‘Tiini’ kwa Sababu Gani?
KATI ya amri nyingi zinazopatikana mara nyingi katika Neno la Mungu, Biblia, ni ile inayosema, ‘Tiini.’ Kwenye Warumi 13:1 tunasoma: “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu,” yaani, serikali. Vijana wanashauriwa ‘watii wazee.’ (1 Petro 5:5) Halafu, tena, mtume Paulo anatoa onyo hili la upole: “Wake, watiini waume zenu.”—Waefeso 5:22.
Wazo la kutii linaudhi wanadamu wengi wasio wakamilifu. Linawaudhi sana hivi kwamba vikundi vya namna zote vinaanzishwa ili kuasi utii, mara nyingi kwa njia yenye jeuri. Kwa mfano, majuzi gazeti Times la New York liliripoti katika siku moja tu mifano inayofuata ya uasi wenye jeuri juu ya mamlaka: “Makombora mawili yalilipuka London ya Kati mapema leo.” ‘Watu tisa waliumizwa katika ile miji mitano ya mikoa ya Manchester, Liverpool, Coventry, Bristol na Southampton.’ Katika ukurasa uo huo kulikuwa na kichwa hiki: “Watu 21 Wajeruhiwa Kombora Lilipukapo Katika Bas Iliyojaa Sana.” Iliripotiwa pia kwamba Iran ilikuwa ikijitayarishia siku ya maombolezo kukumbuka “waandamanaji waliouawa wakipambana na vikosi vya usalama.” Kwa kweli, watu wote hao walikuwa wakiasi utii kwa mamlaka zilizopo.
Kwa sababu gani Biblia inaamuru, ‘Tiini’? Ni nani wanaopaswa kutii, na kutii nani? Kwa sababu gani watu wanaudhiwa sana na wazo la kutii?
Watu wanaudhiwa sana na wazo la kutii kwa sababu ya mwendo wa uasi ulioanza kufuatwa na wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. Waliwapa wazao wao urithi wa maelekeo ya kuasi, roho ya kutokutii sheria kwa njia ya choyo ambayo haijapata kuonekana kwa kiasi kikubwa kama sasa, sawasawa na Yesu alivyotabiri. (Mathayo 24:12) Lakini, pasipo shaka sehemu fulani ya lawama inakalia wale ambao wametumia vibaya mamlaka.
Hata hivyo, shauri linalosema ‘tiini’ linategemea kanuni zinazofaa. Ni wazi lazima iwe kwamba wengine watasimamia au kuongoza mambo na wengine lazima watii. Namna gani hivyo? Kwa sababu hakuna mwanadamu anayeweza kukaa kwa kujitegemea yeye peke yake. Kila mtu anahitaji msaada wa mwingine wa vitu vya kimwili na utumishi mbalimbali kwa ajili ya kile ambacho yeye mwenyewe anaweza kumtolea huyo mwenzake kwa njia fulani. Yote hayo yanahitaji mpango wa kitengenezo. Ili mpango wa kitengenezo ufanikiwe ni lazima kuwe na mamlaka inayotambuliwa, zaidi ya kuwa na akili zinazopatana. Taifa, serikali au mkoa, mji au kijiji, yote ni matengenezo ya kisiasa yanayohitaji mtu fulani atoe usimamizi na wengine wasimamiwe au wawe watii. Kanuni hiyo inahusu karibu kila upande mwingine wa utendaji wa kibinadamu, uwe ni wa kilimwengu au wa kidini, wa hadharani au wa kinyumbani.
Lakini, na iangaliwe kwamba hata wale walio na mamlaka wanahitaji kutii nyakati fulani. Kwa mfano, mtu hawezi kuvunja sheria za barabarani na asipate adhabu. Wakati mtu anapoenda hospitali akapasuliwe anajikuta akiwa na wajibu wa kutii madaktari, wakunga na wengine wanaofanya kazi hospitalini. Huenda mfanya biashara akawa na wafanya kazi wengi chini yake, lakini anapoenda kwenye kundi la Kikristo la kwao, huenda akawa na wajibu wa kutii wazee wanaomsimamia yeye na waabudu wenzake.
Utii kwa Serikali
Katika jamii ya sasa ya kibinadamu, serikali zinahitajiwa kabisa ili watu waishi kwa ustaarabu na kupata usalama wa kiasi fulani, zaidi ya kuwa na utumishi mwingi wanaofanyiwa na serikali, katika mitaa yao au katika taifa zima. Kwa hiyo, ni wazi kwamba lazima kuwe na nia ya kupenda, au angalau kukubali kusimamiwa, upande wa wanaoongozwa ili serikali hizo ziweze kutimiza kusudi zinalotaka. Ndiyo sababu Neno la Mungu linaamuru Wakristo ‘watii kwa maana hakuna mamlaka isipokuwa kwa njia ya Mungu.’ Kwa hiyo Wakristo wanapaswa kutii sheria za nchi, wakidhamiria kulipa kodi, kutii kanuni zinazoongoza magari barabarani na kutimiza wajibu mwingine mbalimbali. Yote hayo yanaleta amani na utengemano.—Warumi 13:1-7, NW.
Lakini, Biblia inaonyesha mahali penginepo kwamba utii huo kwa serikali za kisiasa si kamili. Unaongozwa na maagizo mengine ya Kimaandiko, kama, “Basi, mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu.” Na tena: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.” Ndiyo, amri inayosema ‘tiini’ serikali za kisasa za huu mfumo wa mambo si kamili, bali ni ya kiasi; inatumika maadamu haipingani na amri yo yote ya Mungu inayosema jambo moja kwa moja.—Mathayo 22:21; Matendo 5:29
Katika Kundi la Kikristo
Kundi la Kikristo ni tengenezo pia, lenye kichwa kimoja juu yake, yaani, Yesu Kristo. Washiriki wote walo wanapaswa kumtii. Basi hata yeye mwenyewe anapaswa kutii. Kutii nani? Baba yake wa kimbingu, Yehova Mungu. Ndiyo, ‘kundi la Kikristo linatii Kristo.’ (Waefeso 5:24, NW) Kwa kweli, “kichwa cha kila mwanamume ni Kristo.”—1 Wakorintho 11:3.
Yesu Kristo, mtu wa kimungu asiyeonekana aliye katika mbingu, anatumiaje ukichwa wake juu ya kundi la kibinadamu linaloonekana hapa duniani? Njia moja ni kupitia Maandiko yaliyoongozwa na Mungu. Kundi linaweza kuonwa kuwa la Kikristo ikiwa tu linatii amri za Yesu mwenyewe na zile zilizotolewa na mitume na wanafunzi wengine wake chini ya uongozi wa Mungu.—Mathayo 18:18; 28:19, 20.
Tena, Yesu anatumia ukichwa wake juu ya kundi la Kikristo kupitia “msaidiaji,” “roho ya ule ukweli,” roho takatifu ya Mungu, au kani ya utendaji. (Yohana 16:7, 13, NW) Halafu, pia, anatumia malaika kutimiza ukichwa wake juu ya kundi lake. (Mathayo 18:10; 24:31; Ufunuo 14:6) Yesu Kristo anatumia pia ukichwa wake juu ya kundi la Kikristo hapa duniani kupitia kikundi cha Wakristo waaminifu wapakwa mafuta, ambao Yesu alisema hivi juu yao: “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.”—Mathayo 24:45-47.
Ili Yesu Kristo aweze kufanyiza kazi aliyoamuru wafuasi wake wafanye, yaani, kufanya wanafunzi kati ya watu wa mataifa yote, ni lazima wafanye kazi kwa amani na upatano. Ni lazima ‘wote wanene mamoja.’ Kwa hiyo lazima wote watii chombo anachopendezwa kukitumia. Ni kama tunavyosoma: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” Kwa hiyo katika kundi la Kikristo “mambo yote [yanapasa] yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu.”—1 Wakorintho 1:10; 14:33, 40.
Zaidi ya hilo, katika kundi la Kikristo washiriki mbalimbali wanashauriwa kila mmoja atii mwenzake. “Hali mnanyenyekeana [mnatiiana, NW] katika kicho cha Kristo.” (Waefeso 5:21) Hasa wale wenye umri mdogo zaidi wanapaswa kutii wanaume wenye umri mkubwa zaidi au wazee: “Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.”—1 Petro 5:5.
Pia, washiriki wote mmoja mmoja wa kila kundi wanapaswa kutii wazee Wakristo waliowekwa, kama vile tunavyosoma: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya [nafsi] zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.” Hivyo kuna sababu mbili za Mkristo kuwa mtii. Moja ni kwa ajili ya uendeshaji mzuri wa kazi, kwa ajili ya amani au upatano, kwa ajili ya kutendesha kiasi kilicho kikubwa zaidi cha kazi, tena kwa njia iliyo bora zaidi. Ile nyingine ni kwamba kukosa kutii kungeweka mzigo juu ya wale wanaoongoza, halafu wale pia wasiotii wangeumia.—Waebrania 13:17.
Katika Kazi za Kimwili
Upande mwingine ambao kanuni ya kutii inatumika ni katika uhusiano wa tajiri wa kazi na mfanya kazi. Wakati mtu anapokubali namna fulani ya kazi ya kuajiriwa, anapaswa kutambua wajibu wake kwa tajiri wa kazi, yaani, kumtii—bila shaka maadamu haombwi afanye jambo linalopingana na dhamiri yake. Kutii tajiri wa kazi maana yake ni kumpa heshima inayostahili cheo chake na kumfanyia kazi ya siku bila udanganyifu, na kutokumwibia cho chote. Kama vile mtume Paulo alivyoshauri, mwajiriwa anapaswa kufanya kazi yake ‘akiwa na nafsi yote kama kwa Yehova, na si kwa wanadamu.’ (Wakolosai 3:23, NW) Tena hilo ndilo jambo linalofaa na pia la hekima kufanya. Ikiwa mtu hawezi kufanya hivyo, anapaswa kubadili mahali pa kazi.
Katika Jamaa
Kwa kuwa jamaa ni kitengenezo kidogo, ni wazi kwamba kanuni ya ukichwa na utii inatumika kwa washiriki wake. Neno la Mungu linaweka daraka juu ya wazazi kuhakikisha kwamba watoto wao wanalelewa vizuri na kutunzwa kwa kila njia. Ndiyo sababu watoto wanaamriwa hivi: “Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” (Wakolosai 3:20) Jambo la kwamba watoto wanapaswa kutii wazazi ni la kiasi na la akili nzuri kwa kuwa linapatana na Maandiko. Wao hawana ujuzi na hawawezi kujitafutia riziki. Tena, Mfalme Sulemani mwenye hekima aliona hivi wakati mmoja: “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali.”—Mithali 22:15.
Kanuni ya ukichwa na utii inatumika kati ya wazazi wenyewe, kwa mume na mke. Ni nani anayetumia ukichwa, mume au mke? Kulingana na Yule aliyefanya mwanamume na mwanamke hapo kwanza, mume ndiye anayepaswa kutumia ukichwa. Mtume Paulo anakumbusha wote kwamba “mwanamume hakuumbwa kwa ajili ya mwanamke, bali mwanamke kwa ajili ya mwanamume.” (1 Wakorintho 11:9) Neno la Mungu linatuambia hivi pia: “Kama vile [kundi] limtiivyo Kristo, vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo.” (Waefeso 5:24) Bila shaka wanawake fulani wa kisasa wataanza ubishi juu ya amri hiyo, lakini acheni tufikirie hilo kidogo.
Hakika inastahili kuangaliwa kwamba ni baada tu ya kushauri wake kwamba mtume Paulo anafuatisha moja kwa moja shauri kwa waume juu ya kupenda wake zao kama vile Yesu alivyolipenda kundi kufikia kulitolea uhai wake. Halafu huko mbele, Paulo anasema kwamba wanaume, wale wenye wake, wanapaswa kupenda wake zao kama miili yao wenyewe, wakiwalisha na kuwatunza sawasawa na miili yao wenyewe. Kwa uhakika, mume akionyesha mke wake upendo wa namna hiyo, mke atafurahia sana kumtii.—Waefeso 5:25-33.
Mpango huo ni wa hekima na haki pia. Kulingana na mambo yalivyo kwa asili mwanamume kwa kawaida ndiye anayefaa zaidi kuchukua uongozi, kuchukua hatua ya kwanza kufanya mambo. Akichukua uongozi wa namna inayofaa, inaelekea sana kwamba mke wake atafurahia kuufuata, kuukubali. Ni jambo la kupendeza kuona yale yaliyosemwa na mmoja wa madaktari mashuhuri wa ugonjwa wa akili mjini New York juu ya habari ii hii. Katika kitabu chake, daktari huyo wa kike anatoa maelezo juu ya visa vingi kuonyesha namna wanawake wanavyoweza kutosheka na ngono za ndoa yao. Ni kwa kufanya nini? Kwa kukubali tu katika akili na mioyo yao ukichwa wa waume zao.
Mke atasaidika akifikiria upande mwingine wa uhusiano kati ya mume na mke, kama anavyoshauriwa na Biblia. Kwa sababu ya maoni ya mke ya moyoni yenye kubadilika-badilika, mume wake anatakwa aonyeshe subira, fadhili, fikira. Mume anaonyesha hayo wakati anapomngojea mkeye mara nyingi amalize kujitayarisha au anapojikuta akihitajika kurekebisha matakwa au mapendezi yake ili afuate matakwa, misisimuko au hali za kupungukiwa za mkeye. Mtume Petro alikuwa na sababu nzuri ya kushauri hivi: “Ninyi waume lazima mwishi pamoja na wake zenu kwa ufahamu unaofaa wa kwamba wao ndio ile jinsia iliyo dhaifu zaidi. Watendeeni kwa heshima, kwa sababu wao pia watapokea, pamoja nanyi, zawadi ya Mungu ya uzima. Fanyeni hivyo ili cho chote kisizuie sala zenu.”—1 Petro 3:7, Good News Bible.
Wala si vibaya kuangalia kwamba jambo linalofurahisha wake wengi zaidi ya mambo yote mengine ni kuwafanya waume wao watake kuwatendea mambo fulani fulani. Inaelekea hiyo ndiyo njia mume alitumia pale mwanzoni ili akubaliwe na mke wake—kwa kumtendea mambo mazuri-mazuri, kutaka kumfurahisha kwa kumfanyia mambo. Na ndivyo ilivyo wakati wote wa maisha ya ndoa. Kinachomletea mke furaha ni mume kuwa na bidii ya kutaka kumfanyia mambo fulani fulani, hata kama ni mambo madogo ya uungwana kama kumsaidia avae koti lake, kukumbuka sherehe walizofanya kuadhimisha siku ya arusi yao, au kumnunulia maua, marashi au kitu kingine. Lakini mke anaweza kumfanyaje mume wake atake kufanya mambo kama hayo? Si kwa kumtawala, si kwa kushindana naye, bali kwa kutambua ukichwa wake, kwa kumpa ile “heshima yenye kina kirefu” ambayo Biblia inasema inamstahili.—Waefeso 5:33, NW.
Kwa kweli, kutokana na yaliyotangulia kusemwa tunaweza kuona sababu gani Biblia inashauri Wakristo ‘watii’ serikali, wale wenye uangalizi katika kundi la Kikristo, matajiri wa kazi, wazazi, waume. Kutii kunanyima mtu jambo fulani, lakini kufanya hivyo kunastahili. Huenda kukamlazimu ajinyime fahari yake, mapendezi yake. Pia kunamaanisha kusitawisha kiasi na unyenyekevu. Mara nyingi kutahitaji uvumilivu, nia ya kumngojea Yehova Mungu anyoshe mambo, badala ya kufanya haraka kutenda jeuri, kama wakati mtu anapotendwa udhalimu wa kisheria. Kutii ndilo jambo la haki na hekima kufanya na pia la upendo. Basi ndilo jambo linalothawabisha zaidi.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]
KUTII SERIKALI MAANA YAKE NI
Kufanya utii wa kiasi
kulipa kodi
Kutii kanuni za magari barabarani
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]
KUTII KUNDI LA KIKRISTO MAANA YAKE NI
Kutii amri za Kristo
Kufanya ushirikiano na wazee waliowekwa
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]
KUTII TAJIRI WA KAZI MAANA YAKE NI
Kumfanyia kwa heshima kazi ya siku bila udanganyifu
Kutoiba
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]
KUTII KATIKA JAMAA MAANA YAKE NI
Mume kuonyesha fikira za upendo
Mke kunyenyekea kichwa wake
Watoto kutii wazazi