Haki Karibuni kwa Ajili ya Mataifa Yote
“Yaliyo—haki kabisa ndiyo utakayoyafuata, ili upate kuishi na kuirithi nchi upewayo na BWANA [Yehova, NW], Mungu wako.”—KUMBUKUMBU 16:20.
1. Kusudi la awali la Mungu lilikuwa nini kwa mwanadamu, na ni jinsi gani tu angeweza kulitimiza?
KUSUDI la Yehova Mungu katika kuumba mwanamume na mwanamke lilikuwa kujaza dunia viumbe wakamilifu. Wote wangemsifu yeye na kutimiza sehemu yao katika kutiisha dunia. (Mwanzo 1:26-28) Kwa kuwa mwanadamu alifanyizwa kwa mfano na sura ya Mungu, alijaliwa sifa za hekima, haki, upendo, na nguvu. Kwa kujizoeza sifa hizo kwa usawaziko, hapo tu ndipo mwanadamu angeweza kutimiza alilokusudiwa na Mfanyizaji wake.
2. Ni kwa kadiri gani kufuatia haki kulivyokuwa kwa maana kwa wana wa Israeli?
2 Kama ilivyoonwa katika makala iliyotangulia, mwanadamu aliasi dhidi ya njia ya Mungu ya kufanya mambo na akahukumiwa kifo. Sasa, kwa sababu ya kutokamilika, haikuwezekana atekeleze kusudi la awali la Mungu kwa aina ya binadamu. Kutoweza kwa mwanadamu kuonyesha haki kamilifu kumeshiriki sana katika ukosefu huo. Basi, si ajabu kwamba Musa aliwakumbusha hivi wana wa Israeli: “Yaliyo haki kabisa ndiyo utakayoyafuata”! Maisha zao na uwezo wa kutwaa Bara Lililoahidiwa zilitegemea kufuata haki.—Kumbukumbu 16:20.
Kivuli cha Mema Yanayokuja
3. Kwa nini ni jambo la maana sisi leo tuchunguze mishughuliko ya Yehova pamoja na Israeli?
3 Mishughuliko ya Yehova pamoja na taifa la Israeli inaimarisha uhakika wetu kwamba kweli yeye ataelewesha mataifa yote haki yake kupitia Mtumishi wake mchaguliwa, Yesu Kristo. Mtume Paulo anaeleza mambo jinsi hii: “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Kwa kuwa Mungu ni “mpenda uadilifu na haki,” yeye alitaka Waisraeli wamwige katika kushughulika kwao mmoja na mwingine. (Zaburi 33:5, NW) Hiyo inaweza kuonwa wazi kwa kuchunguza chache za sheria 600 walizopewa Israeli.
4. Matatizo ya haki za kiraia yalishughulikiwaje chini ya Sheria ya Musa?
4 Matatizo ya haki za kiraia hayakuwako wakati Sheria ya Musa ilipofuatwa. Kuhusu mtu asiye Mwisraeli aliyekuja kuishi humo barani, Walawi 19:34 inataarifu hivi: “Mgeni akaaye pamoja nawe atakuwa kama mzalia kwenu; mpende kama nafsi yako.” Ni mpango wa haki na upendo kama nini! Isitoshe, mahakimu na mashahidi kadhalika walishauriwa hivi: “Usiandamane na mkutano kutenda uovu; wala usitie ushahidi wako katika neno lo lote kwa kugeukia kando na kuandamana na mkutano ili kupotoa hukumu [haki, NW]; wala usimpendelee mtu mnyonge katika neno lake.” (Kutoka 23:2, 3) Ebu fikiria hilo—haki ikitekelezwa hali moja kwa matajiri na maskini kadhalika!
5. Linganisha sheria za uhalifu chini ya Sheria ya Musa pamoja na zile za leo.
5 Chini ya orodha ya Sheria ya Musa, sheria za uhalifu zilizidi kwa mbali ubora wa sheria-katiba zilizo katika vitabu vya mataifa leo. Kwa kielelezo, mwibaji hakutiwa gerezani awe lemeo juu ya watu waliofanya kazi kwa bidii wakiwa watiifu kwa Sheria. Ilikuwa lazima afanye kazi na kulipia maradufu au zaidi kile alichokuwa ameiba. Kwa hiyo mwibiwa hakupata hasara yoyote. Tuseme kwamba mwibaji angekataa asifanye kazi wala asilipe. Katika kisa hicho, aliuzwa utumwani mpaka aliporudisha kitu kile. Ikiwa aliendelea kuonyesha mwelekeo wa kichwa kigumu, aliuawa. Hivyo mwibiwa alitendewa haki, na hicho kikawa kizuilio imara kwa wengine ambao huenda wakawa na mbetuko wa kuiba. (Kutoka 22:1, 3, 4, 7; Kumbukumbu 17:12) Waaidha, kwa kuwa uhai ni mtakatifu machoni pa Mungu, muuaji yeyote aliuawa. Hiyo ilimwondoa taifani mwovu mwenye nia ya kuua. Hata hivyo, wauaji wasiokusudia walionyeshwa rehema.—Hesabu 35:9-15, 22-29, 33.
6. Kuchunguza sheria za Israeli kunatuongoza kukata shauri gani?
6 Basi, nani anaweza kukana kwamba haki haikutia alama mishughuliko yote ya Mungu ya kuhukumu taifa la Israeli? Kwa sababu hiyo, ni faraja kama nini, na tumaini kama nini, linalojaa ndani yetu tunapofikiria sana jinsi ahadi ya Mungu kwenye Isaya 42:1 itakavyotimizwa kupitia Kristo Yesu! Hapo tunapewa uhakikishio huu: “Atawatolea mataifa hukumu [haki, NW]”
Haki Yasawazishwa na Rehema
7. Eleza juu ya mishughuliko ya Yehova yenye rehema pamoja na Israeli.
7 Haki ya Mungu inasawazishwa na rehema. Hiyo ilionyeshwa wazi Waisraeli walipoanza kuasi dhidi ya njia adilifu za Mungu. Sikiliza elezo la Musa juu ya vile Yehova alivyowatunza kwa rehema wakati wa miaka yao 40 jangwani: “Alimkuta katika nchi ya ukame, na katika jangwa tupu litishalo; alimzunguka, akamtunza; akamhifadhi kama mboni ya jicho; mfano wa tai ataharikishaye kioto chake; na kupapatika juu ya makinda yake, alikunjua mbawa zake, akawatwaa, akawachukua juu ya mbawa zake. BWANA [Yehova, NW] peke yake alimwongoza.” (Kumbukumbu 32:10-12) Baadaye, taifa lilipogeuka likaasi imani, Yehova alisihi hivi: “Rudini sasa, na kuziacha njia zenu mbovu, na matendo yenu maovu.”—Zekaria 1:4.
8, 9. (a) Ni kwa kadiri gani Mungu alivyowaonyesha Wayahudi haki yake yenye rehema? (b) Ni afa gani la mwisho lililowafikilia, lakini inaweza kusemwa nini juu ya njia ya Mungu ya kushughulika nao?
8 Toleo la Yehova la rehema lilipata masikio yenye uziwi. Kupitia mnabii Zekaria, Mungu alisema: “Hawakusikia, wala kunisikiliza.” (Zekaria 1:4) Kwa hiyo haki yenye rehema ya Mungu ilimharakisha kutuma Mwana wake mzaliwa pekee kuwasaidia wamrudie Yeye. Yohana Mbatizaji alijulisha Mwana wa Mungu kwa kusema: “Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu!” (Yohana 1:29) Kwa miaka kadhaa, Yesu aliwafundisha Wayahudi njia sawa za Mungu bila kuchoka, akifanya miujiza isiyohesabika na hivyo kuthibitisha kwamba alikuwa ndiye Mkomboaji aliyetabiriwa. (Luka 24:27; Yohana 5:36) Lakini watu hawakusikiliza wala kuitikadi. Kwa sababu hiyo, Yesu alisukumwa na moyo kupaaza sauti hivi: “Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako! ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka! Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.”—Mathayo 23:37, 38.
9 Mungu kwanza aliacha kutekeleza hukumu yake kali kwa miaka mingine 47, mpaka 70 W.K. Halafu akaruhusu Waroma waharibu Yerusalemu na kupeleka maelfu ya Wayahudi utekwani. Tunapofikiria ustahimilivu na saburi ya Yehova kwa kipindi cha karne nyingi, ni nani asiyeweza kuona alama ya haki katika mishughuliko yake yote pamoja na nyumba ya Israeli?
Haki kwa Mataifa Yote
10. Haki ya Mungu ilifikishwaje kwa mataifa yote?
10 Baada ya Israeli kukataa Yesu, Yakobo alisema: ‘Mungu hapo kwanza aliwaangalia Mataifa ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake.’ (Matendo 15:14) “Watu” hao, kutia na Wayahudi wale wachache waliokubali Yesu kuwa ndiye Mesiya, wanajumlika pamoja kufanyiza “Israeli [wa kiroho] wa Mungu” mwenye wafuasi 144,000 wa Yesu Kristo waliozaliwa kwa roho. (Wagalatia 6:16; Ufunuo 7:1-8; 14:1-5) Mwitikadi wa kwanza asiyetahiriwa asiye Myahudi alikuwa Kornelio. Kornelio na watu wa nyumba yake walipokubali njia ya Mungu ya wokovu, Petro alisema: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki [uadilifu, NW] hukubaliwa na yeye.” (Matendo 10:34, 35) Paulo anaeleza kwa upana uhaki wa kutopendelea kwa Yehova anaposema hivi: “Hapana Myahudi wala Mgiriki, hapana mtumwa wala mtu huru, hapana mtu wa kiume wala wa kike; kwa maana nyinyi nyote ni mtu mmoja katika muungano pamoja na Kristo Yesu. Waaidha, ikiwa nyinyi ni wa Kristo, nyinyi kweli ni mbegu ya Abrahamu, warithi kuhusiana na ile ahadi.”—Wagalatia 3:28, 29, NW.
11. Ni ahadi gani aliyopewa Abrahamu, nayo itatimizwaje?
11 Hapa tunakumbushwa juu ya ahadi nzuri ajabu ambayo Yehova alimpa Abrahamu. Kwa msingi wa nia ya huyo mzee wa ukoo kumdhabihu Isaka mwana wake mpendwa, Mungu alimwambia yeye hivi: “Kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki . . . na katika uzao [mbegu, NW] wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:16-18) Ahadi hiyo itatimizwaje? ‘Mbegu ya Abrahamu,’ ambayo ni jumla ya Yesu Kristo na wafuasi wake wapakwa mafuta 144,000 wanaothibitika kuwa waaminifu mpaka kifo, itatawala aina ya binadamu ikiwa kwenye mbingu kwa miaka elfu moja. (Ufunuo 2:10, 26; 20:6) Kuhusu wakati huo wenye baraka, Yehova anatuhakikishia hivi: “Kwa wingi wa utawala wa kimwana-mfalme na kwa amani kutakuwa hakuna mwisho.” Kwa nini? Kwa sababu “utawala wa kimwana-mfalme” wa Ufalme huo wa Kimesiya ‘utategemezwa kwa njia ya haki na uadilifu mpaka wakati usio dhahiri.’—Isaya 9:7, NW.
12. Tayari baraka za agano la Kiabrahamu zinapatwaje?
12 Lakini hakuna uhitaji wa kungoja mpaka uanze Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo ili kuona shangwe ya baraka za agano la Kiabrahamu. Tayari baraka hizo zinapatwa na “umati mkubwa” wa watu “kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na ndimi.” Kwa ‘kufua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya MwanaKondoo,’ Yesu Kristo, wao wamekuja kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Yehova. Kama Abrahamu, wamekuwa rafiki za Yehova! Haki inaitia alama kweli kweli njia ya Yehova ya kuwapa wokovu mamilioni ya watu kutoka mataifa yote.—Ufunuo 7:9, 14, NW.
Je! Wewe Unaitikia Njia za Mungu za Haki
13, 14. (a) Ni uchunguzi gani ambao sisi sote binafsi tunapaswa kufanya moyoni? (b) Shukrani yetu kwa Yehova inaweza kuonyeshwaje?
13 Je! moyo wako umeguswa na kusukumwa kwa kina kirefu na njia ya Mungu ya haki na upendo katika kutoa Mwana wake mzaliwa pekee awe ukombozi kwa ajili yako? Wazia hisia za Abrahamu wakati Yehova alipomwomba amdhabihu mwana wake, mmoja aliyempenda sana! Lakini hisia za Mungu zinaingia kwa kina kirefu zaidi. Fikiria hisia zake wakati Mwana wake mpendwa alipokuwa akitendwa mambo ya kumvunjia heshima, yale matusi ya wapitanjiani, lile umivu kali sana sana la mti wa mateso. Wazia tendo-mwitikio la Mungu kwa mlio wa Yesu: “Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?” (Mathayo 27:39, 46) Hata hivyo, haki ilidai kwamba Yehova Mungu amruhusu Mwana wake afe kwa njia hiyo ili athibitishe ukamilifu wake kwa kuondolea malawama uadilifu wa Mungu. Waaidha, kwa kuruhusu Mwana wake afe, Yehova alitufungulia njia ya wokovu.
14 Basi, kwa uhakika shukrani yetu kwa Yehova na Mwana wake inapasa kutusukuma tukiri peupe hivi: “Wokovu wetu ni kwa Mungu wetu . . . na kwa Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 7:10, NW) Kwa kuitikia tukiwa na mwelekeo chanya, tunaonyesha itikadi yetu katika maneno ya Musa: “Njia [za Yehova] zote ni haki.” (Kumbukumbu 32:4) Ni furaha kama nini ambayo lazima iwe tunaletea mioyo ya Yehova na Mwana wake tunapozikiri kisha kuzifuatia njia za Mungu zenye haki za wokovu kwa mwanadamu!
15. Maneno ambayo Yesu alimwambia Nikodemo yana umaana gani kwetu?
15 Je! sisi hatuna furaha kwamba waitikadi wenzetu katika miaka ya 1870 walichukua msimamo imara kuhusu suala la dhabihu ya ukombozi? Je! hatufurahi kwamba sisi leo ni wa tengenezo ambalo limepiga moyo konde jinsi hiyo hiyo kufuata sana haki na njia ya Mungu yenye upendo kwa ajili ya wokovu wa mwanadamu? Ikiwa ndivyo, basi inatupasa sisi tuelekeze fikira maalumu kwenye maneno ambayo Yesu alimwambia Nikodemo: “Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi . . . Bali yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu [kwa upatano pamoja na Mungu, NW].” Ili kuepuka hukumu kali ya Mungu, ni lazima tuthibitishe imani yetu katika Mwana kwa kutenda ‘matendo ya upatano pamoja na Mungu.’—Yohana 3:17, 18, 21.
16. Wanafunzi wa Yesu wanaweza kumtukuzaje Baba wa kimbingu?
16 Yesu alisema: “Baba yangu anatukuzwa katika jambo hili, kwamba nyinyi mwendelee kuzaa tunda jingi na kujithibitisha wenyewe kuwa wanafunzi wangu. Ikiwa nyinyi mnashika amri zangu, nyinyi mtabaki katika upendo wangu, sawa na vile mimi nimeshika amri za Baba na ninabaki katika upendo wake.” (Yohana 15:8, 10, NW) Ni nini baadhi ya amri hizo? Moja inapatikana kwenye Yohana 13:34, 35, ambapo Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Amri mpya nawapa, Mpendane . . . Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” Tunda la upendo linaonekana wazi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Yesu aliamuru hivi pia: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20, NW) Je! wewe binafsi unafanya hayo ‘matendo ya upatano pamoja na Mungu’?
17. Ni tokeo gani linaloonyesha kwamba kazi ya kuhubiri na kufundisha ni wonyesho wa haki ya Yehova?
17 Haki ya njia ya Yehova katika kuruhusu wafuasi wa Yesu wafanye hayo matendo ya kuhubiri na kufundisha yaonekana wazi tunapofikiria yaliyotimizwa na Mashahidi wa Yehova katika mwaka mmoja tu. Wakati wa 1988, walibatizwa wanafunzi wapya 239,268! Je! hiyo hailetei shangwe moyo wako?
Mungu wa Haki Atafanya Kitendo Upesi!
18. Ni maswali gani yangeweza kutokezwa kwa sababu ya kunyanyaswa kwa watu wa Yehova?
18 Kazi ya kutoa ushuhuda haikuendeshwa bila upinzani. Yesu aliambia wafuasi wake: “Ikiwa waliniudhi [walininyanyasa, NW] mimi, watawaudhi ninyi.” (Yohana 15:20) Historia ya ki-siku-hizi ya Mashahidi wa Yehova inashuhudiza ukweli wa taarifa hiyo. Marufuku, vifungo gerezani, mapigo, na hata maumizo-umizo yamepata Mashahidi katika nchi baada ya nchi. Maneno ya kiunabii ya Habakuki yanakuja tena akilini mwetu: “Sheria inakuwa yenye kufa ganzi, na haki haitokezi mbele kamwe.” Kwa sababu hiyo, nyakati fulani, hata watu wa Yehova huenda wakahisi wakitaka kuuliza hivi: ‘Kwa nini Yehova anawatazama tu wale wanaoshughulika kwa hila? Kwa nini Yeye anaendelea kuwa mnyamavu wakati mtu fulani mwovu anapomeza kabisa mtu fulani aliye mwadilifu zaidi ya yeye?’—Habakuki 1:4, 13, NW.
19. Eleza ni kielezi gani ambacho Yesu alitoa kinachotusaidia kuelewa mambo kulingana na kituo cha rai ya Mungu.
19 Yesu alitoa kielezi kinachosaidia kujibu maswali hayo na kutuwezesha tuone mambo kama Mungu ayaonavyo. Kwenye Luka 17:22-37, Yesu alieleza hali zenye jeuri ambazo zingetia alama mwisho wa huu mfumo wa mambo. Alisema zingelinganika na zile zilizotangulia Gharika katika siku ya Noa na uharibifu wa Sodoma na Gomora siku za Loti. Ndipo, kama ilivyoelezwa kwenye Luka 18:1-5, Yesu akageukia wanafunzi wake “akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa.” Yesu alisimulia juu ya mjane aliyekuwa katika uhitaji mkubwa na juu ya “kadhi [hakimu]” aliyekuwa katika cheo cha kutosheleza mahitaji yake. Mjane aliendelea kuomba kimaskini hivi: “Nipatie haki na adui wangu.” Kwa sababu ya udumifu wake, mwishowe hakimu ‘alimpatia haki.’
20. Kielezi cha Yesu kina somo gani kwetu?
20 Somo ni nini kwetu leo? Akimtofautisha na Yehova hakimu huyo asiye mwadilifu, Yesu alisema: “Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu. Na Mungu, je! hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao? Nawaambia, atawapatia haki upesi.”—Luka 18:6-8a.
21. Tunapaswa kuwa na rai gani juu ya matatizo yetu ya kibinafsi na tuyashughulikieje?
21 Sikuzote kumbuka kwamba wakati matatizo yetu ya kibinafsi yanapohusika, ikionekana kwa njia yoyote kwamba kuna ukawivu katika kujibiwa maombi rasmi yetu, hiyo si kwa sababu Mungu hana nia ya kufanya hivyo. (2 Petro 3:9) Ijapo tuteswe na mnyanyaso wa namna fulani au ukosefu wa haki kama yule mjane, tunaweza kuwa na imani kwamba Mungu atahakikisha haki inafanywa hatimaye. Tunaweza kuonyeshaje imani hiyo? Kwa kusali kwa uendelevu na kutegemeza sala zetu kwa kudumisha mwendo wa kutenda kwa uaminifu. (Mathayo 10:22; 1 Wathesalonike 5:17) Kwa uaminifu wetu, tutathibitisha kwamba duniani kuna imani, kwamba kuna wapenda haki wa kweli, na kwamba sisi tumo miongoni mwao.—Luka 18:8b.
“Furahini, Enyi Mataifa, Pamoja na Watu Wake”
22. Musa alimaliza wimbo wake kwa shangwe gani ya ushindi?
22 Karne nyingi zilizopita, Musa alimalizia wimbo wake kwa shangwe hii ya ushindi: “Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake; kwa maana atatwaa kisasi kwa damu ya watumwa wake, atawatoza kisasi adui zake, tena atafanya kafara kwa nchi yake, na watu wake.” (Kumbukumbu 32:43) Siku ya Yehova ya kisasi inakaribia zaidi wakati wote. Sisi ni wenye shukrani kama nini kwamba yeye angali anajizoeza saburi pamoja na haki!
23. Ni tokeo gani la kufurahisha linalowangojea wale wanaoshiriki furaha ya watu wa Mungu?
23 Njia ingali wazi kwa wale walio katika mataifa yote “wafikilie toba,” lakini hakuna wakati wa kupoteza. Petro alionya hivi: “Siku ya Bwana [Yehova, W] itakuja kama mwivi.” (2 Petro 3:9, 10) Haki ya Mungu inadai kwamba mfumo huu mwovu uharibiwe karibuni. Uharibiwapo, sisi na tupatikane miongoni mwa wale ambao wameuitikia wito wenye kufurahisha: “Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake.” Ndiyo, na tuwe miongoni mwa wale wenye furaha ambao wameona kwamba haki hutia alama njia zote za Mungu!
Wewe Ungejibuje?
◻ Kwa nini Sheria ya Musa inapasa kuimarisha imani yetu katika haki ya Mungu?
◻ Ni nini kinachopasa kutushurutisha tuitikie njia za Mungu za haki?
◻ Yehova anaweza kutukuzwaje?
◻ Leo, ni wapi tu ambapo furaha ya kweli inaweza kupatikana?
[Picha katika ukurasa wa 25]
“Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”—Matendo 10:34, 35.
[Picha katika ukurasa wa 28]
Mungu atasababisha wafanyiwe haki wachaguliwa wake wanaopaaza sauti ya kumlilia