-
Kupuuza Maonyo na Kumtahini MunguMnara wa Mlinzi—1987 | Desemba 15
-
-
Kupuuza Maonyo na Kumtahini Mungu
Wala hata maji yalipoinuka kufika kwenye vifundo vya nyayo zao wao hawakutaka kukimbia.”—El País, Kolombia.
KICHWA hicho kutoka karatasi ya habari za kila siku ya Kolombia kilikazia moja ya sababu za upotevu mbaya sana wa uhai katika poromoko kubwa la maji na miamba yenye moto katika Armero Novemba 1985. Dora Elisa Rada Esguerra, mwendeshi mmoja wa mitambo ya simu katika Armero, kwa kutiwa chonjo na yale majivu yenye kuanguka na mto wenye kufurika, aliamua kukimbia. Ndipo yeye alipoonya wafanya-kazi wenzake mahali pa kubadilishia laini juu ya tanzia iliyokuwa ikija. Yeye alieleza hivi baadaye: “Wao waliona maji yale, ambayo yalikuwa . . . yakitiririka, kwa nguvu, kwa nguvu sana, lakini hata hivyo wao hawakusogea.” Dora alikimbia kutoka mji huo wenye kupatwa na angamizi.
Wale waendeshi-mitambo-ya-simu wengine walikufa pamoja na majeruhi wapatao 21,000 katika bubujiko la matope yenye moto, barafu, na mawe makubwa-makubwa ambayo yalinguruma yakibingirika chini kutoka ule mlima wenye kulipusha moto wa Nevado del Ruiz. Miongoni mwa wale waliofagiliwa mbali alikuwa meya wa mji ule na walio wengi kati ya jeshi la polisi wa hapo, kuonyesha kwamba ni kama hakuna mtu ye yote ambaye alichukua kwa uzito tisho hilo —mpaka ilipokuwa kuchelewa mno.
Kwa Sababu Gani Wao Hawakukimbia?
Kulikuwa na ishara na maonyo ya msiba uliokuwa ukikaribia. Kwa sababu gani watu wengi sana katika Armero waliyapuuza? Katika mahali pa kwanza, maonyo kutoka kwa maafisa yalikuja yakiwa yamechelewa, wakati ambapo msiba ulikuwa tayari ukipiga mji ule. Kabla ya hapo, watu walikuwa wameambiwa watulie, kwamba labda kungekuwa na furiko lakini halingekuwa jambo zito. Badala ya hivyo, mji ule ulifutwa kwa kuondolewa na ukuta mkubwa sana wa kifo ambao ulimiminika chini kwenye mto Lagunilla.
Inaelekea kuwa watu fulani hawakutaka kuacha makao yao na miliki zao, wakijua kwamba baada ya muda mfupi wachukua nyara wangenyemelea na kuiba. Jambo hilo liligeuka kuwa tisho halisi. Waporaji kadha walipigwa risasi na jeshi. Watu fulani ambao waliokoka msiba ule walirudi kwenye makao yao yaliyofurikishwa wakakuta kwamba kufuli zilikuwa zimepigwa risasi zikang’olewa milangoni na vitu vyenye thamani vikawa vimeibwa. Lakini walio wengi wa wanamji hawakuishi muda mrefu kutosha ili waweze kurudi kwenye makao yao. Na katika visa vilivyo vingi, hakukuwa na makao ya kurudia.
Labda watu fulani walihisi kwamba Mungu au yule bikira Mariamu angejitia katika jambo hilo kwa niaba yao. Hata hivyo, je! ni jambo la kiakili kutazamia Mungu ajitie leo kwa niaba ya watu fulani wakati misiba ya kiasili inapotokea? Kwa sababu gani watu fulani waokolewe na hatua ya kujitia kwa Mungu katika mambo yao na wengine, walio katika hali kama hizo, waruhusiwe kuangamia?
Je! kuna msingi imara kwa mtu kuwa na itikadi kwamba yeye anaweza kuishi maisha yaliyotiwa hirizi ya kuwa na himaya maalum kutoka kwa Mungu? Mathalani, je! dreva wa gari anaweza kutumaini katika “malaika mlinzi” wake au “mtakatifu” ambaye yeye anampenda zaidi? Wakatoliki wengi mno wenye mioyo myeupe walio na medali kubwa-kubwa za “Mtakatifu” Christopher wamekufa katika aksidenti za magari kuonyesha kwamba jambo hilo haliaminiki. Au je! Mkristo anapaswa kuwa na itikadi ya kwamba yeye ana himaya maalum ya Mungu wakati anaposafiri katika ndege? Namna gani, juu ya himaya maalum wakati anaposhiriki katika mchezo fulani hatari? Je! ni jambo la kiakili kutahini Mungu katika hali hizo?
Mkono wa Yehova Si Mfupi
Maandiko yanatusaidia kuona kwamba kuna hali ambazo katika hizo Yehova Mungu angeweza kujitia katika mambo kwa niaba ya watu wake wakati kule kuhubiri habari njema za Ufalme kunapoathiriwa au wakati kundi lake linapotishwa. Nabii Isaya anatuhakikishia hivi: “Tazama, mkono wa BWANA [Yehova, NW] haukupunguka, hata usiweze kuokoa; wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia.”—Isaya 59:1.
Biblia inatoa vielelezo vya wazi juu ya mkono wa Yehova wenye kutoa himaya kuhusiana na mitume. Mfalme Herode, akiwa amejiondokea akajipatia upendeleo wa Wayahudi, aliagiza Petro atiwe gerezani chini ya ulinzi mkali. Kundi katika Yerusalemu lilisali kwa bidii sana kwa ajili yake. Ni jambo gani ambalo lilitukia? Malaika wa Yehova alikuja na kufungua Petro kutoka jela. Hata Petro alistaajabishwa na jambo lililokuwa likitukia. Mwishowe yeye aling’amua lililokuwa likitukia na kusema: “Sasa nimejua yakini ya kuwa Bwana [Yehova, NW] amempeleka malaika wake na kunitoa katika mkono wa Herode.”—Matendo 12:1-11.
Usimulizi uo huo unatuambia kwamba Herode alikuwa tayari amekwisha kumwondolea mbali mtume Yakobo, yule ndugu wa Yohana. Yehova aliruhusu ufia-imani huo utukie. Basi, inaonekana wazi kwamba ingawa Yehova anaweza kutoa himaya na ukombozi, yeye huenda akaruhusu matukio yafanyike kama kawaida, na hivyo aruhusu watu fulani kati ya watumishi wake waliojitoa kwake kwa bidii wathibitishe ukamilifu wao hata mpaka kifo. Maneno ya Yakobo, yule ndugu nusu wa Yesu yanafaa: “Hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. Badala ya kusema, Bwana [Yehova, NW] akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.”—Yakobo 4:14, 15; Linganisha Ayubu 2:3-5.
Jambo moja ni hakika, katika nyakati za misiba ya kiasili na aksidenti, ile kanuni ya Biblia inatumika kwa watu wote kwa usawa ule ule mmoja: “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (Mhubiri 9:11, NW) Na ingawa inafaa kusali kuomba msaada na himaya katika nyakati za mnyanyaso, sisi tunalazimika kutambua kwamba “Kunyanyashwa hakuepukiki kwa wale ambao wamepiga moyo konde kuishi maisha za Kikristo kweli kweli.”—2 Timotheo 3:12, Phillips.
Roho ya Akili Timamu
Ingawa ni kweli kwamba katika nyakati zilizopita Yehova amechukua kitendo kuwapa himaya watu wake, kama vile wakati yeye alipookoa Israeli kutoka Misri na kutoka majeshi ya Farao, lingekuwa jambo la kimbelembele kufikiri kwamba lazima Mungu ampe himaya kila Mkristo asipatwe na matokeo ya ‘wakati na hali isiyotazamiwa’ au kutoka matokeo ya ukosefu wake mwenyewe wa kutumia busara. Barua ya Paulo kwa Wakristo kule Roma, ambao labda watu fulani-fulani kati yao walikufa baadaye katika nyanja za kuonyeshea michezo hatari wakiwa wafia-imani, inahusika katika jambo hili: “Mimi naambia kila mmoja aliye huko kati ya ninyi asifikiri mengi zaidi juu yake mwenyewe kuliko inavyohitajiwa kufikiri; bali afikiri ili aweze kuwa na akili timamu, kila mmoja kama vile Mungu amemgawia yeye kipimo cha imani.” (Warumi 12:3, NW) Tafsiri ya J. B. Phillips inasema: “Jaribuni kuwa na kadirio la utimamu wa akili juu ya uwezo wenu mbalimbali wa kufanya mambo.”
Shauri ambalo limeelezwa hapo lina utumizi ulio sawa na huo leo, ingawa ni katika hali tofauti. Ikiwa Mkristo anawazia kwamba yeye anaweza kuendesha gari kwa uzembe au akiwa chini ya uongozi wa kileo na bado aponyoke kwa sababu yeye ana himaya ya Mungu, je! hiyo inaonyesha “akili timamu”? Je! Mkristo huyo ana ‘kadirio la akili timamu juu ya uwezo wake mbalimbali wa kufanya mambo’? Pia, ikiwa yeye anatia mwanadamu mwenzake katika hali ya kuweza kupatwa na hatari, je! yeye kweli kweli ‘anapenda jirani yake kama yeye mwenyewe’?—Mathayo 22:39, NW.
Sasa acheni tutumie ile roho ya akili timamu kwenye hali ambapo mwanadamu amesimamisha imara mitaa ya kuishi katika maeneo yenye kuelekea-elekea kupatwa na matetemeko ya dunia au ambako milima yenye utendaji wa kulipusha moto ni tisho ambalo halijatokea bado lakini ni la kweli kweli. Kielelezo kizuri ni lile eneo ambalo tayari limetajwa lenye kuzunguka ule mlima wenye kulipusha moto wa Nevado del Ruiz katika Kolombia. Kulingana na El País, karatasi ya habari za kila siku ya Kolombia, msanii wa ramani za ujenzi César Zárate alitayarisha uchunguzi mmoja katika 1982 ambao ulionyesha kwamba ule Mto Lagunilla ulikuwa umefurikisha Armero wakati uliopita na kwamba mji ule ulikuwa bado hauna kinga za kutosha. Pia ilijulikana kwamba ule mlima wa kulipusha moto wa Nevado del Ruiz ulikuwa umelipuka mara sita tangu 1570. Kulingana na vyanzo vya kihistoria, mlima huo wenye kulipusha moto una kawaida ya utendaji wenye kujirudia-rudia ambayo inatukia-tukia baada ya kati ya miaka 140 na miezi 9 na miaka 110 na miezi 2.
Habari hizo zilipelekwa kwenye chapa ya Jumapili ya karatasi ya habari ya Kolombia, El Tiempo majuma kadha kabla ya ule msiba wa Armero. Hizo zilisema waziwazi hivi: “Furiko lile linalofuata . . . litatukia karibu na katikati ya Novemba mwaka huu. Ishara zenye kuonyesha vitabia-vitabia hivyo zimekwisha kuonwa: Moshi kutoka lile shimo-mlima la ‘Arenas.’ Mvua ya majivu na gesi-gesi. Kuchafuliwa kwa maji na mazao. Harufu-harufu zenye kuleta kichefu-chefu cha kutaka kutapika. . . . Mlio wa mngurumo uliotoka Septemba 11 katika ule mlima wenye kulipusha moto. Kuendelea-endelea kuyeyuka kwa theluji juu ya kilele cha mlima . . . Kwa hiyo, ni wakati wa kufanya kitendo.”
Hata hivyo, makala hiyo haikuchapishwa. Labda ilionwa kuwa mpayuko wa bure tu wa kuonya juu ya afa. Wahariri wa El Tiempo baadaye walipunguza uzito wa kutoichapisha kwa kusema ulikuwa “ukosefu wa mwono wa mapema, ukosefu wa kuelewa kwa haraka, au itikadi ya kijinga kwamba hakuna jambo lingetukia.”
Ingawa hivyo, katika wakati ule ule ambao uliratibiwa, Nevado del Ruiz ulilipusha sehemu yao ya juu katika usiku wa Novemba 13, 1985. Watu zaidi ya 20,000 walipoteza maisha zao katika Armero, na kulikuwa maelfu ya majeruhi kutoka Chinchiná na miji mingine ya karibu-karibu. Miongoni mwa wale ambao walikufa katika Armero walikuwa 41 wa Mashahidi wa Yehova na washirika wao. Kwa kukosa mashauri yenye kufaa watu fulani kati yao walikuwa wamekimbilia Jumba la Ufalme ambalo lilikuwa katika ardhi ya chini zaidi. Wao walifagiliwa mbali na kuzikwa pamoja na Jumba hilo. Kwa furaha, Mashahidi wengine waliweza kukimbia kwenye ardhi ya juu zaidi na wakaokolewa.
Kwa wazi, ni rahisi kuwa na hekima baada ya huo uhakika. Lakini angalau funzo la masomo linaweza kupatikana kutokana na matukio hayo mabaya sana.
Maonyo ya Kale Yapuuzwa
Biblia inatoa vielelezo vya watu fulani ambao walipuuza maonyo yaliyotolewa kwa wakati unaofaa au wakafikiri ‘jambo hilo halingeweza kutukia katika wakati wao’ au katika eneo lao la dunia. Kituko kimoja ni wakati Loti alipoonywa kukimbia kutoka Sodoma na Gomora. Yeye aliwatia chonjo wana-wakwe zake akisema: “Ondokeni mtoke katika mahali hapa kwa sababu BWANA [Yehova, NW] atauharibu mji huu”! Wao walitikia jinsi gani? “[Loti] akawa kama achezaye machoni pa wakweze.” ‘Mchezo’ huo ulikuwa wa muda mfupi. Yehova alifanya inye kiberiti na moto juu ya ile miji iliyohukumiwa maangamizi, yenye tabia zilizopotoka. Wana-wakwe hao walikufa pamoja na wakaaji wasio na adili wa jimbo hilo. Inaonekana mke wa Loti alikimbia kutoka Sodoma akiwa na mashaka na kusitasita. Yeye “akatazama [“akaanza kutazama kutoka, NW] nyuma yake [Loti] akawa nguzo ya chumvi.”—Mwanzo 19:12-26.
Zaidi ya miaka 1,900 iliyopita, Yesu alitoa unabii kwamba Yerusalemu wa kale ungepatwa na uharibifu mbaya sana. Yeye alitoa maelezo marefu ya waziwazi juu ya matukio ambayo yangetukia kabla ya kuachwa ukiwa kwa mji ule akisema: “Hapo mtakapoona mji wa Yerusalemu umezungukwa na majeshi [“yenye kupiga kambi” NW] ndipo jueni ya kwamba uharibifu wake umekaribia. Ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani, na walio katikati yake wakimbilie nje, na walio katika mashamba wasiuingie.”—Luka 21:20-24.
Wakati majeshi ya Kiroma yalipozunguka Yerusalemu katika mwaka wa 66 W.K., Wakristo katika mji huo walitambua ile ishara ambayo Yesu alikuwa ametoa. Ndipo, akiwa katika hali ya kuweza kabisa kupata ushindi kamili, Jenerali Sesho Galo akaondoa vikosi vyake kwa njia isiyoelezeka. Hiyo ilikuwa ndiyo nafasi ambayo Wakristo walikuwa wakingojea, na wao walikimbia upande ule mwingine wa Yordani. Katika 70 W.K., Waroma walirudi wakiwa chini ya Jenerali Tito na wakaharibu Yerusalemu. Mamia ya maelfu ya Wayahudi ambao waliendelea kukaa mle ndani ya mji uliohukumiwa maangamizi walikufa wakati wa kuzingirwa na wakati wa vita.
Ni kweli, katika vituko hivyo onyo la kimungu lilitolewa. Lakini jambo la kuangalia ni kwamba ni wachache tu waliotii ule ujumbe na kukimbia. Walio wengi hawakujali. Wao walikataa kuchukua onyo la Mungu kwa uzito.
Ni Katika Njia Gani Sisi Tunaweza Kumtahini Mungu Ifaavyo?
Hata katika misiba ya kiasili, kumekuwa mara nyingi na maonyo—ile historia iliyotangulia ya hali za eneo lile, ishara za juzi-juzi, au habari za kisayansi—ambayo yanaonyesha uwezekano mkubwa wa kutokea hatari katika muda wa kipindi fulani. Labda eneo fulani lina maelekeo ya kufurika-furika. Wakati huo mtu mwenye kutumia akili kwa kiasi lazima apime mambo yote ili kuamua kama inahitajiwa kabisa ahamie wilaya nyingine na kama ataweza kuendeleza uhai wake kule. Bila shaka, haiwezekani kutabiri wakati na mahali pa kila msiba wa kiasili. Hata hivyo, uhakika wa kwamba kuna uwezekano wa kupatwa na msiba unaweza kufikiriwa katika kuhesabu gharama na pia ile kadiri ya kinga inayopatikana ikiwa lililo baya zaidi litatukia. Lakini si jambo la kiakili kutazamia himaya maalum kutoka kwa Mungu. Kufanya hivyo kungekuwa kutia Mungu kwenye mtihani katika njia ambayo si halali au isiyosawazika.
Hata hivyo, katika maana tofauti, Yehova anatualika sisi tumtahini. Kule nyuma katika wakati wa nabii Malaki, Israeli walikuwa wakimtahini Mungu kwa njia yenye makosa kwa kutoa dhabihu hafifu-hafifu juu ya madhabahu. Kwa mkate wao uliotiwa uchafu na matoleo ya wanyama vilema, wao walionyesha kwamba walidharau meza ya Yehova. Kupitia Malaki, Yehova alialika wao wageuke kabisa na kurekebisha mwendo wa vitendo vyao. “Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu [mkanitahini, NW] kwa njia hiyo, asema BWANA [Yehova, NW] wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha.”—Malaki 3:10
Ndiyo, kuhusiana na baraka za kiroho, sisi tunaweza ‘kujaribu,’ au kuthibitisha ukweli wa uaminifu wa Yehova. Ikiwa sisi tutatafuta kwanza Ufalme wake na uadilifu wake, ndipo, kama Yesu alivyosema, ‘mambo mengine yote yanayohitajiwa kabisa yataongezwa kwetu.’ Yesu alisema pia: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kubisha nanyi mtafunguliwa.” Ikiwa wanadamu wasio wakamilifu wanawapa watoto wao zawadi za fadhili, “ni zaidi hivyo kama nini kwamba Baba yenu ambaye yumo katika mbingu atatoa vitu vyema kwa wale wanaoomba yeye [kwa kupatana na mapenzi yake]?”—Mathayo 6:33; 7:7-11; 1 Yohana 5:14, NW.
Katika wakati uu huu, onyo linapewa kwa mataifa kusema kwamba karibuni Yehova ataanzilisha kitendo chake cha malipo dhidi ya sehemu zote za mfumo wa mambo wa Shetani. (Ufunuo 16:14, 16; 18:20) Mamilioni ya watu wenye busara wanatii ujumbe huo unaohubiriwa na Mashahidi wa Yehova na wanajitenga wenyewe kwenda upande wa utawala wa Ufalme wa Mungu. Wao wanaenda nje ya ushirika mfisadi wa kisiasa na kidini kabla haijawa kuchelewa mno. (Ufunuo 18:4) Kwa kufanya hivyo, wao wanajitayarisha kwa ajili ya uzima wa milele chini ya utawala wa Kristo wa dunia yetu, ambayo itageuzwa iwe paradiso ya haki na usawa. Je! wewe unatii hili?—2 Petro 3:13; Tito 1:2.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Diploma iliyopatikana katika magofu ya Armero ni kikumbusho cha kuhuzunisha kwamba maelfu hawakutii maonyo
[Picha katika ukurasa wa 22]
Je! tabia zako za kuendesha gari zinaonyesha utimamu wa akili ya Kikristo?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Lile eneo ambalo sasa ni ukiwa ambapo mji wa Armero ulisimama. Zaidi ya watu 20,000 waliangamia hapa
Gari hili lililobomolewa laeleza kifupi ule msiba uliopiga Armero
-
-
Utafutaji wa Ukweli WathawabishwaMnara wa Mlinzi—1987 | Desemba 15
-
-
Utafutaji wa Ukweli Wathawabishwa
KWA SABABU ya kutotoshelezwa sana akiwa mhubiri wa kawaida katika kanisa la Kipresbiteri, muungwana mmoja wa kiume alianza kutafuta-tafuta kanisa la kweli la Mungu. Aliandika matakwa kumi ambayo alihisi kanisa la kweli limepaswa kuwa nayo. Tayari alikuwa anaelewa kwa usahihi jinsi fundisho la moto wa mateso, kutokufa kwa nafsi, na kadhalika halipatani na maandiko. Kwa muda wa miaka 30 aliongoza utafutaji huu. Alipofikiwa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alianza kumtupia makombora ya maswali, kama vile: “Kundi dogo ni nani? Ni nani walio wale 144,000 na kondoo wengine?” Alipopata majibu yenye kutosheleza, alikubali kuwa funzo la Biblia. Baada ya miezi mitatu alisema hivi kwa yule Shahidi: “Basi, Ndugu, lililo kanisa la kweli la Mungu ni Mashahidi wa Yehova.” Sasa yeye ni mwenye umri wa miaka 71 na ana furaha kwa kuwa amelipata kanisa la kweli baada ya utafutaji wa miaka 30!
-