Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kusoma Maandiko kwa Mkazo Unaofaa
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 21

      Kusoma Maandiko kwa Mkazo Unaofaa

      Unahitaji kufanya nini?

      Kazia maneno makuu ya habari unayozungumzia. Soma kwa hisia inayofaa.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Uzito wa maandiko yanayosomwa hudhihirishwa kwa mkazo unaofaa.

      UNAPOZUNGUMZA na wengine kuhusu mambo ambayo Mungu amekusudia, iwe unamhubiria mtu au unahutubu jukwaani, unapaswa kutegemea Neno la Mungu. Mara nyingi mazungumzo hayo hutia ndani kusoma Biblia, na tunapaswa kuisoma vizuri.

      Mkazo Unaofaa Unatia Ndani Hisia. Tusome maandiko kwa hisia. Ebu ona mifano michache. Unaposoma kwa sauti Zaburi 37:11, sauti yako inapasa kuonyesha furaha ya kutazamia amani ambayo imeahidiwa katika andiko hilo. Unaposoma Ufunuo 21:4 kuhusu mwisho wa kuteseka na kifo, sauti yako ionyeshe shukrani za moyoni kwa sababu ya faraja hiyo nzuri ajabu ambayo imetabiriwa hapo. Soma Ufunuo 18:2, 4, 5 kwa sauti ya dharura kwa sababu linatuhimiza tutoke kwenye “Babiloni Mkubwa” mwenye dhambi tele. Hisia tunayoonyesha itoke moyoni lakini isipite kiasi. Kadiri nzuri ya hisia inategemea andiko unalosoma na jinsi unavyolitumia.

      Kazia Maneno Yanayofaa. Kama unazungumzia sehemu fulani tu ya andiko, kazia sehemu hiyo unaposoma. Kwa mfano, ikiwa unataka kuelezea maana ya “kutafuta kwanza ufalme” unaposoma Mathayo 6:33, usikazie “uadilifu wake” wala “vitu vingine vyote.”

      Tuseme umepanga kusoma Mathayo 28:19 katika hotuba utakayotoa katika Mkutano wa Utumishi. Utakazia maneno gani? Ikiwa unataka kutia watu moyo wawe na bidii kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani, kazia ‘kufanya wanafunzi.’ Na kama unataka kuzungumzia daraka la Mkristo la kuwajulisha kweli za Biblia watu wa nchi za kigeni au kama unataka kuwatia moyo wahubiri wengine watumikie katika sehemu zenye uhitaji zaidi, unaweza kukazia “watu wa mataifa yote.”

      Mara nyingi tunasoma andiko kujibu swali au kuunga mkono jambo fulani ambalo wengine hubisha. Ikiwa unakazia kila wazo katika andiko hilo kwa kadiri ileile, wasikilizaji wanaweza kukosa kuelewa kusudi lako la kusoma andiko hilo. Wewe unaweza kufahamu wazi kusudi lako la kulisoma lakini huenda wao wasilifahamu.

      Kwa mfano, unaposoma Zaburi 83:18 katika Biblia ambayo ina jina la Mungu, mwenye nyumba anaweza kukosa kufahamu jambo linaloonekana kuwa wazi la kwamba Mungu ana jina ikiwa unakazia sana ile sehemu inayosema “Uliye juu.” Kazia jina “Yehova.” Lakini, unapotumia andiko hilo kuonyesha kwamba Yehova ni mwenye enzi kuu, kazia maneno “Uliye juu.” Vilevile unapotumia Yakobo 2:24 kuonyesha kwamba imani inapaswa kuonyeshwa kwa matendo, kukazia ‘kutangazwa kuwa mwadilifu’ badala ya kukazia “kazi” kunaweza kufanya wengine wasipate maana.

      Tunaweza kupata mfano mwingine mzuri katika Waroma 15:7-13. Hii ni sehemu ya barua ambayo mtume Paulo aliandikia kutaniko lenye mchanganyiko wa watu wa Mataifa na Wayahudi wa asili. Anasema hapo kwamba huduma ya Kristo haiwafaidi tu Wayahudi waliotahiriwa bali inawafaidi pia watu wa mataifa ili “mataifa yapate kumtukuza Mungu kwa ajili ya rehema yake.” Kisha ananukuu maandiko manne kuthibitisha jambo hilo. Unapaswa kusoma manukuu hayo kwa njia gani ili kukazia jambo ambalo Paulo alimaanisha? Ikiwa unatia alama maneno ya kukazia, unaweza kutia alama “mataifa” katika mstari wa 9, “nyinyi mataifa” katika mstari wa 10, “mataifa yote” na “vikundi vyote vya watu” katika mstari wa 11, na “mataifa” katika mstari wa 12. Ebu jaribu kusoma Waroma 15:7-13 kwa mkazo huo. Unapofanya hivyo, hoja ya Paulo itakuwa wazi na kueleweka kwa urahisi.

      Njia za Kutia Mkazo. Unaweza kutumia njia kadhaa kukazia maneno muhimu ambayo unataka yawe wazi. Njia unayotumia kutia mkazo ilingane na andiko unalosoma na muktadha wa hotuba yako. Hapa pana madokezo machache.

      Kutia mkazo kupitia sauti. Njia hii inahusisha kubadili sauti kwa njia yoyote inayofanya maneno yenye maana yawe wazi kuliko maneno mengine katika sentensi. Unaweza kutia mkazo kwa kuinua sauti au kuipunguza. Katika lugha nyingi, kuinua sauti kunaweza kuongeza mkazo. Lakini katika lugha nyinginezo, kuinua sauti kunaweza kubadili maana ya jambo unalosema. Ukipunguza mwendo wako na kuongea polepole unapofikia maneno makuu, maneno hayo hutokea kwa uzito zaidi. Katika lugha ambazo huwezi kukazia maneno fulani kwa kubadili sauti, unaweza kufuata desturi za kukazia maneno katika lugha hizo.

      Kutua kifupi. Unaweza kutua kifupi kabla ya kusoma sehemu kuu ya andiko au baada ya kuisoma, au kabla na baada ya kuisoma. Kutua kifupi kabla tu ya kusoma wazo kuu hufanya watu wawe na hamu ya kujua jambo linalofuata na kutua baada tu ya kulisoma hufanya jambo hilo lieleweke zaidi. Lakini ukitua-tua sana, hakuna jambo litakalokuwa wazi.

      Kurudia jambo kuu. Unaweza kukazia jambo fulani kwa kutua na kulisoma tena. Njia nzuri ya kutua inayotumiwa mara nyingi ni kumaliza kusoma andiko lote kisha urudie kusoma wazo kuu unalotaka kukazia.

      Ishara. Mara nyingi ishara za mwili na za uso zinaweza kuongezea hisia jambo unalosema.

      Hali ya sauti. Katika lugha fulani, nyakati nyingine maneno yanaweza kusomwa kwa sauti inayotokeza maana fulani na kuyatia mkazo. Pia unahitaji kutumia busara kuhusu jambo hili hasa unapotumia maneno ya dhihaka.

      Wengine Wanaposoma Maandiko. Mwenye nyumba anaposoma andiko, anaweza kukazia maneno yasiyostahili kukaziwa au labda asikazie neno lolote. Ufanye nini basi? Kwa ujumla ni vizuri ufafanue maana unapomwonyesha jinsi maandiko hayo yanavyotumika. Baada ya kufanya hivyo, unaweza kukazia hasa maneno yanayotokeza maana katika Biblia.

      KUJUA JINSI YA KUTUMIA MKAZO

      • Jiulize hivi kuhusu andiko lolote ambalo utasoma: ‘Maneno haya yanaonyesha hisia gani? Nionyeshe hisia hizo kwa njia gani?’

      • Chunguza maandiko unayopanga kutumia. Jiulize hivi kuhusu kila mojawapo ya maandiko hayo: ‘Andiko hili litatimiza kusudi gani? Nahitaji kukazia maneno gani kutimiza kusudi hilo?’

      MAZOEZI: (1) Chunguza andiko ambalo unataka kutumia katika utumishi wa shambani. Fanya mazoezi ya kulisoma kwa hisia inayofaa. Ukikumbuka jinsi unavyotaka kulitumia, lisome kwa sauti ukikazia neno au maneno yanayofaa. (2) Katika kichapo kinachotumiwa wakati huu kwenye funzo, chagua fungu moja ambalo lina manukuu ya maandiko. Chunguza jinsi ambavyo maandiko yametumiwa hapo. Tia alama maneno yanayotokeza maana. Soma fungu lote kwa sauti kwa njia inayokazia vizuri maandiko.

  • Kutumia Maandiko Vizuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 22

      Kutumia Maandiko Vizuri

      Unahitaji kufanya nini?

      Hakikisha unatumia andiko kulingana na muktadha wake na kulingana na Biblia yote kwa ujumla. Pia tumia andiko kulingana na maelezo ambayo yamechapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”

      KWA NINI NI MUHIMU?

      Kufundisha wengine Neno la Mungu ni jambo zito sana. Mungu anataka watu wapate “ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Kwa hiyo tuna wajibu wa kufundisha Neno la Mungu kwa usahihi.

      KUFUNDISHA wengine si kusoma tu maandiko ya Biblia. Mtume Paulo alimwandikia hivi mshiriki wake Timotheo: “Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.”—2 Tim. 2:15.

      Ili tufanye hivyo, ni lazima tufafanue maandiko kulingana na mafundisho ya Biblia. Hiyo inamaanisha tufikirie muktadha badala ya kuchagua tu maneno yanayotupendeza na kutoa maoni yetu wenyewe. Kupitia nabii Yeremia, Yehova aliwaonya watu wasiwasikilize manabii waliodai kusema maneno yake lakini kumbe walisema “maono ya mioyo yao wenyewe.” (Yer. 23:16) Mtume Paulo aliwaonya Wakristo wasichafue Neno la Mungu kwa falsafa za wanadamu alipoandika: “Tumeyakataa kabisa mambo ya kichinichini yaliyo ya kuaibikia, si kutembea kwa ujanja, wala tukilighushi neno la Mungu.” Siku hizo, wauzaji wa divai wenye pupa walikuwa wakitia divai maji ili iwe nyingi wapate pesa zaidi. Sisi hatughushi Neno la Mungu kwa kulichanganya na falsafa za wanadamu. Paulo alitangaza kwamba “sisi si wachuuzi wa neno la Mungu kama watu wengi walivyo, bali tunasema kwa weupe wa moyo, ndiyo, tukiwa waliotumwa kutoka kwa Mungu, mbele ya Mungu, kwa ushirika na Kristo.”—2 Kor. 2:17; 4:2.

      Nyakati nyingine unaweza kunukuu andiko ili kukazia kanuni fulani. Biblia imejaa kanuni zenye mwongozo bora zinazotusaidia kushughulika na hali mbalimbali za maisha. (2 Tim. 3:16, 17) Lakini hakikisha kwamba unatumia kwa usahihi kanuni hizo na usitumie andiko vibaya, ukifanya andiko lionekane kana kwamba linasema jambo ambalo wewe unataka liseme. (Zab. 91:11, 12; Mt. 4:5, 6) Ni lazima utumie andiko kulingana na kusudi la Yehova, kupatana na Neno lote la Mungu.

      ‘Kulitumia sawasawa neno la ile kweli’ pia kunatia ndani kufahamu vile Biblia inavyosema. Biblia si “rungu” la kutwangia watu wengine. Walimu wa kidini waliompinga Yesu Kristo walinukuu Maandiko, lakini walipuuza mambo mazito ambayo Mungu alitaka yaonyeshwe kama vile haki, rehema, na uaminifu. (Mt. 22:23, 24; 23:23, 24) Yesu alionyesha utu wa Baba yake alipofundisha Neno la Mungu. Bidii ya Yesu kwa ajili ya ile kweli iliambatana na upendo mwingi aliowaonyesha watu aliofundisha. Tujaribu kuiga mfano wake.—Mt. 11:28.

      Tunawezaje kuwa na hakika kwamba tunatumia maandiko vizuri? Kusoma Biblia kwa ukawaida kunasaidia. Pia tunahitaji kutambua kwamba Yehova ametuandalia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” jamii ya Wakristo watiwa-mafuta ambayo Yehova anatumia kuandalia nyumba ya waamini chakula cha kiroho. (Mt. 24:45) Funzo la binafsi na kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida na kuishiriki kutatusaidia kufaidika na mafunzo yanayoandaliwa kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara.

      Ikiwa kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kinapatikana katika lugha yenu, jifunze kukitumia vizuri na kitakusaidia sana kuelewa kwa urahisi jinsi ya kupata mwongozo unaohitaji ili kutumia vizuri mamia ya maandiko ambayo hutumiwa mara nyingi katika huduma ya shambani. Ikiwa unataka kutumia andiko ambalo hulifahamu, kwa unyenyekevu fanya utafiti ili ulitumie sawasawa neno la ile kweli.—Mit. 11:2.

      Onyesha Vizuri Jinsi Andiko Linavyohusika. Unapowafundisha wengine, hakikisha wanaelewa vizuri uhusiano ulioko kati ya habari unayozungumzia na maandiko unayotumia. Ukiuliza swali kabla ya kusoma andiko, waonyeshe wasikilizaji jinsi andiko hilo linavyojibu swali lile. Ikiwa unatumia andiko kuunga mkono jambo fulani unalosema, hakikisha mwanafunzi anaona wazi jinsi andiko hilo linavyothibitisha jambo hilo.

      Mara nyingi haitoshi tu kusoma andiko, hata kama unalisoma kwa mkazo. Kumbuka kwamba mtu wa kawaida hafahamu vizuri Biblia na ukisoma andiko mara moja tu labda hatakuelewa. Kazia sehemu ya andiko inayohusu jambo unalozungumzia.

      Kwa kawaida unaweza kukazia jambo kwa kutenga maneno makuu, yaani maneno ambayo yanahusiana na jambo unalozungumzia. Njia rahisi zaidi ni kurudia kutaja maneno yenye mambo unayotaka kukazia. Ikiwa unazungumza na mtu fulani, unaweza kuuliza maswali ambayo yanaweza kumsaidia kutambua maneno makuu. Wasemaji wengine wanapohutubu, wao hupendelea kukazia maneno makuu kwa kutumia maneno mengine yenye maana sawa au kwa kurudia kutaja wazo kuu. Na ukiamua kufanya hivyo, hakikisha wasikilizaji wanaona jinsi jambo unalozungumzia linavyohusiana na andiko unalosoma.

      Ikiwa umetenga maneno makuu, basi umeweka msingi mzuri. Sasa jenga kwenye msingi huo. Kabla ya kusoma andiko, je, umeonyesha wazi sababu ya kulisoma? Ikiwa ndivyo, onyesha jinsi maneno ambayo umekazia yanavyohusiana na matarajio ya wasikilizaji kuhusu andiko hilo. Onyesha vizuri uhusiano ulioko. Hata kama utangulizi wa andiko hilo haukuwa dhahiri sana, onyesha sababu ya kulisoma.

      Mafarisayo walimwuliza Yesu swali ambalo walifikiri ni gumu, yaani: “Je, yaruhusika kisheria mtu kutaliki mke wake kwa kila namna ya sababu?” Yesu alitumia Mwanzo 2:24 kujibu. Ebu ona kwamba Yesu alitaja sehemu tu ya andiko hilo, kisha akaonyesha jinsi sehemu hiyo inavyohusika. Baada ya Yesu kutaja kwamba mwanamume na mke wake watakuwa “mwili mmoja,” alimalizia kusema: “Kwa hiyo, kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.”—Mt. 19:3-6.

      Unapaswa kufafanua andiko kwa kadiri gani ili liwe wazi? Hiyo inategemea wasikilizaji na umuhimu wa jambo unalozungumza. Kusudi lako liwe kufafanua andiko kwa njia rahisi na ya moja kwa moja.

      Tumia Maandiko Kutoa Sababu. Matendo 17:2, 3 linapozungumzia huduma ya mtume Paulo huko Thesalonike, linatuambia kwamba ‘alitoa sababu kutokana na Maandiko.’ Kila mtumishi wa Yehova anapaswa kujaribu kukuza uwezo huu. Kwa mfano, Paulo alisimulia mambo yaliyohusu maisha ya Yesu na huduma yake, akaonyesha kwamba mambo hayo yalitabiriwa katika Maandiko ya Kiebrania, kisha akamalizia kwa nguvu akisema: “Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ninayewatangazia nyinyi.”

      Paulo alinukuu Maandiko ya Kiebrania mara nyingi alipowaandikia Waebrania. Mara nyingi alitenga neno au maneno fulani kisha akaonyesha umuhimu wake ili kukazia jambo au kulifafanua vizuri. (Ebr. 12:26, 27) Katika masimulizi ya Waebrania sura ya 3, Paulo alinukuu Zaburi 95:7-11. Ona kwamba alifafanua sehemu tatu za maandiko hayo: (1) alitaja moyo (Ebr. 3:8-12), (2) umuhimu wa neno “Leo” (Ebr. 3:7, 13-15; 4:6-11), na (3) maana ya maneno haya: “Hawataingia katika pumziko langu.” (Ebr. 3:11, 18, 19; 4:1-11) Jaribu kuiga mfano huo unapoonyesha jinsi kila andiko linavyohusika na jambo unalozungumzia.

      Ona jinsi Yesu alivyotoa sababu vizuri akitumia Maandiko katika Luka 10:25-37. Mtaalamu mmoja wa Sheria alimwuliza: “Mwalimu, ni kwa kufanya nini mimi nitarithi uhai udumuo milele?” Kwanza, Yesu akamwuliza mtu huyo maoni yake juu ya swali hilo, kisha Yesu akakazia kwamba ni muhimu kufanya kile ambacho Neno la Mungu linasema. Ilipokuwa wazi kwamba mtu huyo haelewi, Yesu alifafanua kabisa neno moja tu katika andiko hilo, “jirani.” Na badala ya kulifafanua tu neno hilo, Yesu alitumia mfano uliomwezesha mtu huyo afikie jibu linalofaa.

      Yesu alipokuwa akijibu maswali, hakunukuu tu maandiko na kutoa majibu rahisi na ya wazi. Alifafanua maandiko hayo na kuonyesha jinsi yanavyojibu swali aliloulizwa.

      Masadukayo walipopinga tumaini la ufufuo, Yesu alikazia sehemu fulani tu ya Kutoka 3:6. Lakini hakuachia hapo tu. Alisababu juu ya andiko hilo na kuonyesha wazi kwamba ufufuo ni sehemu ya kusudi la Mungu.—Mk. 12:24-27.

      Ili kuwa mwalimu bora ni muhimu kukuza uwezo wa kutumia Maandiko kutoa sababu vizuri na kwa matokeo mazuri.

      JINSI YA KUKUZA UWEZO HUO

      • Soma Biblia kwa ukawaida. Jifunze kwa makini Mnara wa Mlinzi, na utayarishe vizuri mikutano ya kutaniko.

      • Hakikisha unajua maana ya maneno unayotumia katika andiko lolote unalotaka kutumia. Soma andiko hilo kwa makini ili uelewe vizuri jambo linalosema.

      • Uwe na mazoea ya kutumia vichapo vyetu vya Kikristo kufanya utafiti.

      MAZOEZI: Fikiria 2 Petro 3:7. Je, linathibitisha dunia itaharibiwa kwa moto? (Unapofafanua maana ya neno “dunia,” pia fikiria maana ya “mbingu.” Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba “dunia” inaweza kuwa na maana ya mfano? Kulingana na mstari wa 7 ni nani, au ni nini kinachoharibiwa? Jambo hilo linalinganaje na tukio la wakati wa Noa linalotajwa katika mstari wa 5 na 6?)

  • Kuonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia Habari
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 23

      Kuonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia Habari

      Unahitaji kufanya nini?

      Wasaidie wasikilizaji waone jinsi habari unayozungumzia inavyohusu maisha yao au jinsi wanavyoweza kuitumia vizuri.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Kama watu hawaoni jinsi wanavyoweza kutumia habari unayosema, wanaweza kukuambia hawataki kusikiliza au wanaweza kuacha kukusikiliza na kuruhusu akili zao zitangetange.

      IWE unazungumza na mtu mmoja au watu wengi, si vizuri kudhani wasikilizaji watapenda habari yako eti kwa sababu unaipenda. Ingawa ujumbe wako ni muhimu, baada ya muda watu wanaweza kuacha kukusikiliza ikiwa huwaonyeshi faida yake.

      Ndivyo ilivyo pia na wasikilizaji katika Jumba la Ufalme. Wanaweza kusikiliza unapotumia mfano au unaposimulia tukio ambalo hawajasikia. Lakini wanaweza kuacha kukusikiliza unapozungumzia mambo ambayo tayari wanajua, hasa ukikosa kujenga hotuba yako juu ya mambo hayo. Unahitaji kuwasaidia waone kwa nini habari hiyo ina faida na pia inawafaidi kwa njia gani.

      Biblia inatuhimiza tufikiri kwa njia inayofaa. (Mit. 3:21) Yehova alimtumia Yohana Mbatizaji kuwaonyesha watu “hekima itumikayo ya walio waadilifu.” (Luka 1:17) Hekima hii inategemea kumcha Yehova. (Zab. 111:10) Wale wanaotambua hekima hii husaidiwa kukabiliana kwa mafanikio na maisha wakati huu, na kushika uhai halisi na wa milele wa wakati ujao.—1 Tim. 4:8; 6:19.

      Kuwaonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia Habari. Ili hotuba yako ifaidi wasikilizaji, mbali na kuifikiria hotuba hiyo wafikirie wasikilizaji. Usiwafikirie tu kwa ujumla. Miongoni mwa wasikilizaji hao mna watu mmoja-mmoja na familia tofauti-tofauti. Huenda kuna watoto wadogo sana, vijana, watu wazima, na wengine ambao ni wazee. Huenda pia miongoni mwao mna wale wanaopendezwa na wale ambao walianza kumtumikia Yehova kabla ya wewe kuzaliwa. Huenda wengine wamekomaa kiroho, na huenda wengine bado wana mielekeo na hali fulani za kilimwengu. Jiulize: ‘Hotuba hii itawasaidiaje wasikilizaji? Nawezaje kuwasaidia kuelewa jambo ambalo nitazungumzia?’ Unaweza kuamua kukazia akili kikundi kimoja au vikundi viwili kati ya vikundi ambavyo tumetaja. Lakini usiwasahau wengine kabisa.

      Ufanyeje ukipewa hotuba inayozungumzia fundisho fulani la msingi la Biblia? Unaweza kufanya nini ili hotuba kama hiyo iwafaidi wasikilizaji ambao tayari wanafahamu fundisho hilo? Jaribu kuimarisha usadikisho wao kulihusu. Kwa njia gani? Kwa kutoa sababu za Maandiko zinazolithibitisha. Pia unaweza kuzidisha uthamini wao kuhusu fundisho hilo la Biblia. Unaweza kuzidisha uthamini wao kwa kuwaonyesha jinsi fundisho hilo linavyopatana na kweli nyinginezo za Biblia na jinsi linavyopatana na utu wa Yehova. Tumia mifano au ikiwezekana simulia matukio halisi maishani yanayoonyesha jinsi ambavyo watu wengine wamefaidika na kubadili maoni yao juu ya wakati ujao walipoelewa fundisho hilo.

      Usieleze kwa ufupi tu jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo mwishoni mwa hotuba yako. Tangu mwanzoni kabisa, kila msikilizaji anapaswa kuona kwamba “habari hii inanihusu.” Baada ya kuweka msingi huo, endelea kuwaonyesha jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo unapokuza kila moja ya mambo makuu ya hotuba na pia unapomalizia hotuba.

      Unapowaeleza akina ndugu jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo, fuata kanuni za Biblia. Hiyo inamaanisha nini? Inamaanisha kuwa mwenye upendo na hisia-mwenzi unapowaeleza jinsi wanavyoweza kutumia habari unayozungumzia. (1 Pet. 3:8; 1 Yoh. 4:8) Hata mtume Paulo alipokuwa akishughulikia matatizo mazito katika Thesalonike, alihakikisha ametaja maendeleo mazuri ya kiroho ya ndugu na dada zake Wakristo waliokuwa huko. Pia alionyesha ana hakika kwamba wanataka kufanya yaliyo sawa kuhusu jambo alilokuwa akizungumzia. (1 The. 4:1-12) Huo ni mfano mzuri sana ambao tunaweza kuuiga.

      Je, kusudi la hotuba yako ni kuchochea akina ndugu ili wahubiri na kufundisha wengine habari njema? Basi wasaidie wawe na shauku na kuthamini pendeleo hilo. Lakini wakati uo huo ukumbuke kwamba watu wana uwezo tofauti-tofauti, na hata Biblia inaonyesha hivyo. (Mt. 13:23) Usiwafanye akina ndugu wahisi hatia. Waebrania 10:24 linatuhimiza ‘tuchocheane kwenye upendo na kazi zilizo bora.’ Tukiwachochea kwenye upendo, watatenda kwa makusudio mazuri. Badala ya kuwaamuru-amuru, tambua kwamba Yehova anataka tuwachochee ‘watii kwa njia ya imani.’ (Rom. 16:26) Basi, tukikumbuka mambo haya tutajaribu kuimarisha imani yetu na imani ya wengine.

      Kuwasaidia Wengine Kuona Faida ya Ujumbe Wetu. Unapohubiri, usisahau kuonyesha faida ya habari njema maishani mwao. Ili ufaulu, unahitaji kufahamu mambo yanayowahangaisha watu katika eneo lenu. Unawezaje kujua mambo hayo? Sikiliza habari kwenye redio au televisheni. Tazama ukurasa wa mbele wa gazeti la habari. Pia jaribu kuwafanya watu wazungumze, na uwasikilize wanapoongea. Unaweza kugundua wana matatizo makubwa kama vile kupoteza kazi, kulipa kodi ya nyumba, ugonjwa, kifo cha mshiriki wa familia, kupatwa na uhalifu, kutendwa isivyofaa na mtu mwenye mamlaka, kuvunjika kwa ndoa, kuwadhibiti watoto, na kadhalika. Je, Biblia inaweza kuwasaidia? Bila shaka, ndiyo.

      Inaelekea kwamba unapoanzisha mazungumzo utakuwa na jambo fulani akilini unalotaka kusema. Lakini ukiona kwamba mtu huyo ana jambo jingine linalomhangaisha sana, usisite kuzungumza naye jambo hilo ikiwezekana, au mwambie utamletea habari ambazo zinaweza kumsaidia. Ingawa tunaepuka ‘kujiingiza katika lile lisilotuhusu,’ tunafurahi kuwapa wengine mashauri ya Biblia ambayo wanaweza kutumia. (2 The. 3:11) Ni wazi kwamba jambo linalowavutia watu zaidi ni shauri la Biblia linalohusu maisha yao.

      Watu wasipoona jinsi ujumbe wetu unavyowahusu, wanaweza kukatiza mazungumzo haraka. Hata wakituruhusu tuendelee kuzungumza, tukikosa kuwaonyesha faida ya habari hiyo hawatafaidika. Lakini tukiwaonyesha faida ya ujumbe wetu, mazungumzo yetu yanaweza kubadili maisha yao.

      Unapofundisha watu Biblia, endelea kukazia jinsi wanavyoweza kutumia habari wanayojifunza. (Mit. 4:7) Wasaidie wanafunzi waelewe shauri, kanuni, na mifano inayopatikana katika Maandiko ambayo inawaonyesha jinsi ya kufuata njia za Yehova. Kazia faida ambazo watapata. (Isa. 48:17, 18) Kufanya hivyo kutawachochea wanafunzi wafanye mabadiliko yanayotakikana katika maisha yao. Wasaidie wampende Yehova na kuwa na tamaa ya kumpendeza, na pia wasaidie wachochewe na moyo wao wenyewe kutumia shauri la Neno la Mungu.

      JINSI YA KUFAULU

      • Mbali na kufikiria habari unapotayarisha hotuba, wafikirie pia wasikilizaji. Toa hotuba hiyo kwa njia ambayo itawafaidi kwelikweli.

      • Usieleze jinsi ambavyo wanaweza kutumia habari hiyo unapofikia mwisho tu wa hotuba. Bali eleza jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo kotekote katika hotuba.

      • Unapofanya matayarisho ya kuhubiri, fikiria mambo ambayo yanawahangaisha watu katika eneo lenu.

      • Unapohubiri, wasikilize watu kwa makini, na ubadilishe mahubiri yako kulingana na hali.

      MAZOEZI: Pitia matoleo ya Huduma Yetu ya Ufalme ambayo unaweza kupata, kisha chagua utangulizi mmoja au tangulizi mbili ambazo unaona zinafaa sana eneo lenu. Jaribu kuzitumia katika utumishi wa shambani.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki