Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ni Wakati Gani Ambapo Mtu Anakuwa Amepita Mipaka?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 4

      Ni Wakati Gani Ambapo Mtu Anakuwa Amepita Mipaka?

      Kweli au si kweli . . .

      Ni kosa kwa watu wawili walio na urafiki wa kimapenzi kushikana katika hali yoyote ile.

      □ Kweli

      □ Si kweli

      Watu wawili wanaweza kuwa na hatia ya uasherati hata ikiwa hawajafanya ngono.

      □ Kweli

      □ Si kweli

      Wapenzi wasipofanya mambo kama vile kubusiana na kukumbatiana, basi hawapendani kikweli.

      □ Kweli

      □ Si kweli

      HAPANA shaka umefikiria jambo hilo sana. Kwa kweli, ikiwa uko katika urafiki wa kimapenzi, inaweza kuwa vigumu kujua mipaka ambayo unapaswa kuweka kuhusu kuonyeshana mahaba. Acheni tuzungumzie taarifa tatu zilizo juu na tuone jinsi Neno la Mungu linavyotusaidia kujibu swali hili, “Ni wakati gani ambapo mtu anakuwa amepita mipaka?”

      ● Ni kosa kwa watu wawili walio na urafiki wa kimapenzi kushikana katika hali yoyote ile.

      Si kweli. Biblia haikatazi kuonyeshana mahaba kwa njia iliyo safi. Kwa mfano, Biblia inazungumzia kisa cha msichana Mshulami na mvulana mchungaji waliopendana. Uchumba wao ulikuwa safi. Hata hivyo, inaonekana kwamba walionyeshana mahaba kwa njia fulani kabla ya kufunga ndoa. (Wimbo wa Sulemani 1:2; 2:6; 8:5) Leo watu wawili wanaofikiria kwa uzito kufunga ndoa wanaweza kuhisi kwamba hakuna ubaya kuonyeshana mahaba katika njia fulani safi.a

      Hata hivyo, watu wawili wenye urafiki wa kimapenzi wanapaswa kuwa waangalifu sana. Kubusiana, kukumbatiana, au kufanya jambo lolote linaloamsha tamaa ya ngono kunaweza kuongoza katika mwenendo mpotovu kingono. Ni rahisi sana hata kwa watu wawili ambao hawana nia mbaya kupoteza usawaziko na kutumbukia katika upotovu wa kingono.—Wakolosai 3:5.

      ● Watu wawili wanaweza kuwa na hatia ya uasherati hata ikiwa hawajafanya ngono.

      Kweli. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “uasherati” (por·neiʹa) lina maana pana. Linatia ndani mahusiano yote ya ngono nje ya ndoa na linakazia matumizi yasiyofaa ya viungo vya uzazi. Hivyo, zaidi ya kufanya ngono, uasherati unatia ndani matendo kama vile kumpiga mtu mwingine punyeto, iwe ni mwanamume au mwanamke, na pia ngono ya kinywa na ulawiti au ufiraji.

      Isitoshe, zaidi ya kushutumu uasherati, Biblia inashutumu mambo mengine pia. Mtume Paulo aliandika: “Matendo ya mwili ni wazi, nayo ni uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu.” Kisha akaongeza: “Wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”—Wagalatia 5:19-21.

      “Uchafu,” au “ukosefu wa usafi,” ni nini? Neno la Kigiriki linatia ndani uchafu wa kila namna, iwe ni katika maneno au matendo. Kwa kweli, ni tendo chafu kuingiza mikono ndani ya nguo za mtu, kumvua mtu nguo, au kumpapasa-papasa mtu sehemu za siri, kama vile matiti. Katika Biblia kuyapapasa matiti kunahusianishwa na shangwe inayopaswa kufurahiwa tu na watu wawili waliofunga ndoa.—Methali 5:18, 19.

      Vijana fulani wanakaidi viwango vya Mungu. Wanapita mipaka kimakusudi, au wanatafuta kwa pupa watu mbalimbali wanaoweza kushiriki pamoja nao uchafu wa kingono. Vijana hao wanaweza kuwa na hatia ya kile ambacho mtume Paulo alikiita “mwenendo mpotovu.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mwenendo mpotovu” linamaanisha ‘matendo ya kupita kiasi, ya kupindukia, ufidhuli, uchu usiozuilika.’ Bila shaka hungependa kufikia hatua ya “kuishiwa na ufahamu wote” kwa kujitoa mwenyewe ili kuwa na “mwenendo mpotovu na kufanya ukosefu wa usafi wa kila namna kwa pupa.”—Waefeso 4:17-19.

      ● Wapenzi wasipofanya mambo kama vile kubusiana na kukumbatiana, basi hawapendani kikweli.

      Si kweli. Tofauti na maoni ya watu fulani, kufanya mambo kama vile kubusiana na kukumbatiana hakuzidishi urafiki. Badala yake, kunafanya watu wasiheshimiane wala kuaminiana. Fikiria kisa cha Laura. “Siku moja wakati mama yangu hakuwapo, mpenzi wangu alikuja nyumbani eti ili kutazama televisheni,” anasema. “Mwanzoni alinishika mkono tu. Kisha, akaanza kunipapasa-papasa. Niliogopa kumwambia aache; nilidhani kwamba atakasirika na kuondoka.”

      Una maoni gani? Je, mpenzi wa Laura alimjali kikweli, au alitaka tu kutosheleza tamaa yake? Je, mtu anayejaribu kukuingiza katika mwenendo mchafu anakupenda kweli?

      Mvulana anapomchochea msichana kukaidi mazoezi yake ya Kikristo na dhamiri yake, anavunja sheria ya Mungu na hapaswi kudai kwamba anampenda msichana huyo kikweli. Vilevile, msichana anayekubali, anajiachilia atumiwe vibaya. Zaidi ya yote, msichana huyo ameshiriki tendo chafu—pengine hata uasherati.b—1 Wakorintho 6:9, 10.

      Weka Mipaka Iliyo Wazi

      Ikiwa mna urafiki wa kimapenzi, mnaweza kufanya nini ili mwepuke kuonyeshana mahaba kwa njia zisizofaa? Njia ya hekima ni kuweka mipaka iliyo wazi mapema. Andiko la Methali 13:10 linasema: “Wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.” Hivyo, zungumza na mpenzi wako kuhusu njia zinazofaa za kuonyeshana mahaba. Kujaribu kuweka mipaka baada ya tamaa kuwaka ni kama kuweka king’ora cha moto katika nyumba baada ya nyumba hiyo kushika moto.

      Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kuzungumzia mambo hayo—hata linaweza kuwa jambo lenye kuaibisha—hasa mwanzoni mwa uchumba. Lakini kuweka mipaka kunaweza kusaidia sana kuzuia matatizo makubwa yasitokee baadaye. Mipaka inayowekwa kwa hekima ni kama vifaa vya kutambua moshi ambavyo vinawasha king’ora mara tu vinapotambua dalili ya moto. Isitoshe, kufaulu kwenu kuzungumzia mambo hayo kunaweza kuonyesha pia ikiwa urafiki wenu utafanikiwa. Kwa hakika, kujizuia, subira, na kutokuwa na ubinafsi ndio msingi wa mahusiano mazuri ya ngono katika ndoa.—1 Wakorintho 7:3, 4.

      Kusema kweli, kushikamana na viwango vya Mungu si rahisi. Lakini unaweza kutegemea mashauri ya Yehova. Katika Isaya 48:17, Yehova anasema kwamba yeye ndiye “Anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake.” Yehova anakutakia kila la heri!

      PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 24

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Kuwa bikira si kasoro. Badala yake, kutunza ubikira ndilo jambo la hekima. Pata kujua ni kwa nini.

      [Maelezo ya Chini]

      a Katika sehemu fulani za ulimwengu, watu ambao hawajafunga ndoa wanapoonyeshana mahaba mbele ya watu, hilo huonwa kuwa jambo lisilofaa na lenye kuchukiza. Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu wasijiendeshe kwa njia inayoweza kuwakwaza wengine.—2 Wakorintho 6:3.

      b Bila shaka, mambo yanayozungumziwa katika fungu hili yanawahusu watu wa jinsia zote.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Upendo . . . haujiendeshi bila adabu.”—1 Wakorintho 13:4, 5.

      PENDEKEZO

      Fanyeni mambo mkiwa pamoja na wengine, au usisitize kuwe na mtu wa tatu. Epukeni hali hatari, kama vile kuwa peke yenu katika gari lililoegeshwa au katika nyumba au chumba.

      JE, WAJUA . . .?

      Ikiwa mnachumbiana, mnahitaji kuzungumzia mambo fulani ya siri. Lakini kuzungumzia mambo waziwazi mkiwa na kusudi la kuamsha tamaa ya ngono ni mojawapo ya mambo machafu —hata mambo hayo yakizungumziwa kupitia simu au ujumbe mfupi.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Ninaweza kuepuka kushawishiwa kutumbukia katika mwenendo usiofaa kwa ․․․․․

      Mpenzi wangu akijaribu kunishawishi nishiriki katika mwenendo mchafu, nita ․․․․․

      Maswali ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu jambo hili ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Ni mipaka gani ambayo unaweza kuweka kuhusu kuonyeshana mahaba na mtu wa jinsia tofauti?

      ● Eleza tofauti kati ya uasherati, uchafu, na mwenendo mpotovu.

      [Blabu katika ukurasa wa 46]

      Mimi na mchumba wangu tumesoma pamoja makala za Biblia zinazozungumzia jinsi ya kuendelea kuwa safi kiadili. Tunathamini jinsi ambavyo zimetusaidia kuendelea kuwa na dhamiri safi.’’—Leticia

      [Sanduku katika ukurasa wa 44]

      Namna Gani Ikiwa Tumepita Mipaka?

      Namna gani ikiwa umetumbukia katika mwenendo usiofaa? Usijidanganye kwa kufikiri kwamba unaweza kutatua tatizo hilo mwenyewe. Kijana mmoja alisema: “Nyakati nyingine ningesali hivi, ‘Tusaidie tusifanye hivyo tena.’ Nyakati nyingine kufanya hivyo kulisaidia, lakini nyakati fulani hakukusaidia.” Hivyo, zungumza na wazazi wako. Pia, Biblia inatoa shauri hili zuri: ‘Waite wanaume wazee wa kutaniko.’ (Yakobo 5:14) Wachungaji hao Wakristo wanaweza kukupa mashauri na karipio ili urekebishe uhusiano wako pamoja na Mungu.

      [Picha katika ukurasa wa 47]

      Je, ungeweka king’ora cha moto katika nyumba baada ya nyumba hiyo kushika moto? Basi msingoje mpaka wakati ambapo tamaa zenu zimewaka ndipo mjaribu kuweka mipaka kuhusu kuonyeshana mahaba

  • Kwa Nini Uendelee Kuwa Bikira?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 5

      Kwa Nini Uendelee Kuwa Bikira?

      “Kuna mkazo mwingi wa kufanya ngono.”—Kelly.

      “Ninahisi kana kwamba nina kasoro kwa kuwa bado mimi ni bikira.”—Jordon.

      “BADO wewe ni bikira?” Swali hilo linaweza kukushtua! Katika sehemu nyingi, kijana ambaye bado ni bikira anaweza kuonwa kuwa mtu wa ajabu au mwenye kasoro. Ndiyo sababu vijana wengi wanafanya ngono mapema maishani!

      Kuvutwa na Tamaa, Kusukumwa na Marika

      Ikiwa wewe ni Mkristo, unajua kwamba Biblia inakuambia ‘ujiepushe na uasherati.’ (1 Wathesalonike 4:3) Hata hivyo, huenda ikawa vigumu kwako kudhibiti tamaa zako za ngono. Kijana mmoja anayeitwa Paul anakiri hivi: “Nyakati nyingine, mimi huanza tu kufikiri kuhusu ngono bila sababu yoyote hususa.”

      Uwe na hakika kwamba hizo ni hisia za kawaida. Hata hivyo, kudhihakiwa na kusumbuliwa sikuzote kwa sababu ya kuwa bikira si jambo la kupendeza! Kwa mfano, namna gani marafiki wako wakikwambia kwamba wewe si mwanamume au mwanamke halisi ikiwa hujafanya ngono? “Marafiki huzungumzia ngono kana kwamba ni raha tupu na jambo la kawaida,” Ellen anasema. “Ikiwa hujihusishi na ngono unaonwa kuwa mshamba.”

      Lakini huenda marafiki wako wasikuambie matokeo ya kufanya ngono kabla ya ndoa. Kwa mfano, Maria ambaye alifanya ngono na mvulana aliyekuwa rafiki yake anakumbuka: “Baadaye nilifedheheka na kuona aibu. Nilijichukia na kumchukia mvulana huyo.” Hali kama hizo hutokea mara nyingi kuliko vijana wengi wanavyofikiri. Ukweli ni kwamba, kufanya ngono kabla ya ndoa mara nyingi hutokeza maumivu ya kihisia na madhara makubwa!

      Hata hivyo, msichana anayeitwa Shanda anauliza, “Kwa nini Mungu aliwapa vijana tamaa za ngono akijua kwamba hawapaswi kuzitosheleza kabla ya ndoa?” Hilo ni swali zuri. Lakini fikiria mambo yafuatayo:

      Je, tamaa za ngono tu ndizo hisia zenye nguvu unazopata? Hapana. Yehova Mungu alikuumba na uwezo wa kuwa na tamaa na hisia nyingi mbalimbali.

      Je, ni lazima utosheleze kila tamaa mara tu inapotokea? Hapana, kwa sababu Mungu alikupa pia uwezo wa kudhibiti matendo yako.

      Basi, tuseme nini? Huenda huwezi kuzuia tamaa fulani zisitokee, lakini unaweza kudhibiti matendo yako. Kwa hakika, kutosheleza tamaa yako ya ngono kila mara inapotokea ni kosa na ni kutotumia akili sawa tu na kumpiga mtu kila mara unapokuwa na hasira.

      Ukweli ni kwamba Mungu hakukusudia tutumie vibaya nguvu zetu za uzazi. Biblia inasema: “Kila mmoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe [au, mwili wake mwenyewe] katika utakaso na heshima.” (1 Wathesalonike 4:4) Kama vile kuna “wakati wa kupenda na wakati wa kuchukia,” vivyo hivyo kuna wakati wa kutosheleza tamaa za ngono na wakati wa kuepuka kufanya hivyo. (Mhubiri 3:1-8) Vyovyote vile, wewe tu ndiwe unayeweza kudhibiti tamaa zako!

      Lakini namna gani mtu akikudhihaki kwa kusema hivi kwa mshangao, “Eti bado wewe ni bikira?” Usiogope. Ikiwa mtu huyo anataka tu kukuaibisha, unaweza kusema: “Ndiyo, bado mimi ni bikira, na ninafurahia jambo hilo.” Au unaweza kusema, “Hilo ni jambo la kibinafsi ambalo silizungumzii na wengine.”a (Methali 26:4; Wakolosai 4:6) Kwa upande mwingine, huenda ukahisi kwamba mtu anayekuuliza swali hilo anahitaji kujua zaidi. Hivyo, unaweza kuamua kumweleza msimamo wako unaotegemea Biblia.

      Je, unaweza kufikiria njia nyingine za kujibu unapoulizwa hivi kwa dhihaka “Eti bado wewe ni bikira?” Ikiwa ndivyo, andika majibu hayo hapa chini.

      ․․․․․

      Zawadi Yenye Thamani

      Mungu anahisi jinsi gani watu wanapofanya ngono kabla ya ndoa? Wazia kwamba umemnunulia rafiki yako zawadi. Lakini kabla hata hujampa zawadi hiyo, anaifungua kwa sababu ya udadisi! Ungeudhika, sivyo? Wazia basi jinsi ambavyo Mungu angehisi ikiwa ungefanya ngono kabla ya ndoa. Anataka ungoje mpaka utakapofunga ndoa ili ufurahie zawadi ya ngono.—Mwanzo 1:28.

      Unapaswa kufanya nini kuhusu hisia zako za ngono? Jizoeze kuzidhibiti. Inawezekana! Mwombe Yehova akusaidie. Roho yake inaweza kuzidisha uwezo wako wa kujizuia. (Wagalatia 5:22, 23) Kumbuka kwamba Yehova “hatawanyima jambo lolote jema wale wanaotembea bila kosa.” (Zaburi 84:11) Kijana mmoja anayeitwa Gordon anasema: “Ninapoanza kufikiria kwamba hakuna ubaya wowote wa kufanya ngono kabla ya ndoa, ninakumbuka hatari za kiroho na kutambua kwamba uhusiano wangu na Yehova ni wenye thamani sana hivi kwamba siwezi kuruhusu uharibiwe na dhambi yoyote ile.”

      Ukweli ni kwamba kuwa bikira si jambo la kushangaza wala haimaanishi kwamba una kasoro. Kwa upande mwingine, upotovu katika ngono unasababisha aibu, kuvunjika moyo, na madhara mengine. Kwa hiyo, usiruhusu propaganda ya ulimwengu ikudanganye kufikiri kwamba una kasoro ukishikamana na viwango vya Biblia. Kwa kutunza ubikira wako, unatunza afya yako, hisia zako, na zaidi ya yote, uhusiano wako pamoja na Mungu.

      PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 24

      [Maelezo ya Chini]

      a Wakati mmoja, Yesu aliamua kunyamaza Herode alipomuuliza maswali. (Luka 23:8, 9) Mara nyingi hakuna haja ya kujibu maswali ya upuuzi.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Ikiwa yeyote . . . amefanya uamuzi huu katika moyo wake mwenyewe, kutunza ubikira wake mwenyewe, yeye atafanya vema.”—1 Wakorintho 7:37.

      PENDEKEZO

      Epuka kushirikiana na watu ambao hawafuati viwango vya juu vya maadili, hata wakidai kwamba wana imani kama yako.

      JE, WAJUA . . .?

      Ni vigumu sana kwa watu wenye mwenendo mpotovu kingono kuacha tabia hiyo eti kwa sababu wamefunga ndoa. Lakini kuna uwezekano mkubwa kwamba wale ambao ni washikamanifu kwa viwango vya Mungu vya maadili kabla ya kufunga ndoa watakuwa washikamanifu kwa wenzi wao baadaye.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Ikiwa ninataka kutunza ubikira mpaka nitakapofunga ndoa, ninahitaji ․․․․․

      Ikiwa rafiki zangu wanafanya iwe vigumu kushikilia azimio langu, nita ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Kwa maoni yako, unafikiri ni kwa nini watu huwadhihaki wale ambao ni mabikira?

      ● Kwa nini inaweza kuwa vigumu kutunza ubikira?

      ● Kuna faida gani za kutunza ubikira mpaka wakati utakapofunga ndoa?

      ● Ni jinsi gani unaweza kumweleza mdogo wako faida za ubikira?

      [Blabu katika ukurasa wa 51]

      “Mimi huepuka kishawishi cha kufanya ngono kwa kukumbuka sikuzote kwamba ‘hakuna mwasherati au mtu asiye safi aliye na urithi wowote katika ufalme wa Mungu.’’’ (Waefeso 5:5)—Lydia

      [Sanduku katika ukurasa wa 49]

      Ukurasa wa Mazoezi

      Ni Nini Hasa Kinachotokea Baadaye?

      Mara nyingi marafiki wako na burudani zinazopendwa wanatumia ujanja kuficha matokeo mabaya ya kufanya ngono kabla ya ndoa. Ona mambo matatu yanayofuata. Unafikiri ni nini hasa kitakachowapata vijana hawa?

      ● Mwanafunzi mmoja anajigamba kwamba amefanya ngono na wasichana wengi. Anasema kwamba ni raha na hakuna madhara yoyote. Ni nini hasa kitakachotokea baadaye—kwake na kwa wasichana hao? ․․․․․

      ● Sinema inaisha ikionyesha vijana wawili ambao hawajafunga ndoa wakifanya ngono ili kuonyeshana upendo. Ni nini kinachoweza kutokea baadaye kihalisi? ․․․․․

      ● Unakutana na mvulana mwenye sura ya kuvutia anayetaka ufanye ngono naye. Anakuambia kwamba hakuna mtu atakayejua. Ukikubali na kisha ujaribu kuficha jambo hilo, ni nini hasa kinachoweza kutokea baadaye? ․․․․․

      [Picha katika ukurasa wa 54]

      Kufanya ngono kabla ya ndoa ni kama kufungua zawadi kabla ya kukabidhiwa

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki