Kile Ambacho Ujitiisho wa Kimungu Wataka Kwetu
“Basi mtiini [jitiisheni kwa, NW] Mungu.”—YAKOBO 4:7.
1. Ni nini kiwezacho kusemwa juu ya aina ya Mungu tunayeabudu?
YEHOVA ni Mungu wa kustaajabisha kama nini! Hakuna aliye sawa naye, hana rika lake, halinganiki, hana kifani katika njia nyingi sana! Yeye ndiye aliye Juu Zaidi ya wote, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima, ambaye ndani yake hukaa mamlaka yote ya kweli. Yeye ni wa tangu milele hata milele na mwenye utukufu sana hivi kwamba hakuna mwanadamu awezaye kumwona akaishi. (Kutoka 33:20; Warumi 16:26) Yeye ana nguvu na hekima zisizo na kikomo, ni mkamilifu kabisa katika haki, na ndiye tashihisi ya (umbo la) upendo. Yeye ndiye Muumba wetu, Hakimu wetu, Mpaji-Sheria wetu, na Mfalme wetu. Kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu huja kutoka kwake.—Zaburi 100:3; Isaya 33:22; Yakobo 1:17.
2. Ujitiisho wa kimungu unahusisha mambo gani?
2 Kwa kufikiria mambo hayo yote ya hakika, hakuwezi kuwa na shaka juu ya wajibu wetu wa kujitiisha kwake. Lakini hilo linahusisha nini kwetu? Mambo kadhaa. Kwa kuwa hatuwezi kumwona Yehova Mungu uso kwa uso, ujitiisho kwake unahusisha mtu kutii mwongozo wa dhamiri yake iliyoelimishwa, kushirikana na tengenezo la Mungu la kidunia, kutambua mamlaka za kilimwengu, na kustahi kanuni ya ukichwa katika mzingo wa familia.
Kushikilia Dhamiri Njema
3. Ili kudumisha dhamiri njema, ni lazima tutii makatazo ya aina gani?
3 Ili kudumisha dhamiri nzuri, ni lazima tutii yale yasiyoweza kufikilizwa—yaani, sheria au kanuni ambazo wanadamu hawawezi kufikiliza. Kwa kielelezo, amri ya kumi ya yale Maneno Kumi, iliyokataza kutamani, haikuweza kufikilizwa na mamlaka za kibinadamu. Jambo tu ni kwamba, hilo lathibitisha chanzo cha kimungu cha yale Maneno Kumi, kwani hakuna kikundi chochote cha kibinadamu chenye kutunga sheria ambacho kingaliweza kutunga sheria ambayo haingeweza kufikilizwa kwa njia ya adhabu ikiwa ingehalifiwa. Kwa sheria hiyo, Yehova Mungu alimpa kila Mwisraeli daraka la kuwa polisi wa nafsi yake mwenyewe—ikiwa angekuwa na dhamiri safi. (Kutoka 20:17) Vivyo hivyo, miongoni mwa kazi za mnofu ambazo zingemzuia mtu asiurithi Ufalme wa Mungu ni “wivu” na “husuda”—maitikio ambayo adhabu haziwezi kufikilizwa na mahakimu wa kibinadamu. (Wagalatia 5:19-21) Lakini ili kushikilia dhamiri njema, ni lazima tuyaepuke hayo.
4. Ili kudumisha dhamiri njema, ni lazima tuishi kulingana na kanuni zipi za Biblia?
4 Naam, ni lazima tuishi kulingana na kanuni za Biblia. Kanuni hizo zaweza kutolewa muhtasari katika zile amri mbili ambazo Yesu Kristo alitaja katika kujibu lile swali kuhusu ni amri gani iliyokuwa kuu zaidi katika mpangilio wa sheria ya Kimusa. “Mpende Bwana [Yehova, NW] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. . . . Mpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mathayo 22:36-40) Yenye kuonyesha kinachohusishwa na ya pili kati ya amri hizo, ni maneno ya Yesu yaliyorekodiwa kwenye Mathayo 7:12: “Yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii.”
5. Twaweza kudumishaje uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu?
5 Ni lazima tufanye yale tujuayo kuwa sawa na tusifanye yale tujuayo si sawa, iwe wengine waona au la. Hilo ni kweli hata ingawa huenda tukaepuka kuadhibiwa kwa sababu ya kutofanya tupaswalo au kwa sababu ya kufanya tusilopaswa kufanya. Inamaanisha kudumisha uhusiano mwema pamoja na Baba yetu wa kimbingu, tukikumbuka lile onyo ambalo mtume Paulo alitoa kwenye Waebrania 4:13: “Hakuna kiumbe kisichokuwa wazi mbele zake, lakini vitu vyote vi utupu na kufunuliwa machoni pake yeye aliye na mambo yote.” Kuendelea kufanya yaliyo sawa kutatusaidia kushindana na mbinu za kiufundi za Ibilisi, kukinza mibano ya ulimwengu, na kupiga vita dhidi ya mwelekeo wa ubinafsi uliorithiwa.—Linganisha Waefeso 6:11.
Ujitiisho kwa Tengenezo la Mungu
6. Ni njia zipi za uwasiliano ambazo Yehova alitumia katika nyakati za kabla ya Ukristo?
6 Yehova Mungu hakutupa sisi haki ya kujiamulia mmoja mmoja jinsi tutakavyotumia kanuni za Biblia maishani mwetu. Tangu mwanzo wa historia ya ainabinadamu, Mungu amewatumia wanadamu kuwa njia za uwasiliano. Hivyo, Adamu alikuwa mnenaji wa Mungu kwa Hawa. Amri kuhusu lile tunda lililokatazwa lilipewa kwa Adamu kabla ya Hawa kuumbwa, kwa hiyo ni lazima iwe Adamu alimjulisha Hawa kuhusu mapenzi ya Mungu kwake. (Mwanzo 2:16-23) Noa alikuwa nabii wa Mungu kwa familia yake na kwa ulimwengu wa kabla ya gharika. (Mwanzo 6:13; 2 Petro 2:5) Abrahamu alikuwa mnenaji wa Mungu kwa familia yake. (Mwanzo 18:19) Musa alikuwa nabii na njia ya Mungu ya kuwasiliana na taifa la Israeli. (Kutoka 3:15, 16; 19:3, 7) Baada yake, hadi Yohana Mbatizaji, manabii, makuhani, na wafalme wengi walitumiwa na Mungu wawasilishe mapenzi yake kwa watu wake.
7, 8. (a) Mesiya alipokuja, ni nani ambao wametumiwa wakiwa wanenaji wa Mungu? (b) Ujitiisho wa kimungu hutaka nini kwa Mashahidi wa Yehova leo?
7 Mesiya, Yesu Kristo, alipokuja, Mungu alimtumia yeye na mitume na wanafunzi walioshirikiana na yeye kwa ukaribu watumikie wakiwa wanenaji Wake. Baadaye, wafuasi waaminifu wapakwa-mafuta wa Yesu Kristo wangetumikia wakiwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” katika kuwasiliana na watu wa Yehova kuhusu jinsi ya kutumia kanuni za Biblia maishani mwao. Ujitiisho wa kimungu ulimaanisha kutambua chombo ambacho Yehova Mungu alikuwa akitumia.—Mathayo 24:45-47; Waefeso 4:11-14.
8 Mambo ya hakika yaonyesha kwamba leo “mtumwa mwaminifu mwenye akili” anashirikishwa na Mashahidi wa Yehova na kuwakilishwa na Baraza Linaloongozwa la Mashahidi hao. Baraza hilo nalo huweka rasmi waangalizi katika vyeo mbalimbali—kama vile wazee na wawakilishi wasafirio—ili waelekeze kazi kwenye kiwango cha mahali fulani. Ujitiisho wa kimungu unataka kila Shahidi aliyejiweka wakfu ajitiishe kwa waangalizi hao kulingana na Waebrania 13:17: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya roho zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.”
Kukubali Nidhamu
9. Ujitiisho wa kimungu huhusisha nini mara nyingi?
9 Mara nyingi ujitiisho wa kimungu ni jambo la kukubali nidhamu kutoka kwa wale wanaotumikia wakiwa waangalizi. Ikiwa nyakati zote hatujitii wenyewe nidhamu inayohitajika, huenda tukahitaji kushauriwa na kutiwa nidhamu na wale wenye ujuzi na mamlaka ya kufanya hivyo, kama vile wazee wa kundi letu. Kukubali nidhamu hiyo ni mwendo wa hekima.—Mithali 12:15; 19:20.
10. Wale wanaotia nidhamu wana wajibu gani?
10 Kwa wazi, wazee wanaotoa nidhamu lazima wao wenyewe wawe vielelezo vya ujitiisho wa kimungu. Jinsi gani? Kulingana na Wagalatia 6:1, hawapaswi tu kuwa na namna nzuri ya kushauri bali pia wanapaswa kuwa wenye kielelezo bora: “Ndugu zangu, mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi mlio wa Roho [sifa za kiroho, NW] mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe.” Yaani, shauri la mzee lapaswa lipatane na kielelezo chake. Hilo lapatana na lile onyo la upole linalotolewa kwenye 2 Timotheo 2:24, 25 na kwenye Tito 1:9. Naam, wale wanaokaripia au kukosoa lazima wawe na uangalifu wasiwe wakali kamwe. Nyakati zote wanapaswa wawe wapole, wenye fadhili, na bado imara katika kutegemeza kanuni katika Neno la Mungu. Wanapaswa wawe wasikilizaji wasiopendelea upande, wakiwaburudisha wale wanaomenyeka na kulemewa na mizigo.—Linganisha Mathayo 11:28-30.
Ujitiisho kwa Mamlaka Zilizo Kubwa
11. Ni nini kinachotakiwa kwa Wakristo katika mahusiano yao pamoja na mamlaka za kilimwengu?
11 Ujitiisho wa kimungu hututaka pia tutii mamlaka za kilimwengu. Tunashauriwa hivi kwenye Warumi 13:1: “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu [kubwa]; kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa [isipokuwa kwa njia ya, NW] Mungu; na ile iliyopo imeamriwa na Mungu.” Miongoni mwa mambo mengine, maneno hayo yanatutaka tutii sheria zinazohusu kuendesha magari barabarani na kuwa wenye kudhamiria kulipa kodi na ushuru, kama vile mtume Paulo aonyeshavyo kwenye Warumi 13:7.
12. Ujitiisho wetu kwa Kaisari ni wa kadiri katika maana gani?
12 Ingawa hivyo, ni wazi kwamba ujitiisho wote wa aina hiyo kwa Kaisari lazima uwe wa kadiri. Ni lazima sikuzote tukumbuke ile kanuni ambayo Yesu Kristo alitoa, kama ilivyorekodiwa kwenye Mathayo 22:21: “Mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu.” Kielezi chini cha Warumi 13:1 katika Oxford NIV [New International Version] Scofield Study Bible huonelea hivi: “Hilo halimaanishi kwamba anapaswa atii sheria zisizo za kiadili au zinazopinga Ukristo. Katika hali hizo ni wajibu wake kumtii Mungu kuliko wanadamu (Mdo. 5:29; cp. Dan. 3:16-18; 6:10ff).”
Ujitiisho wa Kimungu Ndani ya Mzingo wa Familia
13. Ujitiisho wa kimungu katika mzingo wa familia hutaka nini kwa washiriki wayo?
13 Katika mzingo wa familia, mume na ambaye ni baba hutumikia akiwa kichwa. Hilo lataka wake watii lile shauri linalotolewa kwenye Waefeso 5:22, 23: “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili.”a Kwa habari ya watoto, wao hawajitungii sheria zao wenyewe bali wanawiwa ujitiisho wa kimungu na baba na mama pia, kama vile Paulo aelezavyo kwenye Waefeso 6:1-3: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki. Waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi, Upate heri, ukae siku nyingi katika dunia.”
14. Ujitiisho wa kimungu hutaka nini kwa vichwa vya familia?
14 Bila shaka, hufanya iwe rahisi zaidi kwa wake na watoto kutoa ujitiisho wa kimungu wa jinsi hiyo wakati waume na akina baba wenyewe wanapoonyesha ujitiisho wa kimungu. Wao hufanya hivyo kwa kuzoea ukichwa wao kulingana na kanuni za Biblia, kama zile zinazopatikana kwenye Waefeso 5:28, 29 na 6:4: “Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea kanisa.” “Nanyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana [Yehova, NW].”
Misaada Katika Kudhihirisha Ujitiisho wa Kimungu
15. Ni tunda gani la roho litakalotusaidia tudhihirishe ujitiisho wa kimungu?
15 Ni nini kitakachotusaidia tudhihirishe ujitiisho wa kimungu katika maeneo hayo mbalimbali? Kwanza, kuna upendo usio na ubinafsi—kupenda Yehova Mungu na wale ambao ameweka juu yetu. Twaambiwa kwenye 1 Yohana 5:3: “Kwa maana huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si nzito.” Yesu Kristo alisema jambo hilohilo katika Yohana 14:15: “Mkinipenda, mtazishika amri zangu.” Kwelikweli, upendo—lile tunda la kwanza la roho—utatusaidia tuthamini yote ambayo Yehova ametufanyia na hivyo utatusaidia tuzoee ujitiisho wa kimungu.—Wagalatia 5:22.
16. Hofu ya kimungu ni ya msaada gani katika kuonyesha ujitiisho wa kimungu?
16 Pili, kuna hofu ya kimungu. Kuhofu kumchukiza Yehova kutatusaidia kwa sababu kunamaanisha “kuchukia uovu.” (Mithali 8:13) Bila shaka, kuhofu kumchukiza Yehova kutatufanya tusiridhiane kwa sababu ya kuhofu mwanadamu. Kutatusaidia tutii maagizo ya Mungu haidhuru ni magumu gani yanayohitaji kushindwa. Zaidi ya hayo, kutatuzuia tusikubali kuvutwa na vishawishi au mielekeo ya kutenda mabaya. Maandiko huonyesha kwamba kumhofu Yehova ndiko kulikomwezesha Abrahamu ajaribu kumtoa dhabihu mwanae mpendwa Isaka, na ni kuhofu kumchukiza Yehova kulikomwezesha Yusufu akinze kwa mafanikio matongozi yasiyo ya kiadili ya mke wa Potifa.—Mwanzo 22:12; 39:9.
17. Imani ina fungu gani katika kuzoea kwetu ujitiisho wa kimungu?
17 Msaada wa tatu ni imani katika Yehova Mungu. Imani itatuwezesha kutii shauri linalotolewa kwenye Mithali 3:5, 6: “Mtumaini BWANA [Yehova, NW] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” Imani itatusaidia hasa tunapoonekana kuwa tunateseka isivyo haki au tunabaguliwa kwa sababu ya rangi, taifa, au kwa sababu ya hitilafu za kiutu. Pia huenda wengine wakahisi kwamba hawafikiriwi wakati hawapendekezwi kutumikia kuwa mzee au mtumishi wa huduma. Ikiwa tuna imani, tutamngojea Yehova arekebishe mambo kwa wakati wake. Kwa wakati huu huenda tukahitaji kusitawisha uvumilivu wenye saburi.—Maombolezo 3:26.
18. Msaada wa nne ni upi katika kuonyesha kwetu ujitiisho wa kimungu?
18 Msaada wa nne ni unyenyekevu. Mtu mnyenyekevu haoni ugumu wa kudhihirisha ujitiisho wa kimungu kwa sababu ‘kwa unyenyekevu, anawahesabu wengine kuwa bora kuliko nafsi yake.’ Mtu mnyenyekevu ana nia ya kujiendesha mwenyewe akiwa “mdogo.” (Wafilipi 2:2-4; Luka 9:48) Lakini mtu mwenye kiburi huchukia kujitiisha na huudhika juu ya hilo. Imesemwa vema kwamba mtu wa aina hiyo huona ni afadhali aangamie akiwa na sifa badala ya kuonywa makosa ili aokolewe.
19. Aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society aliandaa kielelezo gani kizuri cha unyenyekevu?
19 Kielelezo kizuri cha unyenyekevu na ujitiisho wa kimungu kilitolewa wakati mmoja na Joseph Rutherford, msimamizi wa pili wa Watch Tower Bible and Tract Society. Wakati Hitla alipopiga marufuku kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani, akina ndugu katika Ujerumani walimwandikia wakiuliza lile wapaswalo kufanya kwa sababu ya mikutano na utendaji wao wa kuhubiri kupigwa marufuku. Yeye alitaja jambo hilo kwa familia ya Betheli na akakiri kwa wazi kwamba yeye hakujua atawaambia nini ndugu Wajerumani, hasa kwa sababu ya adhabu kali sana iliyohusika. Alisema kwamba ikiwa yeyote angejua la kuwaambia, yeye angefurahia kulisikia. Hiyo ilikuwa roho ya unyenyekevu kama nini!b
Manufaa za Kudhihirisha Ujitiisho wa Kimungu
20. Ni baraka zipi zinazotokana na kudhihirisha ujitiisho wa kimungu?
20 Huenda ikafaa kuuliza, Ni manufaa zipi za kudhihirisha ujitiisho wa kimungu? Kwa kweli, kuna mengi. Tunaepuka mahangaiko na mifadhaiko ambayo huwapata wale wanaotenda kwa kujitegemea. Tunafurahia uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu. Tuna ushirika ulio bora kabisa pamoja na ndugu zetu wa Kikristo. Zaidi ya hayo, kwa kujiendesha wenyewe kisheria, twaepuka matata yasiyohitajika kutoka mamlaka za kilimwengu. Twafurahia pia maisha ya familia yenye furaha tukiwa waume na wake, tukiwa wazazi na watoto. Isitoshe, kwa kudumisha ujitiisho wa kimungu, tunatenda kupatana na shauri linalotolewa kwenye Mithali 27:11: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.”
[Maelezo ya Chini]
a Mhudumu mmoja aliye painia alimwambia painia mmoja mseja akisifu staha na uungaji mkono wenye upendo wa mke wake. Painia huyo mseja akafikiri kwamba rafiki yake angalipaswa pia aseme jambo fulani juu ya sifa nyingine za mke wake. Lakini miaka kadhaa baadaye, wakati painia huyo mseja alipooa, alitambua jinsi uungaji mkono wenye upendo upande wa mke ulivyo muhimu kwa furaha ya ndoa.
b Baada ya kusali sana na kulichunguza sana Neno la Mungu, Joseph Rutherford aliona wazi jibu alilopaswa kuwapa ndugu katika Ujerumani. Halikuwa jukumu lake kuwaambia la kufanya na lisilo la kufanya. Wao walikuwa na Neno la Mungu, lililowaambia kwa wazi wapaswayo kufanya kwa habari ya kukutana pamoja na kutoa ushahidi. Kwa hiyo akina ndugu Wajerumani walianza kufanya kazi kichinichini lakini waliendelea kutii amri za Yehova za kukutana pamoja na kutoa ushahidi wa jina lake na Ufalme wake.
Maswali ya Kupitia
◻ Ni watu gani ambao Mungu ametumia wakiwa njia za uwasiliano, na watumishi wake waliwiwa nini nazo?
◻ Ujitiisho wa kimungu wahusu mahusiano gani mbalimbali?
◻ Ni sifa zipi zitakazotusaidia tuonyeshe ujitiisho wa kimungu?
◻ Ujitiisho wa kimungu hutokeza baraka zipi?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Mungu alitumia tengenezo la hekalu la Yerusalemu ili kuwasilisha mapenzi yake kwa watu wake
[Picha katika ukurasa wa 18]
Maeneo ambayo katika hayo twaweza kudhihirisha ujitiisho wa kimungu