SURA YA 8
Wahudumu wa Habari Njema
YEHOVA alimtuma Mwanaye, Yesu Kristo, ili atuwekee kielelezo bora cha kuiga. (1 Pet. 2:21) Mtu anapokuwa mfuasi wa Yesu, anahubiri habari njema akiwa mhudumu wa Mungu. Akionyesha kwamba jambo hilo lingeburudisha kiroho, Yesu alisema: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu.” (Mt. 11:28, 29) Wote ambao wamekubali mwaliko huo wameona ahadi hiyo ikitimia!
2 Akiwa Mhudumu Mkuu wa Mungu, Yesu alichagua watu fulani wawe wafuasi wake. (Mt. 9:9; Yoh. 1:43) Aliwazoeza katika huduma na kuwatuma wafanye kazi ileile aliyokuwa akifanya. (Mt. 10:1–11:1; 20:28; Luka 4:43) Baadaye aliwatuma wengine 70 wakatangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Luka 10:1, 8-11) Yesu alipowatuma wanafunzi wake, aliwaambia hivi: “Yeyote anayewasikiliza ninyi ananisikiliza mimi pia. Na yeyote anayewapuuza ninyi ananipuuza mimi pia. Isitoshe, yeyote anayenipuuza mimi anampuuza pia Yule aliyenituma.” (Luka 10:16) Kwa kusema hivyo, Yesu alikazia jukumu zito alilowapa wanafunzi wake. Walipaswa kumwakilisha Yesu na Mungu Aliye Juu Zaidi! Ndivyo ilivyo leo kwa wale wanaokubali mwaliko huu wa Yesu: Njoo “uwe mfuasi wangu.” (Luka 18:22; 2 Kor. 2:17) Mungu anawapa wale wanaokubali mwaliko huo utume wa kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufundisha.—Mt. 24:14; 28:19, 20.
3 Kwa kuwa tumekubali mwaliko wa Yesu na kumfuata, tumebarikiwa ‘kumjua’ Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Yoh. 17:3) Tumefundishwa njia za Yehova. Ametusaidia kufanya upya akili yetu, kuvaa utu mpya, na kupatanisha maisha yetu na viwango vyake vya uadilifu. (Rom. 12:1, 2; Efe. 4:22-24; Kol. 3:9, 10) Kwa kuwa tunathamini mambo hayo kutoka moyoni, tumechochewa tujiweke wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji. Tunapobatizwa tunakuwa wahudumu waliowekwa rasmi.
4 Sikuzote kumbuka kwamba tunapaswa kumtumikia Mungu tukiwa na mikono isiyo na hatia na moyo safi. (Zab. 24:3, 4; Isa. 52:11; 2 Kor. 6:14–7:1) Kupitia imani katika Yesu Kristo, tumepata dhamiri safi. (Ebr. 10:19-23, 35, 36; Ufu. 7:9, 10, 14) Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wafanye mambo yote kwa utukufu wa Mungu ili wasiwakwaze wengine. Pia, mtume Petro alionyesha kwamba mwenendo mzuri wa Kikristo unaweza kuwavuta wasioamini waikubali kweli. (1 Kor. 10:31, 33; 1 Pet. 3:1) Unawezaje kumsaidia mtu astahili kuwa mhudumu wa habari njema?
WAHUBIRI WAPYA
5 Mara tu unapoanza kuongoza funzo la Biblia na mtu anayependezwa, mtie moyo awaambie wengine mambo anayojifunza. Anaweza kuwahubiria isivyo rasmi watu wa ukoo, marafiki, wafanyakazi wenzake, na watu wengine. Hiyo ni hatua muhimu ya kuwafundisha wapya kuwa wafuasi wa Yesu Kristo wakiwa wahudumu wa habari njema. (Mt. 9:9; Luka 6:40) Mwanafunzi mpya anapokua kiroho na kuzoea kuhubiri isivyo rasmi, bila shaka ataomba kuhubiri rasmi pamoja na kutaniko.
KUTIMIZA MATAKWA
6 Kabla ya kumwalika mtu ahubiri pamoja nawe nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza, unapaswa kuhakikisha kwamba anatimiza matakwa fulani. Mtu anapohubiri pamoja nasi anajitambulisha kuwa Shahidi wa Yehova. Hivyo ni wazi kwamba amepatanisha maisha yake na viwango vya Yehova vya uadilifu na anaweza kuwa mhubiri wa kutaniko ambaye hajabatizwa.
7 Unapojifunza na mtu na kuzungumzia kanuni za Biblia, inaelekea utamfahamu vizuri. Huenda umeona kwamba anaishi kupatana na yale anayojifunza. Hata hivyo, wazee wangependa kuzungumzia mambo fulani pamoja nawe na mwanafunzi wako.
8 Mratibu wa baraza la wazee atapanga wazee wawili (mmoja wao akiwa mshiriki wa halmashauri ya utumishi) wazungumzie mambo hayo pamoja nawe na mwanafunzi wa Biblia. Katika makutaniko yenye wazee wachache, mzee na mtumishi wa huduma wanaweza kushughulikia jambo hilo. Ndugu waliochaguliwa wanapaswa kufanya hivyo bila kukawia. Mwanafunzi akitoa ombi siku ya mkutano wa kutaniko, huenda ikawezekana kwa ndugu hao kuzungumza nawe na mwanafunzi wako baada ya mkutano. Kikao kinapaswa kuwa chenye kustarehesha. Kabla mwanafunzi hajakubaliwa kuwa mhubiri, mambo yafuatayo yanapaswa kuzingatiwa:
(1) Anaamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu.—2 Tim. 3:16.
(2) Anajua na kuamini mafundisho ya msingi ya Maandiko ili atakapoulizwa maswali, ajibu kulingana na Biblia bali si mafundisho ya dini za uwongo au maoni yake mwenyewe.—Mt. 7:21-23; 2 Tim. 2:15.
(3) Anatii amri ya Biblia ya kushirikiana na watu wa Yehova kwenye mikutano ya kutaniko ikiwa ana uwezo wa kufanya hivyo.—Zab. 122:1; Ebr. 10:24, 25.
(4) Anajua yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu uasherati, kutia ndani ngono kati ya watu ambao hawajafunga ndoa, uzinzi, kuwa na wake wengi, na kufanya ngono na mtu wa jinsia moja, na anaishi kupatana na mafundisho hayo. Ikiwa mtu huyo anaishi na mtu wa jinsia tofauti ambaye si mtu wake wa ukoo, ni lazima wawe wamefunga ndoa kisheria.—Mt. 19:9; 1 Kor. 6:9, 10; 1 Tim. 3:2, 12; Ebr. 13:4.
(5) Anatii amri ya Biblia inayokataza ulevi na hatumii dawa za kulevya isipokuwa kwa ajili ya matibabu.—2 Kor. 7:1; Efe. 5:18; 1 Pet. 4:3, 4.
(6) Anaona umuhimu wa kuepuka kushirikiana na watu wasioheshimu viwango vya Biblia.—1 Kor. 15:33.
(7) Amevunja kabisa ushirika na dini zote za uwongo ambazo huenda alishirikiana nazo. Ameacha kuhudhuria ibada hizo na hategemezi shughuli zao wala kushiriki katika shughuli hizo.—2 Kor. 6:14-18; Ufu. 18:4.
(8) Hajihusishi hata kidogo na mambo ya kisiasa ya ulimwengu.—Yoh. 6:15; 15:19; Yak. 1:27.
(9) Anaamini na kuishi kupatana na kile kinachosemwa katika Isaya 2:4 kuhusu mizozo ya mataifa.
(10) Anatamani kabisa kuwa Shahidi wa Yehova.—Zab. 110:3.
9 Ikiwa wazee hawana uhakika jinsi mwanafunzi anavyoelewa baadhi ya mambo hayo, wanaweza kusoma na kuzungumzia maandiko yaliyotajwa. Ni muhimu aelewe kwamba wale wanaoshirikiana na Mashahidi wa Yehova katika kazi ya kuhubiri lazima waishi kupatana na matakwa hayo ya Kimaandiko. Maelezo yake yatawasaidia wazee kujua kama anaelewa matakwa hayo na ikiwa anastahili kuanza kushiriki katika huduma ya shambani.
10 Wazee wanapaswa kumweleza bila kukawia ikiwa anastahili. Mara nyingi jambo hilo hufanywa mwishoni mwa mazungumzo. Ikiwa anastahili, wazee watamkaribisha kwa uchangamfu kuwa mhubiri. (Rom. 15:7) Anapaswa kutiwa moyo ashiriki katika huduma ya shambani haraka iwezekanavyo na atoe ripoti ya utumishi wa shambani mwishoni mwa mwezi. Wazee wanaweza kumweleza kwamba mwanafunzi wa Biblia anapostahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa na kutoa ripoti ya utumishi wa shambani kwa mara ya kwanza, Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri yenye jina lake huwekwa kwenye faili ya kutaniko. Wazee hukusanya taarifa hizo za kibinafsi kutoka kwa mhubiri ili tengenezo liweze kushughulikia utendaji wa kidini wa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote na ili mhubiri ashiriki katika shughuli za kiroho na kupokea msaada wa kiroho. Zaidi ya hilo, wazee wanaweza kuwakumbusha wahubiri wapya kwamba taarifa zozote za kibinafsi hushughulikiwa kulingana na Sera ya Mashahidi wa Yehova ya Kulinda Taarifa Ulimwenguni Pote inayopatikana kwenye tovuti ya jw.org.
11 Kufahamiana vizuri na mhubiri mpya na kupendezwa kikweli na yale anayotimiza kunaweza kumtia moyo. Kunaweza kumchochea kutoa ripoti ya utumishi wa shambani kwa ukawaida kila mwezi na kujitahidi zaidi kumtumikia Yehova.—Flp. 2:4; Ebr. 13:2.
12 Wazee wanapoona kwamba mwanafunzi wa Biblia anastahili kushiriki katika huduma ya shambani, itafaa apewe kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova. Atakapotoa ripoti yake ya utumishi wa shambani kwa mara ya kwanza, kutaniko litatangaziwa kwamba yeye ni mhubiri mpya ambaye hajabatizwa.
KUWASAIDIA VIJANA
13 Watoto wanaweza pia kustahili kuwa wahubiri wa habari njema. Yesu aliwapokea watoto wadogo na kuwabariki. (Mt. 19:13-15; 21:15, 16) Ingawa ni jukumu la wazazi kuwasaidia watoto wao, wengine kutanikoni wanaweza kuwasaidia vijana ambao wamechochewa kushiriki katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Ikiwa wewe ni mzazi, mfano wako mzuri katika huduma ya shambani utawachochea sana watoto wako wamtumikie Mungu kwa bidii. Mtoto ambaye ni mfano mzuri na anayetamani kuonyesha imani yake kwa kuwahubiria wengine habari njema, anaweza kusaidiwaje?
14 Ni vizuri wazazi wazungumze na mmoja wa wazee wa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko ili kuona ikiwa mtoto huyo anastahili kuwa mhubiri. Mratibu wa baraza la wazee atapanga wazee wawili (mmoja wao akiwa mshiriki wa halmashauri ya utumishi) wakutane na mtoto huyo na mzazi mmoja au wote wawili ambao ni waamini, au mlezi wake. Ikiwa mtoto ana ujuzi wa msingi wa kweli za Biblia na anaonyesha wazi kwamba anataka kushiriki katika utumishi, jambo hilo litathibitisha kwamba amefanya maendeleo. Baada ya kufikiria mambo hayo na mengine yanayowahusu watu wazima, wazee hao wanaweza kuamua ikiwa mtoto huyo anastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. (Luka 6:45; Rom. 10:10) Wanapokutana na mtoto, hakuna haja ya kuzungumzia baadhi ya mambo ambayo kwa kawaida yanawahusu watu wazima tu.
15 Wakati wa mazungumzo, wazee wanapaswa kumpongeza mtoto kwa maendeleo yake na kumtia moyo ajitahidi kufikia ubatizo. Kwa kuwa wazazi wamejitahidi kumfundisha mtoto wao kweli, wao pia wanastahili kupongezwa. Ili kuwasaidia wazazi kumsaidia zaidi mtoto wao, wazee wanapaswa kuwaonyesha habari yenye kichwa “Ujumbe kwa Wazazi Wakristo,” kwenye ukurasa wa 179-181.
WAKFU NA UBATIZO
16 Ikiwa umemjua na kumpenda Yehova kwa kupatanisha maisha yako na matakwa yake na kwa kushiriki katika huduma ya shambani, unahitaji kuimarisha uhusiano wako pamoja naye. Jinsi gani? Kwa kujiweka wakfu kwake na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji.—Mt. 28:19, 20.
17 Kuweka wakfu humaanisha kutenga kwa ajili ya kusudi takatifu. Kujiweka wakfu kwa Mungu kunamaanisha kusali kwake na kumwahidi kwamba utatumia maisha yako kumtumikia na kutembea katika njia zake. Humaanisha kumwabudu yeye peke yake milele. (Kum. 5:9) Hilo ni jambo la kibinafsi unalofanya faraghani. Hakuna mtu anayeweza kufanya hivyo kwa niaba yako.
18 Hata hivyo, haitoshi tu kumwambia Yehova faraghani kwamba unataka kuwa mali yake. Unahitaji kuwaonyesha wengine kwamba umejiweka wakfu kwa Mungu. Unafanya hivyo kwa kubatizwa katika maji, kama Yesu alivyofanya. (1 Pet. 2:21; 3:21) Ikiwa umeamua kumtumikia Yehova na unataka kubatizwa, unapaswa kufanya nini? Unapaswa kumwambia mratibu wa baraza la wazee. Atapanga wazee kadhaa wazungumze nawe ili kuhakikisha kwamba unatimiza matakwa ya Mungu kwa ajili ya wale wanaotaka kubatizwa. Kwa habari zaidi, tafadhali soma “Ujumbe kwa Mhubiri Ambaye Hajabatizwa,” kwenye ukurasa wa 182-184 wa kitabu hiki na “Maswali kwa Ajili ya Wale Wanaotaka Kubatizwa,” kwenye ukurasa wa 185-207.
RIPOTI YA MAENDELEO YA HUDUMA
19 Kwa miaka mingi, ripoti za maendeleo ya ibada safi ulimwenguni pote zimewatia moyo watu wa Yehova. Tangu Yesu Kristo alipowaambia wanafunzi wake kwamba habari njema ingehubiriwa duniani kote, Wakristo wa kweli wametamani sana kujua jinsi ambavyo kazi hiyo ingetimizwa.—Mt. 28:19, 20; Marko 13:10; Mdo. 1:8.
20 Wafuasi wa Yesu walifurahia kusikiliza ripoti za maendeleo ya kazi ya kuhubiri. (Marko 6:30) Kitabu cha Biblia cha Matendo kinatuambia kwamba kulikuwa na watu 120 hivi roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Muda mfupi baadaye idadi ya wanafunzi iliongezeka hadi 3,000 hivi, kisha 5,000 hivi. Iliripotiwa kwamba ‘Yehova aliendelea kuwaongezea kila siku watu waliokuwa wakiokolewa’ na kwamba “umati mkubwa wa makuhani wakawa waamini.” (Mdo. 1:15; 2:5-11, 41, 47; 4:4; 6:7) Habari hizo za ongezeko ziliwatia moyo sana wanafunzi! Ripoti hizo zenye kusisimua ziliwachochea kuendelea kufanya kazi waliyopewa na Mungu, licha ya mateso makali yaliyoanzishwa na viongozi wa dini ya Kiyahudi!
21 Karibu mwaka wa 60 na 61 W.K., Paulo katika barua yake kwa Wakolosai aliandika kwamba habari njema ilikuwa ikizaa “matunda na kuongezeka ulimwenguni kote” na “ilihubiriwa katika uumbaji wote chini ya mbingu.” (Kol. 1:5, 6, 23) Wakristo wa karne ya kwanza walitii Neno, na roho takatifu iliwatia nguvu kutimiza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote kabla ya mfumo wa mambo wa Kiyahudi kufikia mwisho wake mwaka wa 70 W.K. Wakristo hao waaminifu walitiwa moyo kwelikweli kusikia ripoti za matokeo ya kazi hiyo!
Je, unajitahidi kutimiza kikamili huduma kabla ya mwisho kuja?
22 Vivyo hivyo, tengenezo la Yehova la kisasa hujitahidi kuweka rekodi sahihi za kazi inayofanywa ili kutimiza Mathayo 24:14 inayosema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Tukiwa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna kazi inayopaswa kufanywa haraka. Kila mmoja wetu anapaswa ajitahidi kutimiza kikamili huduma kabla ya mwisho kuja. Yehova atahakikisha kwamba kazi hiyo inakamilika, na tukishiriki kuifanya, tutapata kibali chake.—Eze. 3:18-21.
RIPOTI YAKO YA UTUMISHI WA SHAMBANI
23 Tunapaswa kuripoti nini? Fomu ya Ripoti ya Utumishi wa Shambani inayochapishwa na tengenezo ina mambo yanayopaswa kuripotiwa. Hata hivyo, maelezo na ufafanuzi ufuatao, utakusaidia sana.
24 Katika safu ya “Machapisho (Yaliyochapishwa na ya Kielektroniki),” andika jumla ya machapisho yote iwe ni yaliyochapishwa au ya kielektroniki uliyowapa watu ambao si Mashahidi waliobatizwa. Katika safu ya “Video Ambazo Zilionyeshwa” andika jumla ya video zote ambazo ulionyesha.
25 Unaporipoti “Ziara za Kurudia,” jumlisha ziara zote za kurudia ulizofanya kwa kusudi la kuchochea upendezi ulioonyeshwa na mtu ambaye si Shahidi aliyejiweka wakfu na kubatizwa. Ziara ya kurudia inaweza kufanywa kwa kumtembelea mtu kibinafsi, kwa kuandika barua, kupiga simu, kutuma ujumbe kupitia simu au barua pepe, au kumpelekea chapisho fulani. Kila mara unapoongoza funzo la Biblia la nyumbani, unaweza kuhesabu ziara ya kurudia. Mzazi anaweza kuhesabu ziara moja ya kurudia kila juma anapoongoza ibada ya familia ikiwa kuna mtoto ambaye hajabatizwa.
26 Ingawa funzo la Biblia huongozwa kila juma, huripotiwa kama funzo moja tu kwa mwezi. Wahubiri wanapaswa kuandika idadi ya mafunzo ya Biblia yaliyoongozwa katika mwezi. Mafunzo ya Biblia ambayo yanaweza kuripotiwa yanatia ndani watu wote ambao si Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa. Unaweza kuhesabu funzo la Biblia unapojifunza na ndugu au dada asiyetenda unapoombwa na mshiriki wa halmashauri ya utumishi au unapojifunza na mhubiri aliyebatizwa karibuni ambaye hajamaliza kitabu Furahia Maisha Milele!
27 Ni muhimu kutoa ripoti sahihi ya “Saa.” Kwa kawaida huo ni muda unaotumia unapohubiri nyumba kwa nyumba, barabarani, unapofanya ziara za kurudia, unapoongoza mafunzo ya Biblia, au unapowahubiria rasmi au isivyo rasmi watu ambao si Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa. Wahubiri wawili wanapohubiri pamoja, wote wanaweza kuhesabu saa, lakini mmoja tu ndiye atakayehesabu ziara ya kurudia au funzo la Biblia litakaloongozwa. Wazazi wawili wanaoshirikiana kuwafundisha watoto wao wakati wa Ibada ya Familia wanaweza kuhesabu saa moja kwa juma. Ndugu wanaweza kuhesabu muda wanaotumia kutoa hotuba za watu wote. Mkalimani wa hotuba ya watu wote anaweza pia kuhesabu muda huo. Muda unaotumiwa kwa shughuli nyingine muhimu kama vile, kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani, kuhudhuria mkutano wa utumishi, shughuli za kibinafsi wakati wa utumishi, na kadhalika hauhesabiwi.
28 Kila mhubiri atatumia dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia kusali na kuamua muda aliotumia kutoa ushahidi. Baadhi ya wahubiri wanahubiri katika maeneo yenye watu wengi, na wengine huhubiri katika maeneo yasiyo na watu wengi hivyo wanatumia muda mwingi kusafiri. Maeneo yanatofautiana; maoni ya wahubiri kuhusu huduma yao hutofautiana. Baraza Linaloongoza haliweki sheria jinsi makutaniko yanavyohesabu muda uliotumika katika utumishi wa shambani, wala hakuna mtu aliyeteuliwa ili kuwahukumu wengine kuhusu jambo hilo.—Mt. 6:1; 7:1; 1 Tim. 1:5.
29 Muda unaotumia katika utumishi wa shambani unapaswa kuripotiwa saa nzima-nzima. Hata hivyo, mhubiri asiyejiweza kwa sababu ya uzee, ulemavu, ugonjwa au udhaifu mwingine wowote, anaweza kuripoti utumishi wa dakika 15, 30, na 45. Hata ikiwa alitoa ushahidi kwa dakika 15 tu kwa mwezi, anaweza kuripoti muda huo. Atahesabiwa kuwa mhubiri wa Ufalme anayetenda. Mhubiri ambaye hajiwezi kwa mwezi mmoja au miezi kadhaa, labda kwa sababu ya ugonjwa au jeraha kubwa, anaweza pia kuhusishwa katika mpango huo. Mpango huo unawahusu wale tu wenye udhaifu mkubwa wa kimwili. Halmashauri ya utumishi itaamua ikiwa mhubiri anastahili kuhusishwa katika mpango huo.
REKODI YA KUTANIKO YA MHUBIRI
30 Ripoti yako ya utumishi wa shambani ya kila mwezi huandikwa kwenye Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri. Rekodi hizo ni za kutaniko unaloshirikiana nalo. Ukitaka kuhamia kutaniko lingine, hakikisha unawajulisha wazee. Mwandishi atahakikisha kwamba rekodi zako zinatumwa kwenye kutaniko unalohamia. Kwa kufanya hivyo, wazee wa kutaniko unalohamia watakukaribisha na wataendelea kukusaidia kiroho. Ikiwa utakuwa mbali na kutaniko lako kwa muda usiozidi miezi mitatu, tafadhali endelea kutuma ripoti yako ya utumishi katika kutaniko lako.
KWA NINI TUNARIPOTI UTUMISHI WETU WA SHAMBANI?
31 Je, nyakati nyingine wewe husahau kutoa ripoti yako ya utumishi wa shambani? Bila shaka sote tunahitaji kukumbushwa mara kwa mara. Lakini tukisitawisha mtazamo unaofaa na tukielewa umuhimu wa kuripoti utumishi wetu wa shambani, inaweza kuwa rahisi kukumbuka kufanya hivyo.
32 Wengine wameuliza: “Kwa kuwa Yehova anajua yale ambayo ninafanya katika utumishi wake, kwa nini nitoe ripoti kutanikoni?” Ni kweli kwamba Yehova anajua yale tunayofanya, naye anajua ikiwa tunamtumikia kwa nafsi yote au tunafanya kidogo kwa kulinganisha na uwezo wetu. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova alirekodi siku ambazo Noa alikaa ndani ya safina na miaka ambayo Waisraeli walisafiri jangwani. Mungu aliweka rekodi ya wale waliokuwa waaminifu na wale ambao hawakutii. Alirekodi jinsi nchi ya Kanaani ilivyotekwa hatua kwa hatua na mambo yaliyotimizwa na waamuzi waaminifu wa Israeli. Naam, alirekodi habari nyingi sana kuhusu matendo ya watumishi wake. Alitumia roho yake kuongoza kuandikwa kwa matukio hayo, na hivyo kutuonyesha umuhimu wa kuandika rekodi sahihi.
33 Matukio ya kihistoria yaliyoandikwa katika Biblia yanaonyesha usahihi wa ripoti na rekodi za watu wa Yehova. Katika visa vingi, masimulizi ya Biblia hayangekuwa yenye kuchochea ikiwa hesabu kamili haingetajwa. Fikiria mifano ifuatayo: Mwanzo 46:27; Kutoka 12:37; Waamuzi 7:7; 2 Wafalme 19:35; 2 Mambo ya Nyakati 14:9-13; Yohana 6:10; 21:11; Matendo 2:41; 19:19.
34 Ingawa ripoti hizo hazionyeshi kila jambo tunalofanya katika utumishi wetu kwa Yehova, zinatimiza kusudi muhimu katika tengenezo la Yehova. Katika karne ya kwanza, baada ya kuhubiri, mitume wa Yesu waliripoti “mambo yote waliyokuwa wamefanya na kufundisha.” (Marko 6:30) Nyakati nyingine, ripoti zinaweza kuonyesha mambo hususa yanayohitaji kushughulikiwa katika sehemu fulani ya huduma yetu. Takwimu zinaweza kuonyesha kama kuna maendeleo katika utendaji fulani, na vilevile ikiwa hakuna ongezeko kubwa la wahubiri. Huenda wahubiri wanahitaji kutiwa moyo au kuna matatizo yanayopaswa kushughulikiwa. Waangalizi wanaohusika watachunguza ripoti hizo na kujitahidi kurekebisha hali yoyote ambayo huenda inazuia maendeleo ya mtu mmoja-mmoja au ya kutaniko lote.
35 Pia, ripoti hulisaidia tengenezo kujua maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Ni maeneo gani yenye matokeo mazuri? Ni maeneo gani yenye ukuzi mdogo? Ni machapisho gani yanayohitajiwa ili kuwasaidia watu wajifunze kweli? Ripoti husaidia tengenezo kujua machapisho yanayohitajiwa katika maeneo mbalimbali ulimwenguni na kisha huhakikisha kwamba yanapatikana.
36 Wengi wetu hutiwa moyo na ripoti. Je, hatusisimuki tunaposikia kuhusu mambo ambayo ndugu zetu wanatimiza wanapohubiri habari njema ulimwenguni pote? Ripoti za ongezeko hutusaidia kuona jinsi tengenezo la Yehova linavyopanuka. Mambo yaliyoonwa huchangamsha moyo, huzidisha bidii yetu na kutuchochea tushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri. (Mdo. 15:3) Ni muhimu kila mmoja wetu atoe ripoti ya utumishi wa shambani na hilo huonyesha kwamba tunawajali ndugu zetu ulimwenguni pote. Kupitia jambo hilo dogo tunaonyesha kwamba tunatii mipango ya tengenezo la Yehova.—Luka 16:10; Ebr. 13:17.
KUJIWEKEA MALENGO
37 Hatuna sababu yoyote ya kulinganisha utumishi wetu wa shambani na wa mtu mwingine. (Gal. 5:26; 6:4) Hali za watu hutofautiana sana. Kwa upande mwingine, tunaweza kupata faida nyingi sana tukiweka malengo halisi tunayoweza kufikia ili kupima maendeleo yetu katika huduma. Tukifikia malengo hayo tutaridhishwa na mambo tuliyotimiza.
38 Ni wazi kwamba sasa Yehova anaharakisha kazi ya kukusanya watu watakaookoka ile “dhiki kuu.” Tunaishi wakati ambapo unabii huu wa Isaya unatimia: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu. Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.” (Ufu. 7:9, 14; Isa. 60:22) Ni heshima kubwa sana kuwa wahudumu wa habari njema katika siku hizi za mwisho!—Mt. 24:14.