Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa Nini Uielewe Biblia?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Desemba 1
    • HABARI KUU | UNAWEZA KUIELEWA BIBLIA

      Kwa Nini Uielewe Biblia?

      “Biblia ni kitabu cha dini kinachojulikana sana. Hata hivyo, ni kitabu cha kigeni na hakiwafai Wachina.”—LIN, CHINA.

      “Hata vitabu vitakatifu vya dini yangu ya Kihindu sivielewi. Nitawezaje kuielewa Biblia Takatifu?” —AMIT, INDIA.

      “Ninaiheshimu Biblia kwa kuwa ni kitabu cha zamani na nimesikia kwamba kimeuzwa zaidi kuliko vitabu vingine. Lakini, sijawahi kuiona.”—YUMIKO, JAPANI.

      Watu wengi ulimwenguni wanaiheshimu sana Biblia. Hata hivyo, wengi wao hawajui yaliyomo katika Biblia. Hali iko hivyo kwa mamilioni ya watu wanaoishi barani Asia na hata katika nchi nyingi ambazo watu wengi wana Biblia.

      Mwanamke akisoma Biblia

      Huenda ukajiuliza hivi, ‘Kwa nini ninahitaji kuielewa Biblia?’ Kujifunza kuhusu kitabu hicho kitakatifu kunaweza kukusaidia:

      • Uridhike na uwe na furaha

      • Ushughulikie matatizo ya familia

      • Ukabiliane na mahangaiko

      • Uwe na uhusiano mzuri na watu

      • Utumie pesa kwa hekima

      Mfikirie Yoshiko, anayeishi Japani. Alitaka sana kujua Biblia ina ujumbe gani, hivyo akaanza kuisoma. Matokeo yalikuwa nini? Anasema hivi: “Biblia imenisaidia kupata kusudi maishani na tumaini la wakati ujao. Sasa nimeridhika.” Amit aliyetajwa mwanzoni aliamua pia kuichunguza Biblia. Anasema: “Nilishangaa. Biblia ina habari zinazomfaa kila mtu.”

      Biblia imeboresha sana maisha ya watu wengi. Kwa nini usiichunguze uone jinsi inavyoweza kukunufaisha?

      Unaweza Kuwa na Familia Yenye Furaha

      Kwa habari zaidi kuhusu jinsi unavyoweza kunufaika kwa kusoma Biblia, tazama broshua Unaweza Kuwa na Familia Yenye Furaha, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

  • Kitabu Kinachoeleweka
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Desemba 1
    • Reading the Bible in printed form and on a mobile phone

      HABARI KUU | UNAWEZA KUIELEWA BIBLIA

      Kitabu Kinachoeleweka

      Kwa kweli, Biblia ni kitabu cha kale. Kina umri gani? Biblia ilianza kuandikwa miaka 3,500 hivi iliyopita huko Mashariki ya Kati. Kipindi hicho utawala wenye nguvu wa ukoo wa Shang ulikuwa ukitawala nchini China na karne kumi hivi baadaye dini ya Budha ilianza nchini India. —Tazama sanduku “Taarifa Fupi Kuhusu Biblia.”

      Biblia inatoa majibu yenye kuridhisha ya maswali muhimu sana kuhusu maisha

      Ili kitabu kiwanufaishe na kuwasaidia watu, lazima kieleweke na kuwafaa. Ndivyo ilivyo Biblia. Inatoa majibu yenye kuridhisha ya maswali muhimu sana kuhusu maisha.

      Kwa mfano, umewahi kujiuliza, ‘Kwa nini tuliumbwa?’ Swali hilo limewasumbua wanadamu kwa maelfu ya miaka, na bado linawasumbua. Hata hivyo, jibu la swali hilo linaweza kupatikana katika sura mbili za kwanza za kitabu cha kwanza cha Biblia, kitabu cha Mwanzo. Simulizi la Biblia katika sura hizo linaanza na “mwanzo,” yaani, mabilioni ya miaka iliyopita, wakati ulimwengu wetu unaotia ndani nyota na dunia ulipoumbwa. (Mwanzo 1:1) Kisha simulizi hilo linaeleza hatua kwa hatua jinsi dunia, viumbe mbalimbali, na wanadamu walivyoumbwa na pia kwa nini vitu hivyo vimeumbwa.

      KITABU KINACHOELEWEKA

      Biblia inatoa ushauri unaotusaidia kutatua matatizo ya kila siku. Ushauri huo unaeleweka kwa urahisi. Kuna mambo mawili yanayofanya ushauri wa Biblia ueleweke.

      Kwanza, lugha ya Biblia iko wazi na inavutia. Badala ya kutumia maneno mengi yasiyoeleweka au magumu, Biblia hutumia maneno tunayoelewa. Mawazo magumu yanasimuliwa kwa maneno tunayotumia kila siku.

      Kwa mfano, Yesu alifundisha mambo yaliyogusa mioyo ya watu kwa kuwasimulia mifano mingi rahisi iliyohusu mambo ya kawaida maishani. Baadhi ya mifano hiyo inapatikana katika Mahubiri ya Mlimani, yaliyoandikwa kwenye kitabu cha Biblia cha Mathayo, sura ya 5 hadi 7. Mchambuzi mmoja wa Biblia aliyeita mahubiri hayo “masomo yanayofaa,” alisema kwamba lengo lake “si kujaza habari nyingi akilini mwetu, bali kutuongoza na kutusaidia kutenda ifaavyo.” Huenda utatumia dakika 15 mpaka 20 ukisoma sura hizo, hata hivyo utashangaa jinsi maneno ya Yesu yalivyo rahisi kueleweka na yenye nguvu.

      Sababu nyingine inayofanya Biblia iwe rahisi kueleweka ni habari zilizo ndani yake. Si kitabu cha hekaya au mambo ya kubuniwa. Badala yake, kulingana na The World Book Encyclopedia kwa sehemu kubwa kitabu hicho kinazungumzia “kuhusu watu wakuu na wa kawaida” na pia “changamoto, matumaini, makosa, na mafanikio yao.” Ni rahisi kwetu kuelewa vizuri masimulizi hayo ya watu na matukio halisi na kujifunza masomo muhimu.—Waroma 15:4.

      KINAPATIKANA KWA WOTE

      Ni lazima kitabu kiwe katika lugha unayojua ili uweze kukielewa. Hata iwe unaishi wapi au unatoka taifa gani, huenda Biblia inapatikana katika lugha unayoelewa. Fikiria mambo yanayohusika ili jambo hilo liwezekane.

      Utafsiri. Awali Biblia iliandikwa katika lugha ya Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki. Jambo hilo lilifanya watu wengi wasiojua lugha hizo washindwe kuisoma. Jitihada nyingi zimefanywa na watafsiri wanyoofu ili Biblia ipatikane katika lugha nyingi zaidi. Kwa sababu ya jitihada zao, leo Biblia imetafsiriwa ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 2,700 hivi. Hilo linamaanisha kwamba zaidi ya asilimia 90 ya watu wanaweza kusoma sehemu fulani za Biblia katika lugha yao ya asili.

      Uchapishaji. Awali, maandishi ya Biblia yaliandikwa katika vitu vinavyoweza kuharibika kama vile mafunjo na ngozi. Ili kufikisha ujumbe, maandishi hayo yalinakiliwa kwa uangalifu. Nakala hizo zilikuwa ghali sana na ni watu wachache tu walioweza kununua. Hata hivyo, baada ya uvumbuzi wa mashine ya kuchapa ya Gutenberg miaka 550 iliyopita, uchapishaji wa Biblia uliongezeka sana. Kulingana na ripoti moja, inakadiriwa kwamba nakala zaidi ya bilioni tano za Biblia, zikiwa nzima au kwa sehemu, zimegawanywa.

      Hakuna kitabu chochote cha dini kinacholingana na Biblia. Kwa kweli, Biblia ni kitabu kinachoweza kueleweka. Hata hivyo, huenda isiwe rahisi kwako kuielewa. Lakini, unaweza kusaidiwa. Unaweza kupata wapi msaada huo? Utanufaikaje? Majibu yanapatikana katika makala inayofuata.

      Taarifa Fupi Kuhusu Biblia

      • Biblia ni mkusanyiko wa vitabu vitakatifu 66.

      • Habari zinazopatikana katika Biblia zinatia ndani historia, sheria, unabii, ushairi, methali, nyimbo, na barua.

      • Ilianza kuandikwa mwaka wa 1513 K.W.K. na kumalizika mwaka wa 98 W.K., kwa kipindi cha miaka zaidi ya 1,600.

      • Wanaume 40 hivi waliandika Biblia wakiongozwa na roho ya Mungu.

      Was Life Created?

      Kwa habari zaidi kuhusu chanzo cha uhai, tazama broshua Uhai—Ulitokana na Muumba? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Inapatikana pia katika www.jw.org/sw

      Biblia—Ina ujumbe Gani?

      Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia, tazama broshua Biblia—Ina Ujumbe Gani? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pia, inapatikana kwenye www.jw.org/sw.

  • Kupata Msaada wa Kuielewa Biblia
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Desemba 1
    • Habari Kuu | UNAWEZA KUIELEWA BIBLIA

      Kupata Msaada wa Kuielewa Biblia

      Wazia kwamba umetembelea nchi ya kigeni kwa mara ya kwanza. Kila kitu ni kipya kwako kuanzia mila, watu, vyakula, na hata pesa. Huenda ukahisi kwamba umechanganyikiwa.

      Huenda ukahisi hivyo unaposoma Biblia kwa mara ya kwanza. Unapoisoma, ni kana kwamba unatembelea ulimwengu wa kale kwa mara ya kwanza. Ukiwa huko unakutana na watu wanaoitwa Wafilisti, desturi zisizo za kawaida kama vile ‘kurarua mavazi,’ au unajifunza kula chakula kinachoitwa mana na kutumia sarafu inayoitwa drakma. (Kutoka 16:31; Yoshua 13:2; 2 Samweli 3:31; Luka 15:9) Mambo hayo yote yanaweza kukuchanganya. Sawa tu na kutembelea nchi kwa mara ya kwanza, bila shaka utafurahi sana ukipata mwenyeji atakayekusaidia kuelewa vizuri mambo hayo.

      MSAADA KATIKA NYAKATI ZA KALE

      Wanadamu wamesaidiwa kuyaelewa maandiko matakatifu tangu yalipoanza kuandikwa katika karne ya 16 K.W.K. Kwa mfano, Musa, kiongozi wa kwanza wa taifa la Israeli, ‘alifafanua’ yale yaliyoandikwa.—Kumbukumbu la Torati 1:5.

      Karne kumi baadaye, bado kulikuwa na walimu wenye sifa za kustahili kufundisha Maandiko. Mwaka wa 455 K.W.K., kikundi kikubwa cha Wayahudi kilichotia ndani watoto wengi, kilikusanyika pamoja katika kiwanja cha watu wote jijini Yerusalemu. Walimu wa Biblia ‘walisoma kwa sauti katika kitabu [hichohicho kitakatifu].’ Walifanya jambo lingine pia. “Wakaendelea kufafanua usomaji huo.”—Nehemia 8:1-8.

      Karne tano baadaye, Yesu Kristo pia alifanya kazi hiyo ya kutoa elimu. Alijulikana na watu kuwa mwalimu. (Yohana 13:13) Alifundisha mtu mmoja-mmoja na hata watu wengi. Pindi moja, alizungumza na kusanyiko kubwa la watu na kutoa Mahubiri maarufu ya Mlimani hivi kwamba “umati ukashangazwa na njia yake ya kufundisha.” (Mathayo 5:1, 2; 7:28) Katika mwaka wa 33 W.K., Yesu alizungumza na wanafunzi wake wawili walipokuwa wakitembea kwenda kijiji cha karibu na Yerusalemu na ‘akawafungulia Maandiko.’—Luka 24:13-15, 27, 32.

      Wanafunzi wa Yesu walikuwa pia walimu wa Neno la Mungu. Katika kisa kimoja, ofisa kutoka Ethiopia alikuwa akisoma Maandiko. Mwanafunzi aliyeitwa Filipo alimfuata na kumuuliza: “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” Mwethiopia akasema: “Kwa kweli, ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?” Kisha Filipo akamfafanulia maana ya Maandiko hayo.—Matendo 8:27-35.

      MSAADA KATIKA NYAKATI ZETU

      Kama walimu wa kale wanaotajwa katika masimulizi ya Biblia, Mashahidi wa Yehova leo wanafanya kazi ya kufundisha Biblia katika nchi 239 duniani. (Mathayo 28:19, 20) Kila juma wanawasaidia watu zaidi ya milioni tisa kuelewa Biblia. Wengi wa wale wanaojifunza Biblia si Wakristo. Mafunzo yanatolewa bure na yanaweza kufanywa katika nyumba ya mwanafunzi au popote pale panapofaa. Wengine wamejifunza kupitia simu au kompyuta.

      Tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova ili kupata habari zaidi kuhusu jinsi utakavyoweza kunufaika na mpango huo wa kujifunza. Utagundua kwamba Biblia ni kitabu kinachoeleweka na chenye “faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu,” ili uwe na ‘uwezo kamili, ukiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’—2 Timotheo 3:16, 17.

      Tazama video Kwa Nini Ujifunze Biblia? kwenye www.jw.org/sw

      Tazama video Ni Nini Hutendeka Kwenye Funzo la Biblia? kwenye www.jw.org/sw

      Msaada Kupitia Intaneti

      Mwanamke akitumia tovuti ya jw.org akiwa ameketi katika mgahawa

      Je, ungependa kuijua Biblia bila kuongozwa na mtu? Unaweza kuanza kwa kutembelea tovuti ya jw.org. Tovuti hiyo ina habari zinazohusu Biblia ambazo zinapatikana bila malipo katika lugha zaidi ya 700. Huenda ukafurahia kujifunza mambo yafuatayo:

      Maswali ambayo watu huuliza mara nyingi

      • Ni nini maana ya uhai?

      • Kwa nini watu hufa?

      • Inakuwaje tunapokufa?

      (Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MAJIBU YA MASWALI YA BIBLIA)

      Matatizo unayokabili

      • Unachoweza kufanya unaposhuka moyo

      • Unachoweza kufanya unapokabili ugonjwa wa kudumu

      • Matatizo ya pesa na madeni

      (Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MAJIBU YA MASWALI YA BIBLIA)

      Msaada kwa ajili ya familia

      • Jinsi ya kuacha kugombana

      • Jinsi ya kuwafundisha watoto kutimiza madaraka yao

      • Jinsi ya kuwafundisha watoto wako maadili

      (Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > WENZI WA NDOA NA WAZAZI)

      Ushauri kwa matineja

      • Ufanye nini ukisumbuliwa kingono?

      • Ufanye nini unapoonewa?

      • Ufanye nini unapohisi upweke?

      (Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MATINEJA)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki