Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Biblia Iliokoka Kuharibika
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 4
    • HABARI KUU | JINSI BIBLIA ILIVYOOKOKA

      Biblia Iliokoka Kuharibika

      TATIZO: Waandishi wa Biblia na wanakili waliandika ujumbe wa Biblia kwenye ngozi na mafunjo.a (2 Timotheo 4:13) Vifaa hivyo vilihatarishaje Biblia?

      Mafunjo huchanika, huchuja rangi na kuchakaa haraka. Wachimbuzi wa vitu vya kale huko Misri, Richard Parkinson na Stephen Quirke, walisema: “Karatasi za mafunjo zinaweza kuoza na kuwa udongo. Zinapohifadhiwa kwa kufukiwa ardhini, zinaweza kuharibika kwa sababu ya kuvu au kutu na zinaweza kuliwa na panya au wadudu, hasa mchwa.” Baada ya mafunjo fulani kupatikana, yaliharibika haraka kwa sababu ya unyevu au joto kali.

      Ngozi hudumu kuliko mafunjo, hata hivyo, ikiwa ngozi itahifadhiwa kwenye mazingira yenye joto kali, unyevu, mwanga au isipotunzwa vizuri inaweza kuharibika.b Pia ngozi inaweza kuharibiwa na wadudu. Ndiyo sababu nakala nyingi za kale hazijadumu mpaka leo. Ikiwa Biblia ingeharibika, basi ujumbe wake haungekuwepo.

      JINSI BIBLIA ILIVYOOKOKA: Sheria ya Wayahudi ilimwagiza kila mfalme ‘kujiandikia katika kitabu nakala ya sheria hii’ yaani, vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. (Kumbukumbu la Torati 17:18) Kwa kuongezea, wanakili wenye ustadi walinakili hati nyingi hivi kwamba kufikia karne ya kwanza W.K, Maandiko yangeweza kupatikana katika masinagogi yote nchini Israeli na hata katika maeneo ya mbali ya Makedonia! (Luka 4:16, 17; Matendo 17:11) Baadhi ya hati hizo za kale ziliokoka jinsi gani hadi kufika wakati wetu?

      1. Mtungi wa udongo; 2. Sehemu ya kitabu cha kukunjwa ya Bahari ya Chumvi

      Hati zinazojulikana kama Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi zilidumu kwa miaka mingi kwenye mitungi ya udongo iliyohifadhiwa katika mapango yaliyo katika maeneo yenye ukame.

      ango ambalo baadhi ya hati za kale za Biblia ziligunduliwa

      Msomi wa Agano Jipya Philip W. Comfort alisema: “Wayahudi walikuwa na kawaida ya kuhifadhi hati-kunjo za Maandiko kwenye mitungi.” Inaonekana kwamba Wakristo waliendelea na desturi hiyo. Hivyo, baadhi ya hati za kale za Biblia zimepatikana kwenye mitungi ya udongo, mapango yenye giza na katika maeneo yenye ukame sana.

      MATOKEO: Maelfu ya sehemu za hati za Biblia zilizo na zaidi ya miaka 2,000 hivi zimedumu kufikia sasa. Hakuna kitabu kingine chochote cha awali kilicho na hati nyingi za kale kama Biblia.

      a Mafunjo ni karatasi ambazo hutengenezwa kutokana na mmea unaoota sehemu zenye maji uitwao mfunjo. Ngozi iliandaliwa kutokana na ngozi za wanyama.

      b Kwa mfano, nakala rasmi ya U.S. Declaration of Independence iliandikwa katika ngozi. Kufikia sasa hati hiyo ambayo hata haijafikia miaka 250, imechuja rangi hivi kwamba maandishi yake hayawezi kusomeka.

  • Biblia Iliokoka Upinzani
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 4
    • HABARI KUU | JINSI BIBLIA ILIVYOOKOKA

      Biblia Iliokoka Upinzani

      TATIZO: Wanasiasa na viongozi wengi wa dini walikuwa na malengo yaliyopingana na ujumbe wa Biblia. Mara nyingi, walitumia mamlaka yao kuwakataza watu kumiliki, kuchapisha, au kutafsiri Biblia. Fikiria mifano miwili:

      • Karibu mwaka wa 167 K.W.K.: Mfalme Antioko Epifane wa Seleuko alijaribu kuwalazimisha Wayahudi wajiunge na dini ya Kigiriki kwa kuamuru nakala zote za Maandiko ya Kiebrania ziharibiwe. Mwanahistoria Heinrich Graetz aliandika hivi: “Maofisa wake walichana na kuchoma vitabu vya kukunjwa vya Sheria popote walipovipata, na wale wote waliosoma vitabu hivyo ili kupata faraja, waliuawa.”

      • Enzi za Kati: Baadhi ya viongozi wa Kanisa Katoliki walikasirika walipowaona watu wa kawaida wakihubiri kweli za Biblia badala ya mafundisho ya Kikatoliki. Hivyo mtu yeyote aliyemiliki vitabu vingine vya Biblia zaidi ya Zaburi ya Kilatini alionwa kuwa mwasi. Baraza moja la kanisa lilitekeleza amri hiyo kwa kuwaagiza wanaume “wawatafute waasi hao kwa uangalifu, uaminifu na bidii. . . kwa kupekua nyumba zote na vyumba vya chini walivyotilia shaka. . . . Nyumba yoyote ambayo wangempata mwasi walipaswa kuiharibu.”

      Ikiwa maadui wa Biblia wangefaulu kuiangamiza, ujumbe wake ungepotea.

      Ukurasa wa tafsiri ya kiingereza ya William Tyndale

      Tafsiri ya Kiingereza ya William Tyndale iliokoka licha ya marufuku, kuchomwa kwa Biblia na hata kuuawa kwa Tyndale mwenyewe mwaka wa 1536

      JINSI BIBLIA ILIVYOOKOKA: Mfalme Antioko alielekeza kampeni zake huko Israeli, hata hivyo, Wayahudi walikuwa wametawanyika katika nchi nyingine nyingi. Wasomi wanakadiria kwamba kufikia karne ya kwanza, zaidi ya asilimia 60 ya Wayahudi hawakuishi Israeli. Wayahudi walihifadhi nakala za Maandiko katika masinagogi yao, Maandiko ambayo yalitumiwa baadaye na vizazi vyao, kutia ndani Wakristo.—Matendo 15:21.

      Wakati wa Enzi za Kati, watu walioipenda Biblia walivumilia upinzani na wakaendelea kutafsiri na kunakili Maandiko. Hata kabla ya kubuniwa kwa mashine za kuchapa katikati ya karne ya 15, sehemu fulani za Biblia zilipatikana katika lugha 33 hivi. Baadaye, Biblia ilitafsiriwa na kuchapishwa kwa wingi zaidi.

      MATOKEO: Licha ya upinzani kutoka kwa wafalme wenye nguvu na viongozi wa dini waliopotoshwa, Biblia imekuwa kitabu pekee kilichotafsiriwa kwa lugha nyingi na kugawanywa katika maeneo mengi. Biblia imeboresha sheria na lugha katika nchi fulani, na imewasaidia watu wengi kubadili maisha yao.

  • Biblia Iliokoka Jitihada za Kubadili Ujumbe Wake
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 4
    • Mnakili akinakili Biblia

      Wamasora walinakili Maandiko kwa uangalifu

      HABARI KUU | JINSI BIBLIA ILIVYOOKOKA

      Biblia Iliokoka Jitihada za Kubadili Ujumbe Wake

      TATIZO: Biblia imedumu licha ya upinzani na uwezekano wa kuharibika kwa vifaa vya kuandikiwa. Hata hivyo, baadhi ya wanakili na watafsiri wamejaribu kubadili ujumbe wa Biblia. Nyakati nyingine, wamejaribu kubadili ujumbe wa Biblia ili ufaane na mafundisho yao, badala ya mafundisho yao kupatana na ya Biblia. Fikiria mifano kadhaa:

      • Mahali pa ibada: Kati ya karne ya pili na ya nne K.W.K., waandishi wa Pentateuki ya Wasamaria waliongezea maneno haya katika Kutoka 20:17 “katika Mlima Gerizimu. Na huko utajenga madhabahu.” Wasamaria walikusudia Maandiko yaunge mkono ujenzi wao wa hekalu lililokuwa katika Mlima Gerizimu.

      • Fundisho la Utatu: Miaka 300 hivi baada ya Biblia kuandikwa, mwandishi wa fundisho la Utatu aliongezea maneno haya katika andiko la 1 Yohana 5:7 “mbinguni, Baba, na Neno, na Roho Mtakatifu, na watatu hawa ni umoja.” Maneno hayo hayakupatikana katika maandishi ya awali. Msomi wa Biblia Bruce Metzger anasema hivi: “Kuanzia karne ya sita na kuendelea, maneno hayo yalipatikana mara nyingi zaidi kwenye hati za Kilatini cha Zamani na Vulgate ya Kilatini.”

      • Jina la Mungu: Watafsiri wengi wa Biblia waliamua kuondoa jina la Mungu kwenye Maandiko kwa sababu ya kufuata desturi za kishirikina za Wayahudi. Badala ya kutumia jina Yehova, walitumia majina ya cheo kama vile, “Mungu” au “Bwana.” Majina hayo yanapotumiwa kwenye Biblia yanaweza kurejelea Muumba, wanadamu, vitu vinavyoabudiwa na hata Ibilisi. —Yohana 10:34, 35; 1 Wakorintho  8:5, 6; 2 Wakorintho 4:4.a

      JINSI BIBLIA ILIVYOOKOKA: Baadhi ya wanakili wa Biblia walikuwa wadanganyifu au hawakuwa waangalifu, hata hivyo wanakili wengi walikuwa stadi na makini sana. Kati ya karne ya sita na ya kumi W.K., Wamasora walinakili Maandiko ya Kiebrania na kutokeza maandishi yanayojulikana kuwa maandishi ya Wamasora. Inaripotiwa kwamba Wamasora walihesabu maneno na herufi ili kuhakikisha kwamba wamenakili kwa usahihi. Walipohisi kwamba nakala za maandishi ya Kiebrania walizotumia zina makosa, waliandika makosa hayo pambizoni. Wamasora hawakubadili maandishi ya Biblia. Profesa Moshe Goshen-Gottstein aliandika hivi: “Wamasora waliona kubadili Maandiko kimakusudi kuwa uhalifu mkubwa sana.”

      Pili, kwa kuwa hati nyingi za kale zinapatikana leo, wasomi wa Biblia wanaweza kutambua makosa kwa njia rahisi. Kwa mfano, kwa miaka mingi viongozi wa dini walifundisha kwamba tafsiri ya Biblia yao ya Kilatini ilikuwa sahihi. Hata hivyo, kama ilivyotajwa mwanzoni mwa makala hii waliongeza maneno yasiyo sahihi katika 1 Yohana 5:7. Makosa hayo yaliandikwa pia katika tafsiri ya Kiingereza ya King James Version! Hata hivyo, hati nyingine za kale zilizogunduliwa zilionyesha nini? Bruce Metzger aliandika: “Maneno [yaliyo kwenye 1 Yohana 5:7] hayapatikani kwenye hati zote za awali (Kisiria, Kikoptiki, Kiarmenia, Kiethiopia, Kiarabu, Kislavonia) isipokuwa kwenye tafsiri ya Kilatini pekee.” Kwa sababu hiyo, tafsiri zilizoboreshwa za King James Version na Biblia nyingine zimeondoa fungu hilo la maneno lisilo sahihi.

      Chester Beatty P46, hati ya mafunjo ya Biblia ya mwaka wa 200 W.K.

      Chester Beatty P46, hati ya mafunjo ya Biblia ya mwaka wa 200 W.K.

      Je, hati za zamani zinathibitisha kwamba ujumbe wa Biblia umeokoka? Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi vilipopatikana mwaka wa 1947, wasomi waliweza kulinganisha maandishi ya Kiebrania ya Wamasora na ya vitabu hivyo vilivyoandikwa zaidi ya miaka elfu moja iliyopita. Mhariri mmoja wa Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi alisema kwamba nakala moja “inatoa uthibitisho usiokanushika kwamba Wayahudi walionakili maandishi ya Biblia katika kipindi cha zaidi ya miaka elfu moja, walifanya kazi hiyo kwa uaminifu na uangalifu mkubwa.”

      Mafunjo ya vitabu vingi vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanapatikana katika Maktaba ya Chester Beatty iliyo Dublin, nchini Ireland, kutia ndani hati za kuanzia karne ya pili W.K., miaka 100 hivi baada ya Biblia kuandikwa. The Anchor Bible Dictionary inasema hivi: “Zaidi ya kuwa na habari nyingi mpya, pia Mafunjo yanaonyesha umakini wa ajabu katika historia ya kunakili maandishi ya Biblia.”

      “Tunaweza kusema kwa uhakika kwamba hakuna maandishi mengine ya kale yaliyonakiliwa kwa usahihi kama hayo.”

      MATOKEO: Kupatikana kwa hati nyingi za kale za maandishi ya Biblia, kumesaidia kuiboresha badala ya kuipotosha. Sir Frederic Kenyon aliandika hivi kuhusu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo: “Hakuna kitabu kingine cha zamani kilicho na uthibitisho mwingi na wa awali kama Biblia na hakuna msomi anayeweza kudai kwamba maandishi tuliyo nayo si ya kweli.” Naye msomi William Henry Green aliandika hivi kuhusiana na Maandiko ya Kiebrania: “Tunaweza kusema kwa uhakika kwamba hakuna maandishi mengine ya kale yaliyonakiliwa kwa usahihi kama hayo.”

      a Kwa habari zaidi, soma nyongeza iliyo kwenye ukurasa wa 195-197 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kinachopatikana kwenye www.jw.org/sw.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki