Mwadhimisho wa Ukumbusho wa 1989
1Jumatano, Machi 22, 1989, itakuwa mwadhimisho wa 1,956 wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Tunapofanya mipango yetu wenyewe ili tuhudhurie, tunahitaji kuwafikiria wengine ambao huenda wakahitaji mwaliko au msaada wetu wa kibinafsi katika njia fulani. Sasa ndio wakati wa kuanza kufanya matayarisho ya Ukumbusho na kufikiria kuwaalika wengine.—Tafadhali angalia “Mambo ya Kutayarisha kwa Ukumbusho” katika ukurasa 4.
2Tunaonaje kuhudhuria Ukumbusho? Tunapaswa kuuona kuwa pendeleo na fursa ya kuonyesha uthamini kwa dhabihu ya Kristo. Ukijua kwamba utakuwa mbali na kundi lako, hakikisha kwamba unajua Jumba la Ufalme la mahali utakapozuru lilipo ili uhudhurie huko.
TUMIA VIKARATASI VYA PEKEE VYA MWALIKO
3Huenda ukaanza kutumia vikaratasi vya pekee vya Ukumbusho mapema katika Machi. Kumbuka, havipasi kutumiwa kama handibili lakini vyapasa kupewa watu binafsi wanaopendezwa. Kwa sababu kwa kawaida watu husahau tarehe na saa, inadokezwa kwamba tuandike vizuri au tupige chapa kwa taipureta Jumba la Ufalme lilipo na wakati wa Mwadhimisho wa Ukumbusho chini au nyuma ya mwaliko. Ikiwezekana, tumia wakati mdogo pamoja na mtu unayealika ili umsaidie aelewe waziwazi maana ya Ukumbusho. Watu ambao wameanza kupendezwa karibuni huenda wakasitasita kwenda kwenye Jumba la Ufalme wao wenyewe. Je! unaweza kujitolea ili uwasafirishe au upange kuwakuta nje ya jumba? Hii itahitaji wakati na jitihada zaidi, lakini msaada wako utathaminiwa. Pia, jitihada ya kipekee inapasa ifanywe ili kusaidia wale ambao wameujua ukweli kwa miaka fulani lakini wamesita kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.—Luka 11:23; Yoh. 18:37b.
MATAYARISHO YANAYOHITAJIWA KABISA
4Wazee wa kundi watataka kuhakikisha kwamba matayarisho yote ya Ukumbusho yamefanywa mapema kwa uangalifu. Hakikisheni mnachagua ndugu wanaostahili kupitisha mifano. Ndugu hao wanapasa kuwa wazee au watumishi wa huduma, wakipatikana. Mwe na hesabu inayotosha ya ndugu ambao wamejitayarisha kufanya hivyo ili kupitishwa kwa mifano kusirefushwe isivyohitajiwa. Baada ya wanaopitisha kutumikia wasikilizaji, wataketi katika mstari wa mbele na msemaji atawatumikia. Hatimaye, mmoja wao atamtumikia msemaji.
5Kila mwaka unapopita, tunakaribia siku ambayo Chakula cha Jioni cha Bwana hakitaadhimishwa tena. Ni hesabu ndogo tu kwa kulinganisha ya ndugu wapakwa mafuta wa Kristo wanaobaki. Yesu aliamuru kwamba kifo chake kikumbukwe mpaka ndugu zake wote wawe pamoja naye katika Ufalme. (Luka 22:19; 1 Kor. 11:25) Mpaka wakati huo, tutakusanyika kila mwaka kwa mwadhimisho wa Ukumbusho kwa utii na kwa uaminifu tukiwa na shangwe na uthamini mkubwa.
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Mambo ya Kutayarisha kwa Ukumbusho
(Ona Mnara wa Mlinzi wa Machi 1, 1985, uku. 17.)
1. Je! kila mtu, kutia msemaji, amejulishwa wakati halisi na mahali pa mwadhimisho? Je! msemaji ana njia ya kusafiri?
2. Je! mipango hususa imefanywa kuandaa mifano?
3. Je! mipango imefanywa ili mtu fulani alete kitambaa safi cha mezani na hesabu ya bilauri na sahani zinazohitajiwa?
4. Ni mipango gani ambayo imefanywa ili kusafisha jumba?
5. Je! wakaribishaji na wapitishaji wamepewa migawo? Je! mkutano umepangwa pamoja nao kabla ya Ukumbusho ili kurudia kazi zao? Lini? Utaratibu utafanywaje ili kuhakikisha kwamba wote wanatumikiwa kwa kufaa?
6. Je! mipango imekamilishwa ili kuwasaidia ndugu na dada wazee na wagonjwa? Je! mipango imefanywa ili kuwatumikia wowote wa wapakwa-mafuta ambao huenda wamezuiwa na hali na hawawezi kuwa kwenye Jumba la Ufalme?