Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Mungu Anakujali?
    Mnara wa Mlinzi—2014 | Agosti 1
    • HABARI KUU

      Je, Mungu Anakujali?

      “Mimi ninateseka nami ni maskini. Yehova mwenyewe ananijali.”a​—MFALME DAUDI WA ISRAELI, KARNE YA 11 K.W.K.

      Tone la maji likianguka kutoka katika ndoo

      “Mataifa ni kama tone kutoka katika ndoo.”—ISAYA 40:15

      Je, ilikuwa sawa kwa Daudi kutarajia Mungu amjali? Je, Mungu anakujali? Watu wengi hawaamini kwamba Mungu mweza-yote anawajali. Kwa nini?

      Sababu moja ni kwamba Mungu ana uhai wa hali ya juu kuliko wanadamu. Akiwa kwenye makao yake yaliyotukuka, mataifa yote “ni kama tone kutoka katika ndoo; nayo yamehesabiwa kuwa kama mavumbi membamba juu ya mizani.” (Isaya 40:15) Mwandishi mmoja asiyeamini Mungu alisema kwamba “ni kiburi cha hali ya juu kuamini kwamba kuna Mungu anayekujali na anayehangaikia matendo yako.”

      Kwa upande mwingine, baadhi ya watu huhisi kwamba tabia zao zinawafanya wasiwe na thamani machoni pa Mungu. Kwa mfano, mwanamume anayeitwa Jim mwenye umri wa makamo anasema hivi: “Kila mara nilisali ili nipate amani ya akili na kujidhibiti, lakini punde si punde, nilikasirika tena. Mwishowe niliamini kwamba nilikuwa mwovu sana na hivyo Mungu hangenisaidia.”

      Je, Mungu yuko mbali sana na wanadamu hivi kwamba hawajali? Yeye huhisije kuhusu wanadamu wenye dhambi? Bila msaada wa Mungu hakuna mwanadamu anayeweza kujibu maswali hayo. Hata hivyo, ujumbe wa Mungu kwa wanadamu, yaani, Biblia hutuhakikishia kwamba yuko karibu na wanadamu na anawajali. Biblia inasema, “kweli, hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Katika makala nne zifuatazo, tutachunguza jinsi ambavyo Mungu amethibitisha kwamba anawajali wanadamu kutia ndani wewe.

      a Zaburi 40:17; Yehova ni jina la Mungu kama lilivyofunuliwa kwenye Biblia.

  • Mungu Anakutazama
    Mnara wa Mlinzi—2014 | Agosti 1
    • HABARI KUU? | JE, MUNGU ANAKUJALI?

      Mungu Anakutazama

      “Kwa maana macho yake [Mungu] yako juu ya njia za mwanadamu, Naye huziona hatua zake zote.”—AYUBU 34:21.

      Baba akicheza na mvulana wake

      Mtoto mdogo zaidi ya wote ndiye anayehitaji kutunzwa sana

      KWA NINI WENGINE HAWAAMINI? Kulingana na utafiti wa hivi karibuni, galaksi yetu peke yake ina sayari bilioni 100 hivi. Kwa sababu ya ukubwa wa ulimwengu wote, watu wengi hujiuliza, ‘Kwa nini Muumba atazame wanadamu duni kwenye sayari ndogo sana?’

      BIBLIA INAFUNDISHA NINI? Mungu hakutupatia Biblia kisha akatuacha. Badala yake, Yehova anatuhakikishia hivi: “Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.”—Zaburi 32:8.

      Mfikirie Hagari, mwanamke Mmisri aliyeishi karne ya 20 K.W.K. Hagari alishindwa kumheshimu mwajiri wake, Sarai, kwa hiyo akafedheheshwa na akakimbilia nyikani. Kwa sababu Hagari alikuwa amefanya kosa, je, Mungu aliacha kumjali? Biblia inasema hivi: “Malaika wa Yehova akamkuta.” Malaika huyo alimhakikishia hivi Hagari: “Yehova ameyasikia mateso yako.” Kisha Hagari akamwambia Yehova hivi: “Wewe ni Mungu mwenye kuona.”—Mwanzo 16:4-13.

      “Mungu mwenye kuona” anakutazama wewe pia. Kwa mfano: Mama mwenye upendo huwatazama kwa makini watoto wake wadogo, kwa sababu mtoto mdogo zaidi ya wote ndiye anayehitaji kutunzwa sana. Vivyo hivyo, Mungu hututazama hasa tunapokuwa dhaifu na tunapokabili hatari. Yehova anasema hivi: “Mimi ninakaa kileleni na katika mahali patakatifu, pia pamoja na mtu aliyepondwa na mwenye roho ya unyenyekevu, ili kuipa uhai roho ya watu wa hali ya chini na kuupa uhai moyo wa wale wanaopondwa.”—Isaya 57:15.

      Hata hivyo, huenda ukajiuliza: ‘Mungu ananitazama jinsi gani? Je, yeye hunihukumu kwa kuangalia tu sura yangu, au huchunguza moyo wangu?’

  • Mungu Anakuelewa
    Mnara wa Mlinzi—2014 | Agosti 1
    • HABARI KUU | JE, MUNGU ANAKUJALI?

      Mungu Anakuelewa

      “Ee Yehova, umenichunguza kabisa, nawe unanijua.”—ZABURI 139:1.

      Uzi wa DNA na kiini-tete

      “Macho yako yalikiona kiini-tete changu.” —ZABURI 139:16

      KWA NINI WENGINE HAWAAMINI? Watu wengi wanahisi kwamba Mungu huwaona wanadamu kuwa wenye dhambi—wasio safi na wasiofaa. Kendra, aliyepatwa na ugonjwa wa kushuka moyo, alijihisi mwenye hatia sana kwa sababu alidhani hangeweza kufuata viwango vya Mungu kikamili. Kwa hiyo, anasema: “Niliacha kusali.”

      BIBLIA INAFUNDISHA NINI? Yehova haangalii tu dhambi zako bali pia anaelewa vizuri kabisa utu wako. Biblia inasema: “Analijua vema umbo letu. Akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” Zaidi ya hayo, hashughuliki nasi “kulingana na makosa yetu” bali anatusamehe kwa rehema tunapotubu.—Zaburi 103:10, 14.

      Mfikirie Daudi, mfalme wa Israeli aliyetajwa kwenye makala ya kwanza ya mfululizo huu. Alipokuwa akisali kwa Mungu alisema hivi: “Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa . . . Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu.” (Zaburi 139:16, 23) Naam, Daudi alikuwa na hakika kwamba ingawa alitenda dhambi—hata dhambi nzito—Yehova angeweza kutambua moyo wake wenye toba.

      Yehova anakuelewa vizuri zaidi kuliko binadamu yeyote yule. Biblia inasema: “Mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Samweli 16:7) Mungu anakujua kwa undani, yaani, chembe za urithi, malezi, mazingira, na mambo yote yanayochangia utu wako. Mungu anaona na kuthamini jitihada zako za kuwa mtu mwema, hata ingawa unakosea.

      Hata hivyo, Mungu hutumiaje mambo anayojua kukuhusu ili kukusaidia?

  • Mungu Anaweza Kukufariji
    Mnara wa Mlinzi—2014 | Agosti 1
    • HABARI KUU | JE, MUNGU ANAKUJALI?

      Mungu Anaweza Kukufariji

      “Mungu, ambaye huwafariji wale walioshushwa chini, alitufariji.” —2 WAKORINTHO 7:6.

      Mwanamke akisoma Biblia

      ‘Mwana wa Mungu alinipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.’​—WAGALATIA 2:20

      KWA NINI WENGINE HAWAAMINI? Hata wanapohitaji faraja kwa hali na mali, baadhi ya watu hudhani haifai kuomba msaada kutoka kwa Mungu ili kukabiliana na matatizo yao. “Ninapofikiria idadi ya watu duniani—na matatizo wanayokabili,” anasema mwanamke aitwaye Raquel, “shida zangu huonekana kidogo sana zikilinganishwa na matatizo yao na hivyo mimi husita kumwomba Mungu msaada.”

      BIBLIA INAFUNDISHA NINI? Mungu amefanya mengi kuwasaidia na kuwafariji wanadamu. Wanadamu wote wamerithi dhambi, hivyo hakuna anayeweza kufuata viwango vya Mungu kikamili. Hata hivyo, Mungu “alitupenda akamtuma [Yesu Kristo] Mwana wake kuwa dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.” (1 Yohana 4:10) Kupitia kifo cha kidhabihu cha Yesu, Mungu amefanya iwezekane kwa wanadamu kupata msamaha wa dhambi, dhamiri njema, na tumaini la uzima wa milele katika ulimwengu mpya wenye amani.a Je, dhabihu hiyo ni kwa ajili ya wanadamu wote, au pia inaweza kukunufaisha wewe binafsi?

      Mfikirie mtume Paulo. Alichochewa sana na dhabihu ya Yesu hivi kwamba akaandika: “Naishi kwa imani ambayo ni kumwelekea Mwana wa Mungu, aliyenipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.” (Wagalatia 2:20) Kwa kweli, Yesu alikufa kabla Paulo hajawa Mkristo. Hata hivyo, Paulo aliona dhabihu hiyo kuwa zawadi ya Mungu kwake binafsi.

      Kifo cha kidhabihu cha Yesu ni zawadi ya kibinafsi kwako wewe pia. Zawadi hiyo inaonyesha jinsi Mungu anavyokuthamini. Inaweza kukupatia “faraja ya milele na tumaini jema” na hivyo ‘kukuimarisha wewe katika kila tendo na neno jema.’—2 Wathesalonike 2:16, 17.

      Hata hivyo, Yesu alidhabihu uhai wake karibu miaka 2,000 iliyopita. Kuna uthibitisho gani kwamba Mungu anataka umkaribie leo?

      a Ili ujifunze mengi kuhusu dhabihu ya Yesu, ona sura ya 5 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

  • Mungu Anataka Umkaribie
    Mnara wa Mlinzi—2014 | Agosti 1
    • HABARI KUU | JE, MUNGU ANAKUJALI?

      Mungu Anataka Umkaribie

      “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” —YOHANA 6:44.

      KWA NINI WENGINE HAWAAMINI? Watu wengi wanaomwamini Mungu wanahisi kwamba hawawezi kumkaribia. “Nilimwona Mungu kuwa tu Muumba wa kila kitu,” anasema Christina, mwanamke aliyekuwa akienda kanisani kila juma huko Ireland. “Lakini sikumjua. Wala sikuwahi kuhisi kwamba yeye ni rafiki yangu.”

      BIBLIA INAFUNDISHA NINI? Yehova hachoki kutusaidia hata tunapohisi tumepotea. Yesu alionyesha jinsi Mungu anavyotujali kwa kutoa mfano huu: “Mtu akiwa na kondoo 100 na mmoja apotee, je, hatawaacha wale 99 milimani na kuondoka kwenda kumtafuta yule anayepotea?” Tunajifunza nini? “Vivyo hivyo Baba yangu aliye mbinguni hatamani kwamba mmoja wa wadogo hawa aangamie.”—Mathayo 18:12-14.

      Kila “mmoja wa wadogo hawa” ni mwenye thamani kwa Mungu. Mungu ‘humtafutaje yule anayepotea?’ Kama andiko lililonukuliwa mwanzoni mwa makala hii linavyosema, Yehova anawavuta watu kwake.

      Mashahidi wa Yehova wakiwa jijini wakimhubiria mwanamume ujumbe wa Biblia

      Ni nani leo wanaowatembelea watu nyumbani na katika sehemu za umma ili kuwatangazia ujumbe wa Biblia unaomhusu Mungu?

      Fikiria jinsi Mungu alivyochukua hatua ya kwanza kuwavuta watu wanyoofu kwake. Katika karne ya kwanza W.K., Mungu alimtuma mwanafunzi Mkristo Filipo kwa ofisa Mwethiopia akazungumze naye kuhusu unabii wa Biblia ambao ofisa huyo alikuwa akisoma. (Matendo 8:26-39) Baadaye, Mungu alimwongoza mtume Petro amtembelee nyumbani ofisa Mroma aliyeitwa Kornelio, ambaye alikuwa akisali na kujitahidi kumwabudu Mungu. (Matendo 10:1-48) Mungu alimwongoza pia mtume Paulo na wenzake kwenye mto fulani nje ya jiji la Filipi. Hapo, walikutana na Lidia “mwabudu wa Mungu” na “Yehova akafungua wazi moyo wake asikilize kwa makini.”—Matendo 16:9-15.

      Katika visa vyote, Yehova alihakikisha kwamba wote waliokuwa wakimtafuta walipata nafasi ya kumjua. Ni nani leo wanaowatembelea watu nyumbani na katika sehemu za umma ili kushiriki pamoja nao ujumbe wa Biblia unaomhusu Mungu? Wengi wangejibu, “Ni Mashahidi wa Yehova.” Jiulize, ‘Je, inawezekana kwamba Mungu anawatumia kunisaidia?’ Tunakusihi usali kwa Mungu ili akusadie kutambua jinsi anavyokuvuta kwake.a

      a Kwa habari zaidi, tazama video Kwa Nini Ujifunze Biblia? kwenye www.jw.org/sw.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki