“Fanyeni Hivi kwa Ukumbusho Wangu”
1 Yesu aliwaamuru wafuasi wake waadhimishe ukumbusho wa kifo chake. (Luka 22:19) Mwadhimisho huo ungekuwa kikumbusha cha dhabihu kubwa ambayo Yesu alitoa kwa ajili ya ainabinadamu. Mwaka huu Mashahidi wa Yehova kote kote ulimwenguni wataadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo Ijumaa, Aprili 17, baada ya jua kushuka.
2 Matayarisho ya Kibinafsi: Tunaweza kujitayarishaje kwa mwadhimisho ufaao wa tukio hili la maana? Njia moja ni kufikiria kwa sala juu ya maisha na huduma ya kidunia ya Yesu. Yeye alikuwa Mkombozi wa ainabinadamu kwa kutoa uhai wake mkamilifu katika dhabihu. (Mt. 20:28) Ili kusaidia kila mmoja athamini uandalizi huo, tunapendekeza mpitie sura 112 hadi 116 za Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi.
3 Kama inavyoonyeshwa katika 1992 Calendar of Jehovah’s Witnesses, usomaji wetu wa Biblia wa kabla ya Ukumbusho mwaka huu unatia ndani mistari iliyochaguliwa kutoka kwa kitabu cha Biblia cha Marko. Usomaji huu wa pekee wa Biblia umeratibiwa wakati wa kipindi cha siku sita kutoka Jumapili hadi Ijumaa, Aprili 12-17. Sisi sote tutataka kutumia wakati unaotosha kutafakari matukio hayo yenye maana.
4 Matayarisho Kamili ya Wazee: Hakikisheni kwamba vikaratasi vya ukaribishaji vya Ukumbusho vinapatikana. Je! kuna viti vya kuwatosha wote wanaotarajiwa kuhudhuria? Mahali ambapo zaidi ya kundi moja litatumia jumba, mipango mizuri inahitajiwa ili kila kundi liwe na wakati wa kutosha kuadhimisha Ukumbusho. Wale wanaotumika wakiwa wakaribishaji wapaswa kujua kazi zao. Watachukua hatua ya kwanza kuwakaribisha watu wapya wanaohudhuria. Msemaji anayestahili sana atakayetoa habari hiyo kwa udhahiri na kwa Maandiko apaswa kuchaguliwa. Wazee au watumishi wa huduma wenye kuchukua daraka wapaswa wapewe mgawo wa kupitisha mifano. Mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu isiyotoholewa yapasa iandaliwe. Kwa vikumbusha vya ziada, angalia toleo la Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 1985, ukurasa 19.
5 Kwa kufanya matayarisho kamili ya mapema, tutaonyesha kwamba tunathamini kabisa umaana wa tukio hili la pekee na kwamba tunatamani kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo kwa kutii amri ya Yesu.—1 Kor. 11:23-26.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
1. Je! kila mtu, kutia na msemaji, wamefahamishwa kuhusu wakati na mahali barabara pa mwadhimisho? Je! msemaji ana usafiri?
2. Je! mipango hususa ya kuandaa mifano imefanywa?
3. Je! mipango imefanywa ya mtu fulani kuleta kitambaa safi cha meza na hesabu ya glasi na sahani zinazotakiwa?
4. Ni mipango gani imefanywa ya kusafisha jumba kabla ya Ukumbusho na kwa usafi mdogo baadaye ikiwa kundi jingine litatumia jumba hilo jioni hiyo?
5. Je! wakaribishaji na wenye kupeana mifano wamegawiwa kazi hizo? Je! mkutano umepangwa pamoja nao kabla ya Ukumbusho ili kupitia kazi zao? Wakati gani? Ni utaratibu gani utakaofuatwa ili kuhakikisha kwamba wote wanapewa mifano istahilivyo?
6. Je! mipango ya kusaidia ndugu na dada wazee-wazee na walio dhaifu kimwili imekamilishwa? Je! mipango imefanywa ya kuwapa mifano wowote wa wapakwa-mafuta ambao huenda wakawa hawawezi kuwapo kwenye Jumba la Ufalme kwa sababu ya ugonjwa?