Moldova
Moldova iko mashariki ya Milima ya Carpathia. Nchi hiyo yenye rutuba ina nyanda, mabonde na makorongo marefu na milima yenye misitu. Moldova ina ukubwa wa kilometa 34,000 za mraba na ina mandhari tofauti-tofauti na wanyama wengi wa aina mbalimbali kama vile mbweha, mbwa-mwitu, sungura, melesi, kulungu, vicheche, na nguruwe-mwitu.
Moldova ina udongo wenye rutuba na hali nzuri ya hewa, hivyo, inazaa matunda, nafaka, mboga, na mazao mengine ya kilimo kwa wingi. Maji yanapatikana kwa wingi katika chemchemi 2,200 na mito na vijito 3,000 ambavyo vinatiririka kusini na kuingia Bahari Nyeusi. Dniester ndio mto mkubwa, na sehemu nyingi za mto huo unaotiririka kwa kasi nchini Moldova zinapitika kwa meli. Moldova inapakana na nchi ya Ukrainia upande wa kaskazini, mashariki na kusini, na Mto Dniester uko kwenye mpaka wa nchi hizo, au unatiririka karibu na mpaka huo. Moldova inapakana na Rumania upande wa magharibi, na Mto Prut unaoingia Mto Danube uko mpakani.
Msukosuko wa Siku za Kale Nchini Moldova
Zamani, njia kuu ya kuelekea Ulaya ilipitia nchi hiyo iliyo kati ya Mto Dniester na Prut, ambayo kwa mamia ya miaka iliitwa Bessarabia na Moldavia. Kutoka mwaka wa 1000 K.W.K. hadi mwaka wa kwanza K.W.K., eneo hilo lilikuwa sehemu ya Skithia. Baadaye, Milki ya Roma ilitawala nchi hiyo kwa kiasi fulani. Ilivamiwa pia na watu kama vile Wagothi, Wahuni, na Waavari. Katika karne ya 13 na 14, Moldavia ilitawaliwa na Waturuki, na katika karne ya 16 ikawa sehemu ya Milki ya Uturuki. Katika Mkataba wa Bucharest wa mwaka wa 1812, Waturuki walisalimisha Bessarabia na nusu ya Moldavia kwa Warusi, na eneo hilo lote likaitwa Bessarabia.
Bessarabia ikawa sehemu ya Rumania mwaka wa 1918. Hata hivyo, ilikuwa sehemu ya miliki ya Urusi kwa muda mfupi katika mwaka wa 1940, na tena katika mwaka wa 1944. Chini ya utawala wa Muungano wa Sovieti, eneo hilo liliitwa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Sovieti ya Moldavia (SSR). Utawala wa Kikomunisti wa Sovieti ulipoanguka hatimaye, SSR ya Moldavia ilikataa utawala wa Sovieti na kuwa nchi huru ya Jamhuri ya Moldova, Agosti 27, 1991.a Jiji la Chisinau, lililokuwa Kishinev, ndilo jiji kuu la Moldova.
Idadi ya watu iliongezeka sana nchini Moldova katika miaka ya 1960, lakini tangu miaka ya 1970 ongezeko hilo limepungua. Kwa sasa kuna watu milioni 4.3 hivi nchini humo. Wakazi wengi wa Moldova hufanya kazi katika mashamba ya mizabibu na viwanda vya divai, na asilimia 3 ya divai yote ulimwenguni inatengenezwa Moldova. Divai kutoka Moldova inapendwa sana Urusi na Ulaya Mashariki. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 71.) Lakini nchini Moldova, kuna shamba lingine kubwa sana la mizabibu ambalo hutoa mazao bora, yaani, sifa kwa Yehova.
“Shamba la Mizabibu la Divai Yenye Kutoa Povu!”
Kupitia nabii Isaya, Yehova alifafanua Israeli wa kiroho kuwa “shamba la mizabibu la divai yenye kutoa povu.” Kama ilivyotabiriwa, shamba hilo la mizabibu ‘limejaza matunda juu ya uso wa nchi yenye kuzaa,’ yaani, chakula cha kiroho chenye lishe. (Isa. 27:2-6) Kwa hiyo, hatua kwa hatua, mamilioni ya “kondoo wengine” wamejiunga na Wakristo waliotiwa mafuta.—Yoh. 10:16.
Watu wa Yehova nchini Moldova wamefurahi sana kushiriki katika utimizo wa unabii huo wa ajabu. Kwa sababu chakula cha kiroho kimetolewa kwa ukawaida na tengenezo la Yehova, sasa kuna mhubiri 1 kwa kila watu 229 nchini Moldova. Katika kijiji kimoja asilimia 25 ya wakazi ni Mashahidi wa Yehova.
Lakini kama tutakavyoona, ongezeko hilo liliambatana na majaribu makali. Kwa miaka 70 hivi, watu wa Mungu walipigwa marufuku, waliteswa, na kufungwa gerezani chini ya utawala wa wafalme wa Rumania, Wafashisti, na Wakomunisti. Hata hivyo, kama katika nchi nyingine, Yehova ametimiza ahadi yake kuhusiana na “shamba la mizabibu la divai yenye kutoa povu” nchini Moldova. Alisema hivi kupitia Isaya: “Mimi, Yehova, ninamlinda yeye. Nitamnywesha maji kila wakati. Ili yeyote asielekeze fikira zake kupigana naye, nitamlinda usiku na mchana.” (Isa. 27:2, 3) Unapotafakari masimulizi ya watu wa Yehova nchini Moldova, ujasiri wao na imani yao na zikuimarishe katika azimio lako la kumsifu Yehova kwa kuendelea kuzaa matunda bora, haidhuru Shetani atatumia vikwazo gani kukuzuia usimtumikie Yehova.
Ndugu Russell Achunguza Shamba
Mwanzoni, matawi ya mzabibu halisi ambayo huzaa matunda huwa machipukizi madogo tu. Ukuzi wa kiroho ulianza vivyo hivyo nchini Moldova. Hebu tuone jinsi Yehova alivyofanya chipukizi hilo dogo lisitawi na kuwa mzabibu mkubwa unaozaa matunda ambao tunaona nchini Moldova leo. (1 Kor. 3:6) Masimulizi yetu yaanza mwishoni mwa karne ya 19, wakati Mwanafunzi wa Biblia, Charles Taze Russell, alipozuru nchi hiyo katika safari yake huko Ulaya.
Katika toleo la Septemba 1891 la gazeti, Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence (sasa ni Mnara wa Mlinzi), Ndugu Russell aliandika kwamba alikuwa amemtembelea Mkristo Myahudi, Joseph Rabinowitch, aliyekuwa wakili. Ndugu Russell alisema kwamba “kumtembelea Ndugu Joseph Rabinowitch nyumbani kwake huko Kischenev, Urusi [sasa ni Chisinau, Moldova] ni mojawapo ya mambo ambayo tumefurahia kufikia wakati huu. Yeye pamoja na familia yake, ambao wote wanamwamini Bwana Yesu, walitukaribisha kwa uchangamfu. . . . Tuliona kwamba anaelewa mafundisho ya kitabu DAWN [kimojawapo cha vitabu Millennial Dawn] na anakubali mafundisho hayo.” Yaelekea wanaume hao walikubaliana kuhusu mafundisho mengi ya Maandiko kwa kuwa Ndugu Russell alimwita rafiki yake wa Moldova “Ndugu Rabinowitch.”
Rabinowitch na familia yake walijitahidi kuwasaidia Wayahudi kumkubali Kristo na kumtumaini Masihi. Kulikuwa na Wayahudi zaidi ya 50,000 jijini Chisinau. Russell alieleza kwamba kando ya nyumba na ofisi zake, kulikuwa na “nyumba mpya nzuri kwa ajili ya ibada, ambayo inaweza kutoshea watu mia moja ishirini na watano hivi.” Rabinowitch alikuwa na mashine mpya ya kupiga chapa inayoendeshwa kwa mkono, ambayo alitumia kuchapa trakti zilizoandikwa hasa kwa ajili ya Wayahudi. Miaka sita hivi baadaye, katika mwaka wa 1897, Rabinowitch alimwandikia hivi Ndugu Russell: “Ndugu Russell Mpendwa: Mwishoni mwa mwaka huu, inanibidi kukushukuru sana kwa uradhi wa kiroho ambao mimi hupata kwa kusoma gazeti lako bora la ZION’S WATCH TOWER, ambalo mimi hulipokea kwa ukawaida. Kwangu gazeti hilo ni kama meli inayoleta chakula cha kiroho kutoka mbali.” Hata hivyo, ingawa mtu huyo alipenda sana kweli ya Biblia, na licha ya bidii yake, ilichukua miaka 30 kabla ya mbegu za Ufalme kutia mizizi na kuanza kutoa mazao nchini Moldova.—Mt. 13:1-8, 18-23.
Wengi Wakatishwa Tamaa na Vita vya Kwanza vya Ulimwengu
Kwa sababu ya mabadiliko ya kisiasa yenye kushtua yaliyokumba Ulaya wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, mbegu za Ufalme zilizopandwa nchini Moldova zilianguka katika udongo wenye rutuba. Baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, vilivyoitwa Vita Vikuu wakati huo, Moldova ilijitenga na Urusi na kujiunga na Rumania. Urusi ilikuwa chini ya utawala wa Kikomunisti wakati huo. Wanajeshi wengi wa Moldova ambao walikuwa wameona mambo ya kutisha vitani, walirudi nyumbani wakiwa wamekata tamaa. Wengi wao walikuwa wamelelewa na wazazi waliokuwa waumini wa Kanisa la Othodoksi, lakini sasa walianza kutilia shaka mafundisho yake.
Mmoja wao alikuwa Ion Andronic, ambaye alirudi kwenye kijiji cha kwao cha Corjeuţi mwaka wa 1919. Upendezi wake uliamshwa alipozungumzia Biblia pamoja na Wasabato na Wabaptisti alipokuwa mfungwa wa vita. Alirudi nyumbani na Biblia aliyopata katika kambi ya gereza, akazungumzia ujumbe wake pamoja na familia yake na majirani wake, nao wakapendezwa pia.
Ilie Groza alikuwa mmoja wa majirani wake. Alikuwa Marekani wakati wa vita na alirudi nyumbani akiwa na “Agano Jipya,” ambalo alikuwa amepata akiwa huko. Familia ya Andronic na Groza, ambao walikuwa marafiki wa karibu, walianza kujifunza Neno la Mungu pamoja. Pia walikuwa na vitabu vilivyochapishwa na Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo.
Ioana, binti ya Ilie Groza, akumbuka hivi: “Nadhani nilikuwa na umri wa miaka sita tu wakati familia yetu ilipoanza kupata vitabu vilivyochapishwa na Wanafunzi wa Biblia. Sijui tulipata wapi vitabu hivyo, lakini ninakumbuka jinsi wazazi wangu na ndugu na dada zangu wakubwa walivyosisimuka walipozungumzia Maandiko yaliyoelezwa wazi katika vitabu hivyo.”
Ion Andronic hakujiweka wakfu kwa Yehova. Lakini familia yake yote na watu wengi wa familia ya Groza walijiweka wakfu. Ioana akumbuka hivi: “Mwanzoni, mikutano yetu ilihudhuriwa na familia yetu na familia ya Andronic pekee. Wazazi wangu walikuwa na binti wanne, na Andronic alikuwa na wavulana na binti kadhaa. Punde si punde Vasile Andronic na dada yangu Feodolina walipendana, na hatimaye wakaoana.
“Baada ya muda, Tudor na Daria Groza, ambao ni watu wa ukoo wetu, walijiunga na kikundi chetu. Tudor alikuwa msomaji wa Biblia mwenye bidii sana. Hata alisafiri hadi kwenye ofisi ya tawi huko Cluj-Napoca, Rumania, ili apate vitabu na ajibiwe maswali yake mengi ya Biblia. Katika miaka ya baadaye alisaidia sana kiroho kutaniko letu dogo.
“Watu wa familia ya Iacuboi, walioishi katika eneo letu, pia walijiunga na mazungumzo ya Biblia nyumbani kwetu. Kabla ya hapo, Petru Iacuboi, kichwa cha familia hiyo, alikuwa amemkaribisha mtu fulani aliyekuwa akisambaza Biblia. Mgeni huyo aliamsha hamu ya Petru ya kusoma Maandiko. Petru alichunguza mafundisho ya Wabaptisti kwa muda mfupi, na alitambua kwamba hayakuwa ya kweli. Ndipo alipojiunga na kikundi chetu cha Wanafunzi wa Biblia kilichoendelea kupanuka.
“Mambo tuliyojifunza yalituchochea sisi sote kuwahubiria kwa bidii habari njema za Ufalme marafiki na watu wetu wa ukoo, ambao wengi wao waliishi katika kijiji chetu na vijiji jirani.”
Ili kuonyesha jinsi ujumbe wa Ufalme ulivyoenea kwa haraka nchini Moldova, gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1921, lilisema hivi: “Ndugu mmoja kutoka Bessarabia [kama Moldova ilivyoitwa wakati huo], ambaye hivi majuzi aliacha kuwa mhubiri katika Kanisa la Wasabato, anaandika hivi: ‘Watu 200 hivi katika kijiji hiki, na vijiji vingine vingi vya karibu, wamekubali kweli.’”
Mapema katika miaka ya 1920, Ilarion Bugaian, muumini thabiti wa Kanisa la Othodoksi katika kijiji cha Şirăuţi, alijifunza kweli. Alimtumikia Yehova kwa uaminifu hadi kifo chake. Mwanafunzi wa Biblia anayeitwa Moise Ciobanu alirudi jiji la Bălţi kutoka Ujerumani. Alikuwa amejifunza kweli alipokuwa gerezani huko Ujerumani wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Muda si muda, kikundi kilianzishwa na baadaye kikawa kutaniko la kwanza jijini Bălţi.
Mashahidi Kutoka Rumania Wasaidia
Katika miaka ya 1920, ofisi ya tawi ya Rumania iliwatuma ndugu waliokuwa na uzoefu huko Moldova ili wasaidie katika kazi ya kuhubiri na kuwaimarisha wale wapya walioshirikiana na watu wa Mungu. Mmoja wa wale wahubiri wa habari njema waliotumwa ni Vasile Ciucaş wa Transylvania. Alijua lugha ya Kirumania na Kihungaria. Kila mara alipotembelea kutaniko jipya huko Corjeuţi Vasile alikaa kwa Ilie Groza na familia yake. Ioana anasema hivi kuhusu ziara hizo zenye kufurahisha: “Nadhani nilikuwa na umri wa miaka minane wakati huo, lakini bado ninakumbuka ziara za Ndugu Ciucaş. Alikuwa ndugu mwenye fadhili sana, na sikuzote alisimulia hadithi zenye kupendeza sana hivi kwamba hatukutaka kwenda kulala! Mimi na dada yangu tuling’ang’ania kukaa karibu naye.”
Mashahidi hao kutoka Rumania, pamoja na wahubiri wenye bidii wa kijiji hicho, walieneza habari njema katika vijiji vya karibu. Cazimir Cislinschii alihubiri habari nzuri za Biblia katika kijiji cha Tabani, umbali wa kilometa 11 kutoka Corjeuţi. Cazimir alikuwa amesikia ujumbe wa Ufalme alipokuwa mwanajeshi huko Rumania. Kati ya watu wa kwanza kukubali mahubiri ya Cazimir huko Tabani ni Dumitru Gorobeţ aliyekuwa mwanafunzi mwenye bidii sana. Kwa sababu ya bidii yake na ya wengine kama yeye, sasa kuna Mashahidi 475 katika kijiji cha Tabani chenye wakazi 3,270.
Mapema katika miaka ya 1920, ujumbe wa Ufalme ulihubiriwa katika kijiji cha Caracuşeni, umbali wa kilometa mbili au tatu hivi kutoka Corjeuţi. Kati ya wanakijiji wa kwanza waliokubali kweli katika kijiji cha Caracuşeni ni Vladimir Lungu aliyebatizwa mwaka wa 1927. Vladimir ambaye alivumilia mateso mengi kwa sababu ya imani yake ya Kikristo alikuwa mwaminifu kwa Yehova hadi kifo chake mwaka wa 2002. Wakati wa maisha yake, watu wengi sana katika kijiji hicho walikubali kweli hivi kwamba sasa asilimia 25 ya wakazi 4,200 wa Caracuşeni ni Mashahidi!
Ndugu mwingine mwaminifu ni Alexandru Mikitkov aliyejifunza kweli mwaka wa 1929 alipokuwa akitembelea jiji la Iasi huko Rumania. Mwana wake Ivan, anasema hivi: “Baba aliporudi kijiji cha kwetu cha Ţaul, mara moja alianza kuhubiri habari njema, na baada ya muda mfupi tulianza kufanya mikutano ya Kikristo nyumbani kwetu.”
Ivan anaongeza hivi: “Baba aliwasiliana na ofisi ya tawi ya Rumania, na mara kwa mara, ndugu wakomavu kutoka Rumania walitutembelea. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba dada yangu mchanga alikufa wakati wa ziara ya ndugu mmoja kutoka Rumania mwaka wa 1931. Kwa sababu familia yetu ilijulikana sana, wanakijiji wengi walikuja kwenye mazishi. Ndugu Vănica, mgeni wetu kutoka Rumania, alitoa hotuba ya mazishi. Alitoa ushuhuda wenye kuvutia na kufunua uwongo ambao makasisi walikuwa wakieneza kwamba Wanafunzi wa Biblia hawafanyi mazishi kwa njia ya heshima. Isitoshe, Ndugu Vănica alieleza wazi tumaini la ufufuo, na hivyo mbegu nzuri ilipandwa katika mioyo ya baadhi ya watu waliohudhuria. Baada ya muda mfupi, wao pia walichukua msimamo imara upande wa kweli ya Biblia.
“Ndugu Vănica aliisaidia sana familia yetu kwa kutuimarisha kiroho. Kwa mfano, kaka yangu, Dumitru, aliamua kuwa mhudumu wa wakati wote. Kwa sababu alitaka kuwasaidia watu wengi iwezekanavyo, alihama nyumbani ili kuhubiri katika maeneo ya Moldova yasiyohubiriwa bado. Wengine katika familia walimwunga mkono kwa moyo wote. Lakini nilimkosa sana kaka yangu. Kwa upande mwingine, tulifurahi sana alipokuja kututembelea na kusimulia mambo mengi yenye kusisimua aliyofurahia katika kazi ya kuhubiri!”
Upinzani wa Makasisi Wazidi
Makasisi wa Kanisa la Othodoksi walipinga kazi ya kuhubiri habari njema tangu mwanzo. Lakini walikasirika hasa wakati waumini wa kanisa lao waliokuwa wamejifunza kweli ya Biblia walipokataa kufanya ishara ya msalaba au kubatiza watoto wao.
Ioana Groza alipokuwa na umri wa miaka kumi hivi, kasisi wa kanisa la Othodoksi la kwao alijaribu kumlazimisha atende kinyume cha imani yake. Anasema hivi: “Baba alikuwa ametuambia sisi watoto kwamba kufanya ishara ya msalaba hakupatani na Maandiko. Lakini tulipokuwa shuleni kasisi alisisitiza tufanye ishara ya msalaba. Nilimwogopa mtu huyo, lakini niliogopa pia kutomtii Baba. Kwa hiyo, badala ya kwenda shuleni nilijificha katika ghala fulani. Baada ya muda, Baba alielezwa kwamba sikuenda shuleni kwa siku kadhaa. Hakunikemea, bali kwa fadhili aliniomba nimwambie sababu ya kutoenda shuleni. Nilipomweleza kwamba nilimwogopa kasisi, Baba alinishika mkono na tukaenda nyumbani kwa mtu huyo.
“Kwa sauti thabiti, Baba alimwambia kasisi hivi: ‘Kama wewe ungekuwa ukimlisha binti yangu, na kumwandalia mavazi na makao, huenda ungeruhusiwa kumwambia kile anachopaswa kufanya kuhusiana na ibada. Lakini kwa sababu sivyo ilivyo, basi usiingilie kile ninachomfundisha mtoto wangu.’ Ninafurahi kusema kwamba baada ya hapo, kasisi huyo hakunisumbua tena.”
Kwa kawaida, makasisi walikuwa watu mashuhuri katika jamii. Kama viongozi wa dini wa siku za Yesu, walitumia mamlaka yao kuharibu jina zuri la watumishi wa Yehova, kusudi waumini wa makanisa yao wawadhihaki ndugu au waogope kuongea nao. Makasisi walitumia sana chuki ya kisiasa kati ya watu wa Moldova na Wasovieti kuwapinga Mashahidi. Kwa mfano, wakati huo watu waliwaogopa na kuwashuku sana Wakomunisti katika nchi jirani ya Muungano wa Sovieti. Kwa hiyo, makasisi wa Kanisa la Othodoksi walisema kwamba Wanafunzi wa Biblia hukataa kufanya ishara ya msalaba kwa sababu wao ni Wakomunisti.
Isitoshe, makasisi hao wajanja walitumia pia mamlaka yao kuwachochea maafisa wa serikali wawapinge watu wa Mungu, kama waandishi na Mafarisayo walivyofanya katika siku za Yesu.—Yoh. 18:28-30; 19:4-6, 12-16.
Kuanzia mwaka wa 1918 hadi 1940, Moldova ilitawaliwa na Rumania, ambayo ilikuwa ufalme wakati huo. Serikali ya Rumania ilimweka waziri wa madhehebu, ambaye aliamua mambo ya dini. Kwa sababu waziri huyo aliwaogopa viongozi wa Kanisa la Othodoksi, alipinga kazi ya Wanafunzi wa Biblia na kujaribu kuwapiga marufuku pamoja na vitabu vyao vya Biblia. Kwa hiyo, aliwashtaki ndugu kwamba walikuwa wakishirikiana na Wakomunisti.
Kwa sababu viongozi wa serikali waliwachukia watu wa Yehova, afisa mmoja wa jeshi la Moldova alimtumia polisi fulani mkuu agizo la serikali lililoidhinishwa Aprili 25, 1925. Agizo hilo lilisema hivi: “Kupatana na Kifungu cha Polisi wa Usalama Na. 17274/925, tuna pendeleo la kukuarifu kwamba Wizara ya Mambo ya Ndani imeamua kupiga marufuku na kukomesha mahubiri ya ‘Wanafunzi wa Biblia,’ na tunataka uchukue hatua zinazohitajika ili kutimiza lengo hilo.”
Ripoti ambayo ofisi ya Rumania ilituma kwenye makao makuu Oktoba 17, 1927, inaonyesha jinsi upinzani huo wa serikali ulivyowaathiri akina ndugu. Kwa ufupi, ripoti hiyo ilisema kwamba mikutano ya makutaniko ilikuwa imesimamishwa na kukatazwa kila mahali, na ‘mamia ya ndugu walikuwa wamefikishwa mbele ya mahakama za jeshi na za umma.’ Pia ilisema hivi: ‘Ni mikutano michache tu iliyoweza kufanywa katika majira ya kiangazi, kwa kuwa wapelelezi na polisi wa siri walipeleleza makutaniko, na bado wanayapeleleza, hasa makutaniko ya vijijini ambayo ni mengi. Mikutano mingi hufanywa misituni, mahali palipofichika vizuri.’
Ripoti hiyo ilisema hivi pia: ‘Kazi ya waangalizi wanaosafiri ilikatizwa mwezi wa Machi. Katika mwezi uo huo, waziri wa mambo ya ndani alitoa amri kali kisiri kwamba wahudumu wa wakati wote wakamatwe na wafungwe. Punde si punde, karibu wahudumu wote wa wakati wote walikuwa wamefungwa. Ijapokuwa hatuogopi wala ndugu hawaogopi, kwa kuwa tumepata upinzani tangu kazi ilipoanzishwa katika nchi hii, wakati huu mbinu zao za kukomesha kazi ya kuhubiri ni zenye mafanikio sana hivi kwamba ni vigumu kuhubiri.’
Mwishoni mwa miaka ya 1920, mtu mmoja-mmoja na familia nzima-nzima jasiri waliendelea kujitenga na Kanisa la Othodoksi na kuchukua msimamo imara upande wa kweli ya Biblia. Jambo hilo linaonyeshwa katika barua ambayo kasisi wa kijiji cha Şirăuţi alimwandikia msimamizi wake mwaka wa 1928. Barua hiyo ilikuwa na majina ya watu na watoto 43 wa kijiji hicho. Ilisema hivi: “Tunafurahi kuambatanisha orodha ya majina ya waumini wa madhehebu ya ‘Wanafunzi wa Biblia.’ Licha ya jitihada zao, hawajafanikiwa wala hawana kanisa, bali wao hukutana katika nyumba za watu.”
Bila shaka dai la kasisi huyo kwamba Wanafunzi wa Biblia “hawajafanikiwa” lilikuwa la uwongo, kwa kuwa watu wengi waliotajwa katika orodha yake walikuwa waumini 43 wa Kanisa la Othodoksi hapo awali. Agripina Barbuţă, mtoto mmoja aliyetajwa katika orodha hiyo, ana umri wa zaidi ya miaka 80 sasa na bado anamtumikia Yehova.
Waliposhindwa kuhubiri nyumba kwa nyumba, ndugu waliwahubiria watu kila walipopata nafasi, hasa watu wa ukoo. Zamani, watu wa ukoo walipenda kutembeleana. Ndugu walitumia nafasi hizo kuwahubiria habari njema. Bila shaka serikali haingeweza kutunga sheria ili kuwakataza watu wa ukoo wasitembeleane.
Jitihada za Kuhalalisha Kazi ya Kuhubiri
Baada ya kazi ya kuhubiri kupigwa marufuku mwaka wa 1925, ndugu kwenye ofisi ya Cluj-Napoca, Rumania, walituma ripoti yenye kurasa 50 kwa waziri wa madhehebu. Ripoti hiyo ilikuwa na maelezo mafupi kuhusu imani na mafundisho yetu, na pia ilitia ndani ombi rasmi la kuondoa marufuku. Hivyo, mnamo Septemba 1927, ndugu mmoja aliruhusiwa kumwona waziri huyo mara tatu. Baada ya kumwona waziri kwa mara ya tatu alitumaini kwamba sheria ingebadilishwa na Mashahidi wangepata uhuru wa ibada. Kwa kusikitisha, serikali ilipuuza maombi ya ndugu huyo. Hali ilizidi kuwa mbaya kwa watu wa Yehova kwa kuwa maafisa waliendelea kutunga matatizo kwa njia ya amri. (Zab. 94:20; Dan. 6:5-9) Hati rasmi iliyotolewa Mei 29, 1932, ilisema kwamba “utendaji wote” wa Wanafunzi wa Biblia “umepigwa marufuku kabisa.”
Hata hivyo, shambulizi hilo juu ya watu wa Mungu halikuungwa mkono katika sehemu zote za Rumania na Moldova. Kwa kadiri fulani, watu wenye mamlaka na maafisa wa maeneo mbalimbali walifanya maamuzi yao wenyewe kuwahusu Wanafunzi wa Biblia. Kwa hiyo, ndugu waliwaendea maafisa hao ili kutetea na kuthibitisha kisheria habari njema katika maeneo yao.—Flp. 1:7.
Jitihada hizo zilifaulu katika sehemu mbalimbali, kama vile jijini Bucharest, Rumania, baada ya ofisi ya tawi kuhamishwa huko kutoka Cluj-Napoca. Baada ya ofisi ya tawi kupambana kwa muda mrefu, shirika la Bible and Tract Society of Jehovah’s Witnesses huko Bucharest liliandikishwa kisheria mwaka wa 1933.
Jambo la kupendeza ni kwamba hata baadhi ya mahakimu maarufu walionyesha wazi kwamba hawakukubali vizuizi ambavyo watu wa Mungu waliwekewa. Kwa mfano, Mei 8, 1935, Mahakama ya Rufani huko Cluj-Napoca iliamua kwa ujasiri kwamba marufuku juu ya kazi ya Mashahidi wa Yehova haipatani na katiba. Uamuzi huo ulisema hivi pia: “Vijitabu [vya Mashahidi wa Yehova] vilivyochukuliwa vinatufundisha tupendane na kumwamini Mungu na Kristo. Kwa hiyo, ni makosa kusema kwamba vijitabu hivyo ni vya uasi; vijitabu hivyo si tisho kwa Serikali.”
Uamuzi wa Busara Wapuuzwa
Hata hivyo, wenye mamlaka waliendelea kupinga kazi ya watu wa Mungu. Kwa mfano, Machi 28, 1934, mkuu wa Idara ya Usalama wa mji wa Soroca, Moldova, alimwandikia mkubwa wake, mkaguzi wa polisi wa eneo la Chisinau, akilalamika kwamba mnamo mwaka wa 1927, katika kijiji fulani karibu na Soroca, kulikuwa na “familia mbili tu za waumini wa madhehebu hayo, lakini wamegeuza . . . familia 33 nyingine.” Aliandika pia kwamba Mashahidi “hulikataa kanisa” na “mapokeo na desturi zake za kidini” na kwamba “badala ya kumwomba kasisi afanye ibada, wanafanya ibada yao wenyewe.” Alimaliza barua yake kwa kusema hivi: “[Mashahidi] wanaendelea kuwageuza watu imani, na jambo hilo linahatarisha utaratibu na usalama wa Serikali.”
Mei 6, 1937, ndugu katika wilaya iyo hiyo walimwandikia hakimu mkuu na kumwomba aifute dini ya Mashahidi wa Yehova kutoka katika orodha ya madhehebu yasiyo halali. Jibu rasmi kutoka kwa wenye mamlaka lilionyeshwa katika barua ambayo meya wa wilaya ya Soroca alimwandikia hakimu mkuu wa wilaya hiyo. Barua hiyo iliyoandikwa Juni 15, 1937, ilisema hivi: “Utendaji wa [Mashahidi wa Yehova] umepigwa marufuku na . . . Wizara ya Madhehebu na Sanaa. Kwa hiyo, hatuwezi kukubali ombi lao la kufuta dini ya Mashahidi wa Yehova kutoka katika orodha ya madhehebu yasiyo [halali], kwa kuwa wao wanaendeleza dini hiyo.”
Jarida rasmi la serikali la Monitorul Oficial, la Julai 12, 1939, lilionyesha uhasama huo kwa kusema kwamba Mashahidi wa Yehova na mashirika yote wanayotumia “yamepigwa marufuku kabisa.” Kama ilivyotajwa mapema, Moldova ilitawaliwa na ufalme wa Rumania wakati huo, na dini kuu katika nchi hiyo ilikuwa Kanisa la Othodoksi ya Mashariki. Kwa kusikitisha, maafisa wengi wenye ubaguzi wa dini walikiuka sheria kwa kuwatendea watu wa Yehova kwa ukatili zaidi kuliko sheria ilivyoamuru.
Maafisa Watenda Kinyama
Mambo yaliyowapata Dumitru Gorobeţ na Cazimir Cislinschii yanaonyesha kwamba mara nyingi upinzani dhidi ya kazi ya kuhubiri ulichochewa na maafisa waliowachukia Mashahidi na waliokuwa waumini washupavu wa Kanisa la Othodoksi. Dumitru na Cazimir walijifunza kweli ya Biblia katika kijiji cha Tabani. Muda si muda, walijulikana sana na kupendwa na ndugu kwa sababu ya sifa zao nzuri na bidii yao katika utumishi. Mwaka wa 1936, walikamatwa na kupelekwa kwenye kituo cha polisi katika mji wa Khotin (sasa mji huo uko Ukrainia).
Kwanza, polisi waliwapiga Dumitru na Cazimir kikatili. Kisha wakajaribu kuwalazimisha wafanye ishara ya msalaba. Lakini walisimama imara licha ya kupigwa tena na tena. Hatimaye, polisi walisalimu amri. Hata waliwaruhusu Dumitru na Cazimir kurudi nyumbani. Lakini ndugu hao waaminifu walivumilia magumu mengi zaidi chini ya utawala wa Wafashisti na Wakomunisti kwa ajili ya habari njema. Dumitru alikufa mapema mwaka wa 1976 huko Tomsk, Urusi, na Cazimir alikufa Novemba 1990 huko Moldova.
Ofisi ya tawi ya Rumania ilisimamia kazi nchini Moldova katika miaka ya 1930. Martin Magyarosi aliyebatizwa mwaka wa 1922, alikuwa msimamizi wa ofisi ya tawi wakati huo. Kwa kuwa waliwahangaikia akina ndugu, hasa kwa sababu ya majaribu waliyokuwa wakikabili, yeye na mwana-mkwe wake, Pamfil Albu, walitembelea makutaniko mengi kaskazini mwa Moldova ili kuwaimarisha na kuwatia watu wa Mungu moyo. Ziara hizo zilikuja kwa wakati unaofaa kabisa! Kwa nini? Kwa sababu baada ya muda mfupi, Vita vya Pili vya Ulimwengu vingeanza Ulaya. Na Moldova iliyoonwa kuwa nchi yenye kutamanika sana, ingevamiwa na kutawaliwa na nchi jirani zenye nguvu, moja baada ya nyingine.
Vita vya Pili vya Ulimwengu Vyaharibu Bara la Ulaya
Muungano wa Sovieti na serikali ya Nazi ya Ujerumani zilitia sahihi mkataba wa amani Agosti 23, 1939. Juma moja baadaye, Septemba 1, 1939, Ujerumani ilivamia Poland na Vita vya Pili vya Ulimwengu vikaanza. Kisha, Juni 26, 1940, Vyacheslav Molotov aliyekuwa Waziri wa Nchi za Kigeni wa Sovieti, aliamuru serikali ya Rumania iisalimishe bila masharti yoyote nchi iliyoitwa Bessarabia kwa Wasovieti. Rumania ilikubali, na majeshi ya Sovieti yaliingia Moldova Juni 28, 1940. Mnamo Agosti 1940, Wasovieti waliliita eneo hilo SSR ya Moldavia, na Chisinau likawa jiji kuu la jamhuri hiyo.
Hata hivyo, Wasovieti hawakuitawala Moldova kwa muda mrefu. Ujerumani ilivunja mkataba wa amani wa mwaka wa 1939 na kuvamia Urusi Juni 22, 1941. Jambo hilo liliipa Rumania nafasi ya kutwaa SSR ya Moldavia kutoka kwa Wasovieti, na kwa kusudi hilo ilijiunga na Ujerumani.
Mbinu hiyo ilifaulu kwa kuwa kufikia Julai 26, 1941, jeshi la Rumania lilikuwa limewafukuza Warusi hadi Mto Dniester. Kwa hiyo, yapata mwaka mmoja baada ya kuvamiwa na Wasovieti, Moldova ilitawaliwa tena na Rumania. Lakini kuanzia Septemba 1940, Rumania ilikuwa na serikali ya kimabavu ya Ufashisti yenye uzalendo mkali iliyoongozwa na Jenerali Ion Antonescu. Serikali yake haikuvumilia watu wasiounga mkono siasa kwa sababu ya uaminifu wao kwa Ufalme wa Mungu.
Majaribu Makali Chini ya Utawala wa Wafashisti
Punde si punde, serikali ya Kifashisti ya Antonescu, iliyoshirikiana na Hitler na muungano wa Ujerumani, Italia, na Japani, ilijaribu kuvunja uaminifu wa Mashahidi wa Yehova kwa kutumia nguvu. Fikiria kisa cha Anton Pântea aliyezaliwa mwaka wa 1919. Anton alijifunza kweli alipokuwa kijana na alikuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Alikuwa karibu kupigwa mara kadhaa, lakini aliepuka jambo hilo kwa muda kwa kutetea kijasiri haki ya kusema juu ya imani yake akiwa raia wa Rumania. Hata hivyo, hatimaye polisi walimkamata. Maafisa Wafashisti walimburuta hadi kwenye kituo cha polisi, wakampiga usiku kucha, kisha, wakamwachilia. Ndugu Pântea ana umri wa miaka 84 sasa na bado ameazimia kumtumikia Yehova kwa uaminifu.
Mtu mwingine mwaminifu ni Parfin Palamarciuc aliyejifunza kweli ya Biblia huko Moldova katika miaka ya 1920. Yeye pia alikuwa mtangazaji mwenye bidii wa habari njema. Mara nyingi, alihubiri katika miji na vijiji kuanzia Chernovtsy hadi Lvov huko Ukrainia bila kurudi nyumbani kwa majuma kadhaa. Kwa sababu Parfin alikataa kujiunga na jeshi, Wafashisti walimkamata mwaka wa 1942 na kumfikisha mbele ya mahakama ya jeshi huko Chernovtsy.
Nicolae, mwana wa Parfin, alisema hivi juu ya matukio hayo: “Ndugu 100 walihukumiwa kifo katika mahakama hiyo. Walikuwa wauawe mara moja baada ya kuhukumiwa. Maafisa waliwakusanya ndugu hao na kuwachagua ndugu kumi ambao wangepigwa risasi kwanza. Lakini hao kumi walilazimishwa kuchimba kwanza makaburi yao, huku wale wengine 90 wakitazama. Lakini kabla ya kuwapiga risasi, maafisa waliwapa nafasi nyingine kukana imani yao na kujiunga na jeshi. Wawili walikana imani; wanane wakapigwa risasi. Kisha wengine kumi wakapangwa katika mstari. Lakini kabla ya kupigwa risasi walilazimishwa kuwazika waliouawa.
“Ndugu walipokuwa wakifukia makaburi, afisa mmoja wa cheo cha juu aliwasili. Aliuliza ni Mashahidi wangapi waliokana imani. Alipoambiwa ni wawili tu, alisema kwamba kama watu 80 wangehitaji kufa ili 20 wajiunge na jeshi, basi ni afadhali wale 92 waliobaki wapelekwe kufanya kazi katika kambi. Kwa hiyo, hukumu ya kifo ilibadilishwa kuwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu. Hata hivyo, yapata miaka mitatu baadaye, jeshi la Sovieti liliwaweka Mashahidi huru kutoka katika kambi za Rumania. Baba yangu aliokoka magumu hayo na mengine mengi. Alikuwa mwaminifu kwa Yehova hadi kifo chake mwaka wa 1984.”
Je, Ni Kosa Kukataa Desturi za Kanisa la Othodoksi?
Vasile Gherman alikuwa kijana, na mke wake alikuwa amejifungua mtoto wa kike wakati Wafashisti walipomkamata Vasile mnamo Desemba 1942. Vasile alishtakiwa kwa “makosa” mawili, kukataa kujiunga na jeshi na pia kukataa binti yake abatizwe katika Kanisa la Othodoksi. Anasema hivi kuhusu kesi hiyo: “Kesi yangu na kesi za ndugu wengine waaminifu 69 zilisikilizwa katika mahakama ya jeshi huko Chernovtsy Februari 1943. Kabla ya kuhukumiwa, wenye mamlaka walitulazimisha kutazama wahalifu sita wakiuawa. Kwa hiyo, tulikuwa na hakika kwamba tungehukumiwa kifo.
“Tulizungumzia jambo hilo na kuazimia kusimama imara katika imani na kujitahidi sana kudumisha shangwe hadi kesi imalizike. Kwa msaada wa Yehova tulifaulu. Kama tulivyotarajia, sisi sote 70 tulihukumiwa kifo, tulihisi kwamba tulikuwa tukiteswa kwa ajili ya uadilifu. Hakuna hata mmoja kati yetu aliyevunjika moyo, na jambo hilo liliwaudhi sana adui zetu. Lakini jambo la kushangaza ni kwamba badala ya kutupiga risasi, wenye mamlaka walibadili hukumu yetu kuwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu huko Aiud, Rumania. Lakini baada ya miezi 18 tu, mnamo Agosti 1944, jeshi la Wasovieti liliwaweka huru wafungwa waliokuwa katika kambi hiyo.”
Mwaka wa 1942, Wafashisti waliwaandikisha watu 800 hivi kutoka kijiji cha Şirăuţi, Moldova, katika jeshi la Jenerali Antonescu. Kati yao kulikuwa na Mashahidi kadhaa kutia ndani Nicolae Anischevici. Nicolae anasema hivi: “Walipokuwa wakituandikisha, polisi walituamuru tushiriki katika sherehe fulani ya kidini. Sisi Mashahidi tulikataa. Tulikataa pia kubeba silaha. Kwa hiyo, polisi walitushutumu kuwa Wakomunisti na wakatukamata. Hata hivyo kabla ya kutufunga, walituruhusu kueleza sababu ya kutojiunga na jeshi.
“Kesho yake tulihamishwa hadi Briceni, kitovu cha mahakama ya wilaya hiyo. Tulivuliwa mavazi yote na miili yetu ikachunguzwa kabisa. Kisha kasisi mwenye cheo cha juu jeshini akatuhoji. Alikuwa mwenye fadhili, alielewa kwamba uamuzi wetu ulitegemea dhamiri, na alipanga tupewe chakula. Na zaidi ya hayo, aliandika kwamba tulikataa kujiunga na jeshi kwa sababu tunamwamini Yesu.
“Kutoka Briceni tulipelekwa hadi kwenye kituo cha polisi huko Lipcani. Huko, polisi walitupiga kikatili hadi usiku. Kisha wakatufunga katika chumba fulani pamoja na ndugu wengine wawili na mwanamke mmoja. Baadaye tuligundua kwamba mwanamke huyo alikuwa mpelelezi. Tulipigwa kila siku, kwa siku kadhaa. Hatimaye, mimi nilipelekwa Chernovtsy ili nihukumiwe katika mahakama ya jeshi. Nilipewa wakili ambaye alinisaidia sana nikiwa huko. Hata hivyo, afya yangu ilikuwa imezorota sana kwa sababu ya mateso hivi kwamba wakuu wa jeshi walifikiri ningekufa. Mwishowe waliamua kunipeleka nyumbani bila kunihukumu.”
Dada Jasiri Wadumisha Uaminifu
Dada pia walikabili mateso kwa sababu ya hasira ya Wafashisti. Mmojawapo ni Maria Gherman (yeye si mtu wa ukoo wa Vasile Gherman lakini walikuwa katika kutaniko moja). Maria alipokamatwa mwaka wa 1943, alipelekwa kwenye kituo cha polisi huko Balasineşti. Anasema hivi: “Polisi walinikamata kwa sababu nilikataa kwenda katika kanisa la Othodoksi. Kwanza walinihamisha hadi Lipcani, Moldova, kisha nikapelekwa Chernovtsy, Ukrainia, ambako nilihukumiwa.
“Hakimu aliniuliza kwa nini nilikataa kwenda kanisani. Nilimwambia kwamba ninamwabudu Yehova tu. Mimi na dada wengine 20 tulihukumiwa kifungo cha miaka 20 kwa sababu ya ‘kosa’ hilo. Baadhi yetu tuliingizwa kwenye chumba kidogo sana pamoja na wafungwa wengine 30. Hata hivyo, mchana nilifanya kazi katika nyumba za matajiri. Watu hao walinitendea vizuri kuliko maafisa wa gereza, angalau walinipa chakula cha kutosha!
“Baada ya muda, tulifaulu kuwasiliana na ndugu waliokuwa katika sehemu nyingine ya gereza. Jambo hilo lilileta faida nyingi kwa kuwa tuliweza kuwasaidia ndugu kupata chakula cha kiroho na cha kimwili pia.”
Mara tu baada ya mateso ya Wafashisti kukoma, ndugu hao waaminifu pamoja na Mashahidi wengine wengi huko Moldova, walikabili shambulizi lingine la imani yao chini ya serikali ya Kikomunisti ya Urusi iliyotawala eneo hilo baada ya Wafashisti.
Mbinu ya Wasovieti ya Kuwahamisha Watu
Ujerumani ilipoelekea kushindwa vitani, baadhi ya maafisa wa serikali ya Rumania iliyoongozwa na Mfalme Michael, walipindua serikali ya Antonescu mwaka wa 1944. Kisha Rumania ilivunja uhusiano wake na muungano wa Ujerumani, Italia, na Japani na ikajiunga na Urusi. Mwaka uo huo, jeshi la Sovieti lilitwaa tena eneo hilo, kwa hiyo, Moldova ikawa tena sehemu ya Muungano wa Sovieti, na kuitwa SSR ya Moldavia.
Mwanzoni, watawala Wakomunisti wa Moldova hawakuwanyanyasa Mashahidi wa Yehova. Lakini amani hiyo haikudumu kwa muda mrefu. Punde msimamo wa Kikristo wa kutounga mkono mambo ya siasa ulipingwa vikali tena, kutia ndani msimamo wa Mashahidi wa kukataa kupiga kura katika uchaguzi wa chama. Chini ya utawala wa Sovieti, kutounga mkono siasa hakukubaliwa hata kidogo. Kwa hiyo, serikali ilinuia kutatua tatizo hilo kwa kuwahamisha Mashahidi wa Yehova na watu wengine “wasiotakiwa” kuanzia mwaka wa 1949.
“Uamuzi uliofanywa na Baraza Kuu la Chama cha Wakomunisti” kuwahusu watu kutoka SSR ya Moldavia ambao wangehamishwa ulionyeshwa katika hati fulani rasmi. Baadhi ya watu hao walikuwa “wamiliki wa mashamba, wenye biashara kubwa, watu walioshirikiana na wavamizi Wajerumani, wale waliowasaidia polisi wa Ujerumani na Rumania, wanachama wa vyama na mashirika ya Wafashisti, shirika fulani la Wafinland lisilokuwa la Kisoshalisti, waumini wa madhehebu yasiyo halali, na pia familia za watu hao wote.” Wote hao walipaswa kupelekwa magharibi mwa Siberia hadi “wakati usiojulikana.”
Uhamisho mwingine ulianza mwaka wa 1951, lakini wakati huo ni Mashahidi wa Yehova pekee waliohamishwa. Stalin mwenyewe aliagiza uhamisho huo ulioitwa Operation North. Zaidi ya familia 720 za Mashahidi, yaani, watu 2,600 hivi, walihamishwa kutoka Moldova hadi Tomsk, magharibi mwa Siberia, umbali wa kilometa 4,500 kutoka Moldova.
Maagizo ya serikali yalisema kwamba watu walipaswa kupewa nafasi ya kutosha kufunga virago vyao kabla ya kupelekwa kwenye magari-moshi. Na zaidi ya hayo, mabehewa yalikuwa “yatengenezwe vizuri ili yafae kuwasafirisha wanadamu.” Lakini maagizo hayo hayakutiwa maanani.
Kwa kawaida, wanajeshi na maafisa wanane hivi walifika nyumbani kwa Mashahidi usiku wa manane. Waliwaamsha na kuwaonyesha barua ya uhamisho. Waliwapa saa chache tu kufunga virago vyao kabla ya kuwapeleka kwenye magari-moshi.
Walisafirishwa kwa mabehewa ya mizigo. Watu 40 hivi walisongamana katika kila behewa kwa majuma mawili ya safari. Hakukuwa na viti na baridi iliingia kwenye mabehewa. Katika pembe moja ya behewa kulikuwa na shimo sakafuni ambalo lilitumiwa kama choo. Kabla ya kuwahamisha ndugu, maafisa walipaswa kuandika orodha ya mali za kila mtu. Hata hivyo, mara nyingi waliorodhesha tu vitu duni; vitu vyenye thamani “vilipotea” tu.
Hata hivyo, licha ya magumu yaliyowapata, ndugu hawakupoteza furaha yao ya Kikristo. Magari-moshi yaliyowasafirisha Mashahidi yalipofika kwenye vituo vya gari-moshi, sauti za nyimbo za Ufalme zilisikika kutoka ndani ya mabehewa. Hivyo, ndugu katika kila gari-moshi walijua kwamba hawakuwa peke yao, bali walikuwa wakihamishwa pamoja na mamia ya Mashahidi wenzao. Kuwaona wengine wakidumisha furaha katika hali hizo ngumu kuliwatia moyo na kuwaimarisha wote wadumishe uaminifu wao kwa Yehova katika hali yoyote ile.—Yak. 1:2.
Imani Inayostahili Kuigwa
Ivan Mikitkov ni mmojawapo wa watu wa Moldova waliopelekwa uhamishoni Siberia. Ivan alikamatwa kwa mara ya kwanza huko Moldova pamoja na Mashahidi wengine mwaka wa 1951, na kupelekwa uhamishoni Tomsk. Alipewa kazi ya kukata miti katika msitu mkubwa wa Siberia unaoitwa taiga. Ingawa hakuishi katika kambi ya kazi ngumu, bado alikuwa chini ya vizuizi, na polisi wa siri walipeleleza utendaji wake wote. Hata hivyo, yeye na ndugu zake wa kiroho waliwahubiria wengine kila walipopata nafasi.
Ivan anasema hivi: “Tulipanga kuwe na makutaniko katika mazingira hayo magumu. Hata tulianza kunakili vitabu. Muda si muda, watu kadhaa ambao tuliwahubiria walikubali kweli na kubatizwa. Lakini, hatimaye wenye mamlaka walitambua utendaji wetu na wakapeleka baadhi yetu kwenye kambi za kazi ngumu.
“Mimi na Mashahidi wenzangu Pavel Dandara, Mina Goraş, na Vasile Şarban, tulihukumiwa kifungo cha miaka 12 katika kambi ya kazi ngumu chini ya usimamizi mkali. Wenye mamlaka walifikiri kwamba vifungo hivyo vikali vingewatisha wengine wasihubiri, lakini mbinu hiyo haikufua dafu. Ndugu zetu waliendelea kuhubiri kotekote walikopelekwa. Niliachiliwa mwaka wa 1966, baada ya kukamilisha kifungo changu. Nilirudi Tomsk na kukaa huko kwa miaka mitatu.
“Mwaka wa 1969, nilihamia Bonde la Donets ambako nilikutana na Maria, dada mwaminifu na mwenye bidii ambaye nilimwoa. Nilikamatwa tena mwaka wa 1983. Wakati huo nilihukumiwa adhabu maradufu, kifungo cha gereza cha miaka mitano, na uhamisho wa miaka mitano. Bila shaka nilihisi kwamba hukumu hiyo ilikuwa ngumu zaidi kuliko ile ya kwanza kwa sababu wakati huu ningetengana na mke na mtoto wangu ambao pia wangepatwa na magumu. Ninashukuru kwamba niliachiliwa mwaka wa 1987, baada ya Mikhail Gorbachev kuwekwa kuwa katibu mkuu wa Chama cha Kikomunisti cha Sovieti. Niliruhusiwa kurudi Ukrainia na hatimaye Moldova.
“Niliporudi Bălţi, jiji la pili kwa ukubwa nchini Moldova, jiji hilo lilikuwa na wahubiri 370 na makutaniko matatu. Leo jiji hilo lina zaidi ya wahubiri 1,700 na makutaniko 16!”
“Je, Unataka Kufa Kama Vasile?”
Wasimamizi wa kambi na wapelelezi wa KGB (Halmashauri ya Usalama wa Kitaifa ya Sovieti) walitunga mbinu za kinyama ili kuvunja uaminifu wa ndugu. Constantin Ivanovici Şobe anasimulia kile kilichompata babu yake Constantin Şobe: “Mwaka wa 1952, Babu alikuwa amefungwa katika kambi moja ya kazi ngumu katika wilaya ya Chita, mashariki ya Ziwa Baikal huko Siberia. Maafisa wa kambi walitisha kumpiga risasi yeye na Mashahidi wengine wasipokana imani yao.
“Kwa sababu ndugu hao walikataa kukana imani yao, maafisa waliwakusanya nje ya kambi karibu na msitu. Giza lilikuwa likiingia walipompeleka Vasile, rafiki wa karibu zaidi wa Babu, msituni na kutangaza kwamba watampiga risasi. Ndugu walingoja wakiwa na wasiwasi. Punde walisikia bunduki zikifyatuliwa.
“Askari walirudi na kumpeleka Shahidi wa pili, babu yangu, msituni. Baada tu ya kuingia msituni, walifika kwenye uwanja fulani wenye makaburi kadhaa yaliyokuwa yamechimbwa, na moja lilikuwa limefukiwa. Afisa mkuu alisema hivi akimwangalia Babu na kuelekeza kidole kwenye kaburi lililofukiwa: ‘Je, unataka kufa kama Vasile, au unataka kurudi nyumbani kwa familia yako ukiwa mtu huru? Una dakika mbili kufanya uamuzi.’ Babu hakuhitaji dakika mbili. Mara moja alijibu: ‘Vasile, mliyempiga risasi, alikuwa rafiki yangu kwa miaka mingi. Sasa ninatarajia kumwona tena atakapofufuliwa katika ulimwengu mpya. Nina hakika kwamba nitakuwa katika ulimwengu mpya pamoja na Vasile. Lakini, vipi wewe?’
“Afisa huyo hakutarajia jibu hilo. Alimrudisha babu na wale wengine kambini. Hata hivyo, babu hakuhitaji kungoja hadi ufufuo ili kumwona Vasile tena. Hiyo ilikuwa mbinu mbovu iliyokusudiwa kuvunja uaminifu wa ndugu.”
Mbinu ya Wakomunisti ya Kueneza Uwongo Haikufaulu
Wakomunisti walichapisha vitabu na vijitabu, na kutengeneza sinema zilizoeneza uwongo juu ya watu wa Mungu ili kuwachochea watu wawachukie na kuwashuku Mashahidi wa Yehova. Kijitabu kimoja kilikuwa na kichwa Double Bottom. Kijitabu hicho kilipewa jina hilo kwa sababu ndugu walikuwa wakitengeneza sehemu ya siri ya kufichia vitabu katika masanduku ya nguo na mikoba yao. Nicolai Voloşanovschi anakumbuka jinsi kamanda wa kambi alivyojaribu kutumia kijitabu hicho kumfedhehesha mbele ya wafungwa wengine.
Nicolai anasema hivi: “Kamanda huyo alikusanya wafungwa wote katika jengo moja kambini. Kisha akasoma sehemu mbalimbali katika kijitabu hicho, kutia ndani sehemu zilizokuwa na maelezo ya uwongo kunihusu. Alipomaliza, nilimwomba ruhusa kuuliza maswali machache. Bila shaka kamanda huyo alikubali ombi langu akidhani kwamba angepata nafasi ya kunifanyia mzaha.
“Nilimwuliza kamanda huyo ikiwa anakumbuka aliponihoji mara ya kwanza nilipokuja kambini. Alisema anakumbuka mahojiano hayo. Kisha nikamwuliza kama anakumbuka maswali ambayo aliniuliza kuhusu nchi niliyozaliwa, uraia wangu, na kadhalika alipokuwa akijaza fomu za kuniandikisha kambini. Tena alijibu ndiyo. Hata aliwaambia wale waliokuwa wakisikiliza majibu niliyotoa wakati huo. Kisha nikamwomba aeleze yale aliyoandika katika fomu hizo. Alikiri kwamba yale aliyoandika hayakupatana na majibu yangu. Niliwatazama wasikilizaji na kusema: ‘Mwaona, kijitabu hiki kiliandikwa kwa njia iyo hiyo.’ Wafungwa walipiga makofi, na kamanda akatoka kwa hasira.”
Njama ya Kusababisha Migawanyiko ili Kushinda
Katika miaka ya 1960, viongozi wa Sovieti walioudhika walitunga mbinu mpya za kuharibu umoja wa Mashahidi wa Yehova. Kitabu Upanga na Ngao (The Sword and the Shield), kilichochapishwa mwaka wa 1999, kinazungumzia baadhi ya ripoti za KGB, ambazo zilikuwa za siri wakati huo, zilizopatikana katika hifadhi za nyaraka za serikali. Ripoti hiyo inasema: “Maafisa wakuu wa KGB ambao waliongoza ‘pambano dhidi ya Mashahidi wa Yehova’ walifanya mkutano mnamo Machi 1959, na kuamua kwamba mbinu bora ingekuwa ‘kuendelea kuwakandamiza [Mashahidi wa Yehova] kwa kusababisha migawanyiko.’ Maafisa wa KGB waliazimia kusababisha migawanyiko miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, kuwavunja moyo, kuwavunjia heshima, na vilevile kuwafunga viongozi wao wakuu kwa mashtaka ya uwongo.”
Mbinu za “kusababisha migawanyiko” zilihusisha jitihada za pamoja za kuwafanya ndugu wawashuku ndugu wenzao kotekote katika Muungano wa Sovieti. Ili kutimiza lengo hilo, KGB ilieneza uvumi kwamba ndugu kadhaa walioongoza walikuwa wameanza kushirikiana na KGB. Wapelelezi wa KGB walieneza uvumi huo kwa ujanja sana hivi kwamba Mashahidi wengi walianza kuwashuku ndugu wenzao.
Mbinu nyingine ya KGB ilikuwa kuwazoeza wapelelezi kujifanya kuwa Mashahidi wa Yehova “wanaohubiri kwa ukawaida,” kisha wangejaribu kustahili kupata madaraka katika tengenezo. Bila shaka, wapelelezi hao walikuwa wakiwasiliana na KGB. Wapelelezi wa KGB pia waliwaendea kisiri Mashahidi wa kweli na kujaribu kuwahonga kwa kiasi kikubwa cha pesa ili waunge KGB mkono.
Jambo la kusikitisha ni kwamba mbinu hizo zilifaulu kwa kadiri fulani kuharibu umoja wa ndugu, kutia ndani ndugu wa Moldova. Hivyo, polepole ndugu walianza kuwashuku ndugu wenzao. Baadhi ya ndugu walijitenga na tengenezo na kuanzisha kikundi ambacho kilijulikana kama upinzani.
Kabla ya matukio hayo, ndugu katika Muungano wa Sovieti walitumia neno “njia,” walipokuwa wakirejezea tengenezo la Yehova, chakula cha kiroho, na ndugu walioongoza. Sasa ndugu walichanganyikiwa na kutilia shaka njia hiyo. Walitatuaje vurugu hiyo? Kwa kushangaza, Serikali ya Sovieti iliwasaidia. Ndiyo, wale waliotunga njama hiyo walisaidia kutatua matatizo waliyosababisha. Vipi?
Walipuuza Roho ya Mungu
Mapema katika miaka ya 1960, wenye mamlaka wa Sovieti waliwafunga “viongozi” wengi wa Mashahidi kutoka sehemu zote za Muungano wa Sovieti katika kambi moja iliyokuwa umbali wa kilometa 150 kutoka jiji la Saransk katika jamhuri ya Mordvinia, magharibi mwa Urusi. Kabla ya hapo, ndugu hawakuweza kuwasiliana vizuri kwa sababu walikaa mbali sana na wenzao, hivyo kutoelewana kulitokea kwa urahisi. Lakini sasa wale wafuasi wa kikundi cha upinzani, na wale wasiojiunga na kikundi hicho, walikuwa pamoja. Kwa hiyo, waliweza kuongea ana kwa ana na kutofautisha kweli na uwongo. Kwa nini wenye mamlaka waliwaweka ndugu hao wote pamoja? Inaonekana walifikiri kwamba ndugu wangezozana, na hivyo kuzidisha migawanyiko iliyokuwapo. Hata hivyo, mbinu hiyo iliyopangwa kwa werevu, haikufua dafu kwa sababu walioitunga walipuuza roho ya Yehova inayoleta umoja.—1 Kor. 14:33.
Ndugu mmoja aliyepelekwa Mordvinia ni Gheorghe Gorobeţ. Anasema hivi: “Muda mfupi baada ya kukamatwa na kupelekwa gerezani, ndugu mmoja aliyekuwa mfuasi wa kikundi cha upinzani alifungwa pamoja nami. Alipoona kwamba ndugu walioongoza bado walikuwa wamefungwa, alishangaa, kwa kuwa alikuwa ameambiwa kwamba sisi sote tuliachiliwa huru na tulikuwa tukiishi raha mustarehe na kupewa pesa na KGB!”
Ndugu Gorobeţ anaongeza hivi: “Katika mwaka wangu wa kwanza gerezani, zaidi ya watu 700 walifungwa kwa sababu za kidini. Wengi wao walikuwa Mashahidi wa Yehova. Sote tulifanya kazi katika kiwanda kimoja na tulikuwa na nafasi ya kuongea na wale waliokuwa wamejiunga na kikundi cha upinzani. Hivyo, mambo mengi yaliyosababisha migawanyiko yalitambuliwa katika mwaka wa 1960 na 1961. Hatimaye, mwaka wa 1962, ndugu wa halmashauri ya nchi waliosimamia kazi katika Muungano wa Sovieti waliandika barua wakiwa katika kambi ya kazi ngumu. Barua hiyo ilitumiwa makutaniko yote katika Muungano wa Sovieti na matatizo mengi yaliyosababishwa na mbinu za KGB yalitatuliwa.”
Kutambua Njia ya Kweli
Ndugu Gorobeţ alirudi Moldova mara alipoachiliwa kutoka katika kambi ya kazi ngumu mnamo Juni 1964. Alipowasili Tabani, aligundua kwamba Mashahidi wengi huko bado walikuwa wamechanganyikiwa kuhusu njia ambayo Yehova anatumia kuwalisha na kuwaongoza watu Wake. Ndugu kadhaa walisoma Biblia peke yake.
Halmashauri ya ndugu watatu waliokomaa kiroho iliwekwa ili kurekebisha hali hiyo. Kwanza walitembelea makutaniko yaliyokuwa kaskazini mwa Moldova, ambako Mashahidi wengi waliishi. Ndugu walipoona kwamba ndugu hao na waangalizi wengine Wakristo bado walikuwa waaminifu licha ya kuteswa sana, walisadikishwa kwamba bado Yehova anatumia tengenezo lilelile lililowafundisha kweli.
Mwishoni mwa miaka ya 1960, KGB ilitambua kwamba kazi ya kuhubiri ilikuwa ikiendelea licha ya mateso na mbinu nyingine. Kitabu Upanga na Ngao kinaeleza hatua ambayo KGB ilichukua: “Maafisa wa [KGB] walishikwa na wasiwasi waliposikia kwamba hata ndani ya kambi za kazi ngumu, ‘viongozi wa Mashahidi wa Yehova walidumisha imani yao inayopinga Ukomunisti na waliendelea kufanya kazi ya Yehova.’ Maafisa wa KGB ambao walikuwa wakitunga njama dhidi ya Mashahidi wa Yehova walifanya mkutano [huko Chisinau] mnamo Novemba 1967 ili kuzungumzia mbinu mpya za ‘kuzuia kazi ya Mashahidi’ na ‘mafundisho yao yanayopinga Ukomunisti.’”
Kunyanyaswa na Ndugu Waasi
Ni jambo la kuhuzunisha kwamba baadhi ya Mashahidi walidanganywa na “mbinu [hizo] mpya” na hivyo kutimiza kabisa lengo la KGB. Baadhi yao walivunja uaminifu wao kwa sababu ya pupa au woga; wengine walikuwa ndugu waliotengwa ambao waliwachukia Mashahidi. Wenye mamlaka walianza kuwatumia ili kuvunja uaminifu wa Mashahidi waaminifu. Mashahidi waliokuwa wamevumilia vifungo vya gereza na kazi ngumu katika kambi walisema kwamba kunyanyaswa na ndugu waliotengwa, ambao baadhi yao walikuwa waasi-imani, lilikuwa jaribu gumu kuliko majaribu mengine yoyote ambayo walipata.
Waasi-imani wengi walikuwa wafuasi wa kikundi cha upinzani. Mwanzoni, kikundi hicho kilikuwa na Mashahidi kadhaa waliokuwa wamechanganyikiwa kwa sababu ya uwongo ulioenezwa na KGB. Lakini baadhi ya wale ambao bado walishirikiana na kikundi hicho mwishoni mwa miaka 1960 walionyesha roho ya jamii ya mtumwa mwovu. Kwa sababu walipuuza onyo la Yesu, walianza “kuwapiga watumwa [wenzao].”—Mt. 24:48, 49.
Hata hivyo, ijapokuwa maafisa wa KGB na wafuasi wao walijitahidi kwa muda mrefu kusababisha migawanyiko ili kuwashinda watu wa Mungu, mbinu yao haikufua dafu. Mapema katika miaka ya 1960, ndugu waaminifu walipoanza kurudisha umoja katika tengenezo nchini Moldova, ndugu wengi nchini humo walikuwa wamejiunga na kikundi cha upinzani. Lakini kufikia mwaka wa 1972, karibu wote walikuwa wakifanya kazi kwa uaminifu pamoja na tengenezo la Yehova.
Mtesaji Aliyefurahia Kusoma Gazeti Letu
Ndugu waaminifu waliobaki Moldova wakati wa utawala wa Kikomunisti waliendelea kufanya kazi ya kuhubiri kwa kadiri walivyoweza. Waliwahubiria watu wa familia zao, marafiki, wanashule na wafanyakazi wenzao. Lakini walihubiri kwa tahadhari sana kwa sababu maafisa wengi wa chama nchini Moldova walikuwa Wakomunisti washupavu. Hata hivyo, si Wakomunisti wote waliowadharau Mashahidi wa Yehova.
Simeon Voloşanovschi anasema hivi: “Polisi walipekua nyumba yetu na kutunyang’anya magazeti na vitabu vingi, ambavyo afisa mkuu aliorodhesha. Baadaye afisa huyo alirudi na orodha hiyo na kuniomba nihakikishe kwamba magazeti na vitabu vyote viliorodheshwa kwa usahihi. Nilipochunguza orodha hiyo, niliona kwamba gazeti moja la Mnara wa Mlinzi, ambalo linazungumzia jinsi ya kufanya maisha ya familia yawe yenye furaha zaidi, halikuwa limeorodheshwa. Nilimwuliza afisa huyo juu ya gazeti hilo. Alijibu hivi kwa aibu: ‘Nililipeleka nyumbani, na tulilisoma pamoja na familia yangu.’ Kisha nikamwuliza, ‘Lakini mlilipenda?’ ‘Bila shaka, tulilipenda sana!’ akajibu.”
Upinzani Wapungua, Ongezeko Laendelea
Wakomunisti waliacha kuwakamata na kuwahamisha watu wa Yehova katika miaka ya 1970. Hata hivyo, mara kwa mara ndugu walikamatwa na kufikishwa mahakamani kwa sababu ya kuhubiri au kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Lakini hawakuhukumiwa vifungo vikali sana.
Kama kwingineko, mpango wa kuwa na baraza la wazee ulianzishwa Moldova mwaka wa 1972. Gheorghe Gorobeţ anasema hivi: “Ndugu walikubali mpango huo mpya kwa shangwe, na kuuona kuwa uthibitisho mwingine wa kwamba roho ya Yehova inaongoza tengenezo lake. Zaidi ya hayo, kwa sababu ndugu wengi zaidi waliwekwa kuwa wazee, makutaniko yalisaidiwa kukomaa kiroho na idadi ya wahubiri iliongezeka nchini Moldova.”
Bila shaka, wakati huo, ndugu walikuwa na ujuzi mwingi wa kuongoza kazi ya kuhubiri na kuchapa vitabu vya Biblia kisiri. Serikali ya Kikomunisti ilipoanza kuwakandamiza Mashahidi, magazeti na vitabu vilichapwa katika sehemu mbili nchini Moldova. Katika miaka mingi ya upinzani mkali ndugu walifanya kazi usiku tu katika sehemu hizo. Kwa hiyo, iliwabidi wafanyakazi kuishi maisha maradufu—maisha ya mchana, walipoendelea na shughuli zao za kawaida kama watu wengine, na maisha ya usiku, walipochapa vitabu kwa ajili ya makutaniko.
Hata hivyo, mambo hayo yalibadilika wakati upinzani na upelelezi ulipopungua. Ndugu waliweza kuendesha matbaa za kuchapa kisiri kwa matokeo mazuri zaidi na kuongeza idadi ya wafanyakazi waliojitolea. Hivyo, vitabu vingi zaidi vilichapwa.
Ndugu pia waliboresha njia zao za kuchapa vitabu. Kwa mfano, walitumia mabamba ya pekee yaliyotayarishwa kwa kutumia taipureta. Pia walirekebisha matbaa ili zichape karatasi pande zote mbili kwa wakati mmoja. Kwa sababu ya maendeleo hayo waliweza kuchapa vitabu vingi zaidi. Hawakuhitaji tena kunakili kwa mkono magazeti na vitabu vya kujifunzia Biblia.
Bila shaka ndugu waliweza kujifunza Biblia zaidi kwa sababu walikuwa na vitabu vingi zaidi. Jambo hilo, na mawasiliano bora, lilisaidia kumaliza kabisa vurugu iliyokuwapo mapema. Hata hivyo, maendeleo hayo yalikuwa mwanzo tu wa mambo mazuri zaidi ambayo watu wa Yehova wangefurahia nchini Moldova.
Ibada ya Kweli Inasitawi
Ijapokuwa serikali ya Kikomunisti ya Sovieti ilikuwa na nguvu nyingi za kisiasa na kijeshi wakati huo, haikufaulu kukomesha ibada ya kweli, bali kupitia mbinu zao za kuwahamisha watu, Wasovieti walisaidia kueneza habari njema hadi ‘sehemu za mbali zaidi za dunia.’ (Mdo. 1:8) Yehova aliahidi hivi kupitia Isaya: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa . . . Hilo ndilo fungu la urithi la watumishi wa Yehova, na uadilifu wao ni kutoka kwangu.” (Isa. 54:17) Maneno hayo yamethibitika kuwa ya kweli kabisa!
Maisha ya Mashahidi wa Yehova yamekuwa rahisi zaidi katika Muungano wa Sovieti tangu nchi hiyo ipate serikali mpya mwaka wa 1985. Hawapelelezwi tena na polisi wa siri au kutozwa faini kwa sababu ya kuhudhuria mikutano ya kidini. Ijapokuwa ndugu huko Moldova waliendelea kufanya mikutano wakiwa watu kumi au wachache zaidi, walianza kufanya makusanyiko madogo ya mzunguko wakati wa sherehe fulani kama vile arusi, au wakati wa mazishi.
Kisha, katika kiangazi cha mwaka wa 1989, ndugu waliohudhuria makusanyiko matatu ya kimataifa katika jiji la Chorzow (karibu na Katowice), Poznan, na Warsaw nchini Poland, walitiwa moyo kuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri. Mamia ya Mashahidi kutoka Moldova walihudhuria. Ndugu hao waaminifu waliokuwa wamezoea kukutanika katika vikundi vidogo walisisimuka sana kumwabudu Yehova pamoja na umati mkubwa wa Mashahidi wenye shangwe kutoka mataifa mengine mengi!
Ndugu huko Moldova walipata baraka nyingine ya kiroho mwaka wa 1991, walipoweza kufanya makusanyiko ya mzunguko hadharani kwa mara ya kwanza. Mwaka wa 1992, walifurahia tukio lingine muhimu, yaani, kusanyiko la kimataifa huko St. Petersburg, Urusi. Mashahidi kutoka Moldova waliohudhuria kusanyiko hilo walikuwa wengi kuliko Mashahidi kutoka nchi hiyo waliohudhuria yale makusanyiko matatu nchini Poland mwaka wa 1989. Naam, Yehova alikuwa amefungua malango ya mbinguni na kuwamwagia watumishi wake waaminifu wenye shukrani baraka nyingi.
Kuwazoeza Waangalizi Wanaosafiri
Walipopata uhuru zaidi, ndugu wa halmashauri ya nchi ya Muungano wa Sovieti na waangalizi wanaosafiri waliweza kuwasiliana kwa urahisi zaidi. Mnamo Desemba 1989, ndugu hao 60 waliokomaa kiroho walikusanyika huko Lvov, Ukrainia, ili wafundishwe. Wazia jinsi wote waliohudhuria darasa hilo walivyofurahi na kujengana kwa kuwa wote walikuwa wamevumilia vifungo vya gereza, kufanya kazi ngumu katika kambi mbalimbali, na magumu mengineyo mengi! Wengi walikuwa marafiki wa karibu tangu nyakati hizo ngumu zilizopita.
Waangalizi wanne kutoka Moldova walihudhuria darasa hilo. Waliporudi, waliwaeleza ndugu na dada katika makutaniko ushauri wenye hekima waliokuwa wamepata huko Lvov, hasa kuhusiana na kazi ya kuhubiri. Kwa mfano, waliwahimiza ndugu waendelee kujihadhari walipohubiri Neno la Mungu, licha ya uhuru waliokuwa nao. (Mt. 10:16) Kwa nini walihitaji kujihadhari? Kwa sababu bado kazi ilikuwa imepigwa marufuku.
Uhitaji Mkubwa wa Majumba ya Ufalme
Tangu kazi ya kuhubiri ilipoanzishwa Moldova, ndugu waliona uhitaji wa kuwa na majumba ya kukutania. Kwa kweli, Wanafunzi wa Biblia waligharimia na kujenga jumba katika kijiji cha Corjeuţi mwaka wa 1922. Jumba hilo lililotumiwa kwa miaka mingi liliitwa nyumba ya mikutano.
Mwishoni mwa miaka ya 1980, upinzani wa serikali ulipoanza kupungua, makutaniko mengi katika miji na vijiji yalikuwa na mamia ya wahubiri. Wahubiri hao wote walikuwa wakikutanika katika nyumba za akina ndugu. Basi, je, wakati wa kujenga Majumba ya Ufalme ulikuwa umewadia? Ili wapate kujua, ndugu waliwatembelea maafisa wa vijiji mbalimbali.
Baadhi ya maafisa hao walikuwa tayari kusaidia. Kwa mfano, mnamo Januari 1990, akina ndugu katika kijiji cha Feteşti chenye wakazi 3,150, kilicho kaskazini mwa Moldova, walienda kumwona meya. Meya huyo aliwaambia kwamba wanaweza kufanya kazi yao kwa uhuru katika kijiji chake. Ndugu hawakumwamini. Kwa hiyo walimwomba ruhusa ya kurekebisha nyumba ndogo ya ndugu fulani ili itumiwe kama Jumba la Ufalme, ingawa kutaniko hilo lilikuwa na wahubiri 185!
Meya aliidhinisha mradi huo na akina ndugu wakaanza kufanya kazi. Hata hivyo, punde walikabili tatizo kubwa. Walihitaji kubomoa ukuta fulani, lakini kama wangeubomoa, huenda nyumba yote ingebomoka! Kwa hiyo kazi ilikoma ghafula. Wafanye nini? Ndugu waliamua kwenda kumwona meya tena na kumweleza tatizo hilo. Walifurahi sana walipopata ruhusa ya kujenga Jumba la Ufalme! Ndugu na dada wote kutanikoni waliunga mkono mradi huo na ujenzi ulimalizika baada ya siku 27 tu.
Kutaniko la Feteşti liligawanywa mara mbili kwa sababu Jumba la Ufalme lilikuwa dogo. Hata hivyo, kutaniko hilo lilikuwa na wahubiri wengi wapya wasiobatizwa. Basi, ndugu waliamua kufanya ubatizo siku ambayo jumba hilo lingewekwa wakfu. Kwa hiyo, baada ya hotuba ya ubatizo, wote walienda hadi kwenye mto uliokuwa karibu na watu 80 walibatizwa ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova.
Bila shaka, makutaniko mengi zaidi yalihitaji Majumba ya Ufalme haraka. Ndugu walikuwa wameona picha za Majumba ya Ufalme katika vitabu, hivyo, akina ndugu katika makutaniko kadhaa waliamua kujenga majumba yaliyofanana na hayo. Wote walitoa mchango kulingana na uwezo wao na walijenga kwa ubunifu mwingi. Kati ya mwaka wa 1990 na 1995, ndugu waligharimia na kujenga zaidi ya Majumba ya Ufalme 30.
Baadhi ya Majumba ya Ufalme yalitumiwa pia kwa ajili ya makusanyiko ya mzunguko. Hata hivyo, watu wengi sana walihudhuria hivi kwamba wengi walisikiliza wakiwa wameketi nje. Kwa hiyo, ndugu walianza kufikiria kujenga Jumba la Kusanyiko. Hawakusita. Mwaka wa 1992, walijenga Jumba la Kusanyiko la kwanza nchini Moldova katika kijiji cha Corjeuţi. Jumba hilo linalotoshea watu 800 lilijengwa kwa miezi mitatu tu. Mwaka uliofuata, Mashahidi wenyewe waligharimia na kujenga Jumba la Kusanyiko linalotoshea watu 1,500 huko Feteşti.
Ujenzi huo wote ulifanywa kwa wakati unaofaa, kwa kuwa mabadiliko ya kisiasa na kuzorota kwa uchumi katikati ya miaka ya 1990, zilifanya thamani ya pesa za Moldova ipungue sana. Kwa hiyo, pesa zilizotumiwa kujenga Jumba la Ufalme mapema katika miaka ya 1990 hazikutosha hata kununua viti miaka michache baadaye!
Ujenzi wa Majumba ya Ufalme Upande wa Kusini
Tofauti na makutaniko yaliyo kaskazini mwa Moldova, makutaniko yaliyo sehemu ya kusini hayakuwa na Majumba mengi ya Ufalme. Kwa hiyo, kwa sababu ya ongezeko kubwa la wahubiri katika miaka ya 1990, makutaniko mengi mapya ya kusini yalikosa mahali pazuri pa kukutania. Shule za umma zilitumiwa, lakini ilizidi kuwa vigumu kuzikodi.
Tengenezo la Yehova liliwasaidia ndugu tena. Baraza Linaloongoza lilifanya mpango wa Hazina ya Majumba ya Ufalme kwa ajili ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika nchi kama Moldova ambako makutaniko hayana pesa nyingi.
Mpango huo umeleta matokeo mazuri. Kwa mfano, jiji kuu la Chisinau lilikuwa na Jumba la Ufalme moja tu mwaka wa 1999. Lakini kufikia Julai 2002, majumba kumi ambayo hutumiwa na makutaniko 30 yalikuwa yamejengwa, na majumba mengine matatu yalikuwa yakijengwa katika jiji hilo lenye makutaniko 37.
Kazi Yahalalishwa Hatimaye
Moldova ilipata uhuru Agosti 27, 1991. Kwa hiyo, marufuku iliyowekwa na serikali ya Sovieti haikuwa halali tena. Hata hivyo, dini ya Mashahidi wa Yehova haikuandikishwa kisheria bado. Idadi yao ilikuwa 4,000 hivi wakati huo.
Baada ya kupata mwelekezo kutoka Baraza Linaloongoza, ndugu katika ofisi ya Moldova walienda mara moja kuwaona maafisa katika idara ya serikali inayoshughulikia mambo hayo ili kutoa ombi la kuhalalisha kazi ya Mashahidi wa Yehova. Wenye mamlaka wa serikali mpya walikubali ombi hilo kwa nia nzuri. Ilichukua muda mrefu kushughulikia ombi hilo, lakini hatimaye, Julai 27, 1994, ofisi ilipokea hati rasmi ya usajili.
Siku hiyo ilikuwa ya pekee sana kwa Mashahidi wa Yehova nchini Moldova! Baada ya kuvumilia marufuku, mateso, na vifungo vya gereza kwa miaka 60 hivi, waliweza kumwabudu Yehova na kuhubiri habari njema kwa uhuru. Waliweza pia kufanya makusanyiko ya wilaya. Mnamo Agosti 1994, mwezi mmoja tu baada ya kazi kuhalalishwa, Mashahidi wa Yehova walifanya kusanyiko la kwanza la wilaya nchini Moldova katika uwanja mkubwa wa michezo huko Chisinau. Kusanyiko hilo lilikuwa lenye kusisimua sana!
Betheli Yapanuliwa
Idadi ya wahubiri wa Ufalme ilikuwa imepita 10,000 mwaka wa 1995. Ofisi ndogo huko Chisinau ilishughulikia mambo fulani kuhusiana na kazi nchini Moldova, lakini ofisi ya tawi ya Urusi, umbali wa kilometa 2,000 kutoka Moldova, ilisimamia kazi kwa ujumla. Hata hivyo, ofisi ya tawi ya Rumania ilikuwa umbali wa kilometa 500 tu kutoka Moldova na wakazi wengi wa Moldova huongea Kirumania. Baadaye Kirumania kilifanywa kuwa lugha rasmi nchini humo. Kwa hiyo, baada ya kufikiria mambo yote kwa makini, Baraza Linaloongoza lilipendekeza kwamba ofisi ya tawi ya Rumania isimamie kazi nchini Moldova.
Lakini ongezeko liliendelea na ile ofisi ndogo huko Chisinau haikuwa na nafasi ya kutosha tena. Ilikuwa wazi kwamba wakati wa kuanzisha Betheli nchini Moldova ulikuwa umewadia. Wanabetheli wa kwanza huko walikuwa Ion na Iulia Rusu. Ndugu Rusu alitumikia kama mwangalizi wa mzunguko wa badala kuanzia mwaka wa 1991 hadi 1994. Mwanabetheli mwingine alikuwa Gheorghe Gorobeţ, aliyetumikia kama mwangalizi wa wilaya hadi alipoalikwa Betheli. Hakuishi Betheli, kwa hiyo, alisafiri kila siku kutoka nyumbani kwake hadi Betheli. Guenther na Rosaria Matzura, ambao walihitimu darasa la 67 la shule ya Gileadi, waliwasili Mei 1, 1996, baada ya kutumikia nchini Rumania kwa miaka kadhaa.
Idadi ya wahubiri ilipoendelea kuongezeka, wafanyakazi wengi zaidi walihitajika Betheli. Lakini hakukuwa na nafasi. Isitoshe, mwaka wa 1998, Wanabetheli huko Moldova walikuwa wakiishi katika makao matano tofauti-tofauti kotekote jijini. Hivyo, ndugu walianza kutafuta kiwanja ili kujenga Betheli. Walishukuru sana wakati maafisa wa serikali jijini Chisinau walipowapa kwa fadhili kiwanja cha meta 3,000 za mraba katikati ya jiji. Wakitarajia ongezeko kubwa hata zaidi, ndugu walinunua kiwanja kilichopakana na kile walichopewa.
Kiunzi cha jengo kilijengwa na kampuni fulani, na ndugu waliojitolea kutoka nchi nyingine pamoja na ndugu na dada kutoka Moldova walimaliza ujenzi huo. Ujenzi ulianza mnamo Septemba 1998, na baada ya miezi 14 tu, Wanabetheli walifurahi kuhamia makao yao mapya. Walisisimuka sana kuwa pamoja hatimaye.
Majengo hayo ya Betheli yaliwekwa wakfu Septemba 16, 2000. Wageni kutoka nchi 11 walihudhuria. Siku iliyofuata, zaidi ya watu 10,000 walikusanyika kwenye uwanja wa michezo kusikiliza hotuba iliyotolewa na ndugu Gerrit Lösch wa Baraza Linaloongoza. Wote waliohudhuria walihisi ule upendo unaowaunganisha watu wa Yehova ulimwenguni pote.
Kwa sasa kuna Wanabetheli 26 nchini Moldova. Baadhi yao ni Wanabetheli kutoka nchi za ng’ambo kama vile David na Miriam Grozescu. Wengine kama vile Enno Schlenzig, walihitimu Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, kisha wakakubali kutumwa Moldova. Kwa hiyo, ijapokuwa familia ya Betheli ya Moldova ni ndogo ina wafanyakazi kutoka nchi nyingi.
Kuwazoeza Wahubiri wa Habari Njema
Katika miaka ya marufuku na mateso, Mashahidi wa Yehova nchini Moldova waliwahubiria wengine habari njema kwa busara kila walipopata nafasi. Lakini sasa wakati wa kuhubiri waziwazi nyumba kwa nyumba na barabarani ulikuwa umewadia. Ndugu walitii na kuanza kuhubiri nyumba kwa nyumba na barabarani. Lakini walipenda hasa kuhubiri barabarani. Hata hivyo, idadi ya wahubiri ilipozidi kuongezeka walihitaji usawaziko. Kwa hiyo, ndugu walitiwa moyo kuhubiri nyumba kwa nyumba zaidi, nao walifanya hivyo kwa uaminifu.
Walipohubiri nyumba kwa nyumba, walitambua kwamba majirani wao walikuwa na njaa ya chakula kizuri cha kiroho. Ili kutosheleza njaa hiyo ya kiroho, tengenezo la Yehova lilichapisha gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na vitabu vinginevyo vya kujifunzia Biblia katika Kirumania na Kirusi. Wahubiri walijitahidi pia kufanya maendeleo katika utumishi kwa kutumia mapendekezo yaliyo katika Huduma Yetu ya Ufalme. Walipata mazoezi mazuri pia kwa kuhudhuria Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kwa ukawaida.
Ndugu wakomavu wenye uzoefu kutoka nchi nyingine wamewasaidia ndugu wa Moldova kufanya mambo kupatana na mielekezo ya tengenezo la Yehova. Ndugu hao stadi, waliojitolea kutoka nchi nyingine wameimarisha na kutegemeza makutaniko kama vijiti vinavyoitegemeza mizabibu.
Kipindi cha Ongezeko Kubwa
Ongezeko kubwa la idadi ya wanafunzi nchini Moldova linaonekana waziwazi katika jiji kuu la Chisinau lenye wakazi 662,000. Mnamo Januari 1991, kabla ya kazi ya Mashahidi wa Yehova kuandikishwa kisheria, jiji la Chisinau lilikuwa na makutaniko mawili tu yenye wahubiri 350 hivi. Lakini Januari 2003, idadi ya wahubiri ilikuwa imeongezeka na kufikia zaidi ya 3,870 katika makutaniko 37! Katika kutaniko moja, wanafunzi wa Biblia 101 walianza kuhubiri katika kipindi cha miezi tisa tu! Kwa sababu ya ongezeko hilo kubwa, kwa kawaida makutaniko hugawanywa baada ya miaka miwili hivi.
Mnamo Agosti 1993, Moldova ilikuwa na wahubiri 6,551. Lakini Machi 2002, idadi ya wahubiri ilikuwa imeongezeka kufikia 18,425. Hilo ni ongezeko la asilimia 280 katika miaka tisa! Katika pindi hiyo, idadi ya mapainia iliongezeka kutoka 28 hadi 1,232.
Makamu wa Meya Awa Painia
Wakomunisti wengi wamepata kumjua Yehova, na baadhi yao walikuwa watu wenye mamlaka. Mmojawapo ni Valeriu Mârza aliyekuwa makamu wa meya wa mji wa Soroca wenye wakazi 39,000 hivi. Katika sherehe zenye gwaride, Valeriu alikuwa miongoni mwa watu mashuhuri waliopigiwa gwaride ya heshima. Kwa hiyo, alijulikana sana mjini.
Hata hivyo, hatimaye Valeriu alianza kujifunza Biblia na akabatizwa. Watu waliitikiaje alipowahubiria? Ndugu Mârza anasema hivi: “Karibu kila mtu alinikaribisha. Nilikuwa na nafasi nzuri sana za kuhubiri, na mimi na mke wangu tulitambua kwamba mji wetu ulikuwa eneo lenye watu wengi wenye kupendezwa!” Muda si muda, Ndugu Mârza aliwekwa kuwa painia wa pekee. Yeye na mke wake walitumikia Betheli pia kwa muda wa mwaka mmoja. Sasa wana pendeleo la kufanya kazi ya mzunguko.
Mapainia Wasaidia
Kwa kulinganisha na idadi ya watu, Moldova ni mojawapo ya nchi zenye wahubiri wengi barani Ulaya. Hata hivyo, bado kuna miji midogo na vijiji vingi visivyo na Shahidi hata mmoja. Kwa sababu ya magumu ya kiuchumi, wahubiri na mapainia wengi hawawezi kuhamia maeneo yenye uhitaji mkubwa. Ili kuhakikisha kwamba habari njema inahubiriwa kotekote, ofisi ya tawi ya Rumania imewaweka mapainia wa pekee 50 hivi nchini Moldova. Zaidi ya mapainia 20 kati yao ni wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, ambayo imefanywa Rumania, Urusi, na Ukrainia.
Wahubiri hao wa habari njema wenye bidii wanapata matokeo mazuri sana. Kwa mfano, mji wa Căuşeni ulikuwa na kikundi kimoja tu chenye wahubiri 15, mapainia wa pekee, Serghei na Oxana Zighel, walipotumwa huko mwaka wa 1995. Ndugu na Dada Zighel waliwasaidia ndugu katika mji huo kuanzisha mafunzo mengi ya Biblia. Wengi walijiunga nao katika utumishi wa wakati wote walipoona furaha waliyopata katika kazi ya upainia. Sasa kuna makutaniko mawili yenye wahubiri 155 hivi mjini Căuşeni, hilo ni ongezeko la asilimia kumi katika miaka saba tu! Sasa Ndugu na Dada Zighel wanafanya kazi ya mzunguko, kwa hiyo, wanaweza kusaidia makutaniko mengi zaidi.
Uhuru Waambatana na Magumu
Utawala wote wa mwanadamu hukumbwa na matatizo. Chini ya ufalme wa Rumania, utawala wa kimabavu wa Kifashisti, na utawala wa Kikomunisti, watu wa Yehova nchini Moldova walikabili marufuku, mateso, uhamisho, na upinzani kutoka kwa makasisi. Leo, Mashahidi wa Yehova, kama watu wengine, hupambana na magumu ya kiuchumi. Kwa hiyo, nyakati nyingine inawabidi wazazi wote wawili kufanya kazi ya kuajiriwa, na watu wengine hata hukosa kazi.
Isitoshe, uhalifu na ufisadi unazidi kwa sababu ya utafutaji wa mali na ukosefu wa maadili katika jamii. Je, watu wa Yehova wanaweza kushinda licha ya mambo hayo yanayoweza kuathiri hali yao nzuri ya kiroho? Bila shaka! Wamejionea kwamba Yehova hawaachi kamwe waaminifu wake wanaomwomba msaada wanapokabili magumu na vishawishi.—2 Tim. 3:1-5; Yak. 1:2-4.
Hali iliyopo sasa inatukumbusha sura ya 14 ya kitabu cha Ufunuo, inayozungumzia mavuno mawili ya mfano. Ya kwanza ni mavuno ya “mzabibu wa dunia,” ambao ni zao bovu linaloongezeka katika siku hizi za mwisho kama ilivyotabiriwa. (Ufu. 14:17-20; Zab. 92:7) Hivi karibuni, “mzabibu” huo pamoja na mazao yake mabovu, yatang’olewa na kutupwa katika “shinikizo kubwa la divai la hasira ya Mungu.” Watumishi wa Yehova wanatamani sana kuiona siku hiyo!
Wanaposubiri siku hiyo, Wakristo watiwa-mafuta na wenzao wanashangilia kwa sababu ya hali yao nzuri ya kiroho. Naam, “shamba [la Yehova] la mizabibu la divai yenye kutoa povu” litaendelea kuzaa chakula kingi cha kiroho chenye lishe, na watu wenye mfano wa kondoo huvutiwa na ukarimu huo. Kwa nini watu wa Mungu wana uhakika huo? Ni kwa sababu Yehova mwenyewe analinda shamba lake la mizabibu analolipenda. (Isa. 27:2-4) Jambo hilo limeonekana wazi kabisa nchini Moldova! Ni kweli kwamba mbinu za Shetani, kama vile mateso, uhamisho, uvumi wa uwongo, na ndugu bandia, zimewaletea watu wa Mungu magumu mengi lakini hawajawahi kushindwa kiroho.—Isa. 54:17.
Naam, “mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima, ambalo Yehova aliwaahidi wale wanaoendelea kumpenda.” (Yak. 1:12) Ukiwa na maneno hayo muhimu akilini, masimulizi ya Mashahidi wa Yehova nchini Moldova na yakuchochee ‘uendelee kumpenda’ Yehova, “kuvumilia jaribu,” na “kuzaa matunda mengi.”—Yoh. 15:8.
[Maelezo ya Chini]
a Jina Moldova litatumiwa katika masimulizi haya badala ya jina Bessarabia na Moldavia, ila tunapozungumzia kipindi ambapo jina lingine lilitumiwa. Ni vizuri kukumbuka kwamba mipaka ya Moldova ya kisasa si sawa na mipaka ya nchi ya kale ya Bessarabia na Moldavia. Kwa mfano, eneo fulani la Bessarabia liko Ukrainia, na sehemu ya Moldavia iko Rumania.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 71]
Divai kwa Ajili ya Urusi na Ulaya Mashariki
Mizabibu inasitawi sana Moldova kwa sababu nchi hiyo ina majira marefu ya kiangazi na udongo wenye rutuba. Kwa hiyo, divai imetengenezwa katika nchi hiyo kwa maelfu ya miaka. Mwishoni mwa karne ya tatu K.W.K., utengenezaji wa divai uliongezeka wakati wakazi wa nchi hiyo walipoanza kufanya biashara na Wagiriki na baadaye na Waroma katika karne ya pili W.K.
Leo, zao kuu la kilimo la Moldova ni zabibu, na kila mwaka, lita milioni 140 za divai hutengenezwa katika viwanda 130 hivi. Karibu asilimia 90 ya divai hiyo huuzwa katika nchi za nje. Urusi hununua asilimia 80 hivi ya divai ya Moldova, na Ukrainia hununua asilimia 7 hivi.
[Sanduku katika ukurasa wa 72]
Maelezo Mafupi Kuhusu Moldova
Nchi: Sehemu ya katikati na ya kaskazini ya Moldova ina misitu, nyanda za juu, na mbuga. Sehemu kubwa ya upande wa kusini ni mbuga iliyolimwa.
Watu: Thuluthi mbili ya wakazi ni wenyeji wa Moldova. Wakazi wengine ni Warusi, watu wa Ukrainia, Waturuki wa kabila la Gagauz, Wabulgaria, na Wayahudi (orodha inaanza na kikundi kikubwa na kumalizia na kile kidogo). Watu wengi wa Moldova ni waumini wa Kanisa la Othodoksi ya Mashariki.
Lugha: Kirumania ndiyo lugha rasmi. Watu wengi wanaongea pia Kirusi, hasa watu wanaoishi mijini, kwa hiyo, ni jambo la kawaida kutumia lugha zote mbili.
Kazi: Uchumi wa nchi hiyo unategemezwa hasa na kilimo na viwanda vya chakula. Sasa viwanda vinafanyiwa marekebisho ili viwe vya kisasa.
Chakula: Zabibu, ngano, mahindi, viazi-sukari, na alizeti ni baadhi ya mazao ya kilimo. Wanyama wanaofugwa hasa ni ng’ombe wa nyama na wa maziwa na nguruwe.
Hali ya hewa: Halijoto ya wastani katika mwezi wa Julai ni nyuzi 21 ya Selisiasi na joto linaweza kupungua hadi nyuzi 4 chini ya kiwango cha kuganda katika mwezi wa Januari. Kwa ujumla hali ya hewa ni yenye joto la wastani na nchi hiyo haikumbwi na baridi kali sana. Kiwango cha wastani cha mvua kila mwaka ni sentimeta 50 hivi.
[Sanduku katika ukurasa wa 83-85]
Wakristo Waliodumisha Msimamo wa Kutokuwamo
George Vacarciuc: Ndugu Vacarciuc alilelewa na wazazi waliokuwa Mashahidi wa Yehova. Mnamo Desemba 1942 aliitwa na Wafashisti ajiandikishe katika jeshi. Kwa sababu alikataa kujiunga na jeshi, alifungwa katika chumba chenye giza tititi kwa siku 16 na kupewa chakula kidogo sana. Wenye mamlaka walimwita tena, na bila kumwambia hukumu yake, walimwahidi kwamba hukumu hiyo ingefutwa kama angejiunga na jeshi. Alikataa tena.
George alihukumiwa kifungo cha miaka 25. Lakini aliachiliwa na jeshi la Sovieti Septemba 25, 1944. Hata hivyo, miezi miwili haikupita na Wasovieti wakajaribu tena kumwandikisha jeshini. Kwa sababu hakukubali kutenda kinyume cha dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia, alihukumiwa kifungo cha miaka kumi katika kambi mbalimbali za kazi ngumu. Kwa muda wa mwaka mmoja, familia yake haikujua mahali alipokuwa. Baada ya miaka mitano, Ndugu Vacarciuc aliachiliwa Desemba 5, 1949. Alirudi nyumbani huko Corjeuţi na aliendelea kuwa mwaminifu hadi kifo chake Machi 12, 1980.
Parfin Goreacioc: Ndugu Goreacioc alizaliwa mwaka wa 1900, na alijifunza kweli ya Biblia katika kijiji cha Hlina kati ya mwaka wa 1925 na 1927. Yeye na ndugu zake, Nicolae na Ion, walifundishwa kweli na Damian na Alexandru Roşu, Wanafunzi wa Biblia wa kwanza katika kijiji hicho.
Parfin na Mashahidi wengine walikamatwa mwaka wa 1933 na kupelekwa hadi mji wa Khotin, ambako walihojiwa na kutozwa faini kwa sababu ya kuhubiri. Katika mwaka wa 1939, kwa sababu ya uchochezi wa kasisi wa kijiji, Parfin alipelekwa kwenye kituo cha polisi katika kijiji jirani cha Ghilavăţ. Polisi walimlaza kifudifudi kwenye kitanda cha mbao, wakamfunga, na kumpiga tena na tena kwenye nyayo.
Wafashisti walipotwaa mamlaka, Parfin alikamatwa tena na kupelekwa gerezani. Hata hivyo, mwaka uo huo, Wasovieti walimweka huru, lakini muda mfupi baadaye walimkamata tena kwa sababu alikataa kujiunga na jeshi. Alifungwa Chisinau kwa miezi kadhaa kisha akaachiliwa.
Wasovieti walimkamata Parfin tena mwaka wa 1947, na kumhukumia adhabu ya uhamisho wa miaka minane kwa sababu ya kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu. Watoto wake walihamishwa hadi Siberia mwaka wa 1951. Lakini hawakujiunga na baba yao wala hawakumwona tena kamwe. Parfin akawa mgonjwa sana alipokuwa uhamishoni na alidumisha uaminifu wake hadi kifo chake mwaka wa 1953.
Vasile Pădureţ: Ndugu Pădureţ alizaliwa mwaka wa 1920 katika kijiji cha Corjeuţi, na alijifunza kweli mwaka wa 1941 chini ya utawala wa Wafashisti. Kwa hiyo, yeye pia aliteswa na Wafashisti na Wasovieti. Aliwaambia Wasovieti hivi kwa ujasiri: “Sikuwapiga risasi Wakomunisti wala sitawaua Wafashisti.”
Vasile alihukumiwa kifungo cha miaka kumi katika kambi ya kazi ngumu huko Urusi kwa sababu aliongozwa na dhamiri yake kuchukua msimamo huo unaopatana na Biblia. Hata hivyo, kifungo hicho kilipunguzwa na baada ya miaka mitano, Agosti 5, 1949, alirudi nyumbani. Alipokamatwa kwa mara ya tatu mpango wa kuwahamisha Mashahidi hadi Siberia ulikuwa umeanzishwa. Kwa hiyo, Aprili 1, 1951, Vasile na familia yake walipanda gari-moshi kwenda Siberia. Baada ya kukaa huko kwa miaka mitano, waliruhusiwa kurudi Corjeuţi, Moldova. Vasile alikuwa mwaminifu hadi kifo chake, Julai 6, 2002, wakati masimulizi haya yalipokuwa yakiandikwa.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 89, 90]
‘Singebadilisha Utumishi Wangu kwa Chochote Kile’
Ion Sava Ursoi
Alizaliwa: 1920
Alibatizwa: 1943
Maisha yake: Alitumikia kama mwangalizi wa mzunguko wakati wa utawala wa Wakomunisti.
Nilizaliwa Caracuşeni, Moldova, na nilijifunza kweli kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Mke wangu alikufa mwaka wa 1942. Wakati wa mazishi yake watu wenye ghasia walinifukuza kutoka makaburini. Kwa nini? Kwa sababu nilikuwa nimeacha dini yangu. Baadaye katika mwaka huo, serikali ya Kifashisti ilijaribu kuniandikisha jeshini. Lakini kwa sababu sikutaka kuunga mkono siasa, nilikataa. Nilihukumiwa kifo, lakini hukumu hiyo ilibadilishwa kuwa kifungo cha miaka 25. Nilihamishwa kutoka kambi moja hadi nyingine. Jeshi la Sovieti lilituweka huru nilipokuwa gerezani huko Craiova, Rumania.
Lakini mara tu baada ya kuachiliwa, Wakomunisti walinifunga gerezani tena. Walinipeleka Kalinin, Urusi. Miaka miwili baadaye, katika mwaka wa 1946, waliniruhusu kurudi nyumbani, ambako nilisaidia kupanga upya kazi ya kuhubiri. Kisha Wasovieti walinikamata tena mwaka wa 1951. Wakati huu walinihamisha hadi Siberia pamoja na Mashahidi wengine wengi. Sikurudi nyumbani hadi mwaka wa 1969.
Ninapofikiria maisha yangu, ninakumbuka pindi nyingi ambapo Yehova alinipa nguvu ya kudumisha uaminifu wangu. Singebadilisha utumishi wangu kwa Muumba kwa chochote kile ulimwenguni. Sasa ninapambana na matatizo ya afya na uzee. Lakini tumaini langu thabiti la kuishi katika ulimwengu mpya, wakati mwili wangu utakapokuwa na nguvu za ujana tena, huimarisha azimio langu la kuendelea “kufanya yaliyo mema.”—Gal. 6:9.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 100-102]
Nina Sababu Nyingi za Kuimba
Alexandra Cordon
Alizaliwa: 1929
Alibatizwa: 1957
Maisha yake: Alikabili magumu chini ya utawala wa Sovieti na kwa sasa yeye ni mhubiri wa habari njema.
Ninapenda sana kuimba na jambo hilo lilinisaidia kupata kweli, na baadaye, liliniimarisha kiroho imani yangu ilipojaribiwa. Nilipokuwa kijana katika miaka ya 1940, nilipata kuwajua vijana fulani huko Corjeuţi waliofurahia kuimba nyimbo za Ufalme na kuzungumzia Biblia walipokuwa na nafasi. Kweli za kiroho nilizojifunza katika mazungumzo hayo na katika nyimbo tulizoimba zilinivutia sana.
Muda si muda, nikawa mhubiri wa habari njema. Mwaka wa 1953, mimi na Mashahidi wengine kumi tulikamatwa kwa sababu ya kuhubiri habari njema. Nilifungwa katika gereza moja huko Chisinau nikingoja kufikishwa mahakamani. Nilidumisha nguvu yangu ya kiroho kwa kuimba nyimbo za Ufalme, jambo ambalo lilimkasirisha askari mmoja. Alisema hivi: “Uko gerezani. Haifai kuimba hapa!”
Nilimjibu hivi: “Nimeimba maisha yangu yote. Kwa nini niache sasa? Unaweza kunifunga gerezani, lakini huwezi kuifunga midomo yangu kwa kufuli. Moyo wangu u huru, nami nampenda Yehova. Kwa hiyo nina sababu nyingi za kuimba.”
Nilihukumiwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu huko Inta karibu na Mzingo wa Aktiki. Katika miezi michache ya kiangazi, mimi na Mashahidi wengine tulifanya kazi msituni. Wakati huo pia, nyimbo za Ufalme ambazo tulijua, zilitusaidia kuwa wenye nguvu kiroho na kuhisi moyoni kwamba tulikuwa huru. Zaidi ya hayo, tofauti na yule askari huko Chisinau, askari huko Inta walitutia moyo tuimbe.
Nilikaa katika kambi ya Inta kwa miaka mitatu, miezi mitatu, na siku tatu. Kisha, msamaha ulitolewa na nikaachiliwa. Nilienda Tomsk, Urusi, kwa sababu sikuruhusiwa kurudi Moldova. Huko niliungana tena na mume wangu ambaye pia alikuwa amefungwa kwa kipindi fulani. Tulikuwa tumetengana kwa miaka minne.
Kwa sababu ya kukamatwa, sikuweza kubatizwa ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova. Hivyo, niliwauliza ndugu huko Tomsk kuhusu jambo hilo. Kwa kuwa wengine pia walitaka kubatizwa, mara moja ndugu walipanga kuwe na ubatizo. Hata hivyo, kwa sababu ya marufuku, waliamua kufanya ubatizo huo usiku katika ziwa lililokuwa katika msitu wa karibu.
Wakati uliopangwa ulipowadia, tuliondoka katika viunga vya Tomsk na kuingia msituni tukiwa wawili-wawili ili mpango wetu usigunduliwe. Watu walipaswa kufuatana wawili-wawili hadi wafike salama kwenye ziwa. Hivyo ndivyo ilivyopangwa. Lakini, dada wawili wazee waliotutangulia mimi na mwenzangu walipotea njia. Sisi tuliwafuata, na kama ilivyopangwa wale waliokuwa nyuma yetu wakatufuata. Punde, mimi, mwenzangu, na watu wengine wanane hivi tulipotea msituni. Tulilowa kabisa kwa sababu ya unyevu vichakani na tulitetemeka kwa baridi. Tulihofia kwamba tungekutana na dubu au mbwa-mwitu ambao wanapatikana katika eneo hilo. Tulikuwa na wasiwasi sana hivi kwamba tulishtuka kila tuliposikia sauti fulani.
Nilitambua kwamba ingekuwa hatari kushikwa na hofu au kukata tamaa, kwa hiyo, nilipendekeza tusimame tuli na kupiga mbinja ya wimbo wa Ufalme, huenda wale wengine wangetusikia. Tulisali pia kwa moyo wote. Wazia furaha yetu tuliposikia sauti ya wimbo uleule ikitufikia polepole katika msitu huo wenye giza! Naam, ndugu zetu walikuwa wamesikia wimbo wetu! Mara moja waliwasha tochi ili tujue mahali walipokuwa. Baada ya muda mfupi, tulizamishwa katika maji baridi sana ziwani, lakini tulifurahi sana hivi kwamba hata hatukusikia baridi.
Sasa nina umri wa miaka 74 na nimerudi Corjeuţi, ambako nilikuwa nimejifunza kweli. Licha ya uzee, bado ninaimba mara nyingi, hasa ili kumsifu Baba yetu wa mbinguni.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 104-106]
Nilijitahidi Kuwaiga Wazazi Wangu
Vasile Ursu
Alizaliwa: 1927
Alibatizwa: 1941
Maisha yake: Alikuwa msimamizi wa kutaniko na alifanya kazi ya kuchapa vitabu kisiri.
Wazazi wangu, Simeon na Maria Ursu, walibatizwa mwaka wa 1929. Kati ya watoto wao watano, mimi ndiye mkubwa. Wakati wa utawala wa Wafashisti, Baba na Mama walikamatwa na kuhukumiwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu kwa sababu hawakuunga mkono siasa. Ndugu na dada wa kiroho wa kutaniko la Corjeuţi walitutunza sisi watoto na walilima shamba la familia yetu. Kwa hiyo hatukukosa chakula kamwe. Nyanya yetu mzee, ambaye hakuwa Shahidi, alisaidia pia kututunza. Nilikuwa na umri wa miaka 14 wakati huo.
Kwa sababu ya mfano mzuri wa wazazi wangu, nilijitahidi sana kuwasaidia ndugu na dada zangu kiroho. Hivyo, niliwaamsha mapema kila asubuhi ili tujifunze sehemu fulani katika kitabu kinachozungumzia Biblia. Hawakufurahi nilipowaamsha, lakini sikuwaruhusu kuendelea kulala. Nilitambua umuhimu wa kujifunza kwa ukawaida. Kwa hiyo, wazazi wetu walipoachiliwa na kurudi nyumbani mwaka wa 1944, walifurahi kuona kwamba hali yetu ya kiroho ilikuwa nzuri. Tulifurahi sana wazazi wetu waliporudi! Lakini furaha yetu haikudumu.
Mwaka uliofuata, Wasovieti walimkamata Baba na kumfunga huko Norilsk, Siberia, kaskazini mwa Mzingo wa Aktiki. Miaka mitatu baadaye, nilimwoa Emilia, dada mchangamfu aliyependa mambo ya kiroho. Nilimjua Emilia vizuri sana tangu utotoni. Mwaka mmoja tu baada ya arusi yetu, mimi na mama yangu tulikamatwa. Tulipelekwa Chisinau, ambako tulihukumiwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu. Emilia aliwatunza kwa upendo ndugu na dada zangu ambao sasa walikuwa wamenyang’anywa wazazi wao na kaka yao.
Hatimaye nikapelekwa Vorkuta ili kufanya kazi katika migodi ya makaa. Kambi hiyo ya kazi ngumu iliyokuwa kaskazini mwa Mzingo wa Aktiki ilijulikana kuwa mbaya sana. Miaka miwili baadaye, mwaka wa 1951, Emilia, ndugu zangu watatu, na dada yangu mmoja walihamishwa hadi Tomsk, magharibi mwa Siberia. Mwaka wa 1955, Emilia aliomba ahamishwe hadi Vorkuta ili aungane nami. Alipokuwa huko alijifungua mtoto wa kike ambaye tulimwita Tamara. Baadaye tulipata watoto wengine wawili.
Msamaha ulitangazwa mnamo Septemba 1957, na tukaachiliwa. Lakini mwezi mmoja baadaye nilikamatwa tena. Nilihukumiwa kifungo cha miaka saba katika kambi ya kazi ngumu huko Mordvinia, karibu na Saransk, Urusi. Ndugu wengine wengi walifungwa huko pia, na wengine walikuja baadaye. Wake wetu walipokuja kututembelea, walituletea kisiri magazeti na vitabu kwa ukawaida. Tulithamini sana jambo hilo. Mnamo Desemba 1957, Emilia alihamia Kurgan, magharibi mwa Siberia, ili amtunze binti yetu, Tamara, aliyekuwa anakaa na wazazi wa Emilia. Kwa sababu hiyo, mimi na Emilia tulitengana kwa miaka saba. Hatukuwa na njia nyingine ya kuzuia Tamara asipelekwe kwenye shule ya serikali.
Niliachiliwa mwaka wa 1964, lakini sikuruhusiwa kurudi nyumbani Moldova. Ijapokuwa sikuweza kusafiri kwa uhuru, niliweza kujiunga na mke wangu na binti yangu huko Kurgan, ambako nilitumikia kama kiongozi wa funzo la kitabu kutanikoni. Mwaka wa 1969, tulihamia Krasnodar katika Milima ya Kaukasus. Baada ya kutumikia huko kwa miaka minane, tukahamia Chirchik, Uzbekistan. Huko nilifanya kazi ya kuchapa vitabu kisiri. Hatimaye, tuliruhusiwa kurudi Moldova mwaka wa 1984. Tulihamia jiji la Tighina lenye wakazi 160,000 na wahubiri 18 tu. Tangu wakati huo idadi hiyo imeongezeka na sasa kuna makutaniko tisa na karibu wahubiri na mapainia 1,000 katika mji huo.
Je, ninajuta kwamba nilikaa miaka mingi katika kambi za kazi ngumu na magereza kwa ajili ya Bwana? Hata kidogo! Nilipobatizwa nikiwa kijana mwenye umri wa miaka 14, tayari nilielewa waziwazi masuala yaliyohusika: ama unampenda Mungu ama unaupenda ulimwengu! Kwa sababu nilikuwa nimeamua kumtumikia Yehova, sikufikiria kamwe kuvunja uaminifu wangu.—Yak. 4:4.
[Picha]
Kushoto: Vasile Ursu
Kushoto kabisa: Vasile na mke wake Emilia, na binti yake, Tamara
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 108-110]
Mvulana Mdogo Mwenye Ua Alinigusa Moyo
Valentina Cojocaru
Alizaliwa: 1952
Alibatizwa: 1997
Maisha yake: Alikuwa mwalimu wakati wa utawala wa Sovieti nchini Moldova, na aliwafundisha watoto kwamba hakuna Mungu.
Mwaka wa 1978, nilikuwa mwalimu katika shule ya watoto wadogo huko Feteşti, Moldova. Sikuamini kwamba kuna Mungu. Katika mkutano mmoja wa walimu, tuliagizwa tujitahidi kuwafundisha watoto wa Mashahidi wa Yehova kwamba hakuna Mungu. Niliona jambo hilo kuwa wazo zuri. Kwa hiyo nilijaribu kubuni njia zenye kuvutia ili kufikia mioyo ya wanafunzi wangu waliokuwa Mashahidi. Nilipata wazo zuri.
Niliwaomba watoto watengeneze matuta mawili ya kupandia maua. Katika tuta moja, watoto wangepanda maua, kuyatilia maji, na kuyapalilia. Lakini hawangelitunza lile tuta lingine. Hilo ni la Mungu, nikawaambia. Mungu atalitunza. Watoto walifurahia kazi hiyo. Walipanda maua, wakayatia maji, na kupalilia tuta lao, huku “shamba dogo la Mungu” likijaa magugu matupu.
Kisha siku moja nzuri yenye jua, niliwakusanya watoto mbele ya matuta hayo mawili. Niliwapongeza kwa jitihada zao nzuri, na baadaye nikasema maneno ambayo nilikuwa nimeyatayarisha vizuri. Niliwauliza hivi: “Je, mnaona kwamba Mungu alipuuza tuta lake? Ni wazi kwamba tuta hili halina mwenyewe.”
Watoto walikubaliana nami kwamba ilionekana hivyo. Kisha nikataja jambo nililotaka kukazia: “Watoto, tuta hili limejaa magugu kwa sababu wanadamu wanawazia tu kwamba kuna Mungu. Kwa hiyo, Mungu angetunzaje maua hayo, na hali hakuna Mungu?”
Nilipokuwa nikiongea, niliwaangalia watoto ili kuona jinsi walivyoitikia. Nilimwona mvulana mdogo, ambaye wazazi wake ni Mashahidi, akishikwa na wasiwasi. Mwishowe hakuweza kujizuia tena. Alikimbia kwenye uwanja uliokuwa karibu, akachuma ua, akaniletea na kusema: “Kama hakuna Mungu ni nani aliyepanda ua hili? Hakuna hata mmoja kati yetu aliyelitunza.” Maneno yake yalinishtua sana. Moyoni mwangu nilijua kwamba maneno ya mtoto huyo yalikuwa yenye kusadikisha kabisa.
Kwa sababu nilikuwa nimelelewa na wazazi Wakomunisti, miaka mingi ilipita kabla sijachukua hatua ya pili, yaani, kujifunza Biblia. Hata hivyo, mwaka wa 1995, niliwaendea Mashahidi na kuomba funzo. Wazia furaha yangu nilipotambua kwamba mmojawapo wa wanafunzi wangu wa zamani sasa alikuwa mwalimu wangu!
Bila shaka serikali ya Kikomunisti ilinipa elimu nzuri. Lakini haikunifundisha masomo ya maana zaidi maishani. Leo, kwa sababu ya Yehova na mvulana huyo mdogo mwenye ujasiri, ninaweza kutumia elimu yangu na ujuzi wangu wa kiroho kuwasaidia wengine kuelewa kwamba kuna Mungu ambaye anawajali sana wanadamu aliowaumba.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 113-115]
Nilizaliwa Uhamishoni
Lidia Sevastian
Alizaliwa: 1954
Alibatizwa: 1995
Maisha yake: Alilelewa na mama Shahidi na baba asiyeamini, lakini hakushirikiana na Mashahidi wa Yehova kwa miaka mingi.
Mama na nyanya yangu walijifunza kweli na kuwa Mashahidi wa Yehova mapema katika miaka ya 1940. Baba alikuwa mtu mwema lakini hakukubali kweli ya Biblia wakati huo. Mwaka wa 1951, Mama alikuwa na watoto wawili na alikuwa na mimba ya mapacha. Yapata mwezi wa Aprili mwaka huo, wenye mamlaka walijaribu kuvunja familia yetu. Baba alipokuwa kazini, Mama, aliyekuwa karibu kujifungua, ndugu na dada zangu walipelekwa kwenye gari-moshi la kwenda Siberia. Hata hivyo, Mama alifaulu kumtumia Baba ujumbe, naye alienda nyumbani haraka. Ijapokuwa hakuwa Shahidi, alipanda gari-moshi na kwenda uhamishoni pamoja na familia yake.
Wakati wa safari ya kwenda Siberia, Mama aliruhusiwa kukatiza safari na kubaki mjini Asino kwa muda mfupi ili ajifungue mapacha. Wengine walilazimika kuendelea na safari hadi wilaya ya Tomsk, ambako Baba alipanga nyumba. Alifanya kazi pamoja na akina ndugu. Majuma machache baadaye, Mama na wale mapacha wachanga walijiunga na familia. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba mapacha hao walikufa kwa sababu ya maisha magumu sana ya familia yetu.
Hata hivyo, watoto wengine wanne walizaliwa uhamishoni, kutia ndani mimi na ndugu yangu pacha. Baba alitutunza sote kwa uaminifu. Hatimaye tuliruhusiwa kurudi nyumbani mwaka wa 1957. Mama aliendelea kutufundisha kupenda kanuni za Biblia, ijapokuwa alipelelezwa sana na polisi wa siri.
Kwa upande mwingine, Baba alihangaikia hasa kuwapa watoto wake elimu bora. Kwa hiyo, nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilijiunga na chuo kikuu huko Chisinau. Baadaye niliolewa na kuhamia Kazakhstan, mbali sana na wazazi wangu na tengenezo la Yehova. Nilirudi Chisinau mwaka wa 1982, na mara moja nilianza kuwatafuta watu wa Yehova, lakini sikufaulu. Kwa miaka minane nilidhani kwamba hakukuwa na mtu mwingine yeyote katika jiji hilo aliyetaka kumwabudu Yehova.
Kisha, siku moja nilipokuwa nikingoja basi, niliwasikia wanawake wawili wakiongea kumhusu Yehova. Nilisonga karibu ili nisikie vizuri zaidi. Wanawake hao walifikiri kwamba mimi ni mpelelezi wa KGB, kwa hiyo walianza kuzungumzia habari nyingine. Walipoondoka niliwafuata, na hilo liliwatia wasiwasi. Kwa hiyo niliwakaribia haraka, na baada ya kuongea nao kwa muda, walisadikishwa kwamba mimi si mpelelezi. Tamaa yangu ya kushirikiana na tengenezo la Yehova ilitimia hatimaye! Hata hivyo, jambo la kusikitisha ni kwamba mume wangu alipinga msimamo wangu.
Tulikuwa na watoto wawili wakati huo. Mwaka wa 1992, nilifanyiwa upasuaji wa uti wa mgongo, kwa hiyo nililazwa hospitalini na sikuweza kutoka kitandani kwa miezi sita. Katika pindi hiyo yenye kushusha moyo, jambo zuri ajabu lilitukia: Mwana wangu Pavel, alichukua msimamo wake upande wa Yehova, akabatizwa mwaka wa 1993 katika kusanyiko la kimataifa huko Kiev. Baada ya muda nilipona kiasi cha kuweza kutembea tena. Kwa hiyo, mwaka wa 1995, mimi pia nilibatizwa ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova.
Leo, watu wengi wa familia yetu ni Mashahidi na ninamshukuru Yehova na mama yangu kwa jambo hilo. Nilikumbuka sikuzote uaminifu wa Mama, na ninafurahi kwamba baba yangu, aliyetutunza kwa uaminifu sana, alikuja kuwa mtumishi wa Yehova kabla ya kifo chake.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 117, 118]
Dhabihu Zetu Si Kitu Zikilinganishwa na za Yehova
Mihai Ursoi
Alizaliwa: 1927
Alibatizwa: 1945
Maisha yake: Aliteswa chini ya utawala wa Wafashisti na Wakomunisti.
Nilianza kuhubiri habari njema mwaka wa 1941. Mwaka wa 1942, nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilikuwa nipate mazoezi ya kijeshi katika shule yetu. Picha za Mfalme Michael wa Rumania, Jenerali Antonescu, na Bikira Mariamu zilikuwa zimetundikwa darasani. Tulipoingia darasani, tulipaswa kupiga magoti mbele ya picha hizo na kufanya ishara ya msalaba. Mimi na vijana wengine wawili tulikataa kupiga magoti.
Polisi walitupiga kikatili kwa sababu ya kukataa. Tulilala shuleni usiku huo. Asubuhi tulipelekwa Corjeuţi ambako tulipigwa tena. Kutoka Corjeuţi, tulipelekwa sehemu mbalimbali, kisha tukatembea kwa miguu umbali wa kilometa 100 hadi mahali ambapo tungehukumiwa katika mahakama ya jeshi. Miguu yangu ilitoka damu kwa sababu ya kutembea sana. Hatimaye niliruhusiwa kurudi nyumbani bila kuhukumiwa, yaelekea kwa sababu ya umri wangu mdogo.
Nilipokuwa na umri wa miaka 18, niliitwa na serikali ya Sovieti nijiandikishe jeshini. Tena nilikataa kuvunja uaminifu wangu na nikapigwa vibaya. Rafiki yangu Gheorghe Nimenco alipigwa pia, naye alikufa majuma sita baadaye kutokana na majeraha aliyopata. Tena niliruhusiwa kurudi nyumbani, nadhani kwa sababu ya umri wangu. Wasovieti walinikamata tena mwaka wa 1947, na wakati huo walitisha kunipiga risasi nisipojiunga na jeshi. Hata hivyo, badala ya kuuawa nilihukumiwa kifungo cha upweke kwa miezi miwili, na baada ya hapo nilipelekwa kufanya kazi kwenye mradi wa kujenga Mfereji wa Volga-Don. Kazi hiyo ilikuwa hatari sana na watu wengi walikufa. Niliponea chupuchupu katika msiba mmoja ambamo watu wengi walikufa na nikarudi nyumbani Moldova.
Nilipokuwa huko nilioa. Mimi na mke wangu Vera, aliyekuwa na mimba, tulihamishwa mwaka wa 1951. Tulisafiri kwanza kwa gari-moshi na baadaye kwa mashua hadi msitu mkubwa sana wa Siberia unaoitwa taiga, ambako nilifanya kazi ya kukata miti. Mimi na Vera tuliishi katika kibanda kimoja pamoja na familia nyingine 16. Tulifurahi tuliporuhusiwa kurudi Moldova mwaka wa 1959.
Mambo kadhaa yameniimarisha katika miaka hiyo migumu na hata sasa. Jambo moja ni imani ya ndugu yangu Ion. (Ona ukurasa wa 89.) Alihukumiwa kifo, lakini alikataa kuvunja uaminifu wake, ijapokuwa hakujua kwamba hukumu yake ingebadilishwa. Ninaimarishwa pia ninapotafakari jinsi ambavyo Yehova amenitunza mimi na mke wangu, tulipovumilia majaribu kwa ajili ya jina lake. Hata hivyo, dhabihu zetu si kitu zikilinganishwa na jinsi ambavyo Yehova alijidhabihu alipomtuma Mwana wake afe kwa ajili yetu. Ninapotafakari dhabihu hiyo ya pekee, ninatiwa nguvu ya kukabili majaribu ya kila siku kwa shangwe.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 121-123]
Yehova Alinitunza kwa Upendo
Mihailina Gheorghiţa
Alizaliwa: 1930
Alibatizwa: 1947
Maisha yake: Alikuwa mjumbe na mtafsiri wakati wa marufuku.
Nilijifunza kweli mwaka wa 1945 na nilifurahia kuhubiri habari njema katika kijiji chetu cha Glodeni, na katika kijiji jirani cha Petrunea. Wakuu wa shule walikataa kunipa cheti cha kuhitimu kwa sababu nilihubiri shuleni. Hata hivyo, nilifurahia kutumia elimu yangu kusaidia kutafsiri magazeti na vitabu vya Biblia kutoka Kirumania na Kiukrainia hadi Kirusi.
Muda mfupi baada ya kubatizwa, nilikamatwa nilipokuwa nikitafsiri na nikahukumiwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu huko Vorkuta, kaskazini ya Mzingo wa Aktiki, ambako niliwapata dada wengine wengi. Licha ya hali ngumu sana, sisi sote tuliendelea kuhubiri. Tulifaulu pia kupata vitabu na magazeti. Na hata tulinakili magazeti na vitabu vingine humo kambini.
Siku moja nilikutana na mwanamke fulani ambaye alikuwa amekamatwa kwa sababu wenye mamlaka walifikiri kimakosa kwamba yeye ni Shahidi. Nilimtia moyo achunguze Neno la Mungu kwa sababu Yehova ana uwezo wa kuweka watu wake huru ikiwa ni mapenzi yake. Hatimaye, alikubali kujifunza Biblia na akawa dada yetu. Muda mfupi baadaye aliachiliwa kabla hajamaliza kifungo chake.
Baadaye nilihamishwa hadi Karaganda, Kazakhstan. Mwishowe, Julai 5, 1956, mimi pia niliachiliwa. Nilihamia Tomsk, ambako nilikutana na kuolewa na Alexandru Gheorghiţa, ambaye alikuwa amefungwa kwa miaka sita kwa sababu ya imani yake. Tuliendelea kuhubiri katika eneo kubwa la Siberia, tukijua kwamba polisi wa siri bado walikuwa wakitupeleleza. Baadaye tulihamia Irkutsk, magharibi mwa Ziwa Baikal. Tuliendelea kunakili vitabu kisiri tukiwa huko. Baadaye tulitumikia Bishkek, Kyrgyzstan. Ijapokuwa tulijihadhari tulipohubiri, Alexandru alikamatwa na kuhukumiwa kifungo cha miaka kumi.
Mwendesha-mashtaka aliniambia kwamba ningeweza kumtembelea Alexandru aliyekuwa gerezani akisubiri kuhukumiwa. Kwa kawaida jambo hilo halikuruhusiwa, kwa hiyo nilimwuliza ni kwa nini alitutendea kwa fadhili hivyo. Aliniambia: “Ninyi ni wenzi wa ndoa wachanga na mna mtoto. Huenda mkafikiria upya uamuzi wenu.” Nilimwambia mwendesha-mashtaka huyo kwamba zamani mimi na Alexandru tuliazimia kumtumikia Yehova kwa uaminifu na bado tunashikilia azimio hilo. Alijibu hivi: “Hata Biblia yenu inasema kwamba mbwa aliye hai ni afadhali kuliko simba aliyekufa.” (Mhu. 9:4) “Ni kweli,” nikamjibu, “lakini mbwa aliye hai ambaye wewe unazungumzia hataurithi ulimwengu mpya wa Mungu.”
Alexandru alifungwa kwa miaka kumi, na kwa mwaka mwingine mmoja alifungwa nyumbani mwake. Baada ya Alexandru kuachiliwa, tulihamia Kazakhstan na kisha Uzbekistan, ili kusaidia katika kazi ya kuhubiri. Hatimaye tulirudi Moldova mwaka wa 1983, tukiwa tumeridhika kwa sababu tulikuwa na pendeleo lisilo na kifani la kuwasaidia watu wenye mioyo minyofu katika sehemu nyingi kumjua Yehova.
Ninapofikiria mambo yaliyopita, ninakubali kwamba maisha yangu hayakuwa rahisi. Lakini hivyo ndivyo ilivyo na watu wasio Mashahidi. Wao pia wamekabili matatizo mengi maishani. Lakini sisi tumeteswa kwa ajili ya habari njema. Kwa hiyo, Yehova ametulinda na kututunza kwa upendo. Zaidi ya hayo, tunajua kwamba baada ya magumu kukoma tutaishi maisha mazuri yenye kuvutia kwa umilele wote.
[Chati/Grafu katika ukurasa wa 80, 81]
MFUATANO WA MATUKIO NCHINI MOLDOVA
1891: C. T. Russell atembelea Kishinev, Bessarabia (sasa ni Chisinau, Moldova).
1895
1921: Ripoti ya mwaka yaonyesha kwamba zaidi ya watu 200 wamekubali kweli ya Biblia.
1922: “Nyumba [ya kwanza] ya mikutano” yajengwa Corjeuţi.
1925: Kazi ya Wanafunzi wa Biblia yapigwa marufuku.
1930
1940: Rumania yasalimisha Bessarabia kwa Muungano wa Sovieti, na jina labadilishwa kuwa SSR ya Moldavia.
1941: Rumania yatwaa Moldova tena. Ufashisti na vita vyasababisha Mashahidi wateswe.
1944: Muungano wa Sovieti wavamia Moldova tena. Mateso yaendelea.
1949: Wasovieti waanza kuwahamisha Mashahidi wa Yehova na wengine.
1951: Stalin aanzisha mpango unaoitwa Operation North.
Miaka ya 1960: KGB yajaribu kusababisha vurugu na migawanyiko miongoni mwa watu wa Mungu.
1965
1989: Mashahidi wapata uhuru wa ibada kwa kadiri kubwa zaidi. Mashahidi kutoka Moldova wahudhuria makusanyiko Poland.
1991: SSR ya Moldavia yabadilishwa jina na kuitwa Jamhuri ya Moldova. Makusanyiko ya Mzunguko ya kwanza yafanywa. Mwangalizi wa eneo la dunia kutoka makao makuu atembelea nchi hiyo kwa mara ya kwanza.
1994: Mashahidi wa Yehova waandikishwa kisheria. Kusanyiko la kwanza la wilaya lafanywa Chisinau.
2000
2000: Betheli mpya huko Chisinau yawekwa wakfu.
2003: Wahubiri watendaji wafikia 18,473 nchini Moldova.
[Grafu]
(See publication)
Jumla ya Wahubiri
Jumla ya Mapainia
20,000
10,000
1895 1930 1965 2000
[Ramani katika ukurasa wa 73]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
UKRAINIA
MOLDOVA
Briceni
Tabani
Lipcani
Şirăuţi
Corjeuţi
Ţaul
Feteşti
Soroca
Bălţi
Petrunea
CHISINAU
Căuşeni
Mto Dniester
Mto Prut
ROMANIA
Iasi
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 66]
[Picha katika ukurasa wa 74]
Ilie Groza, mmoja wa Mashahidi wa kwanza nchini Moldova
[Picha katika ukurasa wa 75]
Tudor Groza
[Picha katika ukurasa wa 78]
Ioana Groza
[Picha katika ukurasa wa 92]
Parfin Palamarciuc na mwana wake Nicolae
[Picha katika ukurasa wa 93]
Vasile Gherman
[Picha katika ukurasa wa 94]
Nicolae Anischevici
[Picha katika ukurasa wa 95]
Maria Gherman
[Picha katika ukurasa wa 96]
Mabehewa ya mizigo yaliyotumiwa kuwahamisha Mashahidi hadi Siberia
[Picha katika ukurasa wa 98]
Ivan Mikitkov
[Picha katika ukurasa wa 99]
Constantin Şobe
[Picha katika ukurasa wa 107]
Nicolai Voloşanovschi na kijitabu “Double Bottom”
[Picha katika ukurasa wa 111]
Gheorghe Gorobeţ
[Picha katika ukurasa wa 126]
Jumba la Kusanyiko huko Feteşti
[Picha katika ukurasa wa 131]
Halmashauri ya nchi ya Moldova, kuanzia kushoto: David Grozescu, Anatolie Cravciuc, na Tiberiu Kovacs