Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Kweli Yalitukia?
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 2
    • Mwili wa Yesu ukiondolewa kutoka katika mti wa mateso wanafunzi wake wakitazama kutoka mbali

      HABARI KUU | KWA NINI YESU ALITESEKA NA KUFA?

      Je, Kweli Yalitukia?

      Mwaka wa 33 W.K., Yesu Mnazareti aliuawa. Alishtakiwa kwa uwongo kuwa mchochezi, akapigwa kikatili, na kutundikwa mtini. Alikufa kwa maumivu makali sana. Lakini Mungu alimfufua, na siku 40 baadaye, Yesu akapaa kwenda mbinguni.

      Simulizi hilo la pekee linatoka katika Injili nne za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambazo hujulikana kama Agano Jipya. Je, kweli mambo hayo yalitukia? Hilo ni swali muhimu sana. Ikiwa mambo hayo hayakutukia, imani ya Kikristo ni bure na tumaini la uzima wa milele katika Paradiso ni ndoto tu. (1 Wakorintho 15:14) Kwa upande mwingine, ikiwa mambo hayo yalitukia, basi kuna tumaini zuri ambalo unaweza kupata. Kwa hiyo, masimulizi ya Injili ni ya kweli au hadithi tu?

      HABARI ZA UHAKIKA

      Tofauti na hekaya zilizobuniwa, masimulizi ya Injili ni sahihi na yanaeleza mambo hususa. Kwa mfano, masimulizi hayo yamejaa majina ya maeneo halisi ambayo yanaweza kutembelewa leo. Yanataja kuhusu watu halisi, ambao wanahistoria wamethibitisha kwamba waliishi.—Luka 3:1, 2, 23.

      Yesu anatajwa na waandishi wa karne ya kwanza na ya pili.a Kifo chake kinachofafanuliwa katika Injili kinapatana na jinsi Waroma walivyokuwa wakiwaua wahalifu. Pia, matukio yanaelezwa kwa unyoofu kutia ndani hata makosa ya baadhi ya wanafunzi wa Yesu. (Mathayo 26:56; Luka 22:24-26; Yohana 18:10, 11) Mambo yote hayo yanaonyesha wazi kwamba waandishi wa Injili walikuwa wanyoofu na walisema mambo kwa usahihi kumhusu Yesu.

      UFUFUO WA YESU

      Ingawa watu wengi hukubali kwamba Yesu aliishi na kufa, baadhi wana mashaka na ufufuo wake. Hata mitume wake hawakuamini waliposikia kwa mara ya kwanza kwamba amefufuliwa. (Luka 24:11) Hata hivyo, waliamini kwamba Yesu amefufuliwa walipomwona katika pindi tofauti-tofauti. Hata katika kisa kimoja, watu 500 walimwona Yesu.—1 Wakorintho 15:6.

      Bila kuogopa kukamatwa na kuuawa, wanafunzi wa Yesu waliwatangazia watu wote ufufuo wa Yesu kwa ujasiri—hata wale waliomuua. (Matendo 4:1-3, 10, 19, 20; 5:27-32) Je, wanafunzi hao wote wangekuwa na ujasiri kama wasingekuwa na uhakika kwamba Yesu amefufuliwa? Kwa kweli, ufufuo wa Yesu umewachochea watu wengi ulimwenguni wavutiwe na Ukristo sasa na wakati uliopita.

      Masimulizi ya Injili ya kifo na ufufuo wa Yesu ni sahihi. Ukiyasoma kwa makini utapata uhakika kwamba matukio hayo ni ya kweli. Usadikisho wako utaimarishwa zaidi ukielewa kwa nini mambo hayo yalitukia. Makala inayofuata inaeleza jambo hilo.

      a Tasito, aliyezaliwa mwaka wa 55 W.K., aliandika kuwa, “Kristo, ambaye ndiye chanzo cha jina [Wakristo], alihukumiwa kifo na gavana wetu Pontio Pilato wakati wa utawala wa Tiberio.” Yesu anatajwa pia na Suetonius (karne ya kwanza); mwanahistoria wa Kiyahudi Yosefo (karne ya kwanza); na Plini Mdogo, gavana wa Bithinia (mwanzoni mwa karne ya pili).

      Kwa Nini Hakuna Uthibitisho wa Vyanzo Vingine?

      Je, tutarajie vyanzo vingine vya karne ya kwanza vitoe uthibitisho kwamba Yesu alikuwa halisi na alifufuliwa? Hapana. Kwanza, vitabu vya Injili viliandikwa miaka ipatayo 2,000 iliyopita. Maandishi machache ya wakati huo yamebaki mpaka leo. (1 Petro 1:24, 25) Pia, si rahisi kwamba wapinzani wa Yesu wangeandika jambo lolote kumhusu ambalo lingewachochea watu wamwamini.

      Mtume Petro anaeleza hivi kuhusu ufufuo wa Yesu: “Mungu alimfufua Huyu katika siku ya tatu na kumfunua, si kwa watu wote, bali kwa mashahidi waliowekwa kimbele na Mungu, kwetu sisi, tuliokula na kunywa pamoja naye baada ya kufufuliwa kwake kutoka kwa wafu.” (Matendo 10:40, 41) Kwa nini si kwa watu wote? Injili ya Mathayo inatuambia kwamba maadui wa Yesu waliposikia habari za ufufuo wake, walipanga njama ya kukomesha habari hizo.—Mathayo 28:11-15.

      Je, hilo linamaanisha kwamba Yesu alitaka ufufuo wake uwe siri? Hapana, kwa kuwa Petro alisema hivi: “Alituagiza sisi tuwahubirie watu na kutoa ushahidi kamili kwamba Huyu ndiye aliyeagizwa na Mungu kuwa mwamuzi wa walio hai na wafu.” Wakristo wa kweli wanafanya hivyo.—Matendo 10:42.

  • Kwa Nini Yesu Aliteseka na Kufa?
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 2
    • Watu wa jamii mbalimbali wakifurahia maisha katika Paradiso

      HABARI KUU

      Kwa Nini Yesu Aliteseka Na Kufa?

      “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.”—Waroma 5:12

      Adamu na Hawa wakiangalia tunda walilokatazwa; Adamu na Hawa wakiwa wamezeeka; jeneza likiwa limebebwa makaburini

      Utajibuje ukiulizwa, “Je, unataka kuishi milele?” Huenda watu wengi wakasema kwamba wanataka lakini wanahisi haiwezekani. Wanasema kifo ni sehemu ya maisha na hakiepukiki.

      Hata hivyo, tuseme swali hilo ligeuzwe na uulizwe, “Uko tayari kufa?” Katika hali ya kawaida, watu wengi watajibu hapana. Hilo linaonyesha nini? Ni asili yetu kutamani kuishi, ijapokuwa tunakabili matatizo. Biblia inaonyesha Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kuishi. Ndiyo maana inasema kuwa, “wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao.”—Mhubiri 3:11.

      Hata hivyo, ukweli ni kwamba wanadamu hawaishi milele. Hivyo basi, ni nini kilitukia? Na Je, Mungu amefanya jambo lolote ili kurekebisha hali hiyo? Majibu ya Biblia yanatia moyo, na yanahusiana na mateso na kifo cha Yesu.

      NI NINI KILICHOTUKIA?

      Sura tatu za kwanza za kitabu cha Biblia cha Mwanzo zinatueleza kwamba Mungu aliwapa mume na mke wa kwanza, Adamu na Hawa, tarajio la kuishi milele na aliwaambia jambo la kufanya ili tarajio hilo litimie. Kisha simulizi hilo linaeleza jinsi walivyoshindwa kumtii Mungu na wakapoteza tarajio hilo. Simulizi hilo linaelezwa kwa njia rahisi hivi kwamba baadhi ya watu wanaona kuwa ni hadithi. Kitabu cha Mwanzo kinaeleza mambo ya kweli kama vitabu vya Injili.a

      Uasi wa Adamu ulitokeza nini? Biblia inasema hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Kwa kumwasi Mungu, Adamu alitenda dhambi. Hivyo akapoteza tarajio la kuishi milele na hatimaye akafa. Tukiwa wazao wake, tumerithi dhambi. Hivyo, tunaugua, tunazeeka, na kufa. Ufafanuzi huo unapatana na jambo ambalo wanasayansi wamegundua kuhusu jinsi watoto wanavyorithi tabia fulani kutoka kwa wazazi wao. Lakini je, Mungu amefanya lolote ili kurekebisha jambo hilo?

      JAMBO AMBALO MUNGU AMEFANYA

      Mungu amefanya mpango ili kurudisha, au kununua tena, kitu ambacho Adamu aliwapotezea wazao wake, yaani, tumaini la kuishi milele. Mungu alifanyaje?

      “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” inasema Biblia katika Waroma 6:23. Hilo linamaanisha kwamba kifo ni matokeo ya dhambi. Adamu alitenda dhambi, hivyo akafa. Vivyo hivyo, tunatenda dhambi na hivyo lazima tupate mshahara wa dhambi, yaani, kifo. Ingawa hatuna hatia, tumerithi dhambi hiyo. Hivyo, Mungu alimtuma Mwana wake, Yesu, abebe ‘mshahara wa dhambi’ kwa ajili yetu. Jambo hilo linawezekanaje?

      Watu wa jamii mbalimbali wakifurahia maisha katika Paradiso

      Kifo cha Yesu kinatufungulia njia ya kupata maisha yenye furaha milele

      Kwa kuwa mtu mmoja, mwanadamu mkamilifu Adamu, alituletea dhambi na kifo kwa sababu ya kutotii, mwanadamu mkamilifu aliyetii hadi kifo alihitajika ili kutuondolea mzigo huo. Biblia inaeleza jambo hilo kwa njia hii: “Kama vile kupitia kutotii kwa mtu mmoja wengi walifanywa watenda-dhambi, vivyo hivyo pia kupitia kutii kwa mtu mmoja wengi watafanywa kuwa waadilifu.” (Waroma 5:19) Yesu alikuwa huyo “mtu mmoja.” Alitoka mbinguni, akawa mwanadamu mkamilifub, na akafa kwa niaba yetu. Matokeo ni kwamba tunaweza kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu na kupata tarajio la kuishi milele.

      KWA NINI YESU ALITESEKA NA KUFA?

      Hata hivyo, kwa nini ilikuwa lazima Yesu afe ili kutimiza hilo? Je, Mungu Mweza-Yote asingeweza kutoa agizo kwamba wazao wa Adamu waruhusiwe kuishi milele? Ni kweli alikuwa na mamlaka ya kufanya hivyo. Lakini kufanya hivyo kungepuuza amri yake kwamba mshahara wa dhambi ni kifo. Amri hiyo si kanuni ndogo inayoweza kupuuzwa au kubadilishwa kulingana na hali. Ni msingi wa haki ya kweli.—Zaburi 37:28.

      Ikiwa Mungu angepuuza haki katika kisa hiki, watu wangejiuliza ikiwa atafanya hivyo tena katika mambo mengine pia. Kwa mfano, je, angetumia haki kuamua ni nani kati ya wazao wa Adamu anayestahili kupata uzima wa milele? Je, anaweza kutumainiwa katika kutimiza ahadi zake? Kutumia haki katika kutuletea ukombozi kunatuhakikishia kwamba sikuzote Mungu atafanya lililo sawa.

      Kupitia kifo cha Yesu cha kidhabihu, Mungu alituletea tarajio la kuishi milele katika Paradiso hapa duniani. Ona maneno ya Yesu katika Yohana 3:16: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” Hivyo, kifo cha Yesu kinaonyesha Mungu anavyotenda haki, lakini pia kinaonyesha jinsi anavyowapenda sana wanadamu.

      Hata hivyo, kwa nini Yesu alihitaji kuteseka na kufa kwa maumivu makali kama inavyoonyeshwa katika Injili? Kwa kupata majaribu makali na kuwa mwaminifu, Yesu alipinga dai la Shetani kwamba wanadamu hawawezi kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu wanapojaribiwa. (Ayubu 2:4, 5) Dai hilo lilionekana halali Shetani alipomshawishi Adamu mkamilifu atende dhambi. Lakini Yesu—ambaye alikuwa sawa kabisa na Adamu—aliendelea kuwa mwaminifu ingawa alipata mateso makali. (1 Wakorintho 15:45) Hivyo akathibitisha kwamba Adamu angeweza pia kumtii Mungu ikiwa angetaka. Kwa kuvumilia majaribu, Yesu alituwekea mfano wa kuiga. (1 Petro 2:21) Kutokana na utii wake, Mungu alimthawabisha Mwana wake, Yesu kwa kumpa uhai usioweza kufa mbinguni.

      JINSI UNAVYOWEZA KUNUFAIKA

      Kifo cha Yesu ni halisi. Njia ya kupata uzima wa milele iko wazi. Je, unataka kuishi milele? Yesu alituonyesha jambo la kufanya aliposema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

      Wachapishaji wa gazeti hili wanakualika ujifunze mengi zaidi kumhusu Mungu wa kweli Yehova, na kumhusu Mwana wake, Yesu Kristo. Mashahidi wa Yehova katika eneo unaloishi watafurahi kukusaidia. Pia unaweza kupata habari zaidi kwa kutembelea tovuti yetu ya www.jw.org/sw.

      a Soma makala yenye kichwa “The Historical Character of Genesis,” ya kitabu cha Insight on the Scriptures, buku la 1, ukurasa wa 922, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      b Yehova alihamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni na kuutia katika tumbo la Maria, na roho ya Mungu ikamlinda Yesu ili asirithi kutokamilika kutoka kwa Maria.—Luka 1:31, 35.

      Mkate usiotiwa chachu ukipitishwa wakati wa Ukumbusho

      “Endeleeni Kufanya Hivi”

      Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu aliwakusanya mitume wake waaminifu na kuanzisha Ukumbusho wa kifo chake. Aliwaambia hivi: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Ili kutii amri hiyo, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanakusanyika kila mwaka kuadhimisha kifo cha Yesu. Mwaka jana, watu 19,862,783 walihudhuria tukio hilo.

      Mwaka huu, Ukumbusho wa kifo cha Yesu utafanyika Jumatano, Machi 23, baada ya jua kutua. Wewe na familia yako pamoja na marafiki mnakaribishwa kuhudhuria na kusikiliza hotuba inayotegemea Biblia. Hotuba hiyo itaeleza kwa nini kifo cha Yesu ni muhimu na jinsi kinavyokunufaisha. Kiingilio ni bure; hakuna sadaka zitakazokusanywa. Tafadhali waombe Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu wakueleze mahali na wakati wa mwadhimisho huo. Au tembelea tovuti yetu ya www.jw.org/sw.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki