wake, ambaye ni mwanafunzi wa chuo kikuu walikuwa wamehubiriwa ujumbe wa ile kweli miaka kadhaa iliyopita, lakini hawakufanya maendeleo kwa sababu ya upinzani wa familia. Walipokuwa njiani kwenda mkutanoni pamoja na Antonio walitaja kwamba wangependa kumwona yule dada aliyezungumza nao kuhusu Biblia kwa mara ya kwanza. Walifurahia sana kukutana naye katika mkutano huo! Walipendezwa sana na mkutano huo na walikuwa na hamu ya kujifunza Biblia. Mwanamke huyo kijana alisema: “Yehova ndiye aliyetuongoza kufika kwenye mkutano huu, na kuanzia sasa tutaendelea kuhudhuria mikutano.” Funzo lilipangwa, nalo huongozwa mara mbili kwa juma.

Nchini Haiti, mke wa mwangalizi wa mzunguko anayeitwa Jacqueline, alikuwa akihubiri pamoja na dada mmoja painia walipomwona mwanamke kijana aliyekuwa ameketi peke yake kando ya barabara akilia. Dada hao walimkaribia na kumwuliza kwa nini amehuzunika sana. Kwanza, mwanamke huyo kijana alikataa kujibu, lakini baada ya kubembelezwa akasema, “Nimefanya kile nilichotaka kufanya.” Jacqueline alitambua mara moja kwamba alikuwa amekunywa sumu, na alipomwuliza ikiwa ndivyo ilivyo, mwanamke huyo akakubali kwa kuinamisha kichwa. Dada hao walimpeleka hospitalini haraka ili atibiwe. Juma lililofuata, yule dada painia alimtembelea na kumtia moyo. Funzo la Biblia lilianzishwa.

Lourdes alipokuwa akilipa vitu katika duka moja kubwa huko Paraguay, alishtuka alipoambiwa kwamba alikuwa na noti bandia. Mfanyakazi aliyemhudumia alimwita mlinzi mara moja. Lourdes na Ingrid, binti yake mwenye umri wa miaka mitano, walipelekwa kwenye chumba kidogo kuwangoja polisi. Mkurugenzi wa duka hilo na yule mlinzi walitaka dada awaeleze mahali alipopata noti hiyo bandia. Lourdes hakukumbuka mahali alipoipata, na aliwaambia hakujua kwamba hiyo ilikuwa noti bandia. Ingrid aliyekuwa ameudhika, alimtazama mkurugenzi na mlinzi na kusema: “Mnatutenda kama wezi. Mama yangu si mwizi. Sisi ni Mashahidi wa Yehova, na hatusemi uwongo.” Mkurugenzi huyo alimwuliza Lourdes ikiwa yeye ni Shahidi, naye akasema ndiyo. Hatimaye, baada ya kupiga simu kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, wanaume hao walisadikishwa kwamba Lourdes ni Shahidi. Walimwomba Lourdes na Ingrid msamaha na kuwaacha waondoke. Baadaye Ingrid alisema kwamba jambo baya zaidi katika kisa hicho ni kwamba walishindwa kununua bisi (popcorn) ambazo alitaka sana.

Ndugu mmoja aliyekuwa akihubiri nchini Kosta Rika aliamua kumhubiria jirani wake aliyekuwa Mkatoliki. Ndugu yetu alikuwa na wasiwasi kwa sababu mtu huyo hakuwapenda Mashahidi; hata alikuwa amewatukana. Ndugu alishangaa, mtu huyo alipomkaribisha na kumweleza jinsi alivyopata kubadili maoni yake kuwahusu Mashahidi. Rafiki yake mmoja alikuwa amemwalika kuhudhuria ibada katika kanisa la Kiinjili kwenye eneo la mbali. Alipoingia kanisani, mtu huyo alialikwa kutoa “ushuhuda,” naye akasema tu kwamba yeye ni Mkatoliki. Watu hawakufurahia jambo hilo, kwa hiyo wakamfukuza. Pia, walimwambia rafiki yake kwamba alikuwa hatarini kutengwa na kanisa kwa sababu alishirikiana na Mkatoliki. Mtu huyo aliondoka kanisani, lakini kwa sababu alikuwa katika eneo la kigeni, mbali na nyumbani kwake, hakuwa na mahali pa kulala. Alibisha mlango wa nyumba fulani na kueleza yale yaliyompata, naye akakaribishwa. Alipata chakula na mahali pa kulala. Wenye nyumba walimhubiria kwa sababu wao walikuwa Mashahidi wa Yehova. Mtu huyo alivutiwa sana kuona kwamba Mashahidi wanawapenda majirani wao kikweli! Sasa anajifunza Biblia pamoja na Mashahidi.

Dada mmoja huko Trinidad anaandika hivi: “Nilipokuwa nikiwahubiria watu barabarani, mwanamke mmoja alinijia na kuomba magazeti ya karibuni. Baada ya kumwachia magazeti kadhaa, nilimwuliza kama angependa kujifunza Biblia bila malipo. Mwanamke huyo alisema kwamba alikuwa amejifunza hapo awali lakini alikuwa amehamia eneo letu hivi majuzi. Nilimwuliza jina lake na anwani yake, lakini alikataa na kusema kwamba ikiwa sisi tunamtumikia Mungu wa kweli, Mungu atanielekeza nyumbani kwake. Siku iliyofuata nilipokuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba, nilibisha mlango mmoja, na mwanamke yuleyule akaja mlangoni. Aliponiona mimi na mwenzangu, alishangaa na kusema huku akicheka, ‘Mlinipataje haraka hivi?’ Nilimwuliza kama anakumbuka alichosema siku iliyotangulia. Alitualika nyumbani, na funzo likaanzishwa. Sasa mwanamke huyo ni mhubiri ambaye hajabatizwa.”

◼ Asia Na Mashariki Ya Kati

Idadi ya Nchi: 47

Idadi ya watu: 3,971,703,969

Idadi ya wahubiri: 574,927

Idadi ya mafunzo ya Biblia: 444,717

Ghanshyam ni painia wa kawaida nchini Nepal. Yeye ni dereva wa teksi. Anapokuwa kazini yeye hukutana na watu kutoka sehemu mbalimbali, na ameona kwamba wengi wao wana haraka, hata saa za jioni, nao hawana wakati mwingi wa kuzungumza. Hata hivyo, anajitahidi sana kuzungumza nao. Kila inapowezekana, anampa abiria trakti inayomfaa na anwani ya Jumba la Ufalme la eneo ambalo yule abiria anaishi. Abiria wengi wamemshukuru, na sasa watano kati yao wanajifunza Biblia pamoja na Ghanshyam.

Nchini Taiwan mume wa dada mmoja alimpigia kelele mke wake mara kwa mara kwa sauti yake yenye nguvu dada huyo alipotaka kuondoka kwenda kwenye mkutano wa Kikristo. Halafu siku moja mume huyo alishikwa na ugonjwa wa ubongo unaosababisha kupooza, na kulazwa hospitalini. Mke wake alimtunza kwa fadhili na kutumia kwa busara kipindi cha ugonjwa wake kumfundisha kweli za Biblia. Alimwambia hivi: “Ubongo wako unahitaji mazoezi, kwa hiyo, nitakueleza mambo machache, nawe ujitahidi kuyakumbuka, sawa?” Mume huyo alikubali kwa sababu alijua ilimbidi kuzoeza ubongo wake. Mke wake alitumia habari kutoka broshua mbalimbali ili kumfundisha kweli za msingi za Biblia, kama vile jina la Mungu, sifa zake, na habari kuu inayozungumziwa katika Biblia. Isitoshe, ndugu wengi walimtembelea na kumtendea kwa fadhili. Jambo hilo lilimvutia sana hivi kwamba baada ya kurudi nyumbani alikubali kujifunza Biblia. Sasa yeye huhudhuria mikutano akiwa ameketi katika kiti cha magurudumu na kutoa maelezo kwa sauti yake yenye nguvu.

Rohana ambaye ni painia wa pekee katika eneo la mashambani huko Sri Lanka, alipata upinzani kutoka kwa mwendeshaji fulani wa baiskeli yenye magurudumu matatu na viti viwili vya abiria. Kila alipomwona ndugu huyo akihubiri, alimtukana kwa sauti kubwa. Siku moja alimwambia Rohana kwamba asipoacha kuhubiri katika eneo hilo, huenda akachomwa kisu. Rohana alimjibu kwa upole. Baadaye, mtu huyo alipatwa na msiba na akalazwa hospitalini akiwa amejeruhiwa vibaya. Rohana alimtembelea hospitalini na kumpa zawadi. Alipoona kwamba Rohana amekuja kumtembelea, alianza kulia na kumwomba amsamehe kwa kumtusi. Mtu huyo alisema hivi: “Bwana, nikifikiria jinsi nilivyokutenda, afadhali ungenipiga kwa rungu badala ya kusafiri kutoka mbali hivyo kuja kunifariji.” Sasa mtu huyo ametoka hospitalini na anaendelea na kazi yake ya kuendesha baiskeli ya abiria. Pia anasoma magazeti yetu kwa ukawaida.

Watu wengi kutoka nchi mbalimbali huja Hong Kong ili kuwafanyia watu kazi za nyumba. Kwa mfano, mwanamke mmoja ambaye alikuwa ameanza kujifunza broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? alipoishi nchini Ufilipino alitaka kuendelea kujifunza Biblia. Lakini hakujua jinsi ya kuwapata Mashahidi, kwa hiyo alitoa sala na kumwomba Mungu amsaidie. Siku moja, alivuka bandari ili afike kwenye eneo kuu la biashara na eneo la bustani lililo katikati ya jiji, ambako Wafilipino wengi hukusanyika mwishoni mwa juma. Aliwatafuta Mashahidi wa Yehova lakini hakuwapata, ingawa wao huhubiri katika bustani hiyo kila Jumamosi na Jumapili. Hata hivyo, aliiona broshua Anataka iliyokuwa imetupwa katika pipa la takataka. Mwanamke huyo aliiokota na kuona kwamba ilikuwa imeandikwa namba fulani ya simu. Namba hiyo ilikuwa ya yule dada ambaye alikuwa ametoa broshua hiyo. Mwanamke huyo alishangaa na kufurahi sana alipoambiwa kwamba dada huyo anafanya kazi katika majengo yaleyale aliyokuwa akifanya kazi. Alianza kujifunza Biblia tena na anahudhuria mikutano.

Mwangalizi wa mzunguko na mzee fulani wa kutaniko huko Jamhuri ya Korea walifanya ziara ya uchungaji kwa wakati unaofaa kabisa. Walimtembelea dada mmoja ambaye alikuwa ameacha kuhubiri miaka kumi iliyopita. Mume wake, ambaye hakuamini kwamba kuna Mungu, alikuwa ameamua kuanza kwenda kanisani baada ya kufanyiwa upasuaji. Ndugu hao walipofika walimkuta mume wake, na baada ya mazungumzo ya kirafiki akakubali broshua Anataka. Yule mzee wa kutaniko alimtia dada yetu moyo alipokuja kujifunza na mumewe. Mume huyo alikubali mwaliko wa kuhudhuria kusanyiko la wilaya, na baada ya kusanyiko hilo aliacha kwenda kanisani na kuanza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Dada huyo alifanya maendeleo pia na kuomba kwamba watoto wao wanne walioishi katika jiji lingine watembelewe. Sasa, mume wa dada huyo, binti yake mkubwa na mume wake, na binti yake mdogo wamebatizwa. Baadaye, mwana wake mkubwa na mke wake walibatizwa pia. Sasa watu sita katika familia hiyo wamekuwa Mashahidi.

Yuki, ambaye ni mwanafunzi wa shule ya upili nchini Japani, aliona ni vigumu kuwaeleza wanafunzi wenzake kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova. Alitambua kwamba anapaswa kutoa ushahidi, na alijua kwamba ilimbidi kuchukua hatua ya kwanza, kwa sababu wanafunzi wenzake hawakuzungumzia mambo ya dini kamwe. Aliamua kutoa sala waziwazi wakati wa chakula cha mchana ili marafiki wake wamwone. Alisali kwa moyo wote asubuhi yote ili apate ujasiri. Kisha, badala ya kutoa sala fupi isiyoweza kutambulika wakati wa chakula cha mchana, aliinamisha kichwa na kusali kwa muda mrefu kidogo. Baada ya kusali, mwanafunzi mmoja alimwuliza ikiwa anajisikia vibaya. Bado, Yuki aliogopa kutoa ushahidi. Alihuzunika sana, na baadaye alimwomba Yehova msamaha na kwa mara nyingine akaomba ujasiri. Siku iliyofuata, baada ya Yuki kutoa sala, mwanafunzi mwenzake alimwuliza tena kama anajisikia vibaya, naye Yuki akawaza, ‘Ni lazima nitoe ushahidi sasa!’ Alieleza kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova. Kwanza mwanafunzi huyo alishangaa, lakini baadaye akamwuliza Yuki maswali mengi sana, kama vile, ‘Unasali kuhusu nini? Jina la Mungu ni nani? Yesu alikuwa nani?’ na kadhalika. Yuki alifurahi sana.

Glenn, anayeishi huko Kupang nchini Indonesia, alikuwa mlevi na alitumia dawa za kulevya. Watu walimkodi ili awatishe au kuwapiga wengine. Alikuwa akiishi kwa wazazi wake wakati Mashahidi wawili wa Yehova walipowatembelea ili kuzungumzia Biblia pamoja nao. Muda si muda Glenn alikubali kujifunza Biblia na alijitahidi sana kuacha mazoea yake mabaya. Siku moja mwenye duka fulani alimpa kiasi kikubwa cha pesa ili ampige mtu fulani. Glenn alifikiria jambo hilo lakini akaamua kutofanya kazi za aina hiyo tena. Alirudisha pesa na kukataa kumpiga mtu huyo. Baadaye alipoingia katika duka lingine, mwenye duka hilo aliogopa kwa sababu alifikiri alikuwa amekuja kumpiga. Glenn alimweleza mwenye duka huyo kwamba sasa anajifunza Biblia na anaishi kwa amani. Mwenye duka huyo alikubali funzo la Biblia na akamwajiri katika duka lake. Glenn alibatizwa kwenye kusanyiko la wilaya mwaka uliopita, na yule mwenye duka alikuwapo.

◼Ulaya

Idadi ya nchi: 46

Idadi ya watu: 728,373,014

Idadi ya wahubiri: 1,490,345

Idadi ya mafunzo ya Biblia: 733,728

Baada ya kifo cha Jacoba, dada mwenye umri wa miaka 88 aliyeishi nchini Uholanzi, watu wake wa ukoo walipata barua rasmi kutoka kwa polisi wa eneo hilo. Alikuwa amewapelekea magazeti kwa miaka mingi bila kukosa. Sehemu ya barua hiyo inasema hivi: “Tulimpenda sana. Alitutembelea kwa ukawaida kwenye kituo chetu, na tulifurahia kunywa chai pamoja naye. Tulivutiwa na ujasiri wake. Hata alipokuwa mzee, alikuwa akisafiri kwa baiskeli, bila kujali hali ya hewa, ili kuwatembelea watu na kueneza imani yake. Tunasikitika kwamba hatakuja tena kututembelea.”

Jambo lifuatalo lilitukia nchini Uswisi. Familia moja ya Mashahidi wa Yehova ilimpa kijana wa Mashahidi wengine funguo za makao yao katika orofa fulani walipoenda likizoni, na kumwomba awalishe samaki ambao waliwafuga katika tangi dogo nyumbani. Mvulana huyo alipokwenda kuwalisha samaki hao mara ya kwanza, alikuwa na tatizo la kufungua mlango. Mwanamke mmoja jirani alisikia kelele na akachungulia mlangoni. Alipomwona mvulana huyo akijaribu kufungua mlango, alikata kauli kwamba yeye ni mwizi, na kuwaita polisi. Mvulana huyo alipotoka baada ya kuwalisha samaki, alikabiliwa na polisi wawili wenye silaha! Walimwuliza: “Unafanya nini hapa?” Aliwajibu: “Nimetoka kuwalisha samaki kama nilivyoombwa kufanya.” Polisi hawakumwamini. Aliwaeleza: “Mimi ni Shahidi wa Yehova, na wale wanaoishi hapa pia ni Mashahidi. Waliniomba niwalishe samaki wao wakiwa likizoni, kwa hiyo wakanipa funguo.” Polisi hao hawakusadikishwa na walitaka kumpeleka kwenye kituo cha polisi. Kijana huyo alisema: ‘Ngoja kidogo, marafiki wangu waliandika namba yao ya simu ya mkononi kwenye karatasi hii; mnaweza kuwapigia simu na kuwauliza kama nimesema kweli.’ Polisi waliwapigia wenye nyumba hiyo simu na kuhakikishiwa kwamba kijana huyo alikuwa amesema kweli. Halafu, wakamwomba msamaha na kuondoka. Familia hiyo iliporudi nyumbani, walimtembelea yule mwanamke jirani aliyekuwa amehamia orofa hiyo hivi karibuni. Walimshukuru kwa kujali makao yao. Walimweleza kwamba mvulana huyo na wao pia ni Mashahidi wa Yehova, na kwamba kijana huyo anaaminika kabisa. Mwanamke huyo hakujua mengi kuwahusu Mashahidi wa Yehova, kwa hiyo walizungumza naye, na akakubali funzo la Biblia.

Dada mmoja alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba nchini Italia, alipata nafasi ya kuongea na mama ambaye hufanya kazi kwa saa nyingi kila siku. Baada ya kwenda nyumbani kwake mara nyingi bila kumpata, dada huyo aliamua kumpigia simu. Mwanamke huyo kijana alimweleza dada yetu kwamba hana wakati wa kujifunza Biblia. Dada alisema: “Kwa dakika 10 au 15 tu, unaweza kujifunza jambo jipya, hata kwa kutumia simu.” Mwanamke huyo akajibu: “Ikiwa funzo hilo litafanywa kwa kutumia simu, ni sawa basi!” Hivi majuzi, dada huyo alimwachia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele na kuanzisha funzo kwa kutumia simu. Kwa kawaida, funzo hilo hufanywa kila Jumamosi asubuhi, lakini badala ya kujifunza kwa dakika 10 au 15 tu, sasa wao hutumia dakika 30.

Angela ni mmojawapo wa wahubiri huko Uingereza ambao wamejitahidi kuwahubiria watu wa nchi nyingine wanaoishi nchini humo. Alipotembelea duka fulani la Wachina linalouza chakula kilichopikwa, mmoja wa wafanyakazi alimwashiria kwa mkono aende zake. Hata hivyo, Angela alipotaka kuondoka, mwanamke mmoja Mchina alikuja mbio kutoka nyuma ya duka hilo huku akitaja jina la Mungu katika lugha ya Kichina. Baada ya mazungumzo hayo ya kwanza, Angela alimpelekea magazeti kwa ukawaida. Ijapokuwa mwanamke huyo alipenda magazeti hayo, alisema kwamba hakuamini kwamba Mungu ndiye aliyeuumba ulimwengu. Aliamini kwamba vitu vyote vilijitokeza vyenyewe tu.

Mwanamke huyo alifanya kazi ya kupika chakula fulani cha Wachina kwenye duka hilo. Angela alimwuliza yeye hutumia vitu vingapi ili kupika chakula hicho. Alijibu: “Vitano.” Angela alipendekeza kwamba wakati atakapopika chakula hicho, avirushe vile vitu vitano hewani ili aone ikiwa chakula hicho kitajitokeza chenyewe. Juma lililofuata, Angela alipotembelea duka hilo, mwanamke huyo Mchina alimkaribisha, akampa kiasi kidogo cha kile chakula alichokuwa ametoka tu kupika, na kusema kuwa sasa anaamini kwamba Mungu ndiye aliyeuumba ulimwengu. Funzo la Biblia lilianzishwa, na mwanamke huyo anafanya maendeleo katika kujifunza kweli za Neno la Mungu.

Nchini Ujerumani, watu wanaotaka kuhifadhi mazingira hupinga mara nyingi wakati takataka zenye mnururisho kutoka mitambo ya nguvu ya nyuklia zinaposafirishwa kwa magari-moshi. Kwa hiyo, takataka kama hizo zinaposafirishwa, reli hulindwa na polisi wengi, ambao kazi yao ni kuondoa vizuizi kwenye reli kabla ya gari-moshi kupita. Mwezi wa Novemba 2003, kulikuwa na mpango wa kusafirisha takataka za aina hiyo karibu na eneo ambalo Gudrun anafanya utumishi wa wakati wote. Anaeleza hivi: “Niliwazia kwamba polisi hao wangeketi na kungoja kwa saa nyingi, kwa hiyo niliamua kuwaendea na kuwatolea magazeti.” Gudrun alipata kwamba polisi hao walikuwa wenye urafiki. Hakuwa na tatizo lolote kupata ruhusa ya kuzungumza nao kwa sababu alibeba kikapu kilichojaa nakala za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Baadhi ya polisi kutoka Bavaria hata walimpiga picha alipokuwa akiwatolea Amkeni! karibu na gari lao. Alisafiri zaidi ya kilometa 120 kwa siku mbili, na aliongea na zaidi ya polisi 100. Aliwaachia magazeti 184, na akasema hivi kwa shauku: “Sitasahau kamwe siku hizo mbili!”

Alipotoka kazini siku moja, Ana María anayeishi Hispania alienda kwenye kituo cha basi, na alipokuwa akingoja basi alianza kusoma baadhi ya matangazo yaliyokuwa yamebandikwa hapo. Alivutiwa na tangazo moja lililosema hivi: “Ninawatafuta Mashahidi wa Yehova ili niendelee na funzo langu la Biblia.” Bila kukawia, Ana María alipiga namba ya simu iliyoonyeshwa, na kupanga akutane na mwanamke huyo anayeitwa Felicitas. Alikuwa amekuja kutoka Ekuado hivi majuzi, ambako alikuwa amejifunza Biblia kwa miaka miwili. Funzo lilipangwa mara moja, na Felicitas na mwanawe wamehudhuria mikutano tangu wakati huo. Wanashukuru kwamba maendeleo yao ya kiroho hayakuzuiwa kwa muda mrefu.

Mwanamke mmoja anayeishi Bulgaria alijiunga na mjukuu wake kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Alivutiwa sana alipoelezwa kwamba jina la Mungu ni Yehova. Kwa sababu jina la Mungu halikupatikana katika Biblia yake, aliamua kwenda kwenye duka la vitabu kununua Biblia inayotumia jina hilo. Mwenye duka alimwuliza kile anachotafuta. Alipomwambia, mwenye duka alisema kwa sauti kubwa: “Wewe ni mfuasi wa madhehebu hayo!” Wakati uo huo, kasisi fulani aliingia dukani. Alipoulizwa, “Jina la Mungu ni nani?” alijibu: “Anaitwa Yehova, na sasa acha kumpigia mwanamke huyu kelele.” Mwenye duka alishangaa. Mwanamke huyo na watu watatu wa familia yake wanafanya maendeleo ya kiroho.

Familia moja nchini Urusi ilikumbwa na msiba: wazazi walifiwa na mwanao mpendwa. Siku moja kabla ya mazishi yake, mamake aliwapigia simu marafiki wote wa mwanaye kwa kutumia namba alizopata katika kijitabu cha mwanaye. Kijitabu hicho kilikuwa na namba ya simu ya familia moja ya Mashahidi wa Yehova, na mama huyo aliwaalika kwenye mazishi. Mashahidi hao hawakuwajua wazazi wa yule kijana, hata hivyo, waliamua kutumia nafasi hiyo kuwafariji. Ndugu aliongea na baba ya kijana huyo juu ya tumaini la ufufuo na kumwachia broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa. Ndugu yetu alimtembelea siku mbili baadaye. Baba huyo alisema hivi: “Broshua hiyo imetuvutia sana. Tumeamua kutenga wakati ili kujifunza Biblia.” Mke wake amejiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na ataanza kuhubiri karibuni.

◼Oceania

Idadi ya nchi: 30

Idadi ya watu: 34,820,382

Idadi ya wahubiri: 94,087

Idadi ya mafunzo ya Biblia: 48,307

Olena alikuwa na miaka 12 tu alipobatizwa Desemba 2003, nchini Hawaii. Tofauti na vijana wanaofuatilia sana raha, Olena ana miradi hususa ya kiroho. Alisema hivi: “Nilifurahia sana kuwa painia msaidizi katika mwezi wa Machi na Mei, na nilifurahia hasa kuhubiri pamoja na mapainia na watu wazima. Kwa mfano, kila Jumamosi alasiri nilikuwa na pendeleo la kuandamana na dada, aliyekuwa mmishonari hapo awali, alipofanya ziara za kurudia na alipojifunza Biblia na Wachina. Nilipendezwa na lugha yao. Mradi wangu mkuu ni kuwa painia wa kawaida katika kutaniko la lugha ya kigeni. Ili nifikie mradi huo, mimi huenda kuhubiri baada ya shule kila Jumatano, na vilevile kila Jumamosi na Jumapili. Pia, mimi hupanga kuwa painia msaidizi kila ninapokuwa na nafasi.” Ni jambo gani lingine ambalo Olena anaonelea linaweza kumsaidia kufikia miradi yake? Alisema hivi: “Ninalinda moyo wangu kwa kuonyesha kwa matendo kwamba kumpendeza Yehova ni muhimu kwangu. Kushirikiana na wale walio na maoni hayohayo kumhusu Yehova hunisaidia kuendelea kutembea kwenye njia ya uadilifu. Kwa sababu ninatumia wakati mwingi kumtumikia Yehova, sina wakati mwingi wa kushirikiana na watu wenye mitazamo ya ulimwengu. Hivyo, ninaepuka kuathiriwa na wazo la kwamba mali na starehe zisizo za maadili zinaweza kuniletea furaha.”

Katika Visiwa vya Solomon ni jambo la kawaida kwa wazazi kuwapa watu wa ukoo mtoto mmoja au wawili ili wawalee. Baada ya kujua matakwa ya Yehova, wazazi wa msichana anayeitwa Deborah walikubaliana na watu wao wa ukoo kumrudisha binti yao nyumbani. Deborah alionaje alipojikuta katika familia hiyo ya Mashahidi ambao wanajishughulisha sana na mikutano, kazi ya kuhubiri, na funzo la Biblia la familia? Deborah anasema hivi: “Hata katika mkutano wangu wa kwanza nilihisi kwamba wale waliokuwapo walifurahi kuniona. Nilitarajia kuwaona makasisi wenye kanzu za kipekee, lakini sikumwona hata mmoja. Ilionekana kama wote walitoa maelezo katika mikutano, hata watoto wadogo.” Muda si muda Deborah alifanya vivyo hivyo. Jambo lingine linalompendeza ni jinsi baba yake anavyomfundisha yeye na ndugu na dada zake wadogo. Anasema hivi: “Baba anatusaidia kutafakari juu ya maisha ya watu wanaotajwa katika Biblia. Jambo hili hunisaidia sana ninapokuwa na tatizo.” Sasa Deborah ni mhubiri ambaye hajabatizwa, na anashukuru sana kwamba kweli ya Neno la Mungu iliwasukuma wazazi wake kumrudisha nyumbani na kumsaidia kuanza kutembea kwenye njia ya uzima.

Sehemu fulani za Papua New Guinea ni zenye milima, na vijiji vingi havina barabara. Baadhi ya vijiji vimetengwa na maisha ya kisasa. Hata hivyo, habari njema ya Ufalme imefika hata kwenye maeneo hayo. Mtu anayeitwa Leanna alihudhuria mkutano mmoja katika mji mkuu, Port Moresby. Ndugu walishangaa alipowaeleza kwamba yeye ni chifu katika kijiji cha mbali milimani, ambako watu hawana vitu vyovyote vya kisasa. Leanna alitembea kwa siku tano porini ili afike barabarani, kisha akasafiri kwa lori hadi mji mkuu. Alisema kwamba miaka minne iliyopita alikuja mjini, na alikutana na ndugu mmoja barabarani aliyempa nakala ya Mnara wa Mlinzi. Leanna alirudi kijijini mwake na gazeti hilo, na baada ya kulisoma akaanza kuwafundisha wanakijiji kwa kulitumia. Alifanya hivyo kila Jumapili kwa miaka kadhaa, na alihifadhi gazeti hilo vizuri kwa kulifunika kwa plastiki. Hatimaye, wanakijiji walimshawishi aende akawatafute wachapishaji wa gazeti hilo. Alisafiri hadi mji mkuu, akawapata akina ndugu, nao wakapanga kujifunza naye. Leanna alikaa na familia ya Mashahidi kwa majuma mawili na alijifunza na kumaliza broshua Anataka. Alipoelezwa kwamba kuna kutaniko katika mji ambao hauko mbali sana na kijiji chake, alifurahi sana na kusema: “Hiyo ni rahisi! Inachukua siku mbili tu kutembea hadi mji huo!” Alirudi kijijini mwake akiwa ameelewa vizuri zaidi kweli ya Neno la Mungu na akiwa na mkoba uliojaa vitabu. Mipango imefanywa kutembelea kijiji hicho karibuni ili kuwafundisha watu Biblia kwa usahihi.

Katika kisiwa cha Kiribati, dada mmoja anayefanya kazi katika ofisi ya tafsiri ya Mashahidi wa Yehova anasimulia jambo lifuatalo: “Asubuhi moja niliweka gazeti la Mnara wa Mlinzi, linalozungumzia moto wa mateso, katika mkoba wangu. Niliamua kuwatolea watu gazeti hili ijapokuwa lilikuwa la zamani. Mimi na mwenzangu tulikutana na mtu mmoja. Tulijitambulisha na baada ya kumweleza kifupi kile ambacho Biblia inasema kuhusu moto wa mateso, tukamwonyesha gazeti hilo. Aliinamisha kichwa chake na kunyamaza kwa muda, kwa hiyo nikamwuliza ikiwa anajisikia vibaya. Alipoinua kichwa, niliona kwamba alikuwa akilia. Alisema kwamba kichwa cha gazeti hilo kilimgusa sana. Mwanaye alikuwa amekufa majuma machache tu yaliyopita, na yeye na mke wake bado walikuwa na huzuni sana. Wote wawili walikuwa wamemwomba Mungu bila kukoma awafariji, kwa sababu walifikiri kwamba mwanao yuko motoni. Aliposikia kile ambacho Biblia inasema kuwahusu wafu alishangaa na kufurahi sana. Funzo lilianzishwa wakati wa ziara ya kurudia. Mara kwa mara mtu huyo husema kwamba alimwomba Mungu amwonyeshe kweli, na kwamba alitamani kupata dini inayofundisha Biblia. Ameanza kuhudhuria mikutano na hujitayarisha vizuri ili atoe maelezo kutoka moyoni wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi.”

Mnamo Desemba 2003, zaidi ya watu 60,000 walihudhuria kusanyiko kubwa kuliko yote ambayo yamewahi kufanywa na Mashahidi wa Yehova huko Australia. Baada ya kurudi kutoka kusanyiko hilo lililofanywa Sydney, Alyscea aliye na miaka sita, alitamani sana kuwaonyesha wanafunzi wenzake kile kitabu kipya, Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Mama ya Alyscea alipokuja kumchukua kutoka shuleni alasiri, alishangaa kuona kwamba maneno “Mtukuzeni Mungu” yalikuwa yameandikwa kwa herufi kubwa kwenye ubao darasani. Asubuhi Alyscea alikuwa amewaeleza walimu watatu na wanafunzi wenzake 24 kuhusu kusanyiko hilo. Wote walivutiwa na kile kitabu kipya na maelezo ambayo Alyscea alitoa kwa shauku kuhusu habari zilizozungumziwa kusanyikoni. Yale maneno “Mtukuzeni Mungu” yalibaki kwenye ubao siku hiyo yote.

[Picha katika ukurasa wa 43]

Rantso (wa pili kuanzia kushoto) pamoja na binamu yake na ndugu zake, Lesotho

[Picha katika ukurasa wa 43]

Nafissatou, Niger

[Picha katika ukurasa wa 48]

Marie, Guadeloupe

[Picha katika ukurasa wa 48]

Antonio, Mexico

[Picha katika ukurasa wa 52]

Ghanshyam, Nepal

[Picha katika ukurasa wa 56]

Jacoba, Uholanzi

[Picha katika ukurasa wa 58]

Angela, Uingereza

[Picha katika ukurasa wa 61]

Olena, Hawaii

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki