Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa Nini Watu Husali?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Oktoba 1
    • HABARI KUU | JE, KUNA FAIDA YOYOTE TUNAPOSALI?

      Kwa Nini Watu Husali?

      “Nilipenda sana kucheza kamari. Nilikuwa na kawaida ya kusali ili nishinde. Lakini sikuwahi kushinda.”—Samuel,a Kenya.

      “Tulipokuwa shuleni tulikariri na kusali sala tulizofundishwa.”—Teresa, Ufilipino.

      “Mimi husali ninapopata matatizo. Ninasali ili kuomba msamaha wa dhambi na ili kuwa Mkristo anayefaa.”—Magdalene, Ghana.

      1. Mwanamume akisali katika meza ya kuchezea kamari; 2. Msichana akisali shuleni; 3. Mwanamke akisali

      Maelezo yaliyotolewa na Samuel, Teresa, na Magdalene yanaonyesha kwamba watu husali wakiwa na malengo mbalimbali, mazuri au mabaya. Baadhi ya watu husali kutoka moyoni; na wengine hawasali kutoka moyoni. Hata hivyo, iwe wanasali ili kufaulu mitihani shuleni, timu wanayoipenda ishinde, Mungu asaidie familia zao, au kwa sababu zozote zile, watu wengi huona kuna uhitaji wa kusali. Kwa kweli, utafiti mwingi uliofanywa unaonyesha kwamba hata baadhi ya watu wasio na dini husali kwa ukawaida.

      Je, wewe husali? Ikiwa ndiyo, basi unasali kwa ajili ya nini? Iwe una kawaida ya kusali au la, huenda ukajiuliza: ‘Je, kuna faida yoyote tunaposali? Je, kuna yeyote anayesikiliza sala?’ Mwandishi mmoja alisema sala ni “aina mojawapo ya matibabu . . . sawa na kuzungumza na samaki unayemfuga.” Wataalamu wa tiba wana maoni hayo pia, nao husema kwamba sala ni aina mojawapo ya “tiba mbadala.” Je, watu wanaotoa sala hupata faida yoyote nyingine?

      Tofauti na maoni ya watu wengi, Biblia inataja kwamba sala ina faida nyingi zaidi ya kuwa tiba. Inasema kwamba kuna mtu anayesikiliza sala zinazotolewa kwa njia inayofaa na kwa mambo yanayofaa. Je, jambo hilo ni la kweli? Acheni tuone uthibitisho.

      a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

  • Je, Kuna Yeyote Anayesikiliza Sala?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Oktoba 1
    • Yesu anatazama mbinguni na kusali huku wanafunzi wake wakiinamisha vichwa vyao

      HABARI KUU | JE, KUNA FAIDA YOYOTE TUNAPOSALI?

      Je, Kuna Yeyote Anayesikiliza Sala?

      Baadhi ya watu huona kwamba kutoa sala ni kupoteza muda kwa sababu hakuna anayesikiliza. Wengine wamesali lakini wanahisi kwamba sala zao hazijajibiwa. Mtu mmoja aliyeamini kwamba hakuna Mungu aliamua kusali hivi siku moja: “Tafadhali ongea nami hata kidogo.” Lakini alisema kwamba Mungu “alikaa kimya.”

      Hata hivyo, Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu husikiliza sala. Biblia inasema hivi tangu zamani: “Yeye [Mungu] hakika atakuonyesha kibali unapotoa sauti ya kilio chako; mara tu atakapokisikia kwa kweli atakujibu.” (Isaya 30:19) Mstari mwingine unaopatikana katika Biblia unasema hivi: “Sala ya wanyoofu ni furaha kwake.”—Methali 15:8.

      Yesu alisali kwa Baba yake, “naye akasikiwa vizuri.”—Waebrania 5:7

      Biblia inataja pia mifano ya watu ambao sala zao zilisikilizwa. Mstari mmoja unasema kwamba Yesu alitoa “maombi kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa” na “akasikiwa vizuri.” (Waebrania 5:7) Mifano mingine inapatikana katika Danieli 9:21 na 2 Mambo ya Nyakati 7:1.

      Hivyo, kwa nini watu fulani huhisi kwamba sala zao hazijibiwi? Ili sala zetu zisikilizwe, tunapaswa kusali kwa Yehova,a ambaye ni Mungu pekee anayetajwa katika Biblia, wala si kwa mungu mwingine au mababu. Mungu pia anataka ‘tuombe kulingana na mapenzi yake,’ yaani, mambo anayopenda. Mungu anatuhakikishia kwamba tukisali kwa njia hiyo, ‘yeye atatusikia.’ (1 Yohana 5:14) Hivyo, ili sala zetu zisikilizwe, tunahitaji kumjua Mungu anayetajwa katika Biblia na kujifunza kuhusu mapenzi yake.

      Watu wengi wanaamini kwamba sala si jambo la kidini tu bali Mungu husikiliza na kujibu sala. Isaac, kutoka Kenya, anasema hivi: “Nilisali ili nipate msaada wa kuielewa Biblia. Muda mfupi baadaye, mtu fulani alikuja na kunisaidia kuielewa Biblia.” Hilda anayeishi nchini Ufilipino, alitaka kuacha kuvuta sigara. Baada ya kuona anashindwa, mume wake alimshauri hivi: “Kwa nini usimwombe Mungu akusaidie?” Alitii ushauri huo na anasema hivi: “Ninashangaa jinsi Mungu alivyonisaidia. Nilianza kupoteza hamu ya kuvuta sigara. Mwishowe niliacha kabisa.”

      Je, Mungu anaweza kukusaidia ikiwa maombi yako yanapatana na mapenzi yake?

      a Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.

  • Kwa Nini Mungu Hutuhimiza Tusali?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Oktoba 1
    • HABARI KUU | JE, KUNA FAIDA YOYOTE TUNAPOSALI?

      Kwa Nini Mungu Hutuhimiza Tusali?

      Mungu anataka tuwe rafiki zake.

      Marafiki huwasiliana ili kuwa na uhusiano mzuri. Vivyo hivyo, Mungu hutuhimiza tusali ili tuwe na urafiki wa karibu naye. Anasema hivi: “Mtaniita na kuja na kusali kwangu, nami nitawasikiliza.” (Yeremia 29:12) Kadiri unavyoongea na Mungu, ndivyo ‘utakavyomkaribia [yeye], naye atakukaribia.’ (Yakobo 4:8) Biblia inatuhakikishia hivi: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia.” (Zaburi 145:18) Tunavyoendelea kusali kwa Mungu ndivyo uhusiano wetu pamoja naye utakavyozidi kuimarika.

      “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia.”—Zaburi 145:18

      Mungu anataka kukusaidia.

      Yesu alisema hivi: “Ni nani kati yenu ambaye mwana wake akimwomba mkate—je, atampa jiwe? Au, labda, akiomba samaki—je, atampa nyoka? Kwa hiyo, ikiwa ninyi . . . mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo nzuri, je, Baba yenu aliye mbinguni hatawapa hata zaidi vitu vyema wale wanaomwomba?” (Mathayo 7:9-11) Naam, Mungu anakuhimiza usali kwake kwa sababu ‘anakujali’ na anataka kukusaidia. (1 Petro 5:7) Pia, anataka umwambie matatizo yako. Biblia inatuambia hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.”—Wafilipi 4:6.

      Wanadamu wana uhitaji wa kiroho.

      Wataalamu wa masomo ya asili ya mwanadamu wamegundua kwamba watu wengi wanahisi kuna uhitaji wa kusali. Hata wale wanaoamini kwamba hakuna Mungu au wanaoamini kwamba mambo yake hayawezi kujulikana wanahisi hivyo pia.a Hilo linathibitisha kwamba wanadamu waliumbwa wakiwa na uhitaji wa kiroho. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Njia moja ya kutosheleza uhitaji huo ni kwa kuwasiliana na Mungu kwa ukawaida.

      Tutapata faida gani tukisali kwa Mungu?

      a Kulingana na uchunguzi uliofanywa na kituo cha utafiti cha Pew Research Center katika mwaka wa 2012, asilimia 11 ya watu nchini Marekani wanaoamini kwamba hakuna Mungu au wanaoamini kwamba mambo yake hayawezi kujulikana, husali angalau mara moja kwa mwezi.

      Sala Inahusisha Nini?

      Biblia inaonyesha kwamba sala inaweza kutia ndani sehemu zote za maisha yetu. Sala inaweza kuhusisha mambo yafuatayo:

      • Kuungama “Niliungama dhambi yangu kwako, wala sikufunika kosa langu.”—Zaburi 32:5.

      • Shukrani “Ni vema kumtolea Yehova shukrani.”—Zaburi 92:1.

      • Kusifu “Nitambariki Yehova nyakati zote; daima sifa yake itakuwa katika kinywa changu.”—Zaburi 34:1.

      • Kuomba Mwongozo “Unitembeze katika njia ya amri zako, kwa maana nimependezwa nayo.”—Zaburi 119:35.

      • Kuomba Nguvu “Nigeukie na kunionyesha kibali. Umpe mtumishi wako nguvu zako.”—Zaburi 86:16.

  • Sala​—Ina Umuhimu Gani Kwako?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Oktoba 1
    • Mwanamke anasali huku akikumbuka hali ya mama yake aliye mgonjwa

      HABARI KUU | JE, KUNA FAIDA YOYOTE TUNAPOSALI?

      Sala Ina Umuhimu Gani Kwako?

      Kabla ya kufanya jambo lolote, ni kawaida kujiuliza hivi: ‘Lina umuhimu gani kwangu?’ Je, tunaonyesha ubinafsi kwa kujiuliza hivyo kuhusu sala? Hapana. Si ajabu kwamba tunataka kujua ikiwa sala ina faida yoyote. Hata mwanamume mwaminifu Ayubu aliuliza hivi: “Kama ningemwita, je, angenijibu?”—Ayubu 9:16.

      Katika makala zilizotangulia, tulichunguza uthibitisho unaoonyesha kwamba sala ni zaidi ya desturi ya kidini au aina fulani ya tiba ya akili. Mungu wa kweli husikiliza sala. Atatusikiliza tukisali kwa njia inayofaa na kuhusu mambo yanayofaa. Anatuhimiza tumkaribie. (Yakobo 4:8) Hivyo, tutarajie nini tukisali kwa ukawaida? Acheni tuchunguze baadhi ya faida tutakazopata.

      Amani ya akili.

      Unapopata matatizo au changamoto maishani, je, wewe huwa na wasiwasi mwingi? Katika nyakati kama hizo, Biblia inatutia moyo ‘tusali bila kuacha’ na kuacha “maombi yenu yajulishwe Mungu.” (1 Wathesalonike 5:17; Wafilipi 4:6) Biblia hutuhakikishia kwamba tukisali kwa Mungu, “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:7) Tutapata amani tukimweleza Baba yetu wa mbinguni mahangaiko yetu. Kwa kweli, anatutia moyo tufanye hivyo. “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza,” inasema Zaburi 55:22.

      “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” —Zaburi 55:22

      Watu wengi ulimwenguni wamepata amani hiyo. Hee Ran, kutoka Korea Kusini, anasema: “Hata ninapokuwa na matatizo makubwa sana, nikisali, ninahisi kama mzigo umepungua na ninahisi nimepata nguvu za kuendelea kuvumilia.” Cecilia, kutoka Ufilipino, anaeleza hivi: “Nikiwa mama, ninahangaikia sana hali ya binti zangu na mama yangu, ambaye sasa hawezi kunitambua. Sala imenisaidia niendelee na shughuli zangu za kila siku bila kuwa na wasiwasi mwingi. Ninajua kwamba Yehova atanisaidia kuwatunza.”

      Inatufariji na kutupatia nguvu tunapopatwa na majaribu.

      Je, unakabili hali ngumu sana, labda inayohatarisha uhai wako au inayohuzunisha sana? Kusali kwa “Mungu wa faraja yote” kunaweza kukupa kitulizo kwa kiasi kikubwa. Biblia inasema kwamba yeye “hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Kwa mfano, pindi moja Yesu alipokuwa amefadhaika sana, ‘alipiga magoti na kuanza kusali.’ Matokeo yalikuwa nini? “Ndipo malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.” (Luka 22:41, 43) Mwanamume mwingine mwaminifu, Nehemia, alitishwa na watu waovu waliojaribu kumzuia asifanye kazi aliyopewa na Mungu. Alisali hivi: “Itie mikono yangu nguvu.” Mambo yaliyotendeka baada ya hapo yanaonyesha kwamba kwa kweli Mungu alimsaidia kushinda woga na kumaliza kazi yake. (Nehemia 6:9-16) Reginald, kutoka Ghana, anaeleza hivi kuhusu sala: “Ninaposali, hasa ninapolemewa na hali ngumu, ninahisi kama nimemwambia mtu anayeweza kunisaidia na ambaye amenihakikishia kwamba sina haja ya kuwa na wasiwasi.” Bila shaka, Mungu anaweza kutufariji tunaposali kwake.

      Hekima kutoka kwa Mungu.

      Baadhi ya maamuzi tunayofanya yanaweza kutuathiri sisi na wale tunaowapenda. Tunawezaje kufanya maamuzi ya hekima? Biblia inasema hivi: “Kwa hiyo, ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, [hasa ya kushughulika na majaribu] na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yakobo 1:5) Ikiwa tutasali ili tupate hekima, Mungu atatumia roho yake takatifu kutuongoza tufanye maamuzi ya hekima. Tunaweza hasa kusali ili tupewe roho takatifu kwa sababu Yesu alituhakikishia hivi: “Baba aliye mbinguni [atawapa] roho takatifu wale wanaomwomba!”—Luka 11:13.

      Mwanamume akisali

      “Mara zote nilisali kwa Yehova ili nipate mwongozo wa kufanya uamuzi unaofaa.”—Kwabena, Ghana

      Hata Yesu alitambua umuhimu wa kusali kwa Baba yake alipotaka kufanya maamuzi mazito. Biblia inatuambia kwamba alipotaka kuwachagua wanaume 12 ambao wangekuwa mitume wake, ‘alisali kwa Mungu usiku wote.’—Luka 6:12.

      Kama ilivyokuwa kwa Yesu, watu wengi leo wamepata amani ya akili wanapoona jinsi Mungu anavyojibu wanapomwomba awasaidie kufanya maamuzi ya hekima. Regina, kutoka Ufilipino, anakabili matatizo ya aina mbalimbali, kama vile kujiruzuku yeye mwenyewe na familia yake baada ya kufiwa na mume, kupoteza kazi, na ugumu wa kulea watoto. Ni nini kilichomsaidia kufanya maamuzi ya hekima? Anasema hivi: “Ninategemea msaada wa Yehova kupitia sala.” Kwabena, kutoka Ghana, anaeleza kwa nini alimwomba Mungu msaada: “Nilipoteza kazi ya ujenzi yenye mshahara mnono.” Anapofikiria maamuzi aliyohitaji kufanya, anasema hivi: “Mara zote nilisali kwa Yehova ili nipate mwongozo wa kufanya uamuzi unaofaa.” Anaongezea hivi: “Nina hakika kwamba Yehova alinisaidia kuchagua kazi inayoniwezesha kutimiza mahitaji yangu ya kiroho na kimwili.” Wewe pia unaweza kupata mwongozo wa Mungu ukisali kuhusu mambo yanayoweza kuathiri uhusiano wako pamoja naye.

      Tumetaja faida chache unazoweza kupata ukisali. (Kwa mifano zaidi, tazama sanduku “Faida za Sala.”) Hata hivyo, ili upate faida hizo unahitaji kwanza kumjua Mungu na mapenzi yake. Ikiwa ungependa jambo hilo, tunakutia moyo waombe Mashahidi wa Yehova wakufundishe Biblia.a Hiyo inaweza kuwa hatua ya kwanza ya kumkaribia “Msikiaji wa sala.”—Zaburi 65:2.

      a Ili upate habari zaidi wasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au tembelea tovuti yetu ya www.jw.org/sw.

      Faida za Sala

      Amani ya akili “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

      Faraja kutoka kwa Mungu “Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tuweze kuwafariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki kupitia faraja ambayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

      Mwongozo wa kufanya maamuzi ya hekima “Kwa hiyo, ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.”—Yakobo 1:5.

      Msaada wa kuepuka kishawishi “Salini, ili msiingie katika jaribu.”—Luka 22:40.

      Msamaha wa dhambi “Watu wangu ambao jina langu limeitwa juu yao wajinyenyekeze na kusali na kuutafuta uso wangu na wageuke kutoka katika njia zao mbaya, basi mimi nitasikia nikiwa mbinguni na kusamehe dhambi yao.”—2 Mambo ya Nyakati 7:14.

      Njia ya kuwasaidia wengine “Dua ya mtu mwadilifu, inapofanya kazi, ina nguvu nyingi.”—Yakobo 5:16.

      Tunatiwa moyo sala zinapojibiwa “Yehova akaendelea kumwambia [Sulemani]: ‘Nimeisikia sala yako na ombi lako la kutaka kibali ambalo uliomba kibali mbele zangu.’”—1 Wafalme 9:3.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki