Urusi
“TANGU kuchomoza kwa jua mpaka kutua kwake jina langu litakuwa kuu kati ya mataifa.” (Mal. 1:11) Unabii huo wenye kustaajabisha uliotolewa na Yehova miaka 2,450 hivi iliyopita unatimizwa leo huko Urusi. Jua linapotua kwa watumishi washikamanifu wa Yehova katika jiji la Kaliningrad lililo magharibi mwa Urusi, tayari wahubiri wanaoishi kwenye Rasi ya Chukchi, ambayo iko kwenye Mlango-Bahari wa Bering unaotenganisha rasi hiyo na Alaska, huliona likichomoza. Kwa kweli, wakati wowote ule kuna watu wanaohubiri Ufalme na kufanya wanafunzi huko Urusi. Yehova alibariki sana bidii ya ndugu na dada wenye ujasiri wakati wa utawala wa Kisovieti. Kama tutakavyoona, ndugu hao walivumilia mateso makali na kwa kufanya hivyo wakaweka msingi uliowezesha kuwe na wahubiri zaidi ya 150,000 huko Urusi leo.
Urusi, ambayo sasa inaitwa “Shirikisho la Urusi,” si nchi ya taifa moja au jamii moja. Kama jina lake linavyoonyesha, ni shirikisho la mataifa, mchanganyiko wa makabila, lugha, na jamii nyingi, kila moja ikiwa na utamaduni wake wa pekee. Masimulizi yetu hayaanzi katika demokrasia ya Urusi ya leo bali katika Milki ya Urusi yenye mchanganyiko wa makabila, lugha, na dini nyingi, iliyokuwapo zaidi ya miaka 100 iliyopita ambayo ilitawaliwa na maliki.
KUWAHUBIRIA KWA UJASIRI VIONGOZI WA KIDINI HUKO MOSCOW
Wakati wa mwamko wa kidini, Semyon Kozlitsky, mwanamume mcha-Mungu aliyehitimu katika seminari ya Kanisa Othodoksi alikutana na Charles Taze Russell, ambaye alikuwa akisimamia kazi ya Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Nina Luppo, mjukuu wa Semyon alieleza hivi: “Babu yangu alienda Marekani mwaka wa 1891 na kukutana na Ndugu Russell. Alikuwa na picha waliyopigwa pamoja na kila mara alikuwa akisema kwamba Ndugu Russell alikuwa ndugu yake.” Mwishoni mwa miaka ya 1800, Ndugu Russell na wenzake walikuwa wakiongoza kazi ya kurudisha ibada ya kweli kwa kufundisha kweli za Biblia zilizobadili maisha ya watu. Kazi hiyo ilihusisha kufunua mafundisho ya uwongo ya dini zinazodai kuwa za Kikristo na walimu wake wa uwongo. Kweli ya Biblia pamoja na bidii kwa ajili ya ibada safi iliyoonyeshwa na Ndugu Russell na wenzake ilimchochea Semyon awahubirie kwa ujasiri viongozi wa kidini huko Moscow. Matokeo yalikuwa nini?
“Bila kufikishwa mahakamani, babu yangu alipelekwa uhamishoni huko Siberia akiwa amefungwa minyororo kwa madai ya kwamba alimtukana askofu mkuu wa Moscow,” asema Nina, “na kwa njia hiyo ujumbe wa Biblia ukafika Siberia mwaka wa 1891.” Mwishowe, Semyon Kozlitsky alipelekwa sehemu ya Siberia ambayo leo ni sehemu ya Kazakhstan. Akiwa huko, alihubiri neno la Mungu kwa bidii mpaka alipokufa mwaka wa 1935.
‘HAKUNA UWEZEKANO WA KWELI KUKUA HUKO URUSI’
Ndugu Russell alitembelea Urusi kwa mara ya kwanza mwaka ambao Semyon Kozlitsky alipelekwa uhamishoni. Kuhusu ziara hiyo, maneno yake “tuliona hakuna hali zinazofaa au uwezekano wa kweli kukua huko Urusi” hunukuliwa mara kwa mara. Je, alimaanisha kwamba watu huko hawakutaka kusikia kweli? Hapana. Serikali ya kidikteta iliwazuia watu kusikia kweli.
Akieleza jinsi hali ilivyokuwa, Ndugu Russell aliandika hivi katika toleo la Machi 1, 1892, la Zion’s Watch Tower: “Huko Urusi, serikali hudhibiti kabisa utendaji wa kila mtu, na mgeni yeyote anayeingia katika nchi hiyo hutiliwa shaka. Lazima aonyeshe pasipoti yake katika kila hoteli na kituo cha gari-moshi kabla ya kuingia au kutoka kwenye jiji au mji wowote. Wenye hoteli huchukua pasipoti yako na kumpa Mkuu wa Polisi, ambaye huiweka mpaka unapotaka kutoka nchini. Wao wanafanya hivyo ili iwe rahisi kujua ni lini mgeni aliingia na kutoka nchini. Maofisa na wenye mamlaka hukutendea kwa heshima, lakini si wenye urafiki, na wanakuonyesha hawafurahii kwamba uko nchini humo. Vitabu au karatasi zozote ulizobeba huchunguzwa kwa makini ili kuhakikisha kwamba hazipingani na mipango yao ya kisiasa.”
Huenda ikaonekana kwamba chini ya hali hizo, kazi ya kuhubiri habari njema haingefanikiwa sana. Hata hivyo, mbegu za kweli hazingeweza kuzuiwa kuota huko Urusi.
“SIKU YA MAMBO MADOGO” YAANZA
Mapema sana katika 1887, Zion’s Watch Tower liliripoti kwamba matoleo ya gazeti hilo yalikuwa yametumwa sehemu mbalimbali, “kutia ndani Urusi.” Mnamo 1904, barua kutoka kwa kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia huko Urusi ilisema kwamba walipokea vichapo vya Biblia, ingawa kwa shida. Barua hiyo ilieleza hivi: ‘Vichapo hivyo vilikuwa vinaonekana waziwazi na karibu wachunguzi wa serikali wavizuie kuingizwa nchini.’ Kikundi hicho kilithamini sana kupokea vichapo hivyo hivi kwamba walisema, “Ni kama dhahabu hapa kwa kuwa ni vigumu sana kuvipata.” Wakionyesha kwamba walielewa kusudi la vichapo hivyo, waliandika hivi: “Bwana na atubariki na kutupa nafasi ya kugawanya vichapo hivi.”
Kazi ya kuhubiri habari njema ilikuwa imeanza Urusi kwa bidii, na ibada ya kweli ilikuwa imeanza kutia mizizi midogo lakini yenye nguvu. Huo ulikuwa mwanzo mdogo. Hata hivyo, kama nabii Zekaria alivyoandika, “ni nani ameidharau siku ya mambo madogo?”—Zek. 4:10.
Katika miaka iliyofuata, ndugu wenye bidii huko Ujerumani walituma vichapo Urusi. Vichapo vingi vilikuwa katika Kijerumani, na watu wengi wanaozungumza Kijerumani wakawa Mashahidi. Mnamo 1907, washiriki wa kanisa la Baptisti la Ujerumani huko Urusi walitumiwa mfululizo wa vitabu Millennial Dawn. Washiriki 15 kati yao walipojiunga na ibada ya kweli, kanisa liliwatenga na ushirika. Baadaye, kiongozi wa kanisa hilo aliyewapinga alikubali kweli zilizokuwa katika kitabu Millennial Dawn.
Katika mwaka wa 1911, wahubiri huko Urusi walipata msaada usiotazamiwa kutoka kwa wenzi wawili walioenda huko baada ya arusi. Baada ya kufunga ndoa, akina Herkendell, wenzi wawili Wajerumani, walisafiri hadi Urusi ili kuwahubiria watu wanaozungumza Kijerumani. Walifurahi sana walipopata vikundi vya wahubiri wa Ufalme na wakawasaidia kiroho.
Mapema, msomaji mmoja huko Urusi aliandika hivi: “Ninathamini sana vichapo kutoka Ujerumani kama vile wana wa Israeli walivyothamini mana kutoka mbinguni. . . . Lakini tunasikitika sana kwamba vichapo hivyo havipatikani katika Kirusi! Mimi hutumia kila nafasi kutafsiri vichapo mbalimbali katika Kirusi.” Kazi ya kutafsiri ilikuwa imeanza; kazi zaidi ya utafsiri ingefanywa.
“WATU WENGI WANATAKA KUMJUA MUNGU”
Mnamo 1911, R. H. Oleszynski, ndugu kutoka Warsaw, Poland, ambayo sehemu yake wakati huo ilikuwa chini ya Milki ya Urusi, alifanya mipango ili trakti Wafu Wako Wapi? kichapishwe katika Kirusi. Alisema hivi katika barua aliyomwandikia Ndugu Russell: “Ninatuma nakala moja . . . Nakala 10,000 ziligharimu rubo 73 (pesa za Urusi) . . . Kuna matatizo mengi, hata hivyo watu wengi wanataka kumjua Mungu.” Watu wanaozungumza Kirusi walipewa trakti hizo pamoja na vichapo vingine, nao walivipeleka Urusi. Kwa njia hiyo, hatua ya maana ilikuwa imechukuliwa kuelekea kutafsiri vichapo katika lugha mpya ya eneo hilo. Baada ya muda mfupi vichapo vingine, yaani, trakti, broshua, na vijitabu vikaanza kuchapishwa. Baada ya muda, akina ndugu walijikaza kutafsiri vichapo vingi na vikubwa kama vile vitabu.
Katika 1912, Ndugu Russell alitembelea Finland, ambayo wakati huo ilikuwa sehemu ya Milki ya Urusi. Kaarlo Harteva, alipewa mamlaka ya kisheria kuwakilisha Watch Tower Bible and Tract Society huko Finland. Septemba 25, 1913, Mwakilishi wa Milki ya Urusi huko New York, aliweka sahihi yake na kutia muhuri wa serikali kwenye hati hiyo ya mamlaka ya uwakilishi.
SAFARI YA MIEZI MIWILI YA KUHUBIRI INAKUWA NDEFU ZAIDI
Muda mfupi kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Joseph F. Rutherford aliondoka Brooklyn na kuanza safari ya kutembelea nchi mbalimbali akiwa mwakilishi wa tengenezo. Wakati wa ziara hiyo, alikutana na Mwanafunzi wa Biblia aliyeitwa Dojczman katika jiji la Lodz huko Poland. Muda mfupi baadaye, Ndugu Dojczman pamoja na familia yake walifunga safari ya kwenda kuhubiri kotekote Urusi. Safari hiyo ilikusudiwa kuwa ya miezi miwili tu, lakini ikawa ndefu zaidi vita vilipoanza.
Baada ya kupitia hali nyingi ngumu, familia ya Dojczman ilihamia mji mdogo kando ya Mto Volga. Kufikia 1918, waliamua kurudi Poland, lakini mlipuko wa ugonjwa wa ndui ukawazuia. Baada ya hilo, mipaka ilifungwa kwa sababu ya kutokea kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe. Watoto wao watatu walikufa wakati huo, mmoja kutokana na ndui, mwingine nimonia, na mwingine kutokana na sababu nyingine.
Kulikuwa na njaa na woga kila mahali. Barabara zilikuwa na maiti za watu waliokufa kutokana na njaa. Mvurugo uliosababishwa na hali hizo ulifanya watu wengi, hasa wageni wauawe hata bila kufikishwa mahakamani kwa madai ya kushirikiana na “adui.” Siku moja, mwanamume mmoja aliyeambatana na askari mwenye silaha waliingia nyumbani kwa Dojczman kwa nguvu.
“Huyu ni adui, mshike!” mwanamume huyo akapaaza sauti.
“Kwani amefanya nini?” askari akauliza.
Kumbe mwanamume huyo alikuwa amepanga njama ili asimlipe Ndugu Dojczman deni la vitu fulani alivyokuwa amemtengenezea. Baada ya kusikiliza pande zote mbili, askari huyo alitambua kuwa madai ya mtu huyo ni ya uwongo na akamtupa nje. Kisha askari huyo akamwambia Ndugu Dojczman kwamba anakumbuka habari fulani ya Biblia waliyokuwa wamezungumzia pamoja. Huenda mazungumzo hayo ndiyo yaliyookoa maisha ya Ndugu Dojczman na familia yake. Mnamo 1921, serikali ya Kikomunisti ilizima uasi wa kijeshi na kukomesha vita vya wenyewe kwa wenyewe. Baada ya hayo, familia ya Dojczman ilifunga safari kurudi Poland.
WANAFUNZI WA BIBLIA NA UTAWALA WA BOLSHEVIKI
Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipokuwa vikipamba moto, mawasiliano kati ya ndugu wa Urusi na wale wa sehemu nyingine yalikatizwa. Kama ndugu wengine wa Kristo ulimwenguni pote, huenda ndugu wa Urusi hawakujua maana kamili ya kutawazwa kwa Kristo. Hawakuwa na habari kwamba karibuni nchi yao ingepatwa na matukio fulani ya maana sana katika karne ya 20, mengi ya matukio hayo yakiwa utimizo wa unabii wa Biblia.
Mwishoni mwa 1917, Mapinduzi ya Urusi yalikomesha utawala wa miaka 370 wa maliki. Pasipo kutambua kuwapo kwa Bwana Yesu Kristo, Wabolsheviki, ambao ndio waliokuwa watawala wapya wa Urusi, walikuwa na mipango ya kuanzisha serikali mpya, ambayo ingekuwa tofauti na zile nyingine zote za wakati uliopita. Kwa hiyo, katika muda wa miaka michache tu, Muungano wa Jamhuri za Kisoshalisti za Sovieti, au USSR, ukaundwa. Hatimaye, muunganohuo ungemiliki karibu asilimia 17 ya eneo lote la dunia.
Inafaa kujua kwamba miaka michache kabla ya yale Mapinduzi ya Urusi, Vladimir Lenin, kiongozi wa kwanza wa Muungano wa Sovieti alisema hivi: “Kila mtu anapaswa kuwa huru kabisa kuwa mshiriki wa dini yoyote ile, na pia kuwaambia wengine kuhusu dini hiyo na kubadili dini. Mtu yeyote mwenye mamlaka hana haki ya kumuuliza mtu kuhusu dini yake: huo ni uamuzi wa mtu binafsi na mtu mwingine hana haki ya kuingilia.”
Katika sehemu fulani za nchi hiyo, kanuni hizo rasmi za Chama cha Kisoshalisti cha Kidemokrasia ziliwaruhusu watu wanyoofu kuwaambia wengine kweli za Biblia. Lakini kwa ujumla, Serikali hiyo mpya ambayo haikuamini kwamba kuna Mungu ilichukia dini ambayo waliiita “kasumba ya watu.” Kati ya hatua za kwanza ambazo Wabolsheviki walichukua ni ile ya kutoa amri ya kutenganisha Kanisa na Serikali. Mafundisho ya kidini yalipigwa marufuku, na mali ya kanisa ikawa ya taifa.
Serikali hiyo mpya ingekuwa na maoni gani kuelekea vikundi vilivyotawanyika vya Wanafunzi wa Biblia, ambao walionyesha ushikamanifu wao kwa Ufalme wa Mungu? Akiandika kutoka Siberia muda fulani baada ya yale mapinduzi ya 1917, Mwanafunzi mmoja wa Biblia alieleza jambo hili lenye kuhuzunisha: “Huenda mnajua hali ilivyo hapa Urusi. Tuna serikali ya Sovieti iliyo na mipango ya Kikomunisti. Ingawa ni kweli kwamba mtu anaweza kuona kwamba wanajikaza kuleta usawa, jambo lolote linalohusiana na Mungu linatupiliwa mbali.”
Kufikia 1923, upinzani dhidi ya Wanafunzi wa Biblia uliongezeka. Akina ndugu waliandika hivi: “Barua hii imeandikwa kwa kusudi la kuwajulisha jinsi hali ilivyo Urusi. . . . Tuna mahitaji ya lazima, yaani, chakula, mavazi, . . . lakini tunahitaji sana chakula cha kiroho. Vitabu vilivyotumwa vimechukuliwa na serikali. Kwa hiyo tunawasihi mtutumie kupitia barua visehemu vidogo-vidogo vya vichapo vyote vinavyopatikana katika Kirusi . . . Wengi wana njaa ya Neno la Kweli. Muda mfupi uliopita, watu watano walionyesha wakfu wao kwa kubatizwa katika maji, na Wabaptisti kumi na watano wamejiunga nasi pia.”
Toleo la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1923, lilisema hivi: “Sosaiti inajaribu kuingiza vichapo Urusi na itaendelea kujitahidi kufanya hivyo, kwa neema ya Bwana.” Kufikia 1925, Mnara wa Mlinzi lilikuwa likipatikana katika Kirusi. Matokeo yake yalionekana mara moja katika kazi ya kuhubiri huko Urusi. Kwa mfano, mshiriki mmoja wa kikundi cha Kievanjeli alishindwa kuelewa jinsi ambavyo Mungu mwenye upendo angeweza kuwatesa watu katika moto wa mateso. Alipowauliza waumini wenzake, walisali kwamba Mungu amwokoe kutokana na mawazo hayo. Baadaye, yeye na mke wake walipewa matoleo ya Mnara wa Mlinzi na mara moja wakatambua kwamba yanasema kweli. Aliandika barua akiomba vichapo zaidi na kusema: “Tunangojea mana kutoka ng’ambo ya bahari.” Ndugu wengine pia huko Urusi walisema kwamba walipokea “mana” hiyo na kuwashukuru ndugu wa Marekani kwa upendo wao wa Kikristo ambao wameonyesha kwa kuchapisha vichapo hivyo vyenye kuimarisha imani.
“NITUMIENI NAKALA MOJAMOJA ZA KILA KITABU”
Barua yenye kugusa moyo kutoka Siberia ilichapishwa katika Mnara wa Mlinzi la Septemba 1925. Mwalimu mmoja kutoka familia maskini alieleza kwamba yeye na familia yake walihamia Siberia kutoka kusini mwa Urusi mwaka wa 1909. Aliandika kwamba alifurahia kusoma vichapo, kisha akaongezea, “Tamaa yangu ya kutoka moyoni ni kuelewa kwa undani kweli takatifu za Mungu ili niwe na uwezo na nguvu zaidi za kupigana dhidi ya giza.” Alimalizia barua yake kwa kuomba vichapo zaidi, akisema, “Tafadhali nitumieni nakala mojamoja za kila kitabu.”
Jibu la mhariri lilichapishwa katika toleo hilohilo. “Kwa muda fulani, tumejaribu kutuma vichapo Urusi, lakini hatujafanikiwa kwa sababu ya upinzani wa serikali ya Urusi. Barua hii, pamoja na nyingine kama hiyo, ni kama mwito kutoka Makedonia: ‘Vuka . . . utusaidie.’ (Mdo. 16:9) Tutakuja kuwasaidia mara tu nafasi inapojitokeza na ikiwa ni mapenzi ya Bwana.”
Kwa kweli, Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vilitimiza sehemu kubwa katika kuhubiriwa kwa habari njema “kuwa ushahidi” katika Kirusi! (Mt. 24:14) Kufikia mwaka wa 2006, idadi ya nakala za vichapo vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova huko Urusi ilifikia 691,243,952, idadi ambayo inapitwa tu na vichapo vya Kihispania, Kiingereza, na Kireno. Yehova amebariki sana bidii ya Mashahidi wake ya kutangaza Ufalme.
KUWAHUBIRIA WARUSI WANAOISHI KATIKA NCHI NYINGINE
Wabolsheviki walipotwaa mamlaka na kuunda Serikali ya Kikomunisti, Warusi wengi walihamia nchi nyingine. Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vya Kirusi vilichapishwa nje ya Muungano wa Sovieti. Kwa njia hiyo, serikali ya Sovieti haingeweza kuzuia kutolewa kwa chakula cha kiroho katika nchi nyingine. Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1920, vichapo vya Kirusi vilikuwa vikiwafikia watu kotekote duniani, na Warusi kutoka Australia, Finland, Latvia, Marekani, Paraguai, Poland, Ufaransa, na Uruguai walituma barua za shukrani.
Mwishowe, ndugu walifanya mipango ili kuwe na mikutano ya Kikristo na kazi ya kuhubiri ifanywe katika Kirusi katika baadhi ya nchi hizo. Huko Marekani, hotuba za Biblia katika Kirusi zilitolewa kwa ukawaida kupitia vituo vya redio. Makutaniko ya Kirusi kama lile lililoko Brownsville, Pennsylvania, yalianzishwa, na makusanyiko yakafanywa. Kwa mfano, katika Mei 1925, akina ndugu walifanya kusanyiko la wilaya la siku tatu katika Kirusi huko Carnegie, Pennsylvania. Watu 250 walihudhuria, na 29 wakabatizwa.
HALI INABADILIKA
Baada ya kifo cha Lenin, serikali ilizidisha mashambulizi dhidi ya dini zote. Mnamo 1926, Shirika la Watu Wanaoamini Hakuna Mungu lilianzishwa. Jina la shirika hilo lilionyesha wazi makusudi yake. Propaganda za kwamba hakuna Mungu zilizoenezwa zilikusudiwa kuondoa kabisa katika mioyo na akili za watu imani katika Mungu. Punde si punde, imani ya kutokuwapo kwa Mungu ilienea kotekote katika eneo hilo kubwa la Muungano wa Sovieti. Mwanafunzi mmoja wa Biblia aliandika hivi katika barua aliyotuma kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote: “Vijana wanakuwa na roho hiyo ya kutomwamini Mungu, na bila shaka hicho ni kizuizi kikubwa cha kujifunza kweli.”
Shirika hilo lilichapisha vichapo kuhusu kutokuwapo kwa Mungu, kutia ndani gazeti lililoitwa Antireligioznik. Mnamo 1928, gazeti hilo lilitangaza hivi: “Wilaya ya Voronezh imejaa madhehebu.” Kati ya madhehebu hayo, lilitaja ‘Wanafunzi 48 wa Maandiko Matakatifu’ ambao “viongozi wao walikuwa Zinchenko na Mitrofan Bovin.” Inapendeza kujua kwamba Mnara wa Mlinzi la Septemba 1926 lilikuwa na barua kutoka kwa Mikhail Zinchenko wa Urusi. Aliandika hivi: “Watu wana njaa ya kiroho. . . . Tuna vichapo vichache sana. Ndugu Trumpi na wengine wanatafsiri na kunakili vichapo vya Kirusi, na kwa njia hiyo tunajilisha kiroho na kutiana moyo. Tunawatumia salamu kutoka kwa ndugu wote huku Urusi.”
Mnamo Septemba 1926, Ndugu Trumpi aliandika kwamba huenda serikali ikaruhusu ndugu wapokee vichapo vya Kirusi. Aliwaomba ndugu wa Betheli ya Brooklyn watume trakti, vijitabu, vitabu, na mabuku ya Mnara wa Mlinzi kupitia ofisi ya tawi ya Ujerumani, huko Magdeburg. Kwa kuitikia ombi hilo, Ndugu Rutherford alimtuma George Young, ambaye alifika Moscow Agosti 28, 1928 (28/8/1928). Katika moja ya barua zake, Young aliandika: “Nimeona mambo mengi yenye kupendeza lakini sijui nitaruhusiwa kukaa hapa kwa muda gani.” Ingawa alifanikiwa kukutana na ofisa wa cheo cha juu huko Moscow, alipata viza iliyomruhusu kuwa nchini humo mpaka Oktoba 4, 1928 tu.
Wakati huohuo, Serikali mpya ya Sovieti haikuwa imetangaza waziwazi msimamo wake kuhusu dini. Hati mbalimbali za serikali zilionyesha kwamba serikali ilitaka vikundi vya kidini viwe sehemu ya wafanyakazi wa serikali. Katika miaka iliyofuata, serikali ilisisitiza jambo hilo. Ni jambo la maana kuelewa kwamba serikali ya Sovieti haikutaka kuwaua watu wa Yehova; ilitaka kugeuza akili na mioyo yao. Ilitaka kuwasadikisha watu wa Mungu watii sera za Kisovieti, kuwalazimisha wawe washikamanifu tu kwa Serikali. Haikutaka kamwe wawe waaminifu kwa Yehova.
Baada ya Ndugu Young kuondoka, ndugu huko Urusi waliendelea kuhubiri kwa bidii kuhusu Ufalme wa Mungu. Danyil Starukhin aliwekwa rasmi asimamie kazi ya kuhubiri Ufalme huko Urusi. Ili kuendeleza kazi hiyo na kuwatia moyo akina ndugu, Ndugu Starukhin alitembelea Moscow, Kursk, Voronezh, na majiji mengine huko Urusi na pia Ukrainia. Akiwa na ndugu wengine, aliwahubiria Wabaptisti katika nyumba zao za sala, akawafafanulia kweli kuhusu Yesu Kristo na Ufalme wa Mungu. Januari 1929 ndugu huko Urusi walifanya mipango ya kupangisha jengo la kanisa huko Kursk kwa dola 200 kwa mwaka ili waweze kuwa na mikutano ya watu wote.
Baadaye mwaka huo, ndugu wa Betheli ya Brooklyn waliomba Wizara ya Biashara ya Muungano wa Urusi iwaruhusu kuingiza nchini vichapo vichache vya Biblia. Vichapo hivyo vilitia ndani nakala 800 za kitabu The Harp of God, nakala 800 za kitabu Deliverance, na pia vijitabu 2,400. Miezi miwili hivi baadaye, vichapo hivyo vilirudishwa vikiwa na muhuri uliosema: “Vimerudishwa kwa sababu vimekataliwa na Msimamizi wa Bidhaa Zilizochapishwa.” Hata hivyo, ndugu hao hawakuvunjika moyo. Wengine walidhani kwamba vichapo hivyo vilirudishwa kwa sababu vilikuwa vimeandikwa katika Kirusi cha kale. Tangu wakati huo, akina ndugu walihakikisha kwamba vichapo vyote vya Kirusi vilitafsiriwa kwa usahihi na kuchapishwa kulingana na muundo wa karibuni wa lugha hiyo.
UHITAJI WA TAFSIRI BORA
Kuanzia 1929, matoleo kadhaa ya Mnara wa Mlinzi yalitangaza kwamba kuna uhitaji wa watafsiri stadi ambao wanaelewa Kiingereza na Kirusi vizuri. Kwa mfano, toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 1930 lilikuwa na tangazo hili: “Ndugu anayestahili ambaye amejiweka wakfu, anayejua Kiingereza na anazungumza Kirusi kwa ufasaha anahitajiwa kutafsiri kutoka Kiingereza hadi Kirusi.”
Yehova aliona uhitaji huo, na watafsiri walipatikana katika nchi mbalimbali. Mmoja wao alikuwa Aleksandr Forstman, ambaye katika mwaka wa 1931 alikuwa tayari akituma makala alizotafsiri katika Kirusi kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote kupitia ofisi ya tawi ya Denmark huko Copenhagen. Ndugu Forstman alikuwa mtafsiri mwenye bidii ambaye aliishi Latvia. Alikuwa na elimu na alielewa Kiingereza na Kirusi vizuri sana hivyo angeweza kutafsiri vichapo vya Biblia haraka. Mwanzoni, alitumia saa chache tu kila juma kutafsiri, kwa kuwa alifanya kazi ya kimwili ili kumwandalia riziki mke wake ambaye hakuwa Shahidi na mtoto wao mmoja. Mnamo Desemba 1932, Ndugu Forstman, alianza kutumia wakati wake wote kutafsiri. Alitafsiri trakti, vijitabu, na vitabu. Alikufa mwaka wa 1942.
Ndugu walikuwa makini sana kutokeza tafsiri bora kabisa ya Kirusi ya vichapo vilivyokuwapo, kwa kuwa walisadiki kwamba muda si muda kazi ya Ufalme ingeandikishwa kisheria Urusi. William Dey, msimamizi wa Ofisi ya Ulaya Kaskazini alimwandikia hivi Ndugu Rutherford: “Marufuku itakapoondolewa Urusi, na hilo litatukia hivi karibuni, ingefaa kuwa na vichapo vilivyotafsiriwa vizuri ili kuvigawa kwa wakaaji milioni 180.”
VIPINDI VYA REDIO
Redio ilitumiwa pia kueneza habari njema katika eneo kubwa la Urusi. Mnara wa Mlinzi la Februari 1929 lilikuwa na tangazo hili: “Hotuba katika Kirusi zitatolewa katika redio.” Vipindi hivyo vilitangazwa kuanzia Estonia hadi Muungano wa Sovieti siku ya Jumapili kila baada ya majuma mawili.
Ndugu Wallace Baxter, msimamizi wa tawi la Estonia alikumbuka hivi baadaye: “Baada ya mazungumzo marefu, makubaliano ya mwaka mmoja yalitiwa sahihi mwaka wa 1929. Punde baada ya vipindi kuanza kutangazwa katika Kirusi, tulifahamishwa kwamba watu huko Leningrad walikuwa wakivisikiliza. Serikali ya Sovieti na viongozi wa kidini huko Estonia waliwaonya watu wasisikilize ujumbe huo wa Ufalme.” Katika 1931, hotuba hizo zilitangazwa katika Kirusi kwenye redio kuanzia saa 11:30 mpaka 12:30 jioni, wakati ambapo wasikilizaji wengi walikuwa nyumbani. Vipindi hivyo vilisimamishwa Juni (Mwezi wa 6) 1934, baada ya kutangazwa kwa miaka mitatu na nusu. Barua kutoka ofisi ya tawi ya Estonia ilieleza sababu ya marufuku hiyo. Ilisema hivi: “Viongozi wa kidini waliiambia serikali [ya Estonia] kwamba hotuba zetu zinazotolewa kupitia redio haziungi mkono Serikali kwa kuwa zina propaganda za Wakomunisti na wale wanaopinga serikali.”
MABADILIKO YAFANYWA
Mnamo 1935 ndugu wa Betheli ya Brooklyn walimtuma Anton Koerber katika Muungano wa Sovieti, wakitumaini kwamba ataanzisha ofisi ya tawi huko. Walitaka kutuma mashini ya kuchapishia nchini humo. Mashini hiyo ingetoka Ujerumani, ambako Adolf Hitler alikuwa tu ameingia mamlakani. Ingawa mpango huo haukufanikiwa, Ndugu Koerber alikutana na ndugu kadhaa huko Urusi.
Kwa miaka mingi, kulikuwa na maendeleo machache katika kazi ya kuhubiri Ufalme huko Urusi. Vichapo vya Biblia vilitafsiriwa katika Kirusi chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Latvia. Lakini ilikuwa vigumu kuingiza vichapo hivyo Urusi. Vichapo vingi vilitwaliwa na kuwekwa kwenye stoo.
Kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu mwaka wa 1939, kulikuwa na Mashahidi wachache sana. Hivyo serikali ya Sovieti haikujishughulisha nao. Lakini sasa mambo yangebadilika. Muda mfupi baada ya Ujerumani ya Nazi kushambulia Poland mwaka wa 1939, Muungano wa Sovieti ulinyakua jamhuri 4 za mwisho kati ya jamhuri zake 15, yaani, Estonia, Latvia, Lithuania, na Moldova. Ghafula, maelfu ya Mashahidi wakajikuta chini ya Muungano wa Sovieti, nchi ambayo muda si muda ingeingia katika vita vikali vya kufa na kupona. Vita hivyo vingesababisha mateso na hali ngumu kwa watu wengi sana. Huo ungekuwa wakati wa Mashahidi wa Yehova kuonyesha ushikamanifu wao kwa Mungu chini ya mateso makali.
WAJITAYARISHA KUSIMAMA IMARA
Ujerumani ilishambulia vikali Muungano wa Sovieti Juni 1941, shambulizi ambalo lilimshtua sana Joseph Stalin, kiongozi wa Sovieti. Kufikia mwisho wa mwaka huo, majeshi ya Ujerumani yalikuwa yamefika vitongoji vya Moscow, na Muungano wa Sovieti ulielekea kushindwa.
Akiwa na hofu nyingi, Stalin alijitahidi kutayarisha taifa lake kwa pambano ambalo Warusi waliliita Vita Vikuu vya Kizalendo. Stalin alitambua kwamba angehitaji kulirudishia kanisa mapendeleo fulani ili mamilioni ambao bado walikuwa wafuasi wa dini wamwunge mkono katika vita hivyo. Mnamo Septemba 1943, Stalin akiwa Kremlin (makao makuu ya serikali ya Urusi) alipokea hadharani viongozi watatu wa cheo cha juu wa Kanisa Othodoksi la Urusi. Hilo lilisaidia kuziba uhasama uliokuwepo kati ya Kanisa na Serikali na makanisa mengi yakafunguliwa kwa ajili ya watu wote.
Kama Mashahidi wa Yehova huko Ujerumani, ndugu nchini Urusi walidumisha msimamo wa kutounga mkono upande wowote wakati wa vita hivyo. Walikuwa tayari kuadhibiwa, na waliazimia kushika sheria ya Bwana wao. (Mt. 22:37-39) Kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote, Mashahidi wa Yehova zaidi ya elfu moja kutoka Ukrainia, Moldova, na jamhuri za Baltiki walipelekwa kwenye kambi za kazi ngumu zilizokuwa katikati mwa Urusi kuanzia 1940 mpaka 1945.
Vasily Savchuk anakumbuka hivi: “Nilibatizwa Ukrainia mnamo 1941 nikiwa na umri wa miaka 14. Wakati wa vita, karibu ndugu wote walipelekwa gerezani au kwenye kambi zilizokuwa katikati ya Urusi. Lakini kazi ya Yehova haikusimama. Dada waaminifu na vijana kama mimi tuliongoza mikutano na huduma. Katika kijiji chetu, kulikuwa na ndugu mmoja ambaye hakuwa ameshikwa kwa kuwa alikuwa mgonjwa. Aliniambia: ‘Vasily, tunahitaji msaada wako. Tuna kazi ya maana ya kufanya na hatuna wanaume wa kutosha.’ Nililia nilipoona jinsi ndugu huyo mgonjwa alivyohangaikia kazi ya Yehova. Nilikubali kufanya lolote lile ambalo lilihitaji kufanywa. Tulijitengenezea mashini za kuchapisha na kuziweka kwenye vyumba vya chini ya ardhi ambapo tulichapisha chakula muhimu cha kiroho. Kisha tukagawa chakula hicho kwa akina ndugu, hasa wale waliokuwa gerezani.”
Ijapokuwa dada na vijana hao walijidhabihu wakichochewa na upendo, chakula hicho cha kiroho hakikutosha. Msaada ulitolewa na ndugu wa Poland waliokuwa wakirudi makwao kutoka Urusi ambao walieleza ofisi ya tawi ya Poland kuhusu hali hiyo. Ndugu Warusi na Waukrainia waliokuwa wakiingia Urusi walibeba chakula cha kiroho, stensili zenye nta, wino, na vifaa vingine.
“WAENDE KILA MMOJA MAHALI PAKE”
Mnamo 1946, ndugu fulani waliokuwa wakiishi Poland walilazimishwa wahamie Sovieti ya Ukrainia. Ivan Pashkovsky anasimulia hivi: “Ndugu waliomba ofisi ya tawi huko Lodz mwongozo kuhusu jambo hilo. Jibu walilopata lilinukuu andiko la Waamuzi 7:7 ambalo linasema: ‘Waende kila mmoja mahali pake.’ Miaka mingi baadaye nilielewa jinsi ambavyo kwa hekima, Yehova aliongoza kazi ya kuhubiri katika maeneo hayo yenye hali ngumu. Tulitambua kwamba ‘mahali’ petu ni popote pale Yehova alipotutuma. Tulitambua kwamba ni jambo la maana kutii amri ya serikali. Kwa hiyo tulijitayarisha kuhamia nchi ambayo watu hawakuamini kwamba kuna Mungu.
“Kwanza tulikutana na kuwasaidia watu 18 waliotaka kubatizwa waliokuwa wamekusanyika katika nyumba ya ndugu mmoja. Pia tulikusanya vichapo vya Kirusi na Kiukrainia na kujaribu kuvipakia vizuri ili visionekane wakati wa ukaguzi. Alfajiri, kijiji chetu kilizungukwa na wanajeshi wa Poland ambao walituambia tujitayarishe kuondoka. Tuliruhusiwa kubeba chakula cha mwezi moja na vitu vingine vya nyumbani tulivyohitaji. Walitusindikiza mpaka kwenye kituo cha gari-moshi. Kwa njia hiyo, Ukrainia ya Sovieti ikawa ‘mahali’ petu.
“Mara tu tulipofika, tulizungukwa na watu pamoja na wenye mamlaka wa mahali hapo. Kwa kuwa tulitaka kutoa ushuhuda mara moja, tuliwaambia kwa ujasiri kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova. Bila kutazamia, siku iliyofuata, katibu wa halmashauri ya kilimo ya mahali hapo alitutembelea. Alisema kwamba baba yake ambaye alikuwa amehamia Marekani alikuwa akimtumia vichapo vya Mashahidi wa Yehova. Tulifurahi sana kusikia hivyo! Tulifurahi hata zaidi alipotupatia vichapo hivyo. Yeye na familia yake walipoanza kuhudhuria mikutano yetu, tulitambua kwamba nchi hii ilikuwa na ‘vitu vingi vyenye kutamanika’ vya Yehova. (Hag. 2:7) Baada ya muda, washiriki wote wa familia hiyo wakawa Mashahidi wa Yehova na walimtumikia Yehova kwa miaka mingi.”
KAZI NYINGI YA KUFANYA
Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu na baada ya hapo, kazi ya kuhubiri nchini Urusi ilikuwa ikifanywa chini ya hali ngumu sana. Ofisi ya tawi ya Poland ilisema hivi katika barua iliyoandikia makao makuu Aprili 10, 1947: “Viongozi wa kidini wanawaogopesha wafuasi wao kwamba wakisoma Mnara wa Mlinzi au trakti yoyote ya Mashahidi wa Yehova, watapelekwa kwenye kambi za kazi ngumu kwa miaka kumi. Kwa sababu hiyo, wakaaji wa nchi hii wana woga na wasiwasi, na watu wanatamani nuru.”
Kitabu cha Mwaka cha 1947 (Kiingereza) kilisema hivi: “Mashahidi hawana vichapo vyovyote, wala Mnara wa Mlinzi lenye jalada linalovutia. . . . Mara nyingi gazeti hilo linanakiliwa kwa mkono na kugawanywa kwa wengine . . . Nyakati nyingine, ndugu wanaopeleka vichapo hivyo wanashikwa na kufungwa wakipatikana na Mnara wa Mlinzi.”
Regina Krivokulskaya anasema hivi: “Niliona ni kana kwamba nchi nzima imezungushwa seng’enge, nasi ni wafungwa hata ingawa hatukuwa gerezani. Waume wetu waliokuwa wakimtumikia Mungu kwa bidii walikaa miaka mingi katika kambi za kazi ngumu na gerezani. Sisi wanawake tulivumilia mengi: Kila mmoja wetu alikosa usingizi usiku, alikuwa na wasiwasi wa kupelelezwa kila mara na Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti (KGB), kupoteza kazi, na majaribu mengine. Wenye mamlaka walijaribu kila njia ili kututoa kutoka kwenye njia ya kweli. (Isa. 30:21) Bila shaka tulijua kwamba Shetani alikuwa anatumia hali hiyo kujaribu kukomesha kazi ya kuhubiri Ufalme. Lakini Yehova hakuwaacha watu wake. Msaada wake ulionekana wazi.
“Vichapo vya Biblia ambavyo viliingizwa nchini kwa siri na kwa shida sana vilitupatia ‘nguvu zinazopita zile za kawaida’ na hekima ya kupambana na hali hiyo. (2 Kor. 4:7) Yehova aliwaongoza watu wake ujapokuwa upinzani mkali kutoka kwa Serikali, bado wapya walijiunga na tengenezo. Inapendeza kwamba tangu walipojiunga na watu wa Yehova, wapya hao walikuwa tayari kuvumilia majaribu pamoja nao. Ni roho ya Yehova tu ndiyo ingeweza kutimiza mambo hayo.”
BARUA ZILIZOTUPWA NJE YA UA
Mnamo 1944, Pyotr, ambaye alimwoa Regina, alifungwa katika kambi moja iliyokuwa katika Wilaya ya Gorki kwa sababu ya msimamo wake wa Kikristo wa kutounga mkono siasa. Hilo halikupunguza kwa njia yoyote bidii yake ya kuhubiri. Pyotr aliandika barua ambazo zilikuwa na maelezo mafupi ya mafundisho ya Biblia. Kisha akaweka kila barua kwenye bahasha, akaifunga kwa kamba iliyokuwa na jiwe na kuitupa nje ya ua wenye seng’enge. Pyotr alitumaini kwamba siku moja mtu fulani atasoma barua hizo, na kwa kweli siku moja msichana mmoja anayeitwa Lidia Bulatova alizisoma. Pyotr alimwona, na akamwomba akaribie ua. Alimwuliza ikiwa angependa kujifunza mengi kuhusu Biblia. Lidia alipendezwa na wakapanga kukutana tena. Baada ya hapo, alikuwa akija na kuchukua barua hizo zenye ujumbe wa maana.
Lidia akawa dada mwenye bidii na mhubiri wa habari njema ambaye alianza kujifunza Biblia na Maria Smirnova na Olga Sevryugina. Wao pia walianza kumtumikia Yehova. Ili kuwategemeza dada hawa kiroho, akina ndugu walianza kuwapa chakula cha kiroho kutoka kambini. Pyotr alitengeneza sanduku ndogo ambalo lilikuwa na mfuko wa ziada ndani. Aliweka magazeti kwenye mfuko huo. Alipanga sanduku hilo litolewe nje ya kambi na kurudishwa na watu ambao si Mashahidi na si wafungwa. Walilipeleka kwenye nyumba ya mmoja wa dada hao.
Baada ya muda mfupi, dada hao walipanga kazi ya kuhubiri katika eneo lao. Polisi waligundua jambo hilo na kama ilivyokuwa wakati huo, wakamtuma mwanamke fulani awapeleleze. Mwanamke huyo aliyekuwa mwalimu alijifanya anapendezwa na kweli, kwa hiyo akina dada hao wakaanza kumtumaini. Kwa kuwa hawakuwa na uzoefu wa kutosha, walifurahia kumwambia “dada” yao mpya kweli za Biblia na baadaye wakamweleza jinsi ambavyo wao wanapata vichapo. Baada ya hayo, Pyotr alipotuma sanduku lile, aliwekwa kizuizini na kuhukumiwa miaka mingine 25. Dada hao pia walifungwa miaka 25 kila mmoja.
“WANAHITAJI KUPATA HABARI KAMILI”
Wakati wa vita na baada ya hapo, serikali ya Sovieti iliendelea kuwapinga sana Mashahidi wa Yehova. Mnamo Machi 1947, ndugu nchini Poland waliripoti kwamba ofisa mmoja mwenye cheo cha juu wa eneo moja lililoko magharibi mwa Muungano wa Sovieti alisema kwamba kufikia mwishoni mwa mwezi wa Mei mwaka huo, hakungekuwa na Shahidi wa Yehova hata mmoja katika eneo hilo. Barua waliyoandika ilisema hivi: “Tulipokuwa tukiandika barua hii, tulipata habari kwamba ndugu na dada 100 walikuwa wamekamatwa katika muda wa siku moja tu.” Barua nyingine ilisema hivi kuhusu ndugu waliokuwa kambini: “Wanadumisha sana utimilifu wao kwa Yehova. Tayari wengi wameuawa, na akina ndugu wanangojea ukombozi wa Yehova kama tu wale ndugu waliokuwa katika kambi za mateso.”
Mashahidi walikamatwa pia kwa kuhubiri na kukataa kupiga kura. Ndugu waliokuwa wakisimamia kazi waliandika hivi mnamo 1947: “Tunadhani kwamba wale wenye vyeo vya juu katika Urusi hawajui kinachowapata ndugu zetu, lakini hawataki kuwaua. Hawana habari za kutosha. [Wenye mamlaka] wanahitaji kupata habari kamili.”
OMBI LA KUANDIKISHWA KISHERIA
Baada ya muda mfupi, ofisi ya tawi ya Poland ilipendekeza kwamba ndugu wawili Warusi pamoja na mwanasheria mwenye ujuzi watayarishe vyeti vinavyohitajika ili kuandikisha kisheria utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti. Barua moja ambayo ndugu wa Poland waliwaandikia ndugu huko Urusi ilisema hivi: “Lazima habari njema ya Ufalme ihubiriwe na kusikiwa kotekote, kutia ndani Urusi. (Marko 13:10)” Barua hiyo ilimalizia hivi: “Iweni na subira. Yehova atageuza machozi yenu kuwa vigelegele vya shangwe.—Zaburi 126:2-6.”
Mnamo Agosti 1949, Mykola Pyatokha, Mykhailo Chumak, na Ilya Babijchuk walituma ombi la kuandikishwa kisheria. Serikali ilikubali kuandikisha kisheria Mashahidi wa Yehova lakini chini ya masharti fulani. Mojawapo ya masharti hayo ilikuwa kwamba ndugu hao watoe orodha ya majina ya Mashahidi wote wa Yehova wanaoishi katika eneo la Muungano wa Sovieti. Ndugu hao walikataa. Hata ingawa kazi ya kuhubiri iliendelea na hesabu ya wahubiri ilikuwa ikiongezeka daima, bado ndugu wengi waliendelea kufungwa gerezani.
‘YEHOVA WAKO HATAKUOKOA KUTOKA HAPA’
Pyotr Krivokulsky anakumbuka kiangazi cha 1945 na kusema: “Baada ya kesi ya akina ndugu kusikilizwa, walipelekwa katika kambi mbalimbali. Katika kambi nilimokuwa, wafungwa wengi walipendezwa sana na kweli. Mfungwa mmoja ambaye alikuwa kiongozi wa dini alikubali kwa haraka kweli aliyosikia na kuchukua msimamo upande wa Yehova.
“Hata hivyo, hali kambini zilikuwa mbaya sana. Wakati mmoja, nilifungiwa katika seli ndogo ambamo hata nisingeweza kusimama. Seli hiyo iliitwa nyumba ya wadudu kwa kuwa ilijaa kunguni. Ilikuwa na kunguni wengi sana hivi kwamba wangeweza kufyonza damu yote ya mwanadamu. Akiwa amesimama mbele ya seli hiyo, inspekta aliniambia: ‘Yehova wako hatakuokoa kutoka hapa.’ Chakula changu cha kila siku kilikuwa gramu 300 za mkate na maji kikombe kimoja. Hakukuwa na hewa humo, hivyo niliegemea kwenye mlango mdogo na kuvuta hewa iliyokuwa ikiingia kupitia njia ndogo sana. Nilihisi kunguni wakinifyonza damu. Kwa siku kumi nilizokuwa katika nyumba ya wadudu, nilimwomba Yehova tena na tena anipe nguvu za kuvumilia. (Yer. 15:15) Mwishowe mlango wa seli hiyo ulipofunguliwa, nilizimia na nilipopata fahamu nilijikuta katika seli nyingine.
“Baada ya hayo, mahakimu wa kambi ya kazi ngumu walinihukumu kifungo cha miaka kumi katika kambi yenye ulinzi mkali kwa ‘kuchochea na kueneza propaganda dhidi ya serikali ya Sovieti.’ Hatungeweza kutuma au kupokea barua katika kambi hiyo. Kambi hiyo ilikuwa ya wafungwa waliofanya uhalifu wa kikatili, kama vile kuua. Niliambiwa kwamba ikiwa sitakana imani yangu, wafungwa hao wanaweza kunitendea lolote wanaloambiwa wafanye. Nilikuwa na uzito wa kilogramu 36 na hata nisingeweza kutembea. Lakini hata katika kambi hiyo niliweza kupata watu wenye mioyo minyoofu ambao walipendezwa na kweli.
“Siku moja nilipokuwa nimelala chini nikisali, mzee mmoja alinikaribia. Aliniuliza: ‘Kwani ulifanya nini ili uletwe mahali pabaya hivi?’ Aliposikia kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova, aliketi chini, akanikumbatia, na kunibusu. Kisha akasema: ‘Mwanangu, kwa muda mrefu sana nimetaka kujifunza Biblia. Tafadhali nifundishe.’ Nilifurahi sana. Mara moja nilitoa vikaratasi vya zamani vya vitabu vya Injili nilivyokuwa nimeshona katika mavazi yangu yaliyopasuka. Macho yake yalilengwa-lengwa na machozi. Tuliongea kwa muda mrefu jioni hiyo. Aliniambia kwamba alifanya kazi katika chumba cha kulia kambini na angenipa chakula. Kwa hiyo tukawa marafiki. Alikomaa kiroho nami nikapata nguvu kimwili. Nina hakika kwamba Yehova ndiye alipanga hayo. Baada ya miezi michache, aliachiliwa huru, nami nikapelekwa katika kambi nyingine katika Wilaya ya Gorki.
“Hali zilikuwa afadhali katika kambi hiyo. Lakini furaha yangu kubwa ilikuwa kuongoza mafunzo ya Biblia na wafungwa wanne. Mnamo 1952, mmoja wa wanyapara kambini alitupata na vichapo. Tulipokuwa tukiulizwa maswali kabla ya kesi yetu, nilifungiwa katika sanduku ambalo halikuwa na hewa, na nilipokuwa nimeanza kukosa pumzi, walifungua sanduku ili nipate hewa kisha wakalifunga tena. Walitaka nikane imani yangu. Sisi sote tulipatikana na hatia. Hukumu yetu ilipokuwa ikisomwa, hakuna yeyote kati ya wanafunzi wangu wa Biblia aliyeingiwa na hofu. Nilifurahia sana jambo hilo. Wote wanne walihukumiwa kifungo cha miaka 25 kwenye kambi. Nilipewa hukumu kali zaidi, lakini ilibadilishwa na kuwa kifungo cha miaka mingine 25 katika kambi yenye ulinzi mkali na kifungo cha nje cha miaka 10. Tulipotoka mahakamani, tulisimama ili kumshukuru Yehova kwa kututegemeza. Walinzi walishtuka na kushangaa ni kwa nini tumefurahi. Tulitenganishwa na kila mmoja akapelekwa katika kambi tofauti. Nilipelekwa kwenye kambi moja yenye ulinzi mkali huko Vorkuta.”
MSIMAMO WAO ULIWAOKOA
Maisha yalikuwa magumu kwenye kambi. Wafungwa wengi wasio Mashahidi walijiua. Ivan Krylov anakumbuka: “Nilipofunguliwa kutoka kambi yenye ulinzi mkali, nilitembelea migodi kadhaa ya makaa ya mawe ambako ndugu na dada zetu walilazimishwa kufanya kazi. Tuliwasiliana na wale waliokuwa wamefaulu kutoa nakala za magazeti yetu na kuwapa wengine nakala hizo. Mashahidi walihubiri katika kila kambi na wengi walipendezwa. Walipoachiliwa wengine walibatizwa katika Mto Vorkuta.”
“Kila mara imani yetu katika Yehova na Ufalme wake ilijaribiwa. Pindi moja mnamo 1948, wafungwa katika kambi moja huko Vorkuta walipanga uasi. Waasi hao waliwaambia wafungwa wengine kwamba wangefaulu kabisa ikiwa wangejipanga katika vikundi, iwe ni vya kitaifa au vya kidini. Kulikuwa na Mashahidi 15 katika kambi hiyo. Tuliwaambia waasi hao kwamba sisi ni Wakristo na hatuwezi kujihusisha katika mambo hayo. Tuliwaeleza kuwa Wakristo wa mapema hawakushiriki katika uasi dhidi ya Waroma. Wengi walishangazwa, lakini tulisimama imara.”
Uasi huo ulitokeza msiba. Askari waliwashinda waasi hao na kuwaingiza katika jengo moja kambini. Kisha wakalimwagilia mafuta na kuliwasha moto. Karibu kila mtu aliyekuwa ndani alikufa. Lakini askari hawakuwaumiza akina ndugu.
Ivan anaendelea kusema: “Mnamo Desemba 1948, nilikutana na ndugu wanane kutoka kambi moja waliokuwa wamefungwa kwa miaka 25. Hali ya hewa ilikuwa mbaya sana katika majira hayo ya baridi kali, nayo kazi kwenye migodi ilikuwa ngumu sana. Hata hivyo, macho ya ndugu hao yalionyesha uhakika na tumaini lenye nguvu. Mtazamo wao uliwaimarisha wafungwa ambao hawakuwa Mashahidi wa Yehova.”
KUPELEKWA UHAMISHONI SIBERIA
Licha ya upinzani wenye ukatili kutoka kwa wenye mamlaka, Mashahidi waliendelea kuhubiri kwa bidii. Hilo liliwakasirisha wakuu wa serikali huko Moscow. Shirika la KGB ndilo lililokasirishwa zaidi. Februari 19, 1951, maofisa wa shirika hilo walimwandikia Stalin barua iliyosema: “Ili kuzuia utendaji unaopinga Muungano wa Sovieti wa kikundi haramu cha wafuasi wa Yehova, MGB [Wizara ya Usalama wa Kitaifa, ambayo baadaye iliitwa KGB] ya USSR inaona ni muhimu kuwahamisha hadi wilaya za Irkutsk na Tomsk.” Shirika la KGB liliwajua Mashahidi wote na lilimwomba Stalin ruhusa ya kuwahamisha watu 8,576 kutoka jamhuri sita za Muungano wa Sovieti na kuwapeleka hadi Siberia. Stalin aliwaruhusu.
Magdalina Beloshitskaya anakumbuka: “Saa nane usiku Jumapili, Aprili 8, 1951, tuliamshwa mlango wetu ulipobishwa kwa kishindo. Mama aliruka kutoka kitandani na akakimbia na kumkuta askari amesimama mlangoni. ‘Mnapelekwa uhamishoni Siberia kwa sababu ya kumwamini Mungu,’ akatangaza. ‘Tunawapa saa mbili mpakie vitu vyenu. Chukueni chochote humu ndani, lakini hamruhusiwi kuchukua mbegu, unga, na nafaka. Pia hamruhusiwi kuchukua fanicha, vifaa vya mbao, na cherehani. Msichukue chochote kilicho nje ya nyumba. Bebeni tu shuka, blanketi, nguo, na mifuko yenu na mtoke.’
“Tulikuwa tumesoma katika vichapo vyetu kwamba kulikuwa na kazi nyingi upande wa mashariki wa nchi yetu. Sasa tulielewa kwamba wakati ulikuwa umefika wa kufanya kazi hiyo.
“Hakuna aliyelia. Askari alishangaa na kusema, ‘Hamjatokwa na machozi hata kidogo.’ Tulimwambia kwamba tangu 1948 tulikuwa tukisubiri kuhamishwa. Tulimwomba ruhusa tuchukue angalau kuku mmoja lakini akakataa. Askari hao waligawana mifugo yetu. Waligawana kuku wetu huku tukiwatazama. Mmoja alichukua watano, mwingine sita, na mwingine akapata watatu au wanne. Kuku wawili tu walipobaki, ofisa aliamuru wachinjwe nasi tukapewa kuku hao.
“Binti yangu mwenye umri wa miezi minane tu alikuwa amelala. Tuliuliza ikiwa tungeruhusiwa kubeba kitanda chake, lakini ofisa akaamuru kivunjwe-vunjwe. Kisha akatupa sehemu ambayo ingeweza kumbeba mtoto.
“Muda si muda, majirani walijua tunapelekwa uhamishoni. Mmoja wao alikuja na mfuko mdogo wenye mkate na tulipokuwa tukiondoka aliutupa ndani ya gari la kukokotwa lililokuwa limetubeba. Askari aliuona na akautupa nje. Tulikuwa watu sita, yaani, mimi, Mama, ndugu zangu wawili, mume wangu, na binti yetu mwenye umri wa miezi minane. Tulipotoka kijijini, tuliingizwa haraka ndani ya gari na kupelekwa kwenye kituo kikuu cha eneo hilo ambako hati zetu zilijazwa. Kisha tukabebwa kwa lori na kupelekwa kwenye kituo cha reli.
“Ilikuwa Jumapili, siku yenye jua lenye kupendeza. Kituo hicho kilikuwa kimejaa watu—wanaohamishwa na waliokuja kutazama. Lori lililokuwa limetubeba lilisimama karibu na behewa la gari-moshi ambamo ndugu zetu tayari walikuwa. Gari-moshi lilipojaa, askari walihakikisha kila mtu yumo kwa kutumia jina lake la pili. Behewa letu lilikuwa na watu 52. Wale waliokuja kutuaga walianza kulia. Lilikuwa jambo la kustaajabisha kwani hata hatukuwajua wengine kati yao. Lakini wao walijua kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova na tulikuwa tunapelekwa uhamishoni Siberia. Gari-moshi lilipiga honi kwa nguvu. Kisha akina ndugu wakaanza kuimba wimbo katika Kiukrainia: ‘Upendo wa Kristo na uwe pamoja nanyi. Tukimpa Yesu Kristo utukufu tutakutana tena katika Ufalme wake.’ Wengi wetu tulikuwa na tumaini hakika na imani kwamba Yehova hatatuacha. Tuliimba mistari kadhaa. Kuimba kwetu kuligusa mioyo sana hivi kwamba baadhi ya askari wakaanza kulia. Kisha gari-moshi likaanza kuondoka.”
“KINYUME NA ILIVYOTARAJIWA”
Dakt. N. S. Gordienko, profesa katika Chuo Kikuu cha Herzen huko St. Petersburg, anaeleza katika kitabu chake kile ambacho wanyanyasaji walitimiza. Aliandika hivi: “Matokeo yalikuwa kinyume na ilivyotarajiwa; walitaka tengenezo la Mashahidi wa Yehova liwe dhaifu katika Muungano wa Sovieti, lakini wakaliimarisha. Katika makao mapya ambako hakuna mtu alikuwa amesikia kuhusu Mashahidi wa Yehova, ‘waliwaambukiza’ wenyeji kupitia imani yao na uaminifu wao kwa imani hiyo.”
Mashahidi wengi walizoea mazingira mapya haraka. Makutaniko madogo yalianzishwa na kugawiwa maeneo. Nikolai Kalibaba anasema: “Kuna wakati huko Siberia tulihubiri nyumba kwa nyumba, au ni sahihi zaidi kusema kwamba tulihubiri kutoka nyumba moja kisha tukaruka nyumba mbili au tatu kabla ya kuhubiri nyumba nyingine. Lakini hilo lilikuwa hatari. Tulifaulu jinsi gani? Tulijaribu kufanya ziara ya kurudia baada ya mwezi mmoja hivi. Tulianza mazungumzo kwa kuuliza, ‘Je, mnauza kuku, mbuzi, au ng’ombe?’ Kisha tungebadili mazungumzo yahusu Ufalme. Shirika la KGB liligundua hilo na makala ilichapishwa katika gazeti kuwaonya watu wasizungumze na Mashahidi wa Yehova. Makala hiyo ilisema kuwa Mashahidi walienda nyumba kwa nyumba wakiuliza ikiwa kuna mbuzi, ng’ombe, na kuku, lakini tulichokuwa tukitafuta hasa ni kondoo!”
Gavriil Livy anasema: “Akina ndugu walijaribu kuhubiri ingawa maofisa wa KGB walikuwa wakiwachunguza. Ikiwa watu katika Muungano wa Sovieti walishuku kuwa unajaribu kuzungumza nao kuhusu dini, waliwajulisha polisi mara moja. Bado tuliendelea kuhubiri ingawa hatukupata matokeo yoyote mwanzoni. Lakini baada ya muda, kweli ilianza kubadili baadhi ya wenyeji. Mmoja alikuwa mwanamume Mrusi ambaye kwa kawaida alilewa sana. Alipojifunza kweli, alipatanisha maisha yake na kanuni za Biblia na akawa Shahidi mwenye bidii. Ofisa wa KGB alimwita na kumwambia: ‘Unashirikiana na akina nani? Hao Mashahidi wote ni Waukrainia.’
“Ndugu huyo alijibu: ‘Nilipokuwa mlevi nililala kwenye mitaro, nanyi hamkujishughulisha nami. Sasa kwa kuwa nimekuwa mtu wa kawaida anayetii sheria, hilo haliwafurahishi. Waukrainia wengi wanaondoka Siberia, lakini wanaacha Wasiberia ambao wamefundishwa na Mungu jinsi ya kuishi.’”
Baada ya miaka michache, ofisa mmoja kutoka Irkutsk aliwaandikia hivi wenye mamlaka huko Moscow: “Wafanyakazi kadhaa wa eneo hili wamesema kwamba wote kati ya hawa [Mashahidi wa Yehova] wanapaswa kupelekwa eneo mmoja huko kaskazini ili wasiwasiliane na mtu mwingine yeyote na waelimishwe upya.” Wenye mamlaka huko Siberia na huko Moscow hawakujua wafanye nini ili kuwanyamazisha Mashahidi wa Yehova.
“TUNGEWAPIGA NINYI NYOTE RISASI”
Mapema mnamo 1957, wenye mamlaka walijaribu njia tofauti. Akina ndugu walifuatwa kila walikokwenda na nyumba zilipekuliwa. Viktor Gutshmidt anakumbuka: “Wakati mmoja niliporudi nyumbani baada ya utumishi, nyumba yote ilikuwa imevurugwa. Maofisa wa KGB walikuwa wakitafuta vichapo. Walinikamata na kunihoji kwa miezi miwili. Yulia, binti yetu mdogo alikuwa na miezi 11, na binti yetu mkubwa alikuwa na miaka 2.
“Inspekta aliniambia hivi aliponihoji, ‘Wewe ni Mjerumani, sivyo?’ Watu wengi waliona neno ‘Mjerumani’ kuwa linarejezea ‘Mfashisti.’ Wajerumani walichukiwa.
“‘Mimi sitetei taifa langu,’ nilisema, ‘lakini ikiwa unauliza kuhusu Wajerumani niliofungwa nao kwenye kambi za mateso za Wanazi, basi ninawaheshimu Wajerumani hao kwelikweli! Waliitwa Bibelforscher, na sasa wanaitwa Mashahidi wa Yehova. Najivunia kwamba hakuna Shahidi aliyewahi kutumia bunduki ya kumimina risasi au kulipua kombora. Ninajivunia sana Wajerumani hao!’
“Inspekta huyo alinyamaza, kwa hiyo nikasema: ‘Nina hakika kwamba hakuna Shahidi wa Yehova ameshiriki katika uasi wowote. Hata kazi ya Mashahidi wa Yehova inapopigwa marufuku, wao huendelea kumwabudu Mungu. Wakati huohuo, Mashahidi hutambua na kutii mamlaka zinazofaa ikiwa sheria zao hazivunji sheria za juu zaidi za Muumba wetu.’
“Ghafula, inspekta huyo alinikatiza na kusema: ‘Hatujawahi kukichunguza kikundi kingine kwa uangalifu kama tulivyowachunguza Mashahidi na utendaji wao. Ikiwa rekodi zingeonyesha jambo lolote dhidi yenu, hata ikiwa ingepatikana kwamba mlimuumiza mtu mmoja tu, tungewapiga ninyi nyote risasi.’
“Kisha nikajiambia hivi: ‘Ndugu zetu ulimwenguni pote wana ujasiri wa kumtumikia Yehova, na mfano wao umetuokoa huku katika Muungano wa Sovieti. Kwa hiyo, huenda kumtumikia Mungu hapa kukawasaidia ndugu zetu katika maeneo mengine.’ Wazo hilo lilinipa nguvu za kushikamana na njia za Yehova.”
MASHAHIDI KATIKA ZAIDI YA KAMBI 50
Msimamo wa Mashahidi wa Yehova wa kutokuwamo na bidii yao shambani katika Muungano wa Sovieti uliendelea kuikasirisha serikali. (Marko 13:10; Yoh. 17:16) Mara nyingi, msimamo wa ndugu zetu uliwafanya wahukumiwe vifungo virefu visivyo vya haki.
Kotekote ulimwenguni katika makusanyiko 199 yaliyofanywa kuanzia Juni 1956 hadi Februari 1957, wahudhuriaji 462,936 waliunga mkono ombi ambalo nakala zake zilitumwa kwenye Baraza la Mawaziri wa Muungano wa Sovieti huko Moscow. Sehemu fulani ya ombi hilo ilisema hivi: “Kuna Mashahidi wa Yehova katika kambi zaidi ya 50 huko Urusi na Siberia na kaskazini kuelekea Bahari ya Aktiki na hata kwenye kisiwa cha Aktiki cha Novaya Zemlya . . . Nchini Marekani na nchi nyingine za magharibi, Mashahidi wa Yehova wameitwa Wakomunisti na katika nchi za Wakomunisti wanaitwa wabeberu . . . Serikali za Wakomunisti zimewashtaki na kuwahukumu kuwa ‘wapelelezi wa wabeberu’ na kuwapa vifungo vya miaka 20 gerezani. Lakini hawajawahi kujihusisha katika utendaji wowote unaovunja sheria.” Kwa kusikitisha, ombi hilo halikuboresha hali ya Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti.
Ilikuwa vigumu hasa kwa familia za Mashahidi wa Yehova nchini Urusi kuwalea watoto wao. Vladimir Sosnin kutoka Moscow, ambaye aliwalea wavulana watatu anasema: “Ilikuwa lazima kwenda kwenye shule ya Usovieti. Walimu na wanafunzi wengine waliwashinikiza wajiingize katika mashirika yaliyoendeleza falsafa za Kikomunisti. Tulitaka watoto wetu wapate elimu, nasi tuliwasaidia katika masomo yao. Haikuwa rahisi kwetu kusitawisha upendo kwa ajili ya Yehova katika mioyo ya watoto wetu. Shule zilijaa maoni kuhusu kuendeleza ujamaa na Ukomunisti. Sisi wazazi tulihitaji subira na kuendelea kuwafundisha.”
WASHTAKIWA KWA KUKATA SIKIO LA BINTI YAO
Semyon na Daria Kostylyev waliwalea watoto watatu huko Siberia. Semyon anasimulia hivi: “Mashahidi wa Yehova walionwa kuwa washupavu wa kidini. Mnamo 1961, Alla, binti yetu wa pili alijiunga na darasa la kwanza. Siku moja alipokuwa akicheza na watoto wengine, mmoja wao alimjeruhi sikio bila kukusudia. Siku iliyofuata, mwalimu alipomuuliza kilichotukia, Alla alinyamaza kwani hakutaka kumshtaki mwanafunzi mwenzake. Mwalimu alijua kwamba wazazi wa Alla ni Mashahidi na akakata kauli kwamba tulimchapa ili kumlazimisha afuate kanuni za Biblia. Shule iliripoti jambo hilo kwenye ofisi ya mwendesha-mashtaka wa umma. Vilevile, kampuni niliyofanyia kazi ilihusishwa. Uchunguzi uliendelea kwa karibu mwaka mzima hadi tulipoitwa kortini mnamo Oktoba 1962.
“Kwa majuma mawili kabla ya kesi, jengo linaloitwa Jumba la Utamaduni lilikuwa na ubao uliosema, ‘Kesi ya madhehebu hatari ya wafuasi wa Yehova itaanza karibuni.’ Mimi na mke wangu tulishtakiwa kwa kumlea mtoto wetu kulingana na Biblia. Pia tulishtakiwa kwamba tulikuwa wakatili. Korti ilidai kwamba tulikuwa tumemlazimisha binti yetu kusali na tulikata sikio lake kwa kutumia kingo zenye makali za ndoo! Alla tu ndiye angeweza kutoa ushahidi katika kesi hiyo, lakini alipelekwa kwenye makao ya watoto mayatima huko Kirensk, kilomita 700 hivi kaskazini ya Irkutsk, tulikokuwa tukiishi.
“Jumba hilo lilijawa na wanaharakati wa chama cha vijana. Kulipokuwa na mapumziko ili korti ifikie uamuzi, umati ulizusha ghasia. Tulisukumwa huku na huku na kutukanwa, na mtu mmoja alisema tutoe nguo zetu za ‘Kisovieti.’ Kila mtu alisema kwamba tunapaswa kuuawa na mmoja wao hata alitaka kutuua papo hapo. Umati ulizidi kupandwa na hasira na bado mahakimu hawakutoka nje. Mapumziko yaliendelea kwa saa nzima. Umati ulipotukaribia, Shahidi mmoja na mume wake ambaye si mwamini walisimama kati yetu na watu hao wakiwasihi wasituumize. Huku wakijaribu kueleza kwamba mashtaka yote yalikuwa ya uwongo, walituondoa mikononi mwa umati huo.
“Mwishowe hakimu alitokea akiwa na wasaidizi wa korti naye akasoma hukumu: kupoteza haki ya kuwalea watoto wetu. Nilikamatwa na kufungwa katika kambi kwa miaka miwili. Binti yetu mkubwa alipelekwa kwenye makao ya watoto yatima na akaambiwa wazazi wake ni washiriki wa madhehebu hatari na kwamba wao wanamwathiri vibaya.
“Mwana wetu aliruhusiwa kukaa na Daria kwa kuwa alikuwa na miaka mitatu tu. Nilipomaliza kifungo changu, nilirudi nyumbani. Kama mbeleni, tungeweza tu kuhubiri isivyo rasmi.”
“TULIJIVUNIA WATOTO WETU”
“Alla alitoka kwenye makao ya watoto mayatima alipofikia umri wa miaka 13, naye akaja nyumbani. Ilikuwa shangwe kama nini kwetu alipojiweka wakfu na kubatizwa mnamo 1969! Karibu na wakati huo, hotuba kuhusu dini zilikuwa zikitolewa kwenye Jumba la Utamaduni katika jiji letu. Tuliamua kwenda kusikiliza. Kama kawaida, Mashahidi wa Yehova ndio waliozungumziwa zaidi. Mmoja wa wasemaji aliinua Mnara wa Mlinzi na kusema, ‘Hili ni gazeti lenye madhara linalovuruga umoja wa Nchi yetu.’ Kisha akatoa mfano: ‘Washiriki wa madhehebu hayo huwalazimisha watoto wasome magazeti haya na wasali. Katika familia moja, msichana mdogo hakutaka kusoma, kwa hiyo baba yake akamkata sikio.’ Alla alishangaa, kwa kuwa alikuwa ameketi hapo akisikiliza hotuba hiyo akiwa na masikio yake yote. Hata hivyo, hakusema lolote kwa kuwa aliogopa angetenganishwa nasi tena.
“Mwana wetu, Boris alipofikia umri wa miaka 13 alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Wakati mmoja, alikuwa akihubiri barabarani na Mashahidi wengine wa umri wake, ingawa bado kazi ilikuwa imepigwa marufuku. Hawakuwa na Biblia wala vichapo vya Biblia. Ghafula, gari likaja mahali walipokuwa na wote wakapelekwa kwenye kituo cha wanamgambo. Baada ya kuwahoji na kuwapekua, wanamgambo hawakupata chochote isipokuwa maandiko machache yaliyoandikwa kwenye karatasi. Wavulana hao waliruhusiwa kwenda nyumbani. Alipofika nyumbani, Boris alijivunia jinsi yeye na wenzake walivyonyanyaswa kwa ajili ya jina la Yehova. Tulijivunia watoto wetu, kwa kuwa Yehova aliwategemeza wakati wa majaribu. Baada ya tukio hilo, mimi na Daria tuliitwa na shirika la KGB mara kadhaa. Ofisa mmoja alisema: ‘Watoto hawa wanapaswa kupelekwa kwenye gereza la vijana. Ubaya ni kwamba hawajafikisha umri wa miaka 14.’ Tulitozwa faini kwa sababu ya mvulana wetu kuhubiri.
“Leo, ninaishi na mwana wangu na wajukuu walio katika kweli. Binti yangu mkubwa anaishi Uzibekistani, na ingawa bado hamtumikii Yehova, anatuheshimu na anaiheshimu Biblia naye hututembelea sana. Mnamo 2001, Daria alikufa, baada ya kumtumikia Yehova hadi mwisho. Ninapokuwa na nguvu za kutosha, mimi huhubiri pamoja na kutaniko kwenye maeneo ya mbali tukiwatafuta watu ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’ (Mdo. 13:48) Ninaamini kwamba hivi karibuni sana Yehova atatimiza tamaa ya kila mmoja wetu, kama ilivyoandikwa kwenye Isaya 65:23.”
WAZAZI WAWEKA MFANO MZURI
Vladislav Apanyuk anatumikia katika Betheli ya Urusi. Anakumbuka jinsi wazazi wake walivyokazia upendo kwa Mungu ndani yake na ndugu na dada zake tangu utotoni: “Mnamo 1951, wazazi wetu walipelekwa uhamishoni kutoka Ukrainia hadi Siberia. Walitufundisha kujifanyia maamuzi huku tukijitahidi kumpendeza Yehova. Nilithamini sana kwamba wazazi wetu walizungumzia kasoro zao hata mbele yetu bila kuaibika. Walipokosea hawakuficha. Ilikuwa wazi walimpenda Yehova. Wazazi walikuwa wenye furaha mara nyingi, hasa walipozungumza mambo ya kiroho pamoja nasi. Tuliona wanapenda sana kutafakari na kuzungumza kumhusu Yehova. Hilo lilituchochea tutafakari kuhusu kweli zinazomhusu Yehova. Tuliwazia jinsi watu watakavyoishi katika ulimwengu mpya, wakati ambapo kila kitu kitapendeza na hakutakuwa tena na magonjwa au vita.
“Nilipokuwa darasa la tatu, sote tuliombwa tujiunge na shirika la vijana la Kisovieti linaloitwa Mapainia. Watoto wengi katika Muungano wa Sovieti waliona hilo kuwa pendeleo kubwa. Wanafunzi wenzangu walingoja siku hiyo kwa hamu kubwa. Kila mmoja wetu alipaswa kuandika kiapo rasmi kwamba alikuwa tayari kujiunga na Mapainia Wasovieti, wajenzi wa wakati ujao wa Ukomunisti. Nilikataa. Kwa hiyo, mwalimu akaniadhibu kwa kunifungia darasani. ‘Huwezi kutoka hadi uandike kiapo hicho,’ akasema. Saa kadhaa baadaye, wanafunzi wenzangu waligonga dirisha na kunisihi nitoke tukacheze. Niliketi darasani nikiwa nimeazimia kutoandika chochote. Mwalimu mwingine alikuja ilipokuwa ikielekea jioni. Aliponiona aliniruhusu niende nyumbani. Huo ulikuwa ushindi wangu wa kwanza. Nilijivunia kufanya jambo ambalo lingeufurahisha moyo wa Yehova. (Met. 27:11) Nilipofika nyumbani, niliwaambia wazazi wangu yote yaliyotokea. Walishangilia, naye Baba akasema, ‘Hongera kijana wangu!’”
BIBLIA YAONWA KUWA INAPINGA USOVIETI
Nyakati nyingine akina ndugu walishtakiwa kwa sababu tu ya kuwa na Biblia. Nadezhda Vishnyak anasema: “Mimi na mume wangu hatukuwa Mashahidi wa Yehova, lakini kweli ilikuwa imegusa sana mioyo yetu. Wakati mmoja, polisi walikuja kazini na kunichukua nikiwa na mavazi ya kazi. Pia walimkamata Pyotr, mume wangu, akiwa kazini. Kabla ya hilo, nyumba yetu ilipekuliwa na polisi wakapata Biblia na kijitabu After Armageddon—God’s New World. Pyotr hakufikiri wangenikamata, kwa kuwa nilikuwa nina mimba ya miezi saba.
“Tulishtakiwa kwamba tuliipinga serikali ya Sovieti. Tuliwaambia tunaiamini Biblia, ambayo ndiyo mamlaka kubwa zaidi kuliko ile ya Sovieti.
“‘Biblia ni Neno la Mungu nasi tunataka kuishi kupatana na kanuni zake,’ nikasema.
“Ulipofika wakati wa kesi yetu kusikilizwa, majuma mawili tu yalisalia ili nijifungue. Kesi ilipokuwa ikiendelea, hakimu aliruhusu vipindi vya mapumziko ili niende nje kutembea nikiwa chini ya ulinzi wa askari mwenye bunduki. Askari huyo aliniuliza nimefanya nini. Nilipata nafasi nzuri ya kumhubiria.
“Hakimu alitangaza kwamba Biblia na vichapo vilivyokuwa vimepatikana nyumbani kwetu vilikuwa ‘vinapinga Usovieti.’ Nilifurahi kwamba zaidi tu ya mimi na mume wangu kushtakiwa kuwa tunapinga Usovieti, mashtaka hayo yalihusu pia vichapo vyetu na Biblia! Tuliulizwa jinsi tulivyokutana na Mashahidi wa Yehova. Tuliposema tulikutana nao katika kambi huko Vorkuta, hakimu huyo alisema hivi kwa sauti, ‘Hebu oneni mambo yanayoendelea katika kambi zetu!’ Sote tulihukumiwa kifungo cha miaka kumi katika kambi za kazi ngumu.
“Pyotr alipelekwa kwenye kambi iliyoko Mordvinia, huko Urusi katikati. Nami nikawekwa katika kifungo cha upweke. Mnamo Machi 1958, nilijifungua mwana wetu. Katika kipindi hicho kigumu, Yehova alikuwa rafiki yangu wa karibu zaidi na msaidizi wangu. Mama yangu alimchukua mwana wetu na kumtunza. Nilipelekwa Kemerovo, Siberia, ambako nilifungwa katika kambi ya kazi ngumu.
“Baada ya miaka minane, niliachiliwa kabla ya muda kamili wa kifungo changu kwisha. Ninakumbuka kwamba katika majengo ya gereza, mnyapara wa jengo letu alitangaza kwa sauti kwamba sikuwahi kusema jambo lolote ‘linalopinga Usovieti’ na kwamba vichapo vyetu vilikuwa vya kidini kabisa. Nilibatizwa mnamo 1966, baada ya kuachiliwa.”
Biblia na vichapo vya Biblia vilikuwa vyenye thamani sana gerezani na kwenye kambi. Mnamo 1958, kwenye kambi huko Mordvinia, akina ndugu walikuwa wakiongoza mikutano kwa ukawaida. Ili wanyapara wasiwakamate, ndugu kadhaa waliwekwa wasimame kila baada ya hatua chache ili watoe onyo wengine walipokuwa wakijifunza Mnara wa Mlinzi. Mnyapara alipotokea ndugu aliyemwona angesema “anakuja,” kisha ujumbe huo ungepitishwa hadi kwa kikundi kilichokuwa kimekutana. Kila mtu angeondoka, na gazeti lingefichwa. Lakini mara nyingi wanyapara walitokea ghafula na bila kutarajiwa.
Wakati mmoja wanyapara walipowakuta ghafula akina ndugu, Boris Kryltsov aliamua kuwakengeusha ili wasilipate gazeti hilo. Alinyakua kitabu na kukimbia nje ya jengo. Wanyapara walimkimbiza kwa muda mrefu, lakini walipomkamata waliona alikuwa amebeba kitabu cha Lenin. Ingawa alitiwa katika kifungo cha upweke kwa siku saba, alifurahi kwamba alikuwa amesaidia gazeti lisichukuliwe.
MBEGU ZA KWELI ZAPANDWA HUKO MOSCOW
Kazi ya kuhubiri huko Moscow ilianzishwa na kikundi kidogo. Boris Kryltsov alikuwa mmoja kati ya ndugu wachache waliohubiri kwa bidii. Anasimulia hivi: “Nilifanya kazi ya usimamizi wa ujenzi. Tulijaribu kuhubiri isivyo rasmi tukiwa kikundi cha akina ndugu na dada. Maofisa wa KGB walipekua nyumba yangu mnamo Aprili 1957 na walipopata vichapo vya Biblia wakanikamata. Inspekta aliponihoji, aliniambia kuwa Mashahidi wa Yehova ndio watu hatari zaidi nchini. Aliniambia: ‘Tukikuacha huru, raia wengi wa Sovieti watajiunga nawe. Ndiyo sababu tunakuona kuwa mtu hatari sana kwa Nchi yetu.’
“‘Biblia inatufundisha tuwe raia wanaotii sheria,’ nilimwambia. ‘Pia inasema tunapaswa kuendelea kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu. Wakristo wa kweli hawajawahi kujaribu kunyakua mamlaka katika nchi yoyote.’
“‘Ulipata wapi vichapo tulivyopata kwako?’ akauliza askari huyo.
“‘Vichapo hivyo vina ubaya gani?’ nikamwuliza. ‘Vinazungumzia tu unabii wa Biblia si mambo ya kisiasa.’
“‘Ni kweli, lakini vinachapishwa ng’ambo,’ akajibu.
“Nilipelekwa kwenye gereza lenye ulinzi mkali huko Vladimir. Nilipekuliwa kabisa, lakini nilishangaa kuwa nilifaulu kuingiza ndani ya gereza hilo matoleo manne ya Mnara wa Mlinzi niliyokuwa nimenakili katika karatasi nyembamba. Ilikuwa wazi kwamba Yehova alinisaidia. Nilinakili upya magazeti hayo manne kwenye seli yangu. Nilijua kwamba mbali na mimi, kulikuwa na Mashahidi wengine, na kwamba hawakuwa wamepata chakula cha kiroho kwa miaka saba. Nilimtumia dada aliyekuwa akisafisha ngazi kupitisha magazeti hayo.
“Ilitukia kwamba mtu aliyekuwa akishirikiana na akina ndugu aliwaambia askari kwamba kuna mtu anayesambaza vichapo vya Biblia. Mara moja walianza kumpekua kila mtu na kuchukua vichapo vyote. Walipokuja kwangu walipata vichapo katika godoro langu. Nilifungwa kwa siku 85 katika kifungo cha upweke. Hata hivyo, Yehova aliendelea kututunza.”
HOTUBA ZILIWASAIDIA WENGINE KUJIFUNZA KWELI
Hotuba zilitumiwa pia kupiga vita vya mawazo dhidi ya Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti. Viktor Gutshmidt anasema: “Kambi yetu ilitembelewa kwa ukawaida na wasemaji waliotoa hotuba zilizotetea wazo la kwamba hakuna Mungu. Kila mara akina ndugu waliuliza maswali. Nyakati nyingine wasemaji walishindwa kujibu maswali rahisi sana. Kwa kawaida jumba lilijaa na kila mtu alisikiliza kwa makini sana. Watu walikuja kwa wingi kwa kuwa walitaka kujua Mashahidi wa Yehova watasema nini mwishoni mwa hotuba.
“Wakati mmoja, kambi yetu ilitembelewa na msemaji ambaye hapo awali alikuwa kasisi katika Kanisa Othodoksi la Urusi. Kila mtu alijua kwamba alikana imani yake alipokuwa kambini na kujiunga na watu wanaoamini hakuna Mungu.
“‘Je, uliamini hakuna Mungu kabla ya kwenda gerezani, au ulianza kuamini hivyo baadaye?’ ndugu mmoja alimwuliza msemaji alipomaliza.
“‘Hebu fikiria,’ akajibu msemaji. ‘Mtu alisafiri kwenda anga za juu naye hakumwona Mungu huko.’
“‘Ulipokuwa kasisi, je, uliamini kwamba Mungu anawatazama wanadamu kutoka kilomita 200 hivi juu ya dunia?’ akauliza ndugu huyo. Msemaji hakujibu. Mahojiano hayo yaliwafanya wafungwa wengi wafikiri, na baadaye wengine walianza kujifunza Biblia pamoja nasi.
“Pindi moja dada mmoja aliomba ruhusa aseme jambo fulani. ‘Sema tu; huenda wewe ni Shahidi wa Yehova,’ akasema msemaji.
“‘Ungesemaje kuhusu mtu anayesimama uwanjani na kupaaza sauti, “Nitakuua!” na huku hakuna mtu yeyote karibu?’ akauliza dada huyo.
“‘Kwa kweli, huwezi kusema ana akili timamu,’ akajibu msemaji.
“‘Ikiwa hakuna Mungu, kwa nini mnapigana naye? Ikiwa hayuko, basi inamaanisha kuwa hakuna mtu wa kupigana naye.’ Wasikilizaji wote wakaangua kicheko.”
NYAKATI ZOTE MHUBIRI ATARUDI
Hotuba za kuendeleza mawazo ya Kisovieti hazikutolewa kambini tu. Zilitolewa katika majiji makubwa kwa ajili ya umma. Wasemaji wenye uzoefu walitembelea hasa maeneo yaliyokuwa na Mashahidi wengi sana, kama vile Vorkuta, Inta, Ukhta, na Syktyvkar. Ndugu Gutshmidt anasema: “Mnamo 1957, msemaji mmoja alikuja kwenye Jumba la Utamaduni la wachimba migodi wa Inta, ambamo watu 300 walikuwa wamekusanyika. Alieleza imani za Mashahidi wa Yehova na jinsi wanavyohubiri. Baada ya kufafanua kwa usahihi mbinu za kuhubiri, ambazo zilitia ndani mapendekezo zaidi ya 15 tunayotumia katika ziara za kurudia, alisema: ‘Ikiwa hutampinga, nyakati zote mhubiri atarudi. Ikiwa bado humpingi katika ziara yake ya pili, atarudi mara ya tatu.’
“Kwa saa mbili alikuwa amezungumzia ziara sita kama hizo neno kwa neno kulingana na mbinu tulizotumia, naye akasoma maandiko yote yaliyotumiwa kutoka kwenye maandishi yake. Mke wangu, Polina, aliniandikia kuhusu hilo nilipokuwa nimefungwa katika kambi, naye akanieleza kwamba akina ndugu waliohudhuria hawakuamini waliyosikia. Baada ya hotuba hiyo, magazeti yalichapisha habari mbaya kuhusu Mashahidi, lakini hayakutoa ufafanuzi kamili kuhusu Ufalme. Isitoshe, hotuba hiyo yote ilitangazwa kwenye redio. Kwa sababu hiyo, maelfu ya wakaaji wa jiji walisikia jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyohubiri na mambo wanayohubiri.
“Mnamo 1962, msemaji kutoka Moscow alifika ili kutoa hotuba kuhusu Mashahidi wa Yehova. Baada ya kuzungumzia historia yao ya kisasa, akasema hivi: ‘Kila mwezi mamilioni ya dola humwagika huko Brooklyn kupitia michango ya kusaidia utendaji wa Mashahidi katika nchi kadhaa. Lakini hakuna hata kiongozi wao mmoja aliye na kabati kubwa la nguo. Wote hula pamoja katika chumba cha kulia chakula, mtunza-chumba pamoja na msimamizi, na hakuna tofauti kati yao. Wote huitana ndugu na dada, kama vile sisi huitana komredi.’
“Kimya kilitanda katika jumba hilo. Kisha akaongeza, ‘Lakini hatutafuata mawazo yao, ingawa yanaonekana kuwa mazuri, kwa kuwa tunataka kuwa na utaratibu kama huo bila kumhusisha Mungu, tutategemea mikono na vichwa vyetu wenyewe.’
“Hilo lilitutia moyo sana kwa sababu kwa mara ya kwanza, tulisikia ukweli kuhusu Mashahidi wa Yehova ukisemwa na wenye mamlaka. Hotuba kama hizo pia ziliwapa watu wengi nafasi za kusikia ukweli kuwahusu Mashahidi wa Yehova kutoka kwa wenye mamlaka. Hata hivyo, watu walihitaji kujionea kuwa mafundisho ya Biblia yanaweza kuboresha maisha yao.”
UPELELEZI HAUKUFAULU NYAKATI ZOTE
Kwa miaka mingi, shirika la KGB lilizoea kusikiliza mazungumzo ya simu, kukagua barua, na kutumia njia nyingine za kupeleleza. Nyakati nyingine maofisa wa KGB wangeweka vifaa vya kunasia mazungumzo nyumbani kwa akina ndugu walioongoza kutanikoni. Grigory Sivulsky, aliyekuwa mwangalizi wa wilaya kwa miaka 25 wakati wa marufuku, anakumbuka jinsi alivyogundua kifaa kimoja kama hicho kwenye dari la nyumba yake mnamo 1958: “Tuliishi huko Tulun, Siberia, kwenye orofa ya pili ya jengo moja nje ya mji. Wakati mmoja niliporudi nyumbani, nilisikia sauti ya mashini ikitoboa dari. Nilitambua maofisa wa KGB walikuwa wakiweka vifaa vya kunasia mazungumzo, mbinu waliyoitumia mara nyingi. Vichapo vingi vilikuwa darini na chini ya paa.
“Jioni, familia yangu iliporudi, niliwaambia kuhusu mashaka yangu nasi tukakubaliana kuwa tutaepuka kuzungumzia mambo ya kutaniko nyumbani. Tuliwasha redio kwa sauti ya juu na kuiacha hivyo juma lote. Mwishoni mwa juma, mimi na ndugu mmoja tulipanda darini na kukuta waya uliounganishwa na kifaa cha kunasia mazungumzo. Waya huo ulipita kati ya mbao mbili, ukapita kwenye paa, na kwenda moja kwa moja hadi jijini kwenye ofisi za KGB. Hakukuwa na shaka kwamba walikuwa wakirekodi kila kitu, lakini walifanikiwa tu kunasa vipindi vya redio.”
KGB YAJIPENYEZA NDANI YA TENGENEZO
Shirika la KGB liliona kwamba mnyanyaso wa moja kwa moja haungepunguza bidii ya Mashahidi. Basi kwa kutumia ujanja na ulaghai, wakaanza kupanda mbegu za shaka kati ya akina ndugu kuelekea wale waliokuwa wakisimamia na tengenezo kwa ujumla. Mbinu moja iliyotumiwa na KGB ilikuwa kupenyeza maofisa wake wenye uzoefu kutanikoni.
Maofisa kadhaa walifanikiwa kusimamia mambo ndani ya tengenezo. Ndugu hao wasio wa kweli walifanya yote waliyoweza kupunguza kazi ya kuhubiri na kutokeza woga na ukosefu wa uhakika uliowafanya watu wawashuku ndugu wanaoongoza. Zaidi ya hayo, walizuia vichapo vya Biblia visiwafikie akina ndugu na wakavipeleka kwenye shirika la KGB. Ripoti moja inasema kwamba maofisa wawili tu waliofanya hivyo kuanzia 1957 hadi 1959 walipeleka zaidi ya nakala 500 za Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine.
Katikati ya miaka ya 1950, ndugu fulani walianza kupoteza imani katika Halmashauri ya Nchi. Uvumi ulienea kwamba baadhi ya washiriki wa Halmashauri ya Nchi walishirikiana na maofisa wa KGB na waliwasaliti akina ndugu waaminifu, kutia ndani wale waliokuwa wakipiga chapa vichapo vyetu. Ivan Pashkovsky anasimulia: “Mnamo Aprili 1959 Halmashauri mpya ya Nchi iliundwa, nami nilikuwa mshiriki wake. Tuliazimia kutetea kweli haidhuru jitihada za Ibilisi za kuvuruga undugu wetu. Kipindi kigumu zaidi katika historia ya Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti kilikuwa kimeanza.”
Shaka zilipoendelea kuongezeka, ndugu fulani waliacha kutuma ripoti za kutaniko kwenye Halmashauri ya Nchi. Wahubiri makutanikoni walihubiri kwa bidii na kutoa ripoti kwa kawaida, lakini hawakujua ripoti zao hazikuwa zinatumwa kwa Halmashauri ya Nchi. Kufikia 1958, kikundi fulani cha akina ndugu kilisababisha maelfu wahubiri wasiwasiliane na Halmashauri ya Nchi. Kwenye miji ya Irkutsk na Tomsk na baadaye kwenye majiji mengine ya Urusi, vikundi vya akina ndugu vilivyojitenga na tengenezo viliendelea kuongezeka. Mnamo Machi 1958, vikundi hivyo vilikuwa vimeanzisha ‘halmashauri yao ya nchi’ vikitazamia itatambuliwa na makutaniko yote.
Baraza Linaloongoza lilifanya kila kitu ili kuwasaidia akina ndugu katika Muungano wa Sovieti warudishe umoja wao katika ibada ya Yehova. Alfred Rütimann, aliyekuwa akiishi Uswisi, alikuwa meneja wa tawi kwenye Ofisi ya Ulaya Kaskazini, ambayo ilisimamia kazi ya kuhubiri ya Muungano wa Sovieti. Mnamo 1959, aliwatumia ndugu nchini Urusi barua akieleza kuwa Yehova atawabariki wale tu wanaodumisha umoja na wanaohubiri habari njema ya Ufalme. Ndugu fulani waliojitenga walikubali na wakaanza kuiamini tena Halmashauri ya Nchi. Hata hivyo, ilichukua miaka mingi kabla ya kurudisha uhakika wao. Muda wote huo, Halmashauri ya Nchi ilisambaza vichapo vya Biblia kupitia ndugu fulani. Ingawa ndugu waliojitenga walisoma vichapo, bado hawakutoa ripoti zao.
Shirika la KGB liliendelea kupanda mbegu za shaka kati ya akina ndugu. Nyakati nyingine, ndugu fulani hawakufungwa, ilhali wengine walifungwa gerezani. Kwa hiyo, akina ndugu walifikiri kuwa wale walioachwa walikuwa wakishirikiana na KGB. Wengi waliwashuku na kuwachambua sana ndugu waliokuwa wakiongoza.
KESI ILIYOTANGAZWA SANA
Ripoti iliyotumwa Moscow na ofisa fulani wa serikali kutoka Irkutsk ilisema hivi: “[Mashahidi wa Yehova katika Wilaya ya Irkutsk] walifanya utendaji mwingi kwa siri. Katika miezi sita ya mwisho ya mwaka wa 1959, shirika la KGB liligundua mashini tano za kuchapishia zilizokuwa kwenye chumba cha chini.” Mashini hizo zilikuwa katika miji ya Zima na Tulun, huko Siberia na pia vijiji vya Kitoy, Oktyabr’skiy, na Zalari. Baada ya mashini hizo kugunduliwa, waliohusika katika uchapishaji huo walikamatwa.
Ndugu wanne waliokamatwa mwanzoni waliandikisha taarifa kuhusu uchapishaji wa vichapo. Kwa hila, wapelelezi waliwalazimisha ndugu hao kuandikisha taarifa hizo. Kisha KGB ikabadilisha taarifa hizo na kuzichapisha kwenye magazeti ya habari. Ndugu hao wanne waliachiliwa huru na ndugu wengine wanane wakashikwa. Kesi yao ingesikilizwa huko Tulun Aprili 1960. KGB ilifanya mipango ili kesi hiyo itangazwe sana. Walipanga kuwatumia wale ndugu wanne kuwa mashahidi wa upande wa mashtaka. Wengi katika makutaniko walifikiri kwamba ndugu hao walikuwa wakishirikiana na KGB.
Wapelelezi wa KGB walinuia kutumia kesi hiyo kuvunja imani ya Shahidi yeyote ambaye angefika mahakamani na kuchochea watu wawachukie Mashahidi. Wakiwa na hilo akilini, wapelelezi wa KGB walipanga watu watembelee chumba kimoja cha chini ambacho akina ndugu walikitumia kuchapisha vichapo kwa miaka mingi. Muda si muda, kulikuwa na uvumi kuhusu utendaji wa “madhehebu” ya siri. Siku ya kesi ilipofika, ukumbi wa mahakama ulijaa watu zaidi ya 300, kutia ndani waandishi wa habari wa magazeti na televisheni, na wengine wao walisafiri kutoka Moscow. Pia Mashahidi wengi wa Yehova walikuwepo.
VURUGU MAHAKAMANI
Hata hivyo, bila kutarajia, mipango ya KGB ilianza kuharibika. Ndugu walioandikisha taarifa hizo waligundua kosa lao. Siku moja kabla ya kesi, wote waliazimia kufanya chochote wanachoweza ili kumpa Yehova utukufu. Wakati wa kesi, walisema kwamba walikuwa wamedanganywa na kwamba taarifa walizoandikisha zilikuwa zimebadilishwa. Kisha wakatangaza hivi: “Tuko tayari kuketi kizimbani pamoja na ndugu zetu.” Kukawa na vurugu mahakamani.
Zaidi ya hayo, walipokuwa wanaulizwa maswali, ndugu waliokuwa kizimbani walifaulu kuyajibu bila kuwasaliti wengine. Kwa mfano, wakati hakimu alipomuuliza Grigory Timchuk ni nani aliyetengeneza mashini ya kuchapishia nyumbani kwake, alijibu, “Mimi ndiye niliyeitengeneza.” Alipoulizwa ni nani aliyechapisha vichapo, alijibu, “Ni mimi.” Alipoulizwa ni nani aliyekuwa akivisambaza vichapo hivyo, alijibu, “Ni mimi.” Alipoulizwa ni nani aliyenunua na kumletea karatasi, kwa mara nyingine alijibu, “Mimi ndiye niliyefanya hivyo pia.” Kisha mwendesha-mashtaka akamuuliza: “Kwani wewe ni nani? Je, wewe ndiye meneja, mleta-bidhaa, na mfanyakazi?”
“BARUA HIYO ILITUTIA MOYO SANA!”
Ilipoonekana hakuna mashahidi upande wa mashtaka, mwendesha-mashtaka aliwashutumu akina ndugu kwamba walikuwa wamepanga njama na wageni. Ili kuthibitisha hilo, alitoa barua kutoka kwa Nathan H. Knorr wa Betheli ya Brooklyn. Mikhail Savitsky, mmoja kati ya akina ndugu waliohudhuria kesi hiyo, anasema: “Kwa sauti mwendesha-mashtaka alianza kusoma barua moja kutoka kwa Ndugu Knorr aliyowaandikia akina ndugu katika Muungano wa Sovieti, ambayo ilikuwa imenaswa na KGB. Mashahidi waliokuwa ukumbini, waliona barua hiyo kama zawadi kutoka kwa Yehova. Ilitutia moyo sana! Tulisikia mashauri yenye hekima kutoka katika Biblia na tulitiwa moyo kuwatumikia ndugu zetu kwa upendo na kuwa waaminifu chini ya majaribu. Isitoshe, Mashahidi wa Yehova walihimizwa wamtegemee Mungu katika mambo yote, wamwombe hekima na mwongozo, na pia washirikiane kwa ukaribu na ndugu waliowekwa rasmi. Mwendesha-mashtaka aliisoma barua hiyo kuanzia mwanzo hadi mwisho. Tulisikiliza kwa makini sana. Ni kana kwamba tulikuwa tumehudhuria kusanyiko!” Ingawa ndugu hao walihukumiwa vifungo mbalimbali, wote waliohudhuria walibaki imara katika azimio lao la kumtumikia Yehova.
KUUNGANA TENA KWA FURAHA KATIKA IBADA
Ilionekana ni kana kwamba KGB walifanikiwa kusimamisha utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti, kwa hiyo wakajitayarisha kwa ajili ya shambulizi la mwisho. Mnamo 1960, zaidi ya ndugu 450 walijikuta wamefungwa kwenye kambi moja huko Mordvinia. Ndugu hao walitia ndani wale waliosimamia kazi katika vikundi vyote viwili, yaani, wale waliokuwa wamejitenga na tengenezo na wale ambao hawakuwa wamejitenga. Wapelelezi wa KGB walifikiri kuwa hilo lingewatenganisha kabisa akina ndugu katika tengenezo. Makala yenye dhihaka ilichapishwa katika gazeti la kambi hiyo ya kazi ngumu ikieleza ndugu gani atapigana na nani. Kinyume cha hilo akina ndugu walitumia nafasi hiyo ya kuwa pamoja kuungana.
Iov Andronic anakumbuka hivi: “Ndugu wenye madaraka walimtia moyo kila Shahidi, kutia ndani hata wale waliojitenga na tengenezo kujitahidi kuwa na umoja. Ndugu hao walikazia uangalifu makala ya Kirusi ya Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1961, yenye kichwa ‘Umoja wa Watu Wote Wenye Nia Nzuri Waahidiwa.’ Makala hiyo ilitoa kanuni na mifano iliyoonyesha jinsi ambavyo Yehova aliwaongoza watu wake nyakati za zamani. Pia, ilizungumzia umuhimu wa kila mmoja kujitahidi kuwa na amani na umoja katika kutaniko la Kikristo. Baada ya kusoma makala hiyo kwa uangalifu, wengi walitambua umuhimu wa umoja wa kitheokrasi na wakafanya mabadiliko yaliyohitajiwa.”
CHAKULA CHA KIROHO KILICHOPONYA
Makala hiyo ya Mnara wa Mlinzi iliwasaidia pia Mashahidi ambao hawakuwa gerezani kuwa na umoja. Ndugu waliowekwa rasmi kusimamia kazi walisali na kuisoma pamoja. Makala hiyo ilisema kwamba, kwa sababu Ndugu Rutherford alikuwa mgonjwa, alitoa hotuba yake ya mwisho katika kusanyiko mnamo Agosti 1941. Akiwatia moyo akina ndugu washikamane na tengenezo la Yehova na wasimfuate kiongozi yeyote wa kibinadamu, alisema hivi: ‘Kila mara jambo fulani linapozuka na kuanza kukua, watu husema kwamba kuna mtu fulani, kiongozi aliye na wafuasi wengi. Ikiwa kuna yeyote hapa anayeamini kwamba mimi ni mmoja wa watumishi wa Bwana na kwamba tunafanya kazi bega kwa bega katika umoja kumtumikia Mungu na kumtumikia Kristo, na aseme Ndiyo.’ Wote walijibu waziwazi na kwa nguvu “Ndiyo!”
Mikhail Savitsky anakumbuka hivi: “Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti walihitaji sana kuwa na umoja wakati huo. Tulimshukuru sana Yehova kwa jinsi alivyotutegemeza kiroho kwa upendo na subira. Mara tu baada ya kusikia makala hiyo ikisomwa, ndugu mmoja aliyekuwa amejitenga na tengenezo aliniambia hivi, ‘Naomba gazeti hilo ili nikalisome pamoja na ndugu wengine huko Bratsk na maeneo mengine.’ Nilimwambia kwamba tulikuwa na gazeti moja tu. Lakini alinihakikishia kwamba atanirudishia baada ya juma moja. Alirudisha gazeti hilo pamoja na ripoti za utumishi za muda mrefu za makutaniko mengi. Mamia ya akina ndugu na dada walirudi katika familia yenye umoja ya waabudu wa Yehova.”
Ivan Pashkovsky, mshiriki wa Halmashauri ya Nchi kwa zaidi ya miaka 30, anakumbuka hivi: “Kupitia ndugu mmoja aliyetoka ng’ambo, tulimwomba Ndugu Knorr awaombe ndugu wote katika nchi yetu waungane na kujitiisha chini ya mpango wa kitheokrasi. Ndugu Knorr alikubali, na mnamo 1962, tulipokea nakala 25 za barua yake katika lugha mbili, Kiingereza na Kirusi. Barua hiyo iliwafanya ndugu wengi watambue kwamba wanahitaji kutumikia pamoja na tengenezo.”
KONDOO WANAISIKIA SAUTI YA MCHUNGAJI WAO
Halmashauri ya Nchi ilijitahidi sana kuwaunganisha akina ndugu. Chini ya hali zilizokuwepo, hilo halikuwa jambo rahisi. Kufikia kiangazi cha 1962, wilaya nzima ilikuwa imeunganishwa na tengenezo. Akina ndugu waliokomaa kiroho waliwekwa rasmi kuwa washiriki wa halmashauri ya pekee. Yehova alibariki jitihada za akina ndugu hao na akawapa “hekima inayotoka juu.” (Yak. 3:17) Aleksey Gaburyak, aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko kuanzia 1986 mpaka 1995, anakumbuka hivi: “Tulikutana na washiriki wa Halmashauri ya Nchi huko Usol’ye-Sibirskoye mwaka wa 1965. Ndugu hao walituomba tuwatafute ndugu na dada wote waliokuwa wametawanyika kwa sababu ya kuhamishwa, kufungwa gerezani, au kwa sababu ya mgawanyiko uliokuwepo na kuwaunganisha tena na makutaniko. Tulipewa anwani kadhaa. Eneo langu lilitia ndani wilaya ya Tomsk na Kemerovo na pia majiji ya Novokuznetsk na Novosibirsk. Ndugu wengine walipewa maeneo tofauti. Tulipaswa kupanga makutaniko na vikundi mbalimbali na pia kuwaweka rasmi na kuwazoeza ndugu wanaostahili. Isitoshe, tulihitaji kupanga jinsi ambavyo vichapo vingewafikia akina ndugu na kupanga mikutano ya kutaniko chini ya marufuku. Kwa muda mfupi tu, tulifanikiwa kuwatembelea ndugu na dada 84 ambao walikuwa wametenganishwa na tengenezo. Jinsi tulivyofurahi kuona kwamba ‘kondoo’ wa Yehova walisikia tena sauti ya Mchungaji Mwema na walimtumikia pamoja na watu wake!”—Yoh. 10:16.
Muda si muda wengi waliokuwa wametenganishwa na tengenezo walijiunga tena na Halmashauri ya Nchi na wakaanza kutuma ripoti zao za utumishi wa shambani. Kufikia mwaka wa 1971, zaidi ya wahubiri 4,500 walikuwa wamejiunga tena na tengenezo la Yehova. Licha ya marufuku iliyokuwepo, kufikia miaka ya katikati ya 1980, kazi ya kuhubiri ilikuwa ikiendelea na wapya walikuwa wakiongezeka katika makutaniko.
MIKANDA YA KAMERA YENYE MAANDISHI MADOGO SANA
Sikuzote, kutoa nakala za chakula cha kiroho kulihitaji jitihada kubwa za akina ndugu waangalifu lakini wenye ujasiri wa Muungano wa Sovieti. Hata hivyo, ndugu hao walitoa wapi chakula hicho cha kiroho?
Njia moja kuu ilikuwa ni kupitia mikanda yenye maandishi madogo. Ndugu waliokuwa katika nchi jirani, walipiga picha magazeti, vitabu, na broshua zilizokuwa zimechapishwa katika Kirusi na Kiukrainia na pia katika lugha nyingine nyingi. Kwa kutumia kamera yenye mkanda wenye urefu wa mita 30, unaoweza kufanya maandishi yawe madogo, walipiga picha ukurasa mmoja hadi mwingine kwa uangalifu sana. Kila kichapo kilipigwa picha mara kadhaa, ili kutokeza nakala nyingi za kugawanywa. Kwa miaka mingi chakula cha kiroho kilipatikana kwa njia hiyo hivi kwamba ikiwa mikanda hiyo ingeunganishwa, ingekuwa na urefu wa kilomita nyingi. Ili iwe rahisi mikanda hiyo kubebwa na kuingizwa katika Muungano wa Sovieti, ilikatwa katika vipande vyenye urefu wa sentimita 20 hivi.
MASHINI ZA KUCHAPISHA KWA SIRI HUKO SIBERIA
Kuchapisha nakala za vichapo vya Biblia haikuwa rahisi, lakini Yehova alibariki kazi hiyo. Kati ya mwaka wa 1949 na 1950, akina ndugu walichapisha na kusambaza nakala 47,165 za vichapo mbalimbali kwenye makutaniko. Kuongezea hilo, licha ya upinzani mkali, Halmashauri ya Nchi iliripoti kwamba katika kipindi hicho, mikutano 31,488 ilifanywa nchini humo.
Uhitaji wa vichapo uliendelea kuwa mkubwa, jambo lililosababisha kuwe na uhitaji wa mashini mpya za kuchapishia. Stakh Savitsky anasema hivi: “Mnamo 1955, tulianza kuchapisha kwa siri nyumbani kwetu. Kwa kuwa baba yangu hakuwa Shahidi wa Yehova tulilazimika kumwomba ruhusa. Kwa muda wa miezi miwili hivi, tulichimba shimo lenye upana wa mita 2 na urefu wa mita 4, liwe kama chumba chini ya varanda yetu. Katika kipindi hicho, tulichimba udongo unaoweza kubebwa na toroli (wheelbarrow) 300 hivi. Ilibidi tutoe udongo huo nje na kuuficha ili kwamba mtu yeyote asigundue ni nini kinachoendelea. Tulipochimba mita moja na nusu tulikuta ardhi iliyoganda. Hivyo, tulipokuwa kazini, Mama aliyeyusha udongo huo kwa moto mdogo wa kuni huku akijaribu asivute uangalifu wa majirani. Baadaye tuliweka mbao sehemu hiyo ili kutengeneza chumba. Baada ya chumba hicho kuwa tayari wenzi fulani waliingia. Walipaswa kufanya kazi na kuishi kwenye chumba hicho cha chini. Mama aliwapikia chakula, akawafulia nguo, na kuwatunza. Mahali hapo pa kuchapishia palitumiwa hadi mwaka wa 1959.
“Mnamo 1957, ndugu waliokuwa wakisimamia kazi ya kuchapisha vichapo waliniuliza: ‘Je, unaweza kufanya kazi mahali pa kuchapishia? Tunahitaji kuchapisha angalau magazeti 200 kwa mwezi.’ Mara ya kwanza nilichapisha magazeti 200, kisha 500. Hata hivyo, uhitaji wa magazeti ulizidi kuongezeka. Kazi hiyo ilipaswa kufanywa usiku kwa sababu sisi tuliokuwa uhamishoni tulipaswa kufanya kazi za uzalishaji chini ya msimamizi wakati wa mchana na tulikuwa na siku moja tu ya mapumziko.
“Mara niliporudi kutoka kazini, nilikuwa nikiingia kwenye chumba cha chini cha kuchapishia. Ni kana kwamba sikuwa nikilala kwa sababu kazi ya kuchapisha ikianza, haingeweza kusimamishwa. Wino ungeweza kukauka, hivyo haingewezekana kukatiza kazi hiyo na kuendelea wakati mwingine. Wakati mwingine nililazimika kuchapisha kurasa 500 na kisha kuzipitia kurasa hizo nikifanya masahihisho kwa sindano ili ziweze kusomeka vizuri. Kulikuwa na sehemu ndogo sana ya kuingiza hewa, hivyo ilikuwa vigumu kwa kurasa zilizotoka tu kuchapishwa kukauka.
“Usiku, nilipeleka magazeti niliyochapisha katika mji wa Tulun, ambao uko kilomita 20 kutoka nyumbani. Baada ya hapo sikujua magazeti hayo yalipelekwa wapi, lakini nilijua yalikuwa yakitumiwa na Mashahidi huko Krasnoyarsk, Bratsk, Usol’ye-Sibirskoye, na majiji na miji mingine.
“Mnamo 1959, ndugu waliokuwa wakisimamia utendaji huo waliniomba nikasaidie kujenga mahali pengine pa kuchapishia huko Tulun, karibu na kituo cha reli. Kwa mara nyingine tena nilianza kufanya kazi kama zile nilizokuwa nimefanya kwenye mahali pa kuchapishia pa awali, kama vile kuchimba udongo na kuingiza umeme. Yehova alitupa hekima. Kisha familia fulani ilihamia mahali hapo na kufanya kazi humo kwa karibu mwaka mzima. Hatimaye, wapelelezi wa KGB walipagundua mahali hapo pa kuchapishia. Iliripotiwa hivi kwenye gazeti la habari la mji huo, ‘umeme uliingizwa katika njia ambayo ilikuwa vigumu hata kwa wataalamu wa umeme kuielewa.’
“Mbali na familia yetu ni ndugu wachache sana waliojua kuhusu kazi ya kuchapisha. Kwa kuwa hakuna yeyote aliyekuwa akiniona nyakati za jioni, ndugu na dada kutanikoni walikuwa na hofu kuhusu hali yangu ya kiroho. Walikuwa wakija nyumbani kwangu kunitembelea ili kunitia moyo, lakini nyakati zote nilikuwa sipatikani. Ndiyo, nyakati hizo tulipokuwa tukichunguzwa sana, utendaji katika mahali pa kuchapishia ulikuwa wa siri sana.”
KUCHAPISHA VICHAPO HUKO MOSCOW
Wenye mamlaka walijua kwamba Mashahidi walikuwa na uhitaji mkubwa sana wa Biblia na vichapo vya Biblia. Baraza Linaloongoza liliomba mara kadhaa ruhusa ya kuchapisha au kuingiza nchini vichapo vya Biblia lakini maombi hayo yalipuuzwa. Kwa kuwa kulikuwa na upungufu mkubwa hivyo wa vichapo, akina ndugu walikuwa wakitafuta njia za kuchapisha vichapo sehemu mbalimbali nchini humo, kutia ndani Moscow, ili kutoa chakula cha kiroho kwa ajili ya makutaniko na vikundi.
Mnamo 1957, Stepan Levitsky, alihukumiwa kifungo cha miaka kumi kwa kosa la kuwa na nakala moja ya Mnara wa Mlinzi, iliyopatikana chini ya kitambaa cha mezani kwenye chumba cha kulia. Stepan anaeleza hivi: “Baada kutumikia kifungo kwa miaka mitatu na nusu, Mahakama Kuu ilifutilia mbali kifungo changu. Kabla ya kuachiliwa kwangu akina ndugu walipendekeza kwamba baada ya kuachiliwa nihamie sehemu iliyo karibu na Moscow ili nihubiri na kushiriki katika utendaji mwingine wa kiroho. Niliishi eneo lililokuwa mwendo wa saa mbili kutoka Moscow na kuanza kuhubiri katika maeneo mbalimbali ya mji huo mkuu. Yehova alibariki jitihada hizo, kwani baada ya miaka michache, kikundi cha akina ndugu na dada kiliundwa huko Moscow. Mnamo 1970, nilipangiwa mzunguko ambao ulitia ndani Moscow, Leningrad (sasa ni St. Petersburg), Gorki (sasa ni Nizhniy Novgorod), Orel, na Tula. Nilipaswa kusimamia kazi ya kuyasambazia makutaniko vichapo.
“Nilikuwa na hakika kwamba yalikuwa ni mapenzi ya Yehova kwamba Moscow na sehemu nyingine za Urusi zipate vichapo vya kutosha vinavyotegemea Biblia. Katika sala nilimweleza Yehova kwamba niko tayari kufanya kazi hiyo. Muda si muda nikafahamiana na mtaalamu mmoja wa uchapishaji ambaye alijua viwanda kadhaa vya uchapishaji huko Moscow. Katika njia ambayo haingezua shaka, nilimuuliza kama inawezekana kuchapisha toleo la kitabu fulani kidogo kwenye kiwanda cha uchapishaji huko Moscow.
“Akaniuliza, ‘Ni kitabu gani?’
“Kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana,” nikamjibu nikiwa na wasiwasi.
“Rafiki yake wa karibu alikuwa akifanya kazi kwenye moja ya viwanda hivyo. Rafiki huyo alikuwa ni Mkomunisti na alikuwa kiongozi wa chama. Alikubali kuchapisha idadi fulani ya vitabu kwa malipo. Jinsi ilivyofurahisha kwa akina ndugu hatimaye kuwa na kichapo hicho cha kujifunzia Biblia!
“Ilikuwa hatari sana kwangu na kwa mchapishaji huyo kuchapisha vichapo kwa njia hiyo. Baada ya kila idadi fulani ya vichapo kuchapishwa, vilipaswa kutolewa kiwandani haraka bila mtu yeyote kugundua. Kwa kawaida kazi hiyo ilifanywa usiku. Yehova alibariki mpango huo na vichapo vingi vya Biblia vilichapishwa katika kiwanda hicho, kutia ndani vitabu “The Truth Shall Make You Free,” Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, na pia kitabu cha nyimbo! Kwa kweli, hicho kilikuwa chakula kwa wakati unaofaa. (Mt. 24:45) Tuliweza kutumia kiwanda hicho kwa miaka tisa.
“Lakini siku moja, msimamizi wa kiwanda alifika ghafula kiwandani hapo kichapo chetu kilipokuwa kikichapishwa. Mtu aliyekuwa akichapisha alibadilisha vitu fulani katika mashini na ikaanza kuchapisha gazeti linalohusu mambo ya afya. Lakini kwa kuwa alifanya haraka, aliweka kurasa sita za kichapo chetu kimakosa ndani ya gazeti hilo na msimamizi akaenda na gazeti moja ofisini mwake. Alipokuwa akisoma gazeti hilo, alishangaa sana kukuta makala iliyokuwa ikizungumzia mambo tofauti kabisa. Alimwita mchapishaji na kumuuliza makala hiyo iliingiaje ndani ya gazeti hilo. Baada ya tukio hilo, KGB walianza kufuatilia kisa hicho. Mchapishaji alipotishwa kwamba atafungwa kifungo kirefu, aliwaambia kila kitu alichojua. Kwa hiyo, wapelelezi wa KGB walinikamata kwa sababu mimi ndiye niliyekuwa ninafahamika kuwa Shahidi wa Yehova pekee mjini Moscow. Nilihukumiwa kifungo cha miaka mitano na nusu.” Mchapishaji alihukumiwa miaka mitatu.
“ACHA HAR-MAGEDONI IJE!”
Ndugu na dada wengi walitumikia vifungo virefu gerezani. Grigory Gatilov alitumikia miaka 15 gerezani naye anakumbuka hivi: “Gereza la mwisho nililofungwa lilikuwa na jina la kupendeza: Liliitwa Bata-Maji Mweupe. Gereza hilo lilikuwa katika eneo linalopendeza huko Caucasus juu ya moja kati ya milima mitano iliyo karibu na mji wa kitalii wa Pyatigorsk. Katika gereza hilo, nilipata nafasi kuwahubiria watu mbalimbali mwaka mzima. Seli yangu ilikuwa ‘eneo’ zuri la kuhubiri na sikuhitaji kwenda popote. Askari wa gereza waliwaleta watu wapya kwenye seli yangu na kuwahamisha baada ya siku kadhaa lakini mimi nilibaki. Ni mara chache sana nilihamishiwa katika seli nyingine. Nilijaribu kumhubiria kila mtu kuhusu Ufalme wa Yehova. Watu wengi walikuwa na maswali kuhusu Har–Magedoni. Wafungwa fulani walishangaa kwamba mtu anaweza kufungwa kifungo kirefu hivyo kwa sababu ya imani yake. ‘Kwa nini usikane imani yako na kwenda nyumbani?’ waliuliza wafungwa wenzangu na mara nyingine hata askari wa gereza. Nilifurahi sana kila wakati mtu fulani alipopendezwa na kweli. Wakati mmoja mtu fulani aliandika kwenye kuta za seli, ‘Acha Har–Magedoni ije!’ Ingawa maisha ya gerezani hayakuwa yenye kufurahisha, nilifurahi kwamba niliweza kuzungumza kuhusu kweli.”
“JE, KUNA WAYONADABU KATI YENU?”
Dada wengi Wakristo wenye bidii katika utumishi wa Yehova walifungwa gerezani pia. (Zab. 68:11) Zinaida Kozyreva anakumbuka jinsi akina dada walivyokuwa na upendo kati yao na kuelekea wafungwa wengine: “Mnamo 1959, muda usiozidi mwaka mmoja tangu nilipobatizwa, mimi, Vera Mikhailova, na Lyudmila Yevstafyeva, tulipelekwa kwenye kambi huko Kemerovo, Siberia. Kambi hiyo ilikuwa na wafungwa 550. Tulipofika tulikuta wanawake kadhaa wamesimama kwenye lango.
“Wakauliza hivi: ‘Je, kuna Wayonadabu kati yenu?’
“Tuligundua kwamba hao walikuwa dada zetu wapendwa. Mara moja walitupa chakula na kutuuliza maswali. Nyuso zao zilionyesha uchangamfu na upendo wa kweli, jambo ambalo sikuwa nimeliona katika familia yangu. Kwa kuwa walijua kwamba sisi ni wageni kambini, dada hao walitutegemeza. (Mt. 28:20) Baada ya muda mfupi tulitambua kwamba mambo ya kiroho yalikuwa yamepangwa vizuri katika kambi hiyo.
“Tukawa kama familia ya kweli. Tulifurahia hasa kipindi cha kiangazi tulipokuwa tukikata nyasi kavu. Wasimamizi wa kambi hawakuwa na hofu kwamba tungetoroka au kuvunja sheria za kambi. Askari mmoja angewalinda dada 20 au 25, ingawa kwa kweli, sisi ndio tuliomlinda! Mtu alipokaribia tungemwamsha ili asiadhibiwe kwa kulala kazini. Alipokuwa amelala, tulizungumzia mambo ya kiroho katika kipindi cha mapumziko. Mpango huo ulikuwa mzuri kwetu na kwake pia.
“Mwishoni mwa mwaka wa 1959, mimi na dada wengine tulipelekwa katika kambi yenye ulinzi mkali. Tulifungiwa kwenye seli yenye baridi ambayo haikuwa na kioo kwenye dirisha. Usiku tulilala kwenye mbao na mchana tulifanya kazi. Wenye mamlaka walitupa kazi ya kuchambua mboga huku wakichunguza tabia zetu. Punde si punde walipoona kwamba hatukuiba kama wafungwa wengine, walituletea nyasi za kulalia na wakaweka kioo kwenye dirisha. Tulikaa kwenye kambi hiyo kwa mwaka mmoja kisha akina dada wote tulihamishiwa kwenye kambi isiyo na ulinzi mkali huko Irkutsk.
“Kambi hiyo ilikuwa na dada 120 hivi. Tulikaa humo kwa mwaka mmoja na miezi mitatu. Majira ya baridi ya kwanza tukiwa huko yalikuwa na baridi kali na theluji nyingi. Tulifanya kazi ngumu katika kiwanda cha mbao. Wanyapara walitupekua mara nyingi wakitafuta vichapo. Ni kama hawakuwa na jambo lingine la kufanya. Tulikuwa na ustadi wa kuficha vichapo hivi kwamba hata nyakati nyingine tulisahau mahali tulipoviweka. Pindi mmoja, mimi na Vera tulificha vikaratasi vilivyokuwa na andiko la siku kwenye makoti yetu ya kazi hivi kwamba sisi wenyewe hatungeweza kuvipata. Lakini mnyapara alivipata na tukafungwa kifungo cha upweke kwa siku tano. Nje kulikuwa na baridi ya nyuzi 40 selsiasi chini ya sufuri na barafu ilifunika kuta za seli hiyo ambayo haikuwa na mfumo wa kupashia joto.
“Kulikuwa na mabenchi yaliyotengenezwa kwa saruji ambayo mtu angeweza kukalia. Tulipohisi baridi sana, tulikunja miguu yetu ukutani tukaketi migongo yetu ikiwa imeshikana na tukalala tukiwa hivyo. Tulipoamka ghafula tulisimama haraka tukihofia kuganda hadi kufa tukiwa tumelala. Tulipewa glasi yenye maji moto na mkate mweusi wa gramu 300 kila siku. Licha ya hayo tulikuwa na furaha kwa kuwa Yehova alitupa ‘nguvu zinazopita zile za kawaida.’ (2 Kor. 4:7) Akina dada walitutendea kwa fadhili tuliporudi kambini. Walitupikia chakula na kutupashia maji moto ili tuweze kuoga.”
“ANAWEZA KUISHI NA WENGINE KWA AMANI”
Zinaida anaendelea kusema hivi: “Ilikuwa vigumu kuhubiri kwenye kambi hiyo kwa sababu kulikuwa na wafungwa wachache na kila mtu aliwajua Mashahidi. Kanuni inayopatikana kwenye 1 Petro 3:1 ilifaa katika hali hiyo. Tuliiita kuhubiri pasipo maneno. Tuliweka kambi yetu ikiwa safi na nadhifu na tulikuwa wenye urafiki na tulishirikiana kwa ukaribu na dada zetu. (Yohana 13:34, 35) Isitoshe tulikuwa na uhusiano mzuri na wafungwa wengine ambao hawakuwa Mashahidi. Tulijitahidi kujiendesha kulingana na Neno la Mungu na tuliwajali wengine. Nyakati nyingine tuliwasaidia kwa njia mbalimbali watu ambao si Mashahidi. Kwa mfano, dada mmoja aliwasaidia wafungwa wengine kufanya hesabu ilipohitajika. Watu wengi walitambua kuwa Mashahidi walikuwa tofauti na watu wa dini nyingine.
“Mnamo 1962, tulihamishwa kutoka kambi ya Irkutsk na kupelekwa hadi kambi moja huko Mordvinia. Tukiwa huko tulijaribu pia kuwa safi na nadhifu. Vitanda vyetu vilikuwa safi na nadhifu kila wakati. Kambi hiyo ilikuwa na wafungwa 50 hivi, wengi wao wakiwa dada zetu. Dada zetu ndio waliofanya kazi ya usafi kwa kuwa wafungwa wengine hawakuipenda kazi hiyo. Sakafu za kambi hiyo zilisafishwa na kusuguliwa kila mara, na wasimamizi wa kambi walitupa vifaa tulivyohitaji. Kulikuwa na watawa wa kike na watu wenye elimu kambini lakini walikataa kufanya kazi hiyo. Kwa hiyo usafi wa kambi ulitegemea jitihada zetu. Kila mara mmoja wa dada zetu alipoachiliwa huru, ripoti kuhusu tabia yake ilisema kwamba yeye ‘anaweza kubadilikana kulingana na hali na anaweza kuishi na wengine kwa amani.’”
MAUA MAREFU YANAKUWA MAHALI PA KUJIFICHA
Zinaida anasema hivi: “Wakati mmoja, dada kadhaa waliziandikia familia zao barua wakiomba mbegu za mimea inayochanua maua makubwa. Tuliwaambia wasimamizi wa kambi kwamba tulitaka kupanda maua maridadi na kuomba tupewe udongo mweusi wenye rutuba kwa kusudi hilo. Tulishangaa walipokubali mara moja. Tulipanda maua ndani ya kambi na kwenye vijia vya kambi hiyo. Muda si muda kambi hiyo ilikuwa na vichaka virefu vya maua ya waridi na maua mengine maridadi na marefu. Bustani iliyokuwa katikati ya kambi ilikuwa na maua maridadi ya dalia na vichaka virefu vya maua ya daisy yenye rangi mbalimbali. Tulitembea huko, tukajifunza Biblia nyuma ya maua na kuficha vichapo vyetu katika vichaka vya waridi.
“Tulifanya mikutano yetu tulipokuwa tukitembea. Tulijigawa katika vikundi vya watu watano. Kila mmoja wa akina dada alikariri mapema fungu moja kati ya mafungu matano kutoka katika kichapo kinachozungumzia Biblia. Kisha baada ya kufungua kwa sala, tungerudia mafungu tuliyokariri na kuyazungumzia. Baada ya kumaliza kwa sala, tuliendelea na matembezi yetu. Magazeti yetu ya Mnara wa Mlinzi yalikuwa vijitabu vidogo [kama picha inayoonyeshwa kwenye ukurasa wa 161]. Kila siku tulijifunza jambo fulani, hasa andiko la siku na kukariri mafungu katika mikutano yetu ambayo tulifanya mara tatu kwa juma. Na si hayo tu, tulijitahidi kukariri sura nzima-nzima za Biblia na kuzirudia ili kutiana nguvu. Kwa njia hiyo hatukuathirika sana vichapo vyetu vilipotwaliwa wakati wa msako.
“Ingawa wasimamizi wa kambi walijaribu kuwauliza wafungwa wengine jinsi ambavyo utendaji wetu ulivyokuwa ukiendeshwa kambini, wafungwa wengi walishirikiana nasi. Kwenye kambi hiyo tulifungwa pamoja na Olga Ivinskaya, ambaye alikuwa rafiki ya mtunga-mashairi na mwandishi maarufu Boris Pasternak, aliyepokea Tuzo la Nobeli kwa vitabu vyake. Olga Ivinskaya, alikuwa mwandishi na kwa kuwa aliwapenda Mashahidi alifurahia kuona jinsi utendaji wao ulivyoendeshwa kambini. Yehova alitupa hekima hasa ili tuweze kuwa na chakula cha kiroho kambini.”—Yak. 3:17.
“IMETOSHA!”
“Tulipata vichapo katika njia mbalimbali,” Zinaida anaendelea kusema. “Ilikuwa wazi kwamba Yehova mwenyewe alikuwa akisimamia utendaji huo kwa kuwa alikuwa ametuahidi: ‘Sitawaacha wala kuwatupa hata kidogo.’ (Ebr. 13:5) Wakati mwingine aliwapofusha walinzi. Pindi moja wakati wa majira ya baridi kali, kikundi chetu kilipokuwa kikiingia kambini baada ya kazi, walinzi walitupekua kama kawaida wakituamuru tutoe nguo zote. Niliingia mwisho nikiwa nimebeba vichapo vipya ndani ya suruali mbili nilizovaa.
“Kwa sababu kulikuwa na baridi, nilikuwa nimevaa nguo nyingi sana. Kwanza, mnyapara wa kike alipekua koti langu la baridi, kisha koti lisilo na mikono ambalo nilivaa ndani yake. Niliamua kuvua nguo hizo polepole nikitumaini kwamba atachoka. Taratibu nikatoa sweta moja, kisha nyingine. Alipokuwa akizipekua nguo hizo kwa uangalifu, nilitoa skafu kadhaa taratibu, kisha nikatoa vesti, kisha shati moja, halafu nyingine. Nilibaki na suruali mbili na viatu vya manyoya. Polepole nilivua kiatu kimoja kisha kingine, halafu nikaanza kutoa suruali ya nje. Kisha nikajiuliza: ‘Nitafanya nini sasa? Akiniambia nivue suruali hii iliyobaki, nitakimbia na kuwatupia akina dada vichapo.’ Nilipomaliza kutoa tu suruali ya nje, mwanamke huyo aliniambia hivi akiwa amekasirika: ‘Imetosha! Toka hapa!’ Mara moja nikavaa nguo zangu na kukimbilia kambini.
“Tulipata wapi vichapo hivyo? Akina ndugu waliviacha mahali fulani tulipokubaliana mapema, nasi tulivichukua kwa zamu na kuviingiza kambini. Vilipoingia kambini, tulivificha mahali salama, na mara kwa mara tulibadili mahali hapo. Pia tulikuwa tukinakili vichapo kwa mkono na kuficha nakala hizo. Tulinakili vichapo hivyo tukiwa tumejifunika blanketi tukitumia mwangaza kutoka kwenye taa ya barabarani ulioingia kupitia dirishani na kupenya kwenye matundu madogo ya blanketi. Sikuzote, tulikuwa na shughuli nyingi ili tusipoteze wakati. Kila tulipokuwa tukienda kwenye chumba cha kulia chakula, sote tulibeba karatasi zenye andiko fulani.”
“WAKATI WAKO UMEFIKA”
Mnamo 1965, bila kutarajia serikali ya Sovieti ilitoa amri ya kuwaachilia huru Mashahidi wote waliopelekwa uhamishoni Siberia kati ya mwaka wa 1949 hadi 1951. Hata hivyo, ndugu na dada wengi hawakuruhusiwa kurudi makwao. Wale ambao hawakutaka kubaki Siberia, waliamua kuhamia maeneo yaliyokuwa na uhitaji wa wahubiri.
Magdalina Beloshitskaya anasema hivi: “Tuliishi uhamishoni Siberia kwa karibu miaka 15. Katika majira ya baridi kali, kulikuwa na baridi kali sana kufikia nyuzi 60 Selsiasi chini ya sifuri, na wakati wa kiangazi kulikuwa na inzi na mbu wengi ambao walituuma hata kwenye mboni za macho. Yehova alitusaidia tuokoke mambo yote hayo. Lakini tulifurahi sana kupanda mbegu za kweli katika eneo hilo lenye baridi la Siberia! Kila mwezi kwa miaka 15, tulitia sahihi hati iliyokuwa katika ofisi ya msimamizi tukisema kwamba hatutajaribu kutoroka kutoka katika eneo tulilohamishiwa. Nyakati nyingine msimamizi alikuja na kulala nyumbani kwetu. Kwenye pindi kama hizo alikuwa mpole sana, na alituuliza maswali mengi kuhusu Biblia na kile ambacho mtu alihitaji kufanya ili kuishi kupatana na mafundisho yake. Alituuliza ni nini kilichotuchochea kufuata njia ya maisha ambayo tulijua ingetufanya tuteswe. Wakati fulani tulimuuliza ikiwa kulikuwa na tumaini la kuachiliwa huru. Alifungua kiganja cha mkono wake na kutuuliza, ‘Kuna tumaini lolote la nywele kuota hapa?’
“Nikamjibu, ‘Hapana.’
“‘Hivyo ndivyo tumaini lenu la kuwa huru lilivyo,’ akasema. Kisha baada ya kufikiria kidogo akaendelea kusema, ‘Ikiwa Mungu wenu hatafanya muujiza kwa njia fulani.’
“Siku moja, wakati wa kiangazi cha 1965, nilienda kwenye kituo cha gari-moshi kutuma barua. Msimamizi aliponiona kwa mbali alisema hivi kwa sauti: ‘Magdalina, unaenda wapi bila ruhusa?’
“‘Siendi popote,’ nikamjibu, ‘natuma tu barua.’ Kisha akanikaribia na kusema: ‘Utaachiliwa leo. Wakati wako umefika.’ Kisha akaniangalia kana kwamba anasema, ‘Mungu amekuweka huru!’ Sikuamini masikio yangu!
“Tuliruhusiwa kwenda mahali popote katika Muungano wa Sovieti isipokuwa kwenye makao yetu ya awali. Ni kana kwamba tulikuwa tunasikia sauti ya Yehova ikituambia: ‘Tawanyikeni, mkahubiri. Huu ndio wakati wa kuhubiri, msikawie, kwa hiyo tawanyikeni.’ Kama tungeruhusiwa kurudi nyumbani, wengi wetu tungerudi kwenye miji tuliyotoka. Lakini kwa kuwa hatukuruhusiwa kufanya hivyo, kila mtu alihamia mahali papya. Familia yetu iliamua kuhamia huko Caucasus.”
Maelfu ya Mashahidi walitawanyika kotekote katika Muungano wa Sovieti. Mwaka huohuo kwenye mkutano wa kiserikali, ofisa mmoja aliuliza hivi akiwa ametatanika: “Ni nani anayeweza kuniambia watu hawa wa madhehebu ya Yehova walifikaje kwenye jiji letu, ambalo limejengwa juzi na vijana waliojitolea? Jiji lenyewe bado jipya kabisa na ghafula watu wa madhehebu ya Yehova wamefika!” Wenye mamlaka hawakujua wafanye nini na Mashahidi. Hakuna mtu anayeweza kuzuia kutimia kwa ahadi ya Mungu ya dunia kujaa ‘ujuzi wa Yehova.’—Isa. 11:9.
“MNA ‘MAJI MATAKATIFU’”
Mashahidi wa Yehova walifungwa kwenye kambi kwa sababu ya kazi ya kuhubiri. Nikolai Kalibaba aliyefungwa miaka mingi kwenye kambi hizo anakumbuka: “Wanne kati yetu walifungwa kwenye kambi katika kijiji cha Vikhorevka kwenye Wilaya ya Irkutsk, ambako ndugu 70 hivi walikuwa wamefungwa. Hakukuwa na maji safi ya kunywa; bomba pekee la maji safi lilikuwa limeunganishwa na bomba la maji machafu, kwa hiyo maji hayo yalikuwa hatari kwa afya. Pia chakula hakikufaa kuliwa, lakini Yehova alitusaidia. Katika kambi hiyo, ni Mashahidi tu waliotaka kufanya kazi. Tulikuwa wafanyakazi wenye bidii. Baada ya muda mfupi wasimamizi wa kambi walitambua hilo, na wakatutuma tukafanye kazi katika kambi nyingine. Hivyo tungeweza kuleta maji safi ya kunywa katika ndoo. Wafungwa wengi walikuwa wakitujia na kusema: ‘Tumesikia kwamba mna “maji matakatifu.” Tupeni angalau nusu glasi.’ Bila shaka tuliwapa maji.
“Kati ya wafungwa hao, kulikuwa na watu wenye nia njema. Baadhi yao walifungwa kwa sababu ya wizi na makosa mengine. Walijifunza kweli na wakawa Mashahidi wa Yehova. Wengine hawakupenda kweli na walitupinga waziwazi. Lakini wakati mmoja, msemaji alipokuja kambini kutoa hotuba dhidi ya Mashahidi wa Yehova, watu hao walitutetea kwa kusema kwamba hotuba hiyo iliwaharibia Mashahidi sifa.”
“TUTAWAJIA TUKIWA VIKUNDI”
Mara nyingi akina ndugu walimwomba Yehova hekima ya kujua jinsi ambavyo wangeweza kutumia hali zao kuendeleza mambo ya Ufalme. Nikolai anaendelea kusema: “Tulipata fununu kwamba tutapelekwa kwenye kambi nyingine huko Mordvinia karibu na Moscow. Kabla ya kuondoka jambo la kupendeza lilitukia. Tulishangaa wakati maofisa na wanyapara fulani ambao walikuwa wamewalinda Mashahidi wa Yehova kwa miaka kadhaa walipotujia na kusema: ‘Tungependa mtuimbie nyimbo zenu na mtueleze zaidi kuhusu mafundisho yenu. Tutawajia tukiwa vikundi vya watu 10 hadi 20, au hata zaidi.’
“Wakiogopa kile ambacho kingetokea iwapo tungegunduliwa, maofisa hao walisema kwamba wangeweka walinzi mahali ambapo tungekutania. Tuliwaambia kwamba kwa kuwa tuna uzoefu mwingi zaidi katika mambo hayo, tutaweka walinzi wetu pia. Walinzi wao walifanya kazi bega kwa bega na walinzi wetu: Kila baada ya hatua chache, kulikuwa na askari kati ya nyumba ya mlinzi na mahali tulipokutania. Unaweza kuwazia mandhari hiyo? Kikundi cha Mashahidi kiliwaimbia nyimbo maofisa na wanyapara, baada ya hapo ndugu alitoa hotuba fupi iliyotegemea kichwa fulani cha Biblia. Ilikuwa ni kana kwamba tuko kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova! Hivyo ndivyo tulivyoongoza mikutano kadhaa na vikundi vya wanyapara na maofisa waliopendezwa. Tuliona jinsi Yehova alivyotutunza sisi na watu hao wenye mioyo minyoofu.
“Tulibeba magazeti mengi kutoka katika kambi hiyo hadi kambi ya Mordvinia,” anasema Nikolai. “Kulikuwa na Mashahidi wengi katika kambi hiyo. Akina ndugu walinipa sanduku ambalo lilikuwa na mifuko ya ziada ndani ambamo vichapo vingeweza kuwekwa. Tulikuwa waangalifu ili wakati wa upekuzi, sanduku hilo lisivute uangalifu wa wanyapara hao. Katika kambi ya Mordvinia, tulipekuliwa kwa uangalifu sana. Mnyapara mmoja alichukua sanduku langu na kusema: ‘Sanduku hili ni zito sana! Lazima kuna hazina ndani!’ Bila kutarajia, aliweka sanduku langu pamoja na vitu vingine upande mmoja na akaanza kupekua mizigo ya watu wengine. Baada ya upekuzi, mnyapara mwingine aliniambia, ‘Chukua virago vyako na uende!’ Sanduku langu halikupekuliwa, kwa hiyo niliingiza kambini chakula kingi cha kiroho ambacho kilihitajika sana.
“Isitoshe, mara nyingi niliweka trakti zilizonakiliwa kwa mkono katika mabuti yangu. Kwa kuwa nilikuwa na miguu mikubwa, kila mara kulikuwa na nafasi ya kuhifadhi karatasi nyingi ndani ya viatu vyangu. Niliweka karatasi hizo chini ya soli ya ndani ya viatu, kisha nikapaka grisi nyingi. Grisi hiyo iliteleza na ilinuka vibaya sana, kwa hiyo wanyapara hawakupekua mabuti yangu.”
“WANYAPARA WALITUCHUNGUZA, NAMI NILIWACHUNGUZA PIA”
Nikolai anaendelea kusema: “Katika kambi ya Mordvinia, akina ndugu waliniweka nisimamie kazi ya kunakili vichapo. Jukumu langu moja lilikuwa kuwachunguza wanyapara ili wale walionakili vichapo kwa mkono wawe na muda wa kuficha kila kitu. Wanyapara walituchunguza, nami niliwachunguza pia. Baadhi ya wanyapara waliazimia kutukamata, na mara kwa mara wangeingia ghafula kwenye kambi. Ilikuwa vigumu sana kuwachunga. Wengine wangekuja kambini mara moja kwa siku. Hawakutuhangaisha.
“Katika nyakati hizo, tulinakili kutoka kwenye nakala halisi, ambazo tulizificha mahali salama. Nakala kadhaa halisi zilifichwa ndani ya jiko, hata kwenye jiko lililokuwa katika ofisi ya msimamizi wa kambi. Ndugu ambao walisafisha ofisi hiyo, walijenga sehemu maalumu katika jiko hilo ambako tuliweka nakala nyingi halisi za Mnara wa Mlinzi. Ingawa wanyapara walitupekua kwa uangalifu sana, sikuzote nakala halisi zilikuwa mahali salama, yaani, katika ofisi ya msimamizi.”
Akina ndugu walikuja kuwa na ustadi wa kuficha vichapo. Walipenda sana kuficha vichapo kwenye vizingiti vya madirisha. Ndugu hata walificha vichapo kwenye tyubu za dawa ya meno. Ni ndugu wawili au watatu tu waliojua mahali nakala halisi zilipowekwa. Kulipokuwa na uhitaji, mmoja wao alichukua nakala halisi na baada ya kuinakili kwa mkono aliirudisha mahali pake salama. Kwa njia hiyo, sikuzote nakala halisi zilibaki mahali salama. Ndugu wengi waliliona kuwa pendeleo kufanya kazi ya kunakili hata ingawa hilo lingemaanisha kuadhibiwa kwa kifungo cha upweke kwa siku 15. Viktor Gutshmidt anakumbuka hivi: “Kati ya miaka kumi niliyofungwa kambini, miaka mitatu hivi nilikuwa katika kifungo cha upweke.”
MNARA WA MLINZI WENYE MAANDISHI MADOGO SANA
Akina ndugu waliona kwamba wasimamizi wa kambi walikuwa wamebuni njia ya pekee ya kusaka vichapo vya Biblia kutoka kwa Mashahidi. Baadhi ya maofisa walifanya hivyo kwa makini sana. Ivan Klimko anasema hivi: “Wakati mmoja katika Kambi Na. 19 ya Mordvinia, askari wenye mbwa waliwaamuru akina ndugu watoke kambini na wakafanya msako mkali. Kila Shahidi alivuliwa nguo zote, kutia ndani matambara aliyokuwa amevaa miguuni. Lakini akina ndugu walibandika kwa gundi karatasi zilizonakiliwa kwa mkono chini ya nyayo za miguu, na hivyo karatasi hizo hazikugunduliwa. Pia walitengeneza vijitabu vidogo ambavyo vingeweza kutoshea katikati ya vidole. Walinzi walipowaamuru watu wote wainue mikono yao, vijitabu hivyo havikuanguka, na hivyo baadhi ya vichapo hivyo havikupatikana.”
Kulikuwa na njia nyingine za kulinda chakula cha kiroho. Aleksey Nepochatov anasema hivi: “Ndugu fulani waliweza kuandika kwa mwandiko mdogo kama utando wa buibui. Ncha ya kalamu ilichongwa na kuwa nyembamba sana hivi kwamba kwenye mstari mmoja wa karatasi mtu angeweza kuandika mistari mitatu au minne ya maandishi. Kasha dogo la kiberiti lingeweza kuwekwa nakala tano au sita za Mnara wa Mlinzi zilizoandikwa kwa mwandiko huo mdogo. Ili kuweza kuandika kwa mwandiko huo, mtu alihitaji kuwa na macho mazuri sana na alipaswa kuwa mvumilivu. Baada ya taa zote kuzimwa na watu wote kulala, ndugu hao waliandika wakiwa wamejifunika blanketi. Walitumia mwangaza wa taa iliyokuwa kwenye lango la kambi ambayo haikuwa inafanya kazi vizuri. Mtu alipofanya kazi hiyo kwa miezi kadhaa macho yake yaliharibika. Mara nyingine mlinzi angegundua, na ikiwa alitupenda angesema, ‘Bado mnaandika-andika tu, mtalala saa ngapi?’”
Ndugu Klimko anakumbuka hivi: “Pindi moja, tulipoteza vichapo vingi na hata Biblia. Vichapo hivyo vilikuwa vimefichwa katika mguu wa bandia wa ndugu mmoja. Baada ya kumlazimisha ndugu huyo atoe mguu wake, walinzi waliuvunja. Kisha walipiga picha kurasa zilizotawanyika na kuzichapisha kwenye gazeti la gereza hilo. Hata hivyo, hilo lilikuwa jambo zuri kwani lilionyesha kwamba Mashahidi wa Yehova walijihusisha katika utendaji wa kidini tu. Baada ya ugunduzi huo, msimamizi wa kambi aliwaambia akina ndugu hivi kwa kejeli, ‘Hii ndiyo Har–Magedoni yenu!’ Hata hivyo, siku iliyofuata, mtu fulani alimwambia kwamba Mashahidi wa Yehova wamekutana, wakaimba nyimbo, na kusoma kama ilivyo kawaida yao.”
KUZUNGUMZA NA MWENDESHA-MASHTAKA MKUU
Mwishoni mwa mwaka wa 1961, mwendesha-mashtaka mkuu wa Shirikisho la Muungano wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Sovieti ya Urusi, alikuja kukagua kambi ya Mordvinia. Alipokuwa akitembea katika kambi hiyo, aliingia mahali ambapo Mashahidi waliishi. Mwendesha-mashtaka mkuu aliwaruhusu ndugu wamuulize maswali machache. Viktor Gutshmidt anakumbuka hivi, “Niliuliza, ‘Je, unadhani dini ya Mashahidi wa Yehova ni hatari kwa watu wa Sovieti?’
“‘Sidhani,’ alisema mwendesha-mashtaka mkuu. Lakini baadaye alisema hivi bila kukusudia, ‘Katika mwaka wa 1959 pekee, rubo milioni tano zilitengwa kwa ajili ya Wilaya ya Irkutsk ili kuwachunguza Mashahidi.’
“Kwa kusema hivyo, alimaanisha kwamba serikali ilijua sisi ni nani, kwa kuwa Serikali ilikuwa imetenga rubo milioni tano zitumiwe katika magereza ili kuwachunguza Mashahidi wa Yehova. Hicho kilikuwa kiasi kikubwa sana cha pesa. Wakati huo, rubo elfu tano zingemwezesha mtu kununua gari au nyumba nzuri. Wenye mamlaka huko Moscow lazima walijua kwamba Mashahidi wa Yehova si watu hatari.
“Mwendesha-mashtaka mkuu aliendelea kusema, ‘Tukiwaambia watu wa Sovieti wawatendee vile wanavyotaka, watawafagilia mbali ninyi nyote.’ Alimaanisha kwamba watu wa Sovieti hawakuwapenda Mashahidi. Maneno yake yalionyesha kwamba mamilioni ya watu walikuwa wameathiriwa na propaganda ya kwamba hakuna Mungu.
“Tulimjibu hivi, ‘Mtaona uhalisi wa mambo wakati Mashahidi watakapofanya makusanyiko kutoka Moscow hadi Vladivostok.’
“Akasema: ‘Huenda watu nusu milioni ndio watakaokuwa upande wenu, wengine wote bado watakuwa upande wetu.’
“Mazungumzo yetu na mwendesha-mashtaka mkuu yaliishia hapo. Hakuwa amekosea. Leo, zaidi ya watu 700,000 wanahudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kotekote katika nchi zilizokuwa chini ya Muungano wa Sovieti. Huko watu wanasikiliza kweli safi za Biblia, badala ya propaganda.”
“UMEWATENGENEZEA MASHAHIDI MAHALI PA KUSTAREHE”
Viktor anaendelea kusema: “Msimamizi wa kambi alimwonyesha mwendesha-mashtaka mkuu maua na miti ambayo Mashahidi walipanda na pia vifurushi ambavyo walipokea na kuviweka katika kambi hiyo bila yeyote kuviiba. Alitazama kila kitu kwa mshangao. Hata hivyo, baadaye tuligundua kwamba mtu huyo aliamuru msimamizi wa kambi aharibu maua na miti yote. Alimwambia hivi msimamizi wa kambi, ‘Umewatengenezea Mashahidi mahali pa kustarehe badala ya kambi ya kazi ngumu.’ Pia aliamuru kwamba Mashahidi wasipokee vifurushi vyovyote na akafunga duka ambalo Mashahidi waliruhusiwa kwenda kununua chakula cha ziada.
“Hata hivyo, akina ndugu walifurahi wakati msimamizi hakufuata maagizo hayo yote. Kwa mfano, akina dada waliruhusiwa kuendelea kupanda maua kama zamani. Katika majira ya kuchipua, walikata maua hayo na kutengeneza mashada makubwa na kuwapa wafanyakazi wa kambi na watoto wao. Ilifurahisha hasa kuwaona watoto walipokutana na wazazi kwenye lango, wakichukua maua yao na kukimbia shuleni wakiwa na furaha. Waliwapenda Mashahidi.”
Viktor anakumbuka hivi: “Siku moja mwanzoni mwa 1964, mnyapara mmoja ambaye ndugu yake alifanya kazi kwenye shirika la KGB, alituambia kwamba Serikali ilikuwa ikipanga kampeni kubwa dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Lakini mwishoni mwa mwaka huo, Nikita Khrushchev aliyekuwa kiongozi wa Serikali, aliondolewa mamlakani kwa ghafula na mateso yakapungua.”
NYIMBO ZA UFALME KWENYE KAMBI YENYE ULINZI MKALI
Katika miaka ya 1960, wasimamizi wa kambi yenye ulinzi mkali huko Mordvinia waliruhusu wafungwa wapokee vifurushi mara moja kwa mwaka na hilo lilikuwa ni kama ‘tuzo la pekee.’ Msako ulifanywa kila mara. Ikiwa yeyote angeshikwa akiwa na karatasi yenye andiko, alifungwa kifungo cha upweke kwa siku kumi. Isitoshe, katika kambi hiyo wafungwa walipewa chakula kidogo kuliko katika kambi nyingine. Kazi ilikuwa ngumu zaidi katika kambi zenye ulinzi mkali; Mashahidi walihitaji kung’oa visiki vya miti mikubwa. Aleksey Nepochatov anasema hivi: “Mara nyingi, tulikuwa tumechoka kabisa. Lakini tulijaribu kuwa makini na hatukuvunjika moyo. Njia moja ambayo akina ndugu walijitia moyo ilikuwa ni kuimba nyimbo za Ufalme. Tuliunda kwaya yenye mpangilio mzuri wa sauti, hivi kwamba hata ingawa hakukuwa na sauti za akina dada, nyimbo hizo zilipendeza sana. Nyimbo hizo ziliwachangamsha Mashahidi na pia maofisa, nao waliwaomba akina ndugu waimbe walipokuwa wakifanya kazi. Pindi moja tulipokuwa tunakata miti, msimamizi alikuja na kutuambia: ‘Imbeni nyimbo chache. Ombi hili limetoka kwa ofisa mkuu mwenyewe!’
“Ofisa huyo alikuwa amewasikia akina ndugu wakiimba nyimbo za Ufalme mara nyingi. Ombi hilo lilikuja kwa wakati uliofaa kwani tulikuwa tumechoka sana. Kwa shangwe tulianza kumsifu Yehova kwa sauti zetu. Kwa kawaida tulipoimba katika kambi, wake za maofisa walitoka nyumbani mwao na kusimama kwenye varanda na kutusikiliza kwa muda mrefu. Walipenda sana wimbo namba 6, ‘Dunia na Itoe Utukufu,’ uliokuwa katika kitabu cha nyimbo cha zamani. Wimbo huo ulikuwa na maneno mazuri na sauti nzuri sana.”
ALIFIKA “NCHI NYINGINE”
Hata katika hali zisizotarajiwa, ilionekana Mashahidi wa Yehova ni watu wa aina gani. Viktor Gutshmidt anakumbuka: “Tulikuwa tumeketi bustanini wakati vifaa fulani vya bei ghali vya umeme vililetwa kambini. Dereva aliyevileta hakuwa ndugu yetu wa kiroho. Alikuwa mfungwa katika kambi yetu, na meneja wa ununuzi aliyemsindikiza alikuwa wa kambi nyingine. Kwa kuwa chumba cha kuhifadhia kilikuwa kimefungwa na msimamizi alikuwa likizoni, Mashahidi waliombwa wavikubali na kuvipakua.
“Tulipakua vifaa hivyo na kuvipanga nje ya chumba hicho kilichokuwa karibu na jengo ambalo akina ndugu walifungwa. Meneja wa ununuzi alikuwa na wasiwasi sana kuhusu kuacha vifaa hivyo bila sahihi ya kuvipokea ya meneja wa chumba cha kuhifadhia. Lakini dereva alimhakikishia: ‘Usiogope. Hakuna atakayevigusa. Umefika “nchi nyingine.” Sahau yanayofanyika nje ya kambi. Ukivua saa ya mkononi na kuiacha mahali popote, kesho utaipata hapohapo.’ Meneja wa ununuzi alisisitiza kuwa bidhaa hizo zina thamani ya rubo nusu milioni, hivyo hangeziacha bila sahihi ya mtu fulani.
“Wasimamizi wa kambi waliwasili na kuamuru gari hilo liondolewe kambini. Mmoja wao alimwambia aache hati ya kuwasilisha bidhaa na kuichukua siku inayofuata. Aliondoka shingo upande. Asubuhi iliyofuata alirudi na kuomba aruhusiwe kuingia kambini ili hati hiyo itiwe sahihi, lakini mlinzi alimpa hati hiyo ikiwa tayari imetiwa sahihi.
“Mlinzi alituambia kwamba meneja huyo alishindwa kuondoka. Kwa nusu saa, alisimama, akakodolea macho lango hilo, kisha akatazama hati zile, akageuka ili aondoke, kisha akageuka tena na kukodolea macho lango kwa mara nyingine. Huenda ilikuwa mara yake ya kwanza kuona jambo kama hilo. Vifaa vya bei ghali vilipokewa na hati ikatiwa sahihi bila yeye kuwapo, na kila kitu kilikuwa kimefanywa kwa unyoofu. Lakini jambo la kushangaza hata zaidi ni kwamba hilo lilitokea kwenye kambi yenye ulinzi mkali ambapo wafungwa wanatambulishwa kuwa ‘wahalifu hatari zaidi.’ Ndiyo, licha ya propaganda dhidi ya Mashahidi, matukio kama hayo yaliwafanya watu wajue Mashahidi wa Yehova ni watu wa aina gani.”
“WAMEANZA KUHUBIRI TENA”
Mnamo 1960, siku chache baada ya akina ndugu kujikuta pamoja katika kambi ya Mordvinia, zaidi ya Mashahidi 100 walichaguliwa ili wahamishwe kwenye Kambi Na. 10, gereza maalumu katika kijiji cha karibu cha Udarnyy. Lilikuwa gereza la kujaribu kuwafundisha upya Mashahidi. Wafungwa walivalia sare zenye mistari kama zilizovaliwa na wafungwa wa kambi za mateso za Wanazi. Mbali na kazi nyingine, Mashahidi walihitaji kuchimbua visiki vikubwa msituni. Kila mmoja alitazamiwa kuchimbua visiki 11 hadi 12 kwa siku. Lakini nyakati nyingine, hata kikundi kizima cha akina ndugu kikifanya kazi kwa siku nzima hawangeweza kuchimbua kisiki kimoja cha mwaloni mkubwa. Mara nyingi waliimba nyimbo za Ufalme ili kutiana moyo. Msimamizi wa kambi alipowasikia wakiimba, mara nyingine angewafokea hivi: “Ninyi Mashahidi mtalala njaa ili mwache kuimba. Nitawafundisha kufanya kazi!” Ndugu mmoja aliyekuwa katika kambi hiyo anakumbuka: “Lakini Yehova alitutegemeza. Licha ya hali ngumu tulikuwa macho kiroho. Sikuzote tulijitia moyo kwa kujikumbusha kuwa tumesimama upande wa Yehova katika suala la enzi kuu ya ulimwenguni pote.”—Met. 27:11.
Kulikuwa na walioitwa eti “walimu” wa gereza na kila seli ilikuwa na mmoja, na hakuna yeyote kati yao aliyekuwa na cheo cha chini kuliko kile cha kapteni. Kusudi lao lilikuwa kuwafanya Mashahidi wakane imani. Walisema yeyote anayekana imani angeachiliwa. Kila mwezi, walimu hao waliandika ripoti kuhusu tabia ya kila Shahidi, nayo ingetiwa sahihi na mfanyakazi wa gereza. Kwa kawaida ripoti ya kila Shahidi ilisema, “Hatendi kupatana na majaribio ya kumwelimisha upya, yuko imara katika imani yake.” Ivan Klimko anasema: “Kati ya miaka kumi niliyohukumiwa, nilitumia miaka sita katika gereza hilo na niliitwa ‘mfungwa hatari anayefanya makosa kwa kurudia’ sawa na ndugu wengine. Maofisa walituambia wenye mamlaka walifanya hali ziwe ngumu sana hasa kwa ajili ya Mashahidi ili watuchunguze.”
Wakati mmoja Iov Andronic aliyefungwa humo kwa miaka mitano alimuuliza kamanda wa kambi hivi, “Tutafungwa hapa mpaka lini?” Akielekeza msituni, kamanda huyo alimjibu, “Hadi nyote mtakapozikwa kule.” Iov anasema: “Tulitenganishwa na wengine ili tusiwahubirie. Tulichungwa sana. Ikiwa mmoja wetu alihitaji kwenda sehemu nyingine ya kambi, alisindikizwa na mnyapara. Miaka kadhaa baadaye tulipohamishwa kwenye kambi yenye ulinzi wa kadiri, wafungwa fulani ambao si Mashahidi walimwambia msimamizi wa kambi: ‘Mashahidi wa Yehova walishinda. Mliwatenga, lakini sasa wameanza kuhubiri tena.’”
OFISA ANAITAMBUA BIBLIA YAKE
Kuingiza kichapo chochote katika Kambi Na. 10 haukuwa mchezo wa watoto, sembuse Biblia. Akina ndugu waliona haiwezekani kuingiza Neno la Mungu humo. Ndugu mmoja aliyefungwa humo kwa miaka michache anasema: “Kwa Yehova hakuna jambo lisilowezekana. Mungu alisikiliza sala zetu. Tuliomba tupate angalau Biblia moja kwa ajili ya Mashahidi 100 waliofungwa humo na kwa kushangaza tukapata Biblia mbili!” (Mt. 19:26) Hilo liliwezekanaje?
Kanali fulani aliajiriwa kuwa mwalimu wa gereza. Lakini ingewezekanaje kwa mtu asiye na ujuzi wowote wa Biblia “kuwaelimisha” Mashahidi? Kwa njia fulani alipata Biblia iliyochakaa. Kabla ya kwenda likizo alimwomba mfungwa fulani mzee aliyekuwa Mbaptisti aijalidi. Aliwaambia wanyapara wasimnyang’anye Biblia hiyo. Mbaptisti huyo aliwaringia Mashahidi kuwa amepata Biblia, naye akakubali kuwapa waisome. Akina ndugu walipopata hazina hiyo yenye thamani, walifumua nyuzi za Biblia hiyo na kuwagawia wafungwa wote Mashahidi kurasa zake ili wazinakili. Siku chache zilizofuata, Mashahidi walitumia seli zao kunakili kurasa hizo. Walitoa nakala mbili za kila kurasa. Ndugu mmoja anakumbuka: “Kurasa zote zilipokusanywa, kulikuwa na Biblia tatu! Kanali alipewa nakala yake iliyojalidiwa upya, nasi tukabaki na zetu mbili. Tulisoma nakala moja na ile nyingine tuliificha kwenye transfoma yenye umeme mwingi. Tulikuwa tumetengeneza sehemu za pekee katika transfoma hizo. Wanyapara waliogopa kuzikaribia, hivyo hakuna aliyezichunguza. Umeme huo ulikuwa mlinzi wetu mwenye kutegemeka.”
Hata hivyo, wakati wa upekuzi mmoja, kanali aliona ukurasa wa Biblia iliyonakiliwa kwa mkono. Alipogundua kilichotokea, alifadhaika sana na akasema kwa mshangao, “Hii ni sehemu ya Biblia ambayo mimi mwenyewe niliingiza kambini!”
KUADHIMISHA UKUMBUSHO
Kila mwaka, akina ndugu walijaribu kuadhimisha Ukumbusho kambini. Miaka yote waliyokuwa katika kambi moja huko Mordvinia, hakuna ndugu aliyekosa tukio hilo. Bila shaka, wasimamizi wa kambi walijaribu kulizuia. Walijua tarehe ya Ukumbusho, na kwa kawaida waliwaambia walinzi wote wawe macho. Hata hivyo, walinzi wengi walichoka kuwachunguza akina ndugu ilipofika jioni kwa sababu hakuna aliyejua wakati na mahali ambapo Ukumbusho ungefanywa.
Akina ndugu walijitahidi kupata divai na mkate usiotiwa chachu. Wakati mmoja walinzi waligundua mifano hiyo kwenye droo siku ya Ukumbusho na wakaichukua. Baadaye, kikundi hicho kilibadilishwa, na ndugu aliyekuwa akisafisha ofisi ya kamanda alichukua mifano hiyo na kuwapa akina ndugu bila kuonekana. Jioni hiyo ndugu waliadhimisha Ukumbusho wakiwa na mifano wakati wa zamu ya kikundi cha tatu. Mifano hiyo ilihitajika sana kwani ndugu mmoja alikuwa mtiwa mafuta.
KUADHIMISHA UKUMBUSHO KATIKA KAMBI YA WANAWAKE
Kambi nyingine zilikuwa na tatizo hilohilo. Valentina Garnovskaya anakumbuka ilivyokuwa vigumu kuadhimisha Ukumbusho katika kambi ya wanawake huko Kemerovo. Anasema: “Kambi hiyo ilikuwa na dada 180. Tulikatazwa kukutana. Kwa miaka kumi tulifaulu kuadhimisha Ukumbusho mara mbili tu. Wakati mmoja tuliamua kuadhimisha Ukumbusho katika ofisi niliyopaswa kusafisha. Akina dada walianza kuingia ofisini bila kuonekana kwa muda wa saa kadhaa kabla ya Ukumbusho. Dada 80 hivi walifika. Tuliweka mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu mezani.
“Tuliamua kuanza bila kuimba, hivyo dada mmoja akatoa sala ya kufungua, na tukaanza kwa shangwe na kwa njia inayofaa. Lakini ghafula tulisikia kelele na tukagundua kuwa wanyapara walikuwa wakitutafuta. Kisha tukaona msimamizi wao akichungulia dirishani, ingawa dirisha hilo lilikuwa juu sana. Mlango ulibishwa kwa nguvu na wakatuamuru tuufungue. Wanyapara waliingia kwa kishindo na kumkamata dada aliyekuwa akitoa hotuba na kumpeleka katika kifungo cha upweke. Kwa ujasiri dada mwingine alisimama atoe hotuba hiyo, lakini wakamkamata pia. Alipochukuliwa, dada mwingine akajaribu kuendelea na hotuba hiyo, kwa hiyo wakatukusanya katika chumba kingine, wakitisha kutuadhibu kwa kifungo cha upweke. Hapo ndipo tulipomaliza mwadhimisho wa Ukumbusho kwa wimbo na kufunga kwa sala.
“Tuliporudi mahali pa kulala, wafungwa wengine walituambia, ‘Mlipotoweka ghafula, tulisema Har–Magedoni imekuja na Mungu amewachukua na kuwapeleka mbinguni akituacha hapa tuangamie!’ Tulikuwa na wafungwa hao kwa miaka kadhaa na hawakuwa wamekubali kweli. Lakini baada ya hapo, baadhi yao walianza kutusikiliza.”
“TULIJIKUSANYA PAMOJA”
Kambi moja huko Vorkuta ilikuwa na Mashahidi wengi kutoka Ukrainia, Moldova, maeneo ya Baltiki, na jamhuri nyingine za Muungano wa Sovieti. Ivan Klimko anakumbuka: “Yalikuwa majira ya baridi kali mwaka wa 1948. Ingawa hatukuwa na vichapo vya Biblia, tuliandika katika karatasi ndogo tulichokumbuka kutoka kwenye magazeti ya zamani na kuzificha ili wanyapara wasizipate. Lakini walijua tulikuwa nazo. Tungepekuliwa kwa muda mrefu na kwa uangalifu sana. Siku zenye baridi kali sana, tulipelekwa nje na kusimamishwa katika mistari ya watu watano. Mara nyingi tulihesabiwa tena na tena. Ilionekana walitazamia tuwape karatasi hizo badala ya kusimama katika baridi hiyo kali. Tulipokuwa tukihesabiwa tena na tena, tulijikusanya pamoja na kuzungumzia jambo fulani la Biblia. Sikuzote tulifikiria mambo ya kiroho. Yehova alitusaidia kuwa watimilifu. Baadaye, hata tuliingiza Biblia kambini. Tuliigawanya sehemu mbalimbali ili Biblia nzima isichukuliwe wakati wa upekuzi.
“Walinzi walielewa Mashahidi wa Yehova hawakustahili kuwa gerezani. Walitusaidia kwa njia yoyote waliyoweza. Baadhi yao ‘walifunga macho’ kila mara tulipoletewa barua. Kwa kawaida, barua hizo zilikuwa na ukurasa mmoja au mbili za Mnara wa Mlinzi. Kurasa hizo, hazikuwa na gramu nyingi, lakini zilikuwa na thamani kuliko kilo kadhaa za chakula. Ingawa Mashahidi walinyimwa chakula na vitu vingine katika kila kambi, walikuwa matajiri kiroho.”—Isa. 65:13, 14.
“ATAKIGAWANYA MARA 50!”
Akina ndugu waliongoza mafunzo ya Biblia kila juma na wale waliopendezwa na kweli. Wafungwa kadhaa—hata wale ambao hawakupendezwa na Biblia—walijua kwamba baada ya saa moja jioni, kulikuwa na mafunzo ya Biblia kambini nao walijaribu kunyamaza. Iov Andronic anakumbuka: “Ilikuwa wazi Yehova anatutunza na kuendeleza kazi yake. Isitoshe, tulijaribu kuonyeshana upendo wa Kikristo kwa kutumia kanuni za Biblia. Kwa mfano, tuligawana chakula tulichopokea, jambo ambalo halikuwa la kawaida kambini.
“Katika kambi moja, Mykola Pyatokha alikuwa na jukumu la kugawia akina ndugu chakula. Ofisa wa KGB alisema hivi wakati mmoja, ‘Mpe Mykola kipande cha peremende, naye atakigawanya mara 50!’ Hivyo ndivyo akina ndugu walivyofanya. Tuligawana kila kitu kilicholetwa kambini, chakula cha kimwili na cha kiroho. Hilo lilitusaidia na likawavutia watu wenye mioyo minyoofu waliopendezwa.”—Mt. 28:19, 20; Yoh. 13:34, 35.
WAONGEZEWA MISHAHARA KWA SABABU YA MWENENDO MZURI
Katika kambi moja wafanyakazi waliowashughulikia Mashahidi wa Yehova walipata nyongeza ya asilimia 30 ya mishahara. Kwa nini? Viktor Gutshmidt anaeleza: “Mweka-hazina wa zamani kambini alinieleza jambo hilo. Aliniambia kwamba katika kambi ambako ndugu wengi walifungwa, wafanyakazi waliambiwa wasikasirike au wasimtukane mtu na walipaswa kuwa wenye busara na watulivu nyakati zote. Wangepata nyongeza kwa mwenendo huo mzuri. Hilo lilifanywa kuonyesha kuwa si Mashahidi wa Yehova tu wanaoishi maisha mazuri na kwamba hakuna tofauti kati yao na watu wengine. Kwa hiyo, wafanyakazi walilipwa kwa mwenendo wao. Kulikuwa na wafanyakazi wengi kambini; wahudumu wa afya, vibarua, wahasibu, na wanyapara, watu 100 hivi. Hakuna aliyetaka kukosa nafasi ya kupata pesa zaidi.
“Siku moja ndugu aliyefanya kazi nje ya kambi alimsikia msimamizi wa kikundi akitoa matusi kwa sauti. Siku iliyofuata ndugu huyo alikutana na msimamizi huyo kambini na kusema: ‘Inaonekana mtu fulani katika nyumba ya walinzi alikukasirisha sana. Ulikuwa ukitoa matusi kwa sauti kubwa sana!’ Mtu huyo akasema: ‘Hapana, nilifadhaika tu siku hiyo. Kwa hiyo nilitoka nje ya kambi ili nijitulize.’ Kwa kweli, haikuwa rahisi kujiendesha kama Mashahidi wa Yehova.”
TULIHUBIRI TULIPOKUWA TUKIWEKA DIRISHA
Akina ndugu walitumia nafasi walizopata kuhubiri na mara nyingine walifanikiwa sana. Nikolai Gutsulyak anakumbuka: “Mara nyingi tulinunua chakula katika kioski cha kambini. Kila nilipochukua chakula, nilisema maneno machache kuhusu Biblia. Mwanamke aliyeuza chakula alisikiliza kwa makini na wakati mmoja aliniomba nimsomee kitu fulani. Siku tatu baadaye, ofisa mmoja aliniita langoni. Aliniambia mimi na Shahidi mwingine tukaweke dirisha kwenye nyumba ya kamanda wa kambi.
“Tuliandamana na askari kwenda jijini. Tulipofika katika nyumba hiyo, tulifunguliwa mlango na mwanamke yuleyule aliyefanya kazi katika kioski cha kambini. Kumbe alikuwa mke wa kamanda! Askari mmoja alisimama ndani, na wawili nje kwenye barabara iliyokuwa kando ya dirisha. Mwanamke huyo alitupa chai na kuomba tumweleze mengi kuhusu Biblia. Tulimwekea kioo dirishani na kumhubiria sana. Mazungumzo yetu yalipoisha, alisema: ‘Msiniogope. Wazazi wangu walimwogopa Mungu kama ninyi.’ Alisoma vichapo kwa siri, bila mume wake kujua kwani aliwachukia Mashahidi.”
“RUDINI KAZINI”
Kulikuwa na watu fulani wenye mamlaka waliopenda Mashahidi na kuwatetea. Katika miaka ya 1970 huko Bratsk, katika Wilaya ya Irkutsk, ofisi ya chama cha Wakomunisti katika kiwanda cha mbao iliamua kuwaachisha kazi Mashahidi wa Yehova. Akina ndugu waliambiwa: “Kwa kuwa hamwipendi serikali ya Sovieti, basi haitawatunza, mwacheni Yehova mnayempenda awatunze.” Ndugu walioachishwa kazi waliamua jambo bora wanaloweza kufanya ni kuhubiri waziwazi, hivyo wakaanza kwenda nyumba kwa nyumba. Katika mlango mmoja uliofunguliwa na mwanamke, ndugu walijitambulisha na kueleza kusudi lao. Kutoka jikoni sauti ya mwanamume iliuliza: “Unaongea na nani? Waruhusu waingie.” Walipoingia ndani ya nyumba, mtu huyo aliuliza: “Kwa nini hamko kazini? Leo ni siku ya kazi.” Akina ndugu walimweleza jinsi walivyopoteza kazi.
Kumbe huyo alikuwa mwendesha-mashtaka aliyekuwa amekuja nyumbani kula chakula cha mchana. Akiwa na hasira, alipiga simu na kuuliza ikiwa ni kweli ofisi hiyo iliwafukuza kazi Mashahidi wote wa Yehova. Baada ya ofisi hiyo kuthibitisha jambo hilo, mwendesha-mashtaka aliuliza: “Kwa msingi gani? Mnajua kwamba mmevunja sheria? Hamna haki ya kufanya hivyo! Ninawaamuru mwarudishe Mashahidi kazini na mwalipe kwa ajili ya miezi mitatu ambayo hawakufanya kazi kwa sababu ya uamuzi wenu.” Mwendesha-mashtaka aliweka simu chini na kuwageukia akina ndugu na kuwaambia, “Kesho, rudini kazini, na mwendelee kufanya kazi hapo.”
“NIMEKUWA NIKIFICHA VICHAPO TANGU 1947”
Kufikia miaka ya 1970, akina ndugu walikuwa stadi kutengeneza, kusambaza, na kuficha vichapo. Hata hivyo, hali zilitokea zilizomtaka mtu afikiri haraka. Grigory Sivulsky anakumbuka: “Mnamo 1976, nyumba yetu ilipekuliwa. Jioni iliyotangulia, niliweka ripoti na anwani za akina ndugu chini ya meza fulani. Wakati wa upekuzi, wapelelezi wa KGB walionekana wakiwa na uhakika kuwa wanajua wanachotafuta na mahali pa kukipata. Mpelelezi mmoja wa KGB aliniambia hivi: ‘Leta koleo na bisibisi, tufungue hiki kiti.’ Nilisali na kujibu kwa uhakika:
“‘Ikiwa mngetupekua ghafula kama mlivyofanya kwa Mashahidi wengine, mngepata kitu fulani. Lakini mmechelewa sana. Hamtapata chochote.’
“‘Kwani tungepata nini?’ akauliza mpelelezi mmoja.
“‘Magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Lakini hamtapata chochote leo.’
“Nilipowapa vifaa walivyoomba, niliwaambia, ‘Baada ya upekuzi mrudishe kiti hicho jinsi kilivyokuwa.’
“Kwa dakika moja, walisimama wasijue cha kufanya. Nilitambua hawana uhakika, nikamgeukia mmoja aliyekuwa kijana na kumwambia: ‘Ninafikiri hujatafuta vichapo vya Mashahidi wa Yehova kwa zaidi ya miaka mitatu. Lakini nimekuwa nikificha vichapo tangu 1947. Msipoteze muda wenu hapa, vichapo vimefichwa mahali salama.’
“Kwa kushangaza, waliondoka. Ripoti na anwani za akina ndugu zilikuwa mahali peupe ambapo mtu yeyote angeweza kuzipata kwa urahisi.”
PERESTROIKA—WAKATI WA MABADILIKO
Marekebisho yaliyoitwa perestroika yaliyotangazwa mnamo 1985 hayakuleta matokeo yaliyotarajiwa. Katika maeneo fulani, Mashahidi walikamatwa na kufungwa gerezani kama awali. Hata hivyo, mnamo 1988 ofisi ya Ujerumani iliandikia makao makuu ya ulimwengu barua ifuatayo: “Mwanzoni mwa mwaka wa utumishi wenye mamlaka walionekana tayari kuwapa [akina ndugu katika USSR] uhuru zaidi wa kukutana au hata kupata vichapo ikiwa wangeandikisha makutaniko yao kwenye serikali za wilaya. Katika maeneo mengi waliadhimisha Ukumbusho bila kusumbuliwa. Wanahisi kwamba mtazamo wa wenye mamlaka kuwaelekea umebadilika sana.”
Baada ya muda, ndugu waliowekwa rasmi waliipa ofisi ya Ujerumani anwani za ndugu waliokubali kupokea vifurushi vya chakula cha kiroho. Nao wangewapa wazee ambao wangehakikisha kila mtu anapata vichapo hivyo vya kiroho. Kufikia Februari 1990 anwani 1,600 zilitumiwa kupokea chakula cha kiroho mara moja kwa mwezi.
Mnamo 1989, maelfu ya Mashahidi kutoka Muungano wa Sovieti walihudhuria kusanyiko la pekee huko Poland. Yevdokia, Shahidi katika jiji la Naberezhnye Chelny anakumbuka: “Tulisali kwa bidii Yehova atusaidie kuhudhuria kusanyiko la kwanza halisi. Msimamizi wangu kazini aliposikia ninataka kutoka nchini aliuliza kwa mshangao: ‘Eti nini? Kwani hutazami televisheni? Mpaka umefungwa na hakuna anayeruhusiwa apite!’
“Nilimjibu kwa uhakika kabisa, ‘Mpaka utafunguliwa.’ Na hivyo ndivyo ilivyokuwa. Kwenye kituo cha forodha huko Brest, ni Mashahidi wa Yehova tu walioruhusiwa kupita. Hata hatukupekuliwa nasi tulitendewa kwa fadhili. Mtu mmoja ambaye si Shahidi alijifanya kuwa anaenda kusanyikoni pamoja nasi. Maofisa wa forodha walimgundua haraka na wakamkamata. Walijuaje hakuwa mmoja wetu? Wote waliokuwa wanaenda kusanyikoni walikuwa na tabasamu changamfu na mifuko midogo tu.”
TWAKARIBISHWA KWA UCHANGAMFU HUKO MOSCOW
Mashahidi wa Yehova waliomba waandikishwe kisheria huko Moscow mnamo 1949. Miaka 40 ilikuwa imepita tangu watoe ombi hilo. Wakati huo, akina ndugu hawangekubali matakwa yaliyowekwa na serikali ya Stalin. Lakini Februari 26, 1990, mwenyekiti wa Kamati ya Mambo ya Kidini huko Moscow alikutana na wawakilishi wa Mashahidi wa Yehova. Pia manaibu wawili wa mwenyekiti na washiriki wengine watatu walihudhuria mkutano huo. Mashahidi wa Yehova waliwakilishwa na watu 15: ndugu 11 kutoka Urusi na jamhuri nyingine za Muungano wa Sovieti, Milton Henschel na Theodore Jaracz kutoka Brooklyn, na pia Willi Pohl na Nikita Karlstroem kutoka ofisi ya tawi ya Ujerumani.
Mwenyekiti alianza mkutano huo kwa kusema: “Tunafurahi kukutana na Mashahidi wa Yehova. Nimesikia mengi kuwahusu lakini hii ndiyo mara ya kwanza kukutana nanyi. Tungependa kuwa na mazungumzo ya wazi kupatana na roho ya glasnost (uwazi).” Akina ndugu walisema wanataka kuwasilisha ombi la kuandikisha kisheria utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti. Mwenyekiti aliendelea kusema: “Tunafurahi kusikia hivyo na mmekuja wakati bora zaidi. Karibuni kutakuwa na majira ya kupanda. Hivyo tunaweza kutazamia matokeo mazuri na matunda mema.”
Wakati mwenyekiti alipowauliza akina ndugu wajitambulishe, ilionekana wazi kwamba Mashahidi wa Yehova walitoka sehemu zote za nchi kuanzia Kaliningrad hadi Mashariki ya Mbali. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema: “Ninawakilisha makutaniko manne katika Wilaya ya Irkutsk. Pia ninatumikia makutaniko katika Mashariki ya Mbali, kwenye maeneo yenye shughuli nyingi ya Khabarovsk na Krasnoyarsk, na katika wilaya za Novosibirsk na Omsk.” Mwenyekiti akasema, “Mna eneo kubwa sana, hata kuliko ukubwa wa mataifa mengi!”
Naibu mmoja wa mwenyekiti akasema: “Tunahitaji kujua vizuri zaidi mambo mnayoamini kwani hatuelewi baadhi yake. Kwa mfano, katika kitabu kimoja mnasema Mungu ataisafisha dunia na kuondoa serikali zote. Hatuelewi jambo hilo.” Ndugu Pohl alijibu hivi: “Mashahidi wa Yehova hawashiriki vurugu zozote. Ikiwa kitabu kinasema hivyo, kinarejezea unabii hususa wa Biblia. Mashahidi wa Yehova wanahubiri kuhusu Ufalme wa Mungu na uzima wa milele katika paradiso duniani.”
Naibu huyo akasema, “Imani hiyo haina ubaya wowote.”
Mwishoni mwa mazungumzo hayo, mwenyekiti alisema: “Tumefurahi sana kukutana nanyi. Mtaandikishwa haraka iwezekanavyo.”
Mnamo Machi 1991, Mashahidi wa Yehova waliandikishwa kisheria huko Urusi. Urusi ilikuwa na zaidi ya watu milioni 150, na wahubiri wa Ufalme 15,987. Akina ndugu na dada nchini Urusi walihitaji kufundishwa zaidi na Yehova.—Mt. 24:45; 28:19, 20.
“TUNA FURAHA NA UHURU ULIOJE!”
Kwa sababu nchi ya Finland ipo karibu na Urusi, Baraza Linaloongoza liliiomba ofisi ya tawi ya Finland isaidie kupanga kusanyiko la kimataifa huko St. Petersburg, Urusi lililofanyika, Juni 26 hadi 28, 1992. Akina ndugu walihisije kukusanyika kwa uhuru baada ya kuishi chini ya marufuku ya zaidi ya miaka 50? Ndugu mmoja anakumbuka: “Tulikuwa maelfu kwenye uwanja wa kusanyiko. Machozi yalibubujika bila kukoma. Ilikuwa furaha na uhuru ulioje! Hatukuwazia kuwa na uhuru kama huo katika mfumo huu wa mambo. Lakini Yehova aliwezesha jambo hilo. Tulikumbuka jinsi tulivyotengwa katika seli tukiwa watano katika kambi yenye ua mrefu na wanne kati yetu wangempasha joto yule wa tano kwa zamu. Uwanja wa kusanyiko ulikuwa na ukuta mrefu. Lakini hatukutaka kutoka hapa. Hatuwezi kueleza hisia hiyo.
“Tulilia muda wote wa kusanyiko. Tulilia kwa shangwe ya kuona muujiza huo. Ingawa tulikuwa na umri wa zaidi ya miaka 70, tulitembea kana kwamba tuna mabawa. Tulisubiri uhuru huo kwa miaka 50. Kwanza Yehova aliruhusu tuhamishwe hadi Siberia, kisha tufungwe gerezani na kwenye kambi. Lakini sasa tulikuwa katika uwanja wa kusanyiko! Yehova ana nguvu kuliko mtu mwingine yeyote. Tulisimama tukitazamana na tukalia. Hakuna yeyote aliyeamini hilo lilikuwa likitukia. Baadhi ya vijana walituzunguka na kutuuliza: ‘Mna tatizo lolote? Je, kuna mtu yeyote aliyewaumiza?’ Lakini hatungeweza kujibu kwa sababu ya kulia. Huku tukilia, mmoja wetu alisema, ‘Tunalia kwa shangwe!’ Tuliwasimulia jinsi tulivyomtumikia Yehova miaka mingi chini ya marufuku. Na sasa hatukuweza kuamini kwamba ghafula Yehova amebadili kila kitu.”
Baada ya kusanyiko hilo lisilosahaulika, ofisi ya tawi ya Finland iliombwa itume mapainia wa pekee 15 nchini Urusi. Julai 1, 1992, Hannu na Eija Tanninen, wenzi wa ndoa wenye bidii kutoka Finland, walifika huko St. Petersburg. Mwanzoni, jambo gumu zaidi walilokabili ni kujifunza Kirusi. Baada ya somo lao la kwanza katika lugha hiyo, walienda kuhubiri na kuwatolea watu funzo la Biblia. Hannu anakumbuka hivi: “Katika miaka ya mapema ya 1990, karibu kila mtu alitaka kujifunza Biblia. Tulipohubiri barabarani, watu walitueleza walipoishi. Wote walitaka vichapo. Ikiwa ungempa mmoja gazeti au trakti, wengine kumi walipoiona walikuja na kuomba vichapo. Watu walichukua vichapo na wakaanza kusoma hapohapo barabarani au kwenye gari-moshi.”
Kuanzia Oktoba 1992, mapainia wengi wa pekee walitoka Poland pia. Kikundi cha kwanza kilitia ndani dada waseja. Baada ya muda mfupi, kikundi cha pili kutoka Poland kiliwasili na kikatumwa St. Petersburg. Baada ya mwaka, kikundi cha mapainia Wapolandi kilitumwa huko Moscow. Miaka ya baadaye, zaidi ya wajitoleaji 170 kutoka Poland, hasa kutoka Shule ya Mazoezi ya Kihuduma (MTS), waliwekwa rasmi nchini Urusi.
MLANGO MKUBWA UNAOONGOZA KWENYE UTENDAJI
Baada ya kusanyiko hilo la kimataifa huko St. Petersburg, Baraza Linaloongoza liliwapa akina ndugu ruhusa ya kununua eneo linalofaa (ekari 17) lililokuwa na majengo ya zamani katika kijiji cha Solnechnoye, karibu na jiji. Ulikuwa wakati wa kujenga Betheli ya Urusi. Ofisi ya tawi ya Finland iliombwa isaidie katika ujenzi huo. Mnamo Septemba 1992 kikundi cha kwanza cha wajitoleaji kutoka Finland kilifika Solnechnoye. Aulis Bergdahl, ndugu katika kikundi hicho aliyekuja kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi, anakumbuka: “Mimi na mke wangu Eva Lisa tulikubali kwa shangwe mwaliko wa kusaidia kujenga Betheli ya Urusi. Ilikuwa wazi kwetu kwamba Yehova anaelekeza mambo. Ndugu ulimwenguni pote walitegemeza kazi.”
Msimamizi wa ujenzi, Alf Cederlöf na mke wake Marja-Leena, waliwachochea sana akina ndugu walioshiriki katika ujenzi. Pia washiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Finland, walitutia moyo sana. Ndugu kutoka makao makuu ya Brooklyn walitutembelea pia. Aulis anakumbuka: “Mnamo 1993, Milton Henschel alitutembelea baada ya kusanyiko la kimataifa huko Moscow. Alitutia moyo sana katika hotuba alizowatolea wajenzi na pia katika mazungumzo ya kibinafsi.”
Kulikuwa na wajitoleaji 700 hivi kutoka nchi za Skandinavia, Ulaya, Amerika, Australia, Urusi, na jamhuri nyingine za uliokuwa Muungano wa Sovieti katika ujenzi wa Betheli hiyo. Walitoka katika utamaduni na malezi mbalimbali na njia tofauti za kufanya kazi. Lakini kazi ilikamilishwa kama Zekaria 4:6 inavyosema, “‘si kwa jeshi, wala kwa nguvu, bali kwa roho yangu,’ Yehova wa majeshi amesema.” Kwa kweli, Yehova alikuwa akiijenga “nyumba” hiyo. (Zab. 127:1) Ndugu Warusi walijitolea kwa hiari katika kazi ya Ufalme. Wengi walikuwa vijana na wapya katika kweli, lakini wengi wao tayari walikuwa mapainia. Walitaka sana kujua jinsi ya kujenga haraka, kwa njia ya hali ya juu, na kushughulikia mambo yanayohusu tengenezo la kitheokrasi.
KUPANGA KAZI
Karibu mwisho wa 1993, washiriki wa Halmashauri ya Nchi ya Urusi walifika Solnechnoye. Walioalikwa walikuwa Ivan Pashkovsky, Dmitry Livy, Vasily Kalin, Aleksey Verzhbitsky, Anatoly Pribitkov na Dmitry Fedunishin. Mwaka mmoja baadaye, Mikhail Savitsky alijiunga nao. Baraza Linaloongoza lilimtuma Horst Henschel kutoka ofisi ya tawi ya Ujerumani awasaidie akina ndugu kupanga kazi.
Jambo la kwanza kupangwa lilikuwa kazi ya kuzunguka. Mwanzoni, kulipangwa mizunguko mitano, miwili huko St. Petersburg na mitatu huko Moscow na maeneo ya karibu. Waangalizi watano wa mzunguko wa kwanza wa wakati wote walikuwa Artur Bauer, Pavel Bugaisky, na Roy Öster huko Moscow na Kzyztov Poplawski na Hannu Tanninen huko St. Petersburg. Baadaye, Roman Skiba aliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko. Matthew Kelly, aliyehitimu shule ya MTS mnamo 1992 huko Marekani, aliwekwa kuwa mwangalizi wa wilaya wa muda.
Hannu Tanninen anakumbuka jinsi ziara za kwanza zilivyokuwa katika miaka ya mapema ya 1990: “Nilituma barua kuhusu ziara kwenye kutaniko moja huko Petrozavodsk, Karelia. Barua hiyo ilionyesha jinsi ya kuongoza mikutano juma hilo. Mimi na mke wangu tulipofika, mzee mmoja alikutana nasi kwenye kituo cha gari-moshi na tukaenda nyumbani kwake. Alinionyesha barua hiyo na kusema, ‘Tulipokea barua yako lakini hatukuielewa, hivyo tukaamua tusifanye chochote hadi ufike utueleze kila kitu.’
“Katika ziara ya kwanza huko Murmansk kulikuwa na wahubiri 385 wakiongoza zaidi ya mafunzo 1,000 ya Biblia. Hata hivyo, wengi zaidi walijifunza Biblia kwani waliopendezwa walijifunza wakiwa vikundi. Kwa mfano, dada mmoja painia alikuwa na mafunzo 13, lakini alikuwa akijifunza na watu zaidi ya 50!
“Mgawo wetu wa pili ulikuwa katika wilaya za Volgograd na Rostov. Huko Volgograd, kulikuwa na makutaniko manne tu na watu zaidi ya milioni moja. Akina ndugu walitaka sana kujua jinsi ya kuongoza mikutano na mafunzo ya Biblia na jinsi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kila ziara tulilazimika kuanzisha makutaniko mapya. Tulipoandika ripoti ya ziara ya mwangalizi wa mzunguko, tulihesabu watu waliobatizwa tangu ziara iliyopita. Kila kutaniko lilikuwa na watu 50, 60, au 80 waliobatizwa tangu ziara iliyotangulia, na zaidi ya 100 walibatizwa katika kutaniko moja! Hivyo, makutaniko 16 yaliundwa katika jiji hilo katika miaka mitatu tu.”
Mnamo Januari 1996, Halmashauri ya Tawi iliwekwa rasmi nchini Urusi. Wakati huohuo, waangalizi wa wilaya wa wakati wote waliwekwa rasmi. Kati yao kulikuwa na Roman Skiba (Siberia na Mashariki ya Mbali), Roy Öster (Belarus, Moscow, na St. Petersburg kufikia Milima ya Ural), Hannu Tanninen (Caucasia kufikia Volga), na Artur Bauer (Kazakhstan na Katikati ya Asia). Siku hizo, zaidi tu ya kutumikia wilaya waliyogawiwa waangalizi hao walitumikia pia mzunguko mdogo.
KUSAFIRI MAENEO YA MBALI
Roman Skiba alikuwa mmoja wa mapainia wa pekee waliofika kwanza nchini Urusi kutoka Poland mapema mnamo 1993. Anakumbuka hivi: “Oktoba 1993, nilipokea mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko. Mzunguko wangu wa kwanza ulitia ndani makutaniko kusini mwa St. Petersburg, Wilaya ya Pskov, na Belarus yote. Hata hivyo, huo haukuwa mzunguko mkubwa zaidi nchini Urusi. Nilihitaji kuzoea kusafiri mbali. Mnamo Novemba 1995, nilipewa mgawo wa kuzunguka kwenye Milima ya Ural na kuwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa wilaya wa badala. Eneo langu lilitia ndani Milima ya Ural, Siberia yote, na Mashariki ya Mbali. Ndugu mmoja alikadiria kwamba wilaya hiyo ingeweza kulingana na nchi 38 zinazotoshana na Poland! Kulikuwa na kanda nane za wakati! Miaka miwili hivi baadaye, ofisi ya tawi iliniomba nitembelee kikundi huko Ulaanbaatar, mji mkuu wa Mongolia.”
Ndugu Skiba anaendelea kusema: “Wakati mmoja ili niweze kufika Yekaterinburg kutoka Noril’sk, iliyoko kaskazini ya Mzingo wa Aktiki, nilihitaji kusafiri kwa ndege mbili, kwanza kutoka Noril’sk hadi Novosibirsk, kisha hadi Yekaterinburg. Safari hiyo ilionekana kana kwamba haitakwisha. Ndege tuliyotumia kutoka Noril’sk ilicheleweshwa kwa saa 12 hivyo mimi na mke wangu Lyudmila tulikaa siku nzima kwenye kituo cha ndege. Uzuri ni kwamba tulikuwa tumejifunza kufanya funzo letu la kibinafsi tunaposafiri.
“Nyakati nyingine, licha ya jitihada zetu zote, tulichelewa kufika kwenye ziara. Ili kufika kwenye kutaniko katika kijiji cha mlimani huko Ust’-Kan, Altai, tulilazimika kuendesha gari kwenye barabara ya mlimani ya vumbi. Kwa kusikitisha, gari letu liliharibika njiani nami nilichelewa kwa saa mbili kufika mkutanoni hivyo hata nisingeweza kukagua rekodi za kutaniko. Tulivunjika moyo na kufikiri kila mtu alikuwa ameondoka. Tulishangaa kama nini kukuta watu 175 wakitusubiri kwenye jumba lililokodishwa, ingawa kutaniko hilo lilikuwa na wahubiri 40 hivi tu! Inaonekana tulipochelewa, watu wengi wanaopendezwa kutoka vijiji vingine vya milimani walifika mkutanoni.”a
MAKUSANYIKO YASIYOSAHAULIKA
Makusanyiko ya wilaya yalifanywa kwa mara ya kwanza katika majiji fulani makubwa, ambako akina ndugu hawakuwa na uzoefu wa kutayarisha makusanyiko. Mnamo 1996, huko Yekaterinburg, akina ndugu walichagua uwanja unaofaa wa michezo ili kufanyia kusanyiko la wilaya. Roman Skiba anakumbuka: “Nyasi ziliota kwenye mabenchi, na ndani ya uwanja mibetula ilikuwa na kimo cha mita mbili. Majuma matatu yalisalia kabla ya kusanyiko, na kulikuwa na makutaniko matatu katika jiji na vitongoji. Msimamizi wa uwanja alishirikiana nasi hata ingawa hakuelewa jinsi tunavyoweza kufanya kusanyiko katika uwanja huo. Akina ndugu walianza kazi, na siku iliyowekwa, uwanja ulikuwa unapendeza. Msimamizi hakuamini macho yake!” Akichochewa na uthamini, msimamizi aliruhusu Shule ya Utumishi wa Painia ifanywe kwenye jengo moja la uwanja huo. Ndugu mmoja anakumbuka, “Baada ya kusanyiko, uwanja huo ulianza tena kutumiwa kwa ajili ya michezo, nayo ilililetea jiji hilo mapato.”
Mara nyingine, ndugu walihitaji kubadilikana na kuwa wadumifu ili wafanye makusanyiko. Mnamo 1999 huko Vladikavkaz, akina ndugu walishindwa kukodisha uwanja kwa ajili ya kusanyiko la mzunguko ambalo lingehudhuriwa na watu 5,000. Kwa hiyo mara moja wakaanza kupanga kugawanya kusanyiko hilo. Programu iliyofupishwa ya siku moja ilifanywa mara tano huko Vladikavkaz katika jumba la sinema lililokodishwa. Mwisho wa juma hilo, programu ya kusanyiko la siku mbili ilifanywa katika maeneo mawili yaliyotenganishwa kwa kilomita mbili hivi katika jiji la Nal’chik. Kusanyiko katika jumba moja lilianza saa mbili baada ya lile la kwanza ili wasemaji wasafirishwe kwenye kusanyiko la pili. Waangalizi fulani wanaosafiri waliona kwamba wangepoteza sauti kabla ya makusanyiko kwisha. Ndugu mmoja alikadiria kwamba alitoa hotuba 35 juma hilo! Kila kitu kilienda sawa hadi programu kwenye ukumbi mmoja ilipovurugwa kipindi cha asubuhi cha Jumamosi kilipokuwa karibu kwisha. Watu waliovalia sare waliingia wakiwa na mbwa na kusema kila mtu aondoke. Kama kawaida akina ndugu na dada walitulia na kuondoka kwenda kula chakula cha mchana na kuzungumza. Iligundulika kwamba mtu fulani mwenye msimamo mkali wa kidini aliwapigia wenye mamlaka simu na kuwaambia kuna bomu katika ukumbi huo. Ukumbi ulichunguzwa na hakuna kilichopatikana hivyo akina ndugu wakaruhusiwa kuendelea na kusanyiko. Baada ya programu kufanyiwa mabadiliko fulani kusanyiko lilimalizwa vizuri na kila mtu akanufaika na programu hiyo.
MAWE, NGAO, NA PANGA
Mbegu za kweli zilienezwa haraka nchini kote. Eija Tanninen, anakumbuka: “Mnamo 1998, tulikuwa tunajitayarisha kwa ajili ya safari ya saa 15 kwa gari-moshi kutoka kusanyiko moja la wilaya hadi lingine. Akina ndugu walituomba tuwabebee vifaa vingi sana vya drama ya kusanyiko. Ilikuwa hatari kwani tulijua wahudumu wa gari-moshi hawakuwapenda abiria wenye mizigo mingi. Tukisaidiwa na akina ndugu tulibeba mawe, ngao, panga, na mifuko iliyojaa nguo za kuigizia kwenye chumba chetu cha watu wanne. Tuliketi humo na vitu vyetu vyote na abiria wengine wawili waliokuwa katika chumba hicho.
“Mhudumu wa gari-moshi alipokuja kukagua tiketi zetu alituuliza kwa nini tunabeba mizigo mingi hivyo. Tulimweleza kwamba hivyo ni vifaa vya drama itakayoonyeshwa katika kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova. Alikuwa mwenye fadhili sana na akatuambia kwamba wakati fulani uliopita, alihudhuria hotuba ambayo mume wangu alitoa tulipotembelea kutaniko katika eneo aliloishi. Tulihisi Yehova ametusaidia.”
WATAZAMAJI WAKATI WA FUNZO
Akina dada wangeweza kufundishana mambo mengi. Eija anakumbuka hivi: “Ninawazia tu jinsi akina dada walivyohitaji kuwa na subira na unyenyekevu tulipoanza huduma yetu huko Urusi, kwani nisingeweza kuzungumza lugha hiyo vizuri. Niliguswa sana kuona akina dada wakiwa na tamaa ya kujifunza kuongoza mafunzo ya Biblia. Wengi walikuwa wapya na wengine walitumikia chini ya marufuku wakati haingewezekana nyakati zote kupokea miongozo ya tengenezo la Yehova.
“Kuanzia 1995 hadi 1996 tulitumikia katika mji wa Volzhskiy. Mara nyingi dada aliponikaribisha kwenye funzo lake la Biblia, dada kadhaa wangeomba waandamane nasi. Mwanzoni sikuelewa kwa nini lakini walinieleza walitaka kuona na kujifunza kuongoza mafunzo ya Biblia. Niliwaambia kwamba ni sawa ikiwa mwanafunzi wa Biblia hapingi na haaibiki. Kwa kawaida dada sita au kumi wangekuja, kwa sababu waliamini hawangemsumbua mwanafunzi wa Biblia na hawakumsumbua. Baada ya miezi kadhaa niliona wanafunzi wengi wa Biblia walioanzisha mafunzo yao wenyewe ya Biblia. Wakati huo, kulikuwa na makutaniko mawili tu huko Volzhskiy. Baada ya miaka kumi kulikuwa na makutaniko 11.”
SALA YAKE ILIJIBIWA
Ilikuwa wazi kuwa si akina ndugu na dada wapya tu walionufaishwa na miongozo ya kitheokrasi, bali pia wale waliomtumikia Yehova muda mrefu chini ya marufuku. Hannu Tanninen, anakumbuka hivi: “Katika hali tofauti mara nyingi tulihisi mwongozo wa malaika na tukajionea matukio yaliyotuvutia sana. Mnamo 1994, tulienda kwenye kutaniko jipya huko Novgorod ambako sasa pia kunaitwa Veliky Novgorod, na akina ndugu wakatupeleka kwenye nyumba ambayo tungeishi juma hilo. Ndani ya nyumba hiyo mlikuwa na mgeni anayeitwa Maria, dada mwenye umri mkubwa aliyekuwa amesafiri kilomita 50 kwa ajili ya tukio hilo. Alikuwa katika kweli kwa zaidi ya miaka 50 na alitamani kukutana na mmoja wa waangalizi wa mzunguko wa kwanza kutumika baada ya marufuku. Tulimwomba atueleze jinsi alivyojifunza kweli. Alituambia kwamba alipokuwa na umri wa miaka 17, alipelekwa kwenye kambi ya mateso huko Ujerumani na akakutana na Mashahidi wa Yehova. Alikubali kweli na akabatizwa kambini na dada mtiwa mafuta. Mwishowe Maria alifunguliwa na akarudi Urusi ili ahubiri habari njema za Ufalme. Baada ya muda alikamatwa na kufungwa kwa sababu ya kuhubiri. Alifungwa kwa miaka mingi katika kambi za kazi ngumu za Sovieti.
“Alipokuwa akimalizia kutusimulia, tuliguswa sana kumsikia dada huyu mnyenyekevu akisema kwamba kwa majuma machache alikuwa akisali Yehova amwonyeshe ikiwa kuna jambo ambalo si sawa kuhusu jinsi alivyokuwa akimwabudu. Baadaye jioni hiyo, nilimwambia kwamba zamani, makala ya “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi ilizungumzia jambo fulani. Ilisema kwamba ili ubatizo uwe halali, ilikuwa muhimu ufanywe na ndugu Mkristo. Maria alishukuru sana. Alihisi alikuwa amepata jibu la swali lake. Alifurahi sana kubatizwa katika beseni kubwa ya bafu. Miaka 50 ilikuwa imepita tangu alipojiweka wakfu katika 1944.”
CHAKULA CHA KIROHO CHASAFIRISHWA MBALI SANA
Tokea mwanzoni mwa 1991, vichapo vilisafirishwa hadi Urusi katika vifurushi vidogo kutoka Ujerumani au Finland. Mnamo Julai 1993, lori la kwanza kutoka Ujerumani lilifika huko Solnechnoye, likiwa na vichapo vyenye uzito wa tani 20. Malori kutoka ofisi ya tawi ya Urusi yalisafirisha vichapo hadi Moscow, Belarus, na Kazakhstan. Haikuwa rahisi kusafirisha vichapo hivyo. Kwa mfano, Kazakhstan ilikuwa umbali wa kilomita 5,000 na akina ndugu walihitaji kufikisha vichapo huko. Pindi nyingine wangecheleweshwa mpakani, na katika majira ya baridi kali malori yalikwama katika theluji.
Sasa, tani 200 za vichapo hupelekwa Solnechnoye kila mwezi. Madereva wa Betheli hutumia nafasi zote kuwatolea ushahidi askari wa mpakani au maofisa wa forodha. Kati yao kuna wachache wanaofurahia kusoma vichapo vya Biblia. Wakati wa upekuzi, polisi mmoja alichambua dini kwa ujumla alipotambua lori la Betheli lilikuwa la shirika la kidini. Alieleza jinsi alivyotukanwa na kasisi aliyemsimamisha kwa kuvunja sheria za barabarani. Akina ndugu walimweleza jinsi Mungu anavyowatendea watu na kusudi lake kwa dunia na wanadamu. Polisi huyo alibadili sauti na akawa na urafiki zaidi. Aliuliza maswali, hivyo akina ndugu wakatoa Biblia na wakafurahia mazungumzo yenye kujenga pamoja. Polisi huyo aliguswa moyo sana hivi kwamba akasema, “Nitawatafuta Mashahidi ili niendeleze mazungumzo.”
Tokea 1995 hadi 2001, ofisi ya tawi ya Japani iliyatumia makutaniko vichapo huko Vladivostok, katika Mashariki ya Mbali. Kutoka huko akina ndugu walisafirisha vichapo kwa meli hadi makutaniko ya Kamchatka. Akina ndugu huko Vladivostok walifahamiana na manahodha wa meli zilizoenda Kamchatka. Nahodha mmoja alikubali kusafirisha vichapo katika chumba chake bila malipo na hata alisaidia kuvipakia. “Ingawa mimi si mwamini,” nahodha huyo akawaeleza, “ninataka kufanya jambo jema. Ninawapenda sana, nami ninapenda utaratibu wenu. Ninapofika kule ninakopeleka vichapo, sihitaji kusubiri muda mrefu vipakuliwe. Watu wenu ni kama ndege; wao huteremka na kunyakua maboksi ya vichapo na kuondoka.”
UKUZI UNATOKEZA UHITAJI
Kwa miaka mingi, Mnara wa Mlinzi lilitolewa mara moja kwa mwezi katika Kirusi, na lilikuwa na kurasa 16 tu zilizochapishwa katika karatasi kubwa kidogo kuliko zinazotumiwa sasa. Makala zote za funzo zilitafsiriwa katika Kirusi na ndugu wote katika Muungano wa Sovieti walizipata, lakini zilichapishwa muda mrefu baada ya zile za Kiingereza. Makala za funzo zilichelewa kwa kati ya miezi sita hadi miaka miwili, na makala za ziada zilichapishwa baadaye. Kuanzia 1981, Mnara wa Mlinzi lilitolewa mara moja kwa mwezi katika Kirusi kwenye kurasa 24, na kuanzia 1985 likaanza kuchapishwa mara mbili kwa mwezi. Gazeti la Juni 1, 1990 likawa la kwanza kuchapishwa sambamba na la Kiingereza likiwa na kurasa 32 na rangi kamili.
Tanja, mmoja wa watafsiri, anakumbuka: “Tukitazama nyuma, tunajua kuwa vichapo vingi tulivyotafsiri na kuchapisha wakati huo havikupatana na kanuni ya kutafsiri kwa lugha ya kawaida na inayoeleweka kwa urahisi. Lakini ilikuwa tafsiri bora zaidi ambayo tungetokeza chini ya hali hizo. Na hicho ndicho chakula kilichohitajiwa na watu wenye njaa kiroho.”
Marufuku ilipoondolewa katika nchi za ule uliokuwa Muungano wa Sovieti, vichapo vyetu vilisambazwa sana. Watafsiri wa Urusi wanaofanya kazi Ujerumani walikuwa tayari kusaidiwa. Mambo mawili mapya yalichangia kuboreshwa kwa tafsiri. Kwanza, akina ndugu na dada kadhaa kutoka Urusi na Ukrainia walienda kwenye ofisi ya tawi ya Ujerumani ili kuzoezwa kutafsiri. Watano kati yao waliwasili Septemba 27, 1991 na wengine walijiunga nao baadaye. Kwa hiyo kikundi cha watafsiri wa Kirusi kikaanza kuboreshwa. Lakini kulikuwa na matatizo kadhaa. ‘Miti na mawe’ yao hayakubadilika mara moja kuwa “dhahabu” lakini yalihitaji kupitia hatua zote zinazotajwa katika Isaya 60:17.
Pili, watafsiri wa Kirusi walianza kufaidika na kazi ya Idara ya Utumishi wa Tafsiri iliyoanzishwa karibuni. Semina ya watafsiri ilifanywa kwenye ofisi ya tawi ya Ujerumani akina ndugu na dada wa kwanza kutoka Urusi walipoenda Selters, huko Ujerumani.
Inafaa kwamba kazi ya kutafsiri ifanywe katika nchi ambayo lugha hiyo inazungumzwa. Kwa hiyo lilikuwa jambo la kusisimua kikundi cha watafsiri wa Kirusi walipoondoka ofisi ya tawi ya Ujerumani mnamo Januari 1994 ili wakaishi katika Betheli iliyokuwa ikijengwa huko Solnechnoye.
Kuna akina ndugu ambao kwa miaka mingi walisaidia kutafsiri kwa ajili ya ndugu waliokuwa katika Muungano wa Sovieti. Ilikuwa vigumu kuachana nao kwani hali za wengine wao hazingewaruhusu waondoke pamoja na watafsiri wa Kirusi waliokuwa wakirudi Urusi. Kikundi cha ndugu na dada 17, pamoja na ndugu wengine 2 ambao wangetumikia kama mapainia wa pekee, kilitoka Selters Jumapili, Januari 23, 1994 huku wao na wale waliobaki wakilia na kukumbatiana.
“MIMI NDIYE MUNGU WA MGONJWA”
Kwa miaka mingi huko Urusi, maoni ya madaktari na wahudumu wa afya kuhusu imani ya kidini ya wagonjwa yalitegemea mambo mawili: elimu yao kwamba hakuna Mungu na matumizi makubwa ya damu katika matibabu ya Wasovieti. Hivyo, Mashahidi waliohitaji matibabu walipoomba wasitiwe damu, madaktari walishangaa au kuwafokea.
Mara nyingi madaktari wangesema, “Hapa, mimi ndiye Mungu wa mgonjwa!” Ikiwa mgonjwa hangekubaliana na daktari, angeondolewa hospitalini mara moja. Isitoshe, mara nyingi msimamo wa Mashahidi unaotegemea Biblia kuhusu kutiwa damu mishipani ulitumiwa na wapinzani kujaribu kupiga marufuku utendaji wetu nchini Urusi.
Mnamo 1995 katika ofisi ya tawi ya Urusi, Dawati la Habari za Hospitali lilianza kufanya kazi ili kuwapa wataalamu wa kitiba habari sahihi kuhusu msimamo wa Mashahidi wa Yehova. Semina kadhaa zilifanywa, nao wazee kutoka zaidi ya Halmashauri 60 za Uhusiano na Hospitali walijifunza jinsi ya kuwapa madaktari na wataalamu wa kitiba habari zinazohitajika kutia ndani jinsi ya kuwapata madaktari ambao wangewatibu wagonjwa Mashahidi bila damu.
Huko Moscow mnamo 1998, madaktari Warusi na madaktari wenzao kutoka nchi nyingine walikuwa na mkutano uliokuwa na kichwa “Upasuaji Usiohusisha Damu,” mkutano wa kwanza wa aina hiyo nchini Urusi. Zaidi ya madaktari 500 kutoka maeneo mengi nchini Urusi walihudhuria. Kati ya 1998 na 2002, madaktari Warusi walipata uzoefu wa kutosha ili kuwa na mikutano mingi kama hiyo katika majiji makubwa ya Urusi. Mikutano hiyo ilikuwa na matokeo mazuri.
Dakt. A. I. Vorobyov, aliyekuwa waziri wa afya na mtaalamu mkuu wa damu katika Shirikisho la Urusi, aliwaandikia barua rasmi wanasheria waliotetea haki za wagonjwa Mashahidi, akisema kwamba baada ya madaktari kubadili maoni yao kuhusu kutia damu mishipani, “idadi ya vifo vya akina mama wanaozaa katika nchi yetu vimepungua kwa asilimia 34.” Kisha Dakt. Vorobyov akasema: “Kabla ya hapo, idadi ya akina mama waliokufa ilikuwa mara nane ya akina mama waliokufa huko Ulaya kwa sababu wakunga waliwapa akina mama damu bila sababu maalumu.”
Mnamo 2001, taasisi zote za kitiba nchini zilitumiwa maagizo na wizara ya afya ya Shirikisho ya Urusi. Maagizo hayo yalisema kuwa daktari anapaswa kuheshimu msimamo wa mgonjwa kukataa kutiwa damu kwa sababu za kidini. Mnamo 2002, wizara ya afya nchini Urusi ilitoa Mwongozo wa Kutumia Visehemu vya Damu. Mwongozo huo unasema mgonjwa atatiwa damu iwapo tu ameandika hati ya kukubali. Pia unaonyesha mgonjwa akikataa kutiwa visehemu vya damu kwa sababu za kidini, basi matibabu ya badala yanapaswa kutumiwa.
Madaktari wengi walibadili mtazamo kuhusu matumizi ya damu baada ya kufanya kazi na wawakilishi wa Dawati la Habari za Hospitali. Daktari mmoja wa upasuaji alisema hivi: “Nimeambiwa na wagonjwa [Mashahidi] na ninyi pia kwamba kukataa kwenu damu hakutegemei hisia bali kunategemea sheria ya Biblia. Niliamua kuthibitisha jambo hilo. Nilisoma mistari yote ya Biblia iliyonukuliwa katika habari mliyonipa. Baada ya kutafakari, nilikubali kwamba msimamo wenu unategemea Biblia. Lakini kwa nini makasisi hawasemi chochote kuhusu hilo? Sasa, mazungumzo kuhusu damu yanapotokea, ninawaambia madaktari wengine kuwa Mashahidi ndio wanaofuata Biblia.” Leo, zaidi ya madaktari 2,000 nchini Urusi huwatibu wagonjwa Mashahidi bila damu.
WANATUMIKIA KWA SHANGWE KATIKA MIGAWO YAO
Arno na Sonja Tüngler ambao walihitimu kutoka Shule ya Gileadi iliyofanyiwa huko Ujerumani, wamekuwa wakitumika katika majiji kadhaa nchini Urusi tangu Oktoba 1993. Kazi ya Yehova imekuwa na matokeo gani katika maeneo ambayo wametumika? Hebu sikiliza masimulizi yao.
Arno: “Tuliwasili kwenye mgawo wetu huko Moscow. Baada ya majuma machache, tulitoa hotuba zetu za kwanza katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Baada ya kuwa Urusi kwa majuma sita, nilitoa hotuba yangu ya kwanza katika kusanyiko. Tulishirikiana na kutaniko lenye wahubiri waliobatizwa 140 hivi, na eneo la kutaniko hilo lilitoshana na mzunguko mmoja huko Ujerumani! Eneo letu la kwanza lilikuwa karibu na nyumba yetu ya mapainia. Tulifurahi kama nini kuwa Mashahidi wa kwanza kuhubiri eneo hilo nyumba kwa nyumba!”
Sonja: “Ingawa hatukujua Kirusi, nyakati nyingine tulihubiri barabarani tukiwa peke yetu. Tuliongea na watu na kuwapa trakti na vichapo vingine. Ndugu na dada wa huko walijiunga nasi mara nyingi, na ilikuwa rahisi kupata mtu wa kwenda naye mahubiri. Ndugu hao walituonyesha fadhili na subira na walitusikiliza tulipozungumza Kirusi kisicho sahihi. Wenye nyumba pia walikuwa na subira. Muungano wa Sovieti ulikuwa umeporomoka, na watu walipendezwa sana na dini.”
Arno: “Kitu kilichotusaidia sana kujifunza Kirusi ni kushiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba na kuongoza mafunzo ya Biblia. Kufikia Januari 1994, mwezi wetu wa nne huko Urusi, tulikuwa tayari tunaongoza mafunzo ya Biblia 22, kwa hiyo tulikuwa na nafasi nyingi za kusikia na kuzungumza Kirusi cha kawaida.
“Wakati huo, watu wengi sana walibatizwa katika makusanyiko; idadi ya waliobatizwa ingeweza kuwa asilimia 10 au zaidi ya waliohudhuria. Makutaniko kadhaa hayakuwa na ndugu waliostahili kutimiza madaraka ya wazee na watumishi wa huduma. Mzee mmoja alikuwa mwangalizi-msimamizi wa makutaniko matano! Aliniomba nitoe hotuba ya Ukumbusho katika mojawapo ya makutaniko hayo. Watu 804 walihudhuria, na iliwabidi waondoke haraka kwenye jumba hilo kwani kutaniko lingine lilihitaji kutumia jumba hilo. Hata hivyo, msemaji wa kutaniko hilo alipatwa na aksidenti ya barabarani alipokuwa akija kwenye jumba hilo, kwa hiyo hangeweza kufika kwa wakati. Ilinibidi nitoe hotuba ya Ukumbusho tena. Wakati huo, kulikuwa na wahudhuriaji 796! Hivyo, katika makutaniko mawili tu, watu 1,600 walihudhuria Ukumbusho. Hilo linaonyesha jinsi watu wengi walivyopendezwa sana na kweli wakati huo.”
YEHOVA ‘ANAHARAKISHA’ MAVUNO
Katika Neno lake, Yehova anaahidi ‘kuharakisha’ kukusanywa kwa ‘vitu vyake vyenye kutamanika.’ (Isa. 60:22; Hag. 2:7) Mnamo 1980, kulikuwa na wahubiri 65 huko St. Petersburg ambao licha ya kupelelezwa sana na KGB, walijaribu kuwa na mazungumzo ya Biblia na wakazi wa jiji hilo. Kufikia 1990, Mashahidi zaidi ya 170 walikuwa wakihubiri barabarani kwa njia isiyo rasmi katika sehemu mbalimbali za jiji hilo. Machi 1991, utendaji wa Mashahidi nchini Urusi uliandikishwa kisheria, na muda mfupi baada ya hapo makutaniko matano yakaanzishwa katika jiji hilo. Kusanyiko la kimataifa lililofanywa St. Petersburg mwaka wa 1992, na pia matukio mengine ya kitheokrasi yalichangia sana ukuzi wa haraka. Mnamo 2006, zaidi ya makutaniko 70 yalikuwa yakihubiri eneo la St. Petersburg.
Katika mwaka wa 1995, kulikuwa na kutaniko moja tu huko Astrakhan, jiji lililokuwa karibu na mpaka wa Kazakhstan. Kutaniko hilo halikuwa na wazee wala watumishi wa huduma. Hata hivyo, akina ndugu walifanya kusanyiko la mzunguko na pia kusanyiko la pekee. Hotuba zilitolewa na wazee waliosafiri kutoka jamhuri ya Kabardino-Balkaria iliyokuwa kilomita zaidi ya 700 kutoka Astrakhan. Ndugu hao hawakujua ni watu wangapi wangebatizwa katika makusanyiko hayo. Roman Skiba anasimulia hivi: “Mimi na mzee mwingine tuliwasili huko majuma mawili kabla ya kusanyiko ili tuweze kwenda kwenye utumishi wa shambani na kutaniko hilo na pia tupitie maswali ya ubatizo pamoja na wale waliotaka kubatizwa. Hata hivyo, hatukupata hata wakati wa kwenda shambani. Tulitumia wakati wetu wote tukizungumza na wahubiri 20 waliotaka kubatizwa!”
Mnamo 1999, ndugu huko Yekaterinburg waliwaalika kwenye Ukumbusho wafanyabiashara kadhaa katika soko moja. Wafanyabiashara hao waliuliza ikiwa wangeweza kuwaalika marafiki wao pia. Mashahidi walishangaa watu 100 hivi walipokuja kwenye jumba! Ingawa walikodi jumba kubwa, ilibidi watu wengine wasimame.
FUNZO LA BIBLIA LENYE WANAFUNZI 50
Kazi ya kuhubiri katika Wilaya ya Ivanovo ilianza mwishoni mwa mwaka wa 1991 wakati Pavel na Anastasia Dimov walipohamia huko. Huo ulikuwa mgawo mgumu kwa kuwa kulikuwa na wakaaji zaidi ya milioni moja katika eneo hilo. Wangeanzia wapi kuhubiri? Waliamua kutumia njia rahisi lakini yenye matokeo. Walijenga kibanda katika uwanja mkuu wa jiji hilo na kuweka broshua, magazeti, na vitabu. Wapita njia walikaribia kibanda hicho, na wengi walipendezwa kikweli. Wote waliopendezwa na kweli walialikwa kwenye mkutano wa funzo la Biblia. Kwa kweli mikutano hiyo haingefaa kuitwa mafunzo ya Biblia ya nyumbani kwa kuwa ilifanywa katika majumba yaliyokodiwa na watu 50 hivi walihudhuria. Mafunzo hayo yaliongozwa kama mikutano na yalikuwa na sehemu mbili. Kwanza, walijifunza kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kisha makala fulani kutoka gazeti Mnara wa Mlinzi ilizungumziwa. Mafunzo hayo yalifanywa mara tatu kwa juma na yalichukua saa tatu. Mikutano kama hiyo ya mafunzo ilifanywa katika sehemu mbalimbali za jiji hilo. Kila mara Pavel aliandika katika ripoti yake kwamba anaongoza mafunzo ya Biblia matatu. Alipoulizwa ni kwa nini anaongoza mafunzo machache hivyo hali wahubiri wengi walikuwa wakiongoza kati ya mafunzo 10 na 20, akina ndugu waligundua kwamba watu 50 hivi waliopendezwa walikuwa wakihudhuria kila funzo! Ilikuwa wazi kwamba Yehova alikuwa akibariki mpango huo kwa kuwa muda mfupi baadaye, wengi waliokuwa wakihudhuria mafunzo hayo walisema kwamba wangependa kuwaambia wengine habari njema. Baada ya mkutano mmoja wa funzo, Pavel alitangaza kwamba wote ambao wangependa kuwa wahubiri wabaki. Hakuna aliyeondoka, na hivyo wote wakawa wahubiri. Idadi ya vibanda vya vichapo iliongezeka jijini humo na punde si punde, vibanda vingi katika viwanja na bustani za jiji hilo vilijaa vichapo.
Wakati ulikuwa umewadia kushiriki katika njia nyingine ya kuhubiri, yaani, huduma ya nyumba kwa nyumba. Lakini wangewezaje kuhubiri ilhali karibu wahubiri wote hawakuwa wamewahi kushiriki katika aina hii ya utumishi? Wale ambao walitaka kujifunza kuhubiri nyumba kwa nyumba waliandamana na Dimov na mke wake katika huduma. Mara nyingi, kulikuwa na wahubiri wengi waliotaka kujifunza. Pindi nyingine, Pavel aliandamana na wahubiri kumi wakati mmoja! Inashangaza kwamba hilo halikuwaogopesha wenye nyumba, nao walifurahi kuzungumza na kikundi hicho. Wenye nyumba wengine hata walialika wote ndani ya nyumba zao.
Punde si punde, wahubiri hao wapya walikuwa na hamu ya kuhubiri maeneo mengine nje ya jiji la Ivanovo, kwa hiyo, safari za kwenda majiji mengine katika Wilaya ya Ivanovo zikapangwa. Wakiwa katika vikundi vya watu 50, waliingia katika gari-moshi na kuanza kuhubiri wakielekea jiji fulani, kisha wakajipanga wawili-wawili. Walipokuwa wakihubiri katika nyumba za ghorofa, waliwaalika watu kwenye mkutano ambao ungefanywa usiku huo. Katika mkutano huo, akina ndugu waliwaonyesha video za Mashahidi wa Yehova. Pia walitoa hotuba. Baada ya mkutano, wote waliohudhuria walielezwa kuhusu mpango wa kujifunza Biblia nyumbani, na wote waliotaka funzo waliwapa akina ndugu majina yao. Kwa sababu ya utendaji huo, karibu makutaniko matano yalianzishwa katika kila jiji katika Wilaya ya Ivanovo.
Mnamo 1994, katika Wilaya ya Ivanovo peke yake, kulikuwa na wahubiri 125, na watu 1,008 walihudhuria Ukumbusho. Mwaka huohuo, watu 62 kutoka Ivanovo walibatizwa katika kusanyiko la wilaya. Idadi ya waliobatizwa siku hiyo ilitosha kuanzisha kutaniko jipya! Sasa katika Wilaya ya Ivanovo, kuna wahubiri wa Ufalme 1,800 wenye bidii katika kazi ya Bwana.
KUKUTANA PAMOJA LICHA YA UPINZANI
Katika majiji mengi, haikuwa rahisi kupata kibali cha kutumia viwanja kwa ajili ya makusanyiko. Kwa mfano, katika jiji la Novosibirsk, wapinzani waliochochewa na viongozi wa dini walisimama mbele ya lango la uwanja ambamo kusanyiko lilikuwa likifanywa. Wapinzani hao walibeba bango moja lililosema: “Jihadhari na Mashahidi wa Yehova.” Hata hivyo, wapinzani hao hawakugundua kwamba herufi mbili za neno la kwanza zilikuwa zimefutika na hivyo ishara hiyo ilisema: “Watunze Mashahidi wa Yehova.”
Katika 1998, akina ndugu walipata upinzani walipojaribu kufanya kusanyiko la mzunguko huko Omsk. Saa chache tu kabla ya kusanyiko, wapinzani waliwachochea wenye mamlaka wamlazimishe msimamizi wa jumba fulani avunje mkataba wa kukodi jumba hilo aliokuwa amefanya na Mashahidi. Mamia ya watu waliowasili kwenye kusanyiko walisimama kando ya jumba hilo. Akihofia usalama wake na wa jumba hilo, msimamizi huyo aliwasihi akina ndugu wawaambie watu wasifanye ghasia. Akina ndugu walimtuliza na kumwambia kwamba hakuna mtu yeyote atakayezusha ghasia. Watu waliokuwa wamekuja kwenye kusanyiko walipigana picha ili kukumbuka tukio hilo kisha wakatawanyika. Msimamizi huyo akasadiki kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wenye amani. Majuma mawili baadaye, kusanyiko lilifanywa katika jumba lingine. Wapinzani walijua hilo kwa kuchelewa mno kwa hiyo hawangeweza kusimamisha kusanyiko hilo. Walifika mahali hapo programu ilipokuwa ikimalizika.
KUSANYIKO “CHINI YA MWANGAZA WA NYOTA”
Kuanzia Agosti 22 hadi 24, 2003, kusanyiko moja kati ya makusanyiko kadhaa katika lugha ya ishara lilipaswa kufanywa katika jiji la Stavropol’ huko Caucasia. Wajumbe waliwasili kutoka majiji 70 ya Urusi. Hata hivyo, karibu kusanyiko hilo lisimamishwe kwa sababu ya upinzani kutoka kwa wasimamizi wa jiji. Siku moja kabla ya kusanyiko hilo, msimamizi wa jumba lililokuwa limekodishwa alifuta mkataba wa kukodi jumba hilo. Lakini Ijumaa, Agosti 22, akina ndugu walifanya mapatano na wasimamizi wa kikundi cha wanasarakasi ili kutumia uwanja wao kwa ajili ya kusanyiko.
Programu ilianza saa 9:00 alasiri, lakini mara tu baada ya kipindi cha mapumziko, umeme wa jengo hilo ulikatwa ghafula. Wahudhuriaji walisubiri kwa utulivu katika viti vyao, na programu iliendelea saa moja baadaye umeme uliporudishwa. Programu hiyo ilimalizika saa 3:30 usiku.
Siku ya pili ya kusanyiko umeme ulikatwa saa 3:30 asubuhi. Punde si punde maji pia yakakatwa. Kusanyiko lingeendeleaje bila maji au umeme? Saa 4:50 asubuhi, Halmashauri ya Kusanyiko iliamua kufungua milango yote ya uwanja huo ili kuruhusu mwangaza wa jua kuingia. Wakitumia ubunifu, ndugu waliweka vioo vikubwa barabarani ili virudishe mwanga katika jumba na kwa msemaji. Ingawa wasikilizaji wangeweza kumwona msemaji, ilikuwa wazi kwamba mwangaza huo ulikuwa mwangavu sana hivi kwamba msemaji hangeona maandishi yake. Hivyo wakitumia vioo vingine, ndugu walielekeza mwangaza huo kwenye mpira mkubwa uliotengenezwa kwa vioo vidogo-vidogo ambao ulikuwa ukining’inia kwenye dari la uwanja huo lililokuwa na umbo la kuba. Uwanja huo ulijaa mwangaza wenye kumeta-meta, na hivyo msemaji na wasikilizaji wote wangeweza kukazia fikira programu. Kusanyiko hilo likawa kusanyiko la pekee kwa kuwa lilifanywa “chini ya mwangaza wa nyota.” Hivyo ndivyo wahudhuriaji wengi walivyoeleza mwangaza huo uliokuwa ukimeta-meta katika uwanja wenye giza.
Muda mfupi baadaye, meya na maofisa kadhaa walifika kwenye uwanja huo. Walishangaa kuona kwamba Mashahidi walikuwa wakiendelea na kusanyiko. Zaidi ya hilo, walivutiwa na mwenendo wa wale waliohudhuria kusanyiko. Hakuna yeyote aliyelalamika, na macho yao yalikaziwa kwenye jukwaa. Mkuu wa polisi, ambaye hapo awali aliwachukia Mashahidi aliguswa sana na yote aliyoona hivi kwamba alisema: “Moyoni mwangu mimi ninawaunga mkono kabisa, lakini ulimwengu tunamoishi hauwapendi.”
Maofisa hao waliondoka, na muda mfupi baadaye umeme ukarudishwa. Licha ya kwamba katika siku mbili za kwanza, programu ilimalizika usiku, wahudhuriaji walibaki kwenye viti vyao hadi wakati wa sala ya mwisho. Ingawa kulikuwa na upinzani, idadi ya wahudhuriaji iliongezeka kila siku. Kulikuwa na watu 494 Ijumaa, 535 Jumamosi, na 611 Jumapili! Ndugu aliyetoa sala ya kumalizia alimshukuru sana Yehova kwa kuwawezesha kuwa na kusanyiko hilo lenye kustaajabisha. Wahudhuriaji walitawanyika kwa furaha wakiwa wameazimia kabisa kumtumikia Baba yao wa mbinguni na kulisifu jina lake.
VIZIWI WANAMSIFU YEHOVA
Viziwi walikuwa kati ya wajumbe kutoka Muungano wa Sovieti waliohudhuria kusanyiko la pekee huko Poland mwaka wa 1990. Baada ya kutiwa moyo kiroho katika kusanyiko hilo, viziwi wachache waliohudhuria kusanyiko hilo wakawa viziwi wa kwanza kupanda mbegu ya Ufalme nchini Urusi na walijitahidi sana kuhubiri. Mapema katika mwaka wa 1992, ingeweza kusemwa kwamba sehemu hiyo ya shamba ilikuwa tayari kuvunwa na kwamba ‘mavuno yangekuwa mengi.’ (Mt. 9:37) Mnamo 1997, kutaniko la kwanza la lugha ya ishara lilianzishwa, na vikundi vingi vya lugha ya ishara vilianzishwa kotekote nchini humo. Katika 2002, mzunguko wa lugha ya ishara ulianzishwa. Huo ndio mzunguko ulio na eneo kubwa sana ulimwenguni pote. Mwaka wa 2006, kulikuwa na Shahidi 1 kiziwi kati ya kila viziwi 300, na kulikuwa na Shahidi 1 kati ya kila watu 1,000 waliosikia.
Tafsiri ya hali ya juu ya vichapo vyetu katika lugha ya ishara ilihitajika. Mnamo 1997, ofisi ya tawi ya Urusi ilianza kutafsiri katika lugha ya ishara. Yevdokia, mmoja wa dada viziwi katika kikundi cha watafsiri wa lugha ya ishara anasema hivi: “Ni pendeleo la pekee kwangu kutumikia Betheli na kutafsiri vichapo vyetu katika lugha ya ishara. Katika ulimwengu, watu hawawatumaini viziwi, nao huwaona kuwa watu wa hali ya chini. Lakini hali ni tofauti katika tengenezo la Mungu. Kwanza, naona kwamba Yehova mwenyewe anatutumaini sisi viziwi, ndiyo sababu ametupa kazi ya kutafsiri kweli katika lugha yetu. Pili, tunajihisi tukiwa huru miongoni mwa watu wa Yehova na tunafurahia sana kuwa sehemu ya familia hii kubwa.”
HABARI NJEMA KATIKA KILA LUGHA
Ingawa Kirusi ndiyo lugha iliyotumiwa sana katika biashara na shuleni katika Muungano wa Sovieti, lugha nyingine 150 hivi zilizungumzwa huko pia. Mnamo 1991, baada ya Muungano wa Sovieti kuvunjika na kuwa nchi 15, watu waliozungumza lugha hizo walipendezwa na kweli, hasa katika nchi zilizokuwa zimejipatia uhuru wakati huo. Kupatana na Ufunuo 14:6, jitihada zilifanywa ili kuwafikia watu wa “kila taifa na kabila na lugha na watu” katika eneo hilo kubwa. Kwa hiyo kukawa na uhitaji wa kutafsiri Mnara wa Mlinzi katika lugha nyingine 14 ili kuandaa chakula cha kiroho kwa ajili ya maelfu ya wanafunzi wapya katika eneo lililo chini ya ofisi ya tawi ya Urusi. Ili kusaidia kuenezwa kwa habari njema, ofisi ya tawi ya Urusi husimamia kutafsiriwa kwa vichapo katika lugha zaidi ya 40, na hivyo kuwezesha kweli ya Biblia kufikia mioyo haraka kuliko hapo awali.
Lugha nyingi kati ya hizo huzungumzwa katika Shirikisho la Urusi. Kwa mfano, mtu anaweza kusikia Kioseti katika majiji ya Beslan na Vladikavkaz; Kiburyati, lugha inayokaribiana na Kimongolia, kikizungumzwa katika eneo linalozunguka Ziwa Baikal; Kiyakuti, mchanganyiko wa Kituruki na Kialtai kikizungumzwa na wafugaji wa mbawala na wakazi wengine wanaoishi mashariki mwa Urusi; na lugha nyingine 30 hivi huko Caucasia. Kitatar ndiyo lugha inayozungumzwa na watu wengi baada ya Kirusi. Zaidi ya watu milioni tano huzungumza lugha hiyo, hasa katika eneo la Tatarstan.
Mara nyingi watu wanaozungumza Kitatar hupenda kusoma vichapo katika lugha hiyo, ingawa wachache husoma vichapo vya Kirusi. Wakati wa kampeni ya Habari za Ufalme Na. 35, mwanamke mmoja aliyeishi sehemu za vijijini alipokea trakti Habari za Ufalme na akaandika barua akiomba broshua Anataka katika Kitatar. Dada fulani alimtumia broshua hiyo pamoja na barua na mwanamke huyo alimjibu kwa kumwandikia barua yenye kurasa nane. Muda si muda alianza kujifunza Biblia akitumia vichapo vya Kitatar. Mwanamume mmoja aliyepokea broshua Je! Kweli Mungu Anatujali? katika Kitatar alisema kwamba broshua hiyo ilimsaidia kubadili maoni yake kuhusu ulimwengu. Matokeo hayo mazuri hayangewezekana bila vichapo vya Kitatar.
Mwanamke mmoja anayezungumza Kimari alipokea Habari za Ufalme Na. 35. Baada ya kuisoma, alitaka kujua mengi zaidi lakini hakukuwa na Mashahidi mahali alipoishi. Aliwasiliana na Mashahidi wa Yehova alipotembea jijini na akapokea kitabu Ujuzi na vichapo vingine katika Kirusi. Baada ya kusoma vichapo hivyo akiwa peke yake, alianza kuhubiri katika eneo lao, na punde si punde akaanza kujifunza na kikundi cha watu waliopendezwa. Alipata habari kwamba kutakuwa na kusanyiko la pekee Izhevsk, naye akafunga safari hadi huko akiwa na matumaini ya kubatizwa. Hata hivyo, akiwa kwenye kusanyiko hilo, aliambiwa kwamba wale wanaotaka kubatizwa lazima wajifunze Biblia kwa undani, na ndugu wakafanya mipango ya kumsaidia kiroho. Yote hayo yalitukia kwa sababu alisoma trakti ya Habari za Ufalme katika lugha yake.
Huko Vladikavkaz, kulikuwa na kutaniko moja tu la Kiosetia, na katika makusanyiko, hakuna hotuba iliyotafsiriwa katika lugha hiyo. Hata hivyo, mnamo 2002, kwa mara ya kwanza, hotuba zilitafsiriwa katika Kiosetia. Ndugu wanaozungumza Kiosetia walishangilia! Hata ndugu waliojua Kirusi walisema kwamba waliguswa sana moyo waliposikia ujumbe wa Biblia katika lugha yao ya kiasili. Jambo hilo lilichangia ukuzi wa kiroho katika kutaniko la Kiosetia na likavuta Waosetia wengi kwenye kweli. Katika mwaka wa 2006, mzunguko wa Kiosetia ulianzishwa, na kwa mara ya kwanza, makusanyiko ya mzunguko yakafanywa katika lugha hiyo.
Pindi moja, waangalizi wasafirio walipokuwa wakitembelea kikundi kimoja kilichokuwa mbali katika kijiji cha Aktash, katika jamhuri ya Altai, watu 30 hivi walikusanyika katika nyumba moja, ingawa kikundi hicho kilikuwa na wahubiri wachache tu. Kila mtu alisikiliza hotuba ya watu wote, lakini wakati wa hotuba ya utumishi ya mwangalizi wa wilaya, karibu nusu ya waliohudhuria waliondoka. Baada ya mkutano, mwangalizi wa wilaya aliwauliza ndugu wa hapo ni kwa nini wengi waliondoka. Mwanamke mmoja Mwaltai mzee alimjibu hivi katika Kirusi ambacho hakikuwa fasaha: “Unafanya kazi muhimu, lakini mimi sikuelewa chochote!” Wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko iliyofuata, hotuba zilitafsiriwa, na wote walifurahia programu yote.
Jiji la Voronezh lina wanafunzi wengi kutoka nchi za kigeni. Mnamo 2000, mtumishi wa huduma aliyezungumza Kichina alipanga kuwafundisha watu Kichina. Mashahidi wengi waliitikia uhitaji wa kujifunza lugha hiyo nao wakaanza kuwahubiria wanafunzi Wachina. Kichina ni lugha ngumu kujifunza lakini akina ndugu hawakukata tamaa. Februari 2004, funzo la kitabu la kwanza katika Kichina lilianzishwa katika jiji hilo. Mwezi wa Aprili mwaka huo, mwanafunzi wa kwanza Mchina alibatizwa, na baada ya miezi miwili, mwingine akabatizwa. Sasa watu wanaopendezwa huhudhuria kwa kawaida funzo hilo la kitabu, na mafunzo ya Biblia 15 hivi yanaongozwa katika Kichina. Kadiri habari njema zinavyozidi kuenezwa katika sehemu zote za shamba hili kubwa, ofisi ya tawi ya Urusi inaendelea kujibu maombi ya watu wanaotaka vichapo zaidi katika lugha nyingi.
MAPAINIA WAZOEZWA
Shule ya Utumishi wa Painia imefanywa nchini Urusi kwa miaka kadhaa. Kila darasa huwa na kati ya wanafunzi 20 hadi 30, wengi wao wakiwa mapainia ambao hawahitaji kusafiri mbali ili kuhudhuria shule hiyo. Hata hivyo, hali haikuwa hivyo shule hiyo ilipofanywa kwa mara ya kwanza nchini Urusi. Roman Skiba anasema hivi: “Nakumbuka vizuri Shule ya Utumishi wa Painia iliyofanywa Yekaterinburg mwaka wa 1996. Ilihudhuriwa na ndugu na dada zaidi ya 40. Ili kuhudhuria shule hiyo, wengi walilazimika kutoka mbali, wengine walisafiri karibu kilomita 1,000.”
Svetlana amekuwa painia wa kawaida katika eneo la lugha ya ishara tangu 1997. Mnamo Januari 2000, alihudhuria shule ya mapainia katika lugha ya ishara. Baada ya shule hiyo, Svetlana alisimulia jinsi ambavyo shule hiyo ilimsaidia kuboresha huduma yake na jinsi ambavyo Mkristo anapaswa kujiendesha katika familia na kutanikoni. Anasema hivi: “Upendo wangu kwa wengine uliongezeka. Pia nilitambua umuhimu wa kushirikiana na ndugu na dada, na sasa nakubali mashauri kwa urahisi. Nimeboresha sana mbinu zangu za kuongoza mafunzo ya Biblia, kwa kuwa sasa mimi hutumia mifano ninapofundisha.”
Alyona ni painia huko Khabarovsk, jiji lililoko Mashariki ya Mbali. Yeye huwasaidia viziwi kujifunza kweli. Ili awe na matokeo, Alyona alitaka kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia katika lugha ya ishara. Alikabili hali gani ngumu? Alyona anasema: “Shule ya mapainia katika lugha ya ishara iliyokuwa karibu ilikuwa Moscow, jiji lililo kilomita 9,000 kutoka Khabarovsk. Ili kuhudhuria shule hiyo, ilibidi nisafiri kwa gari-moshi kwa siku nane kwenda na siku nane kurudi.” Lakini hakujutia kufanya hivyo kamwe!
Mbali na shule zilizokusudiwa kuwasaidia wale waliokuwa wakihubiri katika lugha ya ishara, mamia ya Shule za Utumishi wa Painia zilifanywa Urusi, kuanzia 1996 hadi 2006. Mazoezi hayo yamechangia sana ukuzi wa kazi ya kuhubiri na pia ukuzi katika makutaniko. Marcin ambaye kwa sasa ni mwangalizi wa mzunguko anakumbuka hivi: “Mnamo 1995, niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee katika Kutaniko la Kuntsëvo huko Moscow. Nilipohudhuria hotuba ya watu wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi katika kutaniko hilo, ni kana kwamba kulikuwa na kusanyiko huko! Kulikuwa na watu 400 hivi katika jumba hilo. Wakati huo, kutaniko hilo lilikuwa na wahubiri 300. Karibu miaka kumi hivi baadaye, makutaniko mapya kumi yalikuwa yameanzishwa kutoka kwa kutaniko hilo moja!
“Nilipokuwa mwangalizi wa mzunguko mwaka wa 1996 na 1997, niliona ukuzi wa kustaajabisha katika mzunguko huo. Nilitembelea kutaniko fulani katika mji wa Volzhskiy ulioko Wilaya ya Volgograd. Niliporudi miezi sita baadaye, kutaniko hilo lilikuwa na wahubiri wapya 75. Lilikuwa kama kutaniko jipya kabisa! Sina maneno ya kueleza jinsi ambavyo wahubiri hao wapya walikuwa na bidii. Mikutano ya utumishi wa shambani iliyofanywa katika nyumba moja katika jengo lenye ghorofa nyingi ilihudhuriwa kwa kawaida na watu 80 hivi. Wengi wao walisimama nje kwenye ngazi kwa kuwa hakukuwa na nafasi ya kutosha.”
WACHANGA WANAMTUKUZA YEHOVA
Vijana wengi wanapendezwa na ujumbe wa Ufalme licha ya upinzani kutoka kwa wazazi wao. Dada mmoja mwenye umri wa miaka 20 anasimulia hivi: “Mnamo 1995, nilipokuwa na umri wa miaka tisa, Mashahidi wa Yehova waliwahubiria wazazi wangu ambao hawakupendezwa na kweli. Nilitaka kujua mengi kumhusu Mungu. Nilifurahi wakati rafiki yangu, ambaye tulikuwa katika darasa moja alipoanza kujifunza Biblia. Nilijiunga naye wakati wa funzo lake. Wazazi wangu walipogundua hilo, walinikataza kushirikiana na Mashahidi. Nyakati nyingine walinifungia nyumbani ili nisiende kujifunza. Hali hiyo iliendelea hadi nilipofikia umri wa miaka 18. Nilienda kusoma katika jiji lingine na nikakutana na Mashahidi huko. Nilifurahi sana kujifunza tena Biblia! Nilianza kumpenda Yehova kwa moyo wangu wote na nikabatizwa katika kusanyiko la wilaya mwaka wa 2005. Mara tu baada ya kubatizwa, nikawa painia msaidizi. Sasa wazazi wangu hawapingi kweli ambazo nimezipenda tangu utotoni.”
Dada mwingine anakumbuka hivi: “Mnamo 1997 nilipokuwa na umri wa miaka 15, Mashahidi walinipa gazeti Amkeni! Nilipenda jina la gazeti hilo na yaliyokuwamo, na nilitaka kuwa nikilipokea kwa kawaida. Baba yangu alipogundua kwamba nilikuwa nikisoma gazeti hilo, aliwakataza Mashahidi kuja nyumbani kwetu. Muda fulani baadaye, binamu yangu alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, na mapema mwaka wa 2002, nilianza kuhudhuria mikutano pamoja naye kwenye Jumba la Ufalme. Nikiwa huko, nilisikia kwamba Mashahidi wa Yehova hutumika wakiwa wamishonari, na hilo likanichochea kutaka kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Mungu. Lakini binamu yangu alinieleza kwamba kwanza lazima niache kuvuta sigara, nipatanishe maisha yangu na mapenzi ya Mungu, na kuwa mmoja wa watumishi wake. Nilifuata shauri lake, na miezi sita baadaye nikabatizwa na mara moja nikaanza upainia msaidizi. Ninafurahi kwamba nimepata kusudi la kweli maishani.”
KUTAFUTA “VITU VYENYE KUTAMANIKA” HUKO SAKHA
Mzunguko mmoja unatia ndani Wilaya ya Amur na eneo lote la Sakha. Wakati wa mwaka wa utumishi wa 2005, kwa mara ya kwanza, kusanyiko la mzunguko na la pekee lilifanywa Yakutsk, jiji kuu la Sakha. Ilipendeza hasa kuona wenyeji wa asili wakihudhuria makusanyiko hayo.
Ili akina ndugu wafaidike, mzunguko huo uligawanywa katika sehemu tano, kila sehemu ikiwa na kusanyiko lake. Kwa waangalizi wanaosafiri, kusafiri kutoka kusanyiko moja hadi lingine kulichukua saa 24 kwa gari-moshi, kisha saa 15 kwa gari na saa 3 kwa ndege.
Eneo hilo lina baridi sana inayofikia nyuzi zaidi ya 50 Selsiasi chini ya sufuri wakati wa majira ya baridi kali. Licha ya hali hiyo, ndugu huhubiri kwenye majengo yenye ghorofa nyingi na pia nyumba kwa nyumba.
Vikundi viwili vya wahubiri vilianzishwa mapema 2005. Kikundi kimoja kiko katika kijiji cha Khayyr kilichoko kilomita 80 kutoka pwani ya Bahari ya Laptev iliyo juu ya Mzingo wa Aktiki. Kijiji hicho kina wakazi 500, wanne kati yao ni Mashahidi. Mwaka wa 2004, Ukumbusho ulifanywa katika kijiji hiki na watu 76 walihudhuria. Ili kutembelea kikundi katika kijiji hiki, mwangalizi wa mzunguko lazima kwanza asafiri kilomita 900 hivi kwa ndege, kisha kilomita 450 kwa gari kwenye barabara zilizofunikwa kwa theluji.
Kikundi kingine kilianzishwa katika kijiji cha mbali sana cha Ust’-Nera kilichoko kilomita 100 kutoka kijiji cha Oymyakon. Nyakati nyingine majira ya baridi kali hufikia nyuzi 60 Selsiasi chini ya sufuri. Ili kuhudhuria kusanyiko la mzunguko mwaka jana, wahubiri kutoka kikundi hiki walisafiri wakitumia magari mawili. Iliwabidi kusafiri umbali wa kilomita 4,000 hivi kwenda na kurudi kupita eneo lisilo na watu lenye baridi ya nyuzi 50 Selsiasi chini ya sufuri.
Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisimulia jambo lililoonwa lenye kupendeza ambalo lilitukia akiwa mita 4,000 angani. “Wakati wa kampeni ya kutoa broshua Endeleeni Kukesha! makusanyiko kadhaa yalifanywa katika mzunguko wetu. Mimi na mwangalizi wa wilaya tulikuwa tukisafiri kwa ndege kuelekea kusanyiko lililofuata. Kwa kuwa tulikuwa tumegawa broshua zote za Endeleeni Kukesha! tulimpa mhudumu wa ndege broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Alituambia kwamba tayari alikuwa amepokea vichapo kadhaa vya Biblia na tulishangaa alipotuonyesha broshua Endeleeni Kukesha! Tulifurahi kuona kwamba ndugu zetu walikuwa wakihubiri kwa bidii! Tulipokuwa tukizungumza, rubani msaidizi alipita. Alipendezwa na mazungumzo yetu hivyo akajiunga nasi. Tulizungumza mpaka karibu mwisho wa safari. Rubani msaidizi alifurahia sana mazungumzo hayo na akachukua magazeti kadhaa kwa ajili ya wahudumu waliokuwa kwenye chumba cha rubani.”
HABARI NJEMA ZAHUBIRIWA HUKO SAKHALIN
Mashahidi waliwasili kwa mara ya kwanza kwenye kisiwa cha Sakhalin mwishoni mwa miaka ya 1970. Kisiwa hicho kiko juu ya kisiwa cha Hokkaido, kaskazini kabisa mwa Japani. Ndugu kutoka Vladivostok ambao walikuwa wakisimamia kazi ya kuhubiri katika kisiwa hicho walimtia moyo Sergey Sagin apanue huduma yake kwa kuhamia katika kisiwa hicho ili kuwahubiria wakaaji wake. Alipokuwa akifanya kazi bandarini, Sergey alijaribu kuanzisha mazungumzo ya Biblia na wafanyakazi wengine. Muda si muda alikuwa akiongoza mafunzo kadhaa ya Biblia. Ingawa baadaye ilimbidi Sergey aondoke, mbegu za kweli zilizaa matunda.
Makusanyiko ya wilaya yaliyofanywa Poland mwaka wa 1989 na 1990 yaliwachochea Mashahidi wengi wa Urusi wapanue huduma yao na kuhamia maeneo yaliyokuwa na uhitaji mkubwa. Mnamo 1990, Sergey na Galina Averin walihama kutoka Khabarovsk, katika Mashariki ya Mbali, hadi Korsakov, jiji la bandarini huko Sakhalin. Miezi michache baadaye, mapainia wawili na wahubiri kadhaa walihamia Yuzhno-Sakhalinsk ambako kulikuwa na Shahidi mmoja tu.
Pavel Sivulsky, mmoja wa mapainia hao, sasa anatumika Betheli. Yeye ni mwana wa Pavel Sivulsky aliyetajwa awali katika simulizi hili. Anakumbuka hivi: “Tulipofika Yuzhno-Sakhalinsk, mimi na ndugu mwingine tuliishi katika hoteli fulani, kwa kuwa hatungeweza kupata nyumba mara moja. Tulianza kuhubiri nyumba kwa nyumba katika eneo lililokuwa karibu na hoteli hiyo na tulipokuwa tukiongea na watu tuliwauliza ikiwa wanajua yeyote aliye na nyumba za kupangisha. Tulikutana na watu ambao waliuliza mahali ambapo wangeenda ili kuendeleza mazungumzo hayo ya Biblia, lakini tuliwaambia kwamba tunaishi hotelini na mara tu tutakapopata nyumba, tutawaalika. Tulisali kwa Yehova kwa bidii tukimwomba atusaidie kupata kazi na nyumba. Yehova alijibu sala zetu. Muda si muda, tulipata kazi na nyumba. Mwanamke fulani alitualika tuishi kwake. Hakututoza kodi na hata alitupikia chakula, jambo ambalo lilitusaidia kutumia wakati mwingi katika huduma. Yehova alituonyesha kwamba alikuwa pamoja nasi. Punde si punde tulikuwa tukiongoza mafunzo mengi ya Biblia na kupanga vikundi vya funzo la kitabu. Miezi miwili baadaye, tulipata nyumba ya kupangisha na tukafanya mikutano yetu humo.”
Kutaniko lilipoendelea kukua, wahubiri wapya walianza kupainia. Walionyesha roho ya upainia kwa kuhamia sehemu nyingine za kisiwa hicho ili kueneza kweli kwa wakaaji wake. Yehova alibariki sana bidii ya wahubiri wa kutaniko hilo lililokuwa likikua haraka sana, na miaka mitatu baadaye, katika 1993, kutaniko hilo lilitokeza makutaniko mapya nane.
Baada ya muda, wahubiri wengi walihama kisiwa hicho kwa sababu ya hali ngumu ya kiuchumi na ili pia kupanua huduma yao. Kama hapo awali, jitihada hizo zilileta ukuzi. Sasa kuna Jumba la Ufalme maridadi katikati ya mji wa Yuzhno-Sakhalinsk, na kisiwa hicho kina mzunguko mmoja wenye makutaniko tisa na vikundi vinne.
MLANGO WAFUNGULIWA LICHA YA WAPINZANI WENGI
Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alisema: “Nimefunguliwa mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji, lakini kuna wapinzani wengi.” (1 Kor. 16:9) Miaka 2,000 baadaye, idadi ya wapinzani haijapungua. Kuanzia 1995 hadi 1998, ofisi ya mwendesha-mashtaka huko Moscow ilifungua mashtaka ya uhalifu dhidi ya Mashahidi. Mashahidi wa Yehova walishtakiwa kwamba walikuwa wakiwachochea watu wachukie dini, walivunja familia, walijihusisha katika utendaji uliopinga Serikali, na waliingilia haki za raia wengine. Waliposhindwa kuthibitisha mashtaka hayo, kesi nyingine ya madai ilifunguliwa dhidi ya Mashahidi mnamo 1998, ikitegemea mashtaka yaleyale yasiyo na msingi.
Mwaka mmoja hivi baadaye, baada ya kutambua kwamba Mashahidi wa Yehova na vichapo vyao haviwachochei watu kuchukia dini, kuvunja familia, au kuingilia haki za wengine, wizara ya haki ilisajili upya Kitovu cha Uendeshaji wa Shughuli za Kidini cha Mashahidi wa Yehova nchini Urusi. Hata hivyo, ofisi ya mwendesha-mashtaka ilifungua mashtaka yaleyale tena dhidi yao!
Maprofesa fulani wa masuala ya kidini wanatambua kwamba Mashahidi wa Yehova wanatumia Biblia peke yake kuwa msingi wa mafundisho yao. Dakt. N. S. Gordienko, ambaye ni profesa wa masuala ya kidini katika Chuo Kikuu cha Ufundishaji cha Herzen huko St. Petersburg alisema hivi: “Wataalamu wanapowashutumu Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya mafundisho yao, hawatambui kwamba kwa kweli wanaishutumu Biblia.”
Ingawa hivyo, Mahakama ya Rufaa ya Moscow ilifutilia mbali kuandikishwa kisheria kwa Mashahidi wa Yehova jijini Moscow. Hata hivyo, hilo halikuwazuia ndugu zetu kutimiza amri ya Biblia ya kuwaambia wengine habari njema. Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba watu wa Moscow wanapaswa kujiamulia wenyewe dini watakayofuata. Kuwazuia kufanya uamuzi huo ambao ni haki yao ni kuingilia uhuru wa kila mkaaji wa Moscow. Kwa hiyo, Mashahidi jijini Moscow wataendelea kutimiza amri ya Yesu Kristo ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kwa sasa, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu inachunguza uamuzi wa Mahakama ya Rufaa ya Moscow.
Mnamo Septemba 1998, wakati kesi ya kufutilia mbali shirika la Mashahidi wa Yehova jijini Moscow ilipoanza kusikilizwa, kulikuwa na makutaniko 43 ya Mashahidi wa Yehova katika jiji hilo. Miaka minane baadaye kulikuwa na makutaniko 93! Yehova amewaahidi watu wake hivi: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa.” (Isa. 54:17) Mwaka wa 2007, Mashahidi wa Yehova walifanya kusanyiko la wilaya katika Uwanja wa Michezo wa Luzhniki, Moscow ambao wakati mmoja ulitumiwa kwa michezo ya Olimpiki. Kusanyiko hilo lilihudhuriwa na watu 29,040, na 655 wakabatizwa.
JINA LA MUNGU NI KUU NCHINI URUSI
Kama ilivyorekodiwa kwenye Malaki 1:11, Yehova Mungu alisema hivi: “Tangu kuchomoza kwa jua mpaka kutua kwake jina langu litakuwa kuu kati ya mataifa.” Kila mara jua linapochomoza, kuna uwezekano wa kupata mtu mwenye mfano wa kondoo katika nchi hiyo kubwa. Katika mwaka wa utumishi uliopita peke yake, zaidi ya watu 7,000 walibatizwa nchini Urusi. Uthibitisho huo usioweza kukanushwa unaonyesha kwamba “Maliki wa maliki,” kama Yesu Kristo anavyoitwa katika Biblia ya Kirusi, yuko pamoja na raia zake wanapoendelea na kazi ya kuhubiri.—Mt. 24:14; Ufu. 19:16.
Mtume Petro alisema kwamba “siku ya Yehova itakuja kama mwizi.” (2 Pet. 3:10) Kwa hiyo, watumishi wa Yehova nchini Urusi wameazimia kutumia wakati uliobaki kuwatafuta wale wenye mwelekeo unaofaa kutoka katika kila taifa, lugha, kabila, na watu.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Waaltai—Watu Tuliopata Kuwapenda” katika Amkeni! la Juni 22, 1999.
[Blabu katika ukurasa wa 110]
“Ikiwa rekodi zingeonyesha jambo lolote dhidi yenu, hata ikiwa ingepatikana kwamba mlimuumiza mtu mmoja tu, tungewapiga ninyi nyote risasi”
[Blabu katika ukurasa wa 128]
“Tukikuacha huru, raia wengi wa Sovieti watajiunga nawe. Ndiyo sababu tunaona wewe ni mtu hatari sana kwa Nchi yetu”
[Blabu katika ukurasa wa 219]
“Watu wenu ni kama ndege; wao huteremka na kunyakua maboksi ya vichapo na kuondoka”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 69]
Siberia Ni Eneo la Aina Gani?
Unaposikia kuhusu Siberia unapata wazo gani? Je, unafikiria eneo lenye baridi kali lisilo na watu? Je, unawazia kuwa ni nchi ambako watu waliopinga serikali ya Sovieti walipelekwa uhamishoni? Ukifikiri hivyo hutakuwa umekosea, lakini kuna mambo mengi zaidi katika eneo hilo.
Siberia ina eneo kubwa sana, ni kubwa kuliko Kanada, ambayo ndiyo nchi ya pili kwa ukubwa duniani. Leo Siberia ina ukubwa wa kilomita milioni 13 za mraba, kuanzia Milima ya Ural kuelekea mashariki mpaka Bahari ya Pasifiki, na kutoka Mongolia na China upande wa kaskazini mpaka Bahari ya Aktiki. Nchi hiyo ina mali nyingi za asili kama vile mbao, mafuta, na gesi. Huko Siberia kuna milima, nyanda, vinamasi, maziwa, na mito mikubwa.
Kwa karne moja na nusu hivi, Siberia ilikuwa eneo ambalo watu walifungwa, walifanyishwa kazi ngumu, na kupelekwa uhamishoni. Katika miaka ya 1930 na 1940, Joseph Stalin aliwahukumu mamilioni ya watu wapelekwe kwenye kambi za kazi ngumu. Mnamo 1949 na 1951, Mashahidi wa Yehova 9,000 hivi kutoka Moldova, Ukrainia, na jamhuri za Baltiki walipelekwa uhamishoni Siberia.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 72, 73]
Maelezo Mafupi
Nchi
Urusi ndiyo nchi kubwa zaidi ulimwenguni, ina ukubwa wa kilomita 7,700 kutoka mashariki mpaka magharibi na kilomita 3,000 kutoka kaskazini mpaka kusini. Kwa ujumla ina ukubwa wa kilomita 17,075,400 za mraba. Inapitia kanda 11 za wakati, kwa hiyo inafikia karibu nusu ya Kizio cha Kaskazini. Nchi hiyo ina mlima mrefu zaidi barani Ulaya na mto mrefu zaidi barani humo. Pia ina ziwa lenye kina kirefu zaidi ulimwenguni.
Watu
Asilimia 80 ya wakaaji ni Warusi. Lakini kuna makabila mengine zaidi ya 70 nchini Urusi. Makabila fulani yana maelfu ya watu na mengine yana watu zaidi ya milioni moja.
Lugha
Lugha kuu ni Kirusi na karibu kila mkaaji anazungumza lugha hiyo. Pia, kuna lugha zaidi ya 100 na baadhi ya lugha hizo ni lugha ya asili ya watu karibu milioni moja.
Kazi
Urusi ni moja ya nchi zilizo na mafuta na gesi kwa wingi zaidi ulimwenguni. Shughuli nyingine kubwa ni upandaji miti, uchimbaji, na utengenezaji wa vitu mbalimbali.
Chakula
Vyakula vizuri vinatengenezwa kwa kutumia nyama, samaki, kabichi (choux), au maziwa yaliyoganda na vyakula hivyo vinaliwa pamoja na mkate mweusi wa rai, viazi, na nafaka fulani. Kwa kawaida, chakula cha Warusi kina mafuta na wanga kwa wingi ili kuwapatia nguvu zinazohitajika wakati wa majira marefu ya baridi. Chakula cha kawaida kinaweza kutia ndani pelmeni (maandazi yaliyotiwa nyama) inayowekwa ndani ya supu au krimu iliyochacha au piroshki (vitu vidogo vilivyookwa) pamoja na kabichi, nyama, jibini, au viazi. Supu zinazopendwa ni kama vile borscht, viazi-sukari, na shchi, au supu ya kabichi.
Hali ya Hewa
Joto ni jingi wakati wa majira ya kiangazi, na katika majira ya baridi kali, baridi ni kali kwelikweli na hakuna mwangaza mwingi. Majira ya kuchipua na majira ya kupukutika kwa majani hupita haraka, kwa hiyo sehemu kubwa ya wakati kunakuwa na kiangazi na majira ya baridi kali.
(Ramani za Urusi kwenye ukurasa wa 116 na 167)
[Picha]
Kremlin
Mlima El’brus, Kabardino-Balkaria
Dubu wa kahawia, Rasi ya Kamchatka
[Picha katika ukurasa wa 92, 93]
Vita vya Kugeuza Mioyo na Akili
Serikali ya Sovieti haikutaka kuwaangamiza Mashahidi. Kusudi lake lilikuwa kuwageuza kwa kuwasadikisha au kuwalazimisha wafuate maoni ya Kisovieti. Ili kufikia lengo hilo, serikali iliajiri shirika la KGB—shirika la upelelezi na usalama wa ndani. Zifuatazo ni njia mbalimbali ambazo KGB walitumia.
Upekuzi: Mashahidi wa Yehova walipekuliwa nyumbani mwao, upekuzi huo ukifanywa hata usiku. Familia fulani zililazimika kuhama kwa sababu ya kupekuliwa mara nyingi.
Kuchunguzwa: Hilo lilitia ndani vifaa vya kunasia mazungumzo ya simu au mazungumzo katika nyumba za akina ndugu, na barua zilichunguzwa kabla hazijawafikia.
Kutozwa faini na kukatiza mikutano: Kotekote nchini, wenye mamlaka walitafuta mahali ambapo akina ndugu walikutana. Wote waliohudhuria wangetozwa faini. Mara nyingi faini hizo zilikuwa pesa zinazolingana kwa wastani na nusu ya mshahara katika mwezi mmoja.
Kuhongwa na kutishwa: Mashahidi fulani waliahidiwa na shirika la KGB kwamba wangepewa magari na nyumba katikati ya jiji la Moscow ikiwa wangeshirikiana nao. Mara nyingi, ndugu waliambiwa kwamba wangehukumiwa miaka mingi katika kambi za kazi ngumu ikiwa hawangeshirikiana na shirika hilo.
Propaganda: Filamu, televisheni, na magazeti yaliwaonyesha Mashahidi kuwa watu hatari sana katika jamii. Hotuba zilitolewa gerezani na katika kambi zikiwalaumu akina ndugu kwa kutumia Biblia kuficha nia yao ya kisiasa. Propaganda ilitokeza ubaguzi; walimu waliwapa watoto wa Mashahidi waliokuwa shuleni alama za chini, na waajiri waliwanyima akina ndugu huduma fulani au mapumziko waliyostahili.
Wapelelezi: Watu fulani katika shirika la KGB walijifanya wanapendezwa na ujumbe wa Ufalme wakajifunza na kubatizwa. Wengine walijitahidi hadi wakapewa madaraka fulani katika tengenezo. Kusudi lao lilikuwa kusimamisha kazi ya kuhubiri kwa kutokeza mashaka na migawanyiko kati ya Mashahidi.
Uhamisho: Mashahidi walihamishiwa katika maeneo ya mbali sana ya nchi. Huko akina ndugu walihitaji kufanya kazi ngumu kwa saa 12 kila siku ili wapate riziki. Katika majira ya baridi kali, walipambana na baridi kali sana, na katika majira ya kiangazi, mbu na mainzi yaliwasumbua.
Kuchukua mali zao na kuwatenganisha: Mali, nyumba na vitu vingine vilichukuliwa. Mara nyingine watoto walitenganishwa na wazazi wao ambao ni Mashahidi.
Kudhihakiwa na kupigwa: Mashahidi wengi, kutia ndani wanawake, walitukanwa na kudhihakiwa. Wengine walipigwa kwa ukatili sana.
Kufungwa gerezani: Lengo lilikuwa kuwafanya Mashahidi wakane imani yao au kuwatenga na ndugu zao.
Kambi za kazi ngumu: Mashahidi walichoka sana kutokana na kazi ngumu kwenye kambi hizo. Mara nyingi, walihitaji kuchimbua visiki vya miti mikubwa sana. Pia, ndugu walifanya kazi ya kuchimbua makaa ya mawe, walijenga barabara, na reli. Wafanyakazi walitenganishwa na familia zao na kuishi kwenye mabanda.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 96, 97]
Nilihukumiwa Kifo Mara Mbili
PYOTR KRIVOKULSKY
ALIZALIWA 1922
ALIBATIZWA 1956
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alisoma kwenye chuo cha kidini kabla ya kujifunza kweli. Alifungwa gerezani na kwenye kambi za kazi ngumu kwa miaka 22, alikufa mwaka wa 1998.
MNAMO 1940, Mashahidi wa Poland walianza kuhubiri mahali nilipoishi nchini Ukrainia. Nilitembelewa na ndugu mtiwa-mafuta anayeitwa Korney. Tulizungumza usiku wote, na nilisadikishwa kwamba kile alichoniambia ni ukweli kumhusu Mungu.
Mnamo 1942 jeshi la Wajerumani lilikaribia, na majeshi ya Wasovieti yakatoka eneo nililokuwa nikiishi. Huo ulikuwa wakati wa mvurugo. Wazalendo wa Ukrainia walisisitiza kwamba nijiunge nao katika vita dhidi ya Wajerumani na Wasovieti. Nilipokataa, walinipiga mpaka nikapoteza fahamu kisha wakanitupa barabarani. Usiku huohuo, walikuja kunichukua na wakanipeleka mahali ambapo watu wengi huuawa. Hapo waliniuliza tena ikiwa ningetumikia watu wa Ukrainia. Niliwaambia kwa mkazo na kwa sauti kubwa, “Nitamtumikia Yehova peke yake!” Kisha wakanihukumu kifo. Mmoja wa askari hao alipotoa amri ya kunipiga risasi, mwingine alichukua bunduki na kusema kwa sauti: “Msimpige risasi! Bado tunaweza kumtumia.” Mtu mmoja alianza kunipiga kwa sababu ya hasira. Aliniahidi kwamba yeye mwenyewe angeniua baada ya juma moja, lakini baada ya siku chache, yeye ndiye aliyeuawa.
Mnamo Machi 1944, jeshi la Wasovieti likarudi kwenye eneo letu, na askari wakawachukua wanaume wote, kutia ndani mimi. Wakati huu, ni jeshi la Wasovieti lililohitaji wapiganaji. Katika mahali pao pa kukutana, nilimkuta Korney, ndugu aliyenifundisha kweli. Kulikuwa na Mashahidi wengine 70. Tulisimama mbali na wengine na kutiana moyo. Askari mmoja alikuja kutuuliza ni kwa nini tumesimama mbali na watu wengine. Korney alimweleza kwamba sisi ni Wakristo na hatuwezi kubeba silaha. Mara moja, alichukuliwa na tukaambiwa kwamba atapigwa risasi. Hatukumwona tena. Walianza kututisha wakisema kwamba sisi sote tutapigwa risasi kama yeye, kisha mmoja baada ya mwingine tuliulizwa ikiwa tutajiunga na jeshi lao. Nilipokataa, askari watatu na ofisa mmoja walinipeleka katika pori. Kamanda alisoma hukumu katika kitabu cha kijeshi: “Kwa kukataa kuvaa mavazi ya kijeshi na kubeba silaha, utauawa kwa kupigwa risasi.” Nilisali kwa Yehova kwa bidii halafu nikaanza kujiuliza ikiwa angekubali utumishi wangu kwake kwani sikuwa nimepata nafasi ya kubatizwa. Mara moja, nikasikia amri, “Muue adui!” Lakini askari walipiga risasi hewani. Kisha ofisa akaanza kunipiga. Nilihukumiwa miaka kumi gerezani na mwishowe nilipelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu katika Wilaya ya Gorki, katikati ya Urusi.
Niliachiliwa mnamo 1956 na baadaye nikamwoa Regina, Shahidi mwaminifu. Baada ya kuwa pamoja kwa miezi sita tu, nilikamatwa bila kutazamia na kuhukumiwa miaka kumi gerezani.
Baada ya kuachiliwa, mkuu mmoja aliniambia, “Hakuna mahali kwa ajili yako katika nchi ya Sovieti.” Alikuwa amekosea. Ni vizuri kama nini kujua kwamba dunia ni ya Yehova na anampa yeyote anayependa aishi juu yake milele!—Zab. 37:18.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 104, 105]
“Wasichana, Kuna Shahidi wa Yehova Yeyote Miongoni Mwenu?”
YEVGENIA RYBAK
ALIZALIWA 1928
ALIBATIZWA 1946
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alizaliwa Ukrainia, alipelekwa Ujerumani kwa nguvu ambako alijifunza kweli. Anaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu nchini Urusi.
JUMAPILI moja kupita dirisha la chumba changu nilisikia watu wakiimba wimbo kwa sauti zilizopangwa vizuri. Waimbaji hao walikuwa Mashahidi wa Yehova. Baada ya muda mfupi nilianza kuhudhuria mikutano yao. Sikuweza kuelewa kwa nini Wajerumani walikuwa wakiwatesa Wajerumani wenzao kwa sababu ya imani yao. Waukrainia wenzangu ambao tulichukuliwa kwa nguvu pamoja walianza kunichukia kwa sababu nilikuwa ninashirikiana na Wajerumani. Siku moja, mmoja wao alinifokea kwa ukali na kunipiga usoni. Rafiki zangu wa zamani wakaanza kunicheka.
Baada ya kuachiliwa mnamo 1945, nilirudi Ukrainia. Babu yangu akaniambia hivi: “Mama yako amekuwa kichaa. Ametupa sanamu zake na sasa ana Mungu mwingine.” Babu alipotoka, Mama alitoa Biblia na kusoma sehemu inayosema Mungu anachukia sanamu. Kisha akaniambia kwamba alikuwa anahudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Nilimkumbatia kwa furaha huku machozi yakinilenga-lenga, nikamwambia kwa sauti ya chini, “Mama mpendwa, mimi pia ni Shahidi wa Yehova!” Sote tulilia kwa furaha.
Mama alikuwa na bidii sana shambani. Kwa kuwa ndugu wote walikuwa wamefungwa kwenye kambi, aliwekwa kuwa mtumishi wa kikundi. Mimi pia nilichochewa sana na bidii yake.
Mnamo 1950, nilikamatwa kwa ajili ya shughuli za kidini, na mahakama ilinihukumu kifungo cha miaka kumi kwenye kambi. Tulipelekwa kwenye mji wa Usol’ye-Sibirskoye, huko Siberia tukiwa dada watano. Kuanzia mwezi wa Aprili 1951, tulikuwa tunafanya kazi ya kujenga reli. Tulibeba mabegani vyuma vizito vya kuunganishia reli. Kila chuma kilibebwa na watu wawili. Tuliondoa na kuweka vyuma vipya vya reli vyenye urefu wa mita 10 na uzito wa kilo 320 kila kimoja. Ilikuwa kazi yenye kuchosha sana. Siku moja tulipokuwa tukirudi nyumbani tukiwa tumechoka kutokana na kazi ngumu, gari-moshi lililokuwa limejaa wafungwa lilisimama mbele yetu. Mwanaume mmoja aliyekuwa anachungulia dirishani alituuliza, “Wasichana, kuna Shahidi wa Yehova yeyote miongoni mwenu?” Uchovu wote ulitoweka. Tulisema kwa sauti ya juu, “Tuko akina dada watano hapa!” Wafungwa hao walikuwa ndugu na dada zetu wapendwa waliokuwa wanasafirishwa kutoka Ukrainia. Gari-moshi liliposimama, walituambia kwa shauku mambo yalivyotokea na jinsi walivyokamatwa na kusafirishwa. Kisha watoto wakatuimbia mashairi ambayo yalitungwa na akina ndugu. Hakuna askari hata mmoja ambaye alitusumbua, na tuliweza kushirikiana na kutiana moyo.
Kutoka Usol’ye-Sibirskoye, tulisafirishwa hadi kwenye kambi kubwa iliyokuwa karibu na jiji la Angarsk. Kulikuwa na akina dada 22 kambini. Walikuwa wamepanga kila kitu, kutia ndani maeneo ya kuhubiri. Hilo lilitusaidia kuimarisha uhusiano wetu na Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 108, 109]
Nilifungiwa Kwenye “Kona ya Tano” Mara Kadhaa
NIKOLAI KALIBABA
ALIZALIWA 1935
ALIBATIZWA 1957
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mnamo 1949 alipelekwa uhamishoni katika Wilaya ya Kurgan, Siberia.
TULIONA ni kana kwamba kila Shahidi katika Muungano wa Sovieti alikuwa akichunguzwa. Maisha hayakuwa rahisi, lakini Yehova alitupa hekima. Mnamo Aprili 1959, nilikamatwa kwa sababu ya shughuli za kidini. Ili nisiwahatarishe ndugu wengine, niliamua kukataa kila kitu. Kachero alinionyesha picha za akina ndugu na akaniomba niwataje majina. Nilimwambia kwamba sikumtambua yeyote. Kisha akanionyesha picha ya ndugu yangu wa kimwili na kuniuliza, “Huyu ni ndugu yako?” Nikamjibu: “Sijui kama ni yeye au siye. Sisemi kitu.” Baada ya hapo, kachero akanionyesha picha yangu na akaniuliza, “Je, huyu ni wewe?” Nikasema, “Huyu mtu anafanana na mimi, lakini siwezi kukueleza kama ni mimi au la.”
Nilifungwa gerezani kwa zaidi ya miezi miwili. Kila asubuhi, niliamka na kumshukuru Yehova kwa upendo wake wenye fadhili. Kisha nilifikiria andiko fulani na baada ya hapo nikalifafanua. Halafu nikaimba wimbo wa Ufalme kimyakimya kwani hatukuruhusiwa kuimba kwa sauti. Mwishowe nilifikiria kichwa fulani cha Biblia.
Katika kambi niliyotumwa tayari kulikuwa na Mashahidi wengi. Hali gerezani zilikuwa ngumu sana na hatukuruhusiwa kuzungumza. Mara nyingi akina ndugu walifugwa kwenye seli zilizotengwa ambazo pia ziliitwa kona ya tano. Nilifungwa kwenye kona ya tano mara kadhaa. Huko wafungwa walipewa mkate wa gramu 200 kwa siku. Nililala kwenye ubao uliofunikwa na mabati. Vioo vya dirisha vilikuwa vimevunjika, na kulikuwa na mbu wengi sana. Nilitumia viatu vyangu kama mto.
Kwa kawaida, kila ndugu alitafuta mahali pake pa kuficha vichapo. Niliamua kuficha vichapo kwenye ufagio niliotumia kufagilia sakafu. Wakati wa upekuzi, msimamizi hata hakufikiria kutafuta ndani ya ufagio, ingawa alipekua kila kitu kutia ndani vitu vidogo. Pia tulificha vichapo ndani ya ukuta. Nilijifunza kutegemea tengenezo la Yehova. Yehova anaona na anajua kila kitu na anamsaidia kila mmoja kati ya watumishi wake waaminifu. Yehova amenisaidia nyakati zote.
Hata kabla ya familia yetu kuhamishwa mnamo 1949, baba yangu alisema kwamba Yehova atafanya mipango ili watu walio maeneo ya mbali huko Siberia wasikie kweli. Sisi tulijiuliza, ‘Hilo linawezekana kweli?’ Ilitokea kwamba wenye mamlaka wenyewe waliwasaidia maelfu ya watu wanyoofu huko Siberia wajue kweli.
Hali katika Muungano wa Sovieti zilipobadilika, akina ndugu walifurahia kwenda Poland kwa ajili ya kusanyiko la kimataifa mnamo 1989. Hicho kilikuwa ni kipindi kizuri ajabu. Baada ya sala ya mwisho, tuliendelea kusimama tukipiga makofi kwa muda mrefu. Tulihisi vizuri sana! Kwa miaka mingi nilikuwa nimezoea matatizo na shida mbalimbali, lakini tulilia mara chache sana. Hata hivyo, tulipoachana na ndugu zetu wapendwa huko Poland, machozi yalitiririka kwa wingi, na hakuna mtu ambaye angeweza au hata alitaka kuyazuia.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 112, 113]
Kufanya Mambo Yote Kwa Ajili ya Habari Njema
PYOTR PARTSEY
ALIZALIWA 1926
ALIBATIZWA 1946
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Pyotr alikutana na Mashahidi wa Yehova mnamo 1943 na alitumikia vifungo katika kambi mbili za mateso za Wanazi na pia katika kambi ya kazi ngumu huko Urusi. Baadaye alitumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko wakati wa marufuku.
BAADA ya kujifunza mafundisho ya msingi ya Biblia huko Ujerumani ya Nazi, mara moja nilianza kuzungumza na marafiki wangu, na wengi wao walijiunga nami katika ibada safi. Mnamo 1943, kasisi fulani alinisaliti kwa Gestapo, ambao walinikamata na kunishutumu kwa kuendesha shughuli za uchochezi kati ya vijana. Baada ya muda mfupi nilijikuta katika kambi ya maangamizi ya Maidanek nchini Poland. Tulithamini sana ushirika pamoja na akina ndugu na dada. Katika kambi, azimio letu la kuhubiri lilitiwa nguvu. Wengi huko walionyesha upendezi katika kweli, na tulitafuta njia za kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Wakati mmoja nilichapwa viboko 25 kwa kiboko ambacho mbele kilikuwa na kamba mbili za ngozi. Nilisimama na kusema kwa sauti katika Kijerumani “Danke schön!” (“Asante!”) Mjerumani mmoja alishangaa na kusema: “Ona jinsi kijana huyu alivyo na ujasiri! Tumemchapa na anatushukuru!” Mgongo wangu ulikuwa na majeraha chungu nzima kwa sababu ya kupigwa.
Kazi ilikuwa ngumu na tulichoka sana. Wale waliokufa walichomwa katika mahali pa kuteketezea maiti, ambapo palifanya kazi mchana na usiku. Nilifikiri kwamba hata mimi karibuni nitateketezwa katika moto huo. Ilionekana ni kana kwamba nisingetoka kambini nikiwa hai. Nilinusurika nilipoumia kidole changu. Wote waliokuwa na afya zaidi walilazimishwa kufanya kazi, na wengine wakapelekwa kwenye kambi nyingine. Baada ya majuma mawili, nilipelekwa kwenye kambi ya mateso ya Ravensbrück.
Karibu na mwisho wa vita, nilisikia fununu kwamba Wajerumani wangetupiga risasi sisi sote. Kisha tukagundua kwamba askari wote walikuwa wamekimbia. Wafungwa walipoelewa kwamba walikuwa huru, kila mtu alitoweka. Nilijikuta Austria, ambako niliombwa nijiunge na jeshi. Nilikataa mara moja, nikisema kwamba nilikuwa nimefungwa katika kambi za mateso kwa sababu ya imani yangu ya kidini. Niliruhusiwa kurudi nyumbani nchini Ukrainia, ambayo wakati huo bado ilikuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti. Mnamo 1949, nilimwoa Yekaterina, ambaye amekuwa mwenzi wangu mwaminifu maishani. Katika mwaka wa 1958, nilikamatwa na kupelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu huko Mordvinia.
Baada ya kuachiliwa, nilishiriki katika kazi ya kuchapisha vichapo vya Biblia. Pindi moja, mnamo 1986, tulifanya kazi usiku wote ili tuchapishe kurasa 1,200. Tuliziweka kwenye sakafu, katika vitanda, na mahali popote tulipoweza. Ghafula bila kutarajia, mpelelezi wa shirika la KGB akatokea, akasema amekuja tu kuzungumza nasi. Yekaterina akamuuliza angependa tuongee tukiwa wapi, bila kufikiria kwamba labda angesema anapenda tuongelee ndani ya nyumba. Lakini inafurahisha kwamba alitaka kuongea nasi katika sehemu ya jiko iliyokuwa nje. Ikiwa angeingia ndani ya nyumba, tungekamatwa.
Hata kufikia wakati huu, tunajaribu kuishi kupatana na wakfu wetu na kufanya kila kitu kwa ajili ya habari njema. Watoto wetu 6, wajukuu 23, na vitukuu 2 wote wanamtumikia Yehova kwa uaminifu, na tunamshukuru Yehova kwa sababu watoto wetu wanaendelea kutembea katika kweli.
[Sanduku katika ukurasa wa 122]
Kifungo cha Upweke
Kulingana na utaratibu wa adhabu nchini Urusi, lilikuwa jambo la kawaida mtu kufungwa kifungo cha upweke kwa makosa kama kukataa kutoa kwa hiari vichapo vya kidini. Wafungwa walipewa nguo za pamba zilizochakaa na kufungiwa kwenye vyumba vya gereza.
Wazia jinsi chumba cha gereza cha kawaida kilivyokuwa. Kilikuwa kidogo, karibu mita tatu za mraba. Kilikuwa na giza, unyevunyevu, uchafu, na chenye baridi kali hasa wakati wa majira ya baridi kali. Kuta zilizojengwa kwa zege zilikuwa zinakwaruza. Kulikuwa na dirisha dogo sana kwenye kuta nene za chumba hicho. Baadhi ya vioo vilikuwa vimevunjika. Taa ya umeme iliyotoa mwanga hafifu, iliwekwa mahali fulani juu kwenye ukuta na kufunikwa na sahani ya chuma yenye matundu madogo. Mbali na sakafu ya zege, kitu pekee cha kukalia kilichokuwamo ndani ya chumba hicho cha gereza ni sehemu ya ukuta iliyotokeza kama benchi. Hungeweza kukaa hapo kwa muda mrefu. Miguu na misuli ya mgongo ingechoka haraka na kuanza kuuma, huku ukuta unaokwaruza ukikukata mgongoni.
Usiku walinzi wangesukuma boksi la mbao ambalo mfungwa alilalia. Liliunganishwa kwa vyuma vidogo vyembamba. Ungeweza kulala juu ya ubao huo uliounganishwa kwa vyuma, lakini baridi ingekufanya uendelee kukaa macho. Hakukuwa na blanketi. Kwa kawaida, mfungwa wa kifungo cha upweke alipewa mkate wenye gramu 300 kwa siku na mchuzi mwepesi mara moja kila baada ya siku tatu.
Choo, ambacho kwa kawaida kilikuwa ni bomba dogo lililokuwa sakafuni kilitoa harufu mbaya. Baadhi ya vyumba vya gereza vilikuwa na feni ambazo zilipuliza harufu mbaya kutoka kwenye mabomba ya maji machafu iingie kwenye vyumba. Nyakati nyingine mnyapara angewasha feni hizo ili kumkatisha tamaa mfungwa na hivyo kumwadhibu zaidi.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 124, 125]
Kambi Na. 1 ya Mordvinia
Kati ya 1959 na 1966, akina ndugu zaidi ya 450, walitumikia kifungo chao kwenye kambi hiyo, ambayo ilikuwa na uwezo wa kuchukua wafungwa 600 kwa wakati mmoja. Ikiwa moja kati ya kambi 19 za kazi ngumu kwenye eneo la Mordvinia, kambi hiyo ilizungukwa na ua wa waya wenye umeme ambao ulikuwa na kimo cha mita tatu. Ua huo ulizungukwa na ua nyingine 13 za nyaya. Kila wakati udongo kuzunguka kambi hiyo ulitifuliwa ili kwamba yeyote atakayetoroka angeacha alama za miguu.
Kwa kuwatenga Mashahidi wa Yehova na watu wengine wa nje ya kambi, wenye mamlaka walijaribu kuwatiisha kwa nguvu au kisaikolojia. Hata hivyo, akina ndugu walifanikiwa kupanga mambo ya kitheokrasi ndani ya kambi hiyo.
Kambi hiyo ikawa mzunguko na ikawa na mwangalizi wake wa mzunguko. Mzunguko huo uliundwa na makutaniko manne yaliyoundwa na vikundi 28 vya funzo la kitabu. Ili kuwasaidia wote wawe imara kiroho, akina ndugu waliamua kufanya mikutano saba kwa juma. Mwanzoni kulikuwa na Biblia moja iliyokuwa ikitumiwa na makutaniko yote, hivyo kulikuwa na ratiba ya kusoma Biblia hiyo kutaniko moja hadi lingine. Nafasi ilipojitokeza, ndugu walinakili Biblia. Vitabu tofautitofauti vya Biblia vilinakiliwa kwenye madaftari na nakala halisi ya Biblia ilifichwa. Kwa njia hiyo akina ndugu waliweza kufuata ratiba iliyopangwa ya usomaji wa Biblia. Funzo la Mnara wa Mlinzi lilipangwa pia. Akina dada waliokuwa wanakuja kuwaona waume zao kambini walibeba nakala ndogo za magazeti. Waliweka nakala hizo midomoni mwao, kwenye visigino vya viatu vyao au walizisuka zikiwa nyembamba pamoja na nywele zao. Akina ndugu wengi walifungwa vifungo vya upweke kwa siku mmoja hadi siku 15 kwa ajili ya kunakili vichapo kwa mkono.
Hiyo ilikuwa sehemu ya upweke mbali na wafungwa wengine. Walinzi waliokuwa wakisimamia sehemu hizo walikuwa waangalifu ili Mashahidi wa Yehova wasisome kitu chochote walipokuwa hapo. Hata hivyo, baadhi ya akina ndugu walifikiria njia za kuwaandalia chakula cha kiroho. Ndugu mmoja angepanda juu ya paa la jengo lililokuwa likiangaliana na ua ambao wafungwa waliofungwa kifungo cha upweke waliruhusiwa kutembea-tembea. Aliandaa mapema vikaratasi vidogovidogo sana ambavyo vilikuwa na andiko fulani la Biblia vikiwa vimekunjwa katika umbo la duara vyenye kipenyo cha sentimita moja. Kisha ndugu huyo angeviweka vikaratasi hivyo vilivyokunjwa kwenye bomba lililokuwa wazi pande zote na kupuliza kuelekea upande alikokuwa ndugu yule aliye kwenye kifungo cha upweke. Ndugu huyo angeinama akijidai kana kwamba anafunga kamba za viatu vyake, na kuokota chakula cha kiroho bila kugundulika.
Kwa ajili ya kifungua kinywa na mlo wa jioni, wafungwa walipewa uji mwembamba uliochanganywa na mafuta kidogo ya mbegu za pamba. Kwa kawaida chakula cha mchana kilikuwa supu ya viazi sukari au mchuzi mwingine pamoja na mlo mkuu wa siku hiyo. Mkate ambao wafungwa walikula ulikuwa unaonekana kama kitambaa kigumu kilichokuwa kikitumiwa kutengenezea viatu! Ivan Mikitkov anakumbuka hivi: “Nilifungwa miaka saba kwenye kambi hiyo, na kila mara tulikuwa na maumivu makali ya tumbo.”
Ndugu walibaki imara katika imani. Kuwa mbali na ndugu zao waliokuwa nje, hakukuvuruga usawaziko wa kiroho wa watumishi hao waaminifu wa Mungu, ambao waliendelea kuonyesha imani na upendo kuelekea Mungu na majirani wao.—Mt. 22:37-39.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 131, 132]
Msichana Mmoja Aliniuliza, “Kwa Nini Unalia?”
POLINA GUTSHMIDT
ALIZALIWA 1922
ALIBATIZWA 1962
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuja kuwa mke wa Viktor Gutshmidt. Alipokuwa gerezani, Polina aligundua jinsi Mashahidi wa Yehova walivyo wema.
NILIUNGA mkono na kuuamini sana mfumo wa Kikomunisti. Hata hivyo, mnamo Mei 1944, Wakomunisti walinikamata na kunipeleka kwenye kambi ya mateso huko Vorkuta. Kwa miaka miwili sikuambiwa kwa nini nilikamatwa. Mwanzoni nilifikiri walikuwa wamekosea na nilingoja waniachilie huru. Badala yake, nilihukumiwa kifungo cha miaka kumi kwenye kambi ya mateso kwa kosa la kutoa maelezo yaliyoonekana kuwa yanapinga Usovieti.
Kwa kuwa nilikuwa na taaluma ya utabibu, kwa miaka miwili nilifanya kazi kwenye hospitali ya kambini. Mnamo 1949, nilihamishwa hadi Inta, kwenye kambi ya wafungwa wa kisiasa. Mfumo wa kurekebisha wafungwa kwenye kambi hiyo ulikuwa na vizuizi vingi. Miongoni mwa wafungwa kulikuwa na hali ya kufungiana kinyongo, ufidhuli, upotovu wa maadili, kutojali, na kuvunjika moyo. Uvumi wa kwamba wafungwa wote kambini watapigwa risasi au watafungwa kifungo cha maisha, ulifanya hali ambayo tayari ilikuwa mbaya iwe mbaya hata zaidi. Chini ya hali kama hizo wafungwa kadhaa wakawa vichaa. Kwa sababu kulikuwa na watu wengi kambini ambao walikuwa wakiwapasha maaskari habari, wafungwa hawakuaminiana na walichukiana. Kila mtu aliishi kivyake bila kujishughulisha na wengine. Ubinafsi na pupa vilienea sana.
Kikundi kimoja cha wafungwa wanawake 40 hivi kilikuwa tofauti sana na wafungwa wengine. Kwa kawaida walikaa pamoja na kwa kushangaza walikuwa safi, wenye kuvutia, wenye huruma, na wenye urafiki. Wengi wao walikuwa wasichana na mabinti wadogo. Nilikuja kugundua kwamba walikuwa wafuasi wa dini, Mashahidi wa Yehova. Wafungwa waliwatendea kwa njia tofautitofauti. Wengine waliwatendea vibaya na kwa uhasama. Wengine walistaajabia tabia zao, hasa upendo miongoni mwao. Kwa mfano, mmoja wao alipokuwa mgonjwa, wengine wangepanga zamu ya kumhudumia. Kwenye kambi hiyo, hilo lilikuwa jambo lisilo la kawaida.
Nilishangazwa kwamba kikundi hicho kilikuwa na watu kutoka mataifa mengi, na bado, walikuwa na urafiki mkubwa miongoni mwao. Kufikia wakati huo nilikuwa nimekata tamaa kabisa ya maisha. Wakati fulani nilipokuwa nimevunjika moyo sana, nilikaa chini na kuanza kulia. Mmoja kati ya wasichana wale alinikaribia na kuniuliza, “Polina, kwa nini unalia?”
Nilimjibu, “Sitaki kuendelea kuishi.”
Msichana aliyeitwa Lidia Nikulina, alianza kunifariji. Alinieleza kusudi la uhai, jinsi Mungu atakavyosuluhisha matatizo ya wanadamu na mambo mengine mengi. Mnamo Julai (Mwezi wa Saba) 1954, niliachiliwa. Kufikia wakati huo Mashahidi wa Yehova walikuwa wamenifundisha mambo mengi na nilifurahia kuwa mmoja wao.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 140, 141]
Niliacha Kuwa Injinia wa Jeshi Nikawa Mhubiri wa Habari Njema
VLADIMIR NIKOLAEVSKY
ALIZALIWA 1907
ALIBATIZWA 1955
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alihamishwa mara 256 kutoka kambi na magereza mbalimbali. Alikufa mnamo 1999.
NILIHITIMU kwenye Taasisi ya Mawasiliano ya Kiufundi ya Moscow mnamo 1932. Hadi mwaka wa 1941 nilifanya kazi kama injinia na mchora-ramani mkuu katika taasisi fulani huko Moscow. Nilibuni vifaa fulani vya pekee kwa ajili ya meli za vita. Nilipelekwa gerezani wakati wa vita na mwishowe nikapelekwa kwenye kambi katikati mwa Kazakhstan, katika kijiji cha Kengir.
Kikundi fulani cha Mashahidi wa Yehova kilinivutia. Walikuwa tofauti na wafungwa wengine. Kati ya wafungwa 14,000 katika kambi tatu za gereza hilo kulikuwa na Mashahidi 80 hivi. Tofauti kati ya Mashahidi hao na wafungwa wengine ilionekana waziwazi hasa wakati wa uasi wa mwaka wa 1954 katika gereza hilo la Kengir. Mashahidi wa Yehova hawakukubali kujitayarisha kwa ajili ya uasi au kushiriki katika uasi wenyewe. Walikuwa watulivu sana na walijaribu kuwaeleza wafungwa wengine msimamo wao. Nilivutiwa sana na tabia yao hivi kwamba nikawauliza kuhusu imani yao. Muda fulani baadaye, nilijiweka wakfu kwa Yehova. Imani ya Mashahidi ilijaribiwa ndani ya kambi, hasa uasi ulipokomeshwa na askari wa jeshi kwa kutumia vifaru.
Wakati mmoja niliambiwa kwamba majenerali wawili walikuja kutoka Moscow ili wakutane nami. Mmoja wao aliniambia hivi: “Vladimir, hebu acha mambo haya. Wewe ni injinia wa jeshi na mchora-ramani. Nchi yako inakuhitaji. Tunataka urudi ukafanye kazi yako. Unawezaje kufurahia kuwa kati ya watu ambao hawana elimu?”
Niliwajibu hivi, “Sina sababu yoyote ya kujisifu. Vipawa vyote vya mwanadamu vinatoka kwa Mungu. Wote ambao wanamtii watafurahia Utawala wa Miaka Elfu wa Ufalme wa Kristo na wakati huo wanadamu watakuwa wakamilifu na wenye elimu kamili.”
Nilifurahi sana kwamba nilipata nafasi ya kuzungumza na majenerali hao kuhusu kweli. Walijaribu mara kadhaa kunisihi nifanye kazi niliyokuwa nikifanya hapo awali. Hata hivyo, niliwaambia wasinisumbue tena bali waniache kwenye kambi hiyo pamoja na ndugu zangu wa kiroho ambao niliwapenda sana.
Mnamo 1955, kifungo changu kilifutwa. Nilianza kufanya kazi katika shirika la uchoraji wa ramani ambalo halikuwa na uhusiano na jeshi. Kwa sababu ya jitihada zangu za kupanda mbegu za kweli kwa wingi, nilianzisha funzo la Biblia pamoja na familia ya injinia mmoja. Muda si muda, yeye na familia yake wakawa Mashahidi wa Yehova na wahubiri wenye bidii. Lakini shirika la KGB lilikuwa likinichunguza na wakati mmoja walipofanya upekuzi walikuta vichapo vya Biblia ndani ya nyumba yangu. Nilihukumiwa kifungo cha miaka 25 na nikapelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu katika jiji la Krasnoyarsk, huko Siberia. Nilihamishwa mara nyingi kutoka kambi na magereza mbalimbali. Wakati mmoja, nilihesabu kwamba maishani mwangu nilikuwa nimehamishwa mara 256.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 147, 148]
Tulihitaji Masanduku Makubwa
NADEZHDA YAROSH
ALIZALIWA 1926
ALIBATIZWA 1957
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alijifunza kweli katika kambi ya mateso ya Ravensbrück. Aliporudi kwenye Muungano wa Sovieti, alifanya kazi kwa miaka mingi akiwapelekea akina ndugu vichapo. Sasa anaishi huko Caucasia.
NILIPOINGIA kwenye kambi ya mateso mnamo 1943, sikutaka kuendelea kuishi. Niliendelea kuwa na mtazamo huo hadi nilipokutana na Mashahidi wa Yehova. Nilifurahi kama nini kurudi nyumbani Ukrainia nikiwa na tumaini hakika la kuishi milele katika paradiso duniani! Nilianza kuwasiliana na akina dada wa kiroho ili niweze kujitegemeza kiroho. Hata hivyo, maofisa wa KGB waligundua barua zangu, na muda si muda nilihukumiwa kifungo cha miaka 15 katika kambi ya kazi ngumu.
Mnamo Novemba 1947, nilipelekwa kwenye kambi huko Kolyma ambako nilitumikia kifungo changu bila kukutana na Shahidi yeyote. Yehova alinisaidia kuhubiri. Mfungwa anayeitwa Yevdokia, alionyesha anapendezwa na Biblia. Tukawa marafiki na kutegemezana kiroho na kimwili. Nilikuwa na ujuzi mdogo sana wa Biblia, lakini nilichokuwa nimejifunza kilitosha kunisaidia kudumisha utimilifu wangu kwa Yehova.
Mapema mnamo 1957, mwaka mmoja baada ya kufunguliwa, nilihamia Suyetikha katika Wilaya ya Irkutsk. Akina ndugu walinipokea kwa uchangamfu na kunionyesha ukarimu. Walinisaidia kupata kazi na nyumba. Lakini kilichonifurahisha zaidi ni kwamba waliniomba nishiriki katika utendaji wa kitheokrasi. Kwa kuwa sikuwa nimebatizwa, walinibatiza katika beseni kubwa la maji. Kwa hiyo nikawa tayari kutimiza madaraka mbalimbali katika tengenezo la Yehova. Madaraka yangu yalitia ndani kusafirisha vichapo vya Biblia na barua.
Vichapo vilihitaji kusafirishwa katika maeneo yote ya Siberia, katikati mwa Urusi, na magharibi mwa Ukrainia. Kila kitu kilihitaji kupangwa mapema na kwa uangalifu. Ili kupeleka vichapo hadi Ukrainia magharibi, tulihitaji masanduku makubwa. Wakati mmoja, kwenye Kituo cha Yaroslavl’ huko Moscow, sanduku moja lilifunguka na vichapo vikamwagika. Kwa utulivu, nilisali huku nikikusanya vichapo hivyo bila haraka. Kwa njia fulani nilifaulu kukusanya kila kitu na kutoka kwenye kituo hicho. Nilifurahi kwamba hakuna aliyeshughulika nami.
Wakati mwingine, nilipitia Moscow nikipeleka masanduku mawili yaliyojaa vichapo kutoka Ukrainia mpaka Siberia. Niliweka sanduku moja chini ya kitanda cha chini katika chumba changu cha gari-moshi. Muda mfupi baadaye wasafiri wawili wa kiume waliingia ndani ya chumba hicho. Walikuwa maofisa wa KGB. Walizungumzia mambo mbalimbali kutia ndani Mashahidi, na wakasema kwamba Mashahidi walikuwa “wakisambaza vichapo na kushiriki kuchochea watu dhidi ya Muungano wa Sovieti.” Nilijaribu kutulia ili wasianze kunishuku, hasa ukifikiria kwamba walikuwa wameketi juu ya vichapo walivyokuwa wakizungumzia!
Iwe nilikuwa nikipeleka vichapo au kutimiza migawo mingine, nilikuwa tayari kukamatwa wakati wowote. Hali mbalimbali nilizopitia zilinifundisha kumtumaini Yehova katika mambo yote.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 158, 159]
“Watu Wenu Ni Tofauti Kabisa”
ZINAIDA KOZYREVA
ALIZALIWA 1919
ALIBATIZWA 1958
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alitumia miaka mingi katika kambi mbalimbali na akafa mnamo 2002.
TANGU utotoni nilitamani kumtumikia Mungu. Mnamo 1942 rafiki yangu wa kike alinipeleka katika Kanisa Othodoksi ambako yeye alikuwa akienda ili, kama alivyosema, ‘nisitupwe katika moto wa mateso.’ Hata hivyo, kasisi alikataa kunibatiza aliposikia kwamba nilitoka katika eneo la Ossetia. Lakini rafiki yangu alipompa pesa alibadili maoni yake na kunibatiza. Nilipokuwa nikitafuta kweli, nilishirikiana na Waadventisti, Wapentekoste, na Wabaptisti. Kwa sababu hiyo, wenye mamlaka walinihukumu kifungo kwenye kambi ya kazi ngumu. Kwenye kambi, nilikutana na Mashahidi na nikatambua kwamba wao walikuwa na kweli. Nilipofunguliwa mnamo 1952, nilirudi nyumbani na kuanza kuhubiri habari njema.
Mapema asubuhi moja mnamo Desemba 1958, nilisikia mlango ukibishwa kwa nguvu. Askari waliingia kwa kishindo na kuanza kupekua nyumba yetu, huku wawili kati yao wakihakikisha nimeketi kwenye kona moja. Baba aliamka na akawa na wasiwasi sana hasa kwa sababu ya wana wake. Wazazi wangu walikuwa na wana watano na binti mmoja, yaani, mimi. Baba alipoona jinsi askari walivyokuwa wakipekua kila chumba kutia ndani dari, alijua kwamba upekuzi huo ulisababishwa na imani yangu. Alinyakua bunduki na kusema kwa sauti, “Wewe ni mpelelezi wa Marekani!” Alijaribu kunipiga risasi, lakini askari walimnyang’anya bunduki. Nisingeweza kuamini kwamba baba yangu angenipiga risasi. Upekuzi ulipokwisha, niliingizwa ndani ya lori lakini nilifurahi kwamba nilikuwa hai. Nilihukumiwa kifungo cha miaka kumi kwa sababu ya utendaji wangu wa kidini.
Mnamo Desemba 1965, nilifunguliwa kabla ya kifungo changu kwisha. Wazazi wangu walifurahi kuniona, lakini baba hakutaka niendelee kuishi nyumbani. Hata hivyo, kwa kushangaza, maofisa wa KGB walimlazimisha baba yangu aniandikishe katika nyumba yake na hata wakanisaidia kupata kazi. Baba alikuwa mkali kwangu kama hapo awali, lakini baada ya muda, mtazamo wake ukaanza kubadilika. Alikutana na akina ndugu na dada walipokuja kunitembelea. Ndugu zangu wa kimwili hawakufanya kazi, walilewa, na walikuwa wakali kuelekea watu wengine. Wakati mmoja baba yangu alisema: “Ninaona kwamba watu wenu ni tofauti kabisa na nilivyofikiri. Nitakupa chumba chako mwenyewe ili mweze kufanyia mikutano humo.” Sikuamini jambo hilo! Baba alinipa chumba kikubwa na akaniambia: “Usiogope. Mnapokutana, nitakuwa mlinzi, na hakuna mtu atakayeingia.” Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa sababu kila mtu alijua kwamba baba yangu hapendi mchezo.
Kwa hiyo tulifanya mikutano yetu katika chumba changu, chini ya ulinzi wa Yehova na wa baba yangu. Watu 30 hivi walihudhuria mikutano hiyo kwani hiyo ndiyo iliyokuwa idadi ya Mashahidi huko Ossetia wakati huo. Ilinifurahisha sana kutazama nje ya dirisha na kuwaona wazazi wangu wakiketi barabarani na kutulinda. Leo huko Ossetia, kuna wahubiri 2,600 hivi wenye bidii wanaotangaza Ufalme wa Yehova.—Isa. 60:22.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 162, 163]
Niliachwa Nikiwa Shahidi Pekee Kambini
KONSTANTIN SKRIPCHUK
ALIZALIWA 1922
ALIBATIZWA 1956
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alijifunza kweli mnamo 1953 katika kambi ya kazi ngumu na akabatizwa humo mnamo 1956. Alifungwa kwa miaka 25 mfululizo kwa sababu ya kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alikufa mnamo 2003.
NILIKUTANA na ndugu anayeitwa Vasily mapema katika mwaka wa 1953 katika seli. Alisema alikuwa amefungwa kwa sababu ya imani yake katika Mungu. Sikuelewa mtu angefungwa jinsi gani kwa sababu ya imani yake. Jambo hilo lilinisumbua sana hivi kwamba singeweza kulala. Siku iliyofuata alinieleza zaidi kuhusu jambo hilo. Hatua kwa hatua, nikasadiki kwamba Biblia ni kitabu kutoka kwa Mungu.
Nilibatizwa mnamo 1956. Mwishoni mwa mwaka huo, wanyapara walitupekua na kupata vichapo vingi vya Biblia. Uchunguzi uliendelea kwa karibu mwaka mmoja, na mnamo 1958 mahakama ilinihukumu kifungo cha miaka 23 kwa ajili ya utendaji wa kidini. Kufikia wakati huo, tayari nilikuwa nimefungwa kwa miaka mitano na nusu katika kambi. Muda wa miaka 28 na miezi 6 ulipita nikiwa gerezani bila hata kuonja uhuru.
Mnamo Aprili 1962, mahakama ilinitangaza kuwa “mhalifu hatari sana,” nami nikahamishwa kwenye gereza lenye ulinzi mkali, ambako nilifungwa kwa miaka 11. Kuna mambo mengi ambayo yalifanya kambi kama hiyo iwe “ya pekee.” Kwa mfano, chakula ambacho mtu alipewa kwa siku kilikuwa cha pesa chache sana (kopeck 11), pesa ambazo hazikutosha hata kununua mkate mmoja wakati huo. Nikiwa na kimo cha sentimita 192, nilikuwa na uzani wa kilo 59 tu. Ngozi yangu ilikuwa inabambuka.
Kwa kuwa nilikuwa mjenzi stadi, mara nyingi nilitumwa kurekebisha nyumba za maofisa. Hakuna mtu aliyeniogopa, na watu walioishi humo hawakushughulika kuficha vitu katika nyumba zao. Mke wa ofisa mmoja alipojua kwamba ningefanya kazi katika nyumba yao, hakumpeleka mtoto wake mwenye umri wa miaka sita kwenye shule ya nasari. Lilikuwa jambo la kushangaza: “mhalifu hatari sana” alikuwa ameachwa peke yake ndani ya nyumba na mtoto mwenye umri wa miaka sita! Ilikuwa wazi kwamba hakuna mtu aliyeamini eti mimi ni mhalifu, na isitoshe, eti mhalifu “hatari sana.”
Hatua kwa hatua, akina ndugu wote kambini waliachiliwa. Mnamo 1974, mimi ndiye niliyekuwa Shahidi pekee kambini. Nilikaa humo kwa miaka mingine saba hadi nilipoachiliwa mnamo Agosti 1981. Yehova aliendelea kunitegemeza kiroho. Jinsi gani? Kwa miaka hiyo saba, nilipokea Mnara wa Mlinzi katika barua. Ndugu mmoja alinitumia barua hizo kwa ukawaida akiwa ameandika makala za kila toleo jipya kwa mkono. Kila wakati, ofisa aliyewekwa kambini kuzuia vitu visiingie alinipa barua hizo zikiwa tayari zimefunguliwa. Mimi na yeye tulijua ujumbe uliokuwa katika barua hizo. Hadi leo, sina uhakika ni nini kilichomchochea ajihatarishe hivyo, lakini ninafurahi kwamba alifanya kazi hapo kwa miaka yote saba. Zaidi ya yote, ninamshukuru Yehova. Katika miaka hiyo yote, nilijifunza kumtegemea Yehova na nikapata nguvu kutoka kwake.—1 Pet. 5:7.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 168, 169]
Baada ya Vita, Nilirudi Urusi
ALEKSEY NEPOCHATOV
ALIZALIWA 1921
ALIBATIZWA 1956
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alijifunza kweli katika kambi ya mateso ya Buchenwald mnamo 1943 na akafungwa kwa miaka 19 huko Urusi. Alitumika akiwa painia wa kawaida kwa zaidi ya miaka 30, muda mrefu kati ya huo kazi ikiwa imepigwa marufuku.
AKIWA na umri wa miaka 20, Aleksey alifungwa katika kambi ya mateso ya Auschwitz, katika Ujerumani iliyokuwa chini ya Wanazi. Baadaye, alihamishwa hadi kwenye kambi ya Buchenwald ambako alijifunza kweli. Muda mfupi kabla ya kuachiliwa, Mashahidi wawili watiwa-mafuta walimwambia: “Aleksey, itakuwa vizuri ukirudi Urusi baada ya vita. Hiyo ni nchi kubwa ambayo inahitaji wavunaji. Hali huko ni ngumu, kwa hiyo jitayarishe kukabiliana na majaribu ya kila namna. Tutakuwa tukisali kwa ajili yako na kwa ajili ya wale wanaokusikiliza.”
Waingereza walimfungua Aleksey mnamo 1945. Alirudi Urusi ambako alifungwa kwa miaka kumi kwa sababu ya kukataa kupiga kura. Anaandika hivi: “Mwanzoni nilikuwa Shahidi pekee kambini. Nilimwomba Yehova mwongozo wa kutafuta kondoo, na punde si punde tukawa 13! Wakati huo wote, hatukuwa na vichapo vya Biblia. Tungenakili maandiko kutoka kwenye vitabu vya hadithi ambavyo tulipata kwenye maktaba ya gereza.”
Aleksey alimaliza kifungo chake cha miaka kumi. Alipoachiliwa, alienda kwenye eneo ambalo alijua watu wengi walimwamini Yesu. Anasema: “Watu walikuwa na njaa ya kiroho. Walinijia usiku na mchana; walikuja na watoto wao. Walihakikisha kila kitu walichosikia kwa kutumia Biblia.”
Kwa miaka michache iliyofuata, Aleksey aliwasaidia zaidi ya watu 70 kufikia ubatizo. Mmoja wao alikuwa Maria ambaye alikuja kuwa mke wake. Anakumbuka hivi: “Maofisa wa KGB walinitafuta. Nilikamatwa na kufungwa kwa miaka 25. Kisha wakamkamata Maria. Kabla ya kesi, Maria alifungwa kwa miezi saba katika kifungo cha upweke. Mpelelezi alimwambia angemwachilia ikiwa angemkana Yehova. Maria alikataa. Mahakama ilimfunga kwa miaka saba katika kambi ya kazi ngumu. Dada yetu wa kiroho alimchukua binti yetu na kumtunza.”
Aleksey na Maria waliachiliwa kabla ya kumaliza vifungo vyao. Walihamia Wilaya ya Tver’. Huko wenye mamlaka na wenyeji waliwapinga vikali, na jirani mmoja alichoma nyumba yao. Miaka iliyofuata, walilazimika kuhama mara nyingi; hata hivyo, kila mahali walipohamia, walifanya wanafunzi.
Aleksey anasema: “Wakati wa kifungo chetu, hatungeweza kusoma Neno la Mungu. Tangu tulipofunguliwa tumejiwekea mradi wa kusoma Biblia kila siku. Kufikia sasa mimi na Maria tumesoma Biblia zaidi ya mara 40. Ni Neno la Mungu ambalo limetupa nguvu na bidii katika utumishi.”
Kwa ujumla, Aleksey ametumia miaka 4 katika kambi za mateso za Wanazi na miaka 19 katika kambi na magereza ya Urusi. Katika miaka 30 ambayo amekuwa painia, yeye na mke wake waliwasaidia watu wengi sana kumjua na kumpenda Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 177, 178]
Askari Alisema Kweli
REGINA KUKUSHKINA
ALIZALIWA 1914
ALIBATIZWA 1947
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Ingawa kwa miaka mingi hakuweza kuwasiliana na kutaniko, aliendelea kuhubiri habari njema.
MNAMO 1947, Shahidi fulani alizungumza nami sokoni. Jioni hiyo nilimtembelea nyumbani kwake nasi tukazungumza kwa saa kadhaa. Mara moja niliamua kwamba kama yeye, nitamtumikia Yehova kwa bidii! Nilimwambia, “Unahubiri, nami pia nitahubiri.”
Mnamo 1949, nilikamatwa huko L’viv, Ukrainia kwa sababu ya kuhubiri na nikatenganishwa na mume wangu na binti zangu wawili wadogo. Mahakama iliyoitwa troika, yaani, kesi iliyokuwa na mahakimu watatu ambayo haikumruhusu mtu yeyote aje kusikiliza, ilinihukumu kifo kwa kupigwa risasi. Akisoma hukumu hiyo, mwanamke aliyekuwa mmoja wa mahakimu, aliongeza hivi, “Kwa kuwa una watoto wawili, tumeamua kupunguza uzito wa hukumu hiyo ya kifo na kukufunga miaka 25.”
Nilipelekwa kwenye gereza ambako kulikuwa na wanaume tu. Tayari walijua kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova. Walipojua kwamba nimehukumiwa kifungo cha miaka 25, walishangaa kwamba nilikuwa mtulivu. Nilipotolewa katika gereza hilo, askari kijana alinipa furushi lenye chakula na kuniambia kwa fadhili, “Usiogope; kila kitu kitakuwa sawa.”
Kufikia mwaka wa 1953, nilikuwa nimetumikia kifungo changu katika kambi iliyokuwa kaskazini mwa Urusi. Kambi hiyo ilikuwa na akina dada wengi kutoka jamhuri mbalimbali za Muungano wa Sovieti. Tulipendana kama familia.
Tulijaribu kutoa ushahidi mzuri kupitia mwenendo wetu, tukitumaini kwamba wengine wangechochewa kumtumikia Mungu. Tulihitaji kufanya kazi ngumu kwa muda mrefu. Nilifunguliwa kutoka kwenye kambi hiyo kabla ya kifungo changu kwisha, lakini nilipelekwa kwenye upweke wa aina nyingine. Kwa zaidi ya miaka mitano, singeweza kuwasiliana na kutaniko. Ilikuwa vigumu zaidi kukabiliana na hali hiyo kuliko kufungwa. Licha ya hali hizo, sikuzote nilihisi utegemezo wa Yehova na upendo wake usiobadilika. Nilisoma Biblia sana na kutafakari niliyosoma, na kufanya hivyo kuliniimarisha kiroho.
Yehova alinisaidia kuwasiliana na Mashahidi kwa njia isiyo ya kawaida. Katika gazeti Soviet Russia, nilisoma makala iliyokuwa ikiwapinga akina ndugu huko Ossetia, kusini-magharibi mwa Urusi. Makala hiyo ilisema kwamba utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulielekezwa dhidi ya Wasovieti. Makala hiyo ilitoa majina hususa ya akina ndugu na dada na kuchapisha anwani zao. Nilifurahi sana! Katika barua, niliwaambia kwamba nilitaka kukutana nao. Tulipokutana, akina ndugu walinitegemeza sana na kusema kwamba Yehova alikuwa ameruhusu makala hiyo ichapishwe ili niweze kuwasiliana na watu wake.
Sasa nina umri wa miaka 92. Naam, yule askari mwenye fadhili alisema kweli. Muda wote wa maisha yangu, licha ya hali ngumu, mambo yamekuwa sawa tu.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 188, 189]
Kuvitia Nguvu “Vigingi vya Hema” Letu
DMITRY LIVY
ALIZALIWA 1921
ALIBATIZWA 1943
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa kwenye Halmashauri ya Nchi ya Urusi kwa zaidi ya miaka 20 na sasa anatumikia akiwa mzee katika kutaniko huko Siberia.
ULIKUWA mwaka wa 1944, miezi sita kabla ya mwisho wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Nilikuwa nimesimama katika mahakama mbele ya jaji wa kijeshi kwa sababu ya msimamo wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote wa kisiasa. Nilihukumiwa kifo kwa kupigwa risasi, lakini baadaye hukumu ilibadilishwa na kuwa kifungo cha miaka kumi katika kambi ya kazi ngumu.
Mnamo Januari 1945, nilipelekwa kwenye kambi moja kaskazini mwa Urusi katika mji wa Pechora, katika Jamhuri ya Komi. Kati ya mamia ya wafungwa waliokuwa kambini, kulikuwa na ndugu kumi. Nasikitika kwamba gazeti pekee nililokuwa nimebeba la Mnara wa Mlinzi lilichukuliwa, kwa hiyo hatukuwa na chakula cha kiroho. Nilikuwa nimechoka sana hivi kwamba singeweza kufanya kazi. Tulipoenda kuoga bafuni, ndugu mmoja aliniambia kwamba nilionekana mifupa mitupu. Kwa kweli, nilikuwa mnyonge sana hivi kwamba nilipelekwa kwenye kambi ya matibabu huko Vorkuta.
Baada ya muda, nilianza kupata nafuu na nikapelekwa kufanya kazi ya kuchimba mchanga. Lakini kabla ya mwezi mmoja kwisha, kazi hiyo ngumu ilinifanya nikonde tena. Daktari alifikiri kwamba ninabadilishana chakula ili nipate sigara, lakini nikamwambia mimi ni Shahidi wa Yehova na sivuti sigara. Nilifanya kazi katika kambi hiyo kwa miaka miwili. Ingawa nilikuwa Shahidi pekee kambini, kila mara kulikuwa na watu waliotaka kusikiliza kweli, na wengine kati yao waliitikia habari njema.
Wakati mmoja, watu wa ukoo walinitumia gazeti la Mnara wa Mlinzi lililoandikwa kwa mkono. Nilifaulu jinsi gani kulipata ilhali kila furushi lilikaguliwa kwa uangalifu na mnyapara? Kurasa za gazeti hilo zilikuwa zimekunjwa mara mbili na kuwekwa chini ya mkebe wenye sehemu mbili na sehemu ya juu ikafunikwa na mafuta mengi. Msimamizi wa gereza alitoboa mkebe huo na kwa kuwa hakushuku chochote, akanipa. Chanzo hicho cha “maji yaliyo hai” kilinifaa kwa muda mrefu.—Yoh. 4:10.
Mnamo Oktoba 1949, niliachiliwa kabla ya kifungo changu kuisha, na katika mwezi wa Novemba nilirudi nyumbani nchini Ukrainia. Tulisikia kwamba ndugu fulani walikuwa wameenda Moscow ili kuandikisha utendaji wetu kisheria, lakini ilionekana kwamba wenye mamlaka hawakuwa tayari kutambua Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti.
Usiku wa Aprili 8, 1951, tuliingizwa kwenye gari-moshi pamoja na familia nyingine za Mashahidi wa Yehova na kupelekwa Siberia. Majuma mawili baadaye, tulifika katikati ya Siberia, katika kijiji cha Khazan, Wilaya ya Irkutsk.
Tuliguswa moyo na andiko la Isaya 54:2, linalosema: “Refusha kamba za hema lako, na uvitie nguvu vigingi vya hema lako.” Tuliona kwamba tunatimiza unabii huo. Ni nani kati yetu ambaye kwa kupenda angehamia Siberia? Niliona kwamba ni lazima tuvitie nguvu vigingi vya hema letu. Kwa hiyo, nimeishi Siberia kwa zaidi ya miaka 55.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 191, 192]
Sikuwa na Mahali Pangu Pa Kuishi
VALENTINA GARNOVSKAYA
ALIZALIWA 1924
ALIBATIZWA 1967
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alifungwa gerezani na kwenye kambi za kazi ngumu kwa miaka 21, miaka 18 kati ya hiyo akiwa bado hajabatizwa. Valentina aliwasaidia watu 44 wajifunze kweli kabla ya kifo chake mnamo 2001.
MIMI na mama yangu tuliishi upande wa magharibi wa Belarus. Nilikutana na Mashahidi wa Yehova mnamo Februari 1945. Ndugu mmoja alikuja nyumbani kwetu mara tatu tu na kutufundisha mambo fulani katika Biblia. Ingawa sikumwona tena, nilianza kuwahubiria majirani na marafiki. Wenye mamlaka walinikamata, na nikahukumiwa kifungo cha miaka nane katika kambi. Walinipeleka kwenye kambi katika Wilaya ya Ulyanovsk.
Nikiwa kambini niliwachunguza wafungwa wengine na kusikiliza mazungumzo yao, nikitumaini kwamba nitakutana na Shahidi wa Yehova. Mnamo 1948, nilimsikia mfungwa mmoja mwanamke akizungumza kuhusu Ufalme wa Mungu. Mfungwa huyo aliitwa Asya. Nilifurahi sana kuzungumza naye kuhusu mambo ya kiroho. Muda si muda, dada wengine watatu waliletwa kambini. Tulikuwa na vichapo vichache, kwa hiyo tulijaribu kuwasiliana mara nyingi iwezekanavyo.
Mnamo 1953 niliachiliwa huru, lakini miaka mitatu na nusu baadaye, nilikamatwa kwa sababu ya kuhubiri na kufungwa kwa miaka kumi. Mwaka wa 1957 nilihamishiwa kwenye kambi ya Kemerovo, ambako kulikuwa na dada 180 hivi. Sikuzote tulikuwa na vichapo vya Biblia. Katika majira ya baridi kali, tulificha vichapo katika theluji, na katika majira ya kiangazi, tulivificha katika nyasi na kwenye mchanga. Wakati wa upekuzi, nilificha hati katika mikono yote miwili, nilijitanda kitambaa kikubwa mabegani na nilishikilia miisho ya kitambaa hicho kwa mikono yangu. Nilipohamishwa kutoka kambi moja hadi nyingine, nilivaa kofia ambayo nilikuwa nimeshona mwenyewe na kuficha magazeti kadhaa ya Mnara wa Mlinzi ndani yake.
Mwishowe nilihamishiwa kwenye kambi fulani huko Mordvinia. Huko kulikuwa na Biblia, ambayo ilifichwa mahali salama. Tungeisoma wakati tu dada mwenye kuitunza alikuwapo. Mara nyingine pekee ambayo nilikuwa nimewahi kuona Biblia ni wakati ilikuwa mikononi mwa ndugu aliyezungumza nami kuhusu kweli katika mwaka wa 1945.
Nilipoachiliwa mwaka wa 1967, nilihamia huko Angren, Uzibekistani. Hapo nilifaulu kuonyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Hii ndiyo mara yangu ya pili kukutana na akina ndugu tangu yule ndugu wa kwanza aliponihubiria. Hiyo ni kwa sababu nilikuwa nimefungwa katika kambi za wanawake peke yao. Ndugu na dada wote katika kutaniko walikuwa na bidii nami nikaja kuwapenda. Mnamo Januari 1969, ndugu wanane na dada watano katika kutaniko letu walikamatwa kwa sababu ya kuhubiri, mimi nilikuwa mmoja wao. Nilihukumiwa miaka mitatu na kuitwa “mhalifu hatari sana.” Mara nyingi nilifungwa kifungo cha upweke kwa sababu ya kuhubiri.
Niliongoza mafunzo ya Biblia na waliopendezwa tukiwa tumejifunika blanketi. Tulikatazwa kuwasiliana tulipotembea. Iwapo tungekutwa tukizungumza, tungeadhibiwa kwa kupewa kifungo cha upweke. Tulitumia vichapo vilivyonakiliwa kwa mkono, na tuliendelea kuvinakili kila mara.
Sikuwa na mahali pangu pa kuishi. Vitu vyangu vyote vilitoshea katika mfuko mmoja, lakini nilifurahi na kuridhika kwa kuwa nilimtumikia Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 200, 201]
Mpelelezi Aniimarisha Kiroho
PAVEL SIVULSKY
ALIZALIWA 1933
ALIBATIZWA 1948
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Wasovieti walijaribu kumwelimisha upya mara nyingi, sasa anatumikia akiwa mzee wa kutaniko nchini Urusi.
MNAMO 1958, nilikamatwa kwa sababu ya utendaji wa kidini. Ofisa aliyenipeleka kwenye gari-moshi aliniambia, “Mtazame mke wako kwa mara ya mwisho kwa sababu hutamwona tena.”
Huko Irkutsk niliwekwa kwenye seli ya pekee ambayo ilitoshea kusimama tu. Baada ya hapo, nilifungwa miezi sita kwenye kifungo cha upweke kabla ya kesi yangu. Nilikuwa nikihojiwa hasa usiku na wapelelezi walijitahidi sana kuvunja imani yangu katika Biblia na kujaribu kunifanya nisilitegemee tengenezo la Mungu. Nilishutumiwa kwa kujiingiza katika shughuli zisizo halali za Mashahidi wa Yehova. Mara nyingine walitumia jeuri, ingawa njia kuu waliyotumia ilikuwa kujaribu kubadili jinsi nilivyofikiri. Nilimsihi Yehova anipe nguvu ya kubaki imara. Alinitegemeza sikuzote.
Wakati mmoja nilipokuwa nikihojiwa, mpelelezi aliniita ofisini mwake na kusema: “Sasa tutakuonyesha kile ambacho tengenezo lenu linafanya. Kisha utaona ikiwa ni kazi ya Mungu au la!”
Akiniangalia kwa makini, aliendelea kusema: “Mwaka huu, kusanyiko lenu huko New York lilihudhuriwa na watu 253,000 katika viwanja viwili. Ukifikiria ukubwa wa tukio hilo, utajua kwamba haingewezekana mfanikiwe bila msaada wa Shirika la Upelelezi la Marekani (CIA). Kusanyiko hilo lilifanywa kwa siku nane. Wajumbe walihudhuria kutoka nchi mbalimbali, walisafiri kwa ndege, gari-moshi, meli, na njia nyingine za usafiri. Je, mambo hayo yote yangefanyika bila msaada wa wenye mamlaka? Ni nani anayeweza kulipia kusanyiko katika viwanja hivyo vikubwa kwa siku nane?”
Kisha mpelelezi huyo akatandaza picha nyingi mezani. Katika picha moja, niliona wajumbe wenye shangwe waliokuwa wamevaa mavazi maridadi ya kitamaduni wakikumbatiana. Picha nyingine ilimwonyesha Ndugu Knorr akitoa hotuba, na nyingine ilionyesha ubatizo na Ndugu Knorr akiwapa waliobatizwa kitabu “Your Will Be Done on Earth.” Hatukuwa tumepokea kitabu hicho, lakini tulisoma kukihusu baadaye katika Mnara wa Mlinzi. Akinitazama usoni, mpelelezi huyo aliniuliza: “Kitabu hiki kinazungumzia nini? Kinazungumza kuhusu mfalme wa kaskazini na kitakachompata. Mashahidi wa Yehova wanawezaje kuwa walipanga mambo hayo bila msaada? Tunajua kwamba matukio kama hayo huhudhuriwa na wanajeshi Wamarekani ili wajifunze kutoka kwenu jinsi ya kupanga shughuli zao za kijeshi. Pia tunajua kwamba milionea mmoja alichanga pesa nyingi kwa ajili ya kusanyiko hilo. Mamilionea hawatupi-tupi pesa ovyo-ovyo!”
Huyo mpelelezi hakujua jinsi nilivyohisi wakati huo. Nilihisi ni kana kwamba nilihudhuria kusanyiko bila hata kutoka gerezani. Nilipata nguvu mpya. Nilihitaji sana kitu kama hicho! Na Yehova alinibariki kwa njia ya pekee. Sasa nilikuwa tayari kuendelea kuvumilia.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 214, 215]
Jumba Lilijaa Mashahidi wa Yehova
VENERA GRIGORYEVA
ALIZALIWA 1936
ALIBATIZWA 1994
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa mwigizaji katika miaka ya 1960 na aliigiza katika filamu ya propaganda ya Kisovieti. Tangu 1995, amekuwa painia wa kawaida huko St. Petersburg.
MNAMO 1960, mwanzoni mwa kazi yangu ya kuigiza, nilikuwa mhusika mkuu katika filamu inayoitwa God’s Witnesses, ambayo ilionyeshwa katika majumba ya sinema ya Muungano wa Sovieti. Filamu hiyo ilihusu “madhehebu hatari ya Mashahidi wa Yehova,” ambayo ilimuua mhusika mkuu, Tanya. Mimi ndiye niliyeigiza sehemu ya Tanya. Kulingana na filamu hiyo, Tanya anatoroka “madhehebu” hiyo usiku na kuingia kwenye dhoruba kali bila kuvaa koti. Akitokomea gizani, sauti fulani inasema kwa huzuni, “Huo ndio uliokuwa mwisho wa Tanya Veselova.” Nilipenda filamu hiyo na nilihisi ni pendeleo kujiunga na vita dhidi ya Mashahidi wa Yehova, ingawa sikujua chochote kuwahusu isipokuwa kile kilichoonyeshwa katika filamu hiyo.
Filamu hiyo ilionyeshwa katika majumba ya sinema na klabu za majiji mengi ya Muungano wa Sovieti. Nilikuwa nikienda kila mahali ilipokuwa ikionyeshwa na kila baada ya onyesho ningetokea jukwaani. Wakati huo, Wasovieti waliamini kabisa kila kitu walichoona kwenye sinema. Kwa hiyo kila mara nilipotokea, kila mtu alifurahi na kusema, “Kumbe bado yuko hai!” Kisha ningewaeleza jinsi filamu hiyo ilivyoundwa na jinsi msimamizi na watu wa kuongeza mbwembwe walivyotengeneza dhoruba kali, ambayo ilionekana ni kama inanisukuma kwenye bonde fulani na kunifunika na theluji.
Siku moja huko Vyshniy Volochek, katika Wilaya ya Kalinin (sasa Tver’), jumba lilikuwa limejaa, lakini jioni hiyo matukio yalikuwa tofauti na yale ya kawaida. Baada ya filamu mzee mmoja aliniuliza maswali kuhusu dini, nami nikashikilia msimamo wa kwamba hakuna Mungu hasa kuhusiana na suala la jinsi uhai ulivyoanza duniani. Hakuna mtu aliyesema chochote kuhusu filamu yenyewe. Nilirudi nyuma ya pazia na kumuuliza msimamizi, “Nilikuwa nikizungumza na nani sasa hivi?”
Alinijibu, “Huyo ni mkuu wa madhehebu ya Mashahidi wa Yehova. Jumba limejaa Mashahidi wa Yehova, hakuna mtu mwingine yeyote.” Hivyo ndivyo nilivyokutana na Mashahidi wa Yehova bila kujua. Baada ya hapo, nilitaka kusoma Biblia lakini sikuipata. Niliolewa na Mpolandi na nikahamia Poland pamoja naye. Mnamo 1977, dada wawili walibisha mlango wetu, na muda si muda nilianza kujifunza Biblia nao. Nilikuja kukipenda sana kitabu hicho, na Mashahidi wakawa marafiki wetu. Mnamo 1985, baba yangu alikuwa mgonjwa na hivyo mimi na mume wangu tukaenda Leningrad (sasa St. Petersburg) kumtunza. Nilisali kwa Yehova anisaidie kukutana na Mashahidi wa Yehova huko.
Mwishowe, nikawa Shahidi wa Yehova. Nimekuwa painia wa kawaida kwa miaka 12 sasa, na mume wangu Zdzisław, ni mtumishi wa huduma katika kutaniko la St. Petersburg.
Ninajua kupitia mambo niliyoona kwamba filamu zinaweza kuwaongoza watu wengi vibaya “kwa njia ya ujanja katika kutunga kosa.” (Efe. 4:14) Nilipokuwa nikiigiza katika filamu hiyo iliyokuwa na propaganda ya Kisovieti, sikufikiria kwamba miaka 30 baadaye ningekuwa Shahidi wa Yehova.
[Sanduku katika ukurasa wa 237]
Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Katika Kirusi
Kwa zaidi ya karne moja, Mashahidi wa Yehova wametumia tafsiri kadhaa za Biblia za Kirusi. Moja ni ile ya Sinodi. Ingawa inatumia lugha ya kale na haitumii jina la Mungu mara nyingi, imesaidia maelfu ya wasomaji Warusi kuelewa kusudi la Mungu. Pia, tafsiri ya Makarios ambayo ina jina la Mungu mara 3,000 hivi, imetumiwa sana. Lakini kadiri Mashahidi huko Urusi walivyoongezeka, ndivyo uhitaji wa tafsiri ya Biblia iliyo sahihi, wazi, na ya kisasa ulivyoongezeka.
Baraza Linaloongoza lilipanga Tafsiri ya Ulimwengu Mpya itafsiriwe katika Kirusi. Kwa zaidi ya miaka kumi, ndugu katika ofisi ya tawi ya Urusi walijitahidi sana katika kazi hiyo kubwa.
Mnamo 2001, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kirusi ilitolewa. Mnamo 2007, wasomaji Warusi ulimwenguni pote walifurahi kupokea chapa kamili ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kirusi. Washiriki wa Baraza Linaloongoza walitangaza kutolewa kwake katika majiji mawili. Theodore Jaracz alitoa tangazo hilo huko St. Petersburg na Stephen Lett akafanya hivyo huko Moscow. Makofi yenye shangwe yalifuata. Watu walisisimuka sana. Dada mmoja aliandika hivi, “Lugha yake ni rahisi, na yenye kueleweka kabisa. Sasa inafurahisha zaidi kusoma Maandiko Matakatifu.” Watu wengi walisema hivi kwa uthamini: “Ni zawadi bora kama nini kutoka kwa Yehova!” na “Tafadhali pokeeni shukrani zetu za kutoka moyoni.” Bila shaka, kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kirusi ni tukio muhimu kwa Warusi wote wanaopenda kweli popote walipo.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 244, 245]
Matatizo Yetu Yalitatuliwa Kwa Siku Moja
IVAN NA NATALIA SLAVA
WALIZALIWA Ivan 1966 na Natalia 1969
WALIBATIZWA 1989
MAELEZO MAFUPI KUWAHUSU Wakiwa mapainia, walihamia eneo lililokuwa na uhitaji mkubwa. Sasa Ivan anatumika katika Halmashauri ya Tawi ya Urusi.
MIMI na Natalia tuliamua kutoka Ukrainia na kuhamia Urusi mapema katika miaka ya 1990. Katika Wilaya ya Belgorod, ambayo ilikuwa na watu milioni moja na nusu hivi, kulikuwa na wahubiri wasiozidi kumi. Hakukuwa na shaka kwamba katika eneo hili “mavuno [yalikuwa] mengi, lakini wafanyakazi [walikuwa] wachache.”—Mt. 9:37.
Tulikuwa tumetoka tu kuoana na tulihitaji kutafuta kazi, ili kujitegemeza. Hata hivyo, hali ya kiuchumi nchini ilizidi kuzorota na watu wengi walipoteza kazi zao. Ili watu wapate chakula, serikali iliwapa tikiti katika sehemu zao za kazi. Kwa kuwa hatukuwa na kazi, hatukupata tikiti. Kwa hiyo, tulihitaji kulipa pesa nyingi ili kununua chakula sokoni. Pia hatukufaulu kupata nyumba na ikatubidi tuishi hotelini. Baada ya kulipia chumba chetu kwa siku 20, tulibaki na pesa kidogo sana. Tulisali kila siku ili Yehova atusaidie tupate kazi na nyumba ya bei ya chini. Wakati huo wote, tulikuwa tukihubiri kwa bidii na kuwatafuta watu wanyofu. Siku ya mwisho ya kukaa hotelini ikafika. Tulinunua mkate na maziwa kwa pesa tulizokuwa tumebakisha. Tulipolala usiku huo, tulimwomba Yehova tena atusaidie tupate kazi na mahali pa kuishi kwani siku iliyofuata tulipaswa kuhama hoteli hiyo.
Asubuhi tuliamshwa na sauti ya simu ikilia. Tulishangaa msimamizi wa hoteli alipotuambia kwamba binamu yangu alikuwa akiningoja sebuleni. Binamu yangu alinipa pesa, akisema kwamba alikuwa amelipwa pesa za ziada kando ya mshahara wake na alitaka kunigawia. Lakini si hayo tu. Baada ya dakika chache, ndugu fulani alitupigia simu na kusema kwamba amepata mahali pa kuishi pa bei nafuu. Isitoshe, siku hiyohiyo tulipata kazi ya kutunza bustani ya shule fulani. Hivyo katika siku moja, matatizo yetu yalitatuliwa. Tulikuwa na pesa kidogo, mahali pa kuishi, na kazi. Hatukuwa na shaka kwamba Yehova alisikia sala zetu.
Mnamo 1991, watu 55 walihudhuria Ukumbusho huko Belgorod; mwaka mmoja baadaye watu 150 wakahudhuria. Mwaka uliofuata watu 354 wakahudhuria. Kufikia 2006, jiji hilo lilikuwa na makutaniko sita, na kulikuwa na wahubiri zaidi ya 2,200 katika Wilaya ya Belgorod.
[Sanduku katika ukurasa wa 250]
Mambo ya Kisheria ya Karibuni
Mnamo Januari 2007, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR) ilitetea haki yetu ya kuabudu bila kuvurugwa na serikali ilipotoa hukumu nzuri ikisema hivi: “Inajulikana kwamba Mashahidi wa Yehova huabudu na kufundisha kupitia kujifunza na kuzungumzia mafundisho ya kidini wakiwa kikundi.”
Ingawa kazi yao iliwekewa vizuizi vya kisheria jijini Moscow mnamo 2004, ndugu zetu wanaendelea kukusanyika bila kujificha na kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Mnamo 2007, walifurahi sana kuadhimisha Ukumbusho na kufanya makusanyiko ya wilaya huko Moscow bila kusumbuliwa. Hali iko hivyo katika sehemu nyingine nchini Urusi.
Ingawa kuna matatizo ya kisheria, ndugu zetu wanaendelea kwa ujasiri kujitetea kisheria wanapokabili upinzani. Kwa mfano, kesi mpya iliwasilishwa katika Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu, dhidi ya Idara ya Polisi ya Lyublino kwa kuvuruga maadhimisho ya Ukumbusho huko Moscow Aprili 12, 2006. Polisi waliwafunga ndugu 14 na kumtisha mwanasheria wao kwa kisu. Ingawa mahakama ya eneo hilo ilitoa hukumu nzuri, uamuzi huo ulibatilishwa na mahakama kuu ya nchi hiyo na kesi ikatupiliwa mbali walipokata rufani. Pia, malalamiko yaliwasilishwa mnamo Julai 2007 dhidi ya maofisa wa serikali waliofanya uchunguzi wa muda mrefu na usiohitajiwa kuhusu utendaji wetu wa kidini huko St. Petersburg.
[Chati/Picha katika ukurasa wa 228-230]
MFUATANO WA MATUKIO—Urusi
1890
1891 Kwa kuhubiri kwa ujasiri, Semyon Kozlitsky anapelekwa uhamishoni katika sehemu ya mashariki ya Milki ya Urusi.
1904 Tawi la Ujerumani linapokea barua kutoka Urusi zikionyesha uthamini kwa kupata vichapo vya Biblia.
1910
1913 Serikali ya Urusi inaitambua ofisi ya Wanafunzi wa Biblia huko Finland, ambayo wakati huo ilikuwa sehemu ya Milki ya Urusi.
1923 Watch Tower Society inaanza kupokea barua nyingi za kuomba vichapo vitumwe Urusi.
1928 Huko Moscow, George Young anapeleka ombi la kuruhusu utendaji wa Wanafunzi wa Biblia nchini Urusi. Wenye mamlaka wanakataa kuongeza muda wa visa yake.
1929 Mkataba unatiwa sahihi pamoja na wasimamizi wa stesheni moja ya redio huko Tallinn, Estonia. Hotuba za Biblia zinasikiwa redioni huko Leningrad na katika majiji mengine.
1930
1939-1940 Muungano wa Sovieti wateka jamhuri za Ukrainia, Moldova, na Baltiki. Kwa hiyo, maelfu ya Mashahidi wa Yehova wanajikuta ndani ya mipaka ya Urusi.
1944 Mamia ya Mashahidi wafungwa gerezani na katika kambi za kazi ngumu kotekote Urusi.
1949 Mashahidi wa Yehova wa Moldova wapelekwa uhamishoni Siberia na Mashariki ya Mbali.
1950
1951 Zaidi ya Mashahidi 8,500 kutoka magharibi mwa Ukrainia, Belarus, Latvia, Lithuania, na Estonia wanapelekwa uhamishoni Siberia.
1956/1957 Wajumbe katika makusanyiko 199 ya wilaya ulimwenguni pote wanaiomba serikali ya Sovieti iruhusu uhuru wa kidini.
Mwishoni mwa miaka ya 1950 Mashahidi zaidi ya 600 wanatengwa katika kambi maalumu za kazi ngumu huko Mordvinia.
1965 Serikali ya Sovieti inatoa agizo la kuwaachilia Mashahidi waliopelekwa uhamishoni Siberia. Mashahidi hao wanahamia maeneo mengine nchini Urusi.
1970
1989-1990 Washiriki wa Baraza Linaloongoza wanakutana na akina ndugu nchini Urusi kwa mara ya kwanza. Mashahidi kutoka USSR wanasafiri kwenda Poland kwa ajili ya makusanyiko ya pekee.
1990
1991 Machi 27, Mashahidi wa Yehova wanaandikishwa kisheria nchini Urusi.
1992/1993 Makusanyiko ya kimataifa yanafanywa huko St. Petersburg na Moscow.
1997 Tawi la Urusi katika kijiji cha Solnechnoye, karibu na St. Petersburg, linawekwa wakfu.
1999 Jumba la Kusanyiko la kwanza nchini Urusi linawekwa wakfu huko St. Petersburg.
2000
2003 Upanuzi wa tawi unamalizika.
2007 Makutaniko na vikundi zaidi ya 2,100 vya wahubiri vinafanya kazi kwa bidii nchini Urusi.
[Grafu]
Jumla ya Wahubiri
Jumla ya Mapainia
Jumla ya Wahubiri
Jumla ya Mapainia
Jumla ya wahubiri katika nchi 15 zilizokuwa nchini ya Muungano wa Sovieti.
360,000
300,000
240,000
180,000
120,000
60,000
40,000
20,000
1890 1910 1930 1950 1970 1990 2000
[Mchoro/Ramani katika ukurasa wa 218]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Matawi mengine yamesaidia kusafirisha vichapo nchini kote
UJERUMANI FINLAND
↓ ↓
Solnechnoye
↓ ↓ ↓ ↓
BELARUS KAZAKHSTAN MOSCOW URUSI
JAPANI
↓
Vladivostok
↓
KAMCHATKA
[Ramani katika ukurasa wa 116, 117]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
MZINGO WA AKTIKI
BAHARI YA AKTIKI
Ncha ya Kaskazini
Bahari ya Barents
Bahari ya Kara
Bahari ya Laptev
Bahari ya Siberia Mashariki
Bahari ya Chukchi
Mng.-B. wa Bering
SWEDEN
NORWAY
DENMARK
COPENHAGEN
UJERUMANI
POLAND
Lodz
WARSAW
Bahari ya Baltiki
FINLAND
ESTONIA
LATVIA
LITHUANIA
BELARUS
Brest
UKRAINIA
L’viv
MOLDOVA
Bahari ya Kaspiani
KAZAKHSTAN
ASTANA
Kengir
UZBEKISTANI
TASHKENT
Angren
CHINA
MONGOLIA
ULAANBAATAR
CHINA
Bahari ya Japani
JAPANI
TOKYO
Hokkaido
Bahari ya Okhotsk
Bahari ya Bering
URUSI
Petrozavodsk
St. Petersburg
Solnechnoye
Kaliningrad
Novgorod
Vyshniy Volochek
MOSCOW
Tula
Orel
Kursk
Voronezh
Udarnyy
Vladimir
Ivanovo
Nizhniy Novgorod
Syktyvkar
Ukhta
Pechora
Inta
Novaya Zemlya
Vorkuta
MIL. YA URAL
SIBERIA
Yekaterinburg
Naberezhnye Chelny
Izhevsk
Saratov
Volzhskiy
Stavropol’
Pyatigorsk
Ml. El’brus
Nal’chik
Nartkala
Beslan
Vladikavkaz
MIL. YA CAUCASUS
Astrakhan
Mto Volga
Tomsk
Novosibirsk
Kemerovo
Krasnoyarsk
Novokuznetsk
Ust’-Kan
Aktash
Biryusinsk
Oktyabr’skiy
Bratsk
Vikhorevka
Tulun
Khazan ya Kati
Zima
Zalari
Usol’ye-Sibirskoye
Kitoy
Angarsk
Irkutsk
Ziwa Baikal
Kirensk
Khabarovsk
Vladivostok
Korsakov
Yuzhno-Sakhalinsk
Sakhalin
Yakutsk
Oymyakon
Ust’-Nera
Kamchatka
Rasi ya Chukchi
Mto Kolyma
Khayyr
Noril’sk
[Ramani katika ukurasa wa 167]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Bahari ya Kaspiani
Bahari ya Baltiki
Bahari ya Barents
Bahari ya Kara
BAHARI YA AKTIKI
Ncha ya Kaskazini
Bahari ya Laptev
Bahari ya Siberia Mashariki
Bahari ya Chukchi
Mlango-Bahari wa Bering
Bahari ya Okhotsk
Bahari ya Japani
KAZAKHSTAN
CHINA
MONGOLIA
MURMANSK
PSKOV
TVER’
MOSCOW
BELGOROD
VORONEZH
ROSTOV
KABARDINO-BALKARIA
ALANIA
IVANOVO
NIZHEGOROD
MORDVINIA
ULYANOVSK
VOLGOGRAD
TATARSTAN
PERM’
JAM. YA KOMI
MIL. YA URAL
SIBERIA
SVERDLOVSK
CHELYABINSK
KURGAN
TYUMEN’
OMSK
TOMSK
NOVOSIBIRSK
ALTAI
JAM. YA ALTAI
KEMEROVO
JAM. YA KHAKASSIA
KRASNOYARSK
JAM. YA TUVA
IRKUTSK
BURYATIA
CHITA
JAM. YA SAKHA
AMUR
KHABAROVSK
PRIMORSKIY KRAY
SAKHALIN
KAMCHATKA
[Picha katika ukurasa wa 66]
Macheo kwenye Rasi ya Chukchi
[Picha katika ukurasa wa 68]
Kibao hiki kilichoandikwa katika Kikazakh na Kirusi, kinaelekeza kwenye kijiji cha Bukhtarma, Siberia ambako Semyon Kozlitsky alipelekwa uhamishoni
[Picha katika ukurasa wa 71]
Akina Herkendell walienda Urusi baada ya arusi yao ili wawasaidie watu waliozungumza Kijerumani
[Picha katika ukurasa wa 74]
Cheti cha mamlaka ya uwakilishi alichopewa Kaarlo Harteva (kulia) ambacho Mwakilishi wa Milki ya Urusi huko New York aliweka muhuri wa serikali
[Picha katika ukurasa wa 80]
Mei 1925, kusanyiko hili la wilaya katika Kirusi huko Carnegie, Pennsylvania, lilihudhuriwa na watu 250, na 29 wakabatizwa
[Picha katika ukurasa wa 81]
Gazeti hili lilitangaza hivi: “Wilaya ya Voronezh imejaa madhehebu”
[Picha katika ukurasa wa 82]
George Young
[Picha katika ukurasa wa 84]
Kwa karibu miaka kumi, Aleksandr Forstman alitafsiri trakti, vijitabu, na vitabu katika Kirusi
[Picha katika ukurasa wa 90]
Regina na Pyotr Krivokulsky, mnamo 1997
[Picha katika ukurasa wa 95]
Olga Sevryugina alikuwa mtumishi wa Yehova kwa sababu ya barua za Pyotr zilizofungwa kwa jiwe
[Picha katika ukurasa wa 100]
Ivan Krylov
[Picha katika ukurasa wa 101]
Mashahidi waliohamishwa walijijengea nyumba huko Siberia
[Picha katika ukurasa wa 102]
Magdalina Beloshitskaya na familia yake walipelekwa uhamishoni Siberia
[Picha katika ukurasa wa 110]
Viktor Gutshmidt
[Picha katika ukurasa wa 115]
Alla mnamo 1964
[Picha katika ukurasa wa 118]
Picha ya karibuni ya Semyon Kostylyev
[Picha katika ukurasa wa 120]
Vladislav Apanyuk alivumilia majaribu kwa sababu ya kujifunza Biblia
[Picha katika ukurasa wa 121]
Polisi walipata kijitabu hiki, “After Armageddon—God’s New World,” nyumbani kwa Nadezhda Vishnyak
[Picha katika ukurasa wa 126]
Boris Kryltsov
[Picha katika ukurasa wa 129]
Viktor Gutshmidt na dada yake (juu), binti zake, na mke wake, Polina, mwezi mmoja hivi kabla ya kukamatwa mnamo 1957
[Picha katika ukurasa wa 134]
Ivan Pashkovsky
[Picha katika ukurasa wa 136]
Mnamo 1959, gazeti “Crocodile” lilichapisha picha ya vichapo hivi vilivyokamatwa katika rundo la nyasi kavu
[Picha katika ukurasa wa 139]
Chini ya nyumba hii kulikuwa na mashini za kuchapishia zilizogunduliwa na KGB mwaka wa 1959
[Picha katika ukurasa wa 142]
Aleksey Gaburyak alisaidia kuwaunganisha wale waliokuwa wametawanyika
[Picha katika ukurasa wa 150]
Mashini ya Kuchapishia Iliyotengenezwa Mtaani
Mashini ya kuchapishia aina ya Rotary
Mtambo wa kutengeneza karatasi
Mashini ya kukatia karatasi
Stepla
[Picha katika ukurasa wa 151]
Stepan Levitsky, dereva wa tramu ambaye kwa ujasiri aliongea na mchapishaji
[Picha katika ukurasa wa 153]
Grigory Gatilov aliwahubiria wengine katika seli yake
[Picha katika ukurasa wa 157]
Maua marefu yalikuwa mahali pa kujificha kwa ajili ya mazungumzo na funzo la Biblia
[Picha katika ukurasa wa 161]
Ukubwa halisi wa gazeti la “Mnara wa Mlinzi” lililotengenezwa kuwa kijitabu kidogo
[Picha katika ukurasa wa 164]
“Uamuzi wa Kamati Maalumu ya Kudumu ya Muungano wa Sovieti”
[Picha katika ukurasa wa 170]
Akina ndugu walificha “hazina” kwenye sanduku hili la nguo lenye mifuko ya ndani au kwenye soli za ndani za viatu
[Picha katika ukurasa wa 173]
Ivan Klimko
[Picha katika ukurasa wa 175]
Kasha dogo la kiberiti lingeweza kuwekwa nakala tano au sita za “Mnara wa Mlinzi” zilizoandikwa kwa mwandiko mdogo
[Picha katika ukurasa wa 184, 185]
Miaka yote waliyokuwa katika kambi moja huko Mordvinia, hakuna ndugu aliyekosa Ukumbusho
[Picha katika ukurasa wa 194]
Nikolai Gutsulyak alimhubiria mke wa kamanda wa kambi
[Picha katika ukurasa wa 199]
Makusanyiko ya Kimataifa
Mnamo 1989, wajumbe kutoka Urusi walihudhuria makusanyiko matatu ya kimataifa huko Poland
Warsaw
Chorzow
Poznan
[Picha katika ukurasa wa 202]
Baada ya kuandikishwa rasmi, kutoka kushoto hadi kulia: Theodore Jaracz, Michael Dasevich, Dmitry Livy, Milton Henschel, mfanyakazi katika wizara ya haki, Anany Grogul, Aleksey Verzhbitsky, na Willi Pohl
[Picha katika ukurasa wa 205]
Milton Henschel akitoa hotuba kwenye Kusanyiko la Kimataifa la 1992 la “Wachukuaji Nuru” katika Uwanja wa Kirov, St. Petersburg
[Picha katika ukurasa wa 206]
Majengo yalinunuliwa huko Solnechnoye, Urusi
[Picha katika ukurasa wa 207]
Aulis na Eva Lisa Bergdahl walikuwa kati ya wajitoleaji wa kwanza kufika Solnechnoye
[Picha katika ukurasa wa 208]
Hannu na Eija Tanninen walipewa mgawo huko St. Petersburg
[Picha katika ukurasa wa 210]
Roman Skiba na mkewe Lyudmila, walisafiri mwendo mrefu akiwa mwangalizi wa wilaya
[Picha katika ukurasa wa 220]
Akina ndugu wakishughulikia vichapo bandarini huko Vladivostok
[Picha katika ukurasa wa 224]
Arno na Sonja Tüngler wamefurahia mapendeleo mengi katika mgawo wao Urusi
[Picha katika ukurasa wa 226, 227]
Kutaniko likifanya mkutano katika msitu karibu na St. Petersburg, 1989
[Picha katika ukurasa wa 238]
Ofisi ya tawi ya Urusi husimamia kazi ya kutafsiri vichapo katika lugha zaidi ya 40
[Picha katika ukurasa wa 243]
Shule ya Utumishi wa Painia ya kwanza kufanywa St. Petersburg, Juni 1996
[Picha katika ukurasa wa 246]
Kuhubiri huko Urusi
Kuhubiri katika Wilaya ya Perm’ na Nartkala
Mahubiri ya barabarani huko St. Petersburg
Mahubiri ya nyumba kwa nyumba huko Yakutsk
Kuhubiri katika masoko huko Saratov
[Picha katika ukurasa wa 252, 253]
Ofisi ya Tawi ya Urusi
Picha iliyopigwa kutoka angani ya majengo ya makazi na bustani
[Picha katika ukurasa wa 254]
Wajumbe 23,537 walihudhuria kusanyiko la wilaya la 2006 huko Moscow
[Picha katika ukurasa wa 254]
Uwanja wa Michezo wa Luzhniki