-
Jinsi Sayansi Inavyoathiri Maisha YakoMnara wa Mlinzi—2015 | Juni 1
-
-
HABARI KUU JE, SAYANSI | IMECHUKUA NAFASI YA BIBLIA?
Jinsi Sayansi Inavyoathiri Maisha Yako
Kulingana na kamusi ya Kiswahili sanifu, sayansi ni “elimu inayotokana na uchunguzi, majaribio, vipimo na kuthibitishwa kwa muda uliopo.” Ni vigumu kufanya mambo yote hayo na mara nyingi kazi hiyo huchosha. Wanasayansi hujitahidi kufanya majaribio kwa majuma, miezi, au hata miaka kadhaa. Nyakati fulani kazi zao hazifanikiwi, lakini katika visa vingi wanasayansi wamenufaisha wanadamu. Fikiria mifano kadhaa.
Kampuni fulani ya Ulaya ilitumia plastiki ngumu na vifaa bora vya kuchujia maji kutokeza kifaa ambacho kinawasaidia watu kuepuka magonjwa yanayotokana na kunywa maji yasiyo safi. Vifaa kama hivyo hutumika wakati wa misiba ya asili, kama wakati wa tetemeko la ardhi lililoikumba nchi ya Haiti mwaka wa 2010.
Huko angani, setilaiti kadhaa hufanyiza kile kinachoitwa Global Positioning System (GPS). Kifaa hicho kilichobuniwa kwa ajili ya matumizi ya kijeshi, kinawasaidia pia madereva, marubani, waongozaji wa meli, wawindaji na watembeaji wa masafa marefu kujua njia. Kwa sababu ya uvumbuzi huo wa wanasayansi, GPS imerahisisha kujua mahali unapotaka kwenda.
Je, unatumia simu, kompyuta au Intaneti? Je, afya yako imeboreshwa au umepona baada ya kutumia dawa? Je, wewe husafiri kwa ndege? Ikiwa ndivyo, basi unafaidika kutokana na yale ambayo sayansi imewafanyia wanadamu. Sayansi imeathiri maisha yako katika njia nyingi nzuri.
YALE AMBAYO SAYANSI IMESHINDWA KUTIMIZA
Katika jitihada za kuongeza ujuzi wao, wanasayansi wa kisasa wamechunguza kwa kina kuhusu asili ya ulimwengu. Wanafizikia wa nyuklia wamechunguza utendaji wa atomu, wakati huohuo wamejaribu kuelewa mwanzo wa ulimwengu kwa kuchunguza jinsi ulivyokuwa mabilioni ya miaka iliyopita. Kadiri wanavyochunguza kwa mapana na marefu, hata katika ulimwengu usioonekana na usiofikika, baadhi ya wanasayansi wanahisi kwamba ikiwa Mungu anayetajwa katika Biblia yupo, basi wangeweza kumwona.
Baadhi ya wanasayansi na wanafalsafa mashuhuri wana maoni zaidi. Wanaendeleza kile ambacho mwandishi wa sayansi Amir D. Aczel alikiita kuwa “mjadala wa wanasayansi unaopinga kuwapo kwa Mungu.” Kwa mfano, mwanafizikia mashuhuri sana alidai kwamba “kukosekana kwa ushahidi wa kuwapo kwa Mungu anayetimiza fungu muhimu katika uumbaji wa ulimwengu ni uthibitisho usiopingika kwamba hakuna mungu.” Wengine husema kwamba utendaji wa Mungu unaotajwa katika Biblia ni “uchawi” na “nguvu fulani za ajabu.”a
Hata hivyo, swali tunalopaswa kujiuliza ni kwamba: Je, wanasayansi wamejifunza vya kutosha kuhusu uumbaji hivi kwamba waweze kufikia mkataa? Jibu rahisi ni, hapana. Sayansi imefanya maendeleo makubwa, lakini wanasayansi wengi wanajua kwamba kuna vitu vingi sana visivyojulikana na vile ambavyo ni tata. Kuhusu kuelewa uumbaji, mwanafizikia na mshindi wa tuzo ya Nobeli Steven Weinberg alisema hivi: “Hatutawahi kamwe kuelewa kabisa uumbaji.” Mtaalamu wa nyota mashuhuri zaidi nchini Uingereza, Profesa Martin Rees, aliandika hivi: “Kuna vitu ambavyo huenda wanadamu hawatavielewa kamwe.” Ukweli ni kwamba wanasayansi bado hawajajua vizuri uumbaji kuanzia seli ndogo zaidi hadi ulimwengu mzima. Ona mifano ifuatayo:
Wanabiolojia hawajui kikamili hatua zinazotokea ndani ya seli zilizo hai. Baadhi ya maswali ambayo bado sayansi haiwezi kujibu kikamili ni kama vile jinsi seli zinavyopata nguvu, zinavyotokeza protini na zinavyojigawa.
Nguvu ya uvutano hutuathiri kila sekunde. Hata hivyo, wanafizikia hawajajua kikamili jinsi jambo hilo linavyotendeka. Hawaelewi vizuri kwa nini uvutano huo hutuvuta chini ardhini tunaporuka au jinsi uvutano huo unavyodumisha mwezi kwenye njia yake ili kuzunguka dunia.
Wanakosmolojia wanakadiria kwamba asilimia 95 hivi ya vitu vinavyofanyiza ulimwengu havionekani na haviwezi kugunduliwa na vifaa vya kisayansi. Wamegawanya vitu hivyo katika makundi mawili, mata nyeusi na nguvu nyeusi. Asili ya vitu hivyo bado haijulikani.
Kuna vitu vingine ambavyo havijulikani vinavyowatatiza wanasayansi. Kwa nini jambo hilo ni muhimu? Mwandishi mashuhuri wa sayansi alisema hivi: “Mambo tusiyoyajua ni mengi sana ukilinganisha na yale tunayoyajua. Sayansi inaweza kukufanya ustaajabu na kukufanya utamani kujifunza zaidi, badala ya kukufanya ujione kuwa hujui mambo mengi.”
Kwa hiyo, kama unajiuliza ikiwa sayansi inaanza kuchukua nafasi ya Biblia na kwamba inapinga kuwapo kwa Mungu, fikiria jambo hili: Ikiwa wanasayansi mashuhuri pamoja na vifaa vyao vyenye nguvu wameweza kuwa na ujuzi mdogo tu kuhusu uumbaji, je, litakuwa jambo linalopatana na akili kuacha kuamini au kutafuta ukweli wa mambo ambayo sayansi imeshindwa kuchunguza? Kuhusu jambo hilo, katika makala ndefu inayoeleza historia na maendeleo ya elimu ya nyota, kitabu Encyclopedia Britannica kinafikia mkataa huu: “Baada ya miaka 4,000 hivi ya utaalamu wa nyota, ulimwengu bado ni tata kama tu vile ambavyo huenda Wababiloni waliuona.”
Mashahidi wa Yehova wanaheshimu haki ya kila mtu ya kufanya uamuzi kuhusu jambo hilo. Tunajitahidi kufuata mwongozo wa Biblia: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Ni kwa msingi huo tunakualika uchunguze jinsi ambavyo sayansi na Biblia zinapatana na kukamilishana.
a Baadhi ya watu huipinga Biblia kwa sababu ya mafundisho ya zamani na ya sasa ya dini kama vile kuamini kwamba dunia ni kitovu cha ulimwengu wote au kwamba Mungu aliumba dunia katika siku sita zenye urefu wa saa 24.—Tazama sanduku lenye kichwa “Biblia na Mambo Yaliyothibishwa Kisayansi.”
-
-
Sayansi Ina MipakaMnara wa Mlinzi—2015 | Juni 1
-
-
HABARI KUU JE, SAYANSI | IMECHUKUA NAFASI YA BIBLIA?
Sayansi ina Mipaka
Katika miaka ya hivi karibuni, vitabu vingi vinavyoeleza maoni ya watu wasioamini kuwapo kwa Mungu vimechapishwa. Vitabu hivyo vimewavutia watu wengi na vimechochea mazungumzo na mijadala mikubwa. Kuhusiana na hilo, mwanasayansi wa mfumo wa neva, David Eagleman aliandika hivi: “Baadhi ya wasomaji wanaamini kwamba wanasayansi wanajua kila kitu.” Kisha akaongezea hivi: “Mwanasayansi bora hukubali kujifunza mambo mapya, na kufanya hivyo kunamwezesha kugundua mambo mapya.”
Tangu zamani, wanasayansi stadi wamefanya ugunduzi wenye kutokeza walipokuwa wakitafuta majibu ya maswali magumu kuhusu uumbaji. Hata hivyo, baadhi yao wamefanya makosa makubwa sana katika jitihada hizo. Isaac Newton alikuwa mmoja kati ya wanasayansi mashuhuri sana. Alieleza jinsi ambavyo nguvu ya uvutano inavyoongoza sayari, nyota, na makundi ya nyota katika ulimwengu. Pia, alianzisha kanuni ya hesabu ambayo hutumiwa kutengeneza kompyuta, safari za angani na fizikia ya nyuklia. Hata hivyo, Newton alifuatilia alkemia, sayansi ya uwongo ambayo hutumia unajimu na uchawi kujaribu kugeuza metali ya kawaida kuwa dhahabu.
Zaidi ya miaka 1,500 kabla ya Newton, mtaalamu wa nyota Mgiriki Ptolemy alichunguza mbingu kwa kutumia macho tu. Ptolemy alifuatilia sayari zilizopita katika anga la usiku na alikuwa stadi katika kuchora ramani. Lakini aliamini kwamba dunia ni kitovu cha vitu vyote. Mwanasayansi Carl Sagan aliandika hivi kuhusu Ptolemy: “Maoni yake kuhusu dunia kuwa ndio kitovu cha ulimwengu yaliyokubaliwa kwa miaka 1,500 ni uthibitisho wa kwamba hata mtu awe na akili kadiri gani bado anaweza kuwa amekosea.”
Leo pia, wanasayansi wanakabili changamoto zilezile. Je, wataweza kuuelewa ulimwengu kikamili? Ingawa ni jambo linalofaa kutambua maendeleo ambayo sayansi imefanya na faida ambazo imetuletea, ni muhimu kukumbuka mipaka yake. Mwanafizikia Paul Davies alisema hivi: “Haiwezekani kupata ufafanuzi kamili unaoeleweka na unaopatana katika kila hali kuhusu ulimwengu wetu.” Maneno hayo yanaeleza ukweli huu usiopingika: Wanadamu hawezi kuelewa kikamili uumbaji. Hivyo, wengine wanapodai kwamba sayansi inaweza kufafanua vizuri chanzo cha kila kitu kilichopo, ni vizuri kuchunguza madai hayo kwa usawaziko.
Ni wazi kwamba Biblia inatimiza uhitaji wetu katika njia ambazo sayansi haiwezi
Biblia hueleza maajabu ya uumbaji kwa maneno haya: “Tazama! Hizo ndizo kingo za njia zake [Mungu], nao ni mnong’ono ulioje wa jambo lililosikiwa juu yake!” (Ayubu 26:14) Kuna hazina kubwa ya ujuzi ambayo inazidi uwezo wa mwanadamu kuelewa. Kwa kweli, maneno ambayo mtume Paulo aliandika miaka 2,000 hivi iliyopita, bado ni ya kweli kabisa: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika!”—Waroma 11:33.
-