Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ni Nini Hutukia Baada ya Kifo?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Agosti 1
    • HABARI KUU | UHAI BAADA YA KIFO​—JE, HILO LINAWEZEKANA?

      Ni Nini Hutukia Baada ya Kifo?

      Watu wazima pamoja na watoto wakiwa wamesimama kando ya jeneza makaburini

      “Nilifikiri kwamba kuna sehemu tatu ambazo mtu huenda anapokufa: mbinguni, motoni, au toharani. Nilijua kwamba sikuwa mtu mwema sana hivi kwamba nistahili kwenda mbinguni au mtu mbaya sana hivi kwamba niende motoni. Sikujua waziwazi mambo yanayompata mtu toharani. Sikuona mambo hayo katika Biblia. Yalikuwa tu maoni ya watu.”—Lionel.

      “Nilifundishwa kwamba watu wote huenda mbinguni baada ya kufa, ingawa sikuridhishwa na fundisho hilo. Nilifikiri kifo ndiyo mwisho wa mambo yote na kwamba hakuna tumaini lolote kwa wafu.”—Fernando.

      Je, umewahi kujiuliza: ‘Ni nini humpata mtu anapokufa? Je, wapendwa wetu waliokufa wanateseka sehemu fulani? Je, tutawaona tena? Tunawezaje kuwa na uhakika?’ Tafadhali ona kile ambacho Maandiko yanafundisha. Kwanza, acheni tuchunguze kile kinachofananishwa na kifo katika Biblia. Kisha tutazungumzia tumaini linalotolewa na Neno la Mungu, Biblia.

      Wafu wako katika hali gani?

      JIBU LA BIBLIA: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe, wala hawana malipo tena, kwa maana kumbukumbu lao limesahauliwa. Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote, kwa maana hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi, mahali unapokwenda.”a—Mhubiri 9:5, 10.

      Kwa ufupi, Kaburi, ni mahali ambapo wanadamu huenda wanapokufa; na ni mahali pa mfano au hali ya kutotenda. Mwanamume mwaminifu Ayubu alielewa nini kuhusu Kaburi? Alipoteza mali zake zote na watoto wake wote kwa siku moja, na kupigwa na majipu yenye maumivu makali mwilini. Ayubu alimsihi Mungu hivi: “Laiti ungenificha katika Kaburi [“motoni,” kulingana na Biblia ya Douay Version ya Wakatoliki], kwamba ungenificha.” (Ayubu 1:13-19; 2:7; 14:13) Ni wazi kwamba, Ayubu alijua kwamba Kaburi si mahali penye moto wa mateso, ambapo angeenda kuteseka zaidi. Badala yake, alipaona kuwa mahali ambapo angepata kitulizo.

      Kuna njia nyingine ya kujifunza kuhusu hali ya wafu. Tunaweza kuchunguza habari za Kimaandiko zilizoongozwa na roho ya Mungu kuhusu watu nane waliofufuliwa.—Tazama sanduku “Masimulizi Nane ya Ufufuo Yanayotajwa Katika Biblia.”

      Hakuna yeyote kati ya watu hao aliyesimulia kwamba alikuwa sehemu fulani akifurahia maisha au akiteseka. Ikiwa watu waliofufuliwa wangekuwa wameenda sehemu hizo walipokufa, je, wasingewasimulia watu kuhusu hilo? Na je, jambo hilo lisingeandikwa katika Biblia iliyoongozwa na roho ya Mungu ili watu wajue? Hakuna jambo lolote kati ya hayo linaloelezwa katika Maandiko. Kati ya wote nane waliofufuliwa hakuna aliyesimulia jambo lolote. Kwa nini? Kwa sababu hawakuwa na fahamu, kama tu kuwa katika usingizi mzito. Kwa kweli, mara nyingi Biblia hutumia usingizi kama mfano wa kuelezea maana ya kifo. Kwa mfano, watumishi waaminifu Daudi na Stefano ‘wamelala usingizi katika kifo.’—Matendo 7:60; 13:36.

      Hivyo, kuna tumaini gani kwa wafu? Je, wanaweza kuamshwa kutoka kwenye usingizi huo?

      a Katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, neno “Kaburi” ni tafsiri ya neno la Kiebrania “Sheoli” na neno la Kigiriki “Hadesi.” Baadhi ya tafsiri za Biblia hutumia neno “motoni,” hata hivyo, fundisho la kwamba wafu wanateseka katika moto wa mateso si la Kimaandiko.

      MASIMULIZI NANE YA UFUFUO YANAYOTAJWA KATIKA BIBLIAb

      Mwana wa mjane Nabii Eliya alimfufua mwana wa mjane aliyeishi Sarefathi, kaskazini mwa Israeli.—1 Wafalme 17:17-24.

      Mvulana Mshunamu Nabii Elisha, mrithi wa Eliya, alimfufua mvulana katika mji wa Shunemu na kumkabidhi kwa wazazi wake.—2 Wafalme 4:32-37.

      Mwanamume katika eneo la mazishi Maiti ya mwanamume ilitupwa ndani ya kaburi lililokuwa na mifupa ya Elisha. Mtu huyo alifufuliwa baada ya mwili wake kugusa mifupa ya nabii huyo.—2 Wafalme 13:20, 21.

      Mwana wa mjane aliyeishi Naini Yesu alisimamisha msafara wa mazishi nje ya jiji la Naini na kumfufua kijana huyo, kisha kumkabidhi kwa mama yake aliyekuwa akilia.—Luka 7:11-15.

      Binti ya Yairo Yairo, ofisa-msimamizi wa sinagogi, alimsihi Yesu amponye binti yake aliyekuwa mgonjwa. Yesu alimfufua binti huyo aliyekufa muda mfupi tu uliopita.—Luka 8:41, 42, 49-56.

      Lazaro, rafiki mpendwa wa Yesu Lazaro alikuwa amekufa kwa siku nne wakati Yesu alipomfufua mbele ya watazamaji.—Yohana 11:38-44.

      Dorkasi Mtume Petro alimfufua mwanamke huyo mpendwa aliyejulikana kwa matendo yake ya fadhili.—Matendo 9:36-42.

      Eutiko Kijana aliyeitwa Eutiko alikufa baada ya kuanguka kutoka ghorofani; na mtume Paulo alimfufua.—Matendo 20:7-12.

      b Ufufuo wa Yesu Kristo ni wa muhimu hata zaidi na unatofautiana sana na ule wa watu nane kama itakavyoonyeshwa kwenye makala inayofuata.

  • Je, Kuna Tumaini Lolote kwa Wafu?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Agosti 1
    • HABARI KUU | UHAI BAADA YA KIFO​—JE, HILO LINAWEZEKANA?

      Je, Kuna Tumaini Lolote kwa Wafu?

      Je, wafu wanaweza kuishi tena?

      JIBU LA BIBLIA: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.

      Yesu alitabiri kwamba wakati ujao chini ya utawala wa Ufalme wake, Makaburi yatabaki wazi. “Nilishangazwa sana niliposoma kwa mara ya kwanza andiko la Yohana 5:28, 29. Lilinipa tumaini hakika, na nilianza kufikiria wakati ujao nikiwa na matumaini,” anasema Fernando, aliyetajwa katika makala iliyotangulia.

      Katika nyakati za kale, mwanamume mwaminifu Ayubu alitarajia kwamba Mungu angemfufua baada ya kufa. Ayubu aliuliza hivi: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” Akiwa na uhakika alijibu hivi: “Mimi nitangojea siku zote za kazi yangu ya kulazimishwa [Kaburini] mpaka kitulizo changu kije. Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.”—Ayubu 14:14, 15.

      Lazaro aliyefufuliwa akimkumbatia dada yake

      Ufufuo wa Lazaro hutupatia tumaini la wakati ujao

      Tumaini la ufufuo halikuwa jambo jipya kwa Martha, dada ya Lazaro. Baada ya Lazaro kufa, Yesu alimwambia hivi: “Ndugu yako atafufuka.” Martha akamjibu hivi: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” Yesu akamwambia hivi: “Mimi ndiye ufufuo na uzima. Yule anayeniamini, hata akifa, atarudi kwenye uzima.” (Yohana 11:23-25) Kisha Yesu akamfufua mara moja Lazaro! Simulizi hilo lenye kusisimua linatuonyesha mambo makubwa ya wakati ujao. Hebu wazia, ufufuo utatukia ulimwenguni pote!

      Je, kuna wengine watafufuliwa ili waishi mbinguni?

      JIBU LA BIBLIA: Neno la Mungu linaeleza kwamba ufufuo wa Yesu unatofautiana na ule wa watu nane wanaotajwa katika Biblia. Watu wote nane walifufuliwa na kuendelea kuishi duniani. Lakini kuhusu ufufuo wa Yesu, tunasoma hivi: “Yesu Kristo . . . yuko mkono wa kuume wa Mungu, kwa maana alienda zake mbinguni.” (1 Petro 3:21, 22) Je, Yesu angeendelea kuwa mtu pekee aliyefufuliwa na kwenda kuishi mbinguni? Mapema Yesu aliwaambia hivi mitume wake: “Nikienda na kuwatayarishia ninyi mahali, nitakuja tena nami nitawapokea ninyi nyumbani kwangu mwenyewe, ili mahali nilipo mimi, ninyi pia muwe hapo.”—Yohana 14:3.

      Kristo alienda mbinguni na kutayarisha mahali kwa ajili ya baadhi ya wanafunzi wake ambao wangeenda huko. Idadi ya wale watakaoishi mbinguni ni 144,000. (Ufunuo 14:1, 3) Lakini wafuasi hao wa Yesu watafanya kazi gani huko?

      Watakuwa na kazi nyingi sana! Maandiko yanasema hivi: “Mwenye furaha na mtakatifu ni yeyote aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; kifo cha pili hakina mamlaka juu ya hao, bali watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.” (Ufunuo 20:6) Wale watakaofufuliwa na kwenda kuishi mbinguni, wataitawala dunia wakiwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo.

      Ni nani wengine watakaofufuliwa baadaye?

      JIBU LA BIBLIA: Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanaeleza hivi katika hotuba aliyotoa mtume Paulo: “Nami nina tumaini kwa Mungu, tumaini ambalo watu hawa pia wanalo, kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.

      Mwanamke akimkumbatia binti aliyefufuliwa katika paradiso

      Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba mabilioni ya watu waliokufa wataishi tena

      “Waadilifu” wanaotajwa na Paulo watatia ndani nani? Fikiria mfano ufuatao. Kabla ya kufa, mwanamume mwaminifu Danieli aliambiwa hivi: “Nawe utapumzika, lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa zile siku.” (Danieli 12:13) Je, Danieli angefufuliwa na kuishi wapi? “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Pia, Yesu alitabiri hivi: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Danieli pamoja na wanaume na wanawake wengine waaminifu watafufuliwa na kuishi tena milele duniani.

      “Wasio waadilifu” wanaotajwa na Paulo watatia ndani nani? Hao watatia ndani mabilioni ya watu ambao wamekufa bila kupata fursa ya kujua na kuishi kulingana na kweli za Biblia. Watakapofufuliwa, watapata nafasi ya kumjua na kumshukuru Yehovaa na Yesu. (Yohana 17:3) Wale wote wanaochagua kumtumikia Mungu wataishi milele kama Yehova.

      Wale wote wanaoamua kumtumikia Mungu watakuwa na tumaini la kuishi milele wakiwa na afya kamili na furaha

      Hali itakuwaje Duniani?

      JIBU LA BIBLIA: Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) “Na hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.”—Isaya 65:21.

      Hebu jiwazie ukiishi katika hali hiyo nzuri ukiwa na wapendwa wako waliofufuliwa! Hata hivyo bado kuna swali: Unawezaje kuwa na uhakika kwamba kutakuwa na ufufuo?

      a Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.

  • Tumaini kwa Wafu​—Unawezaje Kuwa na Uhakika?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Agosti 1
    • HABARI KUU | UHAI BAADA YA KIFO​—JE, HILO LINAWEZEKANA?

      Tumaini Kwa Wafu Unawezaje Kuwa na Uhakika?

      Je, ni sahihi kuamini kwamba wafu wataishi tena? Mtume Paulo aliamini hivyo. Aliongozwa na roho takatifu kuandika hivi: “Ikiwa ni katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi ndio wa kusikitikiwa zaidi kati ya watu wote. Hata hivyo, sasa Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.” (1 Wakorintho 15:19, 20) Paulo aliona ufufuo kuwa jambo halisi. Alikuwa na uhakika huo kwa sababu Yesu mwenyewe alifufuliwa.a (Matendo 17:31) Ndiyo sababu Paulo alimwita Yesu “matunda ya kwanza” yaani, alikuwa mtu wa kwanza kufufuliwa na kupewa uzima wa milele. Ikiwa Yesu alikuwa wa kwanza, ni wazi kwamba kungekuwa na wengine ambao wangefufuliwa.

      Mwanamke akisoma Biblia na kupata tumaini hakika la wakati ujao

      Ayubu alimwambia hivi Mungu: “Utaitamani sana kazi ya mikono yako.”​—Ayubu 14:14, 15

      Kuna sababu nyingine inayoweza kukupatia uhakika wa tumaini la ufufuo. Yehova ni Mungu wa kweli. ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Yehova hajawahi na hatawahi kamwe kusema uwongo. Je, angeahidi kuhusu ufufuo, hata kutuonyesha kwamba anaweza kufufua wafu na kisha asitende kulingana na ahadi yake? Jambo hilo halipatani na akili hata kidogo!

      Kwa nini Yehova ameahidi kufufua wafu wakati ujao? Kwa sababu ya upendo. Ayubu aliuliza hivi: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” Kisha akasema hivi: “Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15) Ayubu alikuwa na uhakika kwamba Baba yake mpendwa wa mbinguni angetamani sana kumfufua. Je, Mungu amebadilika? Biblia inajibu hivi: “Mimi ni Yehova; sikubadilika.” (Malaki 3:6) Mungu bado anatamani kuwaona wafu wakifufuliwa na kuishi tena wakiwa na afya nzuri na furaha. Ni sawa tu na jinsi ambavyo mzazi mwenye upendo angetamani kumfufua mtoto wake mpendwa. Tofauti ni kwamba, Mungu ana uwezo wa kufanya chochote apendacho.—Zaburi 135:6.

      Kifo ni kibaya, hata hivyo Mungu ana suluhisho kamili

      Yehova atamwezesha Mwana wake kuwaletea shangwe nyingi wale wote wanaoomboleza kwa sababu ya kufiwa na wapendwa wao. Yesu anahisije kuhusu ufufuo? Kabla ya kumfufua Lazaro, Yesu alihisi uchungu moyoni kama walivyohisi dada na marafiki wa Lazaro, naye “akatokwa na machozi.” (Yohana 11:35) Pindi nyingine, Yesu alikutana na mjane wa Naini, aliyefiwa na mwana wake pekee. Yesu “akamsikitikia, akamwambia: ‘Acha kulia.’” Kisha akamfufua mwana huyo. (Luka 7:13) Hivyo, Yesu anajua vizuri huzuni na uchungu wa kufiwa. Yesu atafurahi sana wakati atakapowaondolea huzuni wanadamu ulimwenguni pote!

      Mwanamume akimkumbatia binti yake

      Je, umewahi kuhuzunika? Huenda ukahisi kwamba kifo ni tatizo lisilo na suluhisho. Hata hivyo kuna suluhisho. Nalo ni ufufuo ambao Mungu atatekeleza kupitia Mwana wake. Kumbuka kwamba Mungu angependa uone hilo litakapotendeka. Angependa uwepo ili kuwapokea wapendwa wako wanapofufuliwa. Hebu wazia ukipanga mambo pamoja nao kwa ajili ya wakati ujao, milele!

      Lionel, aliyenukuliwa mapema, anasema hivi: “Hatimaye, nilijifunza kuhusu ufufuo. Mwanzoni, ilikuwa vigumu kuamini, na sikumwamini aliyeniambia jambo hilo. Lakini nilichunguza jambo hilo katika Biblia na kutambua kwamba lilikuwa la kweli! Ninasubiri kwa hamu sana kumwona tena babu yangu.”

      Je, ungependa kujua mengi zaidi? Mashahidi wa Yehova wangependa kukuonyesha katika Biblia kwa nini wanaamini kwamba kutakuwa na ufufuo wakati ujao.b

      a Ili kuwa na uhakika kwamba Yesu alifufuliwa, soma kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? ukurasa wa 78-86, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      b Tafadhali soma sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki