Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuzaliwa Mara ya Pili—Je, Ni Njia ya Kupata Wokovu?
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 1
    • Kuzaliwa Mara ya Pili—Je, Ni Njia ya Kupata Wokovu?

      UNGEJIBU jinsi gani swali hili: “Je, umezaliwa mara ya pili?” Mamilioni ya wanadini ulimwenguni wangejibu kwa mkazo, “Ndiyo!” Wanaamini kwamba, kuzaliwa mara ya pili, au kuzaliwa tena, kunawatambulisha Wakristo wote wa kweli na ndiyo njia pekee ya kupata wokovu. Maoni yao ni sawa na ya viongozi fulani wa dini kama mwanatheolojia Robert C. Sproul, aliyeandika hivi: “Ikiwa mtu hajazaliwa mara ya pili, . . . basi yeye si Mkristo.”

      Je, wewe ni mmoja wa wale wanaoamini kwamba kuzaliwa tena ndiyo njia ya kupata wokovu? Ikiwa ndivyo, bila shaka ungependa kuwasaidia watu wa jamaa yako na marafiki waipate njia hiyo na kuanza kuifuata. Lakini ili wafanye hivyo, wanahitaji kuelewa tofauti kati ya mtu aliyezaliwa tena na yule ambaye hajazaliwa tena. Unaweza kuwaeleza jinsi gani maana ya kuzaliwa tena?

      Wengi wanaamini kwamba maneno “kuzaliwa tena” yanarejelea mtu anayetoa ahadi nzito kwamba atamtumikia Mungu na Kristo, na kwa njia hiyo anaanza kuwa na uhusiano na Mungu ambao unakubalika. Kamusi moja ya karibuni inamfafanua mtu aliyezaliwa tena kuwa “Mkristo aliyeokoka.”—TUKI English-Swahili Dictionary—Toleo la Tatu.

      Je, ungeshangaa kujua kwamba Biblia haisemi hivyo? Je, ungependa kujua Neno la Mungu linafundisha nini kuhusu kuzaliwa tena? Bila shaka utafaidika ukichunguza kwa makini habari kuhusu kuzaliwa tena. Kwa nini? Kwa sababu kuelewa kwa usahihi jambo hilo kunahusisha maisha yako na matarajio yako ya wakati ujao.

      Biblia Inafundisha Nini?

      Katika Biblia nzima, maneno “kuzaliwa tena,” au kuzaliwa mara ya pili, yanapatikana tu katika andiko la Yohana 3:1-12, linalosimulia mazungumzo yenye kupendeza kati ya Yesu na kiongozi fulani wa dini huko Yerusalemu. Simulizi hilo lote la Biblia limenukuliwa katika sanduku kwenye ukurasa wa 4. Tunakutia moyo usome habari hiyo kwa makini.

      Katika simulizi hilo, Yesu anakazia mambo kadhaa kuhusu “kuzaliwa upya.”a Kwa kweli, mazungumzo ya Yesu yanatusaidia kujibu maswali haya matano muhimu:

      ◼ Kuzaliwa upya ni muhimu kadiri gani?

      ◼ Je, mtu binafsi anaweza kuamua kuzaliwa upya?

      ◼ Kusudi la kuzaliwa upya ni nini?

      ◼ Mtu anazaliwa upya jinsi gani?

      ◼ Uhusiano kati ya Yehova na yule anayezaliwa upya unabadilika jinsi gani?

      Tutachunguza maswali hayo moja baada ya lingine.

      [Maelezo ya chini]

      a Maneno “kuzaliwa upya” yanapatikana katika 1 Petro 1:3, 23. Maneno hayo ya Biblia yana maana sawa na “kuzaliwa tena,” au kuzaliwa mara ya pili, nayo yanatokana na neno la Kigiriki, gen·naʹo.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]

      “Ninyi Lazima Mzaliwe Tena”

      “Basi kulikuwa na mtu mmoja kati ya Mafarisayo, aliyeitwa Nikodemo, mtawala wa Wayahudi. Huyo alimjia wakati wa usiku na kumwambia: ‘Rabi, tunajua kwamba wewe ukiwa mwalimu umekuja kutoka kwa Mungu; kwa maana hakuna anayeweza kufanya ishara hizi ambazo unafanya isipokuwa Mungu awe pamoja naye.’ Yesu akajibu akamwambia: ‘Kwa kweli kabisa ninakuambia, Mtu asipozaliwa tena, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.’ Nikodemo akamwambia: ‘Mtu anawezaje kuzaliwa akiwa mzee? Je, anaweza kuingia katika tumbo la uzazi la mama yake mara ya pili na kuzaliwa?’ Yesu akajibu: ‘Kwa kweli kabisa ninakuambia, Mtu asipozaliwa kwa maji na roho, hawezi kuingia katika ufalme wa Mungu. Kile ambacho kimezaliwa kwa mwili ni mwili, na kile ambacho kimezaliwa kwa roho ni roho. Usistaajabu kwa sababu nimekuambia, Ninyi lazima mzaliwe tena. Upepo huvuma mahali ambapo unataka, nawe unasikia mvumo wake, lakini hujui mahali ambapo huo unatoka wala mahali unapoenda. Ndivyo alivyo kila mtu ambaye amezaliwa kwa roho.’ Nikodemo akajibu, akamwambia: ‘Mambo haya yanaweza kutukia jinsi gani?’ Yesu akajibu, akamwambia: ‘Je, wewe ni mwalimu wa Israeli na bado hujui mambo haya? Kwa kweli kabisa ninakuambia, Yale tunayoyajua tunayasema na yale ambayo tumeyaona tunatoa ushahidi juu yake, lakini ninyi hampokei ushahidi ambao tunatoa. Ikiwa nimewaambia ninyi mambo ya duniani na bado hamwamini, mtaamini jinsi gani nikiwaambia mambo ya mbinguni?’” —Yohana 3:1-12.

  • Kuzaliwa Upya—Je, Ni Muhimu?
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 1
    • Kuzaliwa Upya—Je, Ni Muhimu?

      KATIKA mazungumzo yake yote na Nikodemo, Yesu alikazia kwamba kuzaliwa upya, au kuzaliwa tena, ni muhimu sana. Alisema nini ili kuonyesha jambo hilo waziwazi?

      Ona jinsi Yesu alivyokazia umuhimu wa kuzaliwa upya alipozungumza na Nikodemo. Alisema: “Mtu asipozaliwa tena, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:3) Maneno “asipozaliwa tena” na “hawezi” yanaonyesha kwamba ni lazima mtu azaliwe upya. Kwa mfano: Mtu akisema, “Jua lisipowaka, hakuwezi kuwa na mwangaza wa mchana,” anamaanisha kwamba ni lazima jua liwake ili kuwe na mwangaza wa mchana. Vivyo hivyo, Yesu alisema kwamba kuzaliwa tena ni jambo la lazima kabisa ili kuuona Ufalme wa Mungu.

      Kisha Yesu akasema, “Ninyi lazima mzaliwe tena,” kana kwamba anataka kuondoa shaka yoyote kuhusu kuzaliwa tena. (Yohana 3:7) Ni wazi kwamba kulingana na Yesu kuzaliwa tena ni takwa—jambo la lazima—ili mtu ‘aingie katika Ufalme wa Mungu.’—Yohana 3:5.

      Kwa kuwa Yesu aliona kuzaliwa upya kuwa jambo muhimu sana, Wakristo wanapaswa kuhakikisha kwamba wanaelewa jambo hili kwa usahihi. Kwa mfano, je, unafikiri Mkristo anaweza kuchagua kuzaliwa tena?

      [Blabu katika ukurasa wa 5]

      “Jua lisipowaka, hakuwezi kuwa na mwangaza wa mchana”

  • Kuzaliwa Upya—Je, Ni Uamuzi wa Mtu Binafsi?
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 1
    • Kuzaliwa Upya—Je, Ni Uamuzi wa Mtu Binafsi?

      NI NANI anayefanya mtu azaliwe upya? Wahubiri fulani wananukuu maneno haya ya Yesu wanapowahimiza wasikilizaji wao wazaliwe tena: “Ninyi lazima mzaliwe tena.” (Yohana 3:7) Wahubiri hao wanatumia maneno hayo kana kwamba ni amri, wakiwaambia watu wazaliwe tena. Hivyo wanahubiri kwamba kila mwamini anapaswa kumtii Yesu na kuchukua hatua zinazohitajiwa ili azaliwe upya. Kulingana na maoni yao, mtu binafsi anaweza kuchagua kuzaliwa upya. Lakini je, maoni hayo yanapatana na mambo ambayo Yesu alimwambia Nikodemo?

      Unaposoma kwa makini maneno ya Yesu, utaona kuwa yeye hakufundisha kwamba mtu binafsi ndiye anayechagua kuzaliwa upya. Kwa nini tunasema hivyo? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kuzaliwa tena’ linaweza pia kutafsiriwa “kuzaliwa kutoka juu.”a Hivyo, mtu anazaliwa upya “kutoka juu,” yaani, “kutoka mbinguni,” au “kutoka kwa Baba.” (Yohana 19:11; Yakobo 1:17) Ndiyo, Mungu ndiye anayefanya mtu azaliwe upya.—1 Yohana 3:9.

      Tukikumbuka kwamba neno la awali la Kigiriki linaweza kumaanisha kuzaliwa “kutoka juu,” si vigumu kuelewa kwa nini mtu binafsi hawezi kuchagua kuzaliwa upya. Fikiria kuzaliwa kwako mwenyewe. Je, uliweza kuchagua kuzaliwa? Hapana. Vivyo hivyo, si juu ya mwamini kuchagua kuzaliwa upya. Tunaweza kuzaliwa upya tu kwa sababu Mungu, Baba yetu wa mbinguni, anafanya tuzaliwe upya. (Yohana 1:13) Hivyo, kwa kufaa mtume Petro anasema hivi: “Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa maana kulingana na rehema yake kubwa alituzaa sisi upya.”—1 Petro 1:3.

      Je, Yesu Alituamuru Tuzaliwe Tena?

      Huenda wengine wakauliza, ‘Ikiwa ni kweli kwamba mtu binafsi hawezi kuchagua kuzaliwa tena, kwa nini Yesu alitoa amri hii: “Ninyi lazima mzaliwe tena”?’ Hilo ni swali zuri. Kwa sababu, kama maneno ya Yesu ni amri, basi angekuwa akituagiza tufanye jambo tusiloweza, na Yesu hangetoa amri kama hiyo. Hivyo basi, maneno lazima “mzaliwe tena” yaeleweke jinsi gani?

      Unapotazama kwa makini lugha ya awali utaona kwamba maneno hayo hayaonyeshi kwamba Yesu alitoa amri. Alikuwa akitoa maelezo tu. Kwa maneno mengine, Yesu aliposema lazima “mzaliwe tena,” alikuwa akieleza ukweli wa mambo, hakutoa amri. Alisema: “Hamna budi kuzaliwa kutoka juu.”—Yohana 3:7, Modern Young’s Literal Translation.

      Ili kuelewa tofauti kati ya kutoa amri na kueleza jambo, fikiria mfano huu. Wazia jiji ambalo lina shule kadhaa. Mojawapo ya shule hizo imetengwa kwa ajili ya wanafunzi ambao ni watoto wa wenyeji wanaoishi mbali na jiji. Siku moja, mwanamume kijana ambaye si mwenyeji anamwambia mkuu wa shule hivi: “Ninataka kujiunga na shule yenu.” Mkuu huyo anamwambia, “Ili ujiunge na shule hii, lazima uwe mwenyeji.” Kwa kweli, maneno ya mkuu wa shule si amri. Hamwagizi mwanafunzi huyo, “Uwe mwenyeji!” Mkuu wa shule anaeleza tu ukweli wa mambo, yaani, takwa la kujiunga na shule hiyo. Vivyo hivyo, Yesu aliposema: “Ninyi lazima mzaliwe tena,” alikuwa tu anaeleza ukweli wa mambo, yaani, takwa la “kuingia katika Ufalme wa Mungu.”

      Wazo hilo la mwisho, yaani, Ufalme wa Mungu, linahusiana na swali lingine kuhusu kuzaliwa upya. Swali hilo ni: Kusudi la kuzaliwa upya ni nini? Kujua jibu la swali hilo ni muhimu ili kuelewa kwa usahihi maana ya kuzaliwa tena.

      [Maelezo ya chini]

      a Katika Biblia kadhaa, Yohana 3:3 limetafsiriwa kwa njia hiyo. Kwa mfano, A Literal Translation of the Bible inasema: “Mtu asipozaliwa kutoka juu, hawezi kuuona Ufalme wa Mungu.”

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Kuzaliwa upya na kuzaliwa kihalisi kunafanana jinsi gani?

  • Kuzaliwa Upya—Kusudi Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 1
    • Kuzaliwa Upya—Kusudi Ni Nini?

      WATU wengi wanaamini kwamba mtu anahitaji kuzaliwa tena ili kupokea wokovu wa milele. Hata hivyo, ona vile Yesu mwenyewe alivyosema kuhusu kusudi la kuzaliwa upya. Alisema: “Mtu asipozaliwa tena, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:3) Hivyo, mtu anahitaji kuzaliwa tena ili kuingia katika Ufalme wa Mungu, si ili kupata wokovu. Huenda wengine wakauliza, ‘Je, semi hizi mbili—kuingia katika Ufalme, na kupata wokovu—zinarejelea thawabu ileile?’ Hapana. Ili kuelewa tofauti, tutafikiria kwanza maana ya maneno “ufalme wa Mungu.”

      Ufalme ni aina fulani ya serikali. Kwa hiyo, maneno “ufalme wa Mungu” yanamaanisha “serikali ya Mungu.” Biblia inafundisha kwamba Yesu Kristo, “mwana wa binadamu,” ndiye Mfalme wa Ufalme wa Mungu na kwamba Kristo atatawala pamoja na wengine. (Danieli 7:1, 13, 14; Mathayo 26:63, 64) Isitoshe, maono fulani ambayo mtume Yohana alipokea yanafunua kwamba wale watakaotawala pamoja na Kristo wamechaguliwa “kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa,” nao “watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:9, 10; 20:6) Pia, Neno la Mungu linafunua kuwa wale watakaotawala wakiwa wafalme ni “kundi dogo” la watu 144,000 “ambao wamenunuliwa kutoka duniani.”—Luka 12:32; Ufunuo 14:1, 3.

      Ufalme wa Mungu uko wapi? “Ufalme wa Mungu” pia unaitwa “ufalme wa mbinguni,” jambo linaloonyesha kwamba Yesu na wafalme wenzake watatawala kutoka mbinguni. (Luka 8:10; Mathayo 13:11) Hivyo, Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni ambayo mtawala wake ni Yesu Kristo pamoja na kikundi cha watawala wenzake ambao wamechaguliwa kutoka kati ya wanadamu.

      Kwa hiyo, Yesu alimaanisha nini aliposema ni lazima mtu azaliwe tena ili “kuingia katika ufalme wa Mungu”? Alimaanisha kwamba mtu anahitaji kuzaliwa tena ili awe mtawala pamoja na Kristo mbinguni. Kwa wazi, kusudi la kuzaliwa upya ni kutayarisha kikundi cha wanadamu wachache kuwa watawala mbinguni.

      Kufikia hapa, tumeona kwamba kuzaliwa upya ni muhimu sana, Mungu ndiye anayeamua kama mtu atazaliwa upya, na kwamba kuzaliwa upya kunawatayarisha wanadamu fulani kuwa watawala mbinguni. Lakini mtu anazaliwa upya jinsi gani?

      [Blabu katika ukurasa wa 7]

      Kusudi la kuzaliwa upya ni kutayarisha kikundi cha wanadamu wachache kuwa watawala mbinguni

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Yesu Kristo na kikundi cha wanadamu waliochaguliwa kutoka kati ya wanadamu watatawala katika Ufalme wa Mungu

  • Kuzaliwa Upya—Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 1
    • Kuzaliwa Upya—Jinsi Gani?

      YESU alizungumza na Nikodemo kuhusu umuhimu wa kuzaliwa upya, yule anayefanya mtu azaliwe upya, kusudi la kuzaliwa upya, na pia jinsi mtu anavyozaliwa upya. Yesu alisema: “Mtu asipozaliwa kwa maji na roho, hawezi kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:5) Hivyo, mtu anazaliwa tena kwa maji na roho. Lakini maneno “maji na roho” yanarejelea nini?

      Maana ya “Maji na Roho”

      Kwa kuwa Nikodemo alikuwa msomi wa Dini ya Kiyahudi, hapana shaka alijua jinsi Maandiko ya Kiebrania yanavyotumia maneno “roho ya Mungu”—nguvu za utendaji za Mungu zinazoweza kuwafanya watu watende maajabu. (Mwanzo 41:38; Kutoka 31:3; 1 Samweli 10:6) Kwa hiyo, Yesu alipotumia neno “roho,” Nikodemo alielewa kwamba alimaanisha roho takatifu, yaani, nguvu za utendaji za Mungu.

      Yesu alimaanisha nini alipotaja maji? Angalia matukio yanayotangulia na yanayofuata mazungumzo ya Yesu na Nikodemo. Yanaonyesha kwamba Yohana Mbatizaji na wanafunzi wa Yesu walibatiza kwa maji. (Yohana 1:19, 31; 3:22; 4:1-3) Ubatizo huo ulijulikana sana huko Yerusalemu. Kwa hiyo, Yesu alipotaja maji, Nikodemo alitambua kwamba alikuwa akizungumza kuhusu maji ya ubatizo bali si maji tu kwa ujumla.a

      Kubatizwa “kwa Roho Takatifu”

      Ikiwa “kuzaliwa kwa maji” kunahusiana na kubatizwa kwa maji, ‘kuzaliwa kwa roho’ kunamaanisha nini? Kabla ya mazungumzo ya Nikodemo na Yesu, Yohana Mbatizaji alikuwa ametangaza kwamba maji na pia roho ingetumika katika kubatiza. Alisema: “Mimi niliwabatiza ninyi kwa maji, lakini yeye [Yesu] atawabatiza ninyi kwa roho takatifu.” (Marko 1:7, 8) Mwandikaji wa Injili anayeitwa Marko anataja wakati wa kwanza ambapo ubatizo wa aina hiyo ulifanywa. Anaandika: “Baada ya siku hizo Yesu akaja kutoka Nazareti ya Galilaya, Yohana akambatiza katika Yordani. Mara moja alipopanda kutoka majini akaona mbingu zikifunguka, na roho ikashuka juu yake kama njiwa.” (Marko 1:9, 10) Yesu alipozamishwa katika Mto Yordani, alibatizwa kwa maji. Mara alipopokea roho kutoka mbinguni, alibatizwa kwa roho takatifu.

      Miaka mitatu hivi baada ya kubatizwa, Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake hivi: “Ninyi mtabatizwa kwa roho takatifu siku chache baadaye.” (Matendo 1:5) Walibatizwa kwa roho wakati gani?

      Siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wa Yesu wapatao 120 walikuwa wamekusanyika katika nyumba fulani huko Yerusalemu. “Ghafula kukatokea kutoka mbinguni kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma, nao ukaijaza nyumba yote ambamo walikuwa wameketi. Nao wakaona ndimi kama za moto . . . , nao wote wakajazwa roho takatifu.” (Matendo 2:1-4) Siku hiyohiyo, watu wengine huko Yerusalemu walihimizwa wabatizwe kwa maji. Mtume Petro aliuambia umati hivi: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu, nanyi mtapokea zawadi ya bure ya roho takatifu.” Watu hao walifanya nini? “Wale waliokubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo wakabatizwa, na katika siku hiyo nafsi karibu elfu tatu zikaongezwa.”—Matendo 2:38, 41.

      Kubatizwa kwa Njia Mbili

      Ubatizo wa maji na wa roho takatifu unafunua nini kuhusu kuzaliwa upya? Unaonyesha kwamba mtu anahitaji kubatizwa kwa njia mbili ili azaliwe upya. Ona kwamba Yesu alibatizwa kwanza kwa maji. Kisha akapokea roho takatifu. Vivyo hivyo, wanafunzi wa kwanza walibatizwa kwanza kwa maji (baadhi yao na Yohana Mbatizaji), kisha wakapokea roho takatifu. (Yohana 1:26-36) Pia, wale wanafunzi wapya 3,000 walibatizwa kwanza kwa maji, kisha wakapokea roho takatifu.

      Tunapozingatia kwamba wanafunzi wapya walibatizwa kwa njia mbili siku ya Pentekoste 33 W.K., tutatarajia mtu azaliwe upya kwa njia gani leo? Katika njia ileile ambayo mitume wa Yesu na wanafunzi wake wa kwanza walizaliwa upya. Kwanza mtu anatubu dhambi zake, anageuka na kuacha mwenendo mbaya, anajiweka wakfu kwa Yehova ili kumwabudu na kumtumikia, na kuonyesha hadharani kwamba amejiweka wakfu kwa kubatizwa kwa maji. Kisha, Mungu akimchagua kuwa mtawala katika Ufalme Wake, anamtia mafuta kwa roho takatifu. Mtu mwenyewe ndiye anayechukua hatua ya kwanza ya kubatizwa kwa maji, lakini Mungu ndiye anayechukua hatua ya pili ya kumbatiza kwa roho. Hivyo, mtu anazaliwa upya anapobatizwa katika njia zote mbili.

      Lakini kwa nini Yesu alitumia maneno ‘kuzaliwa kwa maji na roho’ alipozungumza na Nikodemo? Alikuwa akikazia kwamba hali ya wale wanaobatizwa kwa maji na kwa roho inabadilika sana. Habari inayofuata inazungumzia badiliko hilo linalotokana na kuzaliwa upya.

      [Maelezo ya chini]

      a Vivyo hivyo, pindi moja mtume Petro alisema hivi kuhusu watu waliotaka kubatizwa: “Je, mtu yeyote anaweza kuyakataza maji?”—Matendo 10:47.

      [Picha katika ukurasa wa 9]

      Yohana aliwabatiza kwa maji Waisraeli waliotubu

  • Kuzaliwa Upya—Kunatimiza Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 1
    • Kuzaliwa Upya—Kunatimiza Nini?

      KWA nini Yesu alitumia maneno ‘kuzaliwa kwa roho’ alipozungumzia kubatizwa kwa roho takatifu? (Yohana 3:5) Neno “kuzaliwa” linapotumiwa kwa njia ya mfano linamaanisha “mwanzo.” Hivyo, maneno “kuzaliwa upya” yanamaanisha “mwanzo mpya.” Kwa hiyo, maneno ya mfano “kuzaliwa” na “kuzaliwa upya” yanakazia kwamba uhusiano kati ya Mungu na wale wanaobatizwa kwa roho takatifu utakuwa na mwanzo mpya. Badiliko hilo katika uhusiano linatokea jinsi gani?

      Alipoeleza jinsi Mungu anavyowatayarisha wanadamu ili watawale mbinguni, mtume Paulo alitumia mfano wa familia. Aliwaandikia Wakristo wa siku zake kwamba ‘wangefanywa kuwa wana’ na kwa hiyo Mungu angewatendea “kama wana.” (Wagalatia 4:5; Waebrania 12:7) Ili kuona jinsi mfano wa kufanywa kuwa mwana unavyomsaidia mtu kuelewa badiliko linalotokea mtu anapobatizwa kwa roho takatifu, fikiria tena ule mfano wa mwanamume kijana anayetaka kujiunga na shule ya wanafunzi ambao ni watoto wa wenyeji.

      Badiliko Linalotokana na Kufanywa Kuwa Mwana

      Katika mfano huo, kijana huyo hawezi kujiunga na shule hiyo kwa sababu yeye si mwenyeji. Sasa, wazia kwamba siku moja, badiliko kubwa linatokea. Kijana huyo anafanywa kuwa mwana kisheria na baba katika familia ya wenyeji. Jambo hilo linaleta mabadiliko gani kwa yule kijana? Kwa sababu amefanywa kuwa mwana, sasa anaweza kuwa na haki sawa na vijana wenyeji—kutia ndani haki ya kujiunga na ile shule. Kufanywa kuwa mwana kisheria kumebadili kabisa maisha yake.

      Jambo hilo linafanana na yale yanayowapata wale wanaozaliwa upya, ingawa kwa njia kubwa zaidi. Fikiria mambo kadhaa yanayofanana. Yule kijana katika mfano atakubaliwa katika ile shule mradi tu atimize takwa la kujiunga na shule hiyo, yaani, kuwa mwenyeji kisheria. Lakini hawezi kutimiza takwa hilo bila msaada. Vivyo hivyo, wanadamu fulani watakuwa watawala katika Ufalme wa Mungu, au serikali ya mbinguni, mradi tu watimize takwa la kuingia humo, yaani, “kuzaliwa tena.” Hata hivyo, hawawezi kutimiza takwa hilo bila msaada kwa sababu Mungu ndiye anayefanya mtu azaliwe upya.

      Ni nini kilichobadili hali ya yule kijana? Kufanywa kuwa mwana kisheria. Bila shaka, asili ya kijana yule haikubadilika alipofanywa kuwa mwana, bado alikuwa mtu yuleyule. Hata hivyo, baada ya kufanywa kuwa mwana kisheria, hali ya kijana huyo ilibadilika. Alikuwa na mwanzo mpya, kana kwamba amezaliwa upya. Alikubaliwa kuwa mwana kisheria, jambo lililompa haki ya kujiunga na ile shule na pia kuwa mtoto wa familia ya yule baba aliyemfanya kuwa mwana.

      Vivyo hivyo, Yehova alibadili hali ya wanadamu wasio wakamilifu kwa kuanzisha mpango wa kisheria wa kuwafanya kuwa watoto wake. Mtume Paulo aliyekuwa mmoja wa watoto hao aliwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Mlipokea roho ya kufanywa kuwa wana, roho ambayo kupitia hiyo tunapaaza sauti: ‘Abba, Baba!’ Roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu.” (Waroma 8:15, 16) Ndiyo, kwa kufanywa kuwa wana, Wakristo hao walifanywa kuwa sehemu ya familia ya Mungu, au “watoto wa Mungu.”—1 Yohana 3:1; 2 Wakorintho 6:18.

      Kusema kweli, asili ya wale ambao Mungu aliwafanya kuwa wana haikubadilika, kwa kuwa bado walikuwa watu wasio wakamilifu. (1 Yohana 1:8) Hata hivyo, kama Paulo alivyoendelea kueleza, baada ya matakwa ya kisheria ya kufanywa kuwa wana kutimizwa, hali yao ilibadilika. Wakati huohuo, roho ya Mungu iliwapa usadikisho wenye nguvu sana kwamba wangeishi mbinguni pamoja na Kristo. (1 Yohana 3:2) Usadikisho huo waliopewa na roho takatifu uliwafanya wawe na maoni tofauti kabisa kuhusu maisha. (2 Wakorintho 1:21, 22) Ndiyo, walikuwa na mwanzo mpya—walizaliwa upya kwa njia ya mfano.

      Biblia inasema hivi kuwahusu wanadamu waliofanywa kuwa wana na Mungu: “Watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.” (Ufunuo 20:6) Wanadamu waliofanywa kuwa wana na Mungu watakuwa wafalme katika Ufalme wa Mungu, au serikali ya mbinguni, pamoja na Kristo. Mtume Petro aliwaambia Wakristo wenzake kwamba wangepokea “urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia” ambao “umewekwa akiba mbinguni” kwa ajili yao. (1 Petro 1:3, 4) Huo ni urithi wenye thamani kama nini!

      Hata hivyo, habari hiyo kuhusu utawala pia inazusha swali hili: Ikiwa wale waliozaliwa tena watatawala wakiwa wafalme mbinguni, watatawala akina nani? Swali hilo litajibiwa katika habari inayofuata.

      [Picha katika ukurasa wa 10]

      Paulo alisema nini kuhusu kufanywa kuwa wana?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki