Uthamini Wako kwa Kifo cha Kristo
1 ‘Mwana wa Adamu alikuja, si ili atumikiwe, bali atumike, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.’ (Mt. 20:28) Hakuna binadamu mwingine yeyote aliyepata kuishi duniani angaliweza kufanya yale Yesu Kristo alifanyia ainabinadamu. Kwa mwendo wake wa maisha na hatimaye kifo juu ya mti wa mateso, tumeongozwa kwenye njia ya kupokea zawadi kubwa zaidi ambayo mtu aweza kupata, yaani uhai wa milele. Na bado, watu wengi hawathamini sana yale Kristo alifanya.
2 Fikiria tukio ambalo Yesu alikuwa nalo na watu kumi wenye ukoma. Walipomwona Yesu, walipaza sauti: “Ee Yesu, Bwana mkubwa, uturehemu!” (Luka 17:13) Yeye aliwarehemu, akiwaagiza, kulingana na Sheria, waende wakawaone makuhani. Walipokuwa njiani, wote kumi wenye ukoma waliponyeshwa.
3 Lakini ni mmoja tu aliyerudi kwa Yesu kumshukuru. Na wale wengine tisa? Walienda njia yao bila kufikiria kumshukuru mfadhili wao. (Luka 17:15-17) Sisi tunafanana na nani? Tunataka tuwe kama yule mtu aliyerudi. Yeye alikuwa na uthamini wa kweli. Je! hivyo ndivyo tunavyohisi kuhusu kifo cha Kristo?
4 Kuonyesha Uthamini Wetu: Kila mwaka Sosaiti hudokeza kwamba mistari hususa katika Biblia isomwe wakati wa juma linalotangulia tarehe ya Ukumbusho. Mistari ya Biblia iliyodokezwa yaweza kupatikana chini ya tarehe za Aprili 12-17 kwenye 1992 Calendar of Jehovah’s Witnesses. Tunaweza kuonyesha uthamini wetu kwa kusoma na kutafakari juu ya matukio hayo yaliyotokea katika maisha ya Yesu kabla tu ya kifo chake.
5 Utendaji wetu wa utumishi wa shambani unahusiana na uthamini wetu kwa Ukumbusho. Wazee watafanya mipango iliyotayarishwa vizuri ili mapainia na wahubiri waweze kupangia utendaji wa shambani ulioongezeka katika Aprili.
6 Huo ni mwezi ambao kwa kawaida makumi ya maelfu hushiriki katika kazi ya upainia msaidizi. Aprili iliyopita 1,994 walishiriki hapa katika Afrika Mashariki. Je! waweza kufanya hivyo Aprili huu? Ikiwa huwezi kufanya upainia msaidizi, panga kuongeza ushiriki wako katika utendaji wa kuhubiri kwa kadiri hali ziruhusuvyo.
7 Jenga Uthamini wa Wengine: Kila mwaka kwenye mwadhimisho wa Ukumbusho, watu wengi wanaopendezwa hukutana nasi. Kwa mfano, kati ya watu 10,650,158 waliohudhuria Ukumbusho ulimwenguni pote Machi uliopita, zaidi ya watu 6,370,000 walikuwa wenye kupendezwa. Hilo laonyesha uwezekano mkubwa wa ukuzi katika tengenezo.
8 Tunapaswa tutumie vikaratasi vya ukaribishaji vilivyochapishwa na Sosaiti na tufanye mipango ya kutoa usafiri kwa wanafunzi wa Biblia na watu waliopendezwa inapohitajiwa. Uwe mwenye kusisimuka kwa uchangamshi unapowaalika.
9 Wasaidie wajue ni kwa nini Ukumbusho ulianzishwa, ni nani wanaoshiriki mifano, na yale yanayofananishwa na mifano. (1 Kor. 11:23-26) Pia, eleza tumaini la wale wanaoshiriki na la watazamaji ambao hawashiriki mifano. (Yn. 10:16; Ufu. 14:3, 4) Hilo litasaidia watu waliopendezwa waelewe kwamba wote wanahitaji ‘kujizoeza imani’ na kwamba kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo mara moja tu kwa mwaka hakutoshi.—Yn. 3:16, NW.
10 Ukumbusho wa kifo cha Kristo ni tukio la pekee sana. Kwa kujitayarishia hilo vema, tunaonyesha kwamba tunathamini kikweli yote ambayo Yehova na Kristo wametufanyia. Kujenga uthamini kwa tukio hilo katika wanafunzi wetu wa Biblia na watu wengine wenye kupendezwa kutawasaidia pia, kujizoeza imani katika fidia iliyoandaliwa na Yehova kupitia Yesu Kristo.